![]() |
“Unauhakika!?” “Acha nikwambie ukweli Junior. Jinsi
ninavyokuwa na Jelini, hutahisi hata kama anamjua Colins. Hutamsikia hata
akiropoka juu yake. Sijawahi kuta jumbe zake tena. Na nimeshakwambia
Jelini hajui kuficha simu zake. Namba zake za siri zote ninazo. Akibadili ananiambia
bila shida, na hajawahi kunizuia simu zake hata mara moja.”
“Nina uhuru na simu zake kama zangu. Sijawahi kuta jumbe
yeyote ya ajabu yakumtilia mashaka. Zaidi ya ile simu yake ya biashara ndio
utakuta kuna wanao mtongoza tu. Lakini hajawahi nitia wasiwasi wa
kumshuku. Nafikiri ndio maana jana nilipaniki. Sikutegemea. Nilijua
mambo ya Colins yaliisha kabisa.”
“Kwa hiyo kwa kujibu swali lako, nina uhakika. Jelini kama
Jelini kwangu ni kweli ananipenda na kuniheshimu sana. Hatuna shida,
na wala huyo Colins hajamfanya kwangu akawa tishio. Wakati wote tukiwa
pamoja, tunakuwa na wakati mzuri. Sijawahi kuwa na aina ya utulivu
pamoja na furaha maishani kama ninapokuwa na Jelini. Aisee nampenda
Jelini.”
“Na acha nikwambie ukweli mwingine. Tulikuwa tukitizamia
fungate yetu kwa hamu sana. SANA. Wote tulikuwa tukiutizamia muda
wetu tutakaoupata wa faragha wa pamoja. Usiku wa kutoagana. Kuamka
pembeni ya kila mmoja wetu.”
“Sijui kama nitakuja shika mwanamke tena, nikaridhika
kama nilivyomshika Jelini, Junior. Anautulivu fulani hivi mkononi! Acha kaka.
Nitachanganyikiwa nisipomuoa Jelini, jumamosi. Siwezi kuja anza na mwanamke
mwingine. Hatakua Jelini, hataweza kuwa Jelini.” “Basi tuombe
kisha tuanze kumsaka. Usiku huuhuu mpaka kieleweke. Tujue moja.” Wawili hao
wakaanza kuomba. Safari hii hata Erza mwenyewe aliweza kuomba. Wakamuombea
ulinzi huko alipo na mtoto, kisha amani.
“Tutampatia wapi na simu zote kafunga?” “James anaweza
tusaidia. Tumpigie yeye tumuombe atusaidie kuangalia kwenye hiyo mitandao yao,
atusaidie kujua alipo.” Wazo la Junior likawa sahihi, wakampigia James.
Kwa James.
“Kwanza
niombe msamaha kwa nililoanzisha. Sikukusudia kuleta vurugu ya namna hii.”
“Hapana James. Sio kosa lako. Mimi ndio nimekosea. Lakini naomba msaada wako.
Kujua alipo ili nikazungumze naye. Usiku huu usipite hivihivi sijazungumza
naye.” “Tumetoka sasahivi kuzungumza na mama. Anawasiwasi sana juu ya Jelini
kuondoka na mtoto. Lakini tumemtuliza, nashauri na wewe mpe muda, atarudi
tu. Hawezi kukaa muda mrefu na mtoto
wa bibi.”
“Siwezi
nikamuacha aendelee kuwa kwenye hali hiyo, James! Tafadhali nisaidie.” Akamsikia kama anacheka kwa masikitiko. “Acha
nikwambie ukweli. Hilo unaloniomba, nimeshalifanya. Nimekata tu simu ya mama,
nikaamua kujua alipo ili angalau kupunguza wasiwasi. Lakini nimekuta restriction
hizo!” “Unamaanisha nini? Mbona kama kuna jambo unashindwa kuniambia?”
Akatulia kidogo kama anayefikiria jinsi ya kuzungumza. “Nisaidie
James ndugu yangu.” “Sitaki kuharibu zaidi.” “Si kwangu. Nimejifunza kutokana
na makosa. Na naahidi mimi mwenyewe nitatafuta nafasi yangu ndani ya
moyo wa Jelini, hata kama kumejaa Colins. Naahidi nitatafuta bila kumuumiza.”
“Na hicho
ndicho pia nilitaka kukwambia Ezra. Colins na Jelini ni penzi ambalo walikuwa wakilitizamia
kwa muda mrefu sana, wakiamini wao wawili wakifanikiwa kuja kuwa pamoja, furaha
yao itakamilika. Walishapanga mpaka watoto watakao kuja zaa pamoja. Na
Colins ndio mwanaume wa kwanza kufanikiwa kuingia moyoni kwa Jelini. Ni
nini nataka kusema?”
“Baada ya
Colins, au katikati yao alishapita Kasa. Nafikiri unamfahamu.” “Namkumbuka.”
“Basi Kasa ni ndoto ya mwanamke yeyote atakayefanikiwa kumpata na Kasa akimpenda.
Na alimpenda Jelini karibia kurukwa na akili. Kwanza tunahisi alirukwa
na akili kwa ajili ya Jelini. Hata angemuomba damu yake, nahisi kwa Jelini
angempa bila maswali.”
“Lakini katika
yote, Colins hakuwahi toka moyoni kwa Jelini. Na haikuwa siri. Kasa alipolijua hilo,
kuwa japokuwa Jelini anakila kitu, na angempa chochote anachotaka, maana
Kasa anapesa chafu isiyo na matumizi. Mimi mchaga nikikwambia anayo pesa,
niamini anayo pesa, maana anamiliki mpaka migodi.” “Kweli anayo pesa.” Mpaka Junior akaafiki.
“Ewaaah!
Hapo unapoishia kuelewa, ndio anzia pesa ya Kasa. Akajaribu kuwa akimpa mahela
Jelini ili kujishindia moyo wake. Lakini akaja kugundua moyo wa Jelini
haufurahishwi na pesa ila kumjali. Basi yule mzee alibadili maisha yake
kiasi cha kukera familia yake na watu wake wa karibu. Maana ana vijana
wakubwa tu. Lakini yote hayo ilikuwa kwa ajili ya Jelini.”
“Ninachotaka
kusema ni, yeye aligundua siri na kujibadilisha yeye. Akatafuta nafasi
yake katikati ya hao wawili, akafanikiwa kumtuliza Jelini japo Colins
hakuwa mbali.” “Unamaanisha nini?” Ezra
akauliza.
“Huna
utakapomuweka Jelini, macho ya Colins yasimuone. Walisumbuana na
Kasa mpaka kutishiana risasi kwa ajili ya Jelini, lakini Jelini ni mtu
wa maneno yake. Japokuwa anampenda sana Colins, ila kwa kuwa alikuwa na Kasa,
hakuwahi kumsaliti. Ndivyo alivyo na wote hao wanamjua. Si mtu
wakujipinga, na si mtu wa kuwa na wanaume wawili.”
“Colins
hajawahi kumtoka moyoni, na kwa jinsi ilivyo mpaka sasa inamaana Jelini
hajatoka moyoni kwake pia japo anataka kuchumbia mwanamke mwingine.”
“Unamaanisha nini?!” James akatulia.
“James?!” “Sitaki
kutibua hii hali Ezra. Nashauri uache, Jelini atarudi tu, mtazungumza.”
“Nakuahidi sitarudia nilichofanya. Tafadhali nisaidie tu kwa namna
yeyote ile.” “Kwa kifupi, hakuna anayeweza kujua Jelini alipo, isipokuwa
Colins tu.” “Kwamba hata ukiingia kwenye mitandao yenu hiyo huwezi?!”
“Nilishafanya hivyo ndio maana nilicheka mwanzo.”
“Nilipovuta
namba zote za Jelini, au chochote kinachomuhusu alipo, nimekuta
kumewekwa security restrictions hizo! Sikuamini. Nikatafuta
kichwa kingine, ninachokiamini cha mambo ya cyber security. Bila
ya kumwambia ni namba za nani na wapi nimekwama, yeye mwenyewe
moja kwa moja akaniambi ni kichwa kimoja tu, anachojua kinaweza
kufungua zile restrictions. Guru.”
“Guru?!” Wote wakajikuta wanauliza kwa pamoja. “Jina
analojulikana nalo Colins huko kwenye ulimwengu wetu. Anapofika kwenye hizo
anga, hanaga mpinzani. Alijaliwa kipaji cha ajabu sana. Pale tulipokuwa
tukifanya naye kazi, kila mtu. Nikimaanisha wote, wazawa na wageni
waliokuwa wakija pale kwenye ile kampuni, walikuwa wakisalimu amri kwake,
na kubakia kumuita ni mungu wa mitandao. Kwamba anaweza amuru chochote
kitokee kwenye kompyuta kikatokea.”
“Kwanza
huyo jamaa mwenyewe alipofungua tu namba ya Jelini, akitaka kujua alipo, huo
ukinzani wake tu, alishituka sana mpaka akaniuliza, ni namba za raisi wa
wapi, nisije mtia matatizoni.” “Kwa jinsi zilivyo fungwa?!” Junior akauliza. “Ewaaah! Naona sasa
mnanielewa. Na najua amefanya makusudi.”
“Naona
kabla ya kuuliza kwa nini, naomba kupata ushauri wako, jinsi yakufanya kuanzia
hapa.” “Hakuna jinsi. Ni aidha msubiri Jelini mpaka arudi mwenyewe, kitu
ambacho mimi nashauri hivyo ili kuyafanya haya mambo yasiende mbali.”
“Chaguzi ya pili ambayo unasita kusema ni kumtafuta Colins?” Esra akauliza.
“Ewaah!
Ambapo, kwa jinsi ninavyokijua kichwa cha Colins, huwezi kumuamsha
sasahivi na kumwambia nifungulie access za Jelini, akafungua.
Hata iweje hatafanya hivyo kwa sababu amefunga kwa makusudi. Inamaana
atataka kujua ni kwa nini tunataka kujua Jelini alipo, tena usiku huu! Na
huna jinsi ya kumdanganya Colins. Lazima ajue ukweli wote.”
“Na akijua
ukweli, ndio atasumbua sana, akiona kila mtu hamjali Jelini. Atajihusisha
na hilo jambo, mpaka atawakera! Kasa anamjua, Jema na mama yake pia wanamjua.
Na huna jinsi yakumkataza akakubali. Walikuwa wakitishana na Kasa
mchana na usiku mpaka kwa risasi.”
“Nikuulize
kitu James?” “Karibu Junior.” “Kwa jinsi unavyowajua, na kwa hali ilivyo,
unafikiri Jelini hatamtafuta Colins kweli?” “Hathubutu hata iweje. Ndio mwiko
wake na wote wanamjua. Huko ameenda kutulia tu, atarudi. Kichwa cha
Jelini hakitaki kupata moto. Kikishapata moto tu, lazima akakitulize. Hatakagi
kelele kichwani mwake ndio maana hajui kugomba na hataki kumuudhi
mtu. Akitulia, atarudi tu. Msiwe na wasiwasi.”
“Hakika nina wasiwasi James. Lazima nimpate Jelini
usiku huu.” “Basi jua lazima, namaanisha ni LAZIMA Colins ahusishwe. Sasa
mimi na wewe hapa tulipo, hatujui kichwa chake kilipo usiku huu, vile atakavyoamua
sasahivi baada ya kusikia haya.”
“Kama kwa
hakika yeye ndio mtu wa mwisho kunisaidia,” “Kama atakusaidia.” Akamkatisha kwa haraka. “Unamaanisha nini tena!?”
“Kwa jinsi ninavyowajua hawa wawili, na Colins anapokuwa
linapokuja swala la Jelini, kwanza hashauriki, pili akijua ukweli,
wewe utakuwa mtu wa mwisho kabisa kutaka hata kusikia jina lako, labda baadaye
Jelini aje akuzungumze vizuri.”
“Kasa
amegeuka kuwa adui yake, hataki hata kumuhisi. Na wangefika mbali sana,
ila Kasa alisaidwa na kijana wake ambaye tulifanya kazi pamoja na Colins. Kwa
hiyo anamfahamu Colins na kile anachoweza fanya. Anasema ilibidi azungumze
na baba yake kwa kituoa maana Kasa ni mkorofi. Mkorofi haswa na
mbishi. Akamuonya kuwa pale alipoharibu kwa Jelini, iwe hivyohivyo,
akiongeza kingine, hamtaki Colins amfuatilie nyuma. Maana atamlipa
kisasi vibaya sana. Na hataweza kumkamata.”
“Sasa
nahisi kuanzia hapo, ndipo alipomficha Jelini mtandaoni. Kwamba japokuwa Kasa
anayo pesa, hata akimtafuta mtu wa namna gani, hawezi kujua Jelini alipo, labda
Jelini mwenyewe amwambie. Lakini si vinginevyo. Mimi nahisi
hivyo. Kama ana sababu ingine, hatasema. Kwa hiyo kwa kifupi, ni kwamba…”
“Kama tunamtaka Jelini usiku huu, ni kumtumia Colins.” “Ewaa! Napo,
narudia tena, inategemeana na Colins. Anaweza asiwe msaada kwetu ila kwa
Jelini.”
“Kwamba
atamtafuta yeye mwenyewe!?” “Hiyo ni LAZIMA. Atamtafuta yeye mwenyewe mpaka
ampate ndipo ataamua kama atujulishe amempata au la. Zaidi wewe
Ezra. Inamaana itategemeana na atakachosikia kutoka kwa Jelini
juu yako. Uwamuzi ni wako. Mama yake nimezungumza naye naona ameridhia
kumuacha mpaka arudi, japo sijamwambia hayo niliyowaambia nyinyi juu ya Colins
na mengineyo.” Kimya, Ezra akifikiria. Junior naye kimya
akimpa nafasi yakufikiria.
James naye kimya. “Sitajisamehe endapo chochote
kibaya kitampata Jelini nikiwa mimi ndio nimesababisha. Acha tu amtafute.
Hata kama ni yeye, amtafute tu ampate na ahakikishe yupo salama. Hilo ndilo
la muhimu. Mengine tutajua mbele ya safari.” “Sawa. Ila nashauri kama mpo
barabarani. Mrudi tu nyumbani, sehemu mtakayo pumzika. Colins hatabiriki.
Anaweza akanibadilikia mimi mwenyewe, usiku huu, na mimi nikawa ni adui
asiyetaka kunisikia mpaka atakapompata Jelini.” “Sawa James. Wewe tujulishe
itakavyokwenda.” “Sawa.” Ndipo wakaagana.
Kwa Colins.
James akaitizama ile simu akifikiria mazungumzo yake na
Colins jinsi yanavyoweza kuisha vibaya, bila kupata jinsi ya kuzungumza
naye akamuelewa. Mwishoe akaona anazidi kupoteza muda, akampigia.
Ikaita mara kadhaa ila akapokea akisikika alikuwa
usingizini. “Kwema James?!” “Samahani kukuamsha. Nilitaka msaada wako.” “Karibu.”
Akaanza kwa ustaarabu kweli ila James akijua baada
ya hapo, haitakuwa shwari tena.
“Tunaomba
msaada wako kujua Jelini alipo.” Pakazuka
ukimya wa muda mfupi, kumbe anaangalia saa. “Kwamba wewe na hao
mnaotaka kujua Jelini alipo, mpaka sasa, usiku mwingi hivi, kati
yenu hakuna anayejua Jelini alipo!?” “Acha kupaniki Colins ni…” “Unazungumza
nini James wewe?! Unajua sasahivi ni saa ngapi? Yaani mpaka sasahivi nyinyi watu
wazima na akili zenu, hamjui Jelini, mtu rahisi hivyo, alipo!?”
“Si ndio
anaendelea kutafutwa! Naom…” “Subiri kwanza. Ni nani ambaye anamtafuta? Kwamba hata
huyo mchumba wake hajui alipo?” “Hajui.” “Kwa nini?!” “Colins. Wewe usitake
kufanya haya mambo kuwa makubwa.” “Kwamba mpaka sasa wewe huoni kama haya mambo
ni makubwa!? Angekuwa haonekaniki Jema, bado ungetulia kama
hivyo!?” Akambadilikia.
“Nakuuliza
James? Unaniambia nisiyafanye mambo kuwa makubwa, wewe huoni kama tayari haya
mambo ni makubwa sana!?” “Nafikiri nimekosea tu kuzungumza.” “Huko ni kutokujali.
Na sikutegemea kwa mtu kama wewe unaweza fanya hivyo! Unaaminiwa na
familia ya mama Jema. Halafu unashindwa kutimiza majukumu madogo tu! Na hapo
una mtoto mmoja tu!” “Jema ni mjamzito.” “Acha kunichanganya zaidi James.”
“Umekasirika
Colins. Utashindwa kumpata Jelini.” “Sio mimi. Hapa namfuata.”
“Tafadhali Colins, naomba nijulishe.” “Unanitania wewe James!?” “Nimekuomba
Colins?” “Yaani yeye na akili zake awafungie nyinyi simu, halafu mimi nivunje uwaminifu
wake kwangu?! Kwa nini nifanye hivyo?” “Ili kutengeneza.” James akasikia gari linafunguliwa. Kwamba ameshajua
alipo, na kweli anamfuata.
“Nisikilize
Colins. Huyo Jelini anatafutwa na mchumba wake, hapa tunapozungumza anasubiria
jibu.” “Kwa nini yeye asijue Jelini alipo kama kweli ni mwanaume anayejua kuwajibika?”
“Kulitokea kutoelewana ndio Jelini akaondoka.” “Acha kunipotezea muda
kwa habari nusunusu James. Wewe unanijua. Mimi si mjinga. Kama unataka niendelee
kukusikiliza, zungumza kitu kinachoeleweka au na mimi nakufungua simu,
nitaenda kujua ukweli kutoka kwa Jelini mwenyewe. Usizidi kuniudhi!”
“Wewe
nilikuomba rasmi kumlinda Jelini. Nikiwa nakuamini. Leo anapotea,
unanyamaza mpaka usiku huu ndio unanitafuta!” “Jana uliponipigia
ukiniambia umepata mchumba, unachumbia, Jelini alikuwepo akasikia
na kushituka kiasi ya kwamba kila mtu akajua. Tulikuwa nyumbani kwa
wakwe zake na mchumba wake alikuwepo.” Hapo
Colins akapoa.
“Jelini
amechumbiwa na mwanadamu Colins. Kama mimi na wewe, lazima kupatwa wivu.
Wakatoka nje kuzungumza juu ya hilo, nafikiri kuna maneno yalizungumzwa…” “Tafadhali
James.” Akawa akama anamuonya, James akaelewa.
“Basi
niseme kuna maneno alizungumza huyo mchumba wake ndio yakamtibua Jelini.
Na kabla hujataka kujua ni maneno gani, mimi sijui alichozungumza mpaka kumtibua
Jelini.” Kimya. “Colins?” “Nitakutafuta
baadaye.” “Kwa nini usiniambie alipo ili…” Simu
ikakatwa. Na hakumpata tena. Alitegemea.
~~~~~~~~~~~~~~~
Haya Tena, Wakiwa Wameshapata Wachumba Wakueleweka, Na Siku Chache Zimebakia Aolewe,
Jelini Na Colins Maisha Yawapa Faragha Nyingine Tena.
Nini Kitaendelea Kwa Wawili Hao Huko Hotelini!
Usipitwe….
![]() |
0 Comments:
Post a Comment