Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 21. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 21.

Wakajikuta wametulia hapo mezani, kila mtu anawaza lake, Colins kapotelea mawazoni, na yeye akabaki akimwangalia huku akiwaza. Chakula kikaletwa. Kama kawaida ya Colins, linapofika swala la mlo, hana kujivunga. Akala chakula chake mpaka akamaliza.

“Unauhakika hutaki hata kubeba kitu? Usije umwa na njaa usiku. Maana najua pale nyumbani hakuta pikwa. Wazazi hawatakuwepo.” “Wamesafiri!?” “Baba amemtoa mkewe kwa usiku mmoja tu. Kesho wote wanatakiwa kazini. Itabidi warudi.” Kamila akanyamaza, Colins akalipia na kumwambia waondoke bila ya kurudia kumuulizia chakula, akijua amekataa.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wakiwa njiani akawaza kwa sauti. “Nimemiss Mike!” Colins akamsikia. “Pole. Ila angalau ukweli wa kesho utasaidia kukutoa njia panda.” “Kwa ukweli wowote ule mbali ya kuwa nampata tena Mike, kwa hakika maisha yangu hayatakuja kuwa kama zamani.” “Nakuelewa kabisa. Kunaweza kukawa na mwanzo mpya, ambao huwezi jua Kamila. Unaweza usiwe mbaya sana.” “Sijui! Sidhani kama nitakuja pata mtu akanipenda na kunijali kama Mike.” Colins akatulia akitafakari. Kimya kwa muda hapo garini.

“Mimi naamini hivi.” Akavunja ukimya. “Ukiwa tayari kupokea huo upendo na kujaliwa, naamini hivi, ukifungua moyo, na ukampa mtu nafasi, kama uliyompa Mike. Kukufahamu vizuri na kukuelewa. Na wewe ukaruhusu moyo wako kumpenda, anaweza asiwe Mike, ila ukashangaa vile Mungu alivyo wa ajabu, kwa kukutumia upendo mwingine wa tofauti.”

“Wewe upo tayari?” “Kwa sasa, tena kwa mara ya pili, bado. Sidhani.” “Unamaanisha nini kwa mara ya pili?” “Jelini ndio alikuwa upendo wangu niliokuwa nimetumiwa na Mungu nikiwa nimekata tamaa. Lakini mimi nilichezea bahati yangu ndio maana naona nisubiri kwanza nisije harakisha nikaharibu tena.”

 “Wanasema third time is a charm. Ndio maana naona niongeze umakini nisikimbilie. Nisije haribu. Kwa hiyo kwa kujibu swali lako, kwa sasa hapana. Ndio maana nakwambia usiogope. Utakuwa sawa. Kwa kuwa nina uhakika. Mungu hakutengeneza Mike mmoja tu. Anao kina Mike wengi tu. Ni wewe tu kufungua moyo na kutoa muda. Utakuja zisimulia kumbukumbu za Mike si kwa kuumia, ila kwa furaha ukisaidia wengine kuwa, Mungu hajaishiwa kina Mike, endapo hatarudi. Na kama yupo dunia hii, nakuahidi kukusaidia mpaka umpate Mike wako.” Kidogo akacheka.

“Umefurahi sasa?” “Kidogo. Umenifariji. Asante.” “Na ili ulale vizuri, kwa kuwa hujala, tukifika nyumbani nakutengenezea mayai mawili tu. Ukila hayo nitakuwa na amani utalala kama jana. Nataka uamke kama leo.” Hapo akaupata moyo wa Kamila. Dhambi zote akasamehewa. Akasahau hata ya asubuhi. Angalau akaanza kuzungumza. Stori zikaendelea.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Ahadi ya mayai bado ipo?” Akauliza wakiwa wanaingia. Nyumba ilikuwa kimya. Kuashiria hata msichana wa kazi ameshalala. “Kabisa. Au unataka chakula kabisa?” “Hata nikitaka chakula tutapata wapi sasahivi?” “Nakupikia kwa haraka.” “Kwamba wewe unajua kupika!?” “Sana tu. Mbona umeshangaa!” “Sijategemea! Huonyeshi kabisa!” Colins akacheka tu. “Mike alikuwa hajui kupika hata chai! Ukimnyima chakula ndio basi.” Hapo hakuchangia. Akanyamaza.

“Ila mayai yatatosha. Naenda kuoga kabisa.” “Kama ni hivyo acha na mimi nikaoge. Sitachelewa. Utanikuta jikoni.” Wakaachana kila mtu akaenda chumbani kwake.

Baada ya muda akamfuata jikoni. “Vinanukia! Ni yai tu hilo?” “Nimeona nifanye omlet ili ushibe vizuri. Kaa.” Akakaa akicheka. “Nini sasa?” “Ujue weweni bosi wangu, mkubwa sana! Halafu nakutumikisha!” “Tukiwa kazini. Sio hapa. Na hunitumikishi.” Akamuandalia na glass ya maziwa. Akamuwekea mbele yake. Akala kama aliyekuwa na njaa. Colins macho kwenye simu yake.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Jana nililala vizuri kwa kuwa nilijua tupo wote.” Colins akatoa macho kwenye simu na kumuangalia kama aliyekuwa amezama kwenye simu. Akamuona analamba midomo yake taratibu na kuingiwa na aibu za kike. Ila alishajua kuna namna akiwa ametulia akimwangalia msichana, wengi hubabaika.

Kule kulamba midomo yake alijua ni sababu ya midomo yake. Alichukua midomo yenye rangi ya pinki kama nyekundu kutoka kwa mama yao. Alivutia na kubabaisha wengi. Sasa alipomgeukia Kamila, mwili mzima wa Kamila gafla ukapigwa kama shoti ndogo ya umeme, akasisimkwa mpaka akalamba midomo yake.

 “Samahani. Umesema?” Akamuuliza na ile sauti yake ya kiume iliyotulia ila kwa sura ya makini kidogo iliyombadili mawazo mrembo. “Asante kwa chakula.” Akabadilisha. Colins akajua ila akaona amuache tu. Tokea mwanzoni alimsikia vizuri tu, ila alitaka uhakika na alichozungumza. Na pia hakutaka wajenge mazoea ya kulala pamoja.

“Umeshiba lakini?” “Ndiyo. Nashukuru.” Akajibu kwa kunyongea kidogo. Colins akamtizama na kurudisha macho kwenye simu. Akamsikia akiondoka na vyombo mpaka kwenye sinki akaanza kuviosha.

Akajiiba kumwangalia. Ukweli Kamila alikuwa akivutia. Lakini alikuwa bado ana mambo mengi yanayoendelea kwenye maisha yake. Colins hakutaka kuanzisha jambo lolote lile hata dogo kwa namna gani linalo muhusu yeye binafsi au kujiingiza kwa namna yeyote ile itakayo mchanganya zaidi yeye Kamila au hata yeye mwenyewe. Akabaki akimwangalia kwa nyuma mpaka alipomaliza ndipo akarudisha macho kwenye simu.

Akahisi anamsogelea kwa hofu. Akamuacha tu mpaka akafika pale na kurudi kukaa ila safari hii akasogeza kiti karibu. Colins akamwangalia. “Upo sawa?” Akatingisha kichwa kukubali.

 “Twende ukalale.” “Na leo utanisubiria nilale au hutaki kujenga mazoea?” Ikawa kama amesoma mawazo yake. “Jana nilipitiwa na usingizi kitandani kwako. Unajua?” “Ndio maana nililala vizuri. Kila nilipokuwa nikigeuka nikikuhisi, nikawa narudi kulala bila shida. Nilijua.” Colins akatoa tabasamu akimwangalia. Eti akaona aibu.

“Kwa nini vibaya?” “Wewe unaonaje? “Mwenzio napenda.” Colins akaanza kucheka. Hakutegemea. “Usinicheke bwana. Nakua siogopi. Au wewe unaona ni vibaya?” Akarudia swali. Akamuona anafikiria kidogo kama anayetafuta jinsi ya kuongea.

“Vibaya, hapana. Sidhani kama vibaya ni neno sahihi. Lakini sioni kama n i sawa.” Akaumia sana moyoni. Kamila alijijua ni mzuri na hajawahi kuwa na mwanaume karibu yake, asivutiwe naye. Leo anampa Colins bahati japo ya kuwa naye kitanda kimoja anakataa! Ikamuuma sana na kushindwa hata kumtizama. Akaangalia chini kwenye mikono yake. Akabaki akiweka vidole kwa kila mtindo.

“Sidhani kama ni sawa tukiendelea kulala wote Kamila. Sio mazoea mazuri. Ila nakuahidi kubaki na wewe mpaka utakapo lala. Na u a. “Acha mimi nikalale.” Akasimama kabisa na kuanza kutoka hapo jikoni. “Kamila?” Akamuwahi kabla hajatoka. Akageuka na uso ulioumia haswa. “Usiku mwema Colins. Kesho.” “Na wewe. Ila usisite kunipigia ukiogopa. Nitakuwa chumbani nikifanya kazi kidogo.” “Naona nijizoeshe tu mpaka niweze. Siwezi kuwa tegemezi daima. Usiku mwema.” Akaondoka.

Akatamani amfuate ila akaona asimamie maneno yake. “Mwisho wa yote ni nini kama si kuchanganyana tu?” Akawaza Colins. “Yupo mwanzoni sana mwa maumivu yake. Hajapitia hata hatua ya kwanza ya tukio lake la mapenzi. Hajaamini kama kweli Mike amepotea. Bado kabisa. Nikianzisha jambo hapa, akimaliza kuomboleza na kichwa kikakaa sawa, mimi nikiwa nilishaanzisha jambo, akagundua alikosea? Hapana. Acha tuache tu hivihivi.” Akaafikiana na mawazo yake. Akazima taa pale jikoni na kurudi chumbani kwake na yeye.

Dhambi Haiozi.

Kesho yake ilikuwa siku ya kusikilizwa tena kesi ya yule mmiliki wa ile hoteli na kina Kemi, kwa swala la ile sumu aliyowekewa Jelini. Na Jelini alitakiwa mahakamani. Akafikiria jinsi ya kusaidia. Akajua njia sahihi ni kumpunguza makali Chris.

Safari hii akamtumia kwenye simu yake kabisa. Ule ujumbe wa Zulfa wa kumshutumu kuwa alimlazimisha kutoa mimba, halafu akamuacha. Akamtumia na picha alizozikuta kwenye kumbukumbu za zamani za Zulfa walizopiga pamoja kwa kificho. Kisha akamtumia ujumbe, ‘fikiria tu jinsi magazeti yatakavyopendeza kwa taarifa hizi.’ Akatuma usiku huo akijua wazi kama hayupo nyumbani kwa mkewe, basi yupo ofisini akijiandaa na kesi ya kesho yake. Akajua atamchanganya tu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akacheka na kuangalia simu yake kuona kama Kamila alimtafuta. Akaona hakuna jumbe wala missed call. Akajua amelala kumbe mwenzie analia. Aliingia chumbani kwake na kujifunika mto usoni, kilio kikaanza. Alilia kwa uchungu sana akikumbuka enzi zake na Mike, akiwa malikia katika ufamle wake, huku watu wakimfuatilia kwa sifa kemkem huko mitandaoni. Leo hana  thamani tena! Kilio kikazidi.

Yeye Colins alipomaliza yake mtandaoni, akajiweka kitandani, hapohapo akapitiwa na usingizi kama mtoto asijue alipo mpaka alamu ya asubuhi ilipomrudisha kwenye ulimwengu wa wenye mengi.

Asubuhi.

 Akakimbilia kuoga. Wakati akivaa akagundua ile simu yenye namba ya Mike ina ujumbe. Akajua Kamila amemuandikia Mike. Akapata hamu ya kujua alichoandika akiwa na uhakika ni ujumbe wa usiku uliopita. Akakaa na kuanza kusoma.

‘Mike! Niitikie mpenzi wangu. Hakuna mtu mwingine ananiona vile jicho lako linaniona. Nimebakia kichekesho na mtu wa kudharauliwa na watu. Uzuri uliosema ninao, kumbe ni jicho lako tu. Lakini sivyo nilivyo kwa wengine. Natamani kurudi kuwa na wewe uliyenijaza bila kuacha nikiwa nimepungukiwa. Moyo wangu unalia kwa uchungu na upweke. Usiku umegeuka kuwa tishio sio kama ilivyokuwa ulipokuwa na mimi. Usiku ulikuwa ni muda wetu. Ulimwengu mzima hunyamaza, nakubakia sisi tu. Naogopa Mike. Nisaidie mpenzi. Rudi kwangu.’

Alishituka sana baada ya kusoma, akajua inamaana usiku hakulala vizuri. Akajisikia majuto kumkatalia kulala naye. Lakini akabaki akifikiria. Kwahakika akajihisi hayupo tayari kulala naye tu. “Nitafanya hivyo mpaka lini! Mwisho wake ni nini! Halafu ndio tunakuwa tukifanya nini hicho!?” Akajiuliza na kukosa jibu. Akaona amalize kujiandaa atoke akaangalie anaendeleaje.

~~~~~~~~~~~~~~~

Chakushangaza akamkuta alishaamka, akamuandalia kifungua kinywa kizuri, yupo tayari anamsubiria mezani, ila amejiinamia. Alipomsogelea akasimama kama aliyemfumania. Akagundua alikuwa ameinamia simu yake. Alijawa wasiwasi na hofu. Uso ukawa kama alivyomkuta siku za mwanzoni.

“Ulilala salama?” “Leo nitajua ukweli juu ya Mike. Naamini Luca hatanidanganya.” “Nafikiri watamuwekea mazingira ya kutodanganya na pia tutahakikisha anatoa uthibitisho.” “Hapo sawa. Maana wasije danganya, kumbe Mike yupo sehemu.” “Ulipata muda wa kulala hata kidogo?” “Ndiyo.” Lakini alionyesha wazi hakulala muda wa kutosha.

“Nimekuandalia kitu cha kula ili twende kazini ukiwa umeshiba.” “Kaa tule wote.” “Naona nitatulia nikishazungumza na Luca nikajiridhisha hanidanganyi. Natamani jibu la kuwa Mike yupo sehemu! Mike ananielewa, Colins. Ananijali hata vile ninavyojisikia. Vile vitu vyangu vyakijinga kwa wengine, kwake ni muhimu, hapuuzi na hanichoki. Nitapata wapi mtu kama huyo hapa duniani? Siwezi ishi bila Mike.” Ile hofu ya mwanzoni ikajirudia kabisa. Akawa kama amechanganyikiwa.

“Naogopa Colins! Naogopa sana. Bora unisaidie nimpate Mike.” “Naomba tulia Kamila. Na naomba usilie. Tutakwenda kuzungumza na Luca kisha tutachukua hatua kuanzia hapo. Usiogope. Sawa?” Akatingisha kichwa akijifuta machozi.

“Umependeza sana. Itabidi mzee Yusuf akuone kabla hujabadili.” Kidogo akacheka akiendelea kujifuta machozi. “Mwenzio nimevaa vizuri nikijiandaa pengine leo nitakutana na Mike!” “Basi ua ndege wawili kwa jiwe moja.” “Nikamringishie mzee Yusuf kwanza?” “Kabisa.” Akacheka taratibu. “Utakuwa sawa Kamila. Usiogope.” Akatulia tu hakujibu. Ila akagundua si mtu mgumu kuishi naye. Anaridhishwa na vitu vidogovidogo.

 Akala kwa haraka wakatoka hapo angalau akiwa ametulia. Haikuchukua muda akapitiwa na usingizi. Akajua ni kweli hakuwa amelala, anausingizi. Akapunguza sauti ya radio ili alale.

Alifika mpaka sehemu ya kuegesha magari hapo hospitalini, hakuzima gari ili A/C iendelee na alale kidogo. Akabaki akifikiria mpaka akarudi kwa Jelini na siku ya kesi yake siku hiyo. Jinsi ya kumsaidia pekee ili asiulizwe maswali ya kumuumiza zaidi yeye akiwa muhanga ikabaki ni kumchanganya zaidi Chris.

Bado ilikuwa mapema tu. Akavuta mkoba wake wenye ile laptop yake. Akamuandikia ujumbe Chris. ‘Wakati ukiendelea kuharibu vizazi vya mabinti za watu, ukimwaga damu zisizo na hatia, huku ukigaramia pesa nyingi kwa mkeo azae, na kuhakikisha unamficha asijue kinachoendelea, jua vilio vya watoto unao waua nje, vinakufuata mpaka kwenye kitanda chako cha ndoa, na huyo mtoto mmoja Mungu aliyekupa ni kusudi kukukumbusha watoto unao waua huko nje.’ Akamtumia na jumbe alizokuwa akitumiwa na Zulfa alipotoa mimba na baada ya kumfungia simu zake.

‘Mkeo na Magazeti yanayopenda kukusifia kila unaposhinda kesi ukiwadhulumu wasio na hatia, watapenda sana kuona haya.’ Akaongeza na huo ujumbe.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akabaki akitafakari mawili matatu. Akiwa hana uhakika wa kujibiwa, lakini akaonelea kumtumia ujumbe na Jelini.

   ~~~~~~~~~~~~~~~

Ø Anataka kumwambia nini Jelini?

Ø Je, Chris amepata ujumbe? Atafanya nini?

Ø Ukweli juu ya Mike unamkabili Kamila ambaye anaamini kurudi kwake, au kukutana naye siku hiyo. Ni nini kitaendelea?

INAENDELEA.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment