Walipofika sehemu ya kuegesha magari, akamuwahi. “Huruhusiwi
kuingia ofisini kwangu hata na walet. Nikimaanisha acha simu yako, saa ya
mkononi na vingine vyote kwenye gari yako, ndipo uingie. Kama hutaki,
basi.” Chris hakuamini ila kutii.
Akasimama wima akimtizama mpaka akatoa kila kitu mifukoni
na kuweka kwenye gari yake. Alipohakikisha mifuko yake ni mitupu ndipo wakaongozana
mpaka ofisini kwake.
“Nikusaidie nini Chris?” Maana alikaa kwa kunyongea kama
mgonjwa. “Nimeamua kuacha kuwawakilisha kina Kemi na Love.” Colins akabaki
akimtizama. “Nimeona nijitoe.” Kimya. “Ndio hilo tu. Nilitaka kukutaarifu.”
“Unanitaarifu mimi kama nani na ili iweje?!” Colins akamshangaa
kabisa.
“Sitaki kujiingiza kwenye vita isiyo yangu.” “Hilo
umeligundua lini?!” “Nimeona heri nijitoe.” “Unanipotezea muda wangu
Chris. Maana hichi unachokifanya hapa ni fujo na si sehemu yake.”
“Nataka tuwe ukurasa mmoja mimi na wewe.” Alimuudhi Colins, mpaka akabadilika
rangi.
“Unataka kuwa ukurasa mmoja na mimi wakati unalipwa
kuniangamiza mimi na watu wengine wasio na hatia!?” Akamuuliza kwa ukali
kabisa. “Hivi unajua mwanamke uliyemuweka kizimbani leo, na kumuhoji,
pengine kama mhalifu, ndiye aliyekuwa mwanamke wangu? Ilikuwa nimuoe
mimi, halafu hao unao watetea wakanitenda? Walinigeuza kichaa
kabisa natembea barabarani kama tahira!”
“Wamemnywesha sumu mwanamke wangu. Ndio walikuwa
wakigongelea msumari wa mwisho kabisa wa kunitenga na mwanamke
wangu. Leo unawatetea kwa kuwafundisha kumdhulumu mtu asiye na hatia!
Alianza biashara yake pengine akiwa hana kitu! Amefika alipofika, unamdhulumu
bila hatia huku ukitupia mbali tuhuma za kunyweshwa sumu mpenzi wangu! Halafu
eti unakuja kwangu unaniambia unataka kuwa ukurasa mmoja! Halafu eti
njia yenyewe unayotumia ni kujitoa kwenye ulichoanzisha na kukichochea!?”
“Inawezekana nimetumia neno lisilo sahihi. Lakini nia ni kurekebisha.
Mimi sikuyajua hayo yote.” “Hukuja hapa nikakwambia unao watetea wanakutoa
muhanga? Ukatoka hapa ukinitusi?” “Kwanza kesi ya leo nimeomba iairishwe
mpaka tujipange mimi na wewe.” “Acha kunipaka mafuta kwa mgongo wa
chupa. Ondoka Chris. Toka ofisini kwangu.”
“Nisikilize Colins. Niliahirisha kesi na pia nimejitoa
kuwa wakili wao. Sasa kwa nini tusijipange upya?” “Unajipanga vipi na mimi
wakati umeanzisha jambo halafu umejitoa!? Yaani unaharibu halafu unakimbia!?
Wewe ni mtu wa namna gani Chris!? Utakuwa ukikimbia uharibifu wako mpaka
lini?” Hapo akamjumuisha mpaka Zulfa.
“Nimekubali kosa. Ndio maana nipo hapa. Niambie basi vile
unataka nirekebishe, nitafanya.” “Unauhakika?” “Ndio maana nipo hapa.
Sina sababu ya kukufuata kama si kutaka kutengeneza.” “Anza kwa kurudi
kuomba kuwa wakili wao.” “Haiwezekani Colins! Nimetoka kuwaambia sitaweza
kuwawakilisha tena.” “Nguvu ileile uliyoitumia mwanzoni kuwaweka upande
wako, ndio uitumie tena kurudi. Unanielewa Chris?” Akabaki ameduwaa.
“Chris?” Akamuita kwa ukali. “Acha mimi nisiwawakilishe.
Halafu niwe na wewe nikusaidie mbinu zaku…” “Toka ofisini kwangu. Unanipotezea
muda. Sina shida na msaada wako. Toka.” “Sawa. Sawa Colins. Tufanye
nimefanikiwa kurudi kuwawakilisha. Ndio inakuaje?” “Simamia haki! Swali gani
hilo?!” Akawa hajaelewa.
“Unanielewa? Anza kusimama kama mwanaume, wajibika.
Acha kukimbia. Tengeneza uharibifu wako. Kila uliyemdhulumu, mpe haki
yake. Sitaki unitetee. Sitaki upendeleo. Simamia haki
kisheria. Simama ukiwa unasikiliza na kutetea haki, hilo tu. Acha uonevu
kwa watu wasio stahili. Rudi kazini.” “Lakini kuna mambo ambayo yameshatokea, siwezi
kurekebisha moja kwa moja.” “Kwa hiyo unataka mimi niache kazi zangu, nikufundishe
jinsi ya kurekebisha uozo wako?” Kimya.
“Tafadhali nipishe nifanye kazi. Na sitaki umtese
Jelini mahakamani kwa maswali yatakayo muumiza. Kwanza mpaka sasa unamtesa kwa
kuendelea kumkutanisha na maadui zake wanao mchukia bila sababu! Unamfedhehesha
na kumpotezea muda. Acha kucheza na haki za watu, Chris.” Akazidi kupandisha
hasira.
“Yaani unatetea watu waliokuwa wamekusudia kumuua!
Wauwaji wale ndio unawapongeza kwa kuwahonga mamilioni ya pesa za
mtu anayejinyima kufanya biashara yake! Unawalipa kwa kufanikiwa
kumnywesha sumu mpenzi wangu! Hakika toka Chris. Toka.” Akasimama kabisa na
kumfungulia mlango.
“Basi nipe muda wa kutengeneza. Naomba tusiende mbali.
Mimi mwenyewe nitatengeneza kila mahali. Kote. Makosa haya na ya nyuma
pia.” Akamuelewa kuwa anamaanisha hata kwa Zulfa. “Nipe muda. Na pia muandae
basi hata wakili wa upande wenu! Yule jamaa hajui kazi. Hakuna mtu atanielewa
mahakamani, nikishindwa na mtu kama yule. Hana uzoefu. Angalau kuonekane
hata kama ipo kesi nzito inayoendelea na ndio kushinda kwenu.”
“Ninachoomba kama kweli narudi mimi kuwawakilisha, basi kuwepo
na mazingira mazuri ya kesi. Angalau kuonekane kuna kesi kwelikweli. Ajiandae.
Ni hilo tu. Mengine nitajua mimi.” Akabaki amemshikilia mlango. Akatoka. Lakini
akawa amemuelewa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Alipotoka na kujiridhisha yupo mwenyewe, akamtafuta
rafiki yake aliyekuwa amesoma naye zamani, ila yeye alikuwa mmarekani, anafanya
kazi kama alizokuwa akifanya zamani na kina James, ila nchini marekani.
Akamtumia ile video, na kumuomba kama anaweza kuisafisha
ili ionekane vizuri zaidi. Akamjibu kwa kumuuliza swali. ‘Ina uharaka
wa kiasi gani?’ ‘Yesterday, na ni muhimu sana.’ ‘Nipe muda.’
‘Nashukuru.’ Colins akamjibu akijua ataifanyia kazi tu.
Ndipo akarudisha akili kazini.
Huku Nyumbani kwa kina Colins
Wakati yupo jikoni, akimsaidia msichana wake wa kazi kuweka
sawa mlo wa jioni, maana siku hiyo hakwenda kazini, Kamila akaamka na kumfuata.
“Vipi mama?” “Naendelea vizuri.” “Kaa hapo nikupe kitu kidogo ule.” Akakaa na
kunyamaza. “Pole mama. Pole sana. Utakuwa sawa, usiogope.” “Nashukuru
kunisaidia kujua ukweli. Angalau sasahivi nitajua moja. Kuliko vile nilivyokuwa
nikihangaika kumtafuta nikijua
wamemficha.” “Utakua sawa. Pole.” Akampa chakula maana hakuwa amekula.
“Sijisikii kula kabisa. Colins amerudi?” “Bado.”
Akanyamaza. “Jitahidi ule kidogo. Itakusaidia.” Akamuwekea chakula, akaendelea
na shuguli zake, akimuacha ale, hapohapo jikoni si mbali na yeye.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Nikuulize swali mama?” “Karibu.” Akamuona amesita. “Ni
nini?” “Jelini ni mzuri sana?” Akashituka sana, hakutegemea hilo swali
zaidi kwa wakati huo! Ila akajikaza. “Kwa uzuri, kwa kweli ni mzuri sana. Halafu nadhifu mno.
Ukimuona kwa haraka unaweza kumdhania sivyo.
Lakini alijaliwa wema wa namna ya kipekee.
Anaupendo ule wa kujali usio wa kujifanya.” Sifa zikaendelea.
“Anaakili ya biashara. Maana kwa sasa anafanya vizuri
sana kwenye biashara zake. Anajituma haswa si mvivu au si legelege kama ambavyo
ungedhania ukimuona. Halafu alimpenda
sana Colins. Sana. Na Colins alimpenda.” “Sasa kwa nini Colins
hakumuoa?” Akaguna na kurudi kukaa mbele yake.
“Acha nikwambie ukweli Kamila binti yangu. Sisi,
nikimaanisha mimi na baba yake ndio tulichangia.
Na tulifanya kosa, lakini out of love. Tukijua tunamuokoa Colins
asijiingize kwa msichana mbaya, kumbe ndio tulikuwa tukimtoa kwenye
mapenzi ya kweli na kumpeleka
pabaya.” Akamueleza kwa kifupi juu ya Love na vile ilivyokuwa.
“Sisi bila ya kujua. Tukajikuta tunajiingiza kwenye kumsaidia Kemi kulipiza kisasi kwa Jelini na kumuumiza
sana Colins. Yote tuliyoletewa kwa uongo
juu ya Jelini kumbe ni kinyume kabisa. Tukamtenga Colins na upendo wa kweli, tukamuweka kwenye mikono miovu.
Kwa hakika aliteswa. Hivyo
unavyomuona yupo kwenye kupona.”
“Na hivi kukusaidia
wewe, ndio imekuwa kinyume. Imekua
msaada kwake yeye mwenyewe. Isingekuwa
kutoa msaada kwako, alikuwa na hali mbaya
sana. Ametoa mawazo kwake, sasahivi
anakuangalia wewe, ndio angalau
unaweza kumuona hata ametulia.”
“Lakini kwangu naona ni kama...” Akasita. “Nini?”
“Anamsimamo Colins! Anamsimamo sana.
Na sidhani kama atakuja mpenda mtu mwingine kama Jelini.
Akianza kumzungumzia Jelini, anakuwa wa tofauti, na maumivu makali, kwamba anaolewa
na mtu mwingine! Sidhani kama atakuja kumpenda mtu tena.” Mama Colins akamuona
vile anavyoongea kwa kulalamika na wivu, akajua tayari amempenda Colins.
Ila hakutegemea! Alitegemea majonzi zaidi juu ya Mike. “Ila nashukuru hata kwa hivi
mnavyonisaidia. Hata hivyo na mimi sijasoma.
Nipo kama huyo Jelini tu. Mike hakuwa hata na shida na mimi kuishia hivi
nilivyo. Na pia sikuwahi kujua kama unaweza kukataliwa ukweni sababu ya kutosoma!” Hilo likamshitusha kidogo mama
Colins.
“Nisikilize Kamila. Kwa upande wetu, nakiri tulikosea
sana. Nyumba haijengwi na usomi.
Kama ni hivyo, Love na Colins wangekuwa
na familia nzuri sana. Lakini imeshindikana.
Bora Jelini ambaye hajasoma mara elfu kwa vile alivyomjali Colins, kuliko huyo
Love msomi.”
“Jelini ambaye hakuwa
na shule ila mapenzi ya kweli kwa
Colins, ilichukua masaa machache sana kumrudisha
Colins kwenye uzima, wakati Love na shule yake alimchanganya mpaka akawa akitembe hajitambui mitaani. Kwa hiyo na sisi tumejifunza mama. Shule siyo inayojenga familia ila mapenzi ya
kweli.” Akatulia na kufikiria kidogo.
“Ila kwa jinsi nilivyomsoma Colins, sijui mama! Hawezi
kuja kupenda tena.” Akajirudia kama ambaye ndio kitu kinamsumbua huko moyoni. “Anahitaji
muda tu na mtu sahihi ambaye hatamkatia
tamaa. Ambaye yupo tayari kumsubiri
na kumuonyesha mapenzi ya kweli.
Hakuna mtu anakataa kupendwa. Ila kwa Colins yupo makini sana kwa sababu wengi
wanavutiwa na vile alivyo.” “Ila kweli ni mzuri!” Akaropoka na kumfanya mama
Colins kucheka.
Kamila akaona aibu. “Sasa hilo ndilo linamfanya achukue muda. Mpaka ahakikishe mtu
anampenda Colins wa ndani kabla wa
huyu wa nje. Na usifikiri hata kwa Jelini ilikuwa rahisi.” “Kweli?!” “Atakuja
kukwambia mwenyewe. Ni mpaka alipojiridhisha Jelini anampenda zaidi ya muonekano ndipo akamfungulia
milango yote. Kwa hiyo na wewe mpe muda.” Kamila akaona aibu.
“Mimi nilikuwa sisemei mimi!” Mama Colins akacheka na
kusimama. “Mimi nilikuwa naulizia tu kwa watu wengine. Kama ikitokea msichana
anampenda halafu yeye hataki hata
kuwa naye karibu! Anakuwa anaweka
msimamo. Hataki mambo fulani fulani.
Anasema labda sio sawa, japo jambo
lenyewe sio lakumvunjia heshima.
Anakua...” Akajishitukia na kunyamaza. Mama Colins akacheka.
“Wewe umekuja wakati muafaka
kwenye maisha yake na yetu. Wote tupo kwenye kujenga si kubomoa. Ndio
maana umeona leo, hata baba yake ambaye yupo busy sana, ameacha shuguli zake zote ilimradi tu kuwa naye kwenye jambo kama hili. Ambalo ni lako, lakini akitaka kumuongezea nguvu na heshima. Sasahivi baba yake hazembei tena. Yupo kwenye
kumuunga mkono. Ikitokea anafungua tu moyo, jua na sisi tupo nyuma yake.”
Akanyamaza.
“Umeelewa?” “Nitakuwa mvumilivu. Si mtaniruhusu kuendelea
kuishi hapa au unafikiri ni nunue tu nyumba nihamie kwangu? Maana sasahivi
nishajua moja, bora maisha yaendelee.” “Kwamba unayo pesa ya kununulia nyumba!?”
“Ninayo mama yangu. Ni hofu tu
yakuanza peke yangu.” “Basi tulia hapa kwa muda. Nina binti yangu na yeye
anasomea mambo ya udaktari anataka kuwa kama baba yake . Huwa anakuja hapa.
Hana neno. Utakuja kukutana naye. Utamfurahia tu. Hapa hakuna atakayekubugudhi
mpaka utakapoamua kuondoka mwenyewe. Lasivyo sisi tutakuozesha sisi wenyewe.” Kamila akafurahi sana.
“Basi mimi nabaki hapahapa mpaka nipate mchumba.
Nisipopata, nabaki hivihivi. Mimi siwezi kuishi mwenyewe. Naogopa.” “Basi tulia
hapa.” Akaanza kula huku wakizungumza machache. Mpaka walipomsikia Colins.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akaenda mpaka jikoni na maua. Kamila akadhania ni yake.
Akashangaa anamkabidhi mama yake. “Hakuna kufa.” Akamnong’oneza na kumbusu
kichwani. Kisha akamwambia kwa sauti. “Nashukuru kukaa na Kamila.” “Kamila
binti yangu. Wala usijali. Pole na kazi.” “Asante.” Akaenda kukaa alipokaa
Kamila.
“Vipi?” “Nipo sawa. Asante kunisindikiza. Angalau nimejua
moja.” “Umeridhika?” “Nimeamini Colins. Nimemuona Mike kwenye jeneza nimeamini
ndiye aliyekuwepo pale kaburini. Sina jinsi ila kukubali ukweli na kuendelea mbele.” “Utakuwa sawa Kamila.
Usiogope. Nimezungumza na wazazi, wanakukaribisha hapa. Ishi hapa kama
nyumbani. Utakuwa sawa. Sisemi kama tutaziba
pengo la Mike, lakini huu unaweza kuwa mwanzo mwingine na ukaupenda tu.”
“Nashukuru. Na mama naye ameniambia hivyohivyo. Naona nitatulia hapa.” Mama
yake kimya tu akiendelea na yake.
“Nimeleta movie, tutaangalia usiku wakati wa kulala.
Tutakuwa wote. Leo sitakuacha peke yako. Tutakaa mpaka ukipitiwa usingizi, ndio
nitaondoka.” “Nashukuru.” Akasimama na kumfuata mama yake.
“Umepima pressure?” “Ipo sawa.” “Kweli au unanipa
tu moyo?” “Baba yako alinipima kabla hatujatoka hotelini. Ipo sawa.” “Kama
hivyo sawa. Umependa maua?” Akamsikia akimuuliza mama yake kwa kumbembeleza.
“Hayo maua yana ujumbe
wake. Unachoshindwa kusema ni nini unahangaika tu.” Ikamfanya na Kamila naye
kuyaangalia vizuri hayo maua na kujaribu kuelewa. Yalijaa rangi ya dhambarau na
nyekundu kidogo tu. “Ni baba huyo, si mimi.” Akamsikia Colins akijitetea.
“Sawa.” Mama yake akajibu kwa kifupi tu na kumuona
anatafuta chupa nzuri maalumu ya hayo maua. Akaijaza maji. Akaanza kuyakata
vizuri na kuyapanga humo, Colins akimwangalia kama aseme kitu anashindwa.
“Ni mazuri, asante.” Akasimama hapo kidogo na kuondoka.
Baada ya muda mfupi akarudi tena na chokleti. “Na hizi
nilikuletea nimesahau kwenye mfuko.” Mama yake akajua anahangaika tu.
Anasumbuliwa na dhamira ila ubishi, anashindwa kuomba msamaha.
Akapokea akicheka. “Sasa unacheka nini?” “Nimefurahi!
Wewe vipi Coly?!” “Sawa. Umependa sasa?” Akawa anahangaika tu hapo. “Hata
sijala!?” “Lakini si unazijua?” “Haya, nitapenda. Asante.” Akacheka na kutoka
kama aliyejisuta.
~~~~~~~~~~~~~~~
Mama yake akamgeukia Kamila. “Ametoka kazini. Umejua siku
yake imekuaje?” Kamila akaelewa. Akasimama kwa haraka. “Njoo kwanza.” Akamfuata.
“Wewe unajua anachokifanya pale?” “Waliniambia ni kama bosi.” “Si kama bosi.
Ile hospitali nzima, ni yeye anayeiongoza. Anamajukumu mazito sana.” “Kumbe!?” “Kabisa. Hakuna
kinachofanyika pale bila yeye. Yupo busy mno. Na bila wewe, ujue
sasahivi asinge bkuwepo hapa. Hii si mida yake. Inamaana amewahi hapa
kwa ajili yako. Sasa tumia hii nafasi vizuri.” “Asante mama. Ila namuogopa!
Anamsimamo huyo!”
“Sasa hiyo ndio nguvu yako. Baba yake yupo hivyohivyo.
Inamaana ndiyo yake kwako,
itabakia kwako tu. Sasahivi yupo
kwenye ndiyo aliyoitoa kwa Jelini.
Ndiyo inayo mfunga. Sasa hapo ni mpaka ahakikishe huko alikotoa hiyo ndiyo
yake, milango yote imefungwa. Hakuna nafasi yake tena. Halafu apate
ambaye yupo tayari kumsubiria na kusimama naye kipindi hiki ambacho ni kigumu
kwake. Sio jambo la siku moja. Na si kazi rahisi au maneno tu. Taratibu.”
“Nitasubiri mama. Naona yeye ananielewa.” “Anza taratibu. Sasahivi mpelekee hii juisi na snack.
Anapenda kula. Hapo utampata. Akishakupokea hivyo, muulize siku yake ilikuaje.
Hakikisha yeye ndio anazungumza. Mpe muda na endelea kumdodosa katika hilo.
Hapo ndio atajua unamaanisha swali lako, kwamba kweli unataka kujua siku yake
imeendaje. Maana lasivyo atakujibu tu nzuri, wakati kuna mengi yanayoendelea, hana wakumwambia.”
“Ukifanikiwa kumpa sikio
lako, akajua unamjali yeye kama yeye,
jua ndio unamsogeza karibu yako. Si
vinginevyo. Hajajaliwa tamaa za wanawake kirahisi. Usimuone hivyo. Kwa hiyo muonekano
tu, au uzuri tu wa mwanamke, havimchanganyi.” Akazungumza naye kwa sauti ya
chini sana akimnong’oneza. Akamuona ameelewa. “Haya mfuate.” “Chumbani kwake!?”
“Popote alipo, akakupokea na kukukaribisha, ndio hapohapo. Nenda.” Akamkabidhi
vitu, akatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
Kila jambo na wakati wake.
Je, huu ni wakati mwafaka kwa Colins
anayehangaikia kulipiza kisasi na kumtoa Jelini kwenye kesi anayojilaumu yeye
amemsababishia! Kwamba
amepewa sumu na Love
aliyekuwa mpenzi wake yeye, japo na Kemi bado yupo! Mama Colins anamuunganisha Kamila, ni wakati muafaka?
Chris amejirudi. Japokuwa anawatetea
kina Kemi&Love lakini anafuata muongozo wa Colins, atachezaje hizo karata
mpaka kumridhisha Colins asimuharibie kwa mkewe na jamii?
INAENDELEA.
0 Comments:
Post a Comment