Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 19. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 19.

Akameza mate akiangalia kile chumba na mizigo yake. Akazungusha macho chumba kizima. Colins akimtizama akiwa bado na hasira ila
akitarajia jibu la kubaki kwake. Na yeye akasimama wima, mikono mfukoni. Kama usinibabaishe. Hasira zimemuwaka, amekumbushwa mbali.

    “Lakini pia nilikununulia kofia zinazofanana na hizo zako. Mike hakuwa mpenzi wa kofia kama wewe, labda bichi au sehemu ya jua kali.” Colins hakutegemea. Maana aliongea kwa upendo na unyenyekevu. “Sidanganyi Colins. Nilinunua kutokana na nilivyokuona wewe. Sema sasahivi nimeshachanganyikiwa sijui zilipo.” Alikuwa akitetemeka, mpaka Colins ikabidi ajirudi.

    “Pengine ipo ndani ya hiyo mifuko uliyoshika.” Ndiyo na yeye akawa kama amegutuka. Akajiangalia, akagundua amejikumbatia na mifuko. Akatoa kwa haraka kwa bahati mbaya ile chupa ya perfume akaigonga ukutani kwa nguvu upande wa pili, mpaka inatua sakafuni, harufu ya manukato yakaanza kuenea hapo taratibu. Kwamba imevunjika.

    Hakujali, akaangalia mfuko mwingine, akakutana na hizo kofia. Akatoa kwa haraka akiwa amepaniki. “Hizi hapa mbili. Angalia. Zinafanana na hiyo uliyovaa. Sema moja ni nyeusi, nyingine nyekundu. Maana nimeona unavaa nyeupe. Na nimenunua hizi sio kwa kutaka kukubadilisha. Ila nimesema kama utataka kuvaa rangi nyingine. Ila ikileta sura mbaya, basi. Nitampa mtu mwingine au hata kuzitupa.” Akawa anamuonyeshea ila kama anayeogopa kumpa.

    Colins mwenyewe akapoa. Akajua amemmalizia yeye hasira za wote. “Usikasirike Colins. Nimekosea. Usinichukie, sijakusudia kukuku…” Akamsogelea na kumshika kabisa mkono ambao viganja vilikuwa ndani ya mfuko wa suruali, ila akamshika kiwiko kwa juu.

    “Samahani. Mimi nimekosa. Usiniache hapa. Naogopa sana.” Akaingiwa na huruma. Kamila ni mnyenyekevu ambaye hajawahi ona! Alitegemea angesusa, na kuamua kubaki. Kwanza pesa anayo, shida yake ni watu tu.

    “Nisamehe.” Akarudia kwa upendo na kumtia hukumu. Akajisikia vibaya! Akaona ameua mbu kwa bunduki. “Basi yameisha. Na mimi unisamehe Kamila. Inawezekana nimezungumza kwa ukali. Lakini nimemaanisha kila nilichokwambia. Watu wamenichezea sana, na wamenirudisha nyuma! Isingekuwa kuzembea kwangu, mimi ndio ningekuwa nikimuoa Jelini sasa hivi. Lakini niliruhusu kila mtu kuingilia maisha yangu nikifumbia macho mambo niliyojua wazi yananitenga na Jelini.”

    “Nipo hapa mpweke si kwa bahati mbaya, ni kwa kuzembea kwangu. Siwezi kuruhusu tena. Mwishoe nitakua mtu wa kuanza kila wakati, nibaki kichekesho daima. Hapana Kamila.” “Sitarudia tena. Nimekosa, nisamehe.” “Basi twende nyumbani. Watakuwa wakitusubiria. Huwa wanawahi kulala sababu ya kazi siku inayofuata.” Ukweli hiyo harufu ilienea vizuri sana hapo chumbani, mpaka Colins mwenyewe aliipenda.

    Nzuri, imepoa. Akajua ni ya pesa nyingi. Akainyamazia tu. Wakati anamsaidia kuweka vitu vyake kwenye gari yake, akamuona akiokota vipande vyake vya chupa ili atupe. Akafanikiwa kusoma jina lake. “Angalia usijikate.” Akawa kama amemgutusha mawazoni. Akasimama, maana alikuwa amepiga magoti akikusanya hivyo vipande. Hakujibu ila akarudi kuendelea kukusanya taratibu.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Njiani alipoa Kamila, ungemuhurumia. Kimya amejikunyata kitini, kama anayeogopa kuzungumza chochote asije haribu. Colins naye akamuacha tu.

Nyumbani kwa kina Colins.

    Walifika kwao ni kama walikuwa wakisubiriwa wao. “Vipi pressure?” Likawa swali la kwanza kwa mama yake, hata kabla ya salamu. “Naendelea vizuri. Mpishe basi mgeni hapo mlangoni Coly, vipi bwana!?” Maana alikuwa amesimama mlangoni, Kamila nyuma yake kama anayemkinga. “Na msije sahamu maagizo yangu.” “Pisha Coly!” Mama yake akawa kama anachungulia kwa nyuma, mzee yeye ndio hakutaka hata kutoka kwenye kochi.

    Akapisha, wakamuona Kamila amesimama hapo na baadhi ya mizingo yake. “Shikamoo mama Colins.” Akasalimia kwa heshima. Mama Colins akacheka.

 “Nimejua kama wewe ni mama yake. Maana mmefanana sana. Amechukua uzuri wako. Colins ni mzuri kama wewe mama.” Mpaka Colins akageuka vizuri. Mama Colins hana mbavu. “Sasa kwa yale mashariti yako, sijui hapa nafanyaje!” Akawa anamkejeli Colins aliyesema wasimuongeleshe Kamila.

    “Bwana mama! Hapo muitikie.” “Aaaha! Sawa. Marahaba Kamila mwanangu. Mimi ndiye mama yake.” Kamila akawa hajaelewa. Ila akamuongezea swali. “Umekula mama?” “Tulikula kabla hatujatoka kazini kwa Colins. Asante kunikaribisha nyumbani kwako. Pazuri, halafu patulivu.” “Karibu sana. Ujisikie kama upo nyumbani kabisa. Twende nikuonyeshe chumba chako.” Mzee hakutaka hata kuingilia. Matunda yalipelekwa kwa mama tu, kuashiria wao bado wanabifu. Akajituliza kochini kimya.

    Colins akaanza kushusha mizigo yake na kumpelekea chumbani kwake. “Chumba kikubwa halafu kisafi! Asante sana.” Akaendelea kushukuru, Colins na baba yake wakisikiliza.

    “Ila mimi usiku huwa naogopa sana.” Colins akasikia akimwambia mama yake, akiwa anaingiza mizigo. Ikabidi asimame kwanza nje ya mlango akisikiliza.

“Huwa silali gizani. Naogopa. Hata Mike hakuwa akizima taa usiku.” “Basi na hapa pia usiwe ukizima.”

    “Ndugu zake Mike walikuwa wanalalamika wanasema namaliza umeme.” “Hapa hakuna shida ya umeme. Wewe washa taa hata masaa 24. Umesikia Kamila mwanangu?” “Hapo sawa. Asante.” “Na nitakuonyesha chumba cha Colins kilipo, na changu. Usiku ukitaka kitu chochote au ukiingiwa na hofu. Unaweza kunigongea mimi au Colins. Tutakaa wote mpaka upate usingizi. Usikae ukiogopa peke yako.” “Sitakuwa nikiwasumbua sana?” “Hata kidogo. Nataka ujisikie upo nyumbani kabisa. Na kuwa huru na tutaomba pamoja kabla ya kulala. Usiogope.” “Wewe ni mama mzuri! Mpole. Halafu unaonekana una upendo.” Mama Colins akacheka kumtuliza.

    “Una kila kitu au kuna kitu unataka?” “Naona nimenunua kila kitu. Asante.” Ndio Colins akaingia akiwa na mizigo ya mwisho. “Makabati yote hayo yapo wazi. Kesho ukisha pumzika, utapata muda wa kuweka vitu vyako vizuri. Acha niwapishe.” “Hutaniombea tena?” Akamuwahi kabla hajatoka. Akamwangalia mwanae kama anayeomba ruhusa.

       “Labda ukiniombea nitalala vizuri. Sijaomba muda mrefu! Ila mimi na Mike tulikuwa tukienda kanisani.” Alipomuona Colins ameridhia, akarudi. “Basi tuombe ulinzi wa kimungu na amani ipitayo amani yote ikufunike.” Haraka sana akakaa, na kufunga macho akionyesha utayari wa maombi. Colins mwenyewe akashangaa. Ikabidi na yeye akae akipandisha mabega juu kama anayemwambia mama yake na yeye haelewi. Ila mama Colins akafurahia ule utayari wa maombi.

    Colins mwenyewe ndio akawa kama amekumbushwa yupo Mungu. Alibeba hasira, hakuwa akikumbuka maswala ya Mungu kabisa. Akatulia. Mama yake akaomba vizuri tu, mpaka akamaliza.

    “Asante. Nimefurahi.” “Karibu Kamila binti yangu. Uwe na usiku mwema. Ukitaka kitu, Colins atakuzungusha humu ndani ili upafahamu vizuri. Usikwame popote. Ila asubuhi yupo mrembo mwingine humu, ameshalala. Utamuona. Sisi huwa tunawahi kuondoka sababu ya kazi.” “Na mimi nitaondoka na Colins. Naenda naye kazini. Napenda kupika.” “Colins alituambia. Hongera mama.” Akacheka. “Asante. Usiku mwema.” Akatoka mama Colins na kuwaacha hapo hao wawili.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Upo sawa?” Maana alimuona ametulia tu hapo kitandani baada ya mama yake kutoka. “Mama yako anaonekana mpole. Halafu hapa pametulia. Usije nisahau asubuhi.” “Siwezi. Lazima tutaondoka wote. Usiwe na wasiwasi.” “Sawa.” Colins akamuacha akitaka kwenda kuoga.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Akiwa ndio amepitiwa na usingizi ujumbe ukaingia kwenye simu yake na kumfanya aamke. Kusoma, unatoka kwa Kamila. ‘Unisamehe nimekuumiza Colins. Lakini haikuwa nia yangu. Nilitaka kuweka furaha kama niliyoiona kwa Mike siku niliyompa ile perfume. Ilikuwa chaguo langu mimi, wala si Mike. Niliipenda sana, ndio nikamnunulia zawadi kama hivyo nilivyofanya kwako. Tena akiwa na yake. Yeye aliipenda sana, akaamua kuendelea kutumia. Furaha niliyoiona kwake, nilitaka kuiona na kwako pia, kwa upendo ulionionyesha.’

    ‘Moyo wangu unaniuma kuona imekua vinginevyo, nimekuumiza. Samahani Colins. Sitaki kukubadilisha au kukuchanganya. Sitaki uchanganyikiwe. Nakutegemea wewe Colins. Ukichanganyikiwa tu, ujue na mimi nitachanganyikiwa. Sitaki uwe mtu mwingine ila wewe. Maana ungekuwa mwingine, usingeweza nisaidia. Wewe kama Colins ndio msaada wangu na sivinginevyo. Nisamehe.’ Colins akazidi kuhukumiwa.

    Akaona amjibu. ‘Naomba nije kukuona, kama si usumbufu.’ ‘Bado nipo macho. Hunisumbui.’ Akamjibu kwa haraka. Colins akaamka na kutoka kitandani kumfuata.

    Akamkuta amejilaza kinyonge.  Akatoa chandarua, akakaa akimwangalia vile alivyojilaza pale. Ungependa kumwangalia.

    “Nilikwambia yamekwisha Kamila!” “Lakini nimekuumiza Colins! Nimeingia kwenye kundi la watu walio kuumiza. Sikudharau. Sikuoni na mapungufu yeyote. Nilitaka ufurahi.” “Sasahivi nimeelewa. Ila acha nikwambie ukweli.”

    “Umenikuta wakati mbaya sana. Tena sasahivi nina nafuu. Moyo wangu umejeruhiwa vibaya sana. Natembea na madonda ambayo yanatonesheka kirahisi sana. Nasikitika na wewe umepita kipindi hiki. Lakini Colins wa zamani, hakuwa mkali kama uliyemuona hotelini leo. Nimekumalizia tu hasira, lakini kwa jinsi unavyonieleza sasahivi, nia yako ni nzuri kabisa, hukuwa na kosa. Umenielewa?”

Akatingisha kichwa kukubali. 

    “Umeniamini?” “Najua mimi sio Jelini, na hutaniona kama yeye. Lakini na mimi nakuheshimu Colins.” “Sasahivi nimeelewa Kamila.” “Kwa hiyo unaniweka kundi gani? La wale waliokuumiza?” Akajua anataka kuwa kundi moja na Jelini. Akasita. Akatulia kwa muda akitafakari. Akamwangalia akakuta anasubiria jibu ambalo hakuwa tayari kumpa.

    “Tafadhali, nipe muda Kamila. Ila jua nimekuelewa na nahitaji kukuelewa zaidi.” “Ila ujue mimi sitakudharau wala sitataka ubadilike. Kwanza upo vizuri Colins. Hakuna chakukubadilisha.” “Nashukuru. Naomba ulale.” “Hujanichukia?” “Hapana. Imenifanya nikufahamu zaidi. Wewe ni mnyenyekevu sana. Ngumu kukuchukia. Na kwa kuwa nimekuelewa, naahidi ile hali ya pale hotelini haitarudia tena. Naomba ulale. Na nitakusubiria.” Akafurahi huyo!

    Akajisogeza karibu kabisa akicheka nakumfanya Colins naye acheke akimwangalia anavyojipanga vizuri. “Nilitaka kukwambia usogee ili nirudishie chandarua ulale vizuri!” “Hapa hamna mbu. Usirudishe. Hivi nikiwa karibu ndio  nitalala kwa haraka.” Colins akacheka akimtizama. Vile alivyomzuri, halafu na unyenyekevu, akamfanya Colins azidi kuvutiwa naye.

    Akatoa kabisa chandarua Colins akimtizama kisha akajilaza karibu yake kabisa akivuta mto. “Nikuwekee kitu chochote kwenye tv au nyimbo?” Akakubali. Akaunganisha hapo, nyimbo zilizokuwa zikumliwaza Jelini, zikaanza kusikika hapo. Akaona ajinyoshe kidogo wakati akimsubiria alale. Akasikia kutulia hapo pembeni ya Kamila, akapitiwa na usingizi kabisa asijue alipo.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Alikuja kuamka saa 11:30 alfajiri. Akamuona Kamila amelala vizuri, hana habari. Akanyata kutoka hapo na kukutana na mama yake koridoni. Alishituka akabaki kama amepigwa ganzi. Mama yake akacheka tu na kuelekea jikoni. Akamfuata. “Haipo kama unavyodhania mama.” “Kwani mimi nimesema nini?”

“Alishindwa kulala, ndio nikaenda, nikapitiwa na usingizi. Siwezi kujichanganya. Kwanza bado anamuombolezea mpenzi wake. Namsaidia tu. Ame…” “Basi utachelewa kazini.” “Unaweza sema..” “We Colins! Tulia bwana. Sasa huko ulipoenda kumbembeleza na wewe umelala salama?” Colins akacheka akitingisha kichwa.

    “Nini sasa? Maana hamna salamu!” “Mimi sijakwenda kumbembeleza mama! Ila..” “Ulipitiwa na usingizi. Sasa umeamkaje?” “Basi bwana. Hata nikikwambia hutanisadiki. Bora niache tu.” Mama yake hana mbavu.

    Akatoka na kurudi. “Hujanifumania mama.” “Yote hayo unayasema mwenyewe. Mimi nimeuliza jinsi ulivyoamka, basi.” “Niambie pressure yako kwanza.” Akajua ameingiwa hofu. “Naendelea vizuri.” “Na hakuna kufa.” “Wewe na baba yako ndio mtulie.” Akamuona amesimama pale mlangoni kama anayefikiria.

    “Usirudi nyuma Coly. Nyuma ni pabaya, siku yako nzima itaharibika. Natamani ningekuwa na jinsi ya kurekebisha, lakini sina. Naomba tuendelee.” “Jelini anaolewa mama. Mmenikatilia vibaya sana. Na mimi nilipata mwanamke anayenipenda kwa dhati, lakini mmemtoa kwenye maisha yangu. Hilo linaniuma. Sina jinsi ya kufanya. Nafikiria eti mwanaume mwingine ndio anamuoa Jelini! Mimi ndio nimemkosa!” Akaongea kwa uchungu na kuondoka. Mama yake akabaki kimya akimuandalia mumewe kifungua kinywa akishindwa cha kujibu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Mix feelings.

Hisia zimeshaanza kuchanganyikana. Kamila kama msaada na hisia za namna yake, halafu Jelini mapenzi yaliyosubiriwa kwa hamu, nakushindwa kutokea.

Akidhania anamsaidia Kamila, Colins anajikuta taratibu anajisaidia yeye mwenyewe. Moyo umeanza kufunguka hata kuweza kumfikiria mama yake. Kuna mambo yanamlazimu kuyafanya, kuweka  mazingira rafiki kwa Kamila, nyumbani kwao. Ameweza hata kuanza kujirudi kwa mama yake.

INAENDELEA


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment