Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 16. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 16.

Wakati yao yakiwaendea sawa huko kanisani, wakishangiliwa nakupewa sifa, wengine wakitamani waliposimama wanne hao, bila kujua mapito yaliyowalazimu kupita ili kufika hapo, huku kwa Colins bado anauguza. Aliporudi ofisini kutoka wodini akakuta anasubiriwa. “Kuna mgeni.” “Ni nani tena jumapili hii?!” “Amejitambulisha kama wakili wa Simba.” Akacheka moyoni akijua ni Chris tu. “Amesema anazunguka kidogo atarudi.” Colins akapitiliza ofisini kwake akimsubiria kwa hamu.

Baada ya muda akaambiwa amefika. Akamruhusu aingie. “Naitwa Christopher ni wakili wa familia ya Simba.” “Umemsahau na Kemi.” Akamuonyesha anamfahamu. Akamtizama kidogo kisha akaendelea. “Lakini hapa nawawakilisha familia ya Simba, zaidi mdau wa hii hospitali, Love.” Kimya akimsikiliza.

“Love kama mmoja wa wamiliki wa hii hospitali na kampuni kwa ujumla, anahaki na mali za hapa. Kisheria anaruhusiwa kutumia mali zake atakavyo.” Colins akabaki akimwangalia tu.

“Sasa basi, kwa kuwa sasahivi ana uhitaji, anataka kutumia sehemu ya mali yake na wazazi wake pia ambao ni wamiliki au waanzilishi wa hii kampuni, wanaunga mkono.” Akatulia akimwangalia.

Akamuona anatoa karatasi kwenye mkoba wake na kumkabidhi, Colins hakupokea. Akaziweka mbele yake. Kimya akimtizama. “Hizo ni karatasi zilizowekwa saini na wamiliki wote wanne kwa upande wa Simba kuidhinisha kutolewa pesa benki. Akiwepo Love mwenyewe, wazazi wake na Loreta. Hundi itahayoandikwa, itaenda moja kwa moja kwenye kumuwekea dhamana Love. Atakaposhinda kesi, hiyo pesa itarudishwa kwenye akaunti za kampuni.” “Hapana.” Akajibu Colins na kumshangaza sana.

“Wewe unakataa kama nani? Maana kama sijakosea, wewe ni mwajiriwa tu, ila una hisa baadhi kama Love au Loreta. Hii ni kampuni ya wazazi wenu.” “Kufupisha hiki kikao ambacho kinanipotezea muda, nitakujibu mimi nakataa kama nani. Kisha nakuruhusu ukashitaki popote unapotaka, tutakutana mahakamani. Ila nina uhakika, hutataka kushindana na mimi Chris.”

“Unanitisha wewe bwana mdogo wa juzi tu! Hudhani kwa mpaka hapa nilipofika nishatishwa sana na wenye uwezo wao na wanaoogopewa hapa nchini! Acha ubabe wa kitoto.” Colins akacheka kwa kumsikitikia.

“Acha dharau.” “Nakusikitikia sana Chris. Kama hujajua, hao unao watetea mpaka kutaka kumdhulumu mtu asiye na hatia, mwenye ile hoteli, ambaye wewe kwa kupitia Love na Kemi, umemshitaki bila hatia, wamekutoa kafara.” “Acha kuni…” “Unaongea sana Chris, hunisikilizi. Nakwambia hivi, hao unao watetea, kwa kutaka watu wengine wasio na hatia, walipe garama yao, nakwambia hivi, wamekutoa kafara. Umejiingiza pabaya sana, mpaka nakusikitikia.”

“Acha kunitisha mimi. Nafuata sheria. Hakuna mtu yupo na kosa mpaka sheria iamue. Love na Kemi hawana hatia. Wewe ni nani mpaka uwahukumu? Na kama huyo mwenye hoteli hana hatia, basi mahakama itaamua. Usinipotezee muda wangu. Ninachotaka ni hundi.”

“Hutapata pesa hapa.” “Unakataa wewe kama nani!?” “Mimi kama mmiliki mkuu wa hapa. Na kukusaidia tu, karudishe majibu kwa waliokutuma kuwa, mbali ya kwamba nina mkataba wa ajira ya hapa, basi wajue, kwa sasa mimi nina hisa kubwa sana kuzidi kila mtu kwenye hii kampuni. Nina miliki zaidi ya asilimia 60 kwenye hii kampuni na katika hao uliowataja hapo juu kama wamiliki hapa, Loreta si mmoja wao. Hana hisa hata moja hapa.” Kabla hajajibu akaendelea.

“Kwa kifupi ili usizidi kunipotezea muda, hii kampuni ni kama yangu. Na unapozungumza na mimi, jua nina zungumza kwa niaba yangu mimi mwenyewe kama mdau mkuu, wazazi wangu na dada yangu, ambao wote hao pia na wao ni wadau hapa. Kwa kukusaidia tu,  sisi kina Komba ndio tuna kauli ya mwisho ya nini kiendelee kwenye hii kampuni.”

“Jambo la msingi nataka usisahau. Usiwahi kurudi hapa kama unaingia chooni. Weka miahadi. Upewe muda wa kuja. Kama ni karatasi, huna haja ya kuniona mimi. Mwachie sekretari. Na nilikuwa nikikuonya, sijui kutisha kama wengine. Siku ingine utakapoingia hapa kama leo, jua nitakutoa na polisi. Uwe na siku njema.”

“Haiwezekani!” “Wewe si umesema unakwenda na sheria? Acha kujiliza hapo kama mtoto mdogo wa kike, nenda kanishitaki, tukutane mahakamani. Vinginevyo acha kunipotezea muda kwa mambo ya kijinga. Umeona wapi mambo yanafanyika kama hivyo unavyotaka kufanya wewe na hao walio kutuma!?”

“Eti kampuni iliyo na wabia kibao, eti baadhi tu ndio wanaidhinisha pesa itolewe benki! Tena kwa matumizi binafsi! Mpaka unanitia wasiwasi na kiwango chako cha kufikiria na utendaji wako kazi! Unakimbizwa kama upepo tu!” “Najua ninachokifanya.” “Una uhakika?” Colins akamuuliza kwa kumdhihaki.

“Nakuuliza wewe, unao uhakika?” “Ndiyo.” “Unajua hata sheria na mikataba ya hii kampuni au umekurupuka tu nakuja hapa kama kondoo unayepelekwa machinjioni, tena siku ambayo hata si ya kazi!?” Kabla hajajibu, akamfukuza. Alikuwa na hasira naye kupita kiasi. Mbali ya kumsaidia kumuweka Kemi uraiani, akakumbuka unyama aliomfanyia Zulfa. Hapo alikuwa na hasira naye kupitiliza.

“Kwanza toka hapa ofisini kwangu. Unanipotezea muda.” Akawa ameshabonyeza kengele aliyokuwa imejengewa kwa kufichwa chini ya meza yake, maalumu kwa kuita walinzi.

Chris akaanza kugomba. Akitetea haki ya familia ya Simba kwa jazba walinzi wakaingia wakamkuta ameng’aka, anawaka kwelikweli kuwa Colins hajui anachokifanya, na atamuonyesha yeye alizaliwa kabla yake na anajua anachokifanya. Colins kimya akimtizama pale mbele ya wale askari wake ili kutoa sababu ya kukamatwa.” Askari akamsogelea.

“Huwezi kutoa vitisho ndani ya ofisi ya mtu.” Kwa kuwa alikuwa ameshapandwa na jazba, akataka kumjibu yule askari, wakamuwahi na kumvuta nje.

“Hakikisheni mnapata taarifa zake kamili, mziandike na apewe onyo kabisa.” Akarushia neno wakimtoa pale. Hapo akawa amemtibua Colins. Akajiapia kutumia nguvu zote, kumfikisha magotini.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akatafuta picha zote za Zulfa akiwa peke yake. Binti aliyekuwa naye kwenye mahusiano. Akaziweka pamoja, kisha akaingia kwenye uwanja wake wa mapambano, hiyo laptop yake, akamtumia kwa email kama salamu tu. Akahakikisha haachi email yake wala ip address yake. Ili asijue inapotoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akiwa amerudisha akili kazini na akili imeshatulia kutoka alivyotibuliwa asubuhi hiyo, hata asijue ni saa ngapi, akasikia hodi taratibu kama mtu asiyetaka kumsumbua. Kuangalia ni Kamila. Akatoa tabasamu kwani alikuwa amebeba chakula. “Nimeambiwa leo una kazi nyingi. Sitakuongelesha. Nakuachia tu chakula.” “Usijali. Ingia. Nimekua na mambo mengi lakini naweza chukua mapumziko mafupi.”

Akaweka kila kitu pembeni na kugeuka vizuri. “Vipi naona mambo yako si mabaya?” “Nilikuwa jikoni na wapishi. Wazee wazuri sana. Wastaarabu, wacheshi na wachokozi.” Colins akacheka.

“Wana maneno mengiii!” “Ndio vizuri. Na chakula kinanukia vizuri! Asante.” “Nimejua hujala, nikaomba kidogo cha wagonjwa, nikakutengenezea pembeni.” Akakipokea na kukiangalia. “Unajua kuweka chakula kwenye sahani! Mpaka kinavutia.” “Asante. Nikuache ule. Nisikuingilie.” “Hamna shida. Nimefurahi umechukua hatua Kamila. Itakusaidia.” Akamuona ameanza kuingiwa hofu. Anabadilika rangi. “Ni nini? Niambie tu.” “Kula kwanza, nitakwambia baada ya kazi. Acha nirudi kule kazini.”

“Kamila!” Akamuita kabla hajatoka, akageuka. “Ni nini?” “Nataka kukuomba kitu lakini kinaweza subiri.” “Nini? Niambie tu, usiogope.” “Waliponituma nipeleke vyakula vya madaktari, wakati napita, niliona chumba cha wauguzi. Wanabadilishia nguo. Kuna kitanda, nilitaka.” Akasita.

Akamuona anaanza kutetemeka mikono. Ashapaniki. “Niangalie Kamila. Unaweza kuzungumza na mimi kitu chochote. Na kama kitashindikana, nitakwambia tutafute suluhu nyingine. Kwa hiyo niambie tu, usiogope. Niambie.” “Naomba nikae hapo kwa muda wakati najipanga, kuliko kukaa kwenye kile chumba cha wagonjwa. Wameniambia ni garama sana! Halafu kinanifanya nijisikie kama mgonjwa!”

“Sawa. Japo garama isikutishe. Ni wagonjwa wachache sana wanamudu vile vyumba. Kwa kuwa ni kweli ni garama, ndio maana unaona kipo wazi mpaka sasa. Ila kama kina kufanya ujisikie kama mgonjwa, hilo linaeleweka.”

“Nashukuru. Na nakuahidi nikijiweka tu sawa, nitaondoka.” “Sawa.” Akaitika hivyo tu kwa kifupi na kuanza kula. “Unaondoka saa ngapi?” Colins akamtizama. Akameza na kumjibu. “Inategemea. Vipi?” “Nauliza tu.” Kisha akatoka. Alimgundua ni mtu aliyejawa hofu, akaona amchukulie taratibu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika majira ya saa 3 usiku, akashituliwa na ujumbe kwenye ile simu yake mpya ambayo Kamila humtumia jumbe Mike, na kushindwa kabisa kugawa hiyo namba na kuiacha kwa ajili hiyo tu. Akaacha kila kitu na kuanza kusoma. ‘Kifo chako kimeacha pengo ambalo sijui litakuja kuzibwa vipi hapa duniani! Ni wewe pekee ndiye unanielewa na kuweza gawa muda wako kwa ajili yangu. Nipo mpweke Mike! Mungu anajua jinsi ninavyojisikia.’

‘Natamani urudi hata kwa muda mfupi tu, unisaidie kimawazo. Nimekwama, naogopa sana. Najaribu kuchukua hatua, kama alivyonishauri Colins. Nimeambiwa ndio jina lake. Ila yeye hajaniambia. Kumbe yeye ndio kiongozi mkubwa wa hii hospitali nzima! Wamenimbia anamamlaka yote, kwa hiyo anamajukumu mazito, siwezi kuwa nikienda ofisini kwake kila ninavyo jisikia. Siruhusiwi tena. Nimekwama.’ Colins akashituka asijue ni nani amemkataza asimuone! Akagundua hata hakurudi kuchukua vyombo.

Akajaribu kuvuta kumbukumbu kama kweli hajawahi kujitambulisha kwake! Akagundua mazingira hayajawahi kuruhusi, wakati wote wamekutana kukiwa na mazingira ya hekaheka. Akafikiria kidogo, akaendelea kusoma. Maana ulikuwa ujumbe mrefu sana.

‘Huwezi amini Mike, nimeomba kuishi hospitalini! Lakini usiwe na wasiwasi, wamenipa na kazi. Nitatoka tu hapa. Halafu usiwe na wasiwasi na hawa ninaofanya nao kazi sasahivi. Ni watu wazima. Wacheshi na wanajiheshimu. Hawana mambo mabaya, na wanataka kesho mimi ndio nipike. Nimefurahi! Narudia kazi yangu ninayoipenda.’

‘Luca amenipokonya pete uliyonivisha na gari. Wamenichukulia nguo zangu zote. Lakini usiwe na wasiwasi. Nipo tu sawa nitaenda kununua nguo zingine, bado nina akiba. Nishauri nikaishi wapi baada ya hapa. Nitumie tu hata ishara. Sijui kabisa wapi patakuwa salama. Tungekuwa wote najua ungeniambia nisiogope, kwa kuwa tupo wote. Popote tutaishi. Ila naogopa vibaka njiani. Nisaidie.’ Alipomaliza tu kusoma akatoka kama akimbie. Akaanza kumsaka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akaenda mpaka kwenye chumba alichoomba aishi, japo hakuwa ameingia ndani, lakini kulisikika na hekaheka! Kuingia na kutoka kusiko isha kwa kila muuguzi wa kike. Akajiuliza huyo Kamila atalalaje humo, na kukosa jibu. Akazunguka mpaka kwenye chumba alichokuwa amelazwa, akaambiwa kule alishatoka na kuaga mapema sana. Ndipo wazo likamjia kuangalia jikoni. Akatoka hapo kama akimbie tena, safari hii akiwa na uhakika atakuwa huko.

~~~~~~~~~~~~~~~

Na kweli akamkuta amekaa peke yake ametulia kama yupo darasani. Hata hakujua kama Colins ameingia. “Mbona umekaa huku peke yako?” Akashituka sana. “Samahani, sikukusudia kukushitua.” “Hamna neno. Nimekaa tu. Nasubiria kule kutulie ndio niende nikalale.” “Hapana. Hutalala pale.” Akaingiwa na wasiwasi.

“Kwenye kile chumba ndio sehemu wanabadili nguo na wengine kupumzika kwa muda mfupi ili kuendelea na kazi. Kwanza sidhani kama utapata kitanda wazi.” Akamuona amekosa raha. “Twende tukatafute sehemu ya kulala kwa muda wakati tukitafuta sehemu ya kudumu.” “Wameniambia una mambo mengi! Sitaki kukusumbua.”

“Ni nani amekwambia hivyo?” “Sekretari wenu. Aliniona napita na chakula kuingia ofisini kwako, nilipotoka akaniita. Alikasirika anasema namfanyia dharau. Niliingia bila ya kumuomba yeye ruhusa. Mimi sikujua! Ndio nikamuomba msamaha. Ila akasema nisirudi tena. Kama nimesaidiwa mara moja, niwe na shukurani nisiendelee kusumbua.” “Pole, lakini usijali. Hunisumbui. Twende.” Wakatoka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akiwa na mengi yanayoendelea kwenye maisha yake, bado Colins anajiona anawajibika kwa Kamila. Ni Nini Kitaendelea kwao na Kamila mwenye Mike nyingi mdomoni?!

Jelini, Ezra, Junior na Emelda yao?!

INAENDELEA.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment