Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 18. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 18.

 

Mama ni mama. Kwenye majira ya saa 4:30 asubuhi, katikati ya kazi, akamwangalia mama yake alipo. Walikuwa na app ya 360. Waliitumia tokea zamani sana wapo nchi za ugaibuni. Wao wanne, kama familia, wakiangalia wanajua kila mmoja alipo. Zaidi kiusalama si kuchunguzana kwa ubaya.

Connie yeye zaidi alitumia app hiyo kumfuatilia baba yake hapo kwenye hospitali kuu ya Muhimbili. Akimchungulia alipo, akajua, na yeye ananafasi, basi anamfuata hata kwa kumshitukiza tu. Atakaa naye akimwangalia anavyotibu au kupata mlo wa pamoja ofisini kwake, kisha kumuacha aendelee na kazi.

Wazazi wao walikuwa watumiaji sana, wakati watoto hao walipokuwa shuleni nchini Marekani. Kutaka kujua walipo na wanachokifanya. Zaidi kipindi cha ukuaji wao. Walipoona watoto wenyewe wametulia, hawapo kwenye makundi mabovu, wanapotakiwa kuwepo ndipo walipo, basi kikaanza kukosa kazi kubwa sana kwao. Ila bado kilitunzwa kwenye simu ya kila mmoja wao kwa miaka mingi tu.

Colins alikuwa amekisusa. Amezira familia baada ya kumtelekeza kwa Love. Lakini siku hiyo akaangalia. Akamuona mama yake yupo kazini.

Kwa mara nyingine tena baada ya muda mrefu wa uchungu na hasira, akamtuma mtu akanunue kikapu kizuri sana, kilichojazwa matunda yaliyotengenezwa vizuri kwa ustadi. Na kupendezesha hicho kikapu. Fruit basket. Akamtuma ampelekee mama yake, bila ujumbe.

~~~~~~~~~~~~~~~

Mama Colins alishakuwa amenyongea kazini kwake. Kwa asili ni mpole sana. Lakini matatizo ya nyumbani yakamfanya mnyonge asimwambie mtu. Ila mama Simba anayejulikana kama mtu wake wa karibu sana kwa miaka mingi, aliyempita wadhifa, akaanza kutoa siri zao kwa kumsanifu yeye kama yeye na kijana wake huyo Colins.

Maneno yakawa yanaenea kutoka kwa mama Simba vile anavyojazwa na mwanae Love juu ya Colins, manesi wenzie wakajua kinachoendelea kwenye familia yake kwa kutoka upande mmoja tu, mama Simba. Yeye aliposikia hakuwahi kukanusha wala kumsema vibaya mama Simba. Kimya tu ila pressure ikimsumbua.

Nyumbani wanakoishi na Colins ni moto. Na kazini nako kukawa si rafiki tena. Maneno yasiyoisha. Nguvu yake ikabaki mumewe ambaye alikuwa na jina zuri, mwanaume wa nguvu, lakini hakuwahi mvua nguo mwanamke yeyote hapo hospitali nzima ya Muhimbili, isipokuwa mkewe tu. Si wanafunzi wa mafunzo ya udaktari anakosoma mwanae Connie, wala si warembo wanaosomea unesi. Mzee akawa muaminifu kwa miaka yote, akimuheshimu mkewe, akijikaza na tamaa.

Sasa ndio baba Colins akawa faraja kwa mkewe akijua yeye ndiye anampitisha hapo. Basi mara chache atapita hapo kumwangalia mkewe akiwa kazini. Atakaa naye kidogo akimfuata nyuma, mwenzie akitumika hapo wodini, akifanya hiki na kile kisha kuondoka, ilimradi tu kumfanya asiwe peke yake na kuhakikisha hiyo pressure anaiangalia kwa karibu. Connie na yeye ikitokea anakijinafasi atapita hapo na kitu kidogo hata chupa ya maji, atamsalimia mama yake na kwenda kufanya kituo kwa dad wake. Colins hakuonekana tena hapo.

~~~~~~~~~~~~~~~

Sasa siku hiyo, majira ya saa sita ndio akaitiwa mgeni aliyekuwa na hicho kikapu kinachopiga kelele ‘zawadi’ maalumu. Akaambiwa kinatoka kwa Colins. Akakipokea na kuanza kutafuta ujumbe kwa haraka kujua amemwambia nini, akakosa.

Mwishoe akaenda kukiweka ofisini kwao, akaenda chooni kulia. Alilia mama Colins, asiamini. Maana ni kama mwanae alimtangazia msamaha usio ramsi. Ila alifurahi sana nafsini kwake na kujua maneno ya asubuhi yake yalimuingia na kumuogopesha kuwa mama yake atakufa. Angalau uso ukapata nuru.

Kamila kwa Colins.

    Kwenye mida ya saa kumi akapata ujumbe kutoka kwa Kamila. ‘Nimekuja na chakula, tule wote kama asubuhi. Ila kama upo na kazi nyingi, nitasubiri.’ Hapohapo akampigia. “Uko wapi!?” “Hapa chini.” Akawa kama hajaelewa. “Unamaanisha hapa hospitalini?!” “Ndiyo.” “Sasa kwa nini hujaja huku juu ofisini?!”   “Nimeogopa Colins. Sitaki kuwaudhi zaidi hao wafanyakazi wako.” “Njoo, usiogope, nimeshazungumza nao. Au una mizigo mizito?” “Hapana. Ni chakula tu. Vitu nishashusha hotelini. Nilikodi gari. Nakuja.” Baada ya muda, akatokea mlangoni, Kamila wa mtandaoni!

~~~~~~~~~~~~~~~

    Alimzubaisha Colins, mpaka Kamila akamuona. Alipigwa na butwaa la wazi kabisa. “Nilienda saluni waliyokuwa wakinitengeneza zamani.” “Umebadilika! Kama sio wewe!” Akacheka. “Wananijulia kichwa changu. Halafu sinaga nywele nyingi. Lakini wao huwa wananijulia sana, ndio maana nawapenda.” “Na nguo pia zimekukaa vizuri sana. Umependeza. Karibu.” Akaweka kila kitu mezani.

“Umenifanya nifikirie na kuchukua hatua. Mike alikuwa akipenda sana nipendeze. Mwenyewe alikuwa anasema mimi ni fahari yake. Akiniona nimependeza basi anafurahia huyo! Sasa nikajiuliza kama ulivyosema, akija kurudi tena gafla, angenikuta vile, ningemuumiza sana. Nimejinunulia tena vitu vya muhimu vyote na nguo nzuri tupu.” Colins akacheka.  

    “Sasa si utaishiwa?” “Mike ameniachia pesa nyingi sana, kama aliyekuwa akijua! Na mimi pale kwa ndugu zake nilijifanya mjinga kabisa, kama sina kitu ili wasije nishitukia. Nilikuwa nikienda kuoga na kadi yangu, nalala nayo kifuani. Siiachi popote. Wakawa wanasema nahangaika kumtafuta Mike kwa kuwa nimeishiwa, nataka arudi anipe maisha ya hali ya juu, kumbe mimi mwenzao nina hela.”

    “Sasa si leo watakuwa wamekushangaa!” “Nimeogopa kurudi kwao. Nikasema wasije nifanyia jambo baya, nikashindwa kujitetea. Wale ndugu zake Mike wakorofi sana. Ila sijapuuza ushauri wako. Nimempigia simu Luca, nimemuaga.” “Akasemaje?” “Hajasema kitu. Amenikatia simu bila hata ya kuniaga.”

    “Pole sana.” “Nitakua sawa. Si ndivyo ulivyoniambia?” “Kabisa. Hata sasahivi unamatumaini makubwa. Tukae tule nikupe habari njema.” Wakakaa kwenye makochi ya pembeni na meza yake.

    “Nashukuru kunifikiria chakula.” “Mwenzio najikomba Colins. Nataka usinisahau. Naogopa.” Colins akaanza, kucheka.

“Usicheke. Ujue sasahivi wewe ndio mtu wangu wa karibu! Au ni tabia mbaya?” “Hata kidogo. Lakini asante kwa chakula. Mimi huwa ni mlaji ila tu muda.” “Nimekuona. Huzembei kwenye kula. Ila sasa mbona huna mwili mkubwa?” “Niliugua kwa muda mrefu sana. Nipo kwenye kurudisha mwili.”

    “Pole. Ila na wewe uniahidi kitu Colins.” “Nini?” “Usiugue. Nahisi safari hii nitachanganyikiwa kabisa. Usiugue hata kidogo. Sawa?” “Na wewe uniombee. Nina uhakika hata Mike hakupenda kukuacha, Kamila. Tuombeane uzima.” Akanyamaza.

    “Tule, na urudishe mawazo hapa. Kuna kitu nataka kukwambia.” “Ni nini?” “Nimekupatia familia ya kwenda kuishi nao.” “Watanikubali!?” “Nimeshazungumza nao. Hawana shida.” Akamuona amekosa raha.

    “Nina uhakika utapafurahia Kamila.” “Kwa nini wewe hunichukui Colins? Au umeoa? Naona kama itakuwa rahisi! Ushanielewa. Hunidharau!” Hapo akawa ameshapaniki, yule Kamila anayeonekana kama amechanganyikiwa, akarudi bayana usoni mwake. Hofu tayari.

    Wewe hunioni kichaa. Unanisikiliza ndio maana nimeweza hata kwenda saluni leo. Kwengine naogopa. Nitakuwa kama naanza upya! Naomba twende wote. Au sio vizuri? Mimi najiheshimu Colins. Sitakuvunjia hesh…” “Tulia kwanza Kamila. Acha kulia. Nyamaza.”

    “Sitakupeleka sehemu ambayo kwanza mimi mwenyewe sijajiridhisha nao. Ni kwa wazazi wangu. Na mimi nitakuwepo hapohapo. Kwa hiyo tutakuwa wote.” Hilo akalifurahia, hata machozi yakakauka.

    “Kama hivyo ni sawa. Mwenzio mimi muoga. Sio watu wote wazuri!  Naogopa.” “Tutakuwa wote. Usiogope.” “Halafu ukiwa unakuja kazini, tunakuja wote. Si sawa?” “Kabisa.” Hapo akatulia na kuendelea kula.

Colins alikuwa akimwangalia kwa kutulia, hachoki. Kwa hakika alipendeza. Uzuri alikuwa akila huku akiwaza yake, hata hakuwa na habari kama anaangaliwa, kwa hiyo wakapata muda mtulivu hapo ofisini wakila.

~~~~~~~~~~~~~~~

    “Nimefurahia chakula. Asante.” “Nafurahia unavyokula Colins! Mpaka unatia raha kukuletea chakula. Ila nina swali. Si umesema naweza kukuuliza chochote au nitakuudhi?” “Niulize tu.”

    “Kwa nini unaishi kwa wazazi mpaka sasa? Au ni kwa ajili yangu?” Akafikiria jinsi ya kumjibu, akaona aifupishe. “Niliugua sana. Ikabidi kuishi nao wakiniuguza. Kipindi hicho ndio baba akaikodisha nyumba yangu. Nimepona na kutaka kurudi kwangu, ndio nikagundua waliikodisha, na mbaya zaidi mpangaji ana mtoto mchanga. Ila amechapewa siku za kuhama, anipishe kwangu.” Akamuona ametulia.

    “Umeelewa?” “Ndiyo. Ila nina swali jingine. Ni lini unahamia kwako?” “Ni sawa tukitembea siku moja moja?”  Akatulia. “Itakusaidia kuishi leo, bila hofu ya kesho.” “Nataka kujipanga. Kama utaondoka, ni bora nifikirie kununua nyumba yangu.” Colins akawa amehisi hajaelewa.

    Ununue au upange?” “Naona bora ni nunue tu ili nitulie sehemu moja, niache kumangamanga.” “Kwamba unahela ya kununua nyumba!?” “Nina hela Colins. Mike alikuwa akinitunzia kama aliyeziona hizi siku. Hapa nina pesa kasoro tu Mike, ndio maana unaona akili haijatulia.” Akatulia, akamuona anafikiria.

    “Mike alikuwa na pesa ndio maana watu walifikiri ndio sababu nampenda. Lakini Colins, Mike alikuwa mtu mzuri sana. Sikuwa na sababu ya kuhangaika. Alinifanya nikatulia, nikajiona nina kila kitu. Ameniachia mahela mengi, lakini najiona sina kitu! Nikikwambia nilienda kumtafuta kijijini kwao, nilikuwa nikimsaka mpaka usiku mashambani na kwenye majumba ya watu.” “Kwa nini usiku?”

    “Akili yangu ilikuwa ikiniambia mchana wanaweza kumfungia vizuri, lakini usiku wanaweza kuzembea.” “Kwa hiyo wewe hukuwa umechanganyikiwa basi! Ulikuwa ukifanya yote ukifikiria kwa makini sana!” “Sana Colins. Watu walikuwa wakidhani nimechanganyikiwa kwa sababu nitakosa maisha aliyonipa Mike, kumbe mimi namtaka Mike mwenyewe. Hata leo wakinirudishia Mike wangu bila pesa, nitamchukua bila kufikiria mara mbili. Ni bora Mike bila pesa, kuliko pesa bila Mike. Havina maana kabisa.”

    “Usingenikuta naogopa hivi! Mike alikuwa ananipa uhakika wa kila kitu. Nilikuwa tajiri wa nafsi, furaha wakati wote. Sijui kama nitarudia ile hali Colins.” “Usikate tamaa.” “Sina jinsi.” Akamsikia akiguna mawazoni.

    Kisha akaendelea. “Mike alijaa kwenye maisha yangu, sikuwahi kuhitaji mtu mwingine. Naweza nikawa nipo nyumbani, yeye kazini busy, lakini ananipigia na kuacha bluetooth sikioni. Anaendelea na kazi, na mimi nipo nyumbani. Ilimradi tu awe na mimi na nisijisikie mpweke!”

    “Na akipanda tu kwenye gari, simu. Tunaongea mpaka anaingia ndani. Hatukuwahi kumaliza mazungumzo. Tunalala tukicheka. Stori za tangia shule zilikuwa haziishi!” Akamuona anafikiria kidogo kisha akaongeza tena.

    “Mmmhh! Kama kweli Mike hayupo hapa duniani, basi Mungu afanye haraka anichukue na mimi, anipeleke alipo.” “Acha kusema hivyo bwana Kamila!” “Nimejawa hofu Colins, siwezi kujisaidia. Kila nikiwaza naishi dunia hii bila Mike, moyo unalipuka kama kumepigwa bomu! Hakika sijui maisha mengine bila Mike.” “Leo umeishi Kamila. Umetoka, umejifanyia usafi na ukapendeza. Umeniletea chakula. Umekaa na mimi hapa. Kesho utapikia wagonjwa wenye uhitaji, chakula kizuri. Huoni kama maisha yako yanabariki wengine?” Akatulia.

    “Pengine uniambie hofu yako ilipo, tuzungumze.” “Naogopa kubaki peke yangu, ndio maana unaniona nakuganda.” “Na mimi sitakuacha peke yako. Ni ahadi nakupa.” “Kweli Colins!?” “Kabisa. Siwezi kukufanyia hivyo.” “Lakini umesema mwisho wa mwezi unaondoka kwenu!” Hapo ndipo akaelewa hofu yake na mengi hapo kumbe yaliletwa na hilo! Alikuwa ametulia mpaka alipojua atahama.

    “Kwanza ujue nyumba yangu imepakana na kwa wazazi. Nitakuonyesha. Sio mbali.” “Lakini sio sawa na kuwa nyumba moja!” “Milango ya kwangu, kwako iko wazi. Muda na wakati wowote ule, unakaribishwa. Wakati nikihama, tutazungumza na tutajipanga kwa kadiri tunavyoendelea, na kuamua pamoja. Ninachokuomba tu, uwe muwazi kwangu.” Akajiweka sawa.

    “Mimi si Mike. Naweza nisifanye kama yeye, kwa kuwa yeye amepata muda mrefu sana wa kukufahamu, ndio maana kama ulivyosema, kabla hujalia shida, alikuwa akikutimizia. Hiyo inaletwa na kufahamiana kwa muda mrefu.”

    Sitegemei uwe Mike, Colins!” “Kama ni hivyo nashukuru. Sasa ukilikumbuka hilo, ongeza na kuwa unaanza. Ila unaanzia pazuri, na mimi ambaye sikufahamu, ila nipo tayari kutembea na wewe kwenye hatua unazotaka kuchukua. Ila uwe unazungumza na mimi. Kuwa muwazi kabisa kwangu. Kama ni kitu cha kukushauri nitashauri ila kama ni kitu cha kukuunga tu mkono, jua upo na mimi. Na sitakuacha.” Akamuona anatulia. Akamuacha afikirie anachokifikiria.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Wakiwa njiani wanarudi hotelini, akamuona ametulia garini. Ila sio tulia mbaya, kama aliyepumzika kwa sehemu. “Colins!” Akamuita taratibu. Akamwangalia. “Asante, umenipa tumaini. Pale ofisini niliogopa! Nilijua ungeniacha tena kwenu, nianze tena upya. Nahisi mimi nina tatizo. Mgumu kuzoea watu. Inanichukua muda. Halafu sasahivi watu hawanielewi.” “Ikitokea wakati mwingine umeingiwa hofu, na kitu chochote, unaahidi kuniambia?” Akacheka na kutingisha kichwa kukubali. Alivutia, mpaka moyo wa Colins ukafurahi.

    “Ila sasa usinichoke, na kusema wewe sio Mike nisikutupie matatizo yangu.” “Siwezi kusema hivyo kwa kuwa najua mimi si Mike, na wala sitakaa kuwa Mike. Ila nimekubali kutembea na wewe kwenye huo mlango mpya uliokubali kuufungua na kutembea huko.” “Nashukuru. Na ukiona nakosea usiache kuniambia.” “Kama umeniruhusu, hamna shida.” “Nakuruhusu.” Wakacheka taratibu Colins akiendelea kukanyaga mafuta kuelekea hotelini.

Madonda Mabichi Yaliyofunikwa na Ngozi Kavu.

Walipofika hotelini, akakuta Kamila amefanya shopping ya nguvu. Mifuko iliyojaa hapo, yeye mwenyewe ikabidi atafute mahali akae. Kwa kuangalia tu aina ile ya mifuko alionyesha ametoka kufanya manunuzi yake kwenye maduka makubwa ya maana. Akajua kweli huyo Mike alikuwa na pesa na amemuacha pazuri. Na bado kufikiria kununua na nyumba!

    “Nahisi sasahivi angalau nina vitu vya kuanzia.” Akawa akizungumza huku akishika ile mifuko yake na kuangalia ndani kama anayetafuta kitu. Mwishoe akatoa mifuko miwili. “Hii ni yako. Nilikununulia na wewe zawadi.” Colins akashituka kidogo.

    “Usingefanya hivyo! Wewe ndio unauhitaji!” “Sio vitu vingi. Vitu kidogo tu. Zaidi ni perfume aliyokuwa akitumia Mike na soksi.” Hapo ndipo akamtibua Colins.

    “Kwamba unataka mimi ninukie kama Mike?!” Swali la kwanza ilionyesha kama hana uhakika sana na anachokifanya mrembo Kamila. “Ni nzuri sana, najua utapenda. Ilikuwa ikikaa kwenye nguo zake, mpaka mwili wake ulikuwa una hiyo harufu.” “Kuna tatizo gani na harufu yangu!?” Hilo swali la pili aliliuliza kwa umakini sana mpaka Kamila aliyekuwa akicheka kwa hisia ikabidi atulie na kumwangalia.

    “Eti Kamila?!” Hapo akauliza kwa ukali kidogo, asijue amekanyaga kwenye donda bichi. “Ni perfume nzuri!” Akajibu kwa upole. “Kwa hiyo umeona yangu haifai, unataka kunigeuza niwe Mike?” Kabla hajajibu, akaongeza.

“Umetoka kuniambia nini? Si kwamba hutegemei niwe Mike?!” Hapo ameshabadilika na rangi kabisa. “Ndiyo.” Kamila akajibu akionekana ameshaogopa haswa.

    “Nisikilize Kamila. Watu wengi sana wanataka kunibadilisha niwe vile wanavyotaka wao. Kila mmoja kwa matakwa yake. Mwanamke niliyekuwa naye kwa muda mrefu sana, alikuwa kama hichi unachonifanyia wewe. Sijui kama unanisikiliza?” Akatingisha kichwa haraka sana kukubali.

    “Aliniendasha mpaka nikachanganyikiwa kabisa, kwa kurukwa na akili. Kila leo alinibadilisha kwa hiki na kile na sikuwahi kumtosheleza. Nilifanya kwa juhudi zangu zote, ili tu kumfurahisha. Kwa miaka yote niliyokuwa naye, sikuwahi kufikia lengo hata siku moja, kwa sababu kila siku alikuja na kitu kipya alicholalamikia na kunilazimishia mimi niwe.”

    “Na mimi nikawa mtumwa wake. Nikahangaika mpaka mwishoe akaona anigeuze tahira kabisa ili niweze kuwa mtumwa wake. Akaendelea kunibadilisha na kuniwekea matakwa yake, nikaishia kuwa kichaa kabisa yule anayetembea bila viatu barabarani. Ndipo aliponiacha na kunikimbia.”

    “Wazazi wangu wenyewe wanataka niishi ndoto zao. Na wmewe tumekutana juzi tu, umeshaona kuna kitu chakunibadilisha. Unaona hivi nilivyo haitoshi, mpaka niwe Mike.”

    “Ni mtu mmoja tu. Msichana mmoja tu. Niliyekwisha kukutana naye hapa duniani. Alinipenda hivi nilivyo na hakuwahi kutaka kunibadilisha.” Akaendelea kama ambaye amepata jukwaa na kipaza sauti.

    “Jelini alinipenda yule msichana, hivi nilivyo. Hakuacha kuvutiwa na mimi na hakuwahi kufikiria kunibadilisha ndio maana moyo wangu umelia sana juu yake. Na kwa mara nyingine tena, umenirudisha kwenye yale maumivu.”

    “Hata hunifahamu! Hujachukua muda hata kujua nini napenda! Kwa nini nipo hivi! Tayari unataka nibadilike!” Kamila alikuwa akitetemeka asitegemee ile zawadi ingegeuka kuwa tatizo kwa kiasi hicho, asijue amekanyaga jipu lenye usaha.“Naomba katika hili usiwahi kusahau Kamila. Unanisikiliza?” Akatingisha kichwa kwa haraka sana, akitetemeka. “Mimi si Mike. Sitakaa kuwa Mike. Na kamwe maishani mwangu, SITAKI kuwa Mike.”

    “Sio sawa kwangu. Mike alibahatika kuishi maisha yake mpaka amekuachia wewe kumbukumbu. Na anacho kitu cha kurudisha mbele za Mungu. Ana hesabu ya maisha yake aliyoyaishi hapa duniani.”

    “Kweli unataka eti na mimi leo, niendelee kuwa Mike?” Kimya. “Halafu ili nani ayaishi maisha yangu? Mke wangu na watoto wangu waishie kuwa na Mike kwenye maisha yao na si mimi? Ili iweje? Kwa faida ya nani?” Kimya akiendelea kutetemeka amejikunyata akiwa amesimama.

    “Na kwa taarifa yako tu, hata nikitumia hiyo perfume leo na kuvaa soksi zake, utaona haitoshi. Utataka nianze kuvaa kama yeye. Utakuja kutaka niwe na zungumza, kula, kuishi kama yeye. Mwisho wake ni nini kama si kunirudisha barabarani nikiwa nimechanganyikiwa kabisa?”

    “Maana mimi sijawahi muona Mike akiishi maisha yake! Sijui anavyofikiria au kutenda, halafu wewe unategemea niwe yeye! Mwisho wake ni nini kama si na wewe kunigeuza mtumwa wako ukinizungusha kwa hiki na kile bila kutoshea?” Kamila kimya akiendelea kutetemeka na mifuko yake mkononi, Colins anawaka kwelikweli.

    “Sasa, mimi ni Colins. Hii harufu unayoisikia kwangu ni yangu. Narudia tena. Mimi si Mike. Sitakaa kuwa Mike. Sitakaa nikajaza pengo lake. Na sitaki kuwa yeye, wala kujaza pengo lake, au hata sitathubutu kuvaa viatu vyake. Alikopita amepita yeye, na kwa jinsi unavyomuimba, inamaana ameitendea haki nafasi yake. Siwezi na sitaki kuendelea kuyaishi maisha yake.”

    “Chochote unachokiona kwangu, jua kinaniwakilisha mimi kama Colins. Hulazimiki kukipenda, na sitegemei upende kitu chochote kutoka kwangu. Iwe kwenye kumbukumbu yako au vinginevyo, usithubutu kunibadilisha Kamila. Huo ni mstari nimechora. Sitaruhusu yeyote auvuke. Wazazi wangu ndio wa mwisho, lakini sasahivi, BASI. Atakayeweza kuwa na mimi kwa hivi nilivyo, sawa, ambaye hawezi. Basi. Unanielewa?” “Ndiyo.” Mpaka mdomo ilikuwa ikicheza.

    “Swali la mwisho ukiwa umeelewa msimamo wangu. Bado unataka kuongozana na mimi nyumbani, au unahitaji muda zaidi wa kufikiria?” Kabla hajajibu akaongeza. “Hiki chumba kimeshalipiwa. Namba yangu ya simu unayo. Ukijifikiria na kuona unanihitaji kwa msaada wowote ule, bado ahadi ipo palepale. Muda na wakati wowote, nipigie. Nikiona kimya, nitaelewa umeamua kuendelea bila mimi. Uamuzi ni upi?” Akamuona anavuta mifuko yake mpaka kifuani juu. Akaikumbatia akitetemeka kwa hofu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ingekuwa wewe Kamila Angechagua kipi!?

INAENDELEA.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment