Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 20. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 20.

Kamila aliamka kama aliyelala kweli. Akatoka akiwa amependeza. Colins 
akacheka. “Sasa wewe mpishi ndio unapendeza kama unakwenda kufanya kazi za ofisini!” “Nina kuwa na nguo za kubadilisha kabisa. Apron na kofia yake. Mwenzio napenda kazi yangu. Sitaki mtu adharau.” “Basi Kamila. Naona utanifanya niangalie ofisi yako kwa jicho jingine.” “Sasa tena sio na wewe ukaombe kazi hapohapo! Sisi tumeshajaa.” Colins alicheka asiamini.

    “Siamini Kamila!” “Wewe bakia kulekule juu, usianze tamaa. Mwenzio kule nimepata mchumba, mzee Yusufu ameniambia kwa mara ya kwanza, anamuolea mkewe, mke wa pili.” “Wewe huyo?” “Wewe usinione hivi.” Colins kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu wa machungu akasikika akicheka.

     “Kwa hiyo usiniambie kupendeza huku ni kwa mzee Yusufu!?” “Hataniona. Naenda kubadili kwanza, ndio niende, ili anione namaanisha kazi. Wameniambia ndio kiongozi wao pale, hataki mchezo. Mkali sana. Ila mwenzio mimi nimependwa. Dula kaniambia.” Colins hana mbavu.

    “Ila ujue mzee Yusufu mkristo!” “Dula kwa wivu wake na yeye alisema hivyohivyo, ila mzee Yusufu ameniambia nisiwe na wasiwasi, mimi anaenda kuniolea bomani.” Colins alicheka kwa sauti, asiamini kama Kamila ndio yupo hivyo! “Kamila!” “Mwenzio nilikuwa na usingizi tu. Jana nimelala vizuri. Sijaogopa wala kushituka mpaka alamu.” Wakawasikia wakitoka wanaongea.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Wakataniana kidogo tu wakiwa njiani, akamuona Colins amepotelea mawazoni kabisa. Akajua ni Jelini ndiye anayewazwa. Akataka kuhakikisha maana alisikia kidogo  mazungumzo kati yake na mama yake. “Pole Colins.” Bila kufikiria kama aliyekuwa akiwaza naye akajikuta akisema, “Aisee maisha hayatabiriki! Ukiambiwa Jelini anaolewa na mwanaume mwingine na si mimi! Nahisi kama ndoto!” Akajua ni kweli.

    “Usingekubali. Ningekuwa mimi kwa Mike, ningempigania.” “Mimi si kama Mike, Kamila. Mike alifanikiwa kuweka kumbukumbu nzuri kwako ndio maana unasema hivyo. Kwangu imekua kinyume. Jelini alinipenda sana. Alinipenda vile nilivyo. Lakini tokea mwanzo wetu, namaanisha siku ya kwanza, nimekua nikimuumiza. Sikumbuki kuacha kumbukumbu kwake ya kumfanya aniimbe kama hivyo wewe kwa Mike.” Kamila akainama.

    “Yeye alikuwa na sababu zote za kuniacha toka siku ya kwanza, lakini mapenzi ndio yalimfanya abaki akinivumilia na kunisubiria akiamini ipo siku nitatulia naye. Lakini nimechelewa. Na aliyeniwahi amefanikiwa kuweka msingi mzuri, halafu kikubwa zaidi, amefanikiwa kupata ahadi ya Jelini ambayo ni kila kitu. Jelini hajipingi kwenye ahadi zake.” Akaamsha maswali kwa Kamila.

    “Unamaanisha nini kuwa yeye aliweka msingi mzuri na sio wewe?” “Jelini ni mzuri sana. Sana.” Wivu tayari kwa Kamila. “Ukimuona kwa haraka unaweza fikiria hongo yake ni nyumba na magari, kwa jinsi alivyojaliwa thamani ya muonekano. Mzuri na anajipenda sana. Lakini pia alijaliwa moyo wa tofauti. Ana upendo usio na unafiki. Yeye hongo anayotaka ni kupendwa tu. Na kilio chake tokea namkuta, anataka mtu wa peke yake, kitu kinachosikika rahisi lakini nilishindwa kumpa.” Akamshangaza kidogo.

    “Kwamba ulikuwa na wanawake wengi?!” “Jelini mmoja, ni kama wanawake 10 kwa mpigo, ila aliyebeba zile tabia zao bora tupu.” Mpaka Kamila akashangazwa. “Ukiwa na Jelini, huwezi hata fikiria mwanamke mwingine. Kwanza kuna jinsi anakuwa mikononi!” Akamuona anavuta hisia nzito, wazi zilijaa penzi. Akamuona amepotelea kabisa mawazoni. Kimya na uso wa huzuni ukawa bayana. Hakuzungumza tena alichotaka kuzungumzia juu ya huyo Jelini. Akawa amekwama kwenye hizo fikra za mapenzi. Kamila naye akaamua amuache mpaka wanafika kazini na kuagana.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Kwenye mida ya saa nne asubuhi baba yake akampigia. Akaiangalia kwa muda mrefu karibu inakatika ndipo akapokea bila hata kuitika.  “Kama nitakuwa nimekosea tena, basi unisamehe. Lakini nia ni kusaidia.” “Umefanya nini tena baba jamani!” “Sio kitu kibaya, ni juu ya Kamila.” Nusura asimame kwa mshituko.

    “Umefanya nini tena!?” “Niliona niwasaidie tu zaidi yeye kumtoa kwenye sintofahamu. Tokea uliponiambia juu yake na alipokwama juu ya mumewe.” “Hakuwa mumewe. Maana nashangaa kwa muda wote huo ameishi na msichana kama Kamila asimuoe! Sidhani kama ni sawa. Hastahili kuitwa mume. Muite tu Mike.” Akajikuta anapandwa jazba kwa jambo ambalo halikuwa la msingi na wala hakuwahi kuliwaza. Akashangaa hapo analipuka. Wivu tayari. Wakati na yeye aliishi na Love bila ndoa.

Mzee akashangaa kidogo. “Ila kisheria anatambulika kama mkewe kihalali! Hawa watu wameishi zaidi ya miaka miwili! Lakini hilo silo lililonifanya nikupigie.” Mzee akawahi kabla hajaharibu.

“Japo hilo limesaidia kwenye hili ninalotaka kukwambia. Kama sio muda mzuri, tunaweza zungumza hata wakati mwingine.” Colins akajaribu kujirudi maana na yeye alijishitukia.

“Imekuaje?” “Nilimtafuta mwanasheria na kuomba amsaidie kisheria kupata taarifa kamili juu ya Mike. Nilimueleza hali ya Kamila na ndugu za Mike. Nikamwambia yeye hataki mali, ila tu ukweli. Ndio akasema atafuatilia kwa hao ndugu akiwatisha kuwa Kamila ana haki zote kama mkewe, anaweza kuwafilisi endapo akiamua, lakini yeye hana shida hiyo, anataka ukweli tu juu ya Mike.” Colins kimya akisikiliza.

“Ametoka kunipigia simu kuwa ameweza kumpata na kuzungumza na Lucas, kama kiongozi wa familia, yupo tayari kwa mazungumzo na kujibu maswali yote ya Kamila.” Colins hakutegemea.

 “Asante sana baba. Utakuwa umemsaidia sana kuendelea na maisha yake. Asante.” “Karibu. Na naona ameshafuatilia huko Wizara ya Vizazi na Vifo. Amehakiki kuwa kweli Mike amefariki kwa kuwa cheti chake na kifo kilishatoka na kilishapelekwa mahakamani. Kwa hiyo taarifa za hapo hospitalini ni sahihi. Mike alifariki muda, na siku hiyo uliyoona hapo hospitalini. Kwa kufupisha habari ili nisikuchukulie muda wako zaidi, taarifa zahapo hospitalini juu ya Mike zipo sahihi.”

“Nakushukuru sana baba. Hili ni jambo kubwa sana kwa Kamila. Ni sawa leo jioni tukutane nao?” “Nitamtaarifu kisha atakupigia. Kila la kheri.” “Nilifikiri utakuwepo!?” “Baada ya muda mrefu sana, mke wangu ana raha. Siwezi subiri, nishatafuta sehemu, nampeleka hata kwa usiku mmoja tu. Kwa hiyo leo usiku hatutakuwepo nyumbani.”

“Naomba umwangalie tafadhali.” “Wala usizungumze kama unanionya mimi! Wewe ndiye unayempa pressure mama yako wala si mimi. Wewe ukitulia, ujue ndio pona yake. Ukiendelea hivyo kwa hakika utamuua.” “Ila na wewe pia unahusika baba. Usitupe lawama kwangu. Wewe ndiye uliyeanza, ukamuingiza kwenye mambo ya Jelini. Wewe ndiye uliyemsababishia maradhi. Sio mimi.” “Tangia unazaliwa mpaka sasa na ukubwa wako huo, ushawahi sikia mimi nikimfoka mama yako hata mara moja?” Kimya.

“Wewe ndiye uliyekuwa ukimfoka na kumsukumizia mbali wakati unajua wewe na Connie ndio kila kitu kwa mama yenu! Aliacha maisha yake yasimame, akabaki kuwalea nyinyi kitu ambacho mama Simba anamsimanga nacho mpaka leo! Halafu unasahau hilo, unamfukuza kwenye maisha yako! Unamsimanga kwa makosa yangu na kusahau garama yote anayolipa kwetu sisi wote watatu! Hutaki akuuguze! Hutaki akusogelee! Mkali kwake! Unaleta mtu baki akuhudumie na ungali unajua jinsi anavyokuthamini! Wewe ulitegemea nini?”

“Wewe ndiye uliyenisababishia baba. Wewe ndio chanzo cha yote.” Akaendelea kujitetea ila si kwa jeuri kama mwanzo. “Kwa hiyo ukaona adhabu yangu ili iniume vizuri, ni uniadhibie mke wangu? Mwanadamu asiye na hatia ila upendo tu.” Kimya. Safari hii baba yake na yeye akamkatia simu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Hiyo siku ikavurugika kabisa kwa Colins. Hukumu huku akijitetea nafsini mwake. Akajitetea kwa hili na lile, ukabakia ukweli juu ya mama yake. Kamila anakuja kumletea chakula cha mchana, akamkuta tofauti. Akajua ni sababu ya Jelini tu, kumbe mwenzie ana vita kali inaendelea nafsini kwake.

Hakumuongelesha sana zaidi ya kushukuru kwa chakula na kutaka kujua anavyoendelea huko. Tena kama bosi kwa mfanyakazi tu. Akaona amuache, aondoke zake. “Anaonekana anampenda sana Jelini. Ngumu kwake hata kuwa rafiki wa kawaida na mtu mwingine.” Akaanza kujilalamisha akiondoka. “Lakini kwani mimi nilimwambia nina nia naye mbaya! Si ni urafiki tu wa kawaida!” Akaendelea kujilalamisha nafsini kwake na yeye.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika mida ya jioni ndio akili ikamkumbuka Kamila. Akaweza kurudisha simu ya huyo mwanasheria. Wakazungumza ndipo akampigia na Kamila. “Umeshinda salama?” “Ndiyo.” “Mbona kama umepoa? Mzima?” “Mimi nipo sawa tu. Tunamalizia kuweka sawa hapa jikoni.” “Mbona kama huna raha na wakati asubuhi uliamka vizuri. Ni nini kimekuudhi tena na kukuchukulia furaha yote!?” Asijue alishampoteza tokea kwenye gari wanaelekea hapo.

“Nipo tu sawa, Colins. Vipi wewe? Nilikuja ulionekana busy!” “Sio sana. Mambo mengi yanaendelea.” “Pole.” “Mimi nipo sawa kabisa, ila nina habari njema. Ukimaliza njoo.” “Sawa.”  Baada ya kama lisaa na nusu akawasili.

~~~~~~~~~~~~~~~

Colins akamwangalia akiacha kila kitu. “Asubuhi ulivutia zaidi sababu ulikuwa na furaha. Sasahivi umenyongea! Ni nini?” “Hamna kitu. Niambie habari njema.” “Kama kungekuwa na kitu, ungeniambia?” “Chakuzungumzika ndiyo.” “Ni vitu gani havizungumziki?” Akanyamaza akiangalia chini.

Colins akatoka kabisa mezani, akavuta kiti akakaa karibu ila mbele yake. “Niangalie Kamila.” Akamwangalia. “Ni nini?” “Nafikiri mimekua na siku ndefu tu. Nipo sawa.” “Bado unafurahia kule jikoni?” “Ni watu wazuri. Nafurahia. Umeniambia kuna habari njema. Ni nini!?” Akamsimulia alichofanya baba yake, na mazungumzo aliyotoka kuyafanya na huyo mwanasheria, Kamila asiamini. Ila hakumwambia juu ya cheti cha kifo. Akaona akajulie hukohuko.

“Kwa hiyo unanafasi ya kukaa na Luca. Ukamuuliza maswali yote unayotaka mpaka ukaridhika. Na anawajibika kisheria kukujibu.” “Naomba twende leo.” Akaangalia muda. “Nahisi tumechelewa, lakini acha nimpigie tena simu tuone. Maana nilipozungumza naye aliniambia ukiwa tayari umtafute. Anaonekana na mtu mzuri.” “Nitashukuru Colins. Acha nijue ukweli juu ya Mike, pengine itanisaidia kutulia kimawazo na kujipanga upya.”

~~~~~~~~~~~~~~~

Akampigia na yeye akapokea bila ya kuchelewa. Akamwambia kama wanaweza kukutana mida hiyo. “Nashauri tuandae mazingira ya kiofisi. Nimpigie simu Lucas, tupange tukutane ofisini kwangu. Au unaonaje? Ili tusipeleke mambo kiholelaholea, ikakosa uzito.” “Naona wazo sio baya. Kwenye  mida ya mchana ni sawa?” Wakapanga na kuagana.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akarudisha majibu kwa Kamila. Akaridhia. Wakaondoka hapo ofisini. Kamila akiwa ametulia. Akaona amuache tu, akijua ni mambo ya Mike, kumbe na yeye anachangia na kumuacha ndio anazidi kumuumiza Kamila aliyezoea kufuatilizwa na Mike. Kimya safari ya kurudi nyumbani.

“Njaa unaniuma Kamila. Naomba tupitie sehemu tule ndio turudi nyumbani.” “Hutaki kwenda kula nyumbani? Leo jioni sikupenda kilichokuwepo pale ndio maana sikukuletea. Ila naweza kwenda kupika nyumbani.” “Kwanza huwajibiki na kula yangu kabisa. Tafadhali usijiongezee hiyo kazi.” “Mimi napenda. Sioni kama ni kazi.” “Kama hivyo sawa. Ila sitaki ujione unawajibika na kula yangu. Ukiweza sawa, ukishindwa pia ni sawa. Unanielewa? Sitaki niwe moja ya jukumu lako.” “Sawa. Lakini naweza kwenda kukupikia nyumbani.” “Nashukuru, lakini nahitaji kula sasahivi, sitaki kusubiria zaidi.” Wakatafuta mahali kwenye vyakula vizuri, wakakaa hapo.

Wakati mtu wa vinywaji amekuja anataka kuwahudumia vinywaji, akatoa na oda ya chakula. “Aisee siwezi subiri.” Kamila yeye akataka soda tu, akasema ameshiba. Colins akajua ameshakula jikoni. Akamuacha. Kumbe Kamila anazidi kuumia kwamba kwa nini hajajali kutokula kwake, Colins hana habari.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wamekutana watu wawili wenye historia mbili tofauti. Kamila aliyekuwa malkia kwenye ufalme wa Mike, kabla hajalia shida, Mike amefanya. Na Colins ambaye bado ana mengi anayofikiria kichwani. Visasi na mapenzi. Akili haijatulia kufikiria vizuri. Kila siku anaiendesha kwa kadiri inavyomjia zaidi kwa mrembo Kamila, lakini moyo upo kwa Jelini, akisubiria pengine atabadili mawazo au muujiza utatokea, Jelini amrudie yeye. Hivyohivyo Kamila akitumaini pengine Mike atakuwa sehemu atakuja kurudi.

Ila je asiponirudia!? Likabaki swali la kila mmoja wao hapo.

Ndio wamebaki mguu mmoja ndani mwingine nje kwa walichonacho na wanachojisikia.

Si kuharibu kabisa chochote walichonacho lakini pia tahadhari wasije jifunga halafu wenza wakarudi wakawakuta kwenye mahusiano mengine.

Full kujiwinda, ila hisia ndio mchanganyiko.

INAENDELEA.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment