Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 26. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 26.

Akiwa ameanza kukata tamaa ya kurudi tena kwa Colins, maana hata ujumbe hakujibu, akasikia hodi mlangoni kwake. Akamkaribisha akijua wazi ni yeye. Akaingia. “Nilijua utakuwa umeshalala!” “Hapana. Nisingelala bila ya kuhakikisha wewe umelala kwanza.” Akamsogelea pale kitandani. Akakaa

“Asante kujali Colins.” Akacheka taratibu akimtizama lakini wazi alionekana ametingwa. “Ningeelewa kama ungehitaji muda wa peke yako.” “Hapana, ahadi ni deni. Nisingeweza kukuacha tu hivihivi.” Hiyo haikusikika vizuri kwa Kamila. “Kwamba yupo hapa kama kutimiza wajibu, si kupenda kwake!” Kidogo ikamsumbua. Ila akajikaza kama kawaida yake, Kamila hataki makuu.

“Pole. Sikujua kama ndio ilikuwa mbaya hivyo!” “Ilikuwa mbaya zaidi hata ulivyosikia. Ilikuwa mbaya sana. Na nilipokuja kurudiwa na akili ndio nikajikuta nimepoteza kila kitu pamoja na Jelini. Nilijawa na hasira, uchungu na majuto kwa muda wote huo mpaka wewe ulipokuja kwenye maisha yangu.” “Kweli Colins!?” Kwa jinsi anavyomchukulia, ikamuwia ngumu kuamini.

“Oooh yeah! Nilikuwa na hali mbaya sana. Muda mfupi uliopita nilitaka kujifungia na kuzidi kukasirika, nikakumbuka wewe upo na unanisubiria. Ikabidi nitoke. Lakini kama si hivyo, hayo ndio yalikuwa maisha yangu. Nakaa tu chumbani nikizidi kuumia. Kwahiyo nazidi kuamini Mungu amekuleta kwenye maisha yetu ili kunisaidia mimi.” Kamila akafikiria, hajui afurahie au la!

“Mwenzio kuna mtu aliniambia hivi. Sihitaji kupata majibu yote kwa wakati mmoja. Hatua ndogondogo kama mtoto mdogo.” Colins akacheka akijua anamzungumzia yeye. “Nimefuata ushauri wako. Sasa hivi mwenzio naishi kwenye familia ya baba na mama. Na wananikarimu. Lakini wakati ule napita pale pagumu na wewe unanishauri hivyo, nilikuwa sioni mwanga. Lakini ona nilipo na wanao nizunguka.” Colins akatulia akimwangalia kwa kutulia.

 “Kwa hiyo na wewe jipe muda Colins. Mungu atakurejeshea vile vizuri ulivyopoteza, kama Ayubu.” Colins akacheka. “Kumbe unajua bibilia!” “Sio kwamba ni mkristo mzuri sana, lakini tulikuwa tukienda kanisani na Mike, halafu wakati mwingine tunaomba pamoja. Halafu usisahau mimi mwenzio mtoto wa masista.” Colins akazidi kucheka akimtizama.

“Kwa hiyo usiogope, na usisahau hata siku moja kuwa Kamila yupo. Najua mimi si Jelini, na sitaweza kuwa yeye kama ulivyoniambia juu ya Mike. Lakini ujue mimi nipo Colins. Na sina nipokwenda.” “Asante Kamila.” Wakaangalina na kucheka taratibu Kamila akainama kama kwa aibu.

“Acha niweke movie tuangalie wakati ukitafuta usingizi.” Akaweka na kurudi kukaa. “Jilaze hapo kwenye mto, niku masaji miguu.” Colins hakutegemea, akabaki kama amepatwa na ububu. “Nina uhakika utapenda, itakufanya utulie kabisa. Lala, nipe miguu.” Akasisitiza na kumfanya ajilaze chali.

Akatoka kwenda kufuata lotion yake, Colins akimsindikiza kwa macho akiwa na nguo yake ya kulalia ila ya heshima tu. Wakati anageuka, na yeye akarudisha macho kwenye luninga kwa haraka.

Akakaa kitandani kabisa. Akamnyanyua miguu taratibu akimtizama. Akaiweka mapajani kwake. Akampapasa kwanza taratibu. Juu mpaka chini. Mikono laini na moto ya Kamila ikamsisimua kiajabu sana.

Akajikaza. Akaanza kumvuta vidole vya miguu taratibu. Akafanya hivyo kwa vyote, tena utaalamu wa namna yake, ulioamsha raha kwa Colins. Ndipo akampaka sasa hiyo lotion yake maana hakuwa na mfuta ya masaji. Alimpaka bila papara, taratibu, kisha akaanza kumchua. Juu mpaka kwenye nyayo na katikati ya vidole. Kwa hakika akaanza kumchanganga Colins.

Hisia zilizokuwa zimekufa kwa muda mrefu akashangaa zinaanza kufufuka. Ikawa Kamila naye kama anayemfanyia makusudi vile! Aliendelea na wakati mwingine alitumia kucha, gafla mzee akasimama! Colins alishituka na kuvuta mto, akajiwekea juu kama kujiziba. Kamila akajifanya kama hajaona. Akaendelea na yake, akiwa ameinamisha kichwa, macho kwenye anachokifanya, akiendelea.

“Asante.” Akamsikia akishukuru. Akamwangalia. “Inanifanya nitulie!” “Ndio vizuri. Lala.” “Na wewe?” “Mimi bora nijue upo pembeni yangu, nitalala tu.” “Unauhakika? Maana kwa hivyo unavyonifanyia, ni kama unanibembeleza!” “Natamani na mimi niwe faraja yako Colins!” Hapo anaongea vidole vyake vinavuta vinyweleo vya miguu taratibu.

“Umeyabadili maisha yangu Kamila. Amini umekua msaada kwangu zaidi nitakavyoweza kukiri kwako.” Maneno yake na moyo wake vilimfanya Kamila kutosadiki kwa asilimia kubwa sana. Akanyamaza na kuendelea na hiyo masaji.

 Akamuona anaanza kulegea ile ya kunogewa kabisa. Akajua amemwamsha kupitiliza. Alichoshangaa na kumuumiza ni vile alivyoweza kujitoa pale. “Nashukuru, lakini naomba nitumie choo, tuje tulale. Na wewe upumzike.” Hakutegemea! Akatoa miguu yake taratibu, suruali ikiwa imemtuna haswa kwamba yupo juu, lakini akatoka na kwenda kutumia choo, hapohapo chumbani. Akamsikia amefungulia maji ya kwenye sinki kama anayeosha uso. Kimya kwa muda.

Kamila akajirudisha kulala kwa unyonge. Hakutegemea katika hali ile na bado akamuacha! Alitegemea mengi hapo, hata kama si mapenzi basi hata kiss za nguvu! Yeye mwenyewe alishaanza kuloa. Kitendo cha kujitoa hapo mikononi mwake na mautundu yote aliyokuwa akimfanyia, ikamuumiza na hapo ndipo alipojihakikishia kwa hakika.

“Huyu hakuna kitu jitakuja kumfanyia akanifurahia kama Jelini.” Akajinung’unisha. Akavuta shuka na kujifunika mpaka shingoni, akiwa ameficha kabisa nguo nzuri ya kulalia aliyokuwa amevaa. Kisha akajivuta pembeni.

Baada ya muda akamuona anatoka. Yupo vilevile, jamaa kagoma kushuka. Akarudi kujilaza hapo pembeni yake. “Pumzima.” Akatingisha kichwa kukubali. Akamuona jinsi alivyo nyongea.

Akajisogeza karibu yake akamgeukia na kumvuta mkono. Wote wakalala ubavu ila wamegeukiana. Aliutoa huo mkono ndani ya shuka. Akaushika vizuri. “Nashukuru kwa masaji. Nimeifurahia sana. Lakini Itabidi nitafute siku maalumu, na sehemu nzuri utakayonifanyia. Lakini si hapa kwa wazazi na si leo.” Kamila akamwangalia akitilisha huruma.

“Unanielewa lakini?” “Ndiyo.” Akamtizama kwa muda kama kutaka uhakika. Wakiwa wanaangaliana kwa karibu kabisa. “Nimekuelewa Colins.” Akarudia kama kumuaminisha ila akajua hajaridhika.

“Wewe ni msichana mzuri sana, na ni mwema wa namna yako, Kamila. Sitaki kukuchanganya na mambo yanayoendelea sasahivi. Haustahili kuchanganywa na chochote, zaidi hizi fujo zinazoendelea kwenye maisha yangu. Si sawa kwako. Tafadhali naomba unielewe, japo najihisi nakaribia ukingoni. Patatulia tu. Sawa?” Akatingisha kichwa kukubali.

Akambusu ule mkono aliokuwa ameushikilia. Akamsikia akivuta pumzi kwa nguvu. Akajua na yeye hali ilishakiwa ya tofauti, anajaribu kutulia. Akamuhurumia, asijue chakufanya.

Ila hata hilo busu akalithamini japo ni la mkono tu. Akamsikia akishukuru. “Asante.” “Wewe ndio nikushukuru. Nitakuja kukwambia ni kwa nini nakushukuru na utaelewa tu. Ila hiki ulichonifanyia hapa, nilikata tamaa. Umenirudishia tumaini. Asante.” “Karibu.” Kisha akajigeuza kumpa mgongo, akalala. Akiwa amekubali matokeo.

ASUBUHI.

Asubuhi ikamkuta hapo kitandani kwa Kamila. Safari hii hakukurupuka vibaya. Akatulia hapo kitandani akitafakari ya jana. Akamtizama Kamila alivyolala pale. Taa ilikuwa ikiwaka. Safari hii amemgeukia. Akamtizama kwa kutulia akiyatafakari maisha.

“Unaweza kuta katika yote, Kamila ndio mke Mungu aliyenitayarishia tokea mwanzo!” Akawaza ila safari hii kwa hofu kidogo. Akamtizama vile alivyolala vizuri na kuvutia. Kamila ni mzuri, ila hisia zipo kwa Jelini!

“Kama kweli ni wangu kwa nini bado najihisi hivi kwa Jelini!” Akawaza akijua historia imeshajirudia. Alichokifanya kwa Jelini, ndio amekifanya kwa Kamila. Ila hajui chakufanya. Colins si mchanganyaji. Akianzisha jambo na mahusiano, husimamia mpaka mwisho, ila huwa ina mcost/mgarimu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Jelini alimkuta kwenye mahusiano magumu na Love, na yeye Kamila amemkuta kwenye mahusiano mazito, yaliyojaa penzi lililo katiliwa, la Jelini. Wote wanapendana, ila mazingira yamewakatalia kuwa pamoja. Colins hawezi kujisaidia, alichojisikia kwa Jelini, hajawahi kujisikia kabla. Jelini alikuja kama kumtoa kwenye jua kali na kumuweka kivulini. Kabla hajatulia kwenye hilo huba, wakamrudisha tena kwenye fukuto. Bado moyo unatamani alicho onjeshwa na Jelini.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu huku akimtizama Kamila. Akajikuta amepotelea mawazoni akimtizama. Bila kutarajia akajikuta na kumbusu kwenye shavu la juu, maana alilala ubavu. Akajishangaa, ila kama akafurahia! Akamtizama na tabasamu, kisha akatoka kitandani.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati anatoka chumbani kwa Kamila, akasikia shuguli jikoni, akajua na mama yake atakuwepo. Akamfuata. “Bado Kamila anaogopa tu?” Akacheka sana akijua anamkejeli. “Wala sitakujibu mama. Umeamka salama?” “Tumalize kwanza yako.” “Hapana mama. Wewe ni mchokozi tu.” “Mimi tena! Sio kwamba najali? Nataka kujua hali zenu!” “Huna lolote.” “Au na leo umepitiwa tena na usingizi?” “Mimi naona wewe unaendelea vizuri.” Akaondoka hapo mama yake akicheka.

“Mchana nakuja tule wote chakula cha mchana.” Akamsikia akiongea huku anapotelea koridoni. “We Colins! Si unakikao na kina Simba wewe? Tafadhali naomba malizana nao, kutulie. Mimi sitaki kuja kudaiwa usiku usiku.” Akarudi.

“Nitamalizana nao mama, usiwe na wasiwasi. Nimejiandaa. Sawa?” “Sitaki maneno maneno ya yule mama mpaka kazini, akilalamika tunawadhulumu haki zao.”  “Kila kitu kitakuwa sawa. Naomba muda nirekebishe. Na hatuwezi kuepuka kulalamika kwao. Hawa watu walizoea kuchota pesa pale hospitalini bila ya nyinyi kujua wala kufuatilia. Wakajinufaisha watakavyo. Sasa, sasahivi nimewadhibiti kwa pesa waliyozoea kuchota kiurahisi, nilazima watalalamika tu. Ila nakuahidi patatulia.” Akamuona amenyamaza.

“Kwa hiyo nije tule wote?” Akamuuliza kwa kumbembeleza. “Nishakuwa na mipango na mama yako.” Akasikia sauti ya baba yake. “Hiyo mipango yako ...” “Ya chakula cha mchana, Colins. Naomba usiingilie.”  Colins akacheka kwa kusikitika.

“Mbona kama nahisi umedandia mipango yangu?” “Muulize mama yako kama jana usiku sijamwambia kama leo nakwenda kula naye. Labda akatae sababu anakupendelea wewe.” “Wewe bwana hutabiriki! Utanifanya nikose ofa ya Colins, halafu uje uniambie umepata mgonjwa wa dharula.” “Mama Colins!” “Si ubishe sasa? Maana na juzi ilikuwa hivyohivyo.” “Leo nimekuapia, lazima. Sasa wewe usikate tamaa. Na umeona jana nimekutoa kabisa na simu nikazima. Siku nzima mpaka asubuhi mimi na wewe tu. Na wewe bisha.” Kamila akasikia wakimgombania huyo mama.

“Wewe kuwa na msimamo. Acha kuyumbishwa na Colins.” “Au tumuulize mwenyewe anataka kwenda na nani!” “Acha ukorofi Colins!  Mimi nilishamuwahi.” “Sasa wewe si umtoe dinner?” “Muulize kama sina miahadi naye na ya dinner huyo.” “Baba! Kwamba unamtoa lunch na dinner!?” “Si upo naye hapo, muulize abishe.” “Sasa kwa nini!?” “Hee! Wewe vipi Colins? Mke wangu, pesa ninayo. Kwa nini kunipangia?” Colins akachoka kabisa.

“Sawa baba. Basi kesho.” “Sasa hapo inategemea na kitakachozaliwa leo.” “Kwamba na kesho tena unataka kumtoa mchana na usiku?!” “Wewe una wasiwasi gani?” “Basi mimi kule nakufukuza kazi.” “Aliyekwambia sitakuja kwenye kliniki zangu ni nani? Wewe tulia. Pengine kesho utapata kimoja wapo. Au unasemaje mke wangu.” “Mmmh!” Wakamsikia anaguna.

“Mama mwenyewe hana imani na wewe!” “Hiyo imani itarudi tu. Wewe nipe siku ya leo nitengeneze.” “Basi bwana baba. Ila ikitokea unapatwa na zile dharula zako, naomba mimi ndio niwe wa kwanza kujulishwa, niende nikale naye.” “Sasa hiyo ndio akili.” Mzee akasikika kufurahia hilo.

“Nilijua tu. Hana uhakika huyo! Ikifika mchana lazima nitamsikia yule msaidizi wake akinipigia simu, amepatwa dharula yupo theater. Kuna mgonjwa mahututi anatakiwa upasuaji wa haraka. Hapo kuja kumsikia tena mwenyewe ni jioni!” Mama Colins akasikika.

“Wewe kuwa na imani bwana! Hiyo ni inategemea. Kwanza haitegemei.” “Si tupo hapa. Tutaona.” “Wewe usijali bwana. Mchana, utaniona.” Mama Colins akanyamaza, Colins akakubali kushindwa. Ila nia yao ni kumfurahisha tu huyo mama. Alishanyongea kwa muda mrefu.

Njia Ya Muongo, Huwa Fupi.

Alipofika tu chumbani kwake kitu cha kwanza akafungua laptop yake kuona kama rafiki yake alimjibu. Akakuta alimjibu na ametengeneza ile video. Haraka sana akaifungua. Akaitizama na kushangazwa mno. Ilionekana kama mchana! Mpaka kitu kilichotumbuzwa ndani ya glasi ya juisi ya embe aliyopewa Jelini kikaonekana bila shida.

Alifurahi Colins akashindwa kujizuia. Akaanza kupiga kelele akishangilia. “Yes! Yesss!” “Ni nini!?” Mama yake akamfuata. “Mungu anawalipa watesi wangu. Na safari hii hakuna wa kukimbia hukumu.” Mzee naye akasogea mlangoni.

Akawasimulia jinsi alivyomuita Jelini kwa mazungumzo, lakini Love na Kemi wakamuwekea sumu. Hao wazazi walishituka! Hawakuwa na taarifa. “Haiwezekani Colins!” “Yaani kesi ilishindikana sababu ya ushahidi tu. Halafu wakili wao akawafundisha na kumuwahi mwenye hoteli eti wao ndio walipwe! Badala yake yaani wao ndio wakaishia kuwa wahanga na washindi. Sasa kuna mtu amenisaidia kunitolea giza, angalia walichofanya.” Wote wawili wakasogea kwenye laptop yake. Wakaangalia mwanzo mpaka mwisho.

Mama Colins akajikuta machozi yakimtoka, mzee amehamaki, macho mekundi. “Sikujua kama huyu binti wa Simba ndio mbaya wa kiasi hiki!” “Ila atalipa. Hakika atalipa. Kila siku atakayoishi hapa duniani, atajuta kuingilia mapenzi yangu na Jelini. Ni heri angefanya chochote lakini si kunitenga na Jelini. Hakika atalipa.” Kamila na yeye akasikia vile anavyoapa kwa uchungu.

“Sasa si unakwenda kuwapa pesa ya kumtolea dhamana? Atalipa vipi?” “Baba!” Colins akaita na kucheka kwa masikitiko. “Yaani hii siku ya LEO na JANA, nilishaziona kabla yake. Nishaziishi na nishajua chakufanya. Nikikwambia nimejipanga, jua nimejipanga.”

“Nikikwambia nitakutafutia pesa mpaka zikukinahi! Jua utapata pesa. Nimejipanga.” “Unataka nifanye nini ili unisamehe Colins? Nimekosa, na pesa sio nia yangu.” “Ilikuwa nia yako baba. Ndio maana ulinitoa kwenye ndoto zangu, mipango yangu, na kunifikisha hapa nilipo sasa. Nalipa garama ya maamuzi yako.” “Najua umenikasirikia hutaki kunisikia. Lakini mimi kama baba, nilikuwa nikikuwazia mema Colins! Nikikuwazia wewe mpaka watoto wa watoto wako. Mimi ninayo pesa Colins! Huna utakachoongeza sasahivi kwenye maisha yangu kikabadilisha hivi nilivyo.”

“Baba mwenye nia njema, anaangalia maisha ya kijana wake kwenye kila pande. Sio pesa tu na elimu. Ulinitoa kwenye maisha yangu, kazi yangu nzuri iliyonipa heshima na kuonyesha kipaji changu kilichotambulika kwenye ile kampuni nzima! Ukaniweka kwenye ndoto zako wewe na Simba.”

“Ukanitoa kwenye mapenzi ya kweli na kuniweka kwa mwanamke muovu, akaishia kunitesa kwenye jumba la thamani, na kuniwekea mapepo. Yote hayo umeyafanya kinyume na matakwa yangu, tena nikikusihi uniachie maisha yangu na nikakupa ukweli halisi, halafu unasema ulikuwa ukiniwazia mema!?” Wakaanza wawili hao asubuhi asubuhi hata saa 12 ilikuwa haijafika.

“Ningejua vipi kama Love ni msichana mbaya wa namna hii wakati alikuwa akinifuata mpaka kazini akilia anakupenda?” “Ungeniamini MIMI kuliko yeye. Hapo ndio ningejua unanipenda na kuniwazia mema. Uliamua kuchukua upande wake, ukamwamini kuliko mimi! Tena mama akiwa anajua undani wetu. Sikuacha kumshirikisha mama jinsi tulivyokuwa na Love. Lakini wote mlinigeuka.” Colins akawa ameshakasirika. Ananguruma nyumba nzima na hasira ya zamani ikawa imesharudi.

“Nimekosa Colins. Nimekosa. Sasahivi nimejifunza, nitaheshimu…” “Itasaidia nini sasahivi, baba?! Itasaidia nini wakati Jelini anaolewa na mwanaume mwingine?” Akazidi kukasirika.

“Hivyo Kamila anavyompenda Mike na kumlilia, ndivyo Jelini alivyo kuwa kwangu. Na mimi nilibahatika kupendwa kama hivyo Mike alivyopendwa na Kamila, lakini mimi mmenikatili. Mike ameondoka hapa duniani akiwa ameshiba mapenzi ya kweli, lakini mimi nitakufa nikiwa nadandia mapenzi ya watu wengine!” Kamila aliposikia hivyo, akaishiwa nguvu kabisa na tumaini dogo lililokuwa limebakia moyoni likafa kabisa.

“Mmeniweka mahali pabaya. Mmeua ndoto na mipango yangu. Mama niliyemuamini na maisha yangu ya sirini kabisa, ulinisaliti. Mkiwa mnajua ukweli. Nawalilia kuwaaminisha, lakini mkaenda kunikabidhisha kwa shetani huyu ili anitese?”

“Colins, nimekosa. Nimekosa. Ila naomba ukumbuke jambo la mwisho. Yote nimefanya kwa sababu nakupenda, na nakuwazia mema. Najua sasahivi huwezi amini, na haitaleta maana tena, lakini usisahau hilo. Habari za Jelini kwangu zililetwa na uthibitisho kabisa. Muulize mama yako. Zilikuwa na uthibitisho ambao na mimi ilibidi kufuatilia, nikagundua kwa asilimia 90 niliyoambiwa ni kweli. Muulize mama yako, kama sikuelekezwa mpaka baa alizokuwa akishinda Jelini na mimi kwenda kuuliza na kuambiwa ni kweli hapo ndipo maskani yake usiku kuchwa.”

“Huyo alikuwa Jelini wa zamani. Na alikuwa bora Jelini aliyekuwa akishinda baa, alijawa upendo. Mwaminifu. Si malaya kama Love ambaye anashinda kanisani huku analala na wanaume hovyo na kuwaleta mpaka ndani ya chumba chetu. Roho yake mbaya. Anajali maslahi yake tu.” “Ningejuaje yote hayo?” “Kwa kunisikiliza mimi kwa sababu mimi ndiye niliyekuwa kwenye maisha ya hao wanawake wote wawili.”

“Nikawafahamu kwenye ngazi ya mahusiano ya kimapenzi lakini si wewe uliwafahamu kwenye ngazi ya ubaba mkwe, wanajionyesha kwako kwa kadiri wanavyojua wewe ungetaka kuona.”

Umenikosea baba. Umeniachia donda la maisha. Nitakufa nikiwa sijaonja mapenzi ya kweli. Nitakufa nikiwa sijui kuishi na mwanamke atakayenipenda kwa dhati mimi kama Colins, na mimi nikaacha historia ya kwanza na nzuri kwa mwanamke. Hakuna mwanamke atakuwa na kumbukumbu zangu nzuri mimi nikiwa wa kwanza kwake, nitaishia kufananishwa kiwango changu na wanaume wengine waliopita kwenye maisha yao. Na hapo naweza kupungua sana, nisifikie kiwango, akaishia kuishi na mimi kwa kunivumilia akikumbuka mapenzi ya kwanza na mimi nikiwa ni matokeo ya kukosa kwake!”

“Jelini anakupenda Colins. Alikiri.” “Unazungumza nini baba yangu? Jelini anaolewa na mwanaume mwingine akijua sijawahi mpenda yeye kama Love. Na hiyo ni wewe umesaidia kuiweka akilini mwake. Anachojua ananipenda sana ila mimi sijawahi kumpenda.”

“Si mara moja nimemuacha Jelini akiwa amejiandaa kabisa, ananisubiria, lakini wewe ukalazimishia niende kwa Love. Si usiku mmoja amelala akilia kwa ajili yangu. Siku mmekuja kwangu na kina Love kuniwekea mapepo, na kunipoteza ufahamu wangu kabisa, ndio siku nilikuwa nakwenda kumuweka sawa, nijirudi, nimuombe nimuoe.”

“Na yote hayo mabaya niliyokuwa nikimfanyia, lakini Jelini alimtuma James kuniambia, yupo tayari kuwa na mimi mpaka nijifunze kumpenda, akidhania simpendi. Aliandaa siku hiyo, akanipikia kabisa, akinisubiria. Na mimi nilishajipanga na kumuomba James aniandalie vikao vya harusi kwamba namuoa Jelini bila nyinyi, nikijua mkija mfahamu Jelini, mtampenda tu. Lakini mkanivamia, mkaniweka mateka, na ndio mkagongelea msumari wa mwisho kwenye kufunga mahusiano yangu na Jelini.”

“Jelini anakumbukumbu za Colins aliyempenda, lakini sijawahi mpenda! Na japokuwa alikuwa akiona picha zangu na Love alizokuwa akizisambaza, mimi sina ufahamu, lakini alikuwa akinisubiria muda wote mpaka akakata tamaa kabisa akiamini kweli sijawahi mpenda, anasubiria penzi ambalo si lake!”

“Mmenifungia humu ndani, mmeshindwa kumtaarifu, mnakuja kumtaarifu mwishoni kabisa! Lakini pia, kwa vile anavyonipenda yule msichana, nikiwa nipo kama kinyago, sitizamiki, nina madonda mwili mzima, ile kuniona tu, akasahau kabisa kama tayari alishatoa ndiyo yake kwa Ezra. Akasahau kila kitu akawa kama ameokota lulu! Kwa mabaya yote hayo, alikuwa tayari kuniuguza kwa mapenzi yote, yeye mwenyewe mpaka alipokuja kukumbushwa yupo Ezra.”

“Niambie baba. Nakuja kupata wapi mwanamke wa kunipenda kwa namna hiyo kama sio nakuja kuishia kwa mwanamke aliyejawa mapenzi ya mwanaume mwingine mimi nikiwa nalinganishwa kuona kama nafikia hicho kiwango? Yaani mimi nitaishia kuwa kwenye mahusiano ya kujithibitisha mpaka kifo changu!” Pakazuka ukimya hapo, wote wakajisahau kama ni waajiriwa.

Mwishoe mzee akamalizia akiwa kama yupo mawazoni. “Ni kweli nimekukatili Colins. Nimekukatili vibaya sana.” Akamalizia hivyo na kuondoka. Mkewe naye akafuata nyuma. Wakamuacha hapo chumbani kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ø Giza limeshajitenga na nuru. Kukiwa na tumaini la kutoka rumande kwa dhamana, uovu wake na Kemi aliyeponea chupuchupu kuwa naye lupango, wawekwa bayana. Love yu mgonjwa wazazi wanahangaika kumtoa akatibiwe. Akiwa na kesi ya wizi, shitaka la kusudio la kutaka kuua, linamuwinda. Colins ameapa kumlipiza kisasi mpaka ajute. Ameshamuweka Chris mtetezi wao upande wake, tayari kulipiza kisasi cha maumivu.

Ø Akiwa anapambana na yote, huku kwa Kamila ni kama anakosa. Amefika mwisho, na yeye akiwa na uhakika Colins hatakuja kumpenda kama Jelini. Na huku nako atakuja kumbuka shuka kumekuchwa!?

Itakuaje?

INAENDELEA.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment