‘Ingekuwa ni
amri yangu, kwa hakika usingepita unakopita sasahivi. Lakini nimeshindwa
kukulinda Jelini. Pole na samahani. Ila jua nakupenda na nakutakia
mema. Naamini utapata ulichokuwa ukikitafuta na mimi kushindwa vibaya sana
kukupa. Unastahili mazuri Jelini, kwa kuwa moyo wako pia ni mwema kwa kila mtu.
Utafanikiwa tu. Na nakutakia kila la kheri.’
Akamtumia huo ujumbe na kuongeza mwingine.
‘Utakapofika
mahakamani, usiogope. Naamini kila
kitu kitaenda sawa. Narudia tena kuomba msamaha
kwako Jelini. Nisamehe kukupitisha hapo. Nia ilikuwa njema. Sikutaka TUACHANE
tu bila maelezo. Unastahili kila
jema, lakini walio kinyume yangu
wameishia kukuumiza wewe, wasijue wananiumiza mimi zaidi. Moyo wangu umpweke, nikijua nakukosa Jelini. Lakini
kwa upande mwingine, nafurahia unaishia pazuri. Kila la kheri.’ Akatuma.
Baada ya muda mfupi akashangaa Jelini amemjibu.
Hakuamini. ‘Colins, kwa hakika. Kutoka ndani ya moyo wangu, nimekusamehe na samahani kukutupia
lawama wewe moja kwa moja. Najua na mimi kuna sehemu nilikosea kwa kuzembea. Nawajibika kukuomba msamaha.
Sitilii mashaka juu ya mapenzi yako kwangu, Colins. Japo nahisi ungeongeza juhudi kidogo tusingekuwa
hapa tulipo. Ila naomba kukushauri kitu.’ Akaendelea kusoma kwa shauku.
‘Inaweza
ikawa ndio ujumbe wangu wa mwisho kwako, lakini amini nataka usiishi mpweke. Hustahili adhabu ya
Love.’
‘Usikubali
akakuacha mpweke. Utakuwa umempa nguvu kubwa sana ambayo hastahili. Unastahili kupendwa na kuwa na furaha. Pale tulipopita mimi na wewe
iwe shule yetu.’
‘Popote utakapoamua
kufungua moyo wako, usirudie makosa tuliyofanya nyuma. Nakuhakikishia
Mungu hajaishiwa na anakuwazia mema Colins. Usifunge moyo wako. Utakuwa sawa.
Unaweza usiamini, lakini bado upo moyoni mwangu, na nakuombea mema na mazuri.
Nataka uwe na furaha Colins. Hata kama hujisikii kuchukua hatua, tafadhali
fanya kwa ajili yangu. Daima
nitakupenda Colins.’
~~~~~~~~~~~~~~~
Colins alimaliza kusoma akajikuta machozi yamefika
kidevuni. Akajifuta kwa haraka sana huku akiangalia kulia na kushoto kama kuna
aliyemuona.
Jelini amezungumza
naye! Amemjibu! ‘Daima
nitakupenda Colins!’ Alijawa furaha! Akabaki akirudia ujumbe wa Jelini
asijue muda unazidi kwenda. Ofisini hajaingia! Yupo ndani ya gari na mrembo
Kamila amelala. Akatulia hapo mpaka Kamila aliposhituka kutoka usingizini.
“Colins! Mbona mpaka pamepambazuka kabisa!?” “Nilitaka
ulale kidogo. Nilijua hukulala vizuri usiku.” “Sasa si tutakuwa tumechelewa
kazini?” “Usijali. Nilitaka ulale vizuri ili uweze kufikiria vizuri
unapozungumza na Luca. Sasa unataka kwenda jikoni au kwa leo utulie
uendelee kesho? Maana tutatoka kama kwenye
mida ya saa 6.” Akaangalia saa. “Acha niende hata kwa muda mfupi tu.” Ndipo
wakatoka garini sasa.
Mfupa Uliomshinda Fisi.
Akiwa ofisini akaona simu ya Noah inaingia. Akapokea
akiwa na mshangao. Kwanza bado ilikuwa asubuhi, na si kawaida yake kumtafuta
mida hiyo. Kwanza mida hiyo kwa Noah ni kama usiku wa manane, anakua
amelala kabisa. Akapokea lakini hakumsikia akizungumza. Akaita mara kadhaa
mpaka akamfanya Ezra aache shuguli zake amtizame.
“Naona imejipiga. Wakati anataka kukata akasikia sauti ya
Hope kama anafoka! Akaongeza sauti na kuweka kwenye spika. Wote wakabaki
kusikiliza. Wakaangaliana kama kuulizana ni wapi! Na nani! Na kwa nini mida
hiyo! Ikawavuta masikio zaidi ndipo wakapata majibu yote.
Alikuwa akimpandishia Emelda kwa jazba haswa. Mwishoe
wakamsikia Emelda akimwambia, “Unachofanya hapo ni kunipotezea muda, Hope.” “Sio
wifi tena!? Mnafiki mkubwa wewe! Mchawi na mwanga wa mchana
kweupe wewe.” Alishituka
Junior! Akatamani iwe ndoto.
“Nakusaidia
tu Hope, unajiumiza wewe mwenyewe. Hayo matusi unayarudiarudia tu. Na
kukusaidia zaidi, huna tusi jipya ukanitusi ambalo sijawahi kutusiwa.
Nimekua nikizungukwa na watu wa aina yako kuanzia nina akili zile za
kuelewa za kitoto mpaka sasa. Huna jipya, ila unajiumiza tu wewe mwenyewe
na kunipotezea muda wangu ambao sina. Naomba nipishe nimalizie shuguli zangu,
nitoke hapa nikamuone mama yangu hospitalini.” Akasikika
Emelda kwa sauti ya kutulia tu.
“Esther yupo sahihi. Ndio amekuja kukuongezea
uchawi! Amekutana na nguvu za Mungu yamemrudi, mnajidai mgonjwa!” Hapohapo Junior akachukua funguo za gari akatoka akikimbia.
Na Ezra naye akampigia Junior, kisha akamwambia asikate.
Akampigia na Hope. Ikaita mpaka ikakatika. Akampigia tena na tena ndipo
akapokea.
“Hicho
unachokifanya hapo kwa Emelda ni fujo, na mimi binafsi sitakuruhusu.”
“Ana…” “Hapana Hope. Junior si mtoto mdogo kiumri wala kiroho. Ana nguvu za
Mungu zinazomlinda, wala malango ya kuzimu hayatamshinda, labda uniambie leo kama
unaamini kama uchawi una nguvu kuliko Mungu.” Akataka kujibu.
“Sina muda
wa kubishana na wewe, ila nakuja pointi ya pili. Kwa kuwa Junior sio mtoto
mdogo kwamba amerubuniwa na Emelda, ni chaguzi yake mwenyewe, na mimi ni
shahidi wa hili, basi, mtafute yeye Junior ndio umpe hayo matusi.
Ila iwe mara yako ya kwanza na ya mwisho kumtusi Emelda. Umesikia
Hope?” Ezra akaendelea.
“Hicho
kikundi chako na Esther mkakifanyie nyumbani kwa Esther, lakini sio hapo alipo
Emelda, tena kwa kipindi hiki kigumu kwake. Anamuuguza mama yake, na bado
anamajukumu ya napo nyumbani akiwa mama mchungaji hayupo, halafu bado anamdogo
wake wa kumsimamia.”
“Sasa basi,
baada ya dakika 5 kama bado utakuwepo hapo, mimi mwenyewe nitakuletea polisi na
kukushitaki kumvamia Emelda. Haya, ondoka na usiongeze neno jingine kwa sababu
ukikiuka tu, shitaka lako linakufuata. Siku njema.” Kimya. Simu ikakatwa.
Hapohapo Ezra akampigia Noah. “Naomba
weka kwenye spika na Hope asikie.” “Tayari.” Noah
akajibu. “Sasa nichukulie video ya Hope akiwa hapo na kila neno atakalozungumza.
Kisha nitumie sasahivi. Nitaanzia kwa mwajiri wake, anayempa ruhusa ya
kuzunguka kwenye majumba ya watu asubuhi asubuhi akitukana badala ya kuwa
kazini akifanya kazi, kisha polisi.”
“Mbona
tayari! Nilikuwa namrikodi kuanzia aliponiamsha kwa kelele zake. Hapa namtumia
mchungaji wake, Esther shoga yake ili asije ruka maneno yote aliyosema
ameambiwa na Esther, kisha kwa yule mwanamme wake, ajue anajiingiza kwa
mwanamke wa namna gani.” “Uchonga…” “Yaani hata hapa unaponijibu, jua na
kurikodi.”
“Umepatwa
nini wewe Hope!? Umechanganyikiwa wewe?” Wakamsikia
Junior upande wa pili. “Kama kuna nguvu za giza je?” “Sasa wewe shida yako nini?
Ninayelogwa si mimi ambaye ulisema hunitaki mimi na misingi yangu ya
maisha? Kinacho kuuma wewe ni nini? Wewe si umesema unaye mwanamme wako na mpo serious?
Sasa kwa nini wewe na Esther hamuangalii ya kwenu mnahangaika na yangu?”
“Esther…” Kabla hajaendelea akamuwahi.
“Mimi sijali Esther amekwambia nini. Ila kama unadhani
Ezra anakutania, basi nikukute hapo. Na iwe mwisho kuzungumza na Emelda hivyo.
Usirudie kumtukana wala kumpandishia sauti. Huyo si mchumba tu.
Mke wangu na mama wa watoto wangu. Hakuna mtakalosema nikaacha kumuoa
Emelda. Sijaribishi kwake. Nimemaliza. Hilo mfikishie Esther na uongeze
kuwa sina shida ya kulogwa na Emelda. Mimi mwenyewe napenda na nataka
aniloge zaidi. Kama nyinyi wawili mna tatizo naye, nifuateni mimi. Lakini yeye
mwiko. Umesikia Hope?”
“Kwanza
toka hapo. Huyo Emelda ana mambo mengi ya msingi, unampotezea tu muda. Anategemewa
kuongoza hiyo nyumba mpaka mama arudi na bado ana mgonjwa hospitalini. Noah?” Akamuita mdogo wake.
“Nipo bro.”
“Hawa wananichezea kupita kiasi na wamevuka mpaka. Leo ndio mwisho kuzungumza
hivyo na Emelda, siwapi nafasi ya pili. Na Hope utakuwa fundisho kwa wote. Piga
simu getini wamshikilie mpaka nitakapo kuja na polisi. Nakaribi…” Kabla hajamaliza, Hope akakimbia kama mwizi. Wakamsikia
Noah akicheka kishabiki haswa. “Nakurikodi Hope. Video yako utaipata. Na kama
umeni block utaikuta kwa mashoga zako, mchungaji wako, wazee wako wa
kanisa na kwa yule mwanamme wako.” Wakamsikia akiongea akicheka kwa kumdhihaki
Hope.
Kila Msingi, Hujengwa kwa garama.
Kwenye mida ya saa 6 mchana Colins akaacha shuguli zake
zote, wakawa wanatoka hapo kuelekea kwa huyo mwanasheria akimsindikiza huyo
Kamila kupata ukweli juu ya Mike. Alikuwa ametulia garini. Baada ya kuendesha
kidogo akamuita Colins taratibu. “Colins!” Akamwangalia. “Asante kuwa na mimi
mpaka sasa. Wewe ni wa kuaminika.
Unasimamia ahadi zako hata kama nakugarimu muda wako muhimu.” “Usijali.
Naamini kila kitu kitakwenda sawa.” Akatulia.
Walifika ofisini kwa huyo mwanasheria wakashangaa kukuta
wazazi wake wanasubiria nje. “Si mmesema hamtakuwepo?” “Tumeona tuwepo na sisi
ili Kamila binti yangu asijisikie mpweke.” “Kweli mama?” “Umeshakuwa mmoja wa
familia Kamila mwanangu. Umetupa nafasi ya heshima kuwepo nyumbani kwetu,
umeshakuwa binti yetu. Tutasimama na wewe katika kila hatua ya maisha yako.
Usiogope.” Colins hakuamini.
Mama yake
alionekana kama aliyepata mapumziko haswa. “Na kazini?!” Akauliza akimtizama
baba yake. “Mimi nikitoka hapa nitakwenda. Kuna wagonjwa lazima nikawaone. Ila
mama yako atapumzima leo. Sasa hivi usiwe na wasiwasi mpaka hili likae sawa.
Acha tuongeze uzito hata kwa hao
kina Luca wajue kuanzia sasa, Kamila hayupo peke yake. Ana wazazi wanao msimamia.
Hawaruhusiwi kumchezea tena.”
“Asante baba!” Colins akashukuru asiamini. Wakawa wamejirudi wakati muafaka
akiwa kweli anawahitaji.
“Baba yako aliona ukitokea tu wewe, Luca anaweza asione uzito.
Akahisi ni kijana tu ambaye unataka kujinufaisha
na Kamila. Asione uzito.” Akachomekea makusudi kama kumsogeza baba yake karibu
naye akimpa sifa na yeye asamehewe. “Sikuwa nimefikiria hilo! Nafikiri yupo
sahihi. Itaongeza uzito. Asanteni.” Wakakaribishwa ndani.
~~~~~~~~~~~~~~~
Baada ya muda mfupi Luca na dada yake wakawasili na wao.
Wakasalimiana na utambulisho. “Hawa wapo hapa kama wazazi wa Kamila.” Wakashangaa sana. “Huyu mtoto si alisema ni
yatima huyu!?” Dada mtu akauliza kwa mshangao. “Ni yatima ndiyo, lakini hawa
ndio wazazi wake kwa sasa. Ndio wanao ishi
naye kwa sasa, na ndio wanao mtunza.
Wanadhamana naye. Kwa chochote
tutakachozungumza hapa, wanaruhusiwa na Kamila kuwepo na kusikiliza.”
“Hata kuhoji maswali.” Akaongeza Kamila mwenyewe.
Wakamwangalia.
“Namaanisha na wao kama walezi wangu wanaruhusiwa kuuliza maswali.”
Wakakubaliana. “Haya, Kamila karibu.” “Mike yuko wapi? Nataka kujua
walipomficha. Hilo tu, mimi sina shida ya pesa ila Mike.” “Acha niwaambie
ukweli. Hilo tu ndio pona ya huyu
msichana. Lasivyo, nilitaka kumfungulia mashitaka ya kumuua Mike.”
“Mimi!?” Kamila akashangaa sana.
“Naombeni tu mnisikilize. Eti Mike awepo nyumbani kwangu
mpaka usiku. Akiwa mzima kabisa. Na alikuwa naye huyu. Halafu eti baada
ya masaa machache alfajiri yake nipigiwe simu eti Mike amefariki! Tena inashukiwa
kama amenyweshwa sumu! Hata kama ni
nyinyi jamani, mngefikiria nini, kama si mtu wa mwisho kuwa naye ndiye
aliyempa hiyo sumu!?” “Mimi nataka kujua
Mike alipo. Na msinidanganye.
Wamesema mimi ni kama mkewe.” Wote mpaka upande wa kina Colins na huyo
mwanasheria wakashangaa kwamba hasikii au!
“Mike amezikwa
makaburi ya Kinondoni.” “Mnadanganya.
Mimi nilikuwa naye hospitalini. Tena nikamuaga kabisa kuwa nitarudi. Akaitika
kabisa.” Akawasimulia ilivyokuwa. “Eti narudi, wananiambia Mike hayupo! Awe ameenda wapi kama si
wamemchukua hawa?”
“Mimi nilipigiwa simu kuwa Mike amefariki na ndani
ameanza kuharibika. Ikabidi kwenda kushuhudia nikiwa siamini. Walichoniambia ni alikuja na msichana pale, akamuacha. Hakika roho yangu ikaniuma
sana. Nikajua huyu alimtelekeza kwa sababu zake mwenyewe.
Hayo mengine sikuyajua mimi!” Luca naye akaongeza.
“Inavyoonekana kwa taarifa za hospitali, Kamila aliporudi
hospitalini siku ile akapewa taarifa za kifo
cha Mike, alishituka sana na kupoteza
fahamu kwa karibia siku tatu.” “Hayo ndio nayasikia
leo! Ila yeye aliporudi nyumbani akaanza fujo
kwelikweli kama mwehu,
anamtafuta Mike. Ndio angalau akaniaminisha
sio yeye aliyemuua Mike.”
“Na ilinibidi kumzika kwa haraka. Muulize dada hapa. Mike
alishaanza kunuka mapema sana, mpaka tukashangaaa ni nini alinyweshwa! Maana ni kama aliharibika
kila kitu ndani! Hatukuwa na sababu ya kumchelewesha ila kumzika.”
“Muongo Luca. Anadanganya kwa sababu hampendi Mike.” “Wala sitadanganya. Mike aligeuka mpinzani na kuamsha hasira ndani yangu.
Hata nyinyi wenyewe fikirieni jamani! Mimi ndio mtoto wa kiume mkubwa kwa mzee wangu. Eti leo mtu baki ndio apewe mali za
familia ndio aongoze! Hata kama ni nyinyi mngefurahia kweli?” Wote kimya.
“Lazima kama mwanadamu nichukie. Lakini si kwa kumficha!
Muda wote huo! Miaka miwili! Namficha
mtu kama Mike, ili iweje? Kama wewe huamini twende ukaone kaburi lake.” “Nitajuaje kama aliyepo
humo ni yeye hamdanganyi? Nyinyi mna
roho mbaya sana.” “Basi tutakuonyesha picha zake za siku ya mazishi yake, uangalie.” Akanyamaza,
wakamuona anaanza kutetemeka. Amebadilika amekua mwekundu mpaka masikio.
“Kamila, una swali jingine au ombi jingine?” “Naomba
uthibitisho kama kweli Mike amefariki. Nafsi yangu inakataa jamani! Mike alikuwa mzima kabisa. Sijapitia naye popote
tokea tunatoka nyumbani kwa Luca au kwamba tulikula kwengine! Kwanza ilishakuwa
usiku mwingi. Eti tunafika nyumbani ndio anaanza kulalamika tumbo, wakati
alikuwa mzima kabisa! Moyo wangu hauamini.” “Dada, mtolee picha na pia
tutakupeleka kwenye kaburi lake.”
“Kingine,
naomba waambie wanipe pete yangu ya
uchumba alinivalisha Mike na gari alinipa mimi zawadi. Ni haki yangu, Luca akanipokonya. Ni hivyo tu ndio nataka.” “Mimi sijui ni nini kimetokea jamani! Ile pete ilipotea
kwenye mazingira ya ajabu, sijui ilikuwaje! Mara nilikuwa nayo, mara ikapotea.”
“Haya, ile gari yenyewe nusura imuue Robi, mwanangu wa kwanza. Alipata ajali mbaya sana. Gari
imeharibika, haijasalia hata kioo! Imefanya kukusanywa na kutupwa. Kwa hiyo
hapa nilipo sina hiyo pete wala gari. Ushahidi huu hapa.” Akatoa simu
yake na kuanza kuwaonyesha picha za ajali aliyonusurika kijana wake. Wote
wakashangaa.
Kamila akazidi kulia. “Na ningesema nimlipe, lakini hizo
mali zimekuwa kama na mkosi! Muulize
dada. Kila siku ni hasara, mpaka biashara
nakaribia kufunga. Naendesha kwa mkopo.
Sina kitu. Hata kama atadai mali, hakuna.
Labda ile nyumba.” “Mimi sina shida na ile nyumba.” Kamila
akajibu akilia na kushangaza wote. Hataki nyumba!
Ila mama Colins akaingilia. “Nyinyi mlimfukuza yatima, tena kama mke wa kaka yenu. Halafu ni kama mlimdhulumu
Mike maisha yake, Mungu naye akatoa
mkono wake kwenu ndio maana na mali na zenyewe zinaondoka.” “Kwa hakika mimi sijamuua
Mike. Na Mungu ni shahidi. Tulikuwa hatuelewani,
lakini si kwa kumuua.”
“Ila mimi inanishangaza jamani! Japokuwa sikuwa karibu na
Mike, na mimi kwa sababu kama za Luca tu, lakini kwa jinsi alivyokuwa Mike, nani atakuwa amemuua!?
Yule kiumbe mbali yetu sisi kumchukia sababu ya kuwa kiongozi wetu kwa mali za
baba yetu, jamani Mike alikuwa mwema. Hata Luca katika hilo atasema.” Dada
mtu akaongeza kama akiwaza.
“Wala sitabisha. Mike alikuwa mtu mzuri. Anaweza akafanya
jambo mpaka ukashangaa. Sidhani kama alikuwa na maadui yule. Kwa hakika sijui
nini kilimpata Mike! Pengine iwe sumu alipewa muda mrefu ikaendelea kumuharibu
taratibu mpaka usiku. Ila kusema kuna mtu anaweza kuweka uadui naye! Si rahisi.
Kwanza mwenyewe utashindwa kwa ile haiba yake Mike. Kuna jinsi Mungu
alimuumba, ngumu kuweka uadui naye.” “MmmH!” Dada mtu akaguna kwa kushangazwa
kabisa. Wote wakabaki kimya kwa muda wakiwaza.
Mwishoe Colins akavunja ukimya. “Tafadhali naomba tuone
picha za Mike. Uthibitisho kwa Kamila.” Ndipo wote wakaonyeshwa picha za siku ya
mazishi ya Mike. Kuanzia yupo kwenye
jeneza mpaka anazikwa. Kamila alilia,
alilia sana. Ikawa ndio kama ukweli ukamuingia, kuwa Mike hayupo duniani.
Akalia sana.
Safari ya makaburi ya Kinondoni ikaanza ili waonyeshwe mahali walipoweka mwili wa
Mike. Wakafika ila Kamila akilia
vilevile. Wakaonyeshwa kaburi lake. Lenye jina lake kamili. Kamila akazidi kulia
akilishika na kurudia kusoma. “Jamani Mike!” Akaendelea kuomboleza kwa uchungu akiwa amepiga magoti
hapo kaburini. Wote kimya, hamalizi! Muda unazidi kwenda.
Luca akaaga kuwa inabidi arudi kazini. Akaondoka na dada
yake. Kamila bado analia. Alikuwa hawezi hata kusimama kwa kulia. Mwanasheria
naye kazi yake ikawa imeisha. Akaondoka. Kamila bado analia
ameshikilia kaburi anamuita Mike kama amsikie.
Mwishoe Colins akambeba na kumuweka kwenye gari ya wazazi
wake. Akawaomba warudi naye nyumbani. “Mimi nilazima nirudi kazini. Ila
nitawahi kutoka. Nakuomba mama, ukae naye mpaka nitakaporudi.” Mama yake
akakubali maana mzee alikuwa na yeye anakwenda kazini. Wakarudi nyumbani,
Colins kazini.
~~~~~~~~~~~~~~~
Mama Colins akaanza kazi ya kumbembeleza huyo Kamila masaa
kwa masaa mpaka akalala hapo kwenye chumba alichopewa kwenye hiyo nyumba yao. Akamuacha
alale akatoka taratibu. Mumewe alishaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
Safari ya Mike hapa duniani imeisha, Jelini haonyeshi kurudi nyuma.
Ezra ni mume kwa hakika. Maisha lazima yaendelee.
0 Comments:
Post a Comment