![]() |
Aliporidhia kuwa huo ndio muda muafaka, pengine
wamesharudi nyumbani, akampigia. Simu ikawa inaita, hamna majibu. Wawili hao
walishazoeshana kupigiana simu wakiwa kitandani wakilala. Kwamba sauti zao ndio
za mwisho masikioni mwao kwa siku. Ila usiku huo hata hakutakiwa usiku
mwema!
Usingizi ukampaa. Akabakiwa na kazi ya kupiga
simu, kumbe mwenzie simu kaacha kwenye pochi, kalala, hana habari na
kinachoendelea huku duniani.
~~~~~~~~~~~~~~~
Asubuhi akaamka. Akaona hizo missed call zaidi ya 20.
Akafyoza. “Yeye si hataki kubabaishwa? Sasa asubiri. Mimi sitingishi
kiberiti. Changu kimejaa. Sina shida.” Akaazimia Jelini. “Kwani lazima
ndoa! Ebo! Mtu asinichanganye mimi.” Akazidi kujipandisha mukari akisahau
mipango yote ya ndoa.
Ni Ezra huyohuyo alimshawishi aache ubahili, aajiri
vijana wakutosha kwamba siku za jumamosi awe na msaada wa kutosha. Kwa hiyo
hapo alikuwa na kazi ndogo tu, anamaliza siku nzito ya kazi kirahisi, na pesa
nzuri bado inaingia.
Akawahi kutoka kabla ya muda wake. Akaenda kufanya
shuguli zake, mapema sana akamaliza. Akarudi nyumbani. Akaoga na kufungasha
mizigo yake na mwanae. Akamchukua Jeremy akimwambia wanakwenda kupumzika sehemu
nzuri. Jeremy akafurahi huyo!
Akampigia simu mama yake kumtaarifu. “Jelini!
Jelini wewe! Hizo hasira zitakupeleka sipo!” “Acha niende nazo kokote zitakaponipeleka.
Maisha ni yangu. Nikijuta ni mimi mwenyewe nitajuta. Haimuhusu
mtu.” “Sawa. Ila ninachokuomba ni uwe mwangalifu mama mzazi. Rudi ukiwa mzima.
Utaniua mama yako endapo chochote kitatokea. Umesikia mama?” Akanyamaza. Kisha akaongeza.
“Nimeondoka
na Jeremy.” Hapo akamvuruga mama yake. “Unarudi
lini?” “Sitaki kuulizwa.” “Hakika utanijibu Jelini. Bora ungeondoka peke yako
na si na Jeremy. Huyo mtoto siku ya jumatatu anatakiwa shule. Umenisikia
Jelini? Hapo sitaki unitanie.” “Kwani nimekwambia sirudi?” “Lini?” “Nimesema
nitarudi, na Jeremy ataenda shule.” “Nasisitiza kuwa jumatatu, asubuhi, huyo
mtoto awe amekaa darasani kwake. Usinitanie.” Hakumjibu.
“Tena awe
amekaa darasani akiwa hana usingizi, yupo tayari kujifunza. Unanisikia
Jelini.” Akaona simu imekatwa. Hapo akamchanganya mama
Jema. Akampigia mara ya kwanza, hajapokea. Akarudia tena. Akajua amepaniki,
akapokea. “Jeremy atarudi.” “Jelini nakuonya wewe mtoto!” “Sasa mimi
nimefanyaje?!” “Nilikwambia nini juu ya maisha yako na wanaume zako?” Kimya.
“Sikukuonya
na kukusisitiza mambo yako na wanaume zako havimuhusu Jeremy?” “Mimi
nimetoka na mwanangu. Sasa kosa lipo wapi?” “Toka naye kwa utaratibu unao
eleweka. Sio kwa sababu wewe umechanganywa, ndio umchanganye na
Jeremy. Sitakuruhusu Jelini.” “Mimi simchanganyi mwanangu.
Nimemchukua kwenda kupumzika naye tu.”
“Sasa,
hakikisha kwenye hayo mapumziko hutii pombe hata tone kinywani mwako.” “Mimi
nimeacha pombe.” “Nakuonya Jelini wewe! Maana mimi na wewe tunafahamiana. Usije
kukutana na kina Doro wengine, ukanywa. Ukajisahau, ukamuacha Jeremy huko nisikokujua
mimi, halafu hana ulinzi, wewe hujitambui.” Mama
Jema akaendelea kukazia hukumu.
“Usiku wa
leo, anipigie simu, nihakikishe yupo mzima na yupo kitandani kwake.” “Mimi sitaki
kuingiliwa.” “Basi mrudishe nyumbani. Lasivyo, nitakusaka hapa mjini
hata na jeshi la polisi, mpaka nikupate, nimchukue Jeremy. Sasa usinijaribu,
maana unanijua.” Na kweli alimjua mama yake. Kwa Jeremy huwa
hazembei.
“Sinywi
pombe na Jeremy atakupigia wakati analala. Sitaki fujo, nataka kupumzika.” “Na
jumatatu, kipindi cha kwanza, kimkute amekaa kwenye dawati lake. Ameshiba, na
hana usingizi. Umenielewa Jelini?” Kimya.
“Jelini?” “Mimi
nilitaka kukaa mpaka jumanne.” “Sio na Jeremy. Mwache nyumbani, wewe nenda
kokote unakotaka. Kwa muda wowote utakao. Akifunga shule, wewe mchukue,
sitakuwa na neno endapo utakuwa ukitimiza masharti yangu huko ulipo. Lakini
huyo mtoto hatakosa shule si kwa starehe zako, wala si kwa hasira
zako. Usitake kunichanganya. Au lasivyo, nafunga biashara zote sasahivi,
naanza kukusaka mpaka nikupate.”
“Huyo
Jeremy atakupigia simu usiku, na jumatatu atakuwa shule.” “Na usinywe pombe.”
“Nishasema sinywi pombe.” “Na hilo ulikumbuke. Sasa nisimsikie Jeremy mida yake
ya kulala.” “Hata lala saa mbili mama, kama siku za shule. Leo nataka kukaa
naye muda mrefu.” “Basi nisilale bila kumsikia.” “Mnanifanya mimi mjinga. Sina
akili.” Akaanza.
Akalalamika hapo akilia, analaumu hili na lile, hamalizi.
“Sasa unaendeshaje na hicho kilio Jelini, kama si kunitafutia balaa
mimi! Ukipata ajali?” Akaendelea kulia. “Wewe nenda kapate muda wa kutulia na
mtoto. Usinywe pombe, hata kwa kushawishika. Jeremy anipigie simu. Jumatatu
awepo shule. Hapo hatutakosana? Kwanza mimi na wewe huwa hatukosani.” Akampamba
hapo huku akimbembeleza mpaka akatulia. Kama kawaida yake kupenda kubembelezwa
ndio udhaifu wake na mama yake alimjulia. Akatulia kabisa ndio
wakaagana.
Bora Aibu Kuliko Fedheha!
Alipoona Ezra anaendelea kupiga. Akamtumia ujumbe. ‘Nimesafiri.
Sipo mjini.’ Akautuma huo ujumbe na kuzima simu kabisa.
Jelini pesa anayo, kazi ni matumizi. Alikuwa aende
Zanzibar, lakini alipoona mama yake anamkazania Jeremy, akaamua kwenda Bagamoyo.
Akatafuta hoteli nzuri ufukweni, starehe yeye na mwanae zikaanza.
Wamekutana wapenda kuongea. Maneno mengi! Stori haziishi. Kucheka kwa
kila jambo na wote wapenda kula.
Kula, kuogelea na kucheka wakati wote.
Wamependeza, ukimuona Jelini utasema nili milionea fulani hivi. Akawa
amejiwakilisha kwa vazi la ufukweni, mahiri sana. Nadhifu. Na vile
alivyopendelewa umbile, kila mtu alikuwa akimwangalia yeye na mwanae. Asijue
hali ya Ezra huko alipomuacha.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akahangaika wee, Jelini hapatikaniki kwa simu. Safari za
nyumbani kwa mama Jema zikaanza. Kila akienda, geti limefungwa. Akawa
anahofia kumfuata kazini, au kumpigia simu. Mama Jema mtu wa kazi, siku ya
jumamosi ndio siku yupo busy kupitiliza. Simu za wanae tu. Jeremy, Jema na
Jelini ndio huwa anapokea simu zao. Jumbe ndio hasomi kabisa hata wanae
wanamjua. Tenda zake zote za siku hiyo, anapokea mwisho ijumaa. Jumamosi ni
utekelezaji tu. Ukitaka mfuate kituoni kwake.
~~~~~~~~~~~~~~~
(Yakobo 3:5-9) Vivyo hivyo ulimi nao ni kiungo
kidogo, nao hujivunia matendo makuu. Angalieni jinsi moto mdogo
uwashavyo msitu mkubwa sana. Nao ulimi ni moto; ule ulimwengu wa
uovu, ule ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili
wote unajisi, huuwasha moto mfululizo wa maumbile, nao huwashwa moto
na Jehanamu. Maana kila aina ya wanyama, na ya ndege, na ya vitambaavyo, na ya
vitu vilivyomo baharini, vinafugika, navyo vimekwisha kufugwa na
wanadamu. Bali ulimi hakuna awezaye kuufuga; ni uovu usiotulia,
umejaa sumu iletayo mauti. Kwa huo tunamhimidi Mungu Baba yetu,
na kwa huo unawawalaani wanadamu walioumbwa kwa mfano wa Mungu.
Kwa Mama Jema.
Kwenye majira ya saa tano usiku kuelekea saa 6 ndio akawa
anarejea nyumbani. Akakuta gari la Ezra nje. Akajua tayari. Kwa kuwa
alikuwa amechoka na hasira za kuchukuliwa Jeremy, hakutaka
usumbufu wa kukaribishana ndani. Akashuka garini.
Ezra na Junior nao wakashuka garini. Wakasalimiana. “Pole
na majukumu mama.” “Nashukuru. Mnaendeleaje?” “Sisi wazima. Ila nimekuwa
nikimtafuta Jelini bila mafanikio.” “Sio wewe umemwambia hajachelewa?!” Mama
Jema akaanza.
Jinsi alivyomuuliza, mpaka Ezra akashindwa kujibu, Junior
akakunja uso na kumtizama Ezra. “Eti Ezra? Hujamshauri Jelini na kumwambia hajachelewa?
Na asikubali kuolewa na mtu eti kwa sababu ametambulishwa kila
mahali mpaka kanisani na kwa wazazi? Tena ukamwambia asiogope kukuumiza
au kukuingiza aibu. Ukamwambia ni bora aibu, kuliko fedheha.
Hukusema hivyo wewe, au Jelini amedanganya?” Junior akawa kama anaota.
“Sikuwa na maana hiyo mama yangu!” “Ila hayo ndiyo
maneno uliyomwambia si ndio?” Kimya. “Ezra! Mimi nimechoka, nataka
kupumzika. Sijakaa tokea asubuhi. Kukaa kwangu ni hapo ndani ya gari, nikiwa
narudi hapa kwangu. Tafadhali tusipoteze muda.”
“Lakini sikuwa namaanisha hivyo inavyosikika!”
“Wewe hujamjua Jelini na kichwa chake. Na nahisi unataka kumuoa mtu usiyemjua
kabisa. Sifa yake ya kwanza, hataki kuchosha akili yake kufikiria
chochote kitakachompotezea muda. Hanaga mawazo mazito kwa sababu hataki kujichosha
kufikiria. Kile unachozungumza mdomoni, anakipokea kama kilivyo
na kukitendea kazi.” Hapo Ezra ndio akakosa nguvu kabisa karibia aegemee
magoti.
“Kingine. Jelini uliyekuwa naye wewe, hakuna mtu anayeamini
kama ni Jelini niliyezaa mimi. Mimi mwenyewe hata malaika angeshuka na
kuniambia Jelini angeweza kuishi maisha aliyoishi na wewe, nisingemsadiki.
Amebadilika sana kwa ajili yako wala si mimi. Kichwa chake yule akiamua
jambo, si wakumrudisha nyuma, hata mimi simuwezi mpaka ulipokuja
wewe.”
“Na sijui kama alikwambia, sisi na milango ya kanisa
tumeanzia pale kwenu. Tena kwa kulazimishwa na Jema, kelele isiyoisha.
Kutufuata hapa mchana na usiku na simu zisizo koma. Mpaka tukakubali yaishe. Tukaanza
kwenda kanisani.”
“Sasa kumuona anaungana na nyinyi mpaka siku za
katikati ya juma, Jelini yupo kanisani! Tena anafanya juhudi mwenyewe, kwa
furaha! Jelini!” Mama Jema akawa anashangaa kabisa. “Kwa hakina hakuna
aliyetegemea.”
“Sasa eti na wewe unaona mwenzio anajitoa vyote
hivyo, tena kwa ajili yako, mpaka kufunga na nyinyi! Jelini
mpenda mlo, asiyejua kupitwa na mlo hata mmoja! Leo anafunga na nyinyi bila
kulalamika, halafu unamwambia anafanya kwa ajili ya mama yake!”
“Haiwezekani! Labda hakuelewa.” “Si umuulize Ezra huyo hapo kama hajasema hivyo?”
Akamwangalia Erza.
“Junior! Inasikika vibaya, kuliko nilivyo
maanisha. Unajua nampenda Jelini.” “Kwa vyovyote utakavyosema sasahivi,
lakini hayo ndio maneno yako wewe mwenyewe, kwake. Kanusha tu
hapa nijue Jelini amedanganya.” Kimya, wote wakimwangalia. Junior akapata jibu
lake.
“Sasa! Wewe unamjua Jelini au unamsikia? Unampa
Jelini njia rahisi ya kutoka! Jelini asiyependa shida! Haya!” “Sasa
atakua amekwenda wapi?!” “Sijui. Amechukua mwanae, ameniambia wanasafiri. Sasa
sijui! Ila nataka kukwambia jambo la mwisho kabla sijawaaga.”
Mama Jema akaendelea, ila walijua ana hasira. Si sura waliyomzoea.
Wakabaki kama wanafunzi wa shule ya msingi, mbele ya
mwalimu mkuu. “Hapo mliposimama nyinyi, au mlipoegesha gari lenu,
mkimsubiria Jelini, nyinyi sio wa kwanza.” “Naelewa mama.” “Hapana
Ezra. Huelewi.” Akaweka msisitizo.
“Mida hii kusubiria getini wewe si wa kwanza,
na usifikiri ndio utakuwa wa mwisho. Na hapa mmejikuta peke yenu ni kwa
sababu Jelini, yeye mwenyewe, amekomesha hiyo misafara ya
hapa. Yanakuja kusimama magari hapa! Utashangaa na kujiuliza anayefuatwa ni
nani! Weza fikiri ni raisi au mtu wa maana sana, kumbe ni Jelini asiye
na shule kichwani.” “Mimi simdharau Jelini!” “Sivyo anavyofikiria sasahivi
baada ya mazungumzo yenu.”
“Mama Jema!” “Kwa nini nikudanganye Ezra?! Wewe mtu mzima
na akili zako anapoambiwa unafanya jambo ‘kwa ajili ya mama
yako’. Unakuwa umeambiwa nini kama si kwamba wewe huna maamuzi
yako binafsi, wala huna akili ya kufikiria, ila unaendeshwa
na mama yako? Eti Junior?” Junior akabaki amepigwa na butwaa.
“Hakika imesikika vibaya! Sikumaanisha hivyo hata
kidogo.” “Ila ulimaanisha hutaki kubabaishwa! Kwamba upo sawa
bila yeye! Mbaya zaidi unamwambia Jelini aliyezoea kubembelezwa tokea
analetwa hapa duniani! Jelini! Wewe hujamjua Jelini. Mimi nilikuwa nambemba
mgongoni, nafanya naye kazi siku nzima. Utainama unapiga deki, na yeye yupo
mgongoni, ndio tulia yake. Ukimuweka chini, ni kilio kama amekatwa mahali. Hawezi
maisha bila mkono.”
“Hataki maisha ambayo yeye habembelezwi. Huna mali
utamuhonga Jelini, ukamridhisha kama kumuweka mkononi, na
kumuonyesha unamuhitaji. Kwanza hana shida ya pesa ya mtu. Hajajaliwa tamaa
ya pesa. Nina uhakika huko alipo, na hivi mimi wa kumkemea juu ya
matumizi sipo, atakuwa anachafua pesa yeye na mwanae, tena pesa yake mwenyewe
hajahongwa na mtu.”
“Shida yake. Udhaifu wake, ndio huo. Umuweke mkononi,
umbembeleze. Tena kwako wewe naona amejitahidi SANA. Eti alikufuata
mpaka nyumbani, tena usiku, anakwambia usimuache! Jelini! Halafu
eti hataki umvue pete! Jelini!” Mama Jema akacheka kwa
masikitiko.
“Jelini ang’ang’anie pete! Pete ambayo nina
uhakika ameshaacha hapo ndani na jumatatu atakuwa na pete kama hiyo
uliyomvalisha, tena kubwa zaidi maana hajui hujibana. Mpenda mazuri na makubwa.”
“Mama!” Ezra akashituka sana.
“Nakwambia wewe hujamjua mtu uliyetaka kumuoa. Kwanza
alikuwa hataki ndoa kabisa! Anasema ndoa ni mateso. Na kunyanyasana
kihisia. Akasimamia hapo mpaka alipoona ndoa ya Jema. Vile James anavyomuenzi
mkewe. Ndio akapata moyo. Lakini si vinginevyo. Hapo umemrudisha kulekule
alikokuwa. Hataki tena.” “Haiwezekani!”
“Wala usipate shida. Pata nafasi na Jema atakwambia akili
ya Jelini. Hajuagi kufikiria. Hataki kujichosha na mipango ya
kesho. Kama hivi kaondoka na mwanae anayemrudishaga hapa, basi ujue huko
ni starehe kwenda mbele, akili ya kesho haipo kabisa.”
“Yaani alale, aamke ajikute na mwanae! Shida zake zote zimeisha.
Sasa hivi huko alipo hana analowaza isipokuwa kile anachokiona pale. Mwanae ambaye
ndio roho yake.”
“Ungekuwa unauwezo wa kumuona sasahivi huko, unaweza
usiamini hata kama alikuwa na mpango wa kuolewa jumamosi ijayo, kitchen
party alhamisi na nina uhakika hata hakumbuki kama bibi yake anakuja
mjini kesho kwa ajili yake. Hivi leo nimezuia dada zangu wasije hapa. Maana walikuwa
waje wakeshe washerehekee naye, kabla ya harusi. Nikawaambia wasije,
maana hakuna harusi tena.” “Usingefanya hivyo mama.” Akamtibua.
“Unazungumza nini Ezra? Mimi ni mama yake Jelini. Namfahamu
kwa kulea mwenyewe bila hata kusaidiwa na jirani. Nazijua akili zake na vile
anavyofanya. Hatajichosha kufikiria lolote. Si la kesho na madhara yake.
Yeye anafanya ya leo. Yakienda sawa ni sawa. Yakienda vibaya, anabadili gia. Sasahivi
anastarehe na mwanae, mengine atakuja kukutana nayo hapa, akirudi. Sasa unataka
nikusanye watu hapa kusherehekea kuolewa kwa nani?” Hapo hasira zikampanda
zaidi.
“Hivi unajua madhara ya maneno uliyomwambia Jelini
kwa kiburi au bado unajiona upo kwenye nafasi ya kunilaumu mimi?” “Hapana
mama yangu. Sikuwa na nia hiyo.” “Nakwambia mama yangu hatoki migombani mpaka
jambo la msingi. Nakwambia anakuja kesho kwa harusi ambayo haipo.
Unafikiri mimi nipo kwenye wakati gani kama si kujidhalilisha hapa
mjini?” Akawaka.
“Sasa kabla hujakosana na mimi zaidi. Maana ukimchanganya
tu Jelini, ujue umekosana na mimi kabisa. Tena utakosana na mimi
vibaya sana. Hutanipenda.” “Sina nia yakumchanganya mama yangu.” “Basi umemtingishia
kiberiti mpaka amechoka.” “Haikuwa nia yangu.” “Ulitegemea nini kwa mtu kama
Jelini!? Kwamba atakutetemekea daima!? Kwa nini!?” Akawa ameshalipuka.
“Ndio shida yenu nyinyi. Mtu akijishusha tu kidogo,
mnataka mpaka kumkanyaga! Badala uenzi kama wenzio, wewe ndio unapandisha
mabega na kuvimba kichwa!? Wewe hujaona wenzio wanavyohangaika na Jelini
mpaka leo japo hawapo kwenye maisha yake? Wakisikia tu Jelini ana shida,
wote wanakimbia. Sasa wewe unafikiri ni kwa nini?” Kimya.
“Washazunguka, wamehangaika, wakagundua hawatapata
mtu kama Jelini. Mwanangu hana makuu! Hana tamaa! Sasa kaamua
kitulia na wewe, na wewe unamringia tena! Jelini! Sawa. Tutakuja
kukuona.” “Nampenda Jelini mama yangu na sikukusudia kumuumiza.”
“Kama kweli, basi usingemwambia uliyomwambia.”
“Nakiri nilipaniki baada ya kumuona anapaniki juu ya Colins.
Nikaingiwa wivu.” “Wewe hukujua kama Colins alikuwa mpenzi wake kabla
yako?” “Nilijua.” “Hukujua kama alikaa muda wote akimsubiria yeye?” “Nilijua.”
“Sasa wewe unachofikiri kwa penzi alilokuwa nalo kwa Colins, kwamba litakufa
gafla tu kwa sababu unamuoa wewe!?” Yaani akafanya kumshangaa kabisa. Hapo ashakasirika
kupindukia. Kwanza alikuwa amechoka. Halafu hugusi mtoto wa mama
Jema akakuona au kukusikia. Anakuwa simba.
“Wewe umeanzana na Jelini ukijua wazi mwanaume
aliyewahi mpenda hapa duniani ni Colins. Amerudi Colins, bado amekuchagua
wewe! Sasa badala uangalie yako, ujenge msingi wenu nyinyi imara,
wakumfanya aendelee kubaki kwako na asijutie maamuzi ya kumuacha
mwanaume anayempenda, eti na wewe unamuonyesha hujali! Kweli!?
Jelini!?”
“Nimekosea mama yangu.” “Na wala si mara moja, na
mwenyewe anajua. Ameyatunza,
akiyavumilia, mpaka yamemfika kooni ndio ameamua kukuachia maisha yako
yaendelee bila yeye anayefanya kwa ajili ya mama yake.” “Nitazungumza naye,
nimuombe msamaha.”
“Nakuonya Ezra, usimchanganye Jelini. Nakuonya kabisa.
Jelini amebeba hatima yake na Jeremy. Usiku huu Jeremy angekuwa amelala hapa
ndani, ila wewe umesababisha hayupo, na sijui alipo.” “Nitarekebisha
mama yangu. Naahidi nitarekebisha makosa yangu.” Akajishusha kabisa japo
ametupiwa lawama zote nzito.
“Kaa chini. Jitafakari. Jua ni nini unataka kabla
hujamtafuta tena. Umenielewa Ezra?” Hapo mama Jema kichaa chake kishapanda.
Wanae agombeshe mwenyewe si mtu mwingine awafanyie jambo.
“Wewe si umesema ni bora aibu kuliko fedheha?”
Kimya. “Sasa, kabla hujapoteza ubora
wa hata hiyo aibu, tulia, jua ni nini unataka kabla hujamtafuta Jelini.
Nishakupa madhaifu yake yote. Tafakari ndio urudi hapa, au
umtafute tena. Kama ni mahari yenu, nitawalipa. Kwani shilingi ngapi bwana!?” Akaondoka
na kuingia ndani na kuwaacha wamesimama hapo. Aliwabadilikia vibaya sana.
Hawakuamini.
Marafiki Wa Katika Kila Hali.
Wakarudi garini, Junior akamuona alivyo na hali mbaya ila
akashindwa chakuzungumza. Kimya kwa muda hata gari hawakuondoa. “Nimeharibu
Junior! Sidhani kama safari hii, katika hili kama nitaweza
tengeneza.” Junior akafikiria bila kupata jibu, na bila kujua
chakuzungumza.
Alimsindikiza hapo, asijue kile alizungumza na
Jelini, na vile kilivyopokelewa masikioni mwake na kutafarisiwa
akili kwa Jelini, mpaka kupokelewa kwa namna ile kwenye moyo wa
mama yake.
Maji yalikuwa yametibuka vibaya sana. Akashindwa
chakumwambia ila akaona wajisalimishe tu kwa Mungu wao. “Acha tuombe
Ezra. We will never go wrong with prayer.” “Siwezi hata kuomba! Ila
nataka ujue sikukusudia kumuumiza Jelini.” Junior akamgeukia vizuri.
“Naomba kukuuliza.” Ezra akamwangalia. “Katika yote.
Tukiwa tumebakia mimi na wewe tu hapa. Bila mtu mwingine
anayetusikiliza. Je, kwa kujua moyo wa Jelini, bado Colins hajamtoka,
wewe binafsi, utaweza ishi naye hivyo alivyo?” Kabla hajajibu akaongeza.
“Na kabla hujajibu, kumbuka reaction yako ya leo
baada ya kumuona anashituka kusikia tu jina lake, na vile alivyokuwa
pale alipojua amepata mwanamke mwingine. Je, utaweza ishi naye hivyo?”
Ezra akatulia akifikiria. Junior naye akampa muda wa kutafakari. Kimya hapo
garini, upepo wa a/c ukifukuza joto na mbu.
Kisha akaongeza. “Kama alivyokwambia mama Jema. Na mimi
naunga mkono. Fikiria kabla hatujaendelea. Fikiria ukiwa umeweka
mbali kabisa maswala ya harusi na garama zote tulizowekeza.
Nataka ufikirie na unipe jibu ukiwa unayaona maisha yenu, baada ya harusi.” Kisha
akawa kama amepata wazo.
“Hebu fikiria Ezra. Yaani baada ya kufunga na kuomba
jana kwa mara ya mwisho kabla ya harusi. Tukiombea hii ndoa, ndio yote haya yanatokea!
Inaweza sikika ni ajali mbaya sana. LAKINI kumbe Mungu anataka kukutambulisha
kwa mwanamke unayetaka kumuoa.” Hapo Ezra akamgeukia vizuri.
“Ninaweza nisiwe sahihi Ezra. Lakini Mungu huwa anatumia upumbavu
wetu sisi wenyewe, kufanya mambo yake. Tulifunga na kuomba kwa hakika,
tukimlilia Mungu kwa ajili ya wanawake tutakao kuja oa. Sasa, leo umemjua
Jelini halisi kabisa. Huyo ndio Jelini mwenyewe, na yote umeyasikia
kutoka kwa mama yake mzazi. Mungu amekufungulia Jelini mkamilifu. Je,
utaweza ishi naye hivyo?”
~~~~~~~~~~~~~~~~
JINSI MANENO YALIVYO NA NGUVU. NENO MOJA LINAWEZA IBUA MAMBO MENGI.
Zikiwa zibebakia takribani siku 7, ndoa ifungwe, Jelini
ameondoka hana mawasiliano
na mchumba. Mama yake yupo
tayari kurudisha mahari.
Je, Ezra naye ana kifua cha kuyavulia maji nguo na
kuyaoga?
Ni Nini Kitaendelea?
Usipitwe.
0 Comments:
Post a Comment