“Ilikuwa ni siku
ambayo sikutakiwa kuwepo pale na kidonda ili wanijaribishe mguu wa bandia. Kwa
hiyo nikajikuta nipo pale kwamba nitasubiria foleni ndefu vile lakini nikijua
nitakachokwenda kuambiwa. Siwezi kupewa mguu wa bandia mpaka kile
kidonda kipone tena. Vai ananisafisha kidonda ila moyoni nilikuwa
nimejawa uchungu wa kupitiliza. Ila akazungumza na mimi kitu kilichonishangaza
sana.”
“Ikawa kama
anazungumza na mimi na vile mapungufu yangu yalivyo. Ikanifanya nijirudi
kabisa. Nikapoa. Akaniacha pale baada ya kunisaidia. Yeye akidhania ni kile
kidonda tu, kumbe akawa amezungumza na moyo wangu. Kufupisha habari ndefu,
tukapotezana na Vai. Sikumuona tena. Mpaka siku moja.” Wakamuona ametulia kwa
muda.
“Hakika ni bora
ukosane na wanadamu ila si Mungu. Nilipita mahali nikaona ni bora kuondoka kabisa
hapa duniani. Nikiwa nishatundika kamba, najiandaa kujinyonga, Joshua
akanipigia simu nikiwa sitarajii simu yake. Kwanza ni usiku, na nilishajua mida
ya usiku anakuwa na familia yake, huwa hatuzungumzi mida ile.” Naya alilia
sana. Watu wote kimya.
“Ikabidi tu nipokee
maana sikujua anataka kuniambia nini! Ila naye ikawa ametumwa na Mungu
kama Vai tu. Kuzungumza na mimi. Akaniambia Mungu amemtuma aniambie, ‘hajamalizana
na mimi’.” Watu wakazidi kushangaa.
“Yeye aliniambia
hajajua ni kwanini ametumwa hivyo na kwa nini wakati huo ambao alikuwa na
wageni. Ila alijua hataweza kusubiri tena, lazima apige na aniambie
hivyo. Kufupisha hiyo habari, akazungumza na mimi sasa akijua ni mpweke. Akaja
kunishauri kuwa lazima kutoka. Nitafute gym nifanye mazoezi mbali na ya
hospitalini. Itanisaidia kutoka ndani na kujichanganya na wengine. Nikafuata
ushauri wake.”
“Nikiwa nimempoteza
Vai, sijui hata nitampatia wapi tena. Kwanza hata sikuwa nikimtafuta. Ni Vai, binti
anayejielewa. Mrembo, halafu mimi mlemavu. Mbaya zaidi wakati huo sikuwa
hata na kazi! Nalishwa na kutunzwa na shemeji. Sikutaka hata kujisumbua naye. Nilijua
sina hata nafasi kwake.
“Sasa wakati natembea
na gongo langu, nachechemea, natoka gym nikasikia mtu ananiita nyuma yangu.
Kugeuka alikuwa Vai na yeye anatoka maeneo hayohayo ila saluni. Alikuwa
amependeza sana.” Watu wakacheka vile alivyoweka msisitizo.
“Mimi mwenyewe
nilibabaika kwa sekunde kadhaa. Ndipo nikamkaribisha kwangu nikijua yeye ni
mwanafunzi, halafu tukakutana akiwa na njaa. Akawa anakwenda kununua chakula.
Na mimi nikawa nimepika mavyakula mengi, sina mtu wakula naye kipindi kile cha
sikukuu za krismasi. Nikamkaribisha kwangu ale, kisha nimfungie kingine abebe.
Kama shukurani tu. Hapakuwa na wazo jingine, kwa sababu kama nilizotangulia
kusema hapo awali, yeye ni Vai mimi bado mlemavu, sina hata mguu bado
nachechemea, sina kitu. Hapakuwa na hata wazo mtu kama yeye anaweza hata
kunifikiria.”
“Basi, kwa jinsi
alivyokuwa amependeza, ikabidi tu nijikaze, nikodi taksii mpaka kwangu. Bwana
Vai amejawa shukurani! Ndipo ikawa kama Mungu kazini. Mimi nikiwa na
kilema kibaya cha kutoridhika. Macho yangu wakati wote kutizama nisicho
nacho, yeye anaona hata maji ni kiburudisha cha ajabu sana. Akikushukuru kwa
jambo, mpaka unatulia na wewe na kuanza kufikiria ulichompa. Ukimwambia jambo
ambalo huna, yeye anakurudisha kwenye kilichopo hapo.”
“Siku yetu ya kwanza nilimsimulia
ukweli wote juu ya historia yangu. Sikujua ni kwa nini. Lakini nilijua kwa
hakika angetishwa na kukimbia. Lakini nikashangaa amejawa utulivu
mpaka nikajikuta nazungumza mambo ambayo sikupata nafasi kujieleza kwa watu wengine
na wao wakaweza kusikia na upande wangu na mimi. Au niseme sikupata mtu ambaye alitaka
kusikia upande wangu, ila yeye.”
“Vai akanisikiliza kwa
kutulia mpaka ikabidi nimuulize mbona hashituki na kukimbia! Kufupisha habari
ndefu, siku ile ndipo kwa mara ya kwanza, baada ya mateso mengi hapa duniani,
ndio kama Mungu akajidhihirisha kwangu kwa wazi kabisa kupitia Vai.
Akawa rafiki, ndugu na faraja ambayo sikujua kama nastahili.”
~~~~~~~~~~~~~~~
Lakini nabii
hana heshima nyumbani kwao. Vai alishakosea sana nyumbani. Ndoto za wazee wao
ilikuwa afike mpaka chuo cha udaktari. Amalize na awe daktari. Akakataa chuo
alipomaliza tu kidato cha nne, kitu kilichowaumiza sana wazazi. Wakati Nanaa
akisoma wao walikuwa ni wale binti wasioshikika. Mjeuri, haambiliki.
Ndugu zake walikuwa hawaamini wakati Bale akieleza mazito na makubwa ya Vai
kwenye maisha yake. Wakati wengine wakishangilia na vigelegele, wao
walijinyamazia tu wakijua anapambwa. Kwanza ni usiku wake. Kimya
wakijiangalizia.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Kuanzia hapo
tukajikuta ni kama mchana na usiku lakini tunaohitajiana kwenye mapungufu yetu.
Tunafuatana kila mahali kama marafiki tu, mpaka nilipojua kwa hakika, sitakujapata
mwanamke mwingine kama Vai. Lakini atanikubali kweli!? Ndio ikawa hofu yangu. Majaribu
ya maisha yakaja kumsogeza na yeye karibu yangu, na kujua mimi ndiye
mume wake. Lakini tena kwa vile nilivyokuwa nimeharibu kwenye jamii ya
wanao nifahamu, ikawa ngumu kuaminiwa na Vai.”
“Tukatulia
tukimsubiria Mungu, tupate kibali sasa kwa hao ndugu ambao nilishawaumiza
kupita kiasi, huku Joshua akituongoza kwenye kusubiria, tukiwapa watu nafasi,
bila kuwazonga ila tukimwamini Mungu, atawagusa na kuridhia kuniamini na
Vai.”
“Haikuwa rahisi hata
kwa Vai ambaye anazungukwa na vishawishi vingi, halafu ananisubiri bila tumaini.
Lakini alikubali kusubiri na mimi. Tukifunga na kuomba mpaka Mungu
alipojibu.”
“Huwa namwangalia Vai
nakujiambia, wakati Mungu akimuumba yeye, aliweka vitu vilivyopungua
kwangu.” Watu wakashangilia.
Akapata nafasi ya
kupiga goti tena, wakichukuliwa video vizuri. Akamvalisha pete, Joshua akabaki
akiangalia kwa hamu ajue kama ameamua kupata kiss kwa mara ya
kwanza au la. Alitulia Joshua akifuatilia kwa makini sana hatua kwa hatua. Mwanzo
mpama mwisho anamaliza kumvisha pete.
Lakini akamuona
anasimama, akamkumbatia vizuri, kisha kumbusu shavuni, basi. Hata
yeye hakuamini! Akapotea pale kabisa mawazoni akitafakari wakati watu
wakishangilia. Bale akaamua kusubiri! Alimtia Joshua wivu wa hali
ya juu. Akapatwa wivu wa ajabu! Akajisikia kupitwa mbali sana na Bale. Kwamba
Bale ameweza kusubiri, yeye alishindwa! Akabaki kimya kabisa
akiangalia watu wakiwapongeza. Kula na kunywa, kisha kikao cha kwanza kikaanza.
Joshua akashindwa
kujizuia, wakati wakitoa pledges yeye akasema mbali na mchango, lakini
pia atalipia fungate yao. Popote watakapochagua na kwa siku zozote
watakazotaka. Mpaka Naya akamtizama kwa mshangao. “Hiyo ni zawadi yangu kwa
Bale.” Hakuna aliyeelewa, ila Bale alihisi. Jinsi alivyomshukuru Joshua, Joshua
akajua amejua ni kwa nini amefanya hivyo. Ikamuongezea hali ya kusubiri
mpaka hiyo siku ya fungate yao.
Pale Majibu Ya Maombi
Yanapochanganywa Na Ugumu Mwingi Wakuumiza Na Kushawishi Kutoshikilia
Muujiza Wako.
Wakiwa wamegawana
kama mwanzo. Kila mmoja kwenye ukumbi walipofunga viti, usiku huo na yeye Junior
akiwa na kijana mwingine wakichangamka ili kutoa hivyo vitu vya Jelini kwa
haraka ila kwa usalama, akasikia simu ikicheza kwenye mfuko wa nyuma. Akajua ni
ujumbe umeingia. Akidhania ni simu yake. Akaona isubiri mpaka amalize.
Ikanguruma tena. Baada ya muda, ikanguruma tena. Kisha tena.
Kwamba zimekua jumbe nne. Ikabidi atoe. Akagundua si simu yake,
aliondoka na simu ya Emelda.
Akafungua kuona.
Zilikuwa jumbe za maneno tatu na sauti moja kutoka kwa Ester. Ile ya sauti
ilionekana kubwa. Akaunganisha na bluetooth yake. Kwa kuwa alikuwa na
kazi, akaendelea kusikiliza huku akifanya kazi na huyo kijana. Ulikuwa ujumbe mzito.
Ester amemrikodia Emelda na kumtumia. Yalikuwa maneno makali. Kama
ingekuwa anaambiwa, asingeamini kama dada yake anaweza kumwambia hivyo
Emelda.
Alimkumbusha Emelda tokea
siku ya kwanza anafika kwao. Jinsi alivyokuwa duni. Akitumia vitambaa
vilivyochakaa kipindi cha hedhi yake. Vile alivyokuwa akinuka harufu mbaya.
Alimsema mengi mpaka Junior mwenyewe akasimamisha kwanza. Ilikuwa ngumu
kusikiliza moja kwa moja. Akaendelea kufanya kazi. Hata aliyekuwa naye alijua
amebadilika.
Alikuwa akitetemeka
kwa wazi kabisa na jasho kumtoka. Wakamliza na kupandisha vitu vyote kwenye
gari. Akamwacha huyo kijana wa Jelini aondoke, akaingia kwenye gari yake.
Akajitumia ule ujumbe wa maneno bila kumalizia. Akafungua jumbe za maneno na
kujitumia pia. Kisha akaondoa gari kurudi alipomuacha Emelda na Jelini kwani
hapo ndipo walipokubaliana kukutana.
Njiani akaona
amalizie tu ule ujumbe wa sauti. Alisikiliza mpaka akajikuta machozi yakimtoka
huku akiendesha. Ezra akapiga. “Sisi huku
tumeshamaliza. Nimemruhusu Teri arudishe vitu, naelekea walipokuwepo kina
Jelini au unahitaji msaada nikufuate?” “Na sisi tulishamaliza muda tu.
Nimetingwa tu ndio maana nimeshindwa kukutaarifu. Ila nipo njiani kuelekea
walipo kina Emelda.” Jinsi alivyozungumza akajua si kwema.
“Vipi, kuna
nini?”
Alijua hawezi kujificha kwa Ezra. “Daah! Natamani haya
ninayoyasikiliza yangekuwa hayatoki kwa Ester, aisee. Nimeshindwa hata
kukutumia! Aisee nimeshindwa.” “Umekutumia wewe?” “Hapana. Emelda.
Sikujua kama niliondoka na simu yake. Sasa wakati nipo ukumbini ndio jumbe
zikaanza kuingia. Nikataka kupuuza mpaka
nikimaliza lakini kadiri zilipokuwa zikiingia, nikahisi ni muhimu. Kutoa, kumbe
ni simu ya Emelda, jumbe zinatoka kwa Ester. Ni
chafu sana. Ni za kumdhalilisha kupita nitakavyokwambia, sitaweza
kukutumia Ezra. Ni picha mbaya, ingekuwa Emelda hatakuwa mke wangu,
ningekutumia.” “Aisee pole sana Junior. Pole
sana kaka.” Junior akabaki akijifuta machozi.
Ezra akajua ameumia
sana. “Utafanyaje?” “Cha kwanza nitahakikisha Emelda
mwenyewe hataona wala kusikia hizi jumbe.” “Ila atajua kama umefuta jumbe
zake.” “Nitamwambia nimezifuta. Lakini Ezra, inatosha. Emelda hatarudi kuishi
pale. Itakuwa ni kama namtelekeza mahali ninapojua atateseka tu.”
“Ester
amemuhakikishia kumlipiza kisasi. Na kumwambia kama anadhania ndio
ameondoka pale nyumbani sasahivi atatawala yeye, asahau. Yeye ni mtoto
wa baba, na hata leo ametuhakikishia kwamba yeye bado ni mmoja wa familia. Anao
uhuru wa kuingia na kutoka pale nyumbani muda na wakati wowote. Amempa usiku wa
leo tu, kesho awe ameachana na mimi. Lasivyo atahakikisha maisha yake ni machungu.”
“Haiwezekani Junior!”
Ezra hakuamini.
“Nakwambia
ninapotamani haya yangekuwa yamesemwa na mtu mwingine na si Ester dada yangu,
niamini aisee. Nakutumia vitisho vyake maana amevituma kwa maneno. Matusi ya
nguoni ndio yapo kwa ujumbe. Na ameapa kumtangaza Emelda pale kanisani kila mtu
amjue hila, ufitini na uchawi anaotumia hata kwa wanaume
maana anahisi hata Edwin si akili zake, amemfanyia mambo ya kishirikina. Ili
amtunze yeye huku pesa zake akitumia kwa mambo ya kiushirikina akiloga
wanaume wengine.”
Ezra mwenyewe akaanza kutetemeka.
“Mungu
wangu! Hiyo itakuwa mbaya sana Junior!” “Itabidi sasa kuingilia kati. Kujulisha
wazazi kabla hajachafua kanisa.” “Kama bado hatujachelewa!” “Na huo ndio
wasiwasi wangu. Maana ukimsikiliza, ni kama aliyepagawa! Si Ester ninayemfahamu
aisee! Amejawa na uchungu! Hasira kali! Sasa katika hili huwezi jua umbali gani
atakwenda. Tafadhali nisaidie kufikiria ni wapi pakumpeleka Emelda usiku huu.
Lakini hatarudi nyumbani na wala si kwa kina Jelini. Inatosha kumangamanga
kwenye majumba ya watu. Acha apumzike.” Ezra akafikiria kwa haraka.
“Upo wapi?” Akamwambia. “Sasa nina wazo. Tumtafutie full funish apartment.
Itakayomtosha yeye na mama yake, pamoja na mdogo wake wakati tukitafuta sehemu
ya kuwaweka mpaka ndoa.” Hilo likakaa sawa. Wakapanga pakuanza kutafuta
hizo apartment usiku huo.
“Basi wewe
wapigie simu kina Jelini, waambie wakimaliza watusubirie, tutawaambia sehemu ya
kutufuata, wakati mimi nazungumza na mama kumtaarifu juu ya Emelda.” “Akikusihi
Emelda arudi?” “Anarudi kwenye mazingira gani, Ezra? Hapana. Ninachojua atataka
kujua sababu. Itabidi niwaambie na kuwaonyesha jumbe zote. Itakuwa kesi ambayo
baba atamtetea Ester. Ester atarudi kwake na kumuacha Emelda kwenye ile nyumba
ambayo baba yupo. Unafikiri kutakuwa na amani tena?” Ezra akavuta pumzi
kwa nguvu akifikiria huku akigeuza gari kuelekea walipokubaliana na Junior,
kutafuta malazi ya Emelda.
“Hamna
jinsi. Lazima tuzungumze na Ester usiku huu. Ili kuzuia hii sumu.” Junior naye alikuwa
akitafuta sehemu ya kugeuza ili kuelekea huko walipokubaliana. Wakakubaliana
kuwa ni jipu lazima kulitumbua tu. Wakaagana, kila mmoja akipiga simu
kama walivyokubaliana. Ezra kwa Jelini, Junior kwa mama.
Kwa wazazi.
“Samahani
mama. Najua mnajiandaa kulala. Lakini nilitaka kukutaarifu kuwa Emelda hatarudi
tena hapo nyumbani. Namtafutia sehemu ya kuishi. Na nashukuru kwa moyo
wa kutaka kusaidia ndugu zake, lakini wataishi na Emelda huko atakapokuwepo.
Nitakusaidia kutafuta msichana wa kazi kuziba pengo lake. Lakini naomba kwa
sasa uhesabu ni kama yupo likizo. Mama Leti aendelee kuja tu.” Huyo mama alishituka,
usingizi wote ukapaa. Akajua historia inataka kujirudia na kwake. “Naomba usikate simu. Tafadhali Junior.” Mama yake
akamsihi.
“Nipo
mama.” “Kwa nini umeamua hivyo?” “Nakutumia sababu 5, ambazo naomba
usikilize kwa makini na kusoma kwa kutulia. Ukiwa umejitoa kwenye nafasi ya
mama yetu, ila kama mama mchungaji wa mtu kama Emelda ambaye umeishi
naye hapo. Halafu uniambie kama ungekuwa wewe, ungefanyaje? Na nakuomba
hakikisha hazimfikii Emelda japo nimetoa kwenye simu yake.” “Kwamba
hajui?!”
“Nafikiri ni Mungu tu mama yangu. Nilijikuta
nimeondoka na simu ya Emelda. Ndio zikaingia nikiwa nayo. Yeye hajui hizi
zilizoingia usiku huu. Na nimekusudia ibakie hivyo. Tafadhali.”
“Sawa. Ila nitakapokupigia tena simu, tafadhali pokea Junior mwanangu.
Usiniache hivi usiku wa leo.” “Siwezi mama.” Akakata na kazi ya kumtumia jumbe zote
alizotuma Ester kwa Emelda ikaanza.
Alipomaliza tu, simu
ikaingia kutoka Ester. Junior akapokea bila ya kusema kitu. Ester akaanza kwa
matusi, kaka yake akimsikiliza. Alipoweka kituo tu, Junior akamjibu. “Kwa bahati nzuri nimejikuta nipo na simu ya Emelda. Kwa
hiyo…” Kabla hajamalizia simu ikakatwa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Maji Yanazidi Kutibuka.
Ni Nini Kitaendelea?
Usipitwe
0 Comments:
Post a Comment