Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 41. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 41.

 

Wakati mawazo yakimrudisha nyuma, akagutuka. “Hapana!” Akapinga kwa nguvu kabisa. “Hawawezi kuniyumbisha.” Akaendelea kuwaza. “Maana nikiyumba mimi, ni kumyumbisha Jelini na Kamila. Na nitaharibu kwa wazazi pamoja na kwa Mill.” Akatafakari ukubwa wa hilo jambo akaona madhara atakayosababisha akirudi kwa Jelini na pengine Jelini kumkubali, ni makubwa sana. Akaonya hisia zake.

    “Kwanza haitakuwa sawa kwa Jelini mwenyewe na Ezra.” Akatamani kama angekuta kosa kwa Ezra, akajipatia sababu, lakini akajikuta Ezra hana hatia ya kumpokonya Jelini. Akajirudi na kuona maamuzi aliyokuwa nayo tokea mwanzo yalikuwa sahihi. “Siwezi kuyumbishwa na maneno yaliyojaa wivu na hasira.” Akasimama kabisa ili kutojipa nafasi ya kuendelea kufikiria zaidi.

Akasimamia maamuzi yake ya tokea mwanzo anamfuata Jelini hotelini na kumuacha. Akatoka kabisa hapo chumbani kumfuata Kamila akikusudia kutengeneza kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Akamkuta jikoni ameanza kuwa busy na msichana wa kazi akimsaidia kuandaa aanze kupika. “Nakupenda Kamila. Nakupenda na hata Jelini anajua kama yupo Kamila kwenye maisha yangu na mimi ndio nimebahatika.” Akaanza kumpata. Akamwangalia. “Na ujue nimekusifia sana kwa Jelini.” Akaendelea akimjua Kamila, moyo mwepesi.

    “Nimejisifia jana, utafikiri niliulizwa!” “Unanipamba tu.” “Sasa kwa nini nikudanganye? Na James mwenyewe anajua kama Kamila ni Mungu kunifuta machozi. Nimewaambia Kamila wangu hana makuu. Hata kama mimi walikuwa wananiona ni mbaya, basi kwa Kamila mimi sina hatia. Kamila wangu ananisitiri. Upendo wake unafunika mapungufu yangu YOTE. Nimejisifu kweli!” “Unanipamba tu.” “Nimpigie simu James nimtege halafu umsikie akisema sifa za Kamila wangu?” Akapandisha mabega akikataa, ila akatoa kilichomkera.

    “Sasa wewe kwa nini unaniacha humu ndani unamkimbilia Jelini?” “Na nimezungumza naye sana jana. Tulikutana mimi na yeye wote tunamapungufu. Ila nikamsihi ajaribu kubadilika, nikamwambia mimi nimejifunza sana kutoka kwako. Nikampa mifano yako na Mike mpaka akatulia. Nimemshauri arudi kwa mchumba wake.” “Kwamba wewe humtaki tena huyo Jelini?!” “Sasa mimi si nishapewa Kamila wangu!” Hapo dhambi zote akasamehewa. Cheko Kamila, hana makuu. Akiwekwa sawa kidogo tu, bila nguvu nyingi, keshalainika.

    “Nakupenda Kamila. Na jana sikukuaga kwa sababu kwanza nilijua utakua umeshalala. Maana mimi mwenyewe aliniamsha kwenye usingizi mzito, nyumba nzima ilikuwa imepoa, hata sikujua kama baba angesikia! Nilitoka kwa kunyata ili nisisumbue yeyote yule. Sikutaka wote tukeshe.” Akamuona amenyamaza.

    “Umenisamehe?” “Kwa kumkimbilia Jelini?” Colins akaanza kucheka. “Usicheke bwana!” “Mimi nahisi hata mbinguni nitavikwa taji. Wakati watu wote wamelala, mpaka malaika, mimi nilienda kuokoa ndoa. Ulitakiwa unipongeze.” “Sasa siku nyingine wewe usiwe na wasiwasi. Kule kumtafuta kwenye kompyuta yako hapo chumbani, nakumpata, kisha kumpa shemeji yake pia utavikwa taji.” “Hilo nimeelewa. Kama wewe ukisema nivunje uaminifu wake kwangu, kwa kutoa siri ya alipo, basi nitafanya hivyo.”

    “Kwanza ulimfuata wapi?” Colins akaanza kucheka akimwangalia. Kamila akakunja uso na kugeuka kabisa. “Usiniambie ni hotelini Colins, bwana!” “Nakwambia hakuna kilichotokea. Na nilimwambia kabisa, kwa heshima yako na Ezra mchumba wake.” Akatulia akitafakari.

    “Kwa hiyo Jelini anajua kama sasahivi una mchumba anaitwa Kamila?” “Sio hivyo tu, na sifa zako kibao anazo. Wewe acha kupika, twende zetu tukamalizie ibada, twende tukale na familia. Ratiba yetu ya leo iendelee kama tulivyo panga.” Akakubali kwa roho moja, akatoka hapo jikoni kwenda kubadili.

Raha Ya Mpatano Baada Ya Ugomvi Wa Wapenzi.

    Colins akamfuata wakati anatoa nguo ndio akawa anaingia. Akamkumbatia akiwa na chupi na sidiria tu. “Sitakusaliti Kamila.” “Hata na Jelini?” “Hata na Jelini.” Zikaanza kissing, wakajisahau, akamtoa chupi. “Nina hamu na wewe Colins!” Akajilalamisha. Akavuta godoro na kulitupia sakafuni, mchezo ukaanza hapo wakiwa wamekumbatiana kama wasianguke.

    Na hivi Kamila ashajua kama Jelini anajua kama yeye ndio mmiliki wa Colins, akajawa sifa huyo! Hisia zikawa juu haswa. Akishikwa kidogo, anapiga bao. Akamng’ang’ania mwenzie kwa uchu, wakikataka kiu vilivyo. Kuja kumaliza, na ibada kule inakaribia kuisha.

    Wawili hao mara ya mwisho ya penzi, waliachana wakijua wangerudi Kigamboni kwenda kuishi wote. Kwa hiyo walikatishwa. Penzi lililofanywa hapo kwanza la wizi wakijua wanaweza wasije pata tena nafasi kama hiyo tena, pili wasijue ni lini tena watapata nafasi kama hiyo. Basi wakakomezea mpaka kupitiliza.

Huku Kuliko Ungua Mpini, Kukabaki Shoka.

    Wakati yupo kanisani. Ameshindwa hata kupiga kinanda siku hiyo, wala gitaa hakuweza, akiwa amekaa kwenye kiti ameinamisha kichwa chini, waumini wengine wakiendelea kumsifu Mungu wao wakiimba na kucheza. Asilimia 99 ya kanisa walikuwa wamesimama wakicheza kwa shangwe, yeye alibaki tu amekaa, ameinamisha kichwa, mikono ameifungamanisha mbele kama anayeomba kumbe anashindwa hata kuzungumza na Mungu wake!

    Akahisi mikono laini inajipenyeza katikati ya viganja vyake. Ezra hakuamini! Maana alijua kwa hakika atakuwa Jelini tu, hakuna msichana mwingine angethubutu kumshika hivyo. Akafungua macho kuangalia, Jelini alikuwa amekaa kiti cha pembeni yake, karibu yake kabisa.

    Akajikuta anapiga magoti mbele yake na kumlalia. Kichwa ameegemeza magotini kwake amefunga macho. Wawili hao wakajisahau, Jelini akaanza kupitisha kucha pembezoni mwa sikio, mkono mwingine anampapasa mgongoni. Uzuri watu walikuwa wamesimama, wao wamekaa kiti cha mwisho kabisa, wachache sana waliona. Wakakaa hivyo kwa muda, kisha akarudi kukaa. Akamwangalia.

    Jelini akamwangalia na kuinama. “Samahani kukuumiza.”  Akanong’ona karibu kabisa ya sikio lake, japokuwa mziki ulikuwa ukitumbuiza kwa nguvu, aliweza kumsikia. Kisha akaongeza. “Na asante kwa kurudi.” Jelini akamshika tu kiganja cha mkono uliokuwa karibu yake. Akapishanisha vidole na kutulia wengine wakiendelea kumsifu Mungu.

    Wakatulia, baada ya muda akamuaga kwa kumnong’oneza sikioni. “Inabidi nirudi nyumbani sasahivi.” “Hatukai mpaka mwisho?” Akamwambia atoke nje wazungumze.

    Wakatoka lakini akampitia mtoto wake kwa Jema na familia yake walipokuwa wamekaa. Akatoka naye nje. Akampandisha garini na kumuwashia gari kabisa ili apate hewa kwa kuwa alipandisha vioo, ndio akatoka kuzungumza na Ezra.

“Lazima nirudi nyumbani sasahivi kwa ajili ya kumrudisha Jeremy kwa mama. Jema ameniambia anawasiwasi hajalala vizuri. Na bibi anaingia muda si mrefu. Nataka anikute ndani.” Alitamani kuuliza mengi. Zaidi kama bado ndoa ipo. Ila akashindwa. Akabaki amesimama mbele yake, kimya.

    Mwishoe Jelini mwenyewe akavunja ukimya. “Mimi sijasoma, lakini nafanyaga maamuzi yangu mimi mwenyewe.” “Najua Jelini. Na naomba unisamehe kwa kukuumiza. Nakiri ni wivu ndio umenifanya nizungumze hivyo, lakini sikudharau.”

    “Halafu mimi sio mtu wa kuendeshwa na mama. Tena nahisi nakusikiliza wewe zaidi kuliko hata mama. Sikutaka kuolewa na wewe eti kwa sababu mama ametaka! Niliamua mimi mwenyewe.” Akaendelea. “Na mimi swala la ndoa kwangu ni muhimu kama wewe. Nataka kuolewa na mtu anaye nihitaji Ezra! Mtu ambaye nimeleta maana kwake sio niwe nimeingia katika moja ya mipango ya mtu, ambaye anataka kuoa. Ndio Jelini nikatokea kama mwanamke. Hivyo hapana.”

    “Nakupenda Jelini.” “Lakini mimi nataka kuolewa na mtu ambaye ananihitaji Ezra, sio mtu ambaye hana shida na mimi kama Jelini, ila mwanamke. Kuniambia unanipenda halafu upo tayari tuachane siku chache kabla ya ndoa! Mimi hiyo imenitisha. Tena unaniambia sijachelewa!” “Nimekosea Jelini. Nimekosa mpenzi wangu, sijui niliingiliwa na nini!”

    “Ila jua nakupenda na nakuhitaji SANA. Sitaki hata kuhisi maisha bila wewe. Inawezekana niliongea kwa kiburi tu nikiwa na hasira, lakini sikuoi wewe kwamba bora naoa mwanamke! Hapana. Kama ingekuwa hivyo, ningekuwa nimeshaoa muda mrefu sana. Wanawake ni wengi. Tena warembo tu, lakini mimi nakutaka wewe Jelini. Nimekosa, na nimejifunza kutokana na makosa. Naahidi haitarudia tena.” Jelini kimya.

    “Umenisamehe?” “Yameisha Ezra. Ila inabidi mimi niondoke sasahivi.” “Naomba nikupigie baadaye tuzungumze.” “Labda usiku wakati wa kulala. Kutakuwa na fujo nyumbani, hapatakuwa na kusikilizana.” Ezra akajua amembadilikia. Jelini si wakutotaka kuzungumza naye eti mpaka usiku! “Uwe na siku njema Ezra.” Akamuaga akitaka kurudi garini.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Mara Junior akatoka. “Jelini! Jelini!” Akageuka maana alishafungua mlango wa gari. Akafunga na kurudi. “Vipi? Upo mzima na mtoto?” “Sisi wazima, ndio tunarudi nyumbani.” “Pole kwa matatizo.” “Nimeshapoa.” Wakanyamaza kama hawajui wazungumze nini tena! Akamwangalia Ezra, akamuona kama hayupo sawa.

    “Nikuulize kitu Jelini?” “Niulize tu.” “Kwa hili lililotokea. Unafikiri bado harusi ipo?” “Mimi sijui!” “Jelini!” “Kwani tokea mimi umenifahamu Junior, ushawahi hata nihisi nina sitasita kwenye mahusiano yangu na Ezra?” Akamuuliza na kuongeza.

    “Au ushaona hata mara moja nipo na nyinyi kama nipo mguu mmoja ndani mwingine nje?” “Hapana Jelini.” “Sasa kwa nini leo ndio mnaniuliza!? Mimi sina akili za kushikiwa. Nina akili zangu binafsi. Na nina uwezo wa kufikiria na kufanya maamuzi yangu mwenyewe.” “Najua Jelini!”

    “Na mimi si mbambaishaji. Nikiamua kufanya jambo, nafanya vizuri, tena kifasaha. Sijawahi kuwapa sababu hata mara moja kama mimi moyo wangu haupo na Ezra. Wakati wote nimesimama na nyinyi na kuonyesha mwenzenu nawahitaji. Lakini mnaniumiza jinsi mnavyonitilia mashaka! Sijui natakiwa kufanya nini ili mniamini!”

    “Basi Jelini. Basi mama. Nakupenda ndio maana sitaki kukupoteza. Nakujali ndio maana unaona nakuuliza. Na hatukudharau hata kidogo. Tafadhali usiumie.” “Nimeumia Junior.” “Pole. Unataka tukuletee nini nyumbani?” “Mimi sitaki kitu. Kwanza kutakuwa na wageni. Na wageni wa mama Jema ni komba. Kutajaa pombe hapo, hapatakuwa na pakupita.” Wakakwama.

    “Acha mimi nimuwahi mama, nimtulize kabla dada zake hawajaja. Nilikuja hapa mara moja tu, kumuona Ezra. Nishamuona, acha niwahi nyumbani, nimrudishie mama, Jeremy. Atulie maana nasikia hajalala.” Akarudi garini na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

    “Mbona huna raha tena!?” “Sijui Junior! Sijui kama ndoa ipo au la! Nimeshindwa kuuliza, nimeshindwa kupata jibu la moja kwa moja. Sijui kama nimesamehewa kabisa! Sijui kama tutarudi kuwa kama zamani! Jelini si wakuondoka bila hata kunishika! Hajui kama tutawasiliana au la! Sijui Junior.”

“Sijui nawaambia nini wazazi! Nahisi nimechanganyikiwa. Natamani kusogeza hii harusi mbele ili niwekane naye sawa, nimrudishe pale tulipokuwa kabla ya hili tukio.” Akawaza na kuongeza.

    “Jelini alikuwa akinipenda sana. Napenda vile alivyokuwa akionyesha ananihitaji. Alivyokuwa akifurahia nikimshika na kutaka kunisikia kila wakati. Sijawahi pata upendo kama wake. Nahisi navurugukiwa kabisa.”

    “Sikiliza Ezra. Tumia huohuo udhaifu wake kumrudisha kwako. Sasa hivi amekasirika. Mbembeleze kabisa ukimuonyesha unamjali na kumuhitaji. Yeye mwenyewe alikuwa amepania safari ya fungate na ndiye ametuhamasisha sisi wote mpaka tumeandaa masanduku ya huko, akiwa mstari wa mbele kundaa sanduku la Emelda pia, na kuhakikisha masanduku yote yapo kwetu tayari kwa safari.”

    “Na akahangaikia hati yake na ya Emelda mpaka Visa zote zikawa tayari.” “Kumbe unakumbuka?” “Nakumbua. Ni yeye mwenyewe Jelini.” Ezra akajibu.

“Sasa ndio ujue Jelini alikuwa yupo tayari na harusi ya jumamosi, ila amekasirika tu. Na japokuwa mama alisema tuwaache wapumzike mpaka siku ya harusi, tunaweza jiiba hata jumatatu mchana wazazi wakiwa kazini, tukaenda mpaka kwao, kujipanga naye upya. Sawa?” Akamtuliza mpaka tumaini likamrudia ndio wakarudi kanisani.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Alirudi kwao akamkuta mama yake yupo kitandani kama mgonjwa. “Mimi nimemrudisha huyo Jeremy. Na muulize kama kuna jambo baya nimefanya.” Kimya. “Na nimewahi kurudi ili bibi anikute ndani. Kwa hiyo usinilaumu. Mimi naenda zangu kunywa dawa ya usingizi. Nalala. Sitaki usumbufu.” “Nashukuru kwa kuwahi kurudi.” “Mimi sio mtoto mbaya.” Mama yake akakaa.

    “Najua. Kwa hiyo harusi ipo au bibi yako akija nimwambie nini?” Akanyamaza. “Eti Jelini, mama yangu mzazi, nikupendaye? Na Mode anakuja kukufunda.” “Nishamwambia mimi ndio nitamfunda.” Angalau mama Jema akacheka.

    “Anakuja sasahivi.” “Mimi nataka kulala mama.” “Basi nitawaambia taratibu. Ila ujue na Jema akitoka kanisani anakuja na familia yake.” “Mimi nalala.” “Hata Jema humtaki?” “Sasa hivi nimekukasirikia wewe.” “Sasa mimi nimefanyaje?!” “Huniamini na Jeremy wakati nishakuonyesha mara kibao mimi nimebadilika, lakini huniamini. Muulize huyo Jeremy kama mimi nimefanya jambo baya.”

    “Basi mama yangu mzazi. Akifunga shule, wewe mchukue popote unapotaka kwenda, ilimradi kila usiku nizungumze naye. Hapo hatutakuwa na neno. Lakini si katikati ya shule, halafu ukiwa umekasirishwa, unakuwa kama unakimbia watu! Sijui alipo! Sijui anapokwenda kulala! Sijui nani atamsogelea, nani atamgusa! Hapo utaniua na pressure.” Akaondoka bila ya kujibu.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Alivyo Jelini, akaingia chumbani kwake na kufunga mlango kabisa. Akaoga tena na kuvaa nguo za kulalia kabisa, akanywa kweli dawa za usingizi. Tena akajiongezea dozi. Akawasha mziki kwa sauti ya kuenea chumba ili kelele za nje zisimkere. Akafunga madirisha yote. Giza. Akajiwashia A/C. Jelini mpenda kitanda, akazima kama mshumaa.

Love Comes To Those Who Belive It

Familia ya Komba walishaandaa mazingira maalumu ya kuchumbiwa kwa Kamila siku hiyo. Wawili hao baada ya penzi zito la mpatano, walijua ibadani wameshachelewa. Wakaoga na kuelekea hotelini ili kukutana na familia huko wakitoka ibadani.

Wakaenda kwenye hoteli ileile iliyokuwa imeacha historia mbaya kwa Colins. Love na Kemi wakiwa wamegongelea msumari wa mwisho wa mapenzi kwa Jelini.

Walishaweka reservation kwa familia nzima. Kwa hiyo wakaenda sehemu na kwenye meza waliyokuwa wameandaliwa. Wakakaa hapo na kuagiza vivywaji wakisubiria waliofanikiwa kwenda kanisani wafike hapo wajumuike nao.

Kukawa na hali ya utulivu iliyomuhakikishia Colins hata kama angeomba ndoa, angekubaliwa tu. Kamila alikuwa ametulia, anaonekana anafuraha. Na mchezo aliotoka kupewa, alikuwa mwepesiii.

 Alipopata ujumbe kutoka kwa Connie kwamba wamefika akamwambia wakatembee kidogo baharini. “Bwana Colins! Mwenzio nimevaa kiatu cha juu, siwezi tembea mchangani!” “Vua mimi nitakusafisha miguu tukirudi.” Akacheka mwenyewe kwa deko! Akavua viatu ndipo wakatoka hapo kuelekea ufukweni.

Sasa kadiri walivyokuwa wakitembea, akagundua Colins anapunguza maneno. Na yeye akatulia wakawa wanatembea kimya kimya. Mbele akaona kitu kilichomvutia macho.

“Ona Colins! Pale pamepambwa vizuri mpaka nataka tujiibe tukapige picha!” Colins akacheka sana kwa furaha akijua aliyemlipa atengeneze hivyo, ametimiza lengo. Mlengwa amefurahia.

“Twende.” “Ndio umepapenda kiasi hicho!?” “Sasa wewe huoni jinsi kulivyotengenezwa kwa unadhifu! Tena hakuna mtu. Twende tujiibe tukapige picha.” “Unauhakika? Tusije..” “Acha woga bwana! Twende.” “Sawa! Tukikimbizwa ujue umejitakia.” Kamila akaanza kucheka mbavu hana, ila akawa amekusudia kwenda.

Wakasogea mpaka pale. Ndipo akagundua lile shada kubwa sana lililotengenezwa kwa maua meupe kwa muundo wa moyo, katikati kuna maneno. Ushabiki, akasogelea karibu asome. ‘Will you Marry me, Kamila?’ Kamila alishituka sana na kumgeukia Colins, akakuta amepiga goti.

“Colins!?” Akamsogelea pale alipopiga goti. “Namaanisha nikikwambia siwezi tena kuishi bila wewe Kamila. Na kama sijakwambia vyakutosha, amini nakupenda. Nakupenda Kamila, na nakuhitaji.” “Lakini hujanijibu, Colins! Iweje Jelini aje arudi na sisi tumeshafika mbali! Sio sawa.” “Nimefunga milango yote yakutoka na kuingia kwa yeyote yule.” “Hata Jelini!?” “Hata Jelini. Na jana nilikutambulisha kwake ramsi. Anakufahamu na ametutakia kila la kheri. Ameniambia nakustahili. Sasahivi ni mimi na wewe, tutengeneze chetu.” Kamila alifuhi huyo!

“Kwa hiyo ndio umekubali?” “Nimefurahi! Nimefurahi sana.” Colins akaanza kucheka. “Sema sasa ‘ndiyo!’ ndio uendelee kufurahia.” “Mwenzio nakupenda Colins. Na nilikuwa natamani tubaki sisi tu. Sasa ulivyoshindwa kunijibu juu ya Jelini, nikaingiwa na wasiwasi. Nikajua tupo pamoja kwa muda, pengine ni mpaka Jelini aolewe ndio uhakika wangu kwako. Halafu ulipomfuata jana usiku ndio nikakata tamaa kabisa. Nikajua mimi tena basi!”

“Na ndio maana nimeamua kufanya sasahivi kukuhakikishia kama ninakupenda wewe, na nimekuchagua wewe hata kama bado Jelini hajaolewa. Nakuhakikishia sasahivi ni mimi na wewe tu. Na kukubali kwako ndio kunisaidia kufunga milango yote hata ya mimi kufikiria mwingine. Ndio nitakuwa nimejifunga kwako tu.” Akazidi kufurahi huyo Kamila, haamini.

“Goti limechoka Kamila! Si ukubali uvae pete, mengine baadaye.” Akaanza kucheka, mbavu hana mwenzie amebakia gotini.

“Anakukomoa?” Wakamsikia Mill. Kamila hakuamini. Akazidi kuruka ruka alipoona wanamsogelea. “Leo kaka utakoma!” James naye akaongeza. “Na kwambia na kesi zangu zote zinaendeshwa hapahapa, hivihivi!” Wote wakazidi kucheka. Kamila anafurahia.

“Sasa Kamila mwanangu, hiyo furaha ungeendelea ukiwa na pete mkononi.” Ndio akarudi kwa Colins. “Nimefurahi Colins! Kwa hiyo utanioa kabisa ile ya kanisani!?” Watu wote wakazidi kucheka.

“Leo mzee siku yako mchangani.” James akazidi kuwachekesha. “Nivalishe halafu unijibu! Nimechanganyikiwa! Sikuwa nimetegemea kabisa! Nimefurahi sana.” Ungeweza ona furaha ya Kamila waziwazi. Hakujificha kama anapenda ndoa.

Hatimaye Colins akamvalisha, wakaanza kupiga makofi na kushangilia. Colins akasimama na kupata kiss, ila Kamila akalifanya fupi na kumnong’oneza. “Sasa hapa na baba yupo!” Colins akashangaa sana. “Kamila!?” “Kweli tena. Mimi naona aibu. Siwezi tena.” Wakawapongeza hapo na picha kuendelea.

~~~~~~~~~~~~~~

Na hivi mzee ndio alikuwa kijana wake wa pekee anaoa, akataka kumbukumbu ya kueleweka. Kulikuwa na mchukua video na picha pia. Aliyewaandalia hapo kwa kupapamba baada ya kuona wanamalizia kufurahia akasogea hapo. Wakamshukuru kwa kazi nzuri. “Naona Kamila mwenyewe amepafurahia sana. Nashukuru.” “Nilikwambia kazi zangu sibabaishi.” “Nashukuru.”

Ndipo wakaondoka eneo la baharini na kurudi kwenye sehemu waliyokuwa wameandaliwa meza chache zilizounganishwa pamoja kwa ajili ya mlo rasmi wa pamoja. Full course meal, ndiyo waliyo kuwa wakihudumiwa siku hiyo. Maalumu kwa ajili ya kuchumbia kwa Colins. Wakala siku hiyo kama tafrija kabisa.

Walikuwa na wakati mzuri sana! Walikuwa watu wa karibu tu na Colins, Mill na watoto wake. Wazazi na Connie akiwa na yeye na mchumba wake, japo bado hawakuwa wamevishana pete, ila alifahamika mpaka nyumbani. Na huyo James ambaye bado alikuwa haamini kama Colins anachumbia mtu mwingine na si Jelini! Ila akakubali Colins amepata msichana mzuri.

Yeye alikuwa peke yake. Alitokea kanisani akamuacha Jema akienda kwao na mtoto pamoja na msichana wa kazi, yeye ndio akakimbilia huko kwenye shuguli. Kisha akawepo Colins mwenyewe na Kamila. Ungejua yapo mapenzi kati yao. Kila wakati kuangaliana, na kupeana kiss fupi.

“Nimependa pete yangu! Nzuri sana. Asante.” Akamwambia Colins. “Na imekupendeza sana. Una vidole vizuri sana Kamila.” “Asante! Ila bado siamini kama na mimi nitaingia kanisani kuolewa! Nilikuwa natamani! Nimefurahi sana.” Akaendelea kufurahia.

~~~~~~~~~~~~~~

Karibu na mwishoni, akahamisha kiti karibu na baba Colins. “Nimefurahi baba! Nimefurahi sana.” “Hongera Kamila binti yangu.” “Wewe ndio nikushukuru zaidi. Mimi sikuwa hata najua kama nitakuja kuolewa! Ila wewe baba yangu, umehakikisha na mimi naolewa. Asante sana.” “Unastahili Kamila binti yangu. Ni haki yako na hilo nitalisimamia mpaka kanisani.” Alijawa furaha huyo! Cheko muda wote.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Sasa, na mimi zamu yangu watu wanilipe pesa yangu yote niliyokuwa nikiwachangia kwenye shuguli zao. Jumamosi ijayo, kikao cha kwanza. Zege hailali.” Baba Colins akasikika akiwa amehamasika haswa. “Hutaki mchezo mzee wangu!” “Kabisa. Nimekua na kazi ya kuozesha watoto wa watu, kwangu kulikuwa kimyaa! Kama sikujaliwa watoto wakati Mungu alinipa watoto wazuri kama mke wangu!” Watu wakazidi kucheka. Ila kikawa kipindi kizuri haswa.

~~~~~~~~~~~~~~

“Jamani, naomba ni propose a toast to James and Jema. Wamebarikiwa mtoto wa pili. Jema ni mjamzito.” James hakuamini. “Kwamba wewe jana ulinisikia ila ukanipuuza!?” “Unaharibu James.” James akatingisha kichwa akiwa haamini. “To James, Jema and family.” Wote wakanyanyua glasi juu na kugonga kwa pamoja wakirudia, “To James, Jema and Family.” Wakanywa kwa pamoja na kumpongeza huyo James. Na kuendelea kufurahia baraka juu ya baraka.

~~~~~~~~~~~~~~

Wakati wao wanasherehekea, kina Simba wapo msibani. Ni kama wao walipoteza mtoto mmoja rasmi. Love hatakaa akatoka jela. Shitaka la mauaji lilikuwa likimuhusu. Ulikuwa wakati wa kuvuna walichopanda kwa shangwe na wivu.

Kasa alijiweka pembeni kabisa kwenye shitaka la Kemi. “Nilishamuonya, tena kwa kurudiarudia. Aachane na Jelini, aangalie maisha yake, lakini hakunisikiliza. Akahangaika na Jelini kama amepagawa. Akahakikisha amemtoa kwenye maisha yangu kabisa. Napo pia hakutulia akaendelea kumfuatilia mtu asiye muhusu.”

“Sasa wote tumeishia kupoteza kwa namna moja au nyingine. Amenipokonya mapenzi ya kweli, yeye mwenyewe amepoteza uhuru wake, wanae watakua bila mama, bila familia nzuri kama mwanzo. Maana mumewe hataki hata kumsikia, na anaoa siku za karibuni. Wote tutajifunza kuishi na matokeo ya mapando ya Kemi.” Kasa alikuwa akimwambia kila aliyekuwa akimuuliza wakitaka kujua atamsaidiaje Kemi.

~~~~~~~~~~~~~~

Mama yake alipotaka kuingilia, Kelvin akamuonya. “Jihusishe kwa mbali sana mama. Hapa nchini utapaona pachungu na huko pia unaweza ukashindwa kuishi. Hii kesi inaangaliwa na macho makali yaliyokusudia kumuona Kemi analipa uovu wake aliorudia tena na tena kuutenda.”

“Na Kemi nilimuonya kama hivi ninavyozungumza na wewe. Tena kwa kurudiarudia, asijiingize kwenye vita ambayo nilimuhakikishia kabisa, hataweza kushinda. Hakunisikiliza mpaka alipojibana mwenyewe na hakuna jinsi ya kujitoa. Sasa na wewe nakuonya mama.”

“Watanifanya nini!?” Akauliza kwa jeuri. “Nashauri uache sasahivi, kabla hujapata majibu ya maswali yako, ukiwa majutoni, ambako hutaweza kujitoa tena. Kwa sababu nakuhakikishia mama, utajuta na hutatoka. Jiweke pembeni kama baba. Muombee Kemi, kama ni muujiza, basi Mungu mwenyewe atende. Ni hilo tu mama yangu. Lasivyo, chochote kibaya ulichowahi kukitenda sirini hapa duniani, utashangaa kinachimbuliwa na kuja kuwekwa mwanangi kama alivyofanyiwa Kemi. Hakuna nchi itampokea tena Kemi. Ubaya wake wote upo kwenye kila ulinzi wa kila nchi hapa duniani. Sasa na wewe usijiingize.” Kelvin akamuonya.

~~~~~~~~~~~~~~

Colins amefanikiwa kushinda nafsi na kusimamia msimamo wake, amejifunga kwa Kamila.

Kwa Jelini nako Je?

Usipitwe…

x

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment