Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 28. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 28.

Njiani nako kimya. Hasira za usaliti wa Love zilikuwa zimeshampanda Colins, hawezi kuzungumza. Na Kamila naye akabakia tu kimya, safari ya kurudi kwao ikaendelea.

Wakati wanakaribia nyumbani Colins akavunja ukimya. “Ulitaka kwenda kununua hilo gari saa ngapi?” “Utakapokuwa wewe na nafasi, ukiniambia, nitazungumza na mzee Yusuf ili nitoke. Na pia kama ukizidiwa na majukumu, tafadhali usiwe na wasiwasi. Bado napakumbuka, naweza nikachukua taksii inipeleke. Nitakapo kwama nitakuomba ushauri. Si ni sawa?” Colins akamtizama kama anayejaribu kusoma kitu.

“Kwani mzee Yusuf amekupa siku za off  lini?” “Nilimwambia nataka kuwa nikienda tu kazini bila off, mpaka nitakapojiweka sawa. Lakini nafikiri kwa sasa nipo tayari.” “Unamaanisha nini?” Akatulia kidogo.

“Eti Kamila?” “Najiona kama naweza timiza ndoto zangu! Niendelee pale aliponiacha Mike, sio kukwama tena au kurudi tena nyuma kama kwenye ajira, ambako Mike alinitoa ili nianzishe kitu changu. Acha nifuate ushauri wako. Niishi kama mtu niliyewahi pendwa, na ninayejua maisha ni nini. Siwezi kuwa tegemezi hivi daima. Nimejitafakari nikagundua Mike aliniachia ramani nzuri tu ya maisha. Nikitulia, nisijichanganye tena, naweza kuifuata na nikafanikiwa tu.”

“Umehisi unajichanganya?” “Kabisa. Najiona nataka vitu vikubwa ambavyo havijawahi kuwa vyangu, na havitakaa kuwa vyangu. Najiweka njia panda bila sababu! Si sawa kwangu. Naona ni bora nishike vyangu na kuviendeleza, na mimi niwe na kitu kinachoeleweka sio kudandia vya watu. Sina sababu yakufanya hivyo kwakweli.” Colins akapata ujumbe wake vizuri.

Alimringia Kamila! Ikawa akimsukuma mpaka amefanikiwa kumfikisha mwisho. Sasahivi Kamila hataki tena. Akaanza kuona anakosa bara na pwani. Akatulia akili ikizunguka. Hajui chakusema, hajui jinsi ya kujirudi. Na pia hakujua kama ni wakati muafaka wa kujirudi! Wakatulia mpaka nyumbani.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wakawakuta wazazi sebuleni. Wakaenda kusalimia. Ila wakagundua wana ukimya usio wa kawaida yao. “Vipi Kamila mwanangu.” “Leo mzee Yusuf ameniachia kupika mboga zote. Amependa huyo, amesema anaongeza mahari.” Wote wakacheka. “Kwa hiyo hapa nilipo nimeaga umasikini?” “Kabisa baba yangu. Wewe subiria mahari kubwa, tena sana.” “Sawa mama.” “Chakula kipo mezani.” Akaongeza mama Colins.

“Mimi nimekula mama yangu. Hapa nimechoka, leo tulikuwa na mapishi mengi. Wagonjwa wa kisukari waliongezeka, wengine wa pressure. Tukawa tunamapishi mengi, siku nzima. Kama hakuna chakusaidia jikoni, naomba niwahi kulala. Maana na kesho ametuambia mapishi ya kuanzia asubuhi itakuwa hivyohivyo.”

“Wewe nenda tu kapumzike. Huko jikoni kupo sawa.” “Basi usiku mwema wazazi wangu. Colins, kesho. Uwe na usiku mwema.” Akabaki akimwangalia, Kamila akamtizama, akaangalia chini na kuondoka. Wazazi wakawaona wakajua kuna jambo.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Vipi nyumba?” Mama yake akauliza kama kumrudisha pale maana macho yalibakia kule alipopotelea Kamila. “Kila kitu kipo sawa. Wameshabadilisha vitasa. Hivi kesho natuma dereva akatoe pale vitu vya Love na Festo.” Wakashituka sana.

“Kwamba Festo alihamia pale!?” “Acha tu. Love ananiuma kama kidonda! Sasa sijui walikuwa wakiishi pale na mimi nikiwepo pale nahangaika mtaani!” “Najua ni ngumu Colins, na mimi ni mtu wa mwisho kutaka kunisikia kukupa ushauri. Lakini jitahidi huko usirudi tena. Ukirudisha tu mawazo yako huko, utakwama na hutakaa ukatoka.” Akanyamaza.

Wakashangaa safari hii hajibu akabaki ameinama kama anayewaza kitu. “Vipi kazini?” Mama yake akamjaribu tena. “Kila kitu kinaenda sawa. Acha nikale na mimi nilale.” Akasimama.

“Colins?” Mama yake akamuwahi. “Najua mwanzo ni mgumu. Lakini jitahidi kutafuta siku hata moja ya mapumziko. Itakusaidia kufikiria mambo mengine.” Akabaki amesimama akifikiria.

“Au bado unaona unahitajika sana?” Akaongeza swali kwa upendo maana Colins aliyekuwa naye kwa chakula cha mchana siye huyu. “Hakuna siku pale hapahitaji mtu wakusimamia. Walizoeshwa vibaya.” “Basi ongeza msaidizi ambaye mtakuwa mkipishana siku. Unahitaji kupumzika.” Baba yake naye akaongeza kwa kujihami. “Nafikiri nitafanya hivyo.” Akaelekea mezani kula. Lakini wakashangaa amepoa sana. Si kwa ukali, ila kama ametingwa na jambo. Wakaona wamuache tu.

Njia Panda.

Baada ya hapo akarudi chumbani kuoga akijiuliza kama ndio aende kwa Kamila au la! Alimuahidi kuwa atakuwa akimsubiria mpaka alale. Lakini Kamila ni kama amembadilikia fulani hivi! Akavaa na kuona amfuate tu chumbani kwake. Akagonga kidogo na kufungua kama kawaida yake lakini akashangaa chumba kimefungwa na funguo kwa ndani. Akajua ndio hakaribishwi tena.

Mara mlango ukafunguliwa akiwa anaonekana ametoka kitandani. “Ahadi ya kukusubiria mpaka ulele, bado ipo palepale.” Akacheka kinyonge akiwa amesimama mlangoni, asimpishe aingie. Akaangalia chini kama anayefikiria kitu, kisha akamjibu. “Nashukuru Colins. Lakini nafikiri nitakua sawa tu. Asante. Nenda na wewe ukapumzike.” Akabaki akimwangalia asiamini.

Akacheka kidogo ya kujibaraguza kisha akaongeza kiutani kama kumtoa njiani. “Usije nisahau asubuhi.” “Unajua siwezi, Kamila.” Akacheka kama kumridhisha lakini wazi alionekana amebadilika. “Basi acha na mimi nijaribu kulala, ili niamke na nguvu. Usiku mwema.” “Asante na wewe.” Akarudi ndani na kufunga mlango akiwa amemuacha amesimama palepale. Akapigwa na butwaa akishindwa hata kusogea, mwishoe akaondoka kurudi chumbani kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akiwa bado yupo kwenye sintofahamu, amepigwa na bumbuwazi, hajui awaze nini, ujumbe ukaingia kwenye simu ya Mike. Akaiwahi kwa haraka sana kujua safari hii Kamila anamwambia nini. Na pia ilikuwa njia rahisi sana kujua kinachoendelea moyoni kwa Kamila kupitia mawasiliano yake na Mike.

‘Mike mpenzi, umeondoka na wapangaji wetu wote na kuniachia majengo ambayo ni mazuri kwa nje, lakini ndani ni matupu. Umeondoka na Utulivu, Furaha, Amani na Upendo pia! Bora ungeniachia hao waliokuwa wapangaji wetu, isingekuwa ngumu kuanza. Lakini nakuahidi mwanzo mpya. Najua itakua ngumu, lakini sitaacha kujaribu mpaka nifikie ulipotaka nifike nikiwa na wote hao wanne wakiwa wamerudi tena kwenye maisha yangu, tuje kukutana tena kwenye maisha ya milele.’ Akaendelea kusoma.

‘Ulinipa vitu vilivyoonekana ni rahisi sana kutoa, kumbe sivyo ilivyo! Wengi wanafikiri kumiliki majengo mazuri na ya thamani ni kila kitu, lakini wanashindwa kumiliki wapangaji tulio miliki mimi na wewe! Daima utabaki wa pekee Mike. Milele nitakukumbuka.’ Ikawa kama kibao usoni kwa Colins. Akajua ile gomba ya asubuhi akiwa amemuahidi hatarudia tena, imemtisha Kamila, asijue na mengine mengi yanachangia.

Asuhubi.

Aliamka kwa kuchelewa sababu ya kulala kwa kuchelewa akiwaza bila kupata majibu. Akajitayarisha kwa haraka. Maana alamu ilimuamsha, akaizima na kurudi kulala. Akatoka kwa haraka, akamkuta Kamila  anamsubiria upande wa kulia chakula, wazazi walishaondoka.

“Samahani sana. Nimekuchelewesha.” Akanyanyua uso akamtizama kama ambaye alikuwa akichat kwenye simu yake kitu kisicho cha kawaida kwa Kamila. Alimfahamu kama yuko peke yake. “Hamna shida. Mimi nipo tayari.” Akasimama kabisa na pochi yake, kisha akarudisha macho kwenye simu. Akamuona anaandika kwa kifupi, na kuweka simu kwenye pochi.

“Umependeza Kamila!” Akacheka kidogo na kushukuru. “Asante na wewe umependeza kama kawaida yako.” Colins akamtizama na tabasamu, wakatoka hapo. Njiani akasikia simu yake kama imeingia ujumbe. Akamuona anatoa, anaendelea kuchat kwa muda mrefu tu kama ambaye hayupo hapo kwenye gari au kama hajali uwepo wa Colins . Akaanza kusumbuka rohoni kana kwamba si kawaida yao kuwa kimya garini, wakati hata jana yake waliendesha kimyakimya na yeye akiwaza yake.

Wakati mwingine alimuona anasoma kisha kufikiria kidogo, anajibu halafu kusubiria majibu kwa muda kidogo. Akaendelea hivyo mpaka wanafika kazini bado anachat. Kuuliza, hawezi. Akashuka na kumtakia siku njema kama anayeitupa tu. Hajamwangalia wala nini, ila kuzungumza huku akichukua kipochi chake na kushuka garini.

~~~~~~~~~~~~~~~

Siku ilikuwa nzito kwa Colins, hajui chakufanya. Hofu ya kupotelewa na Kamila ilikuwa bayana lakini akawa hajui chakufanya wala kujirudi. Akatamani kama angeendelea vilevile akiwa chini yake mpaka atakapokuwa tayari naye, lakini Kamila ameonyesha hatafanya hivyo tena. Alishamwambia hana sababu ya kufanya hivyo tena, anaendelea na yake.

Kazi zikaendelea mpaka kwenye majira ya saa tano na nusu hivi akamtumia ujumbe. ‘Naona naweza pata nafasi baada ya nusu saa hivi, tunaweza kutoka kwenye saa sita.’ Akabaki akisubiria majibu, kimya.

Akasubiri baada ya hiyo nusu saa akampigia. Wakati inakaribia kukatika akapokea. “Pole, simu ilikuwa kwenye pochi na mimi napika.” “Hamna shida. Uliona ujumbe wangu?” “Wala sikuwa na simu. Samahani. Acha niangalie.” “Hamna haja, tunaweza kuzungumza tu. Nimepata nafasi, tunaweza kutoka sasahivi tukaangalie magari.” “Nilishakwenda kwenye majira ya saa tatu hivi, palikuwa hakuna mambo mengi, ndio mzee Yusufu akaniruhusu muda huo ili nirudi mapema tusaidiane kwenye chakula cha mchana.” Colins akapoa ila akajikaza.

“Umefanikiwa?” “Kwa asilimia fulani.” “Unamaanisha nini? Hukupata gari unayopenda?” “Hapana. Mill amenishauri kuliko kununua gari ambalo nitakuja uza, tena pengine kwa hasara, wakati nikisubiria gari ninayotaka, ni bora aniazime yake nitumie mpaka yangu itakapokuja. Kwa hiyo amenisaidia kuagiza, akiwa ananipa yake nitumie. Nitakueleza vizuri baadaye. Ni sawa nikikuaga kwa sasa? Kuna kitu kipo jikoni napika.” “Hamna shida. Baadaye.” “Asante.” Simu ikakatwa.

“Mill tena ni nani huyo!?” Colins akabaki amekodoa macho akijiuliza mwenyewe. “Daah!” Akabaki hajui tena chakufanya. Akili ilishavurugika hata kazi tena zikawa haziendi.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa hakika kichwa kilishindwa kufanya kazi kabisa. Akaona bora atoke hapo. Akamwangalia mama yake alipo. Akashangaa kuwaona wapo pamoja na baba yake kwenye mgahawa. Akajua wamekutana kwa chakula cha mchana. Akajikuta anachukua funguo za gari na kutoka kuwafuata.

Hawakutegemea kumuona Colins. “Umejuaje tulipo!?” “App ya 360.” Akajibu akikaa ila wakamuona hayupo sawa. “Au nitawaingilia?” “Nimetaka kumtoa tu mama yako kwenye yale mazingira ya kazini kwa muda mfupi, wala hakuna cha peke yetu. Agiza chakula.” Walimjua Colins kwa chakula.

Akaagiza kinywaji na chakula wao wakiendelea kula taratibu. “Vipi kazini mama?” “Naendelea hivyohivyo.” “Si uje ufanye kazi pale. Nitakupa uongozi wa manesi wote pale. Na nitakulipa vizuri.” Baba yake akamwangalia kama aliye hamaki kwa hilo. Ila mkewe kimya. “Na sio kwamba nakupa kazi kwa kukuonea huruma, ni kwa sababu nataka ujuzi wako na kuwa na mtu wangu wa karibu pale. Wana uzembe mwingi inabidi kuwafuatilia kila wakati.”

Siwezi kuacha kazi kule kabla sijastaafu. Nitapoteza mafao yangu. Nitakua sawa.” “Chukua likizo bila malipo huku ukisogeza siku mpaka ustaafu.” Wakamuona amenyamaza. “Na hutakuwa ukikimbia mama Coly.” Mumewe akawa kama amemsoma mkewe. “Nataka Connie akimaliza shule yake kabisa, akiwa daktari kamili, akiwa anapita round na mimi niwepo. Ndio ndoto zangu, jamani! Mwanangu amejitahidi na kujinyima kweli. Nataka kujivunia kiziwanda wangu akiwa anapita pale, na mimi nipo. Kuondoka sasahivi nitakuwa nakimbia na kumpa yule mama nguvu. Hivyo hapana.” Wakawa wamemuelewa.

“Nimekuelewa mama.” Akakubali akionekana ana mawazo. Akapotelea mawazoni. Mama yake akajihisi amefanya upendeleo. “Ila naweza nikachukua likizo hata ya miezi 6, nije kukusaidia kupaweka pale sawa, kisha nirudi kazini kwangu, ili Connie na yeye anikute.” Akamwangalia kama aliyemtoa mawazoni.

“Unataka kufanya kwa kuwa unapenda au kwa kunihurumia? Maana mimi nitakua sawa tu. Nataka wewe uwe na mazingira mazuri nyumbani na kazini.” “Ni kwa kutaka kwangu mwenyewe.” Colins akabaki akimwangalia. “Nini sasa?” “Si umetoka kunikatalia wewe, ukitaka kumuunga mkono Connie na si mimi?” Akaanza kucheka. “Umejishitukia na kuhukumiwa?” Akamuuliza na kufanya wote wacheke.

“Samahani Coly, mwanangu.” “Usijali.” Kisha akatulia. Wakaangaliana hao wazazi wawili. Kinywaji chake kikaletwa. “Nikija utanilipa kiasi gani?” “Kikubwa mpaka utakataa kurudi Muhimbili.” Wakacheka sana. “Muulize baba jinsi nilivyobadilisha malipo ya wafanyakazi. Madaktari pale walikuwa wakizembea kuja sababu ya pesa ndogo, lakini sasahivi wanapigania shift za pale.” “Ni kweli.” Mzee akaafiki.

“Hongera Coly. Umefika mbali kwa muda mfupi!” “Lakini havina raha! Havina raha kabisa. Kila nikikamilisha jambo vizuri, nategemea kujisikia hali fulani, lakini sipati. Nazidi kujisikia…” Akasita. Kama anayefikiria. “Mpaka sioni maana ya maisha!” Akajikuta akizungumza cha moyoni mbele ya wazazi wake. Kimya kwa muda wote wakijua maisha yamekosa maana sababu ya kumpoteza Jelini.

“Labda ukihamia kwako, ukawa na uhuru wako. Na Kamila anaweza saidia kukuchangamsha. Anaonekana ni biti mzuri, Coly. Mpe nafasi.” “Amekataa kuhama na mimi. Ameamua kubaki na nyinyi pale.” Wote wakashangaa.

“Kamila!?” “Si ndiye tunayemzungumzia au?” “Nahisi kuna kitu hakijakaa sawa Coly. Kamila niliyezungumza naye mimi jana, alikuwa yupo tayari kukusubiria kabisa!” Colins akamtizama na kukunja uso. “Kamila anaonekana anakupenda, ila anajua bado moyo wako upo kwa Jelini.” Hapo akanyamaza. Chakula chake kikaletwa, akaanza kula.

“Jelini anaolewa Coly. Usije kosa bara na pwani.” Mama yake akaongea kwa tahadhari. “Nahisi nimeshachelewa.” Akajibu tu hivyo na kuendelea kula akionekana amebadilika kabisa. Wakaona wamuache. Akala kwa haraka, akaondoka na kuwaacha hapo.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati yupo na sitaki nataka, dunia bado inaendelea kuzunguka. Haimsubiri yeye. Kamila ameshapata ujumbe wake, ameamua kuendelea na yake. Mill tena ni nani!? Swali lilobakia kichwani kwa Colins, kazi haziendi tena.

INAENDELEA.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment