Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 15 - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 4 - SEHEMU YA 15

    “Nisikilize Kamila. Eti mimi naona nikinyume na hivyo! Nisikilize tu tufikirie pamoja. Usilie, nisikilize tu.” Akamfanya amsikilize. “Wewe umesema Mike alikupenda sana. Ulimuona akiishi kwa juhudi zake na kufikiria. Kwa nini hayo yote usiyaenzi kwa kupambana uishi vile angependa uishi kuliko kutoa maisha yako ambayo yeye aliyahangaikia mchana na usiku ili uwe na furaha? Kuutoa uhai wako kwa namna hiyo ni kupuuza juhudi za Mike.” Akamuona hapo anasikiliza.

“Kuanzia sasa, ishi kama mtu uliyependwa sana na kuonyeshwa njia maishani. Sidhani kama Mike alikutoa sehemu moja ili uangamie! Maana kwa kujiua ujue unamkosea Mungu, na hawezi kuja kukuweka sehemu moja na mtu kama Mike. Huko unakofikiri unamfuata Mike, hutamkuta. Mungu atakupeleka pabaya ambako utakutana na uasi mbaya zaidi ya huu unaoukimbia hapa duniani, na kamwe mtu mwema kama Mike hutakuja kumuona tena maishani.” Akamuona anaanza kutulia kabisa kama kimeanza kuingia akilini.

“Kama kweli unampenda Mike, anza kuishi kama yeye ili ukiondoka hapa duniani, ukakutane naye huko.” “Sijui pakuanzia!” “Unakumbuka jana uliomba kazi na ukapata?” Akakubali. “Leo ulitakiwa kuanza kazi, lakini umelala hapa, ukijaribu kuharibu juhudi zote za Mike! Sidhani kama ikitokea leo Mike anarudi, anakukuta na hali hiyo, atafurahia!” Akakataa akilia.

“Wewe unakipaji kikubwa sana. Hicho kikusaidie kuendesha maisha yako. Acha kulala kwenye makochi, au kwenye gari. Maisha aliyokuachia Mike, sisemei nyumba na gari, hapana. Ramani aliyokuachia ya maisha, hiyo ndiyo nazungumzia, ukipambana, unaweza kuja kuyaishi. Tena vizuri tu.”

“Na auhitaji kujua kila kitu kwa wakati mmoja. Chukua hatua moja moja kama ulivyosema jana usiku. Utafanikiwa tu.” Akamuoana anavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu. Akamuona anajishika shingoni.

“Panauma?” Akamuuliza kwa kujali. Akatingisha kichwa taratibu kukubali. “Moyo wangu unauma zaidi. Natamani kama ningeondoka na Mike hapa duniani.” “Pole sana. Pole Kamila.” Akajifunika na kuendelea kulia kwa sauti ya chini, ila kwa uchungu sana. Akakumbuka kilio kama hicho kukisikia kutoka kwa Jelini. Akamsogelea pale kitandani, tena akakaa kabisa.

Alikuwa akigugumia kwa uchungu kana kwamba anakatwa sehemu.  Akamtoa mkono ndani ya shuka akamvuta karibu yake. “Sijui unavyojisikia. Ila ninajua kwa hakika, ‘it’s going to get better.’ Nakuahidi hivyo. Jipe tu muda. Umesikia?” Akatingisha kichwa kukubali.

“Pata muda wa kupumzika, kisha utoke kitandani, nenda kule jikoni. Nimekuona jana. Ni kitu unafurahia sana kufanya. Ukiwekeza mawazo yako hapo, utajikuta akili inawaza mambo sahihi na utaweza tu. Sawa?” Hapo anazungumza naye akiwa amemshika mkono. Akambembeleza mpaka akatulia.

    “Tuone shingoni.” Akawa anasita. “It’s okay. Nionyeshe tu.” Akamuona machozi yanamtoka tena. Akajisahau akamfuta kwa upendo. “Nionyeshe.” Akajifungua amtizame shingo nzima. “Nitaulizia kama kuna dawa ya kupunguza maumivu.” Akatingisha kichwa kukubali na kurudi kujifunika. Akabaki akimwangalia mpaka akajishitukia mwenyewe.

    “Acha nikuulizie dawa.” Akaona atoke tu. Baada ya muda akarudi. Macho yakagongana. “Najua hunifahamu Kamila. Lakini ni sawa nikuombe uniahidi kitu?” Akavuta tena pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu kama anayejaribu kutulia, kisha akatingisha kichwa kukubali.

Akarudi kukaa tena na kumshika mkono. Kamila akajiweka sawa. “Niahidi hiki ulichokifanya leo, yaani kujidhuru, hutarudia tena.” Akaanza kulia tena kwa uchungu. “Tumekubaliana utamuenzi Mike kwa kuishi kile alichotamani kuona kwako. Si ndiyo?” Akatingisha kichwa kukubali.

    “Nina hamu naye! Hakika nina hamu naye sana! Mungu anajua jinsi ninavyomuhitaji. Mike ananipenda sana jamani, hakuna mwanadamu atakuja kunipenda kama Mike! Sijui maisha mengine bila yeye Mike. Moyo wangu unauma sana. Nimejawa hofu, naogopa, nahisi nitakosea sana. Sijui maisha yanakuaje bila Mike!”

    “Nilikuwa nikivumilia hata pale ninapoishi sasahivi nikijua atarudi tu. Siamini kama ndio basi tena, jamani!” Akalia hapo kwa uchungu kisha akaongeza. “Ila sitarudia tena kumfedhehesha Mike wangu. Sitajidhuru tena.” Akamfuta machozi. “Usiwe na haraka. Hatua ndogondogo kama mtoto. Endelea kupokea kila siku kama ulivyosema jana. Hata sasahivi usiache. Fanya hivyohivyo.” Akakubali.

“Pumzika. Watakuja kukuletea dawa ya kukupaka hapo shingoni. Kisha ulale kabisa. Ukiamka unaweza kwenda jikoni. Si unapakumbuka?” “Nafikiri. Nikishindwa nitauliza.” “Au nipigie simu, nitakuja kukufuata nikupeleke. Wana maagizo yako. Ukifika tu, watajua ni wewe. Usiwe na wasiwasi.” “Asante.” Akashukuru na kutulia. Colins akaona aondoke tu. “Nitakuwa ofisini. Ukikwama popote usisite kunitafuta. Vinginevyo nitakuona baadaye.” Akatoka.

Dhahabu Inapopitishwa Kwenye Moto.

Jelini alivyokuwa amepania hiyo siku ya mwenzie! Alihakikisha anapendeza. Na kwa kuwa alijua wangeanzia kanisani, basi akambebea nguo nyingine. Nzuri sana inayoendana na kaumbile kake na mpambaji, Emelda hajui.

Wakati wanamaliza kikao, kina Junior wanatakiwa kanisani wajiandae na ibada ya sifa, akamwambia Junior amwambie Emelda amfuate garini. Bila kujua akamfuata. “Sasa wake za twins, kazi yetu ni kupania kupendeza.” Emelda akaanza kucheka.

“Sasa mbona hata huulizi kikao kiliendaje?” “Tushakubaliana kuna harusi, hayo mengine stori za baadae. Ingia garini, badilisha nguo, upambwe. Sitaki mazoea na Junior. Sio kwa sababu amekuona asubuhi, basi ajue ndio utakua hivyohivyo!” Emelda kucheka meno yote nje.

“Gauni zuri sana Jelini! Asante kipenzi.” “Sasa ukichanganya na kaumbile kako, rangi! Mate yatamtoka Junior.” Kazi ya kumtengeneza ikaanza wakiwa wamejificha nyuma kabisa, wamekaa kiti cha nyuma, Jelini maneno mengi kiti cha mbele cha dereva, mwenzie anacheka mbavu hana.

~~~~~~~~~~~~~~~

Waliingia kanisani baada ya kipindi cha sifa kuanza. Kwa hakika Emelda alionekana nadhifu. Mchungaji alikuwepo kwenye kupiga gitaa la bezi, Junior ndio muongoza sifa, safari hii Ezra alikuwa akipiga kinanda. Mama mchungaji alikuwa akicheza mpaka jasho. Ungejua Junior ndiye anayeimbisha. Na yeye alizijulia nyimbo anazopenda mama yake. Basi lazima aziimbishe hizo kama kuchanganya ni chache tu. Basi hapo ibada hukamilika kwa mama yake. Na akimuona mumewe anapiga gitaa, basi vigelele vyake husikika, mwanzo mwisho.

Muda aliokuwa akingojea Emelda kwa maombi akifunga bila dalili za kuja kujibuwa, ukawadia. Ila akitamani sana kujua aina ya pete atakayovalishwa. Mchungaji akasimama. Akatoa matangazo yote. Kisha akafika kwenye wakati wenyewe.

“Kuna maombi unaomba kwenye umri fulani. Na unamsihi Mungu, yatokee ukiwepo hapa duniani, isiwe kama ahadi ya Ibrahimu ya uzao mwingi lakini akafa hajaona.” Kanisa zima kimya.

“Sasa na mimi Mungu ameanza kunijibu na kunipa fulsa ya kuanza kushuhudia kwa macho. Ezra na Junior njooni hapa mbele.” Wakasimama na kukimbilia mbele. Lakini jinsi alivyorudi Junior, amebadili nguo, amependeza kirasmi kama mwenzie Ezra, watu wakahisi jambo. Maana alivaa kitanashati kijana wakati akiimbisha ili kuweza kucheza kwa uhuru wote.

“Hawa wawili bwana! Wanaweza kukuchonganisha na Mungu hivihivi!” Watu wakacheka. “Unaweza ukawaombea jambo. Likifanikiwa kwa mmoja halafu mwingine hajafanikiwa, ujue kwao wao hayo maombi hayajajibiwa bado. Unabakiwa na deni la kuendelea kuombea. Hapatatulia mpaka wote wapate.” Watu wakazidi kucheka wengine wasielewe ila kuhisi.

“Sasa siku chache zilizopita, Ezra alijibiwa.” Mchungaji akaendelea. “Jelini mama upo wapi?” Akasimama cheko, meno yote nje! “Njoo mama.” Alivyokuwa amependeza, naye Ezra hana dogo, akaenda kumpokea na kumshika mkono kabisa, watu wakipiga vigelegele mpaka juu madhabahuni.

“Sasa msifikiri kwangu hapo nilimaliza kazi! Nilikuwa na deni nikikumbushwa kuombea mchana na usiku, mpaka na Junior naye alipojibiwa.” Wengine wakashangaa. Maana huyo Junior ametoka kuvunja uchumba na kutangaza mpya ndani ya juma moja tu! Mpaka Hope akashangaa na kutaka kumjua huyo mchumba mpya!

“Sasa safari hii nimewaambia hata wao. Zege hailali. Hawa wachumba tutakao ombea safari hii ndio kina mama wa wajukuu zangu!” Watu vigelegele haswa, zaidi mama mchungaji.

“Leo Junior anachumbia, na tangazo lao la kwanza la ndoa linatoka leoleo. Wote wanne. Kwa hiyo mwenye kipingamizi na wao, awahi haraka na ushahidi wa kueleweka. Vinginevyo, jumapili ya nne kuanzia sasa, nawatoa hawa wanne wote sokoni.” Kelele na miluzi kutoka kwa vijana.

 “Nitasimama hapahapa, niwatamkie baraka, mpaka kifo kiwatenganishe, nibakie na kazi ya kuombea wajukuu. Hakuna kurudi nyuma tena.” Vigelegele.

“Haya Junior, kazi kwako.” Wote macho kwa Junior. Wakamuona anavuta pumzi kwa nguvu kama anayetaka kufanya kazi nzito. Watu vigelegele wakijua ndio anachumbia sasa. Ezra na Jelini wanamcheka. “Jikaze.” Ezra akamrushia neno. Akatingisha kichwa akicheka kisha kuchukua kipaza sauti na kuanza kutoka hapo jukwaani, akiongea.

“Kuna watu hupita kwenye maisha yetu kutukumbusha sisi ni wa kina nani, kisha wanaondoka. Wanaweza kukuacha na maumivu lakini wanakuwa wametimiza kusudi lao na hufanyika msaada kwenye maisha yako yote.”

 “Halafu kuna viatu vya watu wengine, sijui Mungu aliumba vipi miguu yao! Yaani viatu vyao, huwa vinawaenea wao wenyewe tu. Hata ukijaribu kumvalisha mtu mwingine, havienei. Unabakia kuwaachia wengine malengelenge ya miguu au madonda kwa kulazimishia viatu visivyo vyao.” Hapo Junior anaongea huku anasogelea upande aliokuwa amekaa Emelda, kila mtu akitaka kujua kwa hamu huyo anayekwenda kumchumbia. Lakini Emelda, msichana wa kazi za ndani, hakuna hata mmoja aliyemdhania.

“Imenichukua muda, nikiwa na hicho kiatu mkononi, nikimpita mwenye nacho, mpaka Mungu akanihurumia kama Hajiri kijakazi aliyezaa na Ibrahimu, baba wa imani, alipokuwa na kiu kali jangwani, akijua mtoto wake atakufa tu, akiwa anamkimbia Sara mke wa Ibrahimu. Kumbe hakuwa mbali na maji, ila hakuwa ameyaona. Macho yake yalifungwa na mengi, mpaka alipoonyeshwa na malaika.” Vikasikika vigelegele vya mama mchungaji.

Bado Jelini na Ezra walikuwa wamesimama mbele madhabahuni, Ezra amemshika mkono Jelini. Wamependeza haswa. Wapiga picha na wachukua video, walikuwa wakimfuata Junior kwa karibu tu kupata tukio zima.

Akaenda mpaka alipokuwa amekaa Emelda, akampita mama yake na mdogo wake akaenda mpaka alipokaa yeye, akapiga goti mbele yake watu wakahamaki wasiamini! Kwamba Junior anaoa msichana wa kazi wa nyumbani kwao!

Akamshika mikono yote miwili. “Nakupenda Emelda. Na naomba uwe mke wangu.” Hivyo tu Emelda akihisi yupo ndotoni. Akatingisha kichwa kukubali. “Niambie kwa maneno basi!” Akaongea kwa kubembeleza. “Wewe unajua ninavyo kupenda Junior!” Wengine wakabaki mdomo wazi, wengine vigelegele wakishangilia. Akambusu mikono yote miwili kwa muda mrefu tu kwa hisia zote, watu wakishangilia, ndipo akamvalisha pete, na kusimama.

~~~~~~~~~~~~~~~

Hata Hope hakuamini! Junior hakumvalisha pete kwa namna hiyo. Kwanza walikwenda naye kwa sonara kupimisha pete yake. Ilikuwa nzuri sana na ilimgarimu sana Junior. Hakutaka kuisubiria. Akaenda ifuata yeye mwenyewe punde sonara alipowatumia ujumbe kuwa ipo tayari.

Akaanza kuivaa kabla ya jumapili, akitangaza ufahari kazini na kwa mashoga zake, ndipo jumapili yake wakaombewa! Leo Junior amepiga goti na kutangaza anampenda Emelda na Emelda anasema Junior anajua ni kwa kiasi gani anampenda! Ndoa ndani ya majuma manne! Upendo huo ulianza lini? Kiroho kikaanza kudunda hapo alipokuwa amekaa. Hasira na wivu.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Haya naomba mje hapa mbele.” Nyimbo zikaanza kupigwa watu wakishangilia. Jelini na Ezra wakaenda kuwapokea wakiwapongeza mpaka kukumbatiana wao wote wanne. Hakika walipendeza na kuvutia haswa. Watu walicheza hapo wakishangilia, wengine wasiamini.

 Jelini akamvuta mkono kuona pete. Wote wakacheka kuona zinafanana. Emelda kama ya Jelini! “Hakika mimi sijawapatia wenzenu!” “Na ibakie hivyohivyo Jelini. Kwanza ulikuwa ukiwatafutia wapi hao wenzetu!?” “Mwaya Junior naye! Si usemi tu!” Ezra na Emelda mbavu hawana. Wakicheka hapo mbele, watu wakiwashangilia.

“Yaani hawa wanne wakirudi kuja kusimama tena hapa mbele kama hivi walivyo, jamani ni kuwafunga pingu za maisha na kubariki watoto wao. Mmesikia Junior na Ezra! Hili zoezi Mungu asaidie lifike mwisho.” Wengine wakazidi kucheka na wao wakacheka wakitingisha vichwa.

Safari hii muoe.”  Akaweka msisitizo akiwa anasikika kwenye kipaza sauti. “Tunaoa baba mbona hivyo!?” “Nataka watu wapumzike!” Vigelegele wao wanacheka. Hao wawili wote walishachumbia kwa mara ya kwanza, hiyo ya pili.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Jamani! Junior anaoa binti yangu.” Mchungaji akafanya washirika watulie. “Maana hawa waliondoka, tukabakiwa na viziwanda wawili. Noah na Emelda, wakinyang’anyana ziwa, sasa naona amebakia Noah peke yake!”

“Hongera kwa kujitunza Emelda binti yangu. Mungu wa mbinguni akubariki wewe na uzao wa tumbo lako.” Akaita watumishi wengine pale mbele akataka na wao wapige magoti, kina Ezra nao pembeni.

“Watoto wako na watoto wa watoto wako wakaitwe heri. Ubarikiwe uingiapo na utokapo kwa vile ulivyotupenda, kutuheshimu, na kututunza mimi na mke wangu, na watu wa nyumba kwangu. Tumbo lako libarikiwe, litoe watoto bora, watakao kutunza wewe na mumeo mpaka kifo chenu.”

 “Nakataa uharibifu wa mimba. Kwako, Jelini na watoto wa watoto wenu. Utasa usitajwe kwenu. Kisiwepo kifo cha bahati mbaya katika nyumba zenu na nyumba za watoto wenu.” Bwana mchungaji aliomba huyo, mpaka ibada ikageuka ikawa ya maombi.

Gafla nguvu za Mungu zikatawala kila mmoja akiguswa na hayo maombi ya mchungaji kwa Emelda. Na wenyewe wakaanza kuomba. Wakageuka kuungana mkono na mchungaji kumbariki huyo Emelda. Ungejua huyo binti amegusa moyo wa mchungaji. Alitamka baraka bila ya kumpunja.

~~~~~~~~~~~~~~~

Mungu hanaga kikao wala wakumuuliza ni kwa nini anapofanya jambo lake. Siku hiyo Emelda alilipwa na Mungu hadharani, hata mama yake asiamini kama ni mwanae! Alivyo badilika Emelda, ungedhania alizaliwa kwenye neema, kumbe Mungu alimtumia kunguru wake, ambaye ni Jelini aliyemuumba na moyo mzuri, ampige msasa.

Kwa muda mfupi tu, Emelda alikuwa nadhifu, na neema ya Mungu ikawa juu yake. Hana anachoweka mwili mwake kisivutie! Fumba na kufumbua, akawa mama mjengo. Jumba la Junior lililokuwa likimtoa roho Hope, leo fukara Emelda ndio atamiliki!

Akiwa anaishi kwenye nyumba ya tembe, akidharaulika na kunyanyaswa huko kijijini kwao, huku mjini Mungu alikuwa akimuandalia makao nadhifu na ya hali ya juu sana. Lakini ilikuwa lazima ampitishe kwenye moto kwanza ili kung’arisha dhahabu yake.

Kupita kuwa mtumwa wa kudharaulika, kutukanwa na kudhulumiwa mpaka kufikishwa pale Mungu alipo muandalia.

Mwanaume mwenye hofu ya Mungu, msomi, mwenye pesa na bado anampenda haswa. Kwa hakika dhahabu iliyopitishwa kwenye moto, siku hiyo iling’aa.

Je, angekimbia majaribu yake? Angekimbia pale Esther alipokuwa akimnyanyasa? Pengine leo asingekuwa ameinuliwa hadharani! Emelda akawa amemaliza mitihani yake ya maisha kwa kipindi hicho, Mungu anampa cheti hadharani. Ilikuwa furaha ya ajabu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ni nini kinachokuumiza na kukufanya ukimbie?

Yapo majibu mengine kutoka kwa Mungu, yamefungamanishwa na majaribu.

SIMAMA ILI UPAMBANE, UVUKE. Kukimbia ni kujichelewesha.

INAENDELEA.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment