“Aliwezaje kusoma
yote hayo na kutulia hivyo!” Junior akajiuliza nafsini mwake na
kumwangalia asijue hali anayopitia huyo Emelda. Hofu ya kitumbua kuingia
mchanga. Lakini akazungumza kitu kilichomshangaza. Ikawa tofauti kabisa na
matarajio yake, mpaka akamtuliza moyo. “Uliponiambia Ester ana maneno machungu,
hukuniambia ni kwa kiasi hiki!” Emelda akacheka taratibu na kunyamaza. Junior
alikuwa na hali mbaya! Ulikuwa ujumbe mmoja ila mrefu wakuumiza. Akajitumia na
yeye huo ujumbe.
Emelda akaona ujumbe
unaingia kwenye simu ya Junior. Kuangalia ulikuwa ule ujumbe. Akamtizama
Junior. “Unataka kufanya nini Junior!? Sitaki haya mambo yazidi kwenda mbali.”
“Kwa hakika kwa sasa hata mimi sijui Emelda. Ila nilihitaji kuwa na huo ujumbe
na mimi kwenye simu yangu.” Akaomba simu yake. Akamtumia na Ezra. Ila kutoka
kwenye simu yake mwenyewe si ya Emelda.
~~~~~~~~~~~~~~~
Kutoka kwenye ujumbe
mzito hivyo, hakuwa amesahau ujumbe wa kwanza. Yeye shida yake ni
Edwin. Alishajua ujumbe uliokuwa umeingia kabla ya wa Ester utakuwa ni kutoka
kwake tu. Na akawa amepatia.
Akafungua. ‘Naamini upo mzima Emelda. Kabla ya kumuomba mchungaji kupata
muda wa mazungumzo na wewe, nimeona nianzie kwako wewe mwenyewe kwanza. Naomba
kesho baada ya ibada, tutoke twende mahali tukazungumze. Kuna jambo nililitunza
kwa muda mrefu moyoni, nikimuomba Mungu anipe wakati muafaka wa kuzungumza na
wewe. Naona sasahivi ndio limepata kibali machoni kwa Bwana. Naamini tutapata
wakati mzuri. Kama ni sawa kwako, tafadhali nijulishe ili nizungumze na
mchungaji.’ Tayari wakawa wameshamvuruga Junior.
“Yaani wakati kwangu
ndio panavurugika eti huyu naye ndio anasema amepata kibali kutoka kwa Bwana!
Wanataka kunizidi mahesabu, hakuna bwana yeyote hapa. Ester ndiye aliyemwambia
huu ndio wakati wa kumtongoza Emelda.” Akabaki akiwaza. Akajitumia na huo
ujumbe na kumtizama Emelda. Ametulia kimya.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Kwa hiyo unaamua
nini juu ya Edwin?” “Hata sijui!” Kwa hakika hilo halikuwa jibu sahihi kabisa.
“Emelda! Kwamba hujui chakufanya na Edwin!?” “Tafadhali nishauri Junior. Sijui
cha kufanya.” “Katika lipi? Maana ni kama uliniambia umenichagua mimi!”
“Na ndivyo ilivyo!” “Sasa mbona tena hujui chakufanya?!” “Namjua ninayemtaka.
Ila sijui jinsi ya kufanya maana wewe hutaki nizungumze na Edwin. Sijui
atajuaje msimamo wangu kama hatanisikia mimi mwenyewe! Maana kama ulivyosema,
hatujui Ester alipokuwa akipokea vitu kutoka kwake alikuwa akimwambia
nini!” Akatulia akifikiria. Ila na huo ujumbe pia akamtumia na Ezra.
~~~~~~~~~~~~~~~
Baada ya muda Ezra na
Jelini wakarudi hapo, Jelini akiwa ametulia furaha, zote kama aliyetoka
kubembelezwa na huyo Ezra. Wakakaa ila moja kwa moja akawasoma usoni akajua
hawapo sawa. “Naomba mnisikilize Junior na Emelda.” Wote wakamwangalia. “Kwanza
Emelda pole sana. Hukustahili maneno kama haya. Na mimi bila hata kufikiria
mara mbili siamini chochote ulichotuhumiwa hapa.” “Unajuaje kaka yangu?”
Akauliza Emelda kwa upole.
“Kwanza mimi si
kaka yako tena. Labda uwe unamkataa Junior.” Wakacheka. “Mimi natamani kubaki
naye. Na ndiyo yalikuwa maombi yangu.” “Basi turudi kwenye swali lako kwamba
mimi nimejuaje! Kila chakula ulichokuwa ukipika na kukiacha kwa Junior, jua na
mimi nimekuwa nikila naye mpaka chai na juisi.” “Lakini kweli.” Junior
akaafiki.
“Hakuna ulichopika
kwa Junior, mimi sijala. Kwa sababu kwanza kila mlo uliokuwa ukileta kwa Junior
ulikuwa ukitupunguzia shuguli ya kupika au kununua chakula. Mpaka juisi
tulikuwa tukigawana na chai vilevile. Sasa kama kweli kulikuwa na uchawi,
mbona na mimi sinitake kukuoa.” Bwana Jelini alicheka, kama mazuri.
“Si umeona? Ni jambo
la kufikiria kwa haraka tu. Wote sisi sasahivi tungekuwa tukikung’ang’ania,
kama kungekuwa kuna uchawi kwenye chakula chako. Halafu kingine, kweli huyu Mungu
tunayemtumikia kweli aweze kutuponya na mabaya yote kasoro uchawi
wako tu!? Yaani uchawi uwe na nguvu dhidi ya nguvu za Mungu, kweli!? Au
ndio kusema hata huyu Ester anatuona na sisi hatuna Mungu! Kwani bibilia
inasemaje?” “Hata mkila vitu vya kufisha, havita
wadhuru.” Akajibu Junior kwa haraka.
“Sawasawa. ‘Aliye ndani yetu ni mkuu kuliko wa dunia hii’.
Halafu, ‘hakuna silaha itakayonyanyuka juu yetu
ikafanikiwa’. Hizo zetu ni ahadi zetu sisi wana wa Mungu.
Inawezekanaje zishindwe kutimia kwetu sisi tu, mimi na Junior halafu,
zikatimie kwa wengine?” “Si kweli.” Akajibu Junior.
“Haya yote nakutaka
wewe Emelda uyafikirie na ndipo ujue, shetani NI KAMA, na wala SI. ‘Ni kama’
simba AUNGURUMAYE. Ni kelele tu. Hana meno ya kula. Anapiga kelele tu,
kukutisha uone kuna jambo zito linaendelea. Ufikiri nyumbani wote ndivyo
watakavyoanza kukuona na mengine mengi, kukutisha tu. Lakini sio
kweli.”
Ezra akaendelea. “Leo
sisi tulikwenda ofisini kwa wazazi kuomba malazi ya mama yako na Mateo.
Hatukwenda kugombana! Na japokuwa habari yako ilishajulikana kabla ya leo, tuliwakuta
wazazi wapo sawa wakiweka mipango yao kwa amani kabisa. Sisi tulitaka Ester
apigiwe ili aseme ukweli mbele ya mchungaji juu ya msimamo wako tokea
mwanzo juu yako na Edwin. Basi. Hapakuwa na jambo la tofauti. Kilichoendelea
baada ya pale ni juu ya Ester, wewe hauusiki. Umenielewa Emelda?” Emelda
akatulia kwa muda.
Wote kimya
wakimwangalia. Mwishoe akaongea kama anayefikiria. “Hata sijui chakufanya!
Nisingependa mama aje kwenye mazingira kama haya!” “Tafadhali niamini
nikikwambia kuwa, hii ni kelele tu ya simba. Wala wazazi hawakuchukulii
hivi. Simba anataka kukutisha tu. Ni mama mwenyewe ndiye ameomba mama
yako afikie pale. Tafadhali usikubali kutishwa na kelele za simba. Hilo ni
moja.”
“La pili, Junior na
Emelda, kuna vita zingine tunashinda kwa kutojibu mashambulizi kabisa. Kunyamaza
kimya. Maana wakati mwingine, unapojibu mashambulizi unakuwa unampa adui
mambo mawili. Anagundua kule ulikojificha, maana ataona kule mshale au
risasi ilipotokea. Kwa hiyo atajua eneo ulipo na kuweza kufanya mashambulizi
kwa urahisi. Na ndipo atajua hata aina ya silaha unayotumia. Inamsadiaa
kujipanga na kutumia silaha yenye nguvu zaidi.”
“Lakini mtakapotulia
mlipo sasahivi. Ila mkiwa mmenia mamoja, mnammaliza kwa urahisi sana.
Hatajua mlipo wala mnachofikiria. Hatajua mnatumia silaha gani. Atabaki akipiga
kelele mpaka anajikuta anachoka na kunyamaza. Nyamazeni kimya.” Hapo hata
Emelda akajisikia kutulia.
“Japokuwa Ezra
amenisimulia kwa kifupi tu. Lakini poleni.” Akaongea Jelini na kuendelea. “Mimi
hapo alipo Emelda nilipita. Nilimsimulia Ezra. Kumbe haya mambo hayana kanisani
wala mtaani! Shetani ni mvurugaji popote anapopata nafasi. Lakini uzuri
wako wewe Emelda, umezungukwa na watu wawili wa muhimu sana. Junior mwenyewe
anaonekana anakupenda kwa dhati na ana msimamo. Halafu unaye Ezra
ambaye tayari ni mtetezi wako anayejua ukweli. Mimi ningekuwa wewe, nisingeogopa
wala kukimbia. Ningesimama kama alivyosema Ezra. Amekushauri vizuri
sana.”
“Na ujue wazi kabisa,
hata ukikimbia sio kwamba huko utakapokimbilia utakuta shwari! Unaweza ukaona
hapa maji marefu, ukakimbilia kwa Edwin ndio ukakutana na familia yake wote
hawakupendi! Unaishia kupendwa na Ester tu ambaye wala si ndugu wa Edwin na
Edwin mwenyewe.” Yaani gafla chati ya Emelda ikapandishwa.
“Mimi nataka kubaki
na Junior. Wala si jambo nalifikiria. Nilishaamua. Ila sema niliingiwa hofu
nikidhani aliyosema Ester, hawa wawili wanaweza kuyaamini. Zaidi kuwawekea vitu
vibaya kwenye chakula. Mungu wangu ni shahidi sisi kwetu hatujui uchawi.” “Wala
huhitaji kuapa au kujitetea. Hata kama ungekuwa na uchawi, kwa asilimia 100,
nakuhakikishia usingenipata. Mimi namjua Mungu ninayemtumikia.
Sihitaji ulinzi wa mafuta wala chumwi au maji ya baraka, kulindwa na huyu Yesu.
Kazi iliyofanyika msalabani ni kweli na amina. Maisha
yangu yamefichwa ndani ya Kristo Yesu. Wala uchawi haunitishi
mimi. Kwanza tusipoteze muda hapo. Turudi kwenye swala la msingi.”
“Jelini na Ezra
tunawashukuru kwa kusimama na sisi. Najua tutaomba kabla ya kutoka hapa. Lakini
nafikiri swala la kutulia, mimi naafikiana na Ezra. Usimjibu kitu Ester,
na najua anajua huu ujumbe naweza nisione kwa vile anavyokujua umsiri au
mtulivu hutaki ugomvi. Na mimi sitamtafuta kwa hili wala chochote kati
yetu. Tunyamaze tu tukijipanga na yetu.”
“Niwaulize swali?”
Jelini akaingilia. “Karibu.” “Kwani wewe Junior ulipanga kuoa lini?” Akashangaa
Ezra na Junior wanaangaliana. Kisha kucheka. “Nini? Au pia kuoa mnataka muoe
siku moja?” Jelini akauliza kwa utani asijue ndio maombi yao hao.
Alipowatizama akapata
jibu. “Jamani nyie haiwezekani! Kwamba mnataka muoe siku moja pia!?”
“Kama mtakubali lakini. Katika hili hatutakuwa wabinafsi tukijua ni siku yenu
na nyinyi. Ila sisi tuliomba tusimamiane harusi zetu na iwe siku moja,
mchungaji mmoja. Baba. Tunaenda honeymoon pamoja.” Hao warembo wawili
wakabaki wamewakodolea macho. Junior na mwenzie mbavu zao! Cheko.
“Mjue nyinyi
mnashangaza sana!” “Tunajua.” Wote wakajibu kwa pamoja. Emelda akacheka.
“Tuanze na Jelini, wewe una ndoto za harusi gani?” Ezra akamuuliza. “Mimi
nataka kuolewa na wewe. Basi.” Wakaangaliana tena. Kisha wakaona
wamuweke sawa, labda hajaelewa. “Labda niulize zaidi maana sisi tuna wasiwasi
na wewe, Jelini. Kwamba wewe hutaona unapokonywa siku yako tukiwa sisi wote
wanne na si nyinyi tu wawili? Kwamba watu wote wawaangalie tu nyinyi siku nzima
sio tena iwe na sisi pia? Mimi na Emelda?!” Jelini akatulia akifikiria.
“Pana ukweli. Lakini
niwaambie, tunaweza fanya ikawa kitu cha kupendeza sana, tukaweka historia
nzuri.” Hao wawili walifurahi mpaka kushangilia. “Sasa wewe umepita. Emelda
je?” “Ila mimi siamini! Pengine ndio maana mnafanikiwa sana!
Kwamba kweli haya yote yanayoendelea kati yangu na Junior kweli hamjali
tena?!” “Yapi!?” Wote wakauliza kwa pamoja na Ezra kuendelea.
“Ester anaendelea na
ndoa yake. Edwin si atakayekuwa mumeo. Sisi ndio tumeshika hatima
yetu. Hatuna mwanya wa kuyumba. Umenielewa Emelda?” “Ndiyo.” “Ukiyumba
tu sasahivi, ujue umetukwamisha sisi wote watatu. Kuanzia sasahivi sisi
tunasimama kama tulivyo, dhidi ya kila silaha au ulimwengu. Huna
utakapopita sisi tusisimame na wewe. Usiogope. Na kama umetishwa
na hili, basi simamia miguu yetu, sisi tutakubeba. Tulia na usijibu
kitu.” “Ila kesho nitakuwa nikihudumu na Edwin. Nitamjibu nini?” Wote
wakamwangalia Junior. Akabaki kimya.
“Kwani nyinyi
mlipanga uchumba wenu mtangaze lini?” Ikabidi Jelini aulize. Simu ya Emelda
ikaanza kuita. Alikuwa Mika. “Mama atakua ameamka. Acha nisogee pembeni
nizungumze naye.” “Sawa.” Junior akajibu. Alipoondoka tu, Junior akajibu. “Baada
ya uchumba wenu nyinyi ndio nilitaka kumvalisha pete.” Akajibu Junior macho kwa
Emelda aliyekuwa akizungumza huku akiondoka hapo.
“Kungekuwa na pete,
eti mimi ningeshauri msivute zaidi ya hapa. Sababu kwa jinsi nilivyosoma ujumbe
wa Ester, huwezi jua amezungumza nini tena na Hope na kumfanya arudi
kinyumenyume, akaanza kulalamika na kutibua hali ya hewa pale kanisani. Pili
tungekuwa tukimjibu Edwin na kumnyima sababu ya kukaa tena na Emelda.”
Wakaangaliana.
“Kwamba wewe
usingejali na kesho pia siku yetu ya kutangazwa uchumba na wao watangaziwe?!”
“Hata kidogo! Nyinyi hamfikiri kama ndio itapendeza zaidi?
Tunaanza safari yetu pamoja!” Walifurahi hao wawili wakashindwa kuamini utayari
wa Jelini waliyekuwa na wasiwasi naye sana.
“Kwa hakika
nimefurahia utayari wako Jelini. Lakini naomba
nimfanyie Emelda na yeye surprise. Amenisubiri kwa shida sana,
tena nikimpuuza. Naombeni katika hili nimtendee haki. Edwin
asiniharakishe nikamnyima kitu kizuri. Tuache kesho iwe siku yenu. Mama
anaandaa tafrija nzuri sana kwa ajili yenu nyinyi wawili. Acha kesho iwe
kwa ajili yenu tu. Mimi nikamchukue mama yake. Nizungumze na Mika,
ambaye ni kama anayeongoza mambo ya kwao na mama yao, ndipo nimchumbie. Au
mnasemaje? Tusiwe tunamuharakisha kwenye hili.”
“Halafu pia, acha
watu wajue kama uchumba wangu na Hope umeisha, kabla sijaanzisha
jingine. Lasivyo hichi anachozungumza Ester usije geuka mtazamo wa kila
mtu. Wakamchukia Emelda wakati maamuzi ni yangu mwenyewe.” “Sio wazo baya.”
Akaafiki Ezra.
“Na kesho akikutana
na Edwin?” Jelini akauliza tena. “Hakika hatatoka na Emelda. Hapo hapana.
Tafadhali fikiria njia ingine Ezra. Lakini sitaki Emelda ampe masikio yake.
Nataka abakie kunisikia mimi tu.” “Hata hivyo kesho kuna shuguli nyumbani.
Hawawezi kutoka kwenda kokote. Baada ya ibada watu walioalikwa watakaribishwa
nyumbani. Hawawezi kutoka.” Hapo akamtuliza Junior ila ukabaki wivu.
Hawa wawili
wanatumika kanisani pamoja. Upande wa madarasa ya watoto. Inamaana hata kama
hawatatoka, lakini watakuwa pamoja kabla, wakati na baada
ya ibada, tena peke yao, huko kwenye madarasa ya watoto! Akabaki akiwaza
Junior ambaye hajawahi kujihusisha hata mara moja na huduma ya watoto.
~~~~~~~~~~~~~~~
Emelda akarudi. “Mama
anataka kukusalimia na kukushukuru.” Junior akapokea simu kwa heshima huyo, mpaka
akamshangaza Emelda. Junior kama apige goti! “Shikamoo
mama.” Akasikia sauti kama ya Emelda ila ya kiutuuzima kidogo ikiitika
upande wa pili. “Nilikuwa kwenye shida. Nashukuru
kunitoa.” Junior akaumia.
“Karibu mama na poleni
sana.” “Asante. Ila mguu umetulia kidogo, msiwe na wasiwasi. Msisumbuke. Usije
acha kazi kwa ajili hii. Mimi nitapona tu.” “Hiyo nafuu unayosikia ni ya muda
sababu ya dawa za kupunguza maumivu. Lazima kutafuta suluhu ya kudumu. Na
hutusumbui kabisa. Hata hivyo na sisi tulitaka kuja kukuona.” “Kama ni hivyo
sawa. Karibuni sana.” “Asante. Tunashukuru.” Kimya.
Huyo mama kumbe akawa
ameshamaliza. Akamtizama Emelda. Akamcheka. “Ujue hapo ameshamaliza. Tena
ameongea sana. Acha tu nimuage.” “Basi muwe na
usiku mwema huko.” Akashangaa anaitika kwamba alikuwepo ila kweli hana
tena cha kuzungumza. Ikabidi tu arudishe simu kwa Emelda. Akaondoka pale.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Mbona nimesikia
safari mimi sijui!” Akalalamika Jelini. Ezra na Junior wakaangaliana. “Mimi
nimetengwa!” Akalalamika kwa unyonge. “Hapana mpenzi wangu. Kwanza nikuombe
msamaha na nikwambie jinsi ilivyo. Maana haya yametokea mimi mwenyewe nikiwa
ukumbini leo tukifunga lile kochi.” Wakamsimulia mwanzo mpaka mwisho. “Kama
kungekuwa na uwezo na mimi ningeenda. Nataka kwenda na wewe Ezra.” Alivyoongea
mpaka Ezra akajikuta anampa kiss ya juu ya mdomo.
Kisha akamuuliza.
“Ukizungumzia uwezo unamaanisha nini?” “Usafiri. Maaana kama mtakuwa nyinyi
watatu, na wao wawili si gari imejaa!” “Safari ndefu kama hiyo huwa
tunatumia gari kubwa ambayo inauwezo wa kubeba watu 8 na mizigo. Zikiwa
za milimani inatulazimu kutumia Range ile yenye gia nzito. Hizi
za karibu tukiwa tu sisi ndio tunatumia gari ya kawaida.” “Kwamba
inabidi mkodi kwa safari?!” Ndio akakumbuka Jelini bado hajawafahamu vizuri.
Ikabidi amueleze. “Katikati
ya nyumba yangu na Junior ndipo tunaegesha magari yote.” Jelini akapatwa na
ububu wa gafla. Akameza mate. “Kwa hiyo kama shida ni usafiri, hilo usitie
shaka.” Junior akamalizia. “Ila swala la kazi Jelini?” Akamrudisha kwenye
kushangazwa na hao vijana wawili. Walionekana wa kawaida mno. Siku nzima
wakifunga viti vyake huko ukumbini. Wamesoma na shahada mbilimbili, kisha
wanaajira ya kueleweka. Tena ajira ya muda mrefu! Ila wakafanikiwa kujishusha,
mali zao zikawa ni msaada tu kuwafanya waishi na watu kwa ukarimu! Akazidi kuvutiwa
nao.
Akarudisha akili
hapo. “Siku zangu ninazohitajika sana ni kama leo. Mengineyo hata mama
anaweza nifanyia. Ningependa kwenda na mimi.” “Basi acha tukaangalie jumatatu
kazini. Tukiweza tutoke na kurudi kabla ya jumamosi.” “Hata hivyo hatutakaa.
Tunakwenda kuwachukua na kugeuza. Tutakuwa tukipokezana kuendesha.” “Kama ndio
hivyo naenda kuzungumza na mama. Akionyesha hamna shida, na mimi nitaongozana
na nyinyi.” Mipango ikazidi kukaa sawa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Juma hilo moja tu likajawa na mengi mno. Kuna waliopata na
kukosa. Kuna walio dhania ni vyao, wakijua ni majibu ya
maombi yao, wakatunza kwasiri, kumbe sivyo! Kuna waliojibiwa maombi yao waliyosubiri kwa muda mrefu, wakajua
wamejibiwa. Kuna
ambao walishajibiwa ila kushindwa kutunza muujiza wao. Kuna waliojibiwa wasijue kama walishajibiwa,
wakabaki kusubiria. Kuna waliojibiwa, wakapokea
na kushindwa kutuliza macho kwenye miujiza yao wakaweka macho yao
kwengine. Halafu kuna waliojua wamejibiwa, wakapokea, na kutunza waking’ang’ania.
0 Comments:
Post a Comment