Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 31. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 31.

 Colins anatoka, anamkuta mama yake amesimama tu jikoni. “Vipi?” Ndio akagutuka. “Mbona umekosa tena raha? Kwema?” “Kwema. Nilikuwa namalizia na mimi nikapumzike.” Akageuka.

“Mbona huniangalii? Nimekuudhi nini tena!?” Colins akasogea kabisa. “Hamna kitu.” “Mama!” “Uliponiambia unahisi umechelewa, ulimaanisha nini?” Colins akabaki akimwangalia. “Coly?” “Haina maana tena mama! Wewe acha tu kama ilivyo.”

“Labda nikuulize, unategemea Jelini aje aachane na mchumba wake akurudie wewe?” Colins akaanza kubadilika sura. Nakushindwa kujibu. “Kabla hujapandisha hasira, naomba utulie na kutafakari. Makosa yalishatendeka. Mimi na baba yako tulishakosea. Maisha ya Jelini yanaendelea kama kawaida. Utabaki na kushikilia ya zamani mpaka lini?” “Hayo yote yanatoka wapi?!” Colins akashangaa sana.

Huwezi kutengeneza nyuma Colins, ila kuanzia pale uliporudiwa na akili zako. Kwa jinsi ulivyoweza kutengeneza kwingine kote, ukijisahau wewe mwenyewe, jua na yako unaweza tengeneza na ukaishia kuwa na furaha. Mungu si mwanadamu hata aseme uongo. Mungu ni mwingi wa upendo. Hajaishiwa upendo hata mara moja na hataanzia kwako. Sasa toka huko unakojificha, na kushikilia kisicho chako, tengeneza yako.” Kabla hajajibu mama yake akaongeza.

“Kuna mambo magumu huwa yanampata mtu, kwa haraka yanakuwa hayana majibu, lakini si kwa Mungu. Wakati mwingine ni yeye mwenyewe anatunza waovu kwa siku ya maangamizi. Soma.{Mithali 16:4} Huwezi jua alitutumia sisi kukuumiza ili aje akupe kitu kizuri zaidi.” “Zaidi ya Jelini!?” “Wewe ulishamuoa Jelini, ukaishi naye kama mke nyumba moja? Ukajua anavyokua akiwa mjamzito na amezaa, kisha mkapita naye kwenye maisha yote, shida na raha! Ugonjwa na uzima. Kisha ukamjua kwa undani wote mpaka sasahivi ubaki unashikilia hutaki kuachia kama hivyo Kamila alivyoishi na Mike?” Kimya akiwa amemfanya afikirie.

“Wewe mwenyewe umesema ulishindwa kutengeneza kumbukumbu nzuri kwake. Sasa kinacho kushinda kuanza upya ni nini kama si kutaka kuendelea kujiharibia zaidi?” Kimya. “Eti Coly?” “Nyinyi ndio mmeniharibia mama!” “Kwa hiyo? Unataka kukaa hapo mpaka lini? Utatulaumu mpaka lini? Utajiadhibu mpaka lini? Maana unachokifanya hapo ni kuendeleza pale sisi tulipoharibu. Tena wewe ndio unafanya vibaya zaidi.” “Kivipi?” Mama yake akabaki akimwangalia.

“Mama?” “Hivi unanisikia kweli ninachokwambia Coly au umeamua kuendelea kubeba hasira tu? Mpaka lini!? Au unachotaka ni nini kitokee ili uweze kusamehe na uendelee?” “Siwezi kusahau?” “Umeshanisikia mimi nikikwambia sahau?!” Akamuuliza kwa ukali kidogo ila kwa sauti cha chini kama akinong’ona. Colins hakutegemea. Akabaki kimya maana ni kama alimvamia.

“Eti Coly? Umesikia hawa wawili jinsi wanavyoimba sifa za Mike. Na vile alivyompenda Kamila. Na Kamila kumsubiria kwa muda wote huo mpaka kujiridhisha kweli amefariki. Lakini mbona mwenzio Kamila amekubali kuendelea, wewe umegomea hapohapo?” Akabaki kimya.

“Jambo hili utabeba mpaka lini baba mzazi wewe? Eti Coly? Utanichukia mimi mpaka lini? Wengine watapita na kubadilika majina kwako, lakini mimi ni mama yako tu. Niwe hai au nimekufa, nitabaki mama daima. Huwezi badilisha. Na baba yako hivyohivyo. Mwenyewe ulisema hukujaliwa wazazi wazuri. Kwa hiyo?!”

“Nilihitaji muda.” Akajirudi taratibu. “Basi ujue unakaribia kuchelewa. Huko unakojificha, unapoteza muda. Ukija kutoka huko, utajikuta unakosa bara na pwani, wakati wenzio maisha yanaendelea, wewe unajiumiza tu. Mimi nakwambia ukweli. Hata ukinichukia zaidi, huo ni ukweli. Unajichelewesha na unajinyima raha na faraja  wewe mwenyewe. “

“Jelini anaolewa, kwake hurudi tena. Kubali huo ukweli na utoke hapo.” Akampita na kuondoka zake, akamuacha amesimama hapo jikoni.

Sharp Corner.

Akasimama hapo akijua mama yake yupo sahihi. Ikawa kama kengele masikioni kwake. Lakini anafanyaje? Aliyebaki karibu yake ni Kamila na kwake nako ameshaharibu. Ni kweli Jelini hatakaa akamrudia tena. Anafanyaje? Akaona kilichobaki kwenye hiyo safari aliyokuwa akiendesha kwa mwendo kasi karibu aingize gari korongoni au tayari amefika ukingoni, basi ni kukata kona kali/sharp corner.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

 Akajikuta anakwenda mpaka chumbani kwa Kamila, akagonga. Baada ya muda mfupi akamfungulia. “Nimekuamsha?” “Hapana. Bado sikuwa nimelala. Vipi?” Akamuona anasita ila anatilisha huruma.

“Nikikukaribisha ndani itakua vibaya?” Colins hakutegemea, maana alibakia mlangoni akijua na hiyo siku atarudishiwa mlangoni. “Nitashukuru Kamila.” Ikawa kama anaibembelezea hiyo nafasi ya kukaribishwa ndani. Akampisha mlangoni. Akaenda kukaa mwanzoni mwa kitanda akainama kama anayetafuta jinsi ya kujieleza. Kamila akaenda kukaa mbali kabisa ila hapohapo kitandani na kunyamaza.

“Nakujali Kamila.” Akavunja ukimya. Kamila akamwangalia. “Nakujali na sitaki kukuumiza.” Kamila akamwangalia kwa muda na kuinama. “Nia yangu haikuwa mbaya kwako. Nataka kukuona na furaha.” “Hujaniumiza Colins. Kwa vyovyote utakavyoniona, jua ni maumivu ambayo tayari ninayo, wala wewe huusiki na kuwepo kwake.” “Una uhakika?” “Kabisa Colins! Ungekuwa mwanaume tapeli, ungenitumia vibaya kwa sababu nilikuwa kwenye kipindi kibaya. Lakini binafsi nimekuheshimu. Nimeona umenithamini na kuniambia ukweli japo nilianza kuonyesha nia mbaya.”

“Naomba usiseme hivyo.” “Ni kweli, wala si uongo. Amini nimejichukia Colins. Sijui nilipatwa na nini! Nahisi ni hofu ya kubaki peke yangu, na wewe ukawa umenielewa, nikapitiliza. Lakini mimi sio msichana wa namna hiyo.” “Sikuelewi vibaya hata kidogo, ila najilaumu.” Kamila akakunja uso akimwangalia.

“Kila Mungu anaponitumia bahati, inanikuta nipo katikati ya mambo mengi, akili haijatulia. Najikuta nikiharibu na kuumiza nilioletewa kwangu kwa upendo.” Kamila akamwangalia kama akijaribu kumuelewa akashindwa, akaangalia pembeni akifikiria.

“Nilimuumiza sana Jelini. Sana. Tokea mwanzo mpaka sasa haamini kama kweli nampenda. Ila ni kwa kuwa alinikuta katikati ya mahusiano ya utata, sikutaka kumchanganya kama hivi wewe. Nimefanikiwa kujitoa huko, kwa shida. Mpaka nakaribia kumalizana huko nilikokuwa, nimejikuta nimempoteza Jelini na hajui kama nilimpenda kwa dhati! Sasa najihisi narudia kosa.” Kamila akamwangalia na kunyamaza.

“Na sijui kwa nini nazungumza yote haya! Samahani. Nahisi nimekuja tu bila kufikiria.” “Usijali. Tafadhali kuwa na amani. Naamini utakuwa sawa tu. Binafsi naona watu wa aina yako ni wachache sana. Umeongezeka kwa Mike na Mill. Hao ndio wanaume niliozungukwa nao, naweza wafananisha na wewe. Usijilaumu, ni tabia nzuri.” Colins hakutegemea.

“Kweli Kamila!?” “Kabisa Colins. Sio kitu kibaya. Binafsi nimekuweka kwenye kundi la hao wachache niliofanikiwa kuwa nao karibu huku wanawake wakiwatolea mate, lakini wakabaki na msimamo. Ngumu kumzungumzia Jerry kwakuwa mwanamke wake anamchunga sana, lakini hao wawili ni kama wewe. Wana msimamo na mambo yao. Hawana tamaa. Wakiwa kwenye mahusiano, wanasimamia hayo mahusiano.”

“Hata Mill kuoa huko, si kwa kupenda au tamaa! Ilimlazimu lakini ni kosa anajutia mpaka leo, kama ulivyomsikia mwenyewe. Alimpenda sana Pam. Anahisi anapata mikosi sababu ya kumuumiza Pam. Ameshindwa kujisamehe kabisa japo alichofanya ni jambo la kawaida kwa wanaume wengine.”

“Kwa hiyo usijiumize Colins. Ni tabia nzuri. Mwanamke atakayefanikiwa kuishia na wewe, atafurahia hili na atakua amebahatika sana. Wewe ni muaminifu kwenye mahusiano. Si mkimbiaji hata maji yakizidi shingoni. Kwa hiyo kamwe usijitilie mashaka. Naamini ni muda tu, Colins. Utakuja kupumzika siku moja na utasahau yote haya.”

“Daah! Sijui ni lini aisee! Mpaka nakata tamaa! Naona naharibu kila mahali na sijui au sina uwezo wa kutengeneza.” “Ni muda tu. Na ninakuhakikishia utasahau. Mimi nazungumzia kwa kuwa nilipita hapo na najua pumziko unalopata unapopata mtu sahihi na yeye akakupenda. Utafurahia na kusahau yote.”

“Fanya kama ulivyoniambia mimi. Weka sawa mambo yako na Jelini. Ukijiridhisha, usiogope kufungua moyo kama ulivyoniambia mimi. Celine aliimba huu wimbo. Mike aliupenda sana. Alisema hivi, ‘Love come to those who believe it.’ Ukiamini, hutaishia pabaya.” Colins hakutegemea.

“Kumbe ni afadhali nimekuja kuzungumza na wewe!” Kamila akacheka na kunyamaza. “Nimefurahi umeweza kunielewa. Nahisi ni kilema kinachowaumiza wengi.” “Ni maumivu ya muda tu, tena si mabaya. Lakini mtu yeyote akitulia na kukutafakari, hicho unachosema ni kilema, utatamani wanadamu wote wawe nacho.” Angalau Colins akacheka.

“Kweli Colins. Una msimamo mzuri. Nenda kapumzike.” “Na wewe unalala?” “Bado. Nimemuona Mill, siamini! Hapa nilikuwa nikichat naye, tena baada ya kuzungumza naye kwenye simu bila kumaliza. Tunakuaga na stori tokea sekondari na mpaka hivi sasa. Ana haiba ya kujali kama Mike, kumpata hivi, ile hofu yote niliyokwambia ninayo, imeisha.” “Nimekuona!” Akacheka wazi akionekana na tumaini jipya.

“Nilikuwa naogopa sana. Mike alikuwa mzuri sana wa mipango.” “Hata Mill amemsifia.” “Sasa bora mwenzangu yeye anaikumbuka, na kuitendea kazi. Lakini mimi nilijawa hofu, nikawa sikumbuki kila kitu.” “Sasa hivi umekumbuka?” Akaanza kucheka akitingisha kichwa akikubali kwa furaha. “Kichwa kingine kimerudi! Sina hofu tena. Na safari hii naandika kabisa. Sitaki kujikuta naanza kila wakati.”

“Utanikimbia kila mahali Kamila! Nyumbani, kwenye gari na kazini! Unaniacha mpweke! Nahisi nishakupoteza na wewe!” “Huwezi poteza kitu ambacho hujawahi kuwa nacho Colins.” Colins akashituka kidogo ila akajikaza na kuuliza.

“Kivipi tena?” “Kwenye gari tulikuwa wote, lakini ulikuwa hata hujui kama nipo! Ulikuwa ukimzungumzia Jelini tu na kupotelea mawazoni hata hujui kama na mimi nipo.” Hapo ndio akawa kama anamfungua macho, asiamini.

“Kweli Kamila?!” “Kabisa. Na kazini kwenyewe ilikuwa ni mpaka nikutafute mimi. Nikinyamaza na wewe hutajali mpaka…” Akasita ila akabadili na kuendelea. “Na hapa nyumbani nilibaki kuwa kama mzigo kwako. Nakuomba vitu vilivyokuwa vikikunyima raha! Hunihitaji Colins. Huwezi kuwa mpweke na wala hutanipoteza kwa sababu hujawahi kuwa na mimi. Utakua tu sawa, usiwe na wasiwasi wakupoteza ambacho haukuwa nacho.” Hakutegemea.

Akamwangalia na kuinama. Akajua huo ndio ukweli. Kwengine kule ni jumla yake. “Daah!” Akamsikia akisikitika. “Utakuwa sawa Colins.” “Na sisi?!” Akamuuliza swali ambalo akashindwa kujibu. “Eti Kamila? Na sisi, baada ya yote hayo, tutakuja kuwa sawa tena!?” Jinsi alivyomuuliza kwa kumbembeleza, hiyo ikamuingia mpaka rohoni. Akamuona kama anayetaka kutokwa na machozi.

Ila akajibu kwa kujihami asijekuwa amemuelewa vibaya. “Naamini tutakuwa sawa Colins. Sasahivi nimekuelewa.” Akamwangalia kwa muda mpaka Kamila akainama. “Nikuombe kitu?” Kamila akamwangalia na kumuuliza, “Nini?” “Naomba usinikatie tamaa. Naomba nipe muda. Usinifungie milango yote. Naomba nitakapoweka mambo yangu sawa, nisiwe nimekupoteza na wewe. Tafadhali Kamila.”

“Mimi nipo Colins. Unakumbuka nilikwambia hivyo?” “Naona mambo yanabadilika kwa haraka haraka! Mpaka naingiwa hofu nahisi kukupoteza tayari.” Akazidi kumlainisha nafsi. “Mimi nipo Colins. Sina ninapokwenda ila tu narudia ndoto zangu. Hichi ulichonipa ni cha thamani sana. Sina nitakapokwenda nikakipata. Nahisi nyinyi wote, mpaka Connie, mtaondoka hapa, mimi mtaniacha.” Colins akacheka akimwangalia.

“Huondoki?” “Niende wapi tena!? Mwenzio nilikuwa nalala kwenye gari na pesa ipo benki. Ilimradi tu niwe na wale watu pale japo walikuwa wakininyanyasa. Mwenzio napenda undugu. Na hivi Mill naye amekaribishwa na wanae!” “Kumbe nyinyi mnachukulia kwa ukubwa huo!” “Hatutanii sisi. Hapa Mill ashajiandaa jumapili kuleta wanae hapa, waanzie kanisani na wazazi. Anataka wanae wabadilike, wawe kwenye familia kama hii pengine itawasaidia. Kwa hiyo hapa sisi tupo sana, mpaka mtatuchoka.” “Wazazi wangu hawana neno. Ndio vizuri tutakuwa wengi.” Angalau akawa ameupata moyo wa Kamila.

Alijaliwa moyo mwepesi. Huhitaji mambo mengi kuupata moyo wake. Anaridhika na vitu vidogovidogo! Mpaka Colins anatoka hapo, amefarijika na Kamila anacheka.

Jumamosi.

Asubuhi akiwa anavaa akasikia hodi. Akatupia jicho kwenye saa ya ukutani. Bado ilikuwa mapema. Akajiuliza ni nani mida hiyo anayemgongea, haikuwa kawaida! Akajifunika kwa haraka na kufungua.

“Colins! Mbona mapema? Kwema!?” “Nimekuja kukuaga, nisiondoke kimyakimya. Nakwenda kazini.” Kamila akacheka kwa kujisuta akikumbuka lalamika yake ya jana usiku.

“Mbona mapema!” “Usingizi nao ulikata mapema, nimeona niende tu nikaanze siku, ili na mimi leo niwahi kutoka, nipumzike. Wewe si upo sawa swala la usafiri?” “Kabisa. Na mimi nitatoka muda si mrefu ili niwahi foleni.” “Basi nitakuona kazini. Kuwa mwangalifu barabarani.” “Na wewe.” Akashangaa anamsogelea na kumpa busu la shavuni. Hakutegemea, ila alifurahia sana. Akacheka na kujishika shavuni. “Asante.” Akamshukuru, Colins akacheka na kuondoka akamuacha ameduaa, mkono shavuni.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kwenye majira ya saa nne hivi akiwa katikati ya maandalizi ya chakula cha mchana, akasikia watu wakisalimia kuanzia mlangoni kisha mzee Yusuf. “Leo umetutembelea bosi wangu! Au ukaguzi?” “Hii ofisi yako wewe mwenyewe ukiwepo, sina shida nayo. Naona mnapamudu. Napita tu kumuona Kamila.” “Sasa hapo tena ndio ujue umeharibu siku yangu nzima!” Kamila akaanza kucheka. Ukaanza utani.

Kina Dula ushabiki! Kamila hana mbavu. “Mzee Yusufu, nimesema napita tu kumuona! Simchukui! Wewe unashinda naye hapa siku nzima! Mimi namuona tu, na zawadi kidogo, basi.” “Zawadi tena!?” “Ni pipi tu mzee wangu! Usiingiwe hofu na wala siwezi kukushinda wewe unayemlisha siku nzima!” “Ulikumbuke hilo Kamila! Mimi nakulisha hapa siku nzima! Sasa sio urubuniwe na pipi tu.” Cheko mtoto wa kike, angalau hapo akapachangamsha, Kamila akamfuata.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wakatoka. “Wenzio wanakuogopa!” “Kweli!? Kwa nini!? Mbona wamenichangamkia tu!” “Wanasema wewe hupendi ujinga kama yule meneja mwingine aliyekuwa hapa. Alilala na kila mwanamke hapa. Kuanzia wafagizi mpaka manesi! Wewe hutaki mazoea ila kazi.” Colins akacheka tu bila ya kuongeza.

“Nimekuletea pipi na kukuomba tule wote chakula cha mchana.” “Asante kwa pipi, lakini hapa nishamrubuni Mill, anakuja kwenye mida ya mchana tule naye, jioni nitawahi kutoka kidogo, nikaone watoto.” Colins akawa amekwama.

“Ila nakushukuru. Nimefurahi.” Colins akabaki akimwangalia. “Nikuletee chakula ofisini au utatoka?” “Kama nitatoka nitakutaarifu. Asante.” Akacheka kwa kuridhika akimwangalia asiamini hayo mabadiliko! Colins anajirudi kwa vitendo wala si maneno!

“Kwa hiyo unahama lini?” Akamuuliza taratibu wakiwa wamekaa tu hapo nje ya jiko. “Sijui Kamila! Sitaki tena kuwa peke yangu.” Akaongea kwa upole. “Sitaki tena kuwa mpweke. Najua unaweza usiamini sababu nimekuumiza, lakini kuja kwako umeyabadili maisha yangu. Umenitoa pabaya nilipokuwa nimekwama, sitaki kurudi huko tena. Kwa hiyo sidhani kama nitahamia Kigamboni. Sitaki kuwa peke yangu.” Kamila akasikiliza, akashindwa chakujibu, akainama akifikiria. Wakatulia kidogo, akaona aage.

“Acha nikuache ukafanye kazi.” “Nimefurahia kuja kuniona Colins. Asante kwa kuja na asante kwa zawadi.” Hivyo alivyoshukuru, akajikuta anampa kiss nyingine ya shavuni. Akasimama. “Nitawahi kurudi nyumbani. Nitakuwa nikikusubiria, ukirudi tuwe wote.” Kamila akabaki ameduaa, mkono shavuni alikoachiwa kiss. Colins akacheka na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akili ikawa ipo kwa Kamila. Kama ambaye ameshachelewa anakimbizana na muda. Kazi zikawa zinaanza kuwa nzito. Wasiwasi kwa Kamila. Mill asije badili mawazo akaamua kubaki naye. Watesi wake, zaidi Love ni kama anakaribia kuwafikisha ukingoni, wapo magotini. Ya Jelini nayo ni kama yanakaribia ukingoni pia, ila si mwisho kabisa. Hataki kuishia njiani kabla hajaona mwisho wake.

Na hataki kuwa na Kamila huku anahangaika na Jelini pamoja na kuhitimisha ramsi na Love. “Utakuwa usaliti kwa Kamila. Hata mimi nisingependa awe na mimi huku akimuhangaikia mwanamme mwingine.” Akazidi kujichanganya mawazoni, akili ikizunguka. Kengele za kuchelewa zikizidi kulia. Na maneno ya mama yake yakizidi kumsumbua akilini. “Nisije kosa kweli bara na pwani!” Akazidi kuwaza.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kipi anaachia kipi anashikilia?!

INAENDELEA.



CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment