Wawili hao wakaanza kusaka sehemu ya kuishi ya Emelda usiku huo. Kukiwa hakuna wasiwasi wa pesa ila sehemu tu. Wasijue kinachoendelea kwao. Ukawa usiku mzito haswa.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Sitageuka kuwa mama
yako. Na Ester hatakua dada zako. Nimekataa.” “Mbona kama hii kesi imekua yangu
gafla!?” “Kwa kuwa wewe ndiye unayemuendekeza Ester. Msichana yule wa mwisho
kabla ya Emelda, hakutuambia juu ya Ester ukamkania? Sasa leo umesikia na sauti
yake kabisa, akikufuru kwa msichana kama Emelda aliyekuwa akimzolea matapishi!
Unataka alaaniwe?” Kimya.
“Au na hiyo sauti
utasema si yake amesingiziwa!?” Kimya. Akamkabidhi simu yake. “Mpigie Ester,
mwambie namuhitaji hapa, sasahivi.” “Hata mimi nimeshituka mama! Najua ni
kufuru mbaya sana. Na nimeingiwa hata hofu mbele za Mungu. Natamani hata
hayo maneno yasingepitishwa hapa kwetu. Lakini huyu mtoto yupo kwenye ndoa
changa, mama J. Kweli tumtoe kwake usiku huu ili tuanzishe kesi?! Hivi mumewe
atatuonaje sisi?” “Kwa jumbe hizi, za mpaka muda huu, inaonekana anao muda wa
ziada. Nashauri hiki kikao kifanyikie hapa na si kwake.” “Kwamba utamfuata!?” Mama
akakaa vizuri.
“Nimekwambia sitampoteza
Junior kwa mwanamke. Sitamsusa kama KWENU walivyonisusia wewe. Maana ni hivi, Emelda atakapotoka
hapa bila maelewano, ujue zile siku chache nilizokuwa nikibahatika na
kina Junior, zitahamia kwa Emelda. Sitawaona tena hapa. Halafu, kwa kuwa
Ester ameahidi kumchafua hata kanisani, inamaana atahama kanisa.
Ujue ndio na Junior atahama. Alipo Junior ndipo alipo
Ezra. Ndio Jelini. Halafu na familia ya kina Jema itahamia huko alipohamia
Emelda, ambapo yupo Ezra na Jelini. Mpaka hapo unanielewa ninachozungumzia?”
Mzee kimya.
“Mimi si mjinga
kumkubali Emelda, kwa sababu najua madhara ya kupinga mapenzi. Ni
kuwaweka wale wapenzi karibu zaidi, kama kweli wanapendana. Kama
kilichotokea kwetu. Kadiri mama yako na dada zako walivyokuwa wakinichukia na
kunifanyia visa, ikatusaidia kutusogeza sisi karibu zaidi. Mwishowe kwakuwa walishindwa
kuwa na sisi wakati ule, sasahivi wanaona aibu kujirudi.”
“Ndicho kinachotaka kutokea
sasahivi kwa Junior. Lakini mimi nimekataa. Mke atakayeolewa na Junior, atapendwa
na kuheshimiwa humu ndani kama Ester. Kwa kuwa, narudia tena. Sitampoteza
Junior, mtoto niliyekuwa nikishinda naye njaa wakati tukiwa sisi si kitu.
Maana hawa wengine wametukuta tukila
milo yote na kusaza tukichagua nini tule, lakini si Junior.”
“Mtoto asiye na makuu
ila kusaidia kila mtu akijinyima yeye! Amemwaga mamilioni ya pesa kwenye huduma
pale kanisani bila kutaka kulipwa.” “Mama J, mke wangu, mimi nipo upande wako
na Mungu wangu ni shahidi. Hizi jumbe zinanitisha mpaka naogopa. Tafadhali
katika hili tusimame pamoja. Ninachozungumzia ni jinsi ya kushugulikia hili
bila kuharibu zaidi.” “Basi chagua. Kikao ni hapa au nimuite Junior na Ezra
nyumbani kwa Ester?” Mzee akafikiria kwa haraka akapata jibu.
“Mimi nina wazo.”
Mama kimya akimtizama. “Nafikiri sisi tukae tuyazungumze halafu Ester
tuzungumze naye kesho mida mizuri ya heshima hata kwa mumewe. Hatatuelewa
kuanza kumuita binti tuliyemkabidhi kwa heshima tena mbele za Mungu usiku huu! Sidhani
kama ni sawa. Emelda hana haja ya kuhama hapa.” Akamkabidhi simu. “Ya nini
sasa?” “Hayo uliyoniambia mimi, mwambie na Junior. Akimleta Emelda hapa, ndipo
tutajua baada ya hapo.” Akasita.
“Kwa hiyo tunakutana
kwa Ester?” Mama akaendelea kusimamia pakali. “Unajua Junior hatanisikiliza
kama ambavyo anakusikiliza wewe!” “Kwa sababu mimi namsikiliza na kumuheshimu.
Huwezi kumpeleka Junior kama mtoto mdogo huku ukimuonyesha upendeleo wa
waziwazi kwa Ester! Hawezi kukubali. Ukiongea naye kwa kuheshimu mawazo yake, hawezi
kukataa. Mimi ameniambia ananitumia sababu 5 za kutorudi kwa
Emelda hapa. Wewe unampa sababu gani za kumrudisha Emelda hapa?”
Kwa Emelda.
Emelda anakutana na
kina Junior anaona jinsi walivyopaniki asielewe kulikoni. Akaomba kuzungumza na
Junior nje ya ofisi walipokuwa wakisubiria jibu la meneja kujua kama kuna
sehemu, yaani apartment ya Emelda. Wakatoka.
“Ni nini kinaendelea
mbona unaonekana haupo sawa!?” “Nakutafutia sehemu ya kuishi wewe na kina mama
wakija.” “Kwa nini sio tena nyumbani!? Mama amegairi?” Akamsimulia juu ya jumbe
alizotuma Ester ila hakumwambia kilichoandikwa
au kurekodiwa. Akashangaa Emelda bado anasubiri sababu ya kutorudi nyumbani kwa
mchungaji.
“Nimezifuta
kwenye simu yako, sitaki uzisikie.” Emelda akabaki anasubiria. “Kwamba mchungaji
ameona ndio amekataa nisirudi kwake?” Yaani yeye Emelda bado akawa anasubiria sababu,
Junior amemaliza.
“Sijawasiliana na
baba ila mama.” “Kwa hiyo ndiye amesema nisirudi au!? Sijaelewa!” “Mimi ndiye
nimeonelea usirudi. Inatosha Emelda.” Akabaki amemkodolea macho. “Huwezi
kuendelea kunyanyasika.” “Juu ya jumbe za Ester!?” Jinsi alivyouliza akamfanya Junior
kutulia kama sasa na yeye haelewi tena! Alijua atajipatia sifa kuwa anajali,
akashangaa Emelda ametulia kama hajamsikia na alijua wazi amemuelewa.
“Sidhani kama wewe
leo umesikia jambo jipya ambalo mimi sijawahi kumsikia Ester akiniambia,
Junior.” “Sio hizi.” Emelda akacheka. “Katika hizo jumbe hakuna inayosema nilikuja
kwenu nanuka na nikitumia mavitambaa yaliyochakaa kwenye siku zangu za hedhi
mpaka yeye aliponisaidia pedi?” “Haiwezekani Emelda!” “Hajasema, nilikuja
kwenu nanuka kwapa mpaka akawa hawezi kulala usiku?” “Naomba acha Emelda.
Tafadhali usirudie.” Mpaka macho yakabadilika yakawa mekundu kama alie.
“Junior, kwa miaka
yote hiyo nimekua nikiishi na Ester chumba kimoja. Na Ester ni yule akiwa kwenye
hedhi anatapika nakuumwa tumbo, hata kama una roho mbaya vipi, huwezi lala
jinsi anavyougulia tumbo na kutapika. Utamuhudumia lakini maneno atakayokuja
kukupa baadaye! Unaweza sema siye yeye!”
“Atakukumbusha jinsi
ulivyomuuguza akiwa kwenye siku zake. Nilivyomdekia matapishi yake na
kufua mashuka yake ya damu, tena taratibu kama unavyomjua Ester, kisha
anakuuliza, ‘utaendelea kuishi hivi mpaka lini?’. Yaani kama vile
nilivyomfanyia ni haki yake!” “Emelda!!” Akacheka wakati mwenzie ana
hali mbaya ya kupitiliza.
“Mimi mbona
nishamzoea! Na najua huwa anachukia sababu huwa namnyamazia, simjibu.”
“Kwa nini uishi hivyo Emelda!?” “Sababu, ya kwanza na kubwa ni mama
yako. Sijawahi ishi na mtu akaniheshimu na kunipenda bila unafiki
kama mama yako. Na kumbuka ni kama alinilipia garama au kuninunua
au weza sema kununua uhuru wangu kutoka kule nilikokuwa nikifanya kazi
mwanzoni na hajawahi nidai ile pesa.”
“Kingine nilikwambia
Junior, nina majukumu ya familia ambayo siwezi ruhusu hisia zangu
ziingilie. Nategemewa kwetu. Watu watatu wananiangalia mimi. Shule ya Mika na
garama zake zote, ni mimi kufanya kazi ili alipe ada na michango yote ya shule
pamoja na matumizi yake binafsi.”
“Bado shule ya Mateo
ambayo inavijimichango vidogovidogo ambavyo bila hivyo wanakuwa wakimnyanyasa
mbele ya wanafunzi wote. Siwezi pata usingizi nikifikiria hajalipa hiyo
michango, inamaana atapitishwa na wale walimu pale kijijini pale tulipopita
mimi na Mika. Fedheha ya hali ya juu. Unakuwa unachekwa na wanafunzi
wote kama ambaye unatembea na kinyesi wakati wote. Bado kula yake na mama!”
“Halafu pia najijua na kuwajua
wanadamu. Sitaweza kwenda sehemu ingine nikapata mama mwenye nyumba
mwingine kama mama yako, Junior. Nina uhakika kwa kuwa nimeishi naye na kuishi
na watu wengine nikaona jinsi wanavyo nichukulia. Wanaoweza kusema, ndio
kama kina Ester. Na wengine ndio hata hawahisi uwepo wangu hata nikiwa
karibu yao, ni kama sipo tu. Lakini si mama yako.” Junior akazidi kuumia
akijisuta na yeye.
“Leo asubuhi
amehakikisha nimeondoka kwakwe kuja kwako nikiwa nimependeza. Mimi msichana
wake wa kazi! Hanitambui mbele za watu kama msichana wake wa kazi! Ananitambulisha
kama binti yake, tunaye nyang’anyana ziwa na Noah! Ndio usemi wake
popote kule. Na ndiko hata Ester naye alikopata huo usemi. Na si uongo.
Hatanifanya nikajisikia mimi kama kijakazi wake.”
“Ikifika kipindi cha
ada ya Mika, namkopa mshahara wa mpaka mbeleni! Mika yupo shule leo,
nakuhakikishia ni kwa sababu ya mama yako. Hanipunji mshahara wangu
wala hanicheleweshei. Ukimfanyia jambo, anashukuru kama hastahili,
wakati ananilipa!”
“LiNoah likiniomba
nimfulie, mama alikuwa akijua nimemfulia au kumsafishia chumba, anamlazimisha anilipe
mpaka na yeye amefanya mazoea. Huna utakachomfanyia Noah, na ulevi wake ule,
sema nahisi kama limeacha! Siku hizi simuelewi vizuri. Amejaa pale ndani kazi
uchokozi asubuhi mpaka usiku!” Junior akacheka kidogo vile alivyojiuliza, maana
aliwajua hao wawili.
“Lakini vyovyote baba
anavyomchukuliaga Noah, lakini huna utakachomfanyia asikushukuru kwa dhati,
tena anakupa kabisa pesa. Mwenyewe anasema sio kama ananilipa, ni ananipoza. Lakini
yote hayo ni kwa sababu ya mama yako. Alikuwa akimwambia Noah kama wewe
ulivyokuwa ukimuomba akufanyie jambo kisha unampa pesa, ndio na yeye afanye
hivyhivyo kwangu. Sasa hembu niambie, nampata wapi mimi mtu kama yeye?”
Kimya.
“Ndipo narudi kwenye
sababu yangu ya kwanza na ya msingi, sina jinsi ya kumlipa mama yako kwa
kuishi na mimi kwa namna anayoishi na mimi isipokuwa kumsaidia. Mama
yako ni mtu mzima, halafu na mama Leti ana matatizo ya mgongo. Kuna mambo mle
ndani hayawezi kufanyika bila mimi. Yaani hata mama akinipa ruhusa
kwenda kwetu, nikirudi nakuta hayajafanyika kwa sababu mama yako amekwama.
Na yeye unamjua, si mvivu ila hana uwezo.”
“Kwa hiyo, kama yeye hajanifukuza,
sitaondoka kwake mpaka tumpatie mtu. Tafadhali Junior. Tusimuadhibu mama
kwa ajili ya Ester. Si mgeni kwangu. Ananiumiza, lakini sio wakumkimbia.”
Junior akachoka kabisa.
“Tusijivuruge. Kesho
ni siku muhimu sana kwa Ezra na Jelini. Twendeni tukalale, tuendelee na mipango
yetu kama kawaida. Tusimpe shetani nafasi. Atatuvuruga mpaka sisi wenyewe tupoteze
malengo. Tujikute tunaendana na ratiba zake, akiwa ameshatutoa kwenye kalenda
ya Mungu.” Wakati Junior amepigwa na baridi kali hata hajajibu, Ezra
akawafuata.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Naona hapa tumefanikiwa.”
Junior akamwangalia. Emelda kimya. “Ni nini tena!?” Akawa kama ameshamsoma
Junior. “Emelda hataki kuondoka nyumbani.” “Sio kwamba sitaki. Natamani
sana, ila isiwe kwa kukimbia. Tutamuadhibu mama yenu. Mimi najua
ninachozungumzia. Mama anahitaji msaada jamani! Hatuwezi kumuacha hivihivi eti
sababu ya Ester! Hapana jamani! Na naomba muwe na amani.” “Hivyo sitaweza.”
“Basi naomba umfikirie mama pia. Halafu naomba niwe muwazi kwenu, kwa hakika
sioni sababu.” Ezra akamtizama Junior kama aliyemuuliza swali aliloelewa.
Akamjibu. “Japokuwa
sijamuonyesha jumbe zenyewe, amerudia mwenyewe neno kwa neno mpaka nimemuomba
aache.” “Haiwezekani Emelda!?” Ezra akahamaki kwa hofu kubwa mpaka ikaonekana
usoni.
“Aliyoyasikia Junior leo,
sio mageni kwangu. Ni kama wimbo tu. Na sina sababu yakumsingizia Ester, mpaka
huwa namuhurumia, nasema anakufuru. Ni hivyo baba yake anasema
anamuombea sana. Lakini hakuna jipya. Kwa hiyo nashauri tukapumzike,
kesho ibadani.” Ezra naye hoi.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akatoka na Jelini.
“Naona kikao kimehamia nje!” “Na naona kinaisha. Emelda anataka kurudi
nyumbani.” Wakamsimulia kwa kifupi sababu ya kutaka kumtoa hapo kwa mchungaji
na yeye kukataa, Jelini naye hoi. Emelda akawacheka taratibu kama alivyo.
“Nyinyi nendeni
mkapumzike, kesho siku yenu. Naomba unisaidie usafiri wa kurudi
nyumbani.” Hapo akamwangalia Junior. Ikabidi tu wakubaliane naye. Wakaomba
pamoja na kuiweka siku ya kesho mikononi mwa Mungu. Wakaombea mipango yao mpaka
kusema ‘Amen’. Kidogo
Junior akawa ametulia.
Penzi Ambalo Halijachanganywa.
{kama tui la kwanza}
“Sasa kesho ni kama
mnatangaza uchumba kwa mara ya kwanza. Ezra atakuvalisha pete kwa upya.” Jelini
akachekelea bila kufikiria. “Lakini si unajua inamaana itabidi utupe hiyo pete twende
nayo, ili kesho akuvalishe pale kanisani mbele…” Alimshitua Jelini! Kabla
hajamaliza akaficha mkono wenye hiyo pete. Kisha akakataa. “Hakika sitaweza
kulala Junior. Hapo mtaninyima raha kabisa.”
Hawakutegemea, maana na machozi yalishaanza kumtoka.
“Jelini! Anakuvalisha
kesho pale kanisani!” Wakaharibu mudi yote ya Jelini. “Siwezi
kulala bila hii pete. Hivyo mimi sitaki. Mnanirudisha nyuma, wakati huko
nilishatoka.” Akaanza kulia. “Basi Jelini. Basi.” Ezra akambembeleza.
“Ila ujue kesho ningekuva…” Akapandisha mabega kabisa kukataa akijisogeza
pembeni.
“Mimi
najijua. Bahati zangu huwa haziji mara mbili. Utashangaa chochote kinatokea,
hii pete haitakaa ikarudi tena hapa kidoleni. Nitarudia yale maisha ya zamani,
ya upweke. Nawasihi katika hili mnielewe jamani. Nina hofu ambayo
hamuwezi kunielewa.”
“Basi Jelini. Basi.” Na Junior naye akamtuliza akikumbuka yake alivuliwa na
kuwekewa mezani.
“Tunaweza ichukua
tukishafika kanisani, pale mkiwa mnaitwa mbele muombewe na wazee.” Hapo napo
ikawa shida. “Mimi nilijua tu jambo lazima
litokee jamani! Sijui kwa nini mimi!” Akalia kabisa.
“Jelini, hiyo pete
mimi nitahakikisha inarudi kidoleni kwako. Chukulia ni kama unachumbiwa kwa
mara ya pili na unapata nafasi ya kujipanga vizuri mbele ya watu wengi!
Ni sifa.” “Mimi sitaki sifa. Sitaki kuchumbiwa
tena. Nataka ibakie vilevile mara moja. Kwanza mimi sihitaji watu wengine. Mimi
watu wangu wote wa muhimu siku ile mlikuwepo. Inatosha. Napenda surprise
yangu ya kwanza na ibakie tu vilevile, ila naombeni msinitoe tena pete
kidoleni. Haitakaa ikarudi hapa. Mimi najijua.” “Basi haitoki.” Ezra
akamsogelea na kumkumbatia kabisa.
“Basi Jelini. Na
samahani. Basi tutamwambia mchungaji awaite tu pale mbele. Atangaze uchumba,
picha zenu ziwekwe pale mbele kwenye screen ili watu wengine waone
mlivyo chumbiana, basi muombewe.” Hilo akakubali.
“Samahani
Junior. Najua mna mipango yenu. Lakini hii pete kwangu ni zaidi ya kuchumbiwa.
Nilipita kipindi kigumu sana kabla hajaja Ezra. Nikimaanisha Ezra aliponirudia kwa
mara ya pili. Ni zaidi ya faraja au tumaini. Ameniongezea kitu ambacho sina
jinsi nikawaeleza mkaelewa. Nikiwa popote, hata nikiamka usiku usingizini,
nikiiona na kuanza mawazo yanayoninyima raha, nikiiangalia, najua Ezra wangu wa
kuaminika yupo sehemu. Ni umbali wa simu tu. Narudi kulala bila shida au nafanya
yangu kwa utulivu. Hapa maombi yangu ni Mungu ajalie iongezeke ya pili
na si kupungua.” “Nimeelewa Jelini, na samahani sana.” Junior akamuhurumia
kwa jinsi alivyoongea kwa hofu. Ujanja wote ulimuisha Jelini cha maneno, Ezra
akambusu hapo mbele yao.
“Nakuahidi ya pili
inakuja muda si mrefu. Tuvumilie kidogo tu.” Jelini wa mikono, alishajaa hapo
mikononi na kujilaza kabisa kifuani, Emelda akapotelea mawazoni kabisa, Junior
akamuona. “Acha nimrudishe Emelda akapumzike. Naamini kesho kila kitu kitakuwa
sawa.” Wakaagana.
“Jelini!” Emelda
akawa kama amekumbuka kitu. “Nashukuru sana kwa mavazi ya kesho.” “Emelda naye!
Kila saa unashukuru tu!” Akacheka na kurudia. “Asante. Naenda kufanyia mazoezi
viatu.” Jelini akamcheka. “Tutakushika mkono usianguke.” “Mpaka kesho nitakuwa
nishaviwezea.” Wakataniana hao wawili ndipo wakaondoka lakini Junior
akamshukuru Jelini kwa kumjali Emelda.
Junior&Emelda.
Junior akawa anamrudisha
Emelda, wakawaacha hapo hao wachumba wakiagana. “Nikuulize kitu Emelda?”
“Ndiyo.” Akamwangalia. “Unaamini kama najutia muda niliopoteza bila
wewe?” “Mimi nakuamini Junior. Tafadhali usiishi kwa hukumu.” “Siwezi. Ila nina
swali jingine.” Akamwangalia. “Unaamini kama nakupenda kwa dhati?”
“Nakuamini Junior! Usingekuwa na mimi sasahivi kama si upendo. Na mimi
nikuulize kitu?” “Niulize tu.” Emelda akamgeukia kabisa.
Kisha akamuuliza.
“Utaishi na mimi kwa hukumu mpaka lini?” Akanyamaza. “Furaha yangu ni
kukuona unafuraha, Junior! Hapo ndio naweza hata kula. Tafadhali naomba
mimi na wewe tuanze ukurasa mpya. Ndio nitajisikia kama maombi yangu
yamejibiwa kiukweli.” Junior akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha, kimya.
“Usitishwe na Edwin
wala Ester. Wewe ndio umewajua kwa undani leo. Lakini mimi nimekuwa nikiishi
nao hivyohivyo lakini bado nikabaki nikikupenda wewe.” “Basi Emelda. Ila
naomba unielewe na mimi. Leo imekuwa siku ngumu sana kwangu. Sana. Tokea
asubuhi mpaka sasa, napata habari mbaya tu zakuniumiza, kasoro wewe kunikubali.”
“Basi naomba hiyo itoshe kukufanya ulale na kuamka vizuri kesho.”
“Noah ameniambia
unaongoza sifa kesho.” Ikawa kama ndio anamkumbusha. “Daah! Nimesahau kabisa!
Alitaka nimtumie nyimbo nitakazoimba, nimekuwa na mambo mengi sijafanya hivyo.”
“Basi nitakukumbusha kabla hujalala.” “Nashukuru.” Mara simu ikaingia.
~~~~~~~~~~~~~~~
USIKU WA HEKAHEKA.
INAENDELEA.
0 Comments:
Post a Comment