Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 33. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 33.

 Better Late Than Never Ndicho alichokuwa amekusudia Colins. Alijua amechelewa, lakini akajiambia hataacha kujaribu. Akaangalia muda ni saa mbili inakwenda na nusu. Wivu. “Hata kama ni kuangalia watoto, ndio mpaka sasahivi jamani! Huyu Mill asije akabadili mawazo akataka kummiliki Kamila yeye mwenyewe.” Akaendelea kuwaza.

Mwishoe akamtumia ujumbe. ‘Bakisha nafasi ya dessert tuje tule wote.’ Akaona simu ya Kamila inaingia. Akajua amesoma ujumbe. “Nimechelewa sana?” “Hapana. Kuna dessert nzuri sana, inayoendana na mapishi yako, nilikununulia, pengine utaipenda. Sikutaka ushibe ukashindwa kula tukiwa wote usiku wa leo.” Akajua ilikuwa ni njia tu ya kumwambia arudi nyumbani, ila akafurahia. Kwamba usiku huo atakuwa na Colins! Akajawa furaha. “Asante kunifikiria. Nakuja. Sipo mbali na nyumbani.” “Basi nitakuwa nikikusubiria.” “Sawa.” Kabla hajakata simu, akaongeza.

“Umekua na wakati mzuri lakini?” “Inatosha kwa leo.” “Mbona kama nakusikia hujafurahia?” “Watoto wamekua, halafu wamebadilika, sio kama mara ya mwisho nilivyowaacha.” “Wamebadilika kwa uzuri au ubaya?” Akaendelea kudodosa kumuonyesha anajali.

“Nafikiri kule kufungwa kwa Mill, na kuwaacha watoto na mkewe pamoja na huyo mwanaume, kuliharibu sana. Sura ni Mill, ila tabia! Mmmh! Mpaka namuhurumia Mill. Ila mwenyewe anaonekana ana imani! Anaamini watabadilika.” “Na mimi naamini hivyo.  Poleni.” Akamsikia akicheka taratibu, na kuongeza.

“Nahisi kama Mike angekuwepo, angemsaidia zaidi kuliko mimi nisiyejua chakufanya! Mike ana namna yake na watu. Mimi najiona sio msaada kabisa! Najiona kama sitaweza kumsaidia kwa chochote.” “Wakati mwingine watu hawategemei msaada mkubwa sana kama ambavyo ungeweza kufikiria. Ile tu kumuonyesha upo, na unajali, inaweza kuwa msaada tosha.”

“Usiwakatie tamaa watoto, na mtie moyo Mill. Ni watoto, wapo kwenye kukua, wamepitishwa kwenye magumu, naamini watakuja kuwa sawa tu. Na wewe usijidharau na kujikatia tamaa. Mungu anajua wewe ni mtu sahihi kwao kwa wakati huu.”

“Nashukuru kunitia moyo. Na kweli Mill anahitaji mtu. Amerudi amejikuta yupo peke yake! Marafiki wamesambaa na maisha yamebadilika. Amekwama peke yake na watoto.” “Inamaana hiyo ni nafasi nzuri kwake. Atapata muda wa kutosha na watoto wake. Sio jambo baya. Wakati mwingine kuna mambo Mungu anaruhusu kwa mtu kwa kusudi. Inawezekana alihitaji huu muda wa peke yake ili atulize akili kwa wanae.” “Pengine kweli! Bora kumbe nimezungumza na wewe! Sasa naona na mimi niliongezeka kwenye tatizo.” Akamsikia akicheka.

“Kwa nini tena?” “Mwenzio nilikuwa sijui chakufanya. Kila wakati nalia. Namwambia bora Mike angekuwepo. Basi nikawa namtia na yeye simanzi. Mwishoe nikamwambia bora niondoke tu. Nikaondoka kwenda madukani ili tu kutuliza mawazo. Nimefika. Nakuja ndani.” “Nije kukupokea?” Mpaka Kamila akashangaa.

“Hamna haja. Sina mizigo mingi, nimenunua vitu vichache tu. Nakushukuru.” Wakaagana ila na maswali. Colins wa jana siye huyu! Huyu amebadilika kweli! Anajali kupita kiasi na ameanza na mabusu ya shavuni! Kumsubiria, na kutaka kumpokea kabisa! Kamila akabaki akijiuliza ila kwa furaha.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akamkuta akimsubiria nje ya mlango. Akaanza kucheka. “Kama umenimiss vile!” Akamuanza akicheka. “Sana. Nimekuzoea Kamila. Najua unaweza usielewe kwa sababu pengine kwa nje sijakuonyesha, lakini uwepo wako kwangu ni faraja. Natamani kuwa na wewe wakati wote.” Kamila asiye na makuu akafurahi huyo!

Akabaki akicheka. “Umekula vizuri?” “Mimi nipo sawa. Na wewe?” “Na mimi nimekula. Ila nimenunua desert nzuri, tuje tule wote.” “Basi acha nikaoge, nije tule. Au umechoka, unataka kuwahi kulala?” “Hapana. Kesho nitakua off, siwahi kulala.”

Kisha akaongeza sauti akiangalia ndani kusudi. “Tunajiandaa kucheza karata. Nataka kumfunga mzee kabla hajalala.” “Acha kumdanganya Kamila.” Sauti ya baba yake ikasikika ndani.

Wote wakacheka. “Huwa anabishaga hivyohivyo, ila anaishia kwenda kulala mnyonge!” “Wewe usiongee sana. Acha muda ujibu.” Kamila akaingia akicheka. “Pole baba yangu. Kumbe ndio hali inakuaga mbaya hivyo?” “Anakudanganya tu. Huwa tunawafunga sana hao wawili. Ni vile Connie hayupo. Lakini humu ndani ushindi uliozoeleka, miaka yote, ni mimi na Connie. Yeye na mama yake ni udhulumishi kila wakati.” “Baba!” “Sasa unachobisha ni nini wakati tutacheza hapa na yeye atapata majibu yake! Wala hakuna sababu yakubishana.” Kamila akazidi kucheka.

“Sasa na Connie anakuja. Leo anakuja kulala nyumbani. Ndio tuone, uache visingizio. Maana huwa haishiwi sababu huyo baba yako.” Wakasikia sauti ya mama yao jikoni. Kamila akazidi kucheka, ila Colins ikamuingia mpaka nafsini mwake.

Inamaana kweli dada yake alikuwa akiogopa kurudi nyumbani sababu yake! Kidogo akanyongea akiamini maneno ya mama yake kuwa ndiye aliyekuwa akipoteza amani ya pale kwao. Ule msamaha na kuzungumza naye, umesaidia!

“Sasa sio aje amechoka, tukafungwa mkase…” “Umesikia Kamila? Ushajua ambao wanafungwa humu ndani. Visingizio ndio kama hivyo!” Kamila akazidi kucheka. “Hawa wawili wanachagua zile siku wanazojua mimi na Connie tumechoka, ndio wanataka kucheza ili kusudi tu, watupate akili ikiwa haiwezi kufikiria, wajichukulie ushindi.”

“Kamila ameshapata jibu baba. Wala usiendelee kujitetea.” Wakazidi kubishana wakicheka. “Basi nakuja sasahivi. Acha nikaoge nije nishuhudie.” Ni kweli Colins alikuwa ameshika amani ya humo ndani. Nyumba ilikuwa imechangamka na kumejaa amani kama zamani, wala Kamila hajawahi ona kabla.

Colins Kabadilishia Gia Kubwa Angani.

Anaingia chumbani kwake akiwa amejawa furaha na hamasa kuwa Colins amejirudi, kumbe ni zaidi ya hivyo! Akakuta kitandani kwake kuna maua rose, mekundu tupu. Pembeni ya hayo maua kuliwekwa kadi kubwa hasw a ndani ya bahasha nzuri nayo ya rangi nyekundu. Kisha kukawa kama kumemwagwa na chocalate pembeni yake. Kamila nusura arukeruke akijua vinatoka tu kwa Colins.

Akatupa kipochi na mizigo yote sakafuni na kuvamia maua. Akayanusa na kujitupa kitandani akiwa ameyakumbatia. Akayaacha kifuani na kufungua kadi imeandikwa hivi, ‘I’m Thankful for you.’ Moyo ukazidi kujawa furaha. Kufungua ndani ilikuwa imeandikwa kwa mkono. Akaanza kusoma.

‘Kamila, sikujua kama kuja kwako kwenye maisha yangu ni upendo wa Mungu kupita kiasi kwangu. Katika mapungufu yangu yote, natambua umuhimu ‘wako’ kwenye maisha yangu.’ Kisha akaendelea.

‘Unaweza usielewe Kamila, lakini umeyabadilisha maisha yangu kwa haraka sana. Sikuwa hivi! Nikidhani nakusaidia wewe, nimekuja kugundua kumbe nilikuwa nikijisaidia mimi mwenyewe.

‘Naweza nikawa sijakuonyesha vya kutosha, uthamani wako kwangu, lakini uwepo wako kwangu, nimegundua imekua faraja niliyokuwa nikiitafuta muda wote, maishani mwangu. Kuna jinsi ulinishika, uliamsha hisia ambazo ziliuwawa muda mrefu sana, kwenye maisha yangu mpaka nilijikatia tamaa. Sikujua kama zingeweza kuja kurudi mpaka WEWE uliponishika.’ Bwana Kamila alifurahia.

Akajua ni ile masaji tu. Akidhania siku ile alijidhalilisha, kumbe amefanya jambo kubwa la kuja kutunzwa moyoni kwa Colins! “Inamaana katika hili nimempita hata Jelini!” Kamila asiye na makuu, akaanza majigambo nafsini kwake akiridhishwa na sifa hiyo.

‘Wanasema better late than never. Najua nimechelewa. Pengine nimekuumiza kwa maneno na vitendo, naomba unisamehe. Lakini mimi mwenyewe sita jisamehe endapo nitashindwa kuomba nafasi kwako.’

‘Nina uwezo wa kwenda kuishi kwangu, lakini moyo wangu umeshindwa kukuacha Kamila. Najihisi wewe ni nafasi ya pekee Mungu amenitumia, sitaki kuipoteza. Umejawa upendo. Hujui kutunza vitu vibaya moyoni. Unajali kupita kiasi! Halafu ni mkarimu.’ Hapo akagutuka. Ametoka kufanya manunuzi, hajamnunulia kitu! “Mkarimu!” Akajisuta.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ila alihofia asije rudia kosa. Kumnunulia zawadi kwa nia njema, halafu kuja kumuumiza. Akatulia akiangalia zawadi alizomjazia yeye pale kitandani, akatamani na yeye angemnunulia hata pipi tu, kama alivyomfanyia yeye na kumpelekea kabisa! Akapotelea mawazoni akijilaumu kushindwa kufanya hivyo akiwa madukani, kisha akumbuka kurudi kusoma.

~~~~~~~~~~~~~~~

‘Naahidi kubadilika ili nisikuumize zaidi. Naweza kuwa nimekuchanganya kutokana na nilivyokuwa nimekwambia juu yangu, na wewe. Lakini huu ndio ukweli ambao pengine nilitaka kuupuuza. Nimegundua nitajipunja mimi mwenyewe endapo nitakukosa wewe, Kamila. Kama sijachelewa, tafadhali naomba nifikirie mimi. Usimpe mtu mwingine nafasi ya Mike moyoni mwako ila mimi. Nakuahidi kuitendea haki, sitakuumiza.’ Ilimgusa Kamila mpaka akajishika moyoni.

‘Kama nilivyokwambia, sitakaa niwe Mike, sitaweza vaa viatu vyake, sitaweza ziba pengo lake, lakini naahidi ukiwa na mimi kama Colins, na wewe hivyohivyo ulivyo. Nikijua na kuelewa wewe sio Jelini, na sitaki uwe Jelini. Nakutaka wewe kama Kamila. Hivyohivyo ulivyo umbwa na Mungu nikiamini ni kwa ajili ya mapungufu yangu. Naamini tukipeana nafasi tutakuwa na wakati mzuri sana hapa dunaini. Nakuhitaji Kamila.’ Kamila hakuamini.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akarudia tena na tena. Na kuhakikisha kweli inatoka kwa Colins. Alijawa furaha! Akamsamehe dhambi zote. Yaani akawa hakumbuki tena hata ya Jelini. Akawa anajiona tu yeye atakavyoanza kupata kiss kutoka kwenye midomo hiyo miekundu kama pinki ya Colins! Atakavyoshikwa naye! Hiyo sauti yake nzito ya kiume atakavyokuwa akiisikia masikioni kwake, akiwa amemkumbatia akimbembeleza! Raha kama zote!

~~~~~~~~~~~~~~~

Akabaki amekaa kitandani anagaragara na maua,  anarudia kusoma huku anakula chokleti, kumbe huko mwenzie mapigo ya moyo yanakwenda kasi akijua Kamila amesoma, na yeye anamlaumu kama Jelini, hamtaki. Tumbo likaanza kumnguruma Colins, kadiri alivyokumbuka maneno aliyokuwa akimwambia Kamila.

“Aisee nimekurupuka vibaya sana! Bora ningefikiria kwanza.” Colins akazidi kuwaza. “Au pengine ningeanza kwa kujirudi taratibu. Ningejipa muda. Yaani kama hivi nilivyofanya leo, ningefanya hata kwa siku 7 mfululizo, ndio nimwambie!” Akaendelea kujivunja moyo.

“Sijui nilikuwa nikifikiria nini! Ndio nitakuwa nimemfukuzia mbali kabisa! Na alivyo mzuri hivi Kamila! Mwanaume yeyote ambaye angepewa nafasi kama yangu, anayejielewa, angempokea kwa haraka sana, tena kwa mikono yote miwili! Nimejichanganya na kujichelewesha kwa ujinga wangu mimi mwenyewe! Daah! Nimemkosa na Kamila naye hivihivi!” Akazidi kujiumiza, akijua yeye mwenyewe amerudisha historia kama ya kwa Jelini. Na Kamila naye atabaki akimlaumu hampendi, anayependwa ni Jelini. Kumbe mwenzie huko ndani, amejawa furaha, hana hata wazo la Jelini!

Mama ni Mama.

Mpaka Connie anafika hapo, Kamila hajatoka chumbani kwake. Wakasalimiana, ila akagundua hayupo sawa na wakati waliagana vizuri tu! Sasa hao watuhumiwa wawili, madaktari wa Muhimbili, wakamgeukia mkombozi wao. Mama yake. Alipoona Connie na baba yake wanamwangalia, akaelewa.

Akamtoa hapo. “Coly, njoo nisaidie kitu hapo jikoni.” Akanyanyuka kwa haraka tu, bila ya kufikiria wala asijue alikuwa amekaa wapi, kumbe ilikuwa sebuleni, katikati ya wote, yeye kimawazo hakuwepo hapo.

“Ni nini tena Colins?!” Mama yake akamuuliza mara walipofika jikoni nakujikuta wapo peke yao. “Hamna shida. Nahisi najipanikisha tu.” “Kwa nini?” “Mbona Kamila hatoki chumbani?” Mama yake akawa hajaelewa. Akamuelezea mama yake kwa kifupi na kuongeza.

“Nimerudia kosa nililofanya kwa Jelini, mama. Halafu nimeharakisha kumwambia kama namuhitaji. Ataona nina mdanganya! Au sijielewi! Sijui ninachotaka!” Akajikuta anajisalimisha kwa mama yake.

“Inawezekana mwenzio hafikirii hayo kabisa! Unajipanikisha tu bila sababu. Nimemsoma Kamila, kwa haraka anaonekana ana moyo mzuri.” “Sasa unajuje kama hata katika hili atalibeba vizuri?” “Sasa kabla hujanikatisha na mimi tamaa, na kunitia wasiwasi wako, nenda ukamgongee ujue kinachoendelea, kuliko hicho unachokifanya sasahivi hapa.”

“Nisije..” “Colins! Niangalie mimi.” “Nakuangalia mama!” “Hapana. Nataka utulize mawazo hapa kwangu, uniangalie na kunisikiliza ninachokwambia. Wewe umepaniki, na kusahau huyu msichana alikuwa akikuomba nafasi hii muda mrefu sana ila wewae ndio hakuwa tayari.” “Sasa si ndio ninachokwambia sasa! Pengine atakuwa amechoka, hataki tena!”

“Mapenzi ya kweli huwa hayafi kwa haraka kiasi hicho. Na katika hili ndio utagundua kama umepeta wako wa ukweli au la. Hii ndio nafasi ya kweli na ya pekee itakayokusaidia kujua kama kweli alikupenda au alibabaishwa na huo uzuri wako tu.” Colins akaanza kucheka.

“Muone! Nenda.” Akambusu mama yake na kumkumbatia kwa muda mrefu. “Ujue nilikumiss sana?” Kisha akaongeza. “Wewe ndio msiri wangu, nashangaa kwa nini unakubali kuyumbishwa!” “Unapoteza muda, nenda Coly. Na usiende kinyonge, utaanza kwa kumboa. Jibebe kijasiri kama ambaye unajielewa na unamaanisha ulichomwandikia.” Akatoka hapo jikoni jasiri kama sio yeye!

~~~~~~~~~~~~~~~

 “Na mimi nilikumiss Connie. Nisubiri tutapata muda mzuri. Tuwafunge madaktari wa Muhimbili, ndio mkalale.” Akatupia neno akipita hapo akielekea chumbani kwa Kamila, angalau wakaanza kucheka tena. “Hizo ni dua za kuku.” “Sawa baba.” Akapotelea koridoni akifuata chumba cha Kamila.

Msamaha ni kwa ajili yetu.

Hufungua milango mingi na migumu ambayo haifunguki kwa chochote isipokuwa kuachilia uchungu moyoni na KUSAMEHE.

Usipitwe na usiku wa Kamila & Colins.

Inaendelea….

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment