~~~~~~~~~~~~~~~
“Wewe Connie nenda kapumzike. Mimi nampa muda atulie,
nimpigie.” “Acha nimpigie mimi.” Hawakutegemea! “Nilimuacha kipindi cha Jelini.
Safari hii nataka kuwa naye.” Wazazi hao kimya. Akampigia.
Ikaita, baada ya muda akapokea. “Ninaye
sonara mzuri sana. Tukimfuata kesho, anaweza tengeneza pete nzuri na kwa haraka.
Tutaandaa mazingira mazuri ya ku propose. Kisha tuulize taratibu za
mahari. Na kwa sababu umerudi kanisani.” “Connie!” Ikabidi aanze kucheka.
“Ulipotea
kanisani Coly! Ila sasa, sababu umerudi,
itakua rahisi kuandikisha ndoa. Njoo nyumbani tujipange vizuri. Usikasirike.
Njoo.” Sauti ya Connie mwenyewe ni ya utulivu,
ukiwa mbali kidogo humsikii. Kidogo akaanza kutulia. “Unakuja?”
“Nageuza. Nakuja. Ila mwambie baba asiniongeleshe tena usiku huu. Aniache
kabisa.” Akakata.
“Anarudi. Ila amesema
usimuongeleshe kabisa.” Mama mtu akahema kwa nguvu akitingisha kichwa
kwa masikitiko. Mzee akazidi kucheka.
“Anataka kutumia dhambi zangu kunifunga macho na mdomo
nisifanye majukumu yangu ya ubaba! Hata kidogo.” “Ushafikisha ujumbe wako, sasa
naomba umuache. Tafadhali Henry.”
“Sawa. Kwani mimi nina neno? Yeye ndiye mwenye neno.”
“Ila katika yote, hili nakushukuru baba Colins. Nilijisahau. Nikataka kurudia kosa. Si sawa
kwa Kamila na kwetu pia. Huyu binti ametuheshimu sana. Kumtoa hapa kimyakimya si sawa. Na ni dhambi.” “Sasa ukikaa
na yule mwanao, kichwa ngumu, usisahau
kumwambia hayo!” “Hicho kichwa sijui karithi wapi?!” Akamkejeli kwa swali
wakijua wazi ni kopi yake, Connie akaanza kucheka
“Sawa. Mimi kwani nakataa! Lakini yeye…” “Huyo anakuja.
Naomba unyamaze Henry.” “Sasa mimi nimefanyaje!?”“Nyamaza.” Akacheka
akitingisha kichwa. Mlango mkubwa ukafunguliwa, wote kimya wakijua ni yeye.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Nilitaka kwenda kulala. Niliposikia maandalizi ya
harusi, nikaona nisubiri nisipitwe. Na mimi nataka kushiriki.” Wote
wakashangaa. “Nilikwambia nini Connie!?” Mzee hana mbavu. “Mimi na mama
tumetoka kumuonya sasahivi hapa! Akaahidi
atatulia.” “Wewe kaa chini tuanze mipango ya harusi. Huu mchezo hautaki
hasira.” Akamtizama baba yake ila akakaa.
Wakamuona ametulia kama anayetaka kusema kitu kinamuia
ngumu kukitoa mdomoni. “Umekubali wazo langu?” Connie akamuuliza kwa kujali. Tuzungumze
kesho, sitaki mwenyewe asikie.” Hapo akapunguza sauti. Wakaelewa.
Akamgeukia baba yake. “Japokuwa unaniudhi SANA, ila
katika hili naona upo sahihi.” Mzee alishangilia huyo nakufanya
wacheke. “Mpaka nimejuta!” “Wewe
mbishi sana bwana! Na jeuri. Kwa
kukubali hivyo! Nahisi naota!” “Nakushukuru kwa kumpokea Kamila kwa kiasi hicho.
Nina uhakika umemtoa hofu kubwa sana aliyokuwa nayo. Alikuwa anahofu akijua kwa
sababu Mike ameondoka, hatapata mtetezi
tena. Nina uhakika kwa hili atatulia japo kwangu umenikatili.” “Wewe
tulia, nikuozeshe kwa heshima. Acha wizi.” Angalau pakatulia hapo. Ila
wakabadili kabisa mazungumzo, kwamba mipango iendelee Kamila akiwa hayupo.
~~~~~~~~~~~~~~~
Hawakukaa sana hapo, wakatawanyika kwenda kulala, kesho
yake siku ya kazi, wote waajiriwa. Ikabidi Colins kwenda chumbani kwa Kamila.
Akagonga, akamfungulia kama aliyekuwa akimsubiria.
“Pole.” “Unanicheka Kamila!?” Kamila akazidi kucheka.
“Hakika siamini!” “Mimi mwenyewe siamini. Ila nimefurahi Colins!
Nimefurahi sana. Nilikuwa nikiwaza hapa, kwamba kama ningekuwa na wazazi
wangu kama hivi tokea zamani, inamaana nisingeishi hata vile na Mike!” Colins
akakaa na kuinama.
Akaenda kukaa pembeni yake. Akamuwekea mkono mgongoni
akimpapasa na kucha. “Pole.” Akamwangalia. “Najua ni kwa kiasi gani ulikuwa
ukitamani twende tukaishi wote kule. Pole.” “Wala sirudi kule.” “Colins!”
“Hakika sirudi. Ile nyumba vile ilivyo ilikuwa imebeba historia mbaya,
yaani wewe ndio umeirudishia uhai. Siwezi rudi kule bila wewe.
Tutaishi tu hapahapa.”
~~~~~~~~~~~~~~~
Wawili hao maisha yakarudi kwa wazazi. Tena safari hii
ikawa kila mtu analala chumbani kwake. Ilibidi Kamila aweze tu, maana alijua
mzee anaangalia. Na Colins naye kikamuingia kichwani na moyoni. Akawa
muaminifu kusubiri kama baba yake alivyomwambia alifanya. Kutomgusa mama
yake mpaka ndoa. Japokuwa alikuwa akimtamani sana Kamila, na mchezo
aliokwisha fanya naye wa nguvu, lakini akawa mwaminifu kwa baba yake. Akamuacha
kabisa, penzi la wizi wakaacha kabisa.
Love Come To Those Who Believes It.
Ilikuwa imebaki juma moja harusi ya mapacha hao
waliokuwa wakimuoa Jelini na Emelda, ifungwe. Mama mchungaji
aliomba watakao weza kufunga, wafanye hivyo kwani alitaka siku hiyo iwe siku maalumu
ya kuombea shuguli nzima ya harusi kabla Emelda na Jelini hawajapotea
kwenye macho ya wengi mpaka kuja kujitokeza tena siku ya kitchen party
kwa watakao hudhuria, kisha harusi. Walipanga kuanzia juma hilo, wapumzike
kabisa, wasitoke hata nje, wawaze ndoa tu.
Akaomba ndugu wa karibu na hao maharusi wajumuike nao. Kina
Ezra wenyewe pamoja na wachumba zao walifunga, wakiwa wamehamasika
haswa. Kwani walishaweka mipango mizito, siku ya
harusi yao nzima. Jinsi itakavyokuwa. Jinsi
watakavyoingia na kucheza ukumbini. Jelini mpenda mziki, akawa ameshatafuta
nyimbo nzuri zitakazoendana na kucheza kwao. Wakatafuta mwalimu maalumu akawa
akiwafanyia mazoezi jinsi wao wanne watakavyocheza siku hiyo ya harusi
yao.
Ulishachaguliwa na
kulipiwa ukumbi wa maana na vyakula vya nguvu
wakijua aina ya wageni wao. Upande wa wakina Junior na Ezra ni wafanyakazi
wa BOT. Kwanza michango yao wenyewe ilikuwa ya neema. Kwahiyo lazima
kuwalisha kutokana na hadhi yao na pesa yao. Maandalizi yalikuwa mazito,
na ungejua wanao oa ni wenye nazo.
Kisha mchungaji ndio alikuwa anaozesha vijana
wake! Kwanza wanajitoa sana kanisani. Kanisa la wenye nazo. Kila mmoja
akasukumwa kutoa kwa mapana na urefu, ilimradi tu harusi hiyo iwe gumzo
na kumfurahisha mchungaji wao.
Na wenyewe hao wawili, waliandaa fungate la nguvu. Kwanza kutaka kujipongeza kwa kuweza kusubiri
mpaka ndoa, na pili walipata wanawake wa ndoto zao. Walijawa furaha na hekaheka
hao, akili ilikuwa siku hiyo ya jumamosi. Kwenye shuguli nzima, na nyuma
ya pazia.
Hati zao wote wanne za kusafiria
zilishakuwa tayari na visa zao zilishagongwa
kabisa, zinawasubiria wao tu. Harusi ifungwe, waende fungate.
~~~~~~~~~~~~~~~
Ndio mama mchungaji akaona jinsi maandalizi yalivyo mazito,
akataka na mkono wa Mungu juu ya yote. Kulikuwa na mwitikio
mkubwa sana, kila kitu kilikuwa kikienda shwari, lakini akataka lazima wapate
siku moja tulivu. Kila kitu kisimame, watulie kwenye uso wa Mungu,
waombe aende nao katika juma hilo. Maana hata kitchen Party yenyewe ya
Jelini na Emelda, kina Junior wenyewe waliweka pesa. Iliandaliwa kama harusi ya
mamilioni!
~~~~~~~~~~~~~~~
Kwa hiyo hata mchungaji na mkewe pia walifunga
pamoja na hao maharusi. Ikawa ibada ni nyumbani kwa mchungaji. Wanakutana hapo kuomba
kwa pamoja kisha kula na kunywa.
Aliandaa vizuri sana ikawa kama tena ni tafrija
ya namna yake. Alifanya kabisa catering. Watu maalumu walimpikia
kila kitu, yeye akiwa kwenye maombi tu siku nzima. Jioni wakiwa kwenye
ibada ya kusifu, kuabudu na maombi haohao watu aliowalipa kumpikia walifika
hapo wakaandaa meza, kama karamu ya mwisho! Vyakula vingi, vizuri na vya
kuvutia.
Mama Jema, dada wa mama Jema, Mode hakukosa. Ni Jelini
tena! Shoga yake anaolewa! Mama mdogo Modesta hakukosa. Tena wakamuonya asifike
kwa mchungaji akiwa amelewa. Cheko limemjaa, furaha zote kuwa Jelini
kapata wa kumtuliza ndani. Mama yao, yaani bibi wa Jelini na Jema, alikuwa
akifika siku ya jumapili kutokea Kilimanjaro.
Jema na familia yake pia walikuwepo. Jelini na mwanae
pamoja na familia ya mchungaji mpaka wengine waliokuwa wametoka kijijini upande wa mchungaji na mkewe waliokuwa wamekuja
kuhudhuria hiyo harusi wote walikuwa sehemu moja wakizungumza pamoja
huku wakiendelea kula baada ya ibada nzuri sana jioni hiyo. Vilijaa vicheko
hapo, furaha na amani, ungejua walifanikiwa kuvuta uwepo wa Mungu
katikati yao.
Moyo Wa Mtu Msitu.
Simu ya James ikaita. Mkewe akamtizama. Akaingalia
akamuona anacheka. Akapokea. “Leo umenikumbuka?” “Wewe ndio umenitupa.” “Mzima lakini?” “Nipo kaka. Namshukuru Mungu anasaidia. Nilitaka kukukaribisha
uhudhurie jambo tulilokuwa tumeanza mimi na wewe, lakini sikufanikiwa kwa
upande wa shemeji yako, ila Mungu amenikumbuka.” James hakutegemea.
“Acha
masihara Colins!” Alipomtaja jina kwa kuhamaki, akafanya wote
wamuangalie baada ya kujua ni Colins. Jelini moyo ukapasuka paa! Kusikia
Colins! “Ni msichana wa wapi?! Lakini acha nikupe kwanza hongera aisee!
Siamini!” Kijiko alichokuwa ameshika Jelini akila, kikadondoka.
Ezra akamwangalia. “Samahanini jamani.” James akajua amesumbua. Akasimama na kutoka
simu sikioni.
Jelini akajishitukia. Akakuta Junior na Ezra wote
wanamwangalia. Akaokota kijiko chake na kuondoka hapo katikati ya watu akijua ashamwaga
mchele kwenye kuku wengi. Ya ndani yote ameyatoa nje. Akaelekea
jikoni kama anayeenda kusafisha hicho kijiko.
Huku Kwa James na Colins.
James alitoka nje barazani
ili asisumbue. “Aisee siamini!” “Hata mimi siamini aisee! Nahisi Mungu
alinihurumia tu. Aisee James, Mungu anajua kufuta machozi.” “Usiniambie!”
“Nimepata msichana huyo! Nahisi ndio maana nilikuwa nikisumbua wasichana
wengine. Huyu ndiye Mungu alimuumba kwa ajili yangu mimi!” James akacheka sana.
“Hakika
tena. Ananijulia kupita nitakavyokwambia ukaelewa. Na alinikuta na hali mbaya!
Mpweke! Hasira za kumpoteza Jelini! Hasira kwa wazazi! Nilikuwa silali aisee!
Lakini amenifanya nimetulia kabisa. Nimejikuta nampenda, na kwa hakika namuhitaji.
Malalamishi yote uliyokuwa ukiyasikia juu yangu, na dhambi zangu
zote, bwana huyu msichana amebeba! Amebeba na ananifanya niishi
kama nisiye na hatia yeyote hapa duniani. Hana lawama kwangu hata
kidogo! Acha nioe kaka, na mimi nitulie.”
“Daah!
Hatimaye!” “Kabisa. Umri umekwenda. Nimepata anayenipenda na kunienzi.” Akatengeneza huo usemi. “Ananipenda na mimi nampenda
kwakweli. Halafu mzuri. Mzuri sana.” James
akazidi kucheka kwa furaha.
“Aisee
hongera sana Colins!” “Nashukuru kaka. Nilikaribia kukata tamaa. Lakini
Mungu amenihurumia. Siku ya jumamosi, tumemuandalia kitu kizuri sana, ili
nimchumbie. Ukiweza, karibu. Ukishindwa, nitaelewa.” “Siwezi kukosa aisee!
Lazima nije nishuhudie. Maana mwanzoni nilikuwa niwe mwenyekiti kabisa wa
harusi yako na Jelini!” Wakacheka.
“Kweli
maisha ni kitendawili!” “Na kwa hakika mipango ya Mungu si kama yetu
James! Hata mimi sikujua kama naweza pata mwanamke mwingine mbali na Jelini, na
nafsi yangu ikafurahi hivi. Aisee nimepata msichana James!” “Acha
masihara!” “Acha kaka! Imekua mwisho wa mahangaiko yangu kwa upande wa
mapenzi. Huyu sisubiri. Nakimbiza kanisani haraka sana.” James akazidi kucheka
mpaka ndani wakawa wanamsikia sasa.
“Hutaki
tena kuporwa!” “Aisee huyu hapana. Huyu nitapambana naye mpaka mwisho.
Na nashukuru wazazi wamesimama na sisi. Mzee amefurahi huyo! Kama sio yeye
aliyekuwa akinichagulia wanawake.” “Atakuwa amejifunza.” “Na Kamila wangu anapendeka
bwana. Hana makuu!” “Hongera sana Colins.” Bado James alikuwa haamini.
“Karibu na
wewe ushuhudie kile Mungu amenitendea mimi na familia yangu. Maana wazazi ni
kama wamepata binti mwingine.” “Lazima nitakuja. Nipe muda na sehemu.” Wakazungumza kidogo, wakaagana. Wawili hao walishapoteza
mtiririko wa mazungumzo kwa muda mrefu.
Alirudi ndani, amejawa tabasamu usoni bado anaangalia
simu kama ambaye bado haamini! Jema akamtizama. Ila akawa muungwana,
akanyamaza kama asianzishe jambo sehemu isiyo yake.
Huku Kwa Jelini.
Ezra alipoona harudi, akamfuata huko jikoni. Akamkuta
anaosha vyombo kwenye sinki. “Humalizii chakula chako?” “Najihisi kushiba.”
Akaendelea kuosha vyombo. “Naomba uache hivyo vyombo, tutoke kidogo.” Wasiwasi
ukamuingia Jelini. Akabaki akimwangalia kwa wasiwasi.
“Kausha mikono, tutoke.” “Nichukue pochi kabisa?”
“Hapana. Tunaenda kuzungumza baraza la nyuma kabisa. Tutarudi.” Akajikausha na
kumfuata nyuma. Kimyakimya mpaka ndani ya baraza. Na lenyewe liliezekwa na
kuzungushiwa uzio wa nyavu tu. Kusiingie mbu. Kulikuwa na viti. Akakaa, ikabidi
na Jelini akae.
“Kuna kitu nataka kukusaidia.” Jelini akamwangalia.
“Hujachelewa.” Jelini akakunja uso kama ambaye hajaelewa. Ezra akaendelea kwa kujiamini.
“Kwangu ndoa ni agano la mpaka kifo. Natamani
kuingia na mtu ambaye amenichagua mimi kama Ezra, na kunipenda.
Sio kwa sababu mama yake anataka awe na mimi. Au amejikuta ni kama amejifunga,
hana njia ya kutoka tena. Sijui kama unanielewa?” Jelini akabaki ameganda.
Hawezi hata kupepesa nyusi.
“Na wewe hivyohivyo. Usikubali kuolewa na mtu eti
kwa sababu amekutambulisha kila mahali mpaka kanisani na kwa wazazi.
Unaogopa kumuumiza au kumuingiza aibu. Ni afadhali aibu,
kuliko fedheha. Unanielewa Jelini?” Akazungumza naye kifasaha haswa kama
anayetoa shule nzito, anataka aeleweke. Kimya. Jelini hakujibu.
Akageuka kabisa vizuri akimwangalia na kumuuliza kwa
msisitizo, kama asiyetaka kubabaishwa. “Umenielewa Jelini?” Asijue ashamkera
mchumba, hasira zimepanda, anajaribu kuzuia. Ila akaishia kujibu. “Sawa.” Ikawa
tena kama ambaye hakutegemea aina hiyo ya jibu.
Yaani katika yote hayo, Jelini akajibu hivyo tu, na
hakuongeza kingine na yeye safari hii
akaonekana na sura ya kujiamini, sio yakubembeleza tena kama
alivyomzoea akimbembeleza na kumuomba asimpokonye pete. Safari hii
akakutana na Jelini mwingine kabisa, sio wakubembeleza mpaka akamtia wasiwasi.
Kabla hajaongeza neno, Junior na Emelda wakawa
wanawatafuta kwa kuwaita. Ikabidi watoke hapo. Mazungumzo yakaishia hapo ila kwa
hakika Ezra alitishika mpaka akajuta kutingisha kiberiti.
~~~~~~~~~~~~~~~
Sasa wakati Ezra anatangulia kutoka, yeye akabakia nyuma
kidogo na kumpigia simu mama yake hapohapo. Akaanza kuzungumza kama mama yake
ndio amempigia. “Vipi mama?” Akasikiliza kidogo na kuendelea. “Sasa
hivi!?” Mama yake akawa hajaelewa huko sebuleni. Ila
yeye akaendelea. “Lakini ni jambo la kumshukuru Mungu. Japo muda umeenda. Tusiiachie
hiyo tenda, twende tu tukamalizane nao. Anza kuaga, na mimi naaga huku. Nakuja
tuondoke sasahivi.” Mama Jema akajua tayari. Kuna ambalo
halijakaa sawa huko.
Hakutaka mengi, kweli akatengeneza uongo wake pale
kwa mchungaji na mkewe. Kuwa wamepata wateja wanaotaka kukutana nao muda huo,
lazima waondoke. Na dada zake nao wakaona waondoke. Wakata maji.
Shuguli isiyo na pombe, si yakukaa muda mrefu. Ilikuwa kesho yake ndio wanakutana
kwa mama Jema. Dada hao walipanga wakanywe huko, na nyama choma mpaka
kukuchwe. Na jumapili mama yao akija pia warudi hapo kwa mama Jema kuendelea kulewa.
Sasa walioona mama Jema na Jelini wanaondoka, na wenyewe haraka sana, wakaaga.
~~~~~~~~~~~~~~~
Wakati wakiendelea kuaga huko sebuleni, huku kwa
Jelini naye alikuwa akizungumza na mama yake, Ezra alikuwa akimsikiliza, na
kumalizia walipowafikia Junior na Emelda.
Ila Junior akamuhisi hayupo sawa. “Kwema?” “Kwema. Ila
inabidi niondoke na mama sasahivi. Tumepata tenda na wanataka kutuona
sisi wenyewe tuwape uhakika, sio wafanyakazi waliowakuta pale. Usiku
mwema. Acha mimi niwahi na mama.” Akaondoka bila hata ya kusubiri yeyote ajibu
kati yao, na wala hakumtizama Ezra. Wakabaki wakimwangalia mpaka akapotea mbele
ya macho yao.
~~~~~~~~~~~~~~~
Ndugu wa mama Jema, wanawake wa kichaga waliofanikiwa
biashara hapo jijini. Kila mmoja ana usafiri wake wa nguvu. Wakaingia kwenye
magari yao, wakatawanyika. Mama Jema, Jeremy na huyo Jelini nao
wakaingia kwenye gari yao, walitokea pamoja.
“Haya, safari hii ni ya wapi?” Ikabidi mama Jema amuulize
maana alishamuona amekasirika haswa. “Tunarudi nyumbani.” Akajibu kwa
jazba. “Kwema?” Mama Jema akajaribu tena. Jelini akaanza kama aliyepata jukwaa.
“Mimi sio wakubabaishwa. Sio kila wakati
mimi ndio natakiwa kumuonyesha mtu kama nampenda na kumuhitaji,
halafu yeye kila wakati ananionyesha hataki kubabaishwa. Kwa kipi
mno?” Akaendelea.
“Yaani kila wakati mtu anakuwa anakuonyesha kama yeye
hana shida sana, wewe ndio uwe unaonekana unashida! Hapana
kwakweli. Kwanza yeye nimemvumilia sana na kuyabadili maisha
yangu yote kwa ajili yake. Mimi sikuwa naenda kanisani na sikuwa
na tatizo.” “Halafu ushazoea mwenyewe ndio wakubembelezwa.”
Mama mtu akachomekea. Maana alijua udhaifu wake.
“Ewaah! Mimi nababaikiwa bwana! Nabembelezwa
na wanaume wazima na akili zao. Na mimi ndio nataka hivyo. Siwezi
nikawa mimi ndio nambembeleza. Kama mtu hawezi basi. Sio lazima
yeye ndio akanioa.” Hapo mama Jema akashituka.
“Jelini?!” “Hapana mama! Kila mtu anaudhaifu
wake. Kubembelezwa ndio udhaifu wangu, na kuna wanao ujulia huo
udhaifu wangu. Kama yeye hawezi basi. Inamaana sio andiko langu. Hawezi
akawa ananiringia mapema hii, hata hajaniweka ndani! Akiniweka ndani je?
Hapana kwakweli.”
“Hata kama na wewe utanisema. Niseme tu. Mimi sijali.
Siwezi ingia kwenye ndoa ya namna hiyo. Kama hana shida na mimi, BASI. Nitaenda
kwa wanao nihitaji kwa kunibembeleza.” Mama Jema kimya.
“Hee! Kwa nini haswa!? Kama anaona mimi sifai,
akatafute mwingine. Asinibabaishe.” “Jelini umekasirika, mama yangu
mzazi. Tulia mama.” “Nimekasirika haswa mama. Yeye sio mwanaume pekee
hapa duniani. Akinishindwa yeye, nitapata wa kwangu. Na mimi nasema
kama yeye. Nataka kuolewa na mtu anayenipenda. Asinichezee akili yangu.”
“Si ameniambia sijachelewa yeye. Basi TUTAONA.
Hanijui vizuri. Acha nimkutanishe na Jelini anayeliza wanaume hapa mjini. Yeye
nimemkubali kirahisi ndio anataka kubweteka! Sasa sio kwangu.
Wanawake wamejaa kibao. Akatafute wakumringia. Mimi ndio naringia
watu. Eti hujachelewa! Kweli?” “Naomba tuanze taratibu Jelini. Tafadhali mama. Harusi
imekaribia. Bibi yako anaingia hapa kesho kutwa, kesho mama zako kama
unavyowajua, wanataka wakeshe pale.”
“Sijali tena mama. Siwezi kuwafurahisha
watu kwa siku chache, halafu eti mimi ndio nikasononeke kwenye ndoa ya
mpaka kifo! Hapana kwakweli. Waje wakeshe, wanywe mpaka wachoke, lakini si kwa
mimi kulipa garama. Kwanza yeye mwenyewe amesema ni bora aibu kuliko
fedheha. Ezra mwenyewe pia hana shida na hii ndoa. Tena kwa kunihakikishia
yeye mwenyewe usiku huu. Sasa mimi nahangaika kwa kipi!” “Kwani imekuaje!?”
Akamsimulia mama yake mwanzo mpaka mwisho.
“Na hii sio mara ya kwanza mama. Ezra anamtindo wa
kunionyesha hataki kubabaishwa. Sasa tutamuona. Yeye si anasema bora
aibu kuliko fedheha? Sasa tutamuona.” “Au hujamuelewa vizuri?!”
“Mama, amefanya kunigeukia kabisa kuniuliza eti kama nimemuelewa
alichoniambia kuwa ‘SIJACHELEWA’.
Nisiolewe na mwanaume eti kwa sababu mama yangu anataka. Kweli mama.”
“Haiwezekani!” “Mungu ni shahidi. Sasa ni maneno gani hayo yakumwambia
mtu kama si udhalilishaji huo? Eti yeye anafikiria mimi Jelini, naolewa
sababu wewe unataka! Kweli!?” Akafyoza kabisa.
“Huko si ni kunidharau kwa hali ya juu, na kuniona
mimi sina akili, nina akili ya kushikiwa? Au kwa sababu anajua
sijasoma ndio maana ananifikiria hivyo!?” “Jelini, unakwenda mbali mama!”
“Hakika amenifikisha mbali. Na huo ujinga mimi sifanyi. Ebo!”
“Yaani mimi nimeishi na watu wanao aminika hapa
duniani, wanaakili zao, wanafanya mambo makubwa ya kushangaza watu,
lakini bado wana amini akili zangu, na…” “Wana kubembeleza?” Mama yake
akamalizia akimwangalia vile alivyowakwa hasira.
“Haswa! Tena si kunibembeleza tu, wananitetemekea
kabisa. Aache kunifanyia michezo ya kitoto. Na ndio atajua hakuna ubora
kwenye chochote. Si aibu, wala si fedheha. Vyote havina ubora.”
Wakawa wamefika kwao, Jelini anawaka kwelikweli wapo kwenye gari hataki kushuka,
anaongea hamalizi.
Mwishoe mama mtu akaona ahitimishe yeye. “Naomba tushuke,
huyu mtoto akalale Jelini. Hayo mengine tutayajua baadaye, kama ndoa ipo
au haipo. Tutajua baadaye.” “Kabisa. Na mimi mtu asinibabaishe.
Kwani lazima kuolewa? Mbona watu wengi tu wanaishi vizuri tu na
hawajaolewa! Asitake kunichanganya mimi. Eti ‘sijachelewa’. Basi nitamuhakikishia
kama kweli na mimi sijachelewa.” Mama Jema hakuongeza neno akijua ndio
habari imeshapinduka. Akajichukulia mjukuu wake na kuingia ndani.
~~~~~~~~~~~~~~~
Mapenzi&Pesa!
Zikiwa zimebakia siku chache wafunge ndoa, bado Ezra anatishwa na penzi la Jelini
kwa Colins. Ametibuwa mambo BILA kutarajia.
Siku waliyokuwa wamefunga na kuombea harusi yao, ndio KUMETIBUKA
vibaya sana.
{Jamani! Shetani naye hujihudhurisha pamoja na wana wa
Mungu wanapokwenda mbele za Mungu. Hanaga mipaka. Ayubu 2:1-2}
Jelini ametoa mengi ya moyoni na Ezra naye ameonyesha hataki kubabaishwa. Kwa
maneno yake mwenyewe, amesema Jelini HAJACHELEWA.
Moyo wa mtu msitu!
Tusisahau, bado Colins hajaoa, na Jelini ndio huyo bado mapigo
ya moyo yanakwenda kasi amsikia!
Ni Nini Kitaendelea Tena!
USIPITWE…
0 Comments:
Post a Comment