“Wamenifungia
sehemu kubwa sana inayoniingizia pesa, aisee! Nipo hatarini kufungwa na
hoteli yangu pia kufungwa. Na bado natakiwa kuwalipa fidia! Wameibua pressure
ambayo nilijua imepona! Sasahivi naishi kwa madawa. Sijui kama nitapona!” “Sasa
huu sio wakati wa kukata tamaa.”
Colins akaendelea.
“Mwambie
wakili wako, anitafute mida jioni. Nina ushahidi mpya wakumsaidia
kushinda kesi. Na hili usizungumze na mwingine yeyote, ili kuwashitukiza washitaki
wako. Lazima kujipanga upya. Ila nakuhakikishia safari hii utashinda kama
ukifuata ushauri wangu.” Akaibua tumaini jipya. Colins akamuweka sawa
na kukata simu.
~~~~~~~~~~~~~~~
Safari ya kwenda kazini kwa wote ikaanza. Kimya njiani
kila mmoja akiwaza lake. Kamila ndio hakuthubutu kuanzisha mazungumzo yeyote
yale. Alishamsikia akiunguruma asubuhi hiyo kwa wazazi wake, kama simba,
akajiweka pembeni. Ila mazungumzo kati yake na wazazi wake yakaendelea
kujirudia kichwani mwake.
Vile alivyoendelea kumlilia Jelini. “Hatakuja kuwa na
nafasi ya msichana mwingine moyoni mwake. Hapa nitajichelewesha na kuendelea
kujiumiza. Bora nijiachie.” Kamila akaendelea kuwaza.
Akakumbuka sifa za Jelini alizoambiwa na mama Colins,
alichoona ni cha tofauti na yeye ni ile hali ya kusema anajituma sana
kwenye biashara zake na amefanikiwa. “Labda ndio maana anashindwa
hata kunifikiria! Ananiona nitakuwa tegemezi daima. Sifananii na Jelini mchapakazi
na mwenye maendeleo.” Akaendelea kuwaza.
“Lazima
kubadilika. Hapa sina changu.” Akaazimia moyoni akiendelea kujipanga na
kutafakari juu ya kuchukua hatua. Yeye Colins alikuwa mbali kimawazo. Kimya.
Kama ambaye yupo peke yake garini. Akamuona ni kama anamipango mingi mawazoni,
akaona bora hivyo. Pakatulia.
Wakati wa Kujenga.
Kwenye majira ya saa nne, akaingia baba yake ofisini
kwake. “Kwema?” “Nataka kuwepo hapa kukuongezea nguvu, ukiwa unamalizana
na kina Simba kwenye ile nyumba ya Kigambini. Najua wamejipanga. Sitaki
liaharibike jambo, tumalizane nao kwa haraka.” “Nashukuru.” “Mambo yanaendaje
lakini?” “Mwanzo ulikuwa mgumu. Uzembe mwingi. Lakini naona sasahivi tunakwenda
sawa. Kila shift nimepata watu. Naona sio mbaya.” Baba yake akatulia
kidogo.
Akamuona kama kuna kitu anataka kuuliza ila anasita. “Ni
nini?” “Nataka kukuuliza kitu, lakini sitaki kukutibua.” Colins akamwangalia akaona
anyamaze. Kisha akafikiria tena akaona amuulize tu, akakuta ametulia tu
akimwangalia.
“Ulitaka kuniuliza nini?” “Kwa yote uliyofanya hapa, na kwa
kiasi hiki! Kweli hufurahii hata kidogo?” “Hizi ni ndoto
zako baba.” “Sawa. Lakini hata katika hili, kweli hujivuni hata kidogo!?”
“Kidogo.” Baba yake akacheka.
“Hukunitendea haki baba.” “Nia yangu ilikuwa nzuri
Colins.” Akanyamaza. “Ila nikwambie kweli tu. Japokuwa imeua mahusiano yetu,
mimi na wewe, lakini kibinafsi najivunia sana.” Colins akamtizama! Ila akaona
amuache tu.
Ila mzee
akashindwa kujizuia tena. Akaendelea kwa tahadhari. “Umepita matarajio yangu.”
“Naona hata ya Simba.” Wakacheka. “Naona yeye na familia yake ndio zaidi.
Hawakukutegemea kabisa! Wapo kwenye mshituko ambao nadhani hautakuja
kuisha. Utabaki kuwa usiku wa giza nene.” Angalau wakazidi kucheka.
Mara sekretari akapiga kumwambia ana wageni. “Waruhusu
waingie.” Mzee akajiweka sawa. Wakaingia. Chris, mama Simba na mumewe.
Wakasalimiana, lakini wazi ni ile ya salamu ya bora yaishe. Chris
alikuwa kwenye heshima zake zote kama anayeomba jambo lisiharibike
hapo. Na yeye Colins akajifanya kama hamjui! Kumbe alishampa vitisho
vyakutosha, hapo ameadabika.
Wakamkabidhi kabrasha. Colins akafungua na
kuanza kusoma. Kila kurasa aliomaliza alimkabidhi baba yake na yeye asome.
Wakaridhia mpaka kiwango cha pesa. Akajua Chris aliwaweka sawa. Hapohapo bila
ya kuchelewa akawaandikia hundi ya pesa yao tasilimu. Tena kutoka kwenye
akaunti yake binafsi wala si ya kampuni. Akawakabidhi wasiamini kwamba Colins
ndio anakiwango hicho chote cha pesa!
“Tumemalizana ramsi kwenye nyumba ya Kigamboni. Mwambieni
Love, haruhusiwi kuonekana kule. Mizigo yake yote nitamtuma dereva
ailete nyumbani kwenu. Muwe na siku njema.” Wakamtizama kama wammeze, ila
walikuwa na mengi. Wakatoka hapo kwa haraka, ili kutoa hiyo pesa benki ya
kuweka dhamana, wakamtoe Love huko lupango, wamkimbize hospitalini.
~~~~~~~~~~~~~~~
Wakamuacha hapo na baba yake. “Hongera kwa kununua
nyumba.” Colins akacheka na kunyamaza. “Nina ushauri.” Colins akamwangalia.
“Naruhusiwa?” “Lini hilo limekuzuia?” Mzee akacheka na kutingisha kichwa. “Ni
nini?” “Kwa sasa, wakati ukisubiria nyumba yako, nashauri kabla nyumba ya Kigamboni
hujaifanya ya biashara, ukaishi huko ili uwe na uhuru.” Hilo
likawa si jambo baya. Lakini akamuona anafikiria.
“Vipi?” “Naona si wazo baya. Ila namfikiria Kamila!” “Kwa
nini usimpe nafasi? Yule binti anakupenda, Colins.” Colins akashangaa sana.
“Umejuaje?!” “Amemwambia mama yako.” Colins akanyamaza. “Mpe nafasi. Anaonekana
ni binti mzuri. Kuwa naye karibu bila kuanzisha mahusiano ya kimapenzi kwanza, ili
kumchunguza na kumfahamu kwa karibu.”
“Huwezi jua pengine kuna kitu kizuri kinaweza
zaliwa. Mungu hawezi kukuacha moja kwa moja, na Jelini hawezi kuwa mtu wa mwisho
kukupenda. Na kabla sijakupandisha hasira, ukanikatalia, naomba ufikirie.
Ni hilo tu.” Mzee akaondoka.
Wakati Wakuvuna Kwa Kila Aliyepanda Lake.
Hawakupishana sana na wakili wa yule mwenye hoteli na Peter
mwenyewe. Kweli alionekana mgonjwa. “Nashukuru kutusaidia.” “Acha kwanza muone
ushahidi wenyewe.” Akawawekea ile video na kuamsha tumaini kubwa kwao.
Akazungumza naye jinsi ya kujipanga kutetea ile kesi. Akampa madhaifu
yake kama alivyoambiwa na Chris.
“Tafadhali jipange na kuwa na hoja za msingi. Wakili
unayeshindana naye anajulikana ni mzuri, na mwenzio anajua kujipanga.
Ukijiweka sawa, kwa hakika kwa huu ushahidi utashinda tu.” Kisha
akaongeza.
“Na sasa pasipoe. Kwa haraka sana wahi mahakamani
sema unaushahidi mpya, unaomba waitishe tena kesi. Najua wewe unajua zaidi.”
Akamtia morali haswa, lakini lengo ni Love asikae sana uraiani.
Yaani awe anatolewa kwa kumkamilishia lengo lake yeye Colins.
Kutoa familia ya Simba kwenye ile nyumba ya Kigamboni,
ibakie kuwa yao kina Komba, kisha arudi jela sasa kwa shitaka la jaribio
la kutaka kuua. Ambako huko atakuwa na shoga yake Kemi, mpaka
kifo. Wakili akatoka hapo kama akimbie.
Kakumbuka Shuka Pashakuchwa.
Ilipofika mida ya usiku, akapata ujumbe kwa Kamila. ‘Mimi nipo
tayari, utakapokuwa tayari unijulishe tafadhali, ili nisogee garini.’ Akaona ampigie. “Leo umekua kimya!” “Kuna
muda nilikuletea chakula nikaambiwa umetoka kwa chakula cha mchana.” “Oooh
yeah! Baba alishindwa kwenda kula na mama, ndio akaniambia niende, ili tusimuache
peke yake. Nahisi nimekuwa na mambo mengi kwa karibukaribu nikasahau
kukutaarifu.” “Ingekuwa mimi ni Jelini, wala
asingesahau kuniaga. Sina maana kwake kabisa!” Kamila akawaza na kunyamaza.
“Kamila?”
“Nipo, nakusubiria huku jikoni.” “Kwa nini usije huku?” “Huku pia nipo tu sawa.
Hamna shida.” “Basi niseme naomba uje kuna kitu nataka kukwambia.” “Sawa. Nakuja.” Wakaagana ila akamuhisi amekua mzito, sio kawaida yake.
Moyo Uliokata Tamaa.
Baada ya muda akamuona amesimama mlangoni. “Karibu.”
Akaingia na kukaa kama aliyepo mbele ya hakimu. “Una ratiba yeyote ile baada
ya hapa?” Akatingisha kichwa kukataa. “Basi naomba nisindikize Kigamboni. Kuna
kitu nataka kukuonyesha kisha tuzungumze.” Akakubali akiwa amepoa haswa.
Safari ya Kigamboni ikaanza akiwa ametulia haswa. “Upo
sawa?” “Ndiyo.” Akajibu hivyo tu na kutulia. Akaona amuache. Safari ikaendelea
mpaka kwenye hilo Jumba lililokuwa likimtoa roho Love.
“Ni pazuri!” Akasifia Kamila akiangaza macho lakini si
kwa kushangazwa kama aliyezoea aina hiyo ya mazingira. Colins hakushangaa
sana kutokana na sifa alizosikia za Mike. Akahisi alikuwa akiishi kwenye
aina hizo za mazingira.
Alishaandaa mafundi kuanzia asubuhi alipoinunua hiyo
nyumba kubadili vitasa vya nyumba nzima. Hapo anafika mafundi wanamsubiria
malipo na funguo mpya.
Akamalizana nao ndipo akaingia sasa ndani. Akamzungusha
Kamila kila mahali, akifuata tu kwa nyuma akiwa anamuonyesha mazingira yote.
Kisha wakarudi sebuleni. “Naomba tukae kidogo.” Akakaa.
“Sasa kwa sababu hapa pamekuwa kwangu rasmi. Sio
pote, inamaana na familia. Na kwa sababu nyumba yangu bado anatumia yule
mpangaji kama nilivyokwambia mwanzoni, hata baba ameshauri nihamie tu hapa kwa
uhuru.” “Hongera Colins.” Colins akacheka akimwangalia.
“Namaanisha. Hapa ni pazuri na kweli utapata uhuru.”
“Sawa. Lakini nakukaribisha na wewe. Tunaweza hamia wote.”
Akabaki akimtizama kwa muda kisha akamuona amekunja uso na kuinama. Colins
hakutegemea.
“Eti Kamila?!” “Unahamia lini?” “Mapema iwezekanavyo.”
Akamjibu huku akijaribu kumsoma. “Mimi naona nitabaki tu pale nyumbani.”
Colins alishituka, hakutegemea! Kabla hajafikisha taarifa moyoni, Kamila
akaongeza.
“Ila naomba msaada wako.” Colins akabaki akimtizama,
ashabadilika rangi. “Kuna sehemu mbili tatu najua wanauza magari. Naomba
ukipata nafasi unisindikize nikanunue gari ili na mimi nipate usafiri wa kunisaidia hapa mjini. Nikipata
kama ile gari aliyokuwa amenipa Mike, ningependelea ile zaidi. Vinginevyo
nitanunua yeyote tu kwa sasa wakati nikiagizia ile, ikija naweza fanyia hii ya
sasa biashara au nikaiuza.” Colins akapoa! Hakutegemea kama atakataa
kuhamia naye hapo. Maana tokea mwanzo ombi lake ilikuwa akihama,
basi ahame naye.
Kulikoni!
Likabakia swali kwa Colins akiwa amenyongea na hisia za kukataliwa
zimemjaa. Akatulia kwa muda, akajikaza. “Sawa. Sioni kama kuna tatizo.”
Kamila akanyamaza ila na yeye kwa kuumia. Hata hakumbembeleza! Akazidi kuamini
yupo sahihi kwenye maamuzi yake. Si kwamba Colins anamuhitaji, ni kumsaidia
tu.
Wakajikuta wote wametulia hapo sebuleni, kwenye madhari
nzuri ya kuvutia, ila mawazo hayopo hapo. Mwishoe Colins akasimama. “Naomba
nisubirie kidogo, tutaondoka muda si mrefu.” Akaondoka hapo akiwa mwekundu
haswa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akakusanya vitu vya Love na kuviweka chumba kimoja.
Akagundua Love alimkusanyia yeye vitu vyake vyote na kwenda kuvitupa chumba
kingine. Wala hakuwa amempangia. Akaangalia na kuumia sana. Akiwa anaangalia
chumba alichokuwa akitumia Love ambacho ndio Master bedroom, akagundua
baadhi ya nguo ngeni kwake, za kiume! Akazidi kuumia. Akajua ni
kweli Festo alikuwa akija kulala hapo.
Swali lakumuumiza likabaki je, alikuwa akiishi naye
hata yeye alipokuwa hapo au la! Hakuwa akikumbuka. Akazidi kukasirika
kadiri alipogundua upo hata mswaki na viatu kabisa! Kama ambaye alikuwa akiishi
hapo! Akatoka kwa hasira, akarudishia mlango na kuamua kutoka kabisa hapo.
Akamuita mlinzi. “Kesho watakuja watu wakusafisha hapa na
maagizo ya kukusanya kila kitu kwenye kile chumba. Waweke kwenye maboksi na
kuacha hapo nje. Dereva atakuja kuchukua.” Hilo likakaa sawa. Akamwambia Kamila
waondoke.
~~~~~~~~~~~~~~~
INAENDELEA.
0 Comments:
Post a Comment