Bado Colins akajisikia
mzigo na Kamila akishindwa kujisaidia. Akaacha majukumu mazito yanayomkabili
hapo kazini, japo usiku ulishakuwa umeendelea, lakini bado alikuwa na
yakufanya, akaacha kila kitu akaanza kazi ya kumtafutia sehemu ya kulala wageni.
Akapata sehemu ambayo ni njiani kwenda nyumbani kwao. Akaona
patamfaa, yeye na Kamila mwenyewe. Akalipia chumba, akamsindikiza chumbani
akiwa amepoa.
“Utakuwa sawa
hapa?” “Nashukuru. Asante.” “Nataka kujua kama utakuwa sawa.” “Naogopa. Lakini
panaonekana pako salama.” “Nikikwambia usiogope, itasaidia?” Akatingisha kichwa
kukubali.
“Usiogope. Lala ukiwa umewasha taa. Usifungue mlango kwa
sababu yeyote ile mpaka papambazuke, na pia kwa yeyote atakayegonga, muulize kwanza kabla hujamfungulia.”
Akakubali. “Kingine, nashauri kesho
ujiweke sawa kabla hujarudi kazini.” “Unamaanisha nini?” “Si bado unaishi na
ndugu zake Mike?” “Ndiyo.”
“Basi nashauri ukaage. Isiwe umeondoka kimyakimya. Na
uchukue mizigo yako pia, ili uanzie pazuri.” “Walichukua vitu vyangu karibu
vyote. Vilivyobakia nikafungia kwenye gari. Luca aliponipokonya gari,
nikamuomba nichukue vitu vyangu lakini akakataa. Akasema kila kitu ni mali yao.”
“Kwa hiyo huna kitu ulichobakiza kule?” “Hamna. Ila nina hela
benki. Naficha kadi yake. Mike alinifungulia kwa jina langu akaniambia nisiwahi
tumia mpaka iwe dharula kweli, akiwa
yeye hayupo. Maana kadi nyingine za benki zilizokuwa na jina langu na Mike, walininyang’anya. Wakaenda mahakamani
kudai pesa. Wakapewa wakagawana, mimi wakaninyima. Ila sikuwaambia kama
nina akaunti ingine. Nilinyamaza tu.” Colins akabaki kimya.
“Ninachotaka kukwambia, hata kama wamechukua, nitanunua
vingine. Halafu naweza kutafuta pakuishi, ila sema naogopa. Sijawahi ishi peke yangu hata mara moja!” “Basi usiwe na
wasiwasi. Zipo sehemu nyingi tu ambazo utakuwa salama.” “Kweli?” “Kabisa.
Usiogope. Tutatafuta taratibu. Na ukitaka kitu chochote. Ukiwa na swali. Muda na wakati wowote, chukua namba yangu, tuwasiliane.” Akatoa simu yake.
Colins akampa namba yake ya zamani.
“Ni sawa nikikupigia ili utunze namba yangu?” Akamuuliza
kwa hofu kidogo. “Ili ikitokea nakutafuta, ujue ni mimi. Na pia sitakusumbua
mpaka iwe lazima sana.” Asijue Colins alishakuwa na namba yake tokea
hawajakutana!
“Wazo zuri. Na naomba usiogope Kamila. Mwanzo ni mgumu kwa yeyote yule. Na kuuliza si ujinga. Halafu ni kweli nipo busy,
lakini si kiasi chakushindwa
kukusikiliza. Umenielewa?” “Nimeelewa, sema kesho niliwaahidi nitapika.”
“Wanahitaji msaada hata kesho kutwa na siku zij azo.” Akamfanya atulie.
“Pata muda wa kesho kujiweka wewe mwenyewe vizuri.
Kuanzia usafi wako binafsi. Mavazi na vitu vingine. Nina uhakika ukiwa sawa
wewe mwenyewe, kwa kuanza hatua ya kwanza, utashangaa jinsi itakavyokuwia
rahisi kuendelea kuchukua hatua zingine.” “Asante. Eti wewe unaitwa Colins?”
Colins akatoa tabasamu.
“Ndiyo. Naitwa Colins.” “Mimi naitwa Kamila. Nitatunza
jina lako.” “Ulikula?” “Sina njaa. Bado nipo kama nime…” Akasita. “Moyo wangu
umekataa kuamini kama sitamuona tena Mike! Nashindwa kuweka kitu chochote mdomoni.”
Akanyongea kabisa.
“Bado siamini kama Mike ameniacha!” “Unafikiri ukienda kuona kaburi lake itasaidia?”
“Sidhani. Nitajuaje kama yeye ndio yupo humo ndani?” Colins akakwama.
“Nahisi kama yupo mahali ananitafuta ila hajui jinsi ya kunifikia! Mike ananipenda sana. Hawezi ishi bila mimi. Hatujawahi
kuwa mbalimbali hata siku moja! Alikuwa hata akipata safari ya dharula vipi,
lazima anifuate twende wote. Alikuwa anasema hawezi kulala, kama sipo naye! Sasa sasahivi nipo najifikiria.
Nakua namuonea pia huruma! Nahisi amekwama mahali, hajui jinsi yakunifikia! Sijui!
Nipo na wakati mgumu!” “Pole sana.” Akamuona ametulia.
Kisha akaongeza. “Nammiss sana. Natamani kama ningeweza kuzungumza na Luca, anihakikishie kama kweli waliyemzika
alikuwa Mike!” “Sasa kwa nini usifanye hivyo?” “Chochote kitakachosikika ni kunisaidia mimi, hawezi kukubali. Anatamani sana kuwa na mimi. Kitendo cha kumkataa,
kinamuuma, ndio anataka kuniumiza na mimi makusudi. Wakati
mwingine ananibembeleza anasema hata nilale naye tu! Kwa hiyo najua nikimuendea
kwa lolote, atataka kwanza mapenzi.”
“Ndugu zake wengine?” “Kwa sasa wanamtegemea yeye
kifedha. Ni kama wote wanaishi kwa rehema zake Luca. Hawakusoma na wala hawana
kazi za kueleweka. Kwa hiyo chochote anachosema Luca, wanamsikiliza. Na hawawezi fanya chochote bila ya kumuuliza
yeye. Ashasema mimi ni mtu mbaya
kwao, nataka kuja kuwageuka baadaye,
nidai haki kama mke wa Mike. Yaani
nichukue mali zote za baba yao, halafu niwadhulumu.
Mimi nikawaambia sina nia hiyo. Ndio akasema basi anioe ili kweli mali zao zibakie kwao. Nikakataa. Ndio akawaambia ndugu zake ni kweli nia yangu ni kuwadhulumu mali za baba yao.”
“Halafu kwa jinsi nilivyosikia, mmoja wao aliropoka tu. Nasikia walipokwenda
mahakamani, waliulizwa kama Mike hakuacha mke na watoto. Wakakataa. Wakasema nilikuwa nikiishi naye tu. Wakaambiwa hata kama
hatukuwa tumefunga ndoa, lakini nimeishi naye kwa muda wote huo, kisheria mimi
ni mkewe, natakiwa mimi ndio niwe mrithi. Nasikia walidanganya kama eti mimi nilishaondoka kwenye maisha ya Mike hata
kabla ya kifo au sijui walidanganya nini, nakusema hata hivyo sikuwa hata
nimezaa naye.”
“Sasa nasikia wanaogopa kunifukuza kwa nguvu, nisije nikawashitaki. Wanajua mimi nina haki
kama mke wa Mike.” “Ambayo ni kweli.” “Kumbe kweli!?” “Kisheria kama mmeishi
nyumba moja kwa zaidi ya miezi 6 nafikiri, mnatambulika kama mke na mume.”
Akatulia akifikiria.
“Lakini, acha tu niondoke. Kwa sababu kwa uhalisia, Mike
aliaminiwa tu na baba yao, kuendeleza mali zake. Sasa kwa kuwa mimi nilikuwa
nikinufaika kupitia kwa Mike, ambaye ni kama alikuwa mfanyakazi tu, haitakuwa
sawa leo kuanza kudai mali za baba
yao.”
“Simtaki Luca,
wala hatakaa akawa mume wangu. Acha nisimuabishe
Mike. Mike alikuwa mtu wa haki. Hata wao wanajua ndio maana pia walikuwa wakimuogopa sana na kumuheshimu japo walikuwa wakimuonea
wivu. Hakuwahi kuchukua kitu kisicho halali yake. Na mara kwa mara alikuwa
akiwaambia kila faida anayotengeneza kwenye mali zao, na kuwapa wenyewe
wagawane. Ila nafikiri wivu ndio ulikuwa ukiwasumbua.”
“Acha tu niondoke kwa amani, ili pia wasije nifuata nyuma
na kunidhuru. Siwaamini. Na naamini
ukweli utakuja jitenga. Kama kweli Mike wangu amekufa kweli, najua nitajua tu.
Na Mungu atanipa nguvu ya kuendelea mpaka nije kukutana naye kwenye huo
ulimwengu ujao.” “Hapo umeongea sahihi. Pata muda upumzike.”
“Nashukuru sana Colins. Si ni sawa nikikuita hivyo au
nitakuwa nikikuvunjia heshima, nikuite bosi kama wengine?” “Huna sababu
yakufanya hivyo. Colins inatosha.” Akacheka. “Kesho nikikamilisha kila kitu,
kesho kutwa nitakuja kazini.” “Sawasawa. Na naweza kukupitia nikiwa natoka
kazini kujua ulipofikia. Ni sawa?” “Nitafurahi.” Wakaagana, Colins akasubiria
nje ya mlango mpaka akafunga milango yote, akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
Alipofika tu kwenye gari akaona anampigia. “Kwema?”
“Samahani. Nimejikuta na funguo mbili za mlango. Kwa kuwa wewe ndio sasahivi
kama mdhamini wangu, na ndio mtu
pekee unajua nilipo. Naomba ukae na funguo moja. Ili hata ikitokea naanguka
ndani, basi kuwe na mtu mwingine wakuweza kuingia ndani.” “Wazo sio baya
kabisa, japo najua hakuna baya litakalo kupata. Usiogope. Narudi kuja
kuchukua.”
Akafurahia hilo wazo, akarudi kuchukua funguo, akamkuta
anamsubiria. Akamkabidhi. “Nakushukuru na samahani nakusumbua.” “Usijali
kabisa. Hivyo unavyo zungumza, ujue ndio itakusaidia. Muda na wakati
wowote, wewe nipigie tu.” Akaonekana kuridhishwa na hilo, ndipo akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
Wakati analala kumalizia hiyo siku ndefu ya jumapili,
ujumbe ukaingia kwenye simu yake mpya. Akajua kuna Kamila anachotaka kumwambia
Mike.
‘Siamini
kama umeondoka Mike wangu. Nina ombi moja kubwa kwako. Nipo na wakati mgumu
sana. Siamini kama umeondoka katika ulimwengu huu ambao mimi nipo. Ila kama
kweli upo popote mpenzi, tafadhali nijulishe kwa njia yeyote ile, nijue bado
upo katika ulimwengu huu. Natamani kujua kwa hakika Mike. Nashindwa kuamini
mpenzi. Kweli walikuzika! Kweli muda mfupi tu ule nilipokuacha pale hospitalini
eti ndio uwe mwisho wa kuonana mimi
na wewe! Bado siamini. Ule hauwezi
ukawa ndio mwisho wetu wa kuonana.’
‘Lakini
hata hivyo, nakwenda kuagana rasmi na ndugu zako. Naogopa wasije niua sababu ya mali. Luca amepandwa na
hasira mbaya sana dhidi yangu tokea nilipomkataa. Acha niwapishe. Ila
sitabadilisha namba ili popote nitakapokuwa, unifikie Mike. Tafadhali
usinyamaze mpenzi. Kama unanisikia, tafadhali nijibu.’
‘Ila nahisi
nimepata mtu mwingine mwenye moyo kama wako Mike. Ni yuleyule, amesema kweli
jina lake ni Colins. Amenisaidia kuhama pale hospitalini. Anaonekana ni mtu
mzuri. Na yeye ananisikiliza kama wewe. Ila yeye namuogopa.’ Akamalizia hapo na kumuacha Colins akitafakari mpaka
kupitiwa na usingizi.
Jumatatu.
Asubuhi na mapema,
akaamkia hapo hotelini. Alitoka kwao alfajiri sana akiwa amesahau kuwa waliagana
na ahadi ya kumtafuta jioni akiwa anatoka kazini ili kujua siku yake iliendaje.
Lakini alimka akili ikimtuma kwenda kumuangalia yeye tu.
Akakanyaga mafuta kama
anayewahi kitu. Haraka mpaka mlangoni. Naye Kamila akafungua mlango kwa haraka
akionekana kama ambaye hakuwa amelala. “Mbona kama hujalala kabisa?!” Akamuona amenyamaza. Akajua tu ni sababu ya
Mike.
“Eti Kamila?” “Mimi siwezi kulala sehemu yote hii peke
yangu. Naogopa, ndio maana Mike alikuwa haniachi peke yangu usiku. Na ndio
maana pia nimeshindwa kuhama pale aliponiacha Mike.”
Akaendelea taratibu tu bado akionekana na majonzi.
“Japokuwa wananisumbua pale, lakini najikuta sipo peke yangu. Nalala hata
kwenye kochi.” Akaanza kutokwa na machozi.
“Na pia
nashindwa kulala kwa kuwa bado inaniwia ngumu kuamini kama Mike hatarudi tena. Naogopa sana. Imekua ni
kama kufumba na kufumbua tu jamani! Yaani siku ile tulikuwa na wakati mzuri tu!
Gafla anaumwa tumbo. Nampeleka hospitalini akiwa anatembea mwenyewe! Eti
namuacha kwa muda mfupi tu, tena kwa kumuaga yeye mwenyewe, ndio iwe basi! Hakika siamini. Moyo wangu
unauma, sijui chakufanya.”
“Bado nahisi
kuna kitu hakipo sawa, lakini sijui ni nini!” Colins akatulia na kubaki akitafakari.
“Najua
unaweza usinielewe kwa kuwa umeshapita muda mrefu, utashangaa kwa nini nilie
mpaka leo, lakini Colins, moyo wangu upo na wakati mgumu! Sijui jinsi ya
kuelewa hili jambo. Nimemtafuta Mike kila nilikohisi wanaweza mficha!
Nimeenda mpaka kijijini kwao kabisa na nikakaa huko siku 10 nikipeleleza kama
wamemuona! Huko nako nimemsaka mpaka kwenye mashamba yao!”
“Nilishakwenda mpaka nyumbani kwa Luca na kwa
ndugu zake hata kabla hawajahamia pale nilipokuwa nikiishi na Mike. Nilikuwa
nikienda kwa kuwashitukiza, namtafuta mpaka chini ya uvungu, wananiona
ni kichaa. Sina ninapopafikiria, sijaenda kumtafuta Mike. Na bado nahisi
pengine ipo sehemu, nimeshindwa kupajua!” Kimya akijaribu kufikiria jinsi ya kumsaidia.
“Najua unachoka na mimi, lakini siwezi
kujisaidia.” “Hapana, Kamila. Mimi naelewa kabisa. Naweza nisijue
maumivu yako kwa kuwa kila mtu anahisia zake, ila hiyo hali ya kutokukubaliana
na ukweli, nilishakaa hapo kwa mateso makali, akili ilikuwa inashindwa
kuelewa. Lakini tofauti yako na yangu, mimi nilikuwa na vithibitisho
vyote kuwa nimepoteza na sitakaa nikampata tena. Kwa hiyo
naweza nikaelewa hali unayopitia. Nilishakuwepo hapo.”
“Na sitakushangaa kwa kulia mpaka sasa au kumtafuta. Hata
kidogo. Unahitaji kumuombolezea Mike na kujiridhisha kwa hakika
juu ya sehemu sahihi alipo. Na linapofika swala la kulia, usijizuie. Na pia ukifikiria
sehemu nyingine unayodhania unaweza kwenda kumtafuta, niambie mimi nitakusindikiza
mpaka uridhike kabisa. Chukua muda wowote ule mpaka utakapo pata nafuu
nafsini kwako na mawazoni. Sita kuhukumu.” “Nashukuru, Colins. Na
asante kunielewa.” “Kabisa.” Akajaribu kutulia.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Sasa kuhusu swala la kulala hapa, unafikiriaje? Au
unataka kurudi kule ulipokuwa ukiishi?” “Hapana. Acha nitajaribu tena na leo.
Ningumu, lakini lazima nianzie
sehemu. Nimekua kwenye nyumba ya watoto yatima. Nikafaulu kwenda bweni, kisha
nikahamia kuishi na Mike, alipoondoka wakahamia ndugu zake. Kwa hiyo ni kama
sijawahi ishi peke yangu.” Colins akabaki akifikiria.
“Nina wazo ambalo nataka nilifikirie kwanza kabla
sijalitekeleza. Kwa sasa tupate kifungua kinywa utoke hapa ukiwa umeshiba, na
mimi niende kazini.” “Kichwa kimevurugika Colins, siwezi kula.” “Naomba
jikaze Kamila. Itakusaidia kufikiria na kuchukua hatua sahihi tena kwa haraka.
Niambie unataka kula nini?” Akambembeleza hapo mpaka akakubali kula. Wakaagiza kifungua
kinywa, wakala pamoja hapohapo chumbani huku wakiangalia taarifa yahabari
asubuhi hiyo.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Nikikusubiria hapa, unaweza kulala kidogo angalau
upunguze usingizi kabla hujatoka?” “Sasa na wewe kazini? Acha tu.” “Usijali.
Lala kidogo. Nikihakikisha umelala kabisa, ndio nitaondoka taratibu. Au
utaogopa?” “Nikishapotelea usingizini sitakuwa na shida. Nashukuru.” Akawa
kweli amebanwa na usingizi. Akapanga kitandani, akihakikisha macho yake
yanamuona Colins. Akageukia kabisa upande aliopo akimtizama kama
anayejihakikishia hayupo peke yake. Hakuchukua muda mrefu akalala Colins akiwa
amepotelea mawazoni.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Miaka miwili bado Kamila anamsubiria na kumtafuta mpenzi
wake!?” Wivu ukaanza kumsumbua Colins. “Ningepata
bahati hiyo mimi!” Akazidi kuwaza akijiumiza moyoni. Mengi yalipita
kichwani. Kumbukumbu za kipindi amechanganyikiwa hajielewi zikamjia.
“Inamaana na mimi ningekuwa na mwanamke kama huyu,
angenitafuta, nakujua nipo matatizoni akanisaidia mapema tu. Jelini alinikatia
tamaa.” Akaendelea kuwaza na kuumia, mpaka akakumbuka
anamajukumu mazito yanayomsubiria. Juma ndio limeanza. Kuangalia, Kamila
alishalala kitambo! Akatoka kwakunyata.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akabakiwa na kazi ya kufikiria pakumuweka huyo Kamila.
Alimtafutia hoteli nzuri, tulivu yakisasa akidhania angefurahia, ndio hakulala!
Yeye hana nyumba, anaishi kwa wazazi. Hasira zikampanda akawapigia simu wazazi
wake wote na kuwaweka kwenye conference call. Wote kimya wakitaka kujua
safari hii ni nini tena!
“Nataka
nyumba yangu.” “Tafadhali kuwa na subira Colins. Yule mpangaji ana mke na mtoto
mchanga. Siwezi kuwafukuza. Katika hilo tafadhali naomba fikiria.” “Siwezi
kufikiria kama nakuwa na wageni wangu, wana shida, halafu mimi nashindwa
kuwasaidia.” “Kwa nini usimkaribishe pale nyumbani?” Mama yake akatoa wazo.
“Ili na
yeye mumfanyie kama mlivyomfanyia Jelini? Mnataka kuendelea kunitesa
mpaka lini jamani!?” “Colins, nimekosa baba. Nakuahidi sitarudia kosa. Safari
hii nita..” Wakasikia simu imekatwa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Lakini huko alipobakia akabaki akifikiria pakumuweka
Kamila, lakini mwishoe anaishia wazo la mama yake si baya. Kwao
kumetulia sana. Mbali na hasira alizobeba kwa mama yake, alimjua ni mtu
mzuri sana. Mpole ndio maaana mama Simba alikuwa akimuonea.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akapiga tena. Wazazi wote wakapokea kama wanaofanya kazi
kwenye kampuni za simu, wakihudumia wateja. “Lakini akija hapo kuna
masharti.” Wakajua amekwama, ila jeuri kama baba
yake.
“Unataka
nini?” Mzee akauliza. “Hakuna
kumuongelesha kabisa. Hata salamu sitaki.” Kimya.
“Mnanisikiliza?”
“Nina swali.” “Hapana mama.” “Sasa ikitokea anasalimia?!” “Usiitike.” “Hapana
Colins. Hivyo mimi sitaweza. Itakuwa..” “Mbona baba akikulazimisha
kufanya jambo unakubali, mimi nakuomba jambo dogo tu, unashindwa?” “Basi kama wewe na baba yako hamjui, nyinyi wawili ndio
mnafanya maisha yangu kuwa magumu sana hapa duniani, mpaka naumwa,
na najua kwa hakika mtaniua siku si nyingi.”
Akaanza mama Colins na kulia juu. “Hivyo
ulivyo sasahivi na hasira, ndivyo alivyokuwa baba yako mpaka tukamtoa Jelini kwenye picha. Akapoa.
Sasahivi umerudi wewe, umempokea, hasira zilezile unaniadhibu
bila kunifikiria wala…” “Mbona wewe hujanifikiria!?”
“Nimekwambia
kwa sababu baba yako yupo kama wewe.
Na yeye alinipitisha hapahapa unaponipitisha wewe. Nimebaki na
mapressure, naumwa, mwili hausikii dawa, wasiwasi, sina raha! Acheni nife,
mpumzike. Labda utakuja kupata mama mwingine ambaye ni mwema kwako, na
hakosei kama mimi.” “Mimi sijasema nataka mama
mwingine.” Mzee akajua tayari ameshakamatika.
“Ila
sidhani kama mama ambaye anampenda mwanae angeweza kumtelekeza kama wewe.” “Nimekosa Colins. Na nipo tayari kutengeneza.” “Jelini wangu anaolewa. Unatengenezaje hapo?” Akaongea kwa uchungu ila sio ukali na hasira. Wote kimya
kwa muda.
“Najua
haitasaidia, lakini nimekosa Colins. Nimekosea sana. Tafadhali tafuta
jinsi ya kumsamehe mama yako, hata kama kwangu utashindwa, mimi nitakuelewa.
Yeye ndio aliye gutuka na kujua kuna kitu hakipo sawa kwako. Japokuwa
kina Simba walikuwa wakituficha hata kujua ulipo wakitudanganya
umesafiri kikazi au upo na majukumu mengi, mwishoe mama yako akashindwa
kabisa kusadiki.”
“Alikuwa na
kazi ya kukutafuta kila mahali alipokuwa akidanganywa na kuhisi upo. Ofisini na
huko Kigamboni. Kazi pia zilimshinda kwa ajili ya kukutafuta wewe. Alishashinda
huko Kigamboni akikusubiria mpaka usiku ndipo akajiridhisha kuwa kuna
kitu hakipo sawa, ndipo nikaingilia kati. Hana hatia.” Hapo hakujibu ila akaendelea.
“Nitarudi
na mgeni wangu jioni.” “Unataka nimtayarishie chumba?” Mama yake akaongea kwa kujikomba. “Bado siwaamini,
nitalala naye chumbani kwangu.” “Kama mkeo?!” “Kwani nimesema ni mwanamke?”
“Kwa hiyo hutuamini sisi na rafiki yako wa kiume, unataka ulale
naye chumba kimoja, na kitanda kimoja!?”
Kidogi akacheka.
“Na hakuna
kumuongelesha mama. Mwacheni kabisa. Kwanza nitakuwa nikija naye na kuondoka
naye. Hakuna kumsogelea na kumpa wakati mgumu. Ni yatima. Hana ndugu, amefiwa
na mtu wake wa karibu ambaye alikuwa kama mume. Alimleta hapa hospitalini.” Akawaeleza kwa kifupi ilivyokuwa mpaka kifo cha Mike.
“Nipo tu kumsaidia
maana ni kama amekwama. Na hata akili yake bado haijarudi kuwa sawa. Na ndugu
wa Mike wanamsumbua sababu ya mali. Kwa hiyo naomba hapo nyumbani kuwe na
mazingira mazuri jamani. Sio kuanza zile tabia zenu za kulazimishia mambo yenu.”
“Sitaki hata
mumshauri kitu. Niachieni mwenyewe. Nakwenda naye taratibu mpaka akiwa tayari
ataendelea na maisha yake.” “Sawa. Unafanya vizuri kumsaidia.” Akatulia kidogo bila ya kujibu, wote kimya kwa muda,
mwishoe akakata simu. Lakini ndio yakawa mazungumzo ya kwanza waliyozungumza angalau
na kufikia mwafaka tena baada ya muda mrefu sana.
~~~~~~~~~~~~~~~
INAENDELEA.
0 Comments:
Post a Comment