Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com MAPENZI & PESA - PART 3 - SEHEMU YA 39. - Naomi Simulizi

MAPENZI & PESA - PART 3 - SEHEMU YA 39.

 

“Ndiyo.” Mzee akaweka msisitizo alipoona wameshangaa. “Yupo kwenye maombi na ameshirikisha wazee wawili na mimi pia. Wakati wewe upo na Hope, mwenzio alikuwa akimwamini Mungu kwa ajili ya Emelda. Leo unataka kumtoa Emelda kwenye njia sahihi, kisha na yeye ukamuache?” Mzee akauliza kwa ukali kidogo.

     Edwin anamfahamu Emelda kwa kufanya naye kazi kwa karibu sana. Wakati wewe ukiwa na Hope, Edwin alikuwa akitumika na Emelda. Amemuona kwa muda mrefu tu wewe ukiwa umemfungia macho huyu binti! Sasahivi unarudi kinyumenyume ukimtaka Emelda ambaye alikuwepo na hajawahi kubadilika! Si sawa kwako, Edwin ambaye naye ni kijana wa pale kanisani na aliyemuwahi Emelda tokea mwanzo na kushirikisha wazee tumuombee na Emelda mwenyewe.”

“Acha nikuulize kitu baba.” “ Uliza tu maana hapa hatugombani na safari hii naomba Ezra usiingilie kabisa ili tumsikie Junior mwenyewe.” Kimya. “ Umenielewa Ezra?” “ Ndiyo baba.” “Haya uliza Junior.”

“Katika nyinyi mnayemuombea Edwin au Edwin mwenyewe, kuna ambaye alishazungumza na Emelda kujua anachotaka?” “Hapo sina uhakika ila najua wapo sehemu nzuri tu. Na Edwin anajiandaa kumchumbia.” “Basi acha nikupe uhakika. Edwin alimtuma Ester kwa Emelda, na Emelda alishamwambia hamtaki Edwin. Mpigie simu Ester kuthibitisha.” “Ester yupo mapumzikoni na mumewe, siwezi kufanya hivyo.” “Mapumziko yao yameisha jana. Na kesho watakuwepo kanisani kwa sababu jumatatu wanatakiwa kazini. Tafadhali mpigie simu muulize ujue alichomjibu Emelda hata kabla mimi sija mchanganya kama unavyodhania na naomba umuulize ni nani anapendwa na Emelda?” Mzee akatulia.

“Najua upo radhi ukosane na mimi kuliko kumsumbua Ester, japo niswali dogo tu ambalo hutachukua muda mrefu.” “Unaanza lawama Junior!” “Ni kweli baba. Hapo hutaki kumsumbua tu Ester.” Mama yao kimya.

“Mimi ninachokuonya ni uwe muangalifu Junior.” “Hapana baba. Unataka kumaliza kesi ili usimwingize Ester. Ila ujue nina kesi naye kubwa sana na safari hii hutaweza kumkingia kifua kwa sababu umeonyesha upendeleo wa waziwazi, na kushindwa kuwa upande wangu.” “Huu upande niliopo mpaka sasa ni wako Junior. Na ndio maana unaona imenibidi kuzungumza na wewe.” “Kama kweli upo upande wangu basi uwe unajua ukweli wote wa huu upande niliopo. Haitajalisha kwangu kama utaupenda au la, ila ujue ukweli. Na hutajua ukweli bila kumsikia Ester mtu unayempenda na kumuamini. Tafadhali mpigie baba.”

Akamwangalia mkewe, kimya akimtizama. Ezra akabaki akimtizama kama anayesubiria kuona atafanya nini. Na ukimya ule wa mkewe, akaona apige. Ester akapokea kwa haraka. “Nilitaka kukupigia leo baba yangu. Nishakuwa na hamu na wewe. Shikamoo.” “Marahaba mama. Umekuwa na wakati mzuri?” “Sana. Na nimekuletea zawadi.” Huwa akifika kwa huyo binti, hawezi jisaidia. Gafla akajawa furaha kama sio yeye. Akacheka kabisa kwa wazi, wote pale wakamtolea macho wakimshangaa. Akajirudi.

“Asante mama. Sasa hapa nipo na mama yako, Ezra na Junior. Tuna swali.” “ Wewe ndiye mwenye swali.” Junior akamrekebisha. “Sawa. Nina swali juu ya Edwin na Emelda. Unajua chochote juu yao?” “Kuna nini tena?!” Ester akashituka. “Tafadhali jibu swali Ester.” “Mbona kama Junior amenikasirikia mimi bila kosa!?” “Unalo na umenikosea Ester. Ila kwa sasa tafadhali mjibu baba.” “Mimi Ninachojua ni Edwin anaamini Emelda ni mkewe. Anaamini hivyo hata ofisini haachi kumzungumzia Emelda na sifa zake.”

“Hakukutuma wewe ukamtongozee kwa Emelda?!” Junior akauliza. “Ndiyo na Hapana.” “Acha kunichezea akili Ester maana huu sio wakati wake.” “Mbona mimi sina kosa!? Hata baba anajua kama Edwin anampenda Ester! Tena hata Noah anajua. Ni wewe peke yako ndiye uliyekuwa hujui kwa sababu ulikuwa ukimpuuza Emelda upo na mchumb...” “Ester!” “Kwani uongo? Nimekuta jumbe zake kibao kwenye simu yako, alizokuwa akikuandikia mchana hadi usiku, na hujawahi mjibu hata mara moja. Bisha.

“Na kabla hujapoteza muda wa kuuliza nimejuaje, nimejua kutoka kwenye simu yako wewe mwenyewe nilikuomba siku moja nimpigie simu baba anifuate kwako. Simu yangu iliishiwa chaji.” Ester akaendelea akisikika kujitetea tayari wala si kujibu tena swali.

“Wakati nazungumza na baba, ujumbe wa Emelda ukaingia. Nikashangaa sana. Nikasoma kujua anakwambia nini! Na kabla hujakasirika ni kwa nini nilisoma, jua nilikuwa kwenye kumchunguza kwa nini alimkataa mwanaume kama Edwin, japo nilishamwambia anao uwezo, akamkataa nikijua wazi Emelda kwao wana shida, mtu kama Edwin anayempenda kwa dhati na hampuuzi, ANGEMFAA.” Alikuwa akiweka msisitizo kwa makusudi ili kumkumbusha kaka yake.

“Ndio nikaona jumbe zote anazokutumiaga halafu wewe HUJIBU hata moja. Ndio nikaumia sana. Na hata mama anajua hili.” Wote wakamgeukia mama yao. “Japokuwa Emelda aliniomba nisimsemee, lakini nilishindwa. Nilikuwa naumia kuona anaweka mategemeo kwako wewe unayekaribia kuoa, na humwambii mtoto wa watu. Unakula vyakula vyake tu, humjibu chochote. Anabaki na tumaini ambalo linamchelewesha kwenye upendo wa kweli. Edwin anampenda Emelda na anamfuatilia kwa karibu sana. Akiona kitu chochote kizuri, anamnunulia yeye mwenyewe au ananituma mimi nikamnunulie na akaniomba nisiwe namwambia kama vinatoka kwake.” “Ester! Ester!”

“Sasa unakasirika nini!? Wewe hujui kama wanawake wanahitaji matumizi hata nguo za ndani?” Kimya. “Sasa wakati wewe ukihudumiwa na Emelda, humjali, Edwin alikuwa akimfikiria. Mpaka nguo za ndani alikuwa akinituma nimnunulie. Lotion, sabuni nzuri za kuogea na deodorant ilikuwa kazi yake kukumbuka na kununua hata kabla hajaishiwa. Sasa hapo kosa langu mimi ni lipi?”

“Tafadhali turudi kwenye swali la msingi Ester. Ulipomwambia Emelda juu ya Edwin, alijibu nini? Na samahani baba, nimeingilia nikitaka kusaidia turudi kwenye mstari, naona tunapotea, mazungumzo yanavuta na wewe umesema bado unaratiba ndefu ya siku.” “Wala si kupotea. Najua unamtetea Junior kama kawaida yako bila kufikiria. Mnatafuta lawama kwa watu kama nyinyi wote hamkuwepo wakati mlikuwepo, na Emelda alikuwepo akiwahudumia bila hata kumlipa!”

“Na kwa taarifa yenu alikuwa akitumia kihela chake kidogo cha mshahara na vyakula vya mama pale nyumbani kuwalisha nyinyi wenye mihela isiyo na kazi, halafu Edwin anamuhudumia. Sasa kabla hamjamnyooshea mtu kidole mjiangalie nyinyi wawili mliokuwa mkimdharau na kumfanya amsubirie Junior akiamini ipo siku atamuoa.” “Na nitamuoa Emelda.” “Haaaah!” Ester akashituka sana.

“ Japokuwa hutaki kujibu, alikujibu nini, lakini…” “Unaoa mke wa mtu Junior na SIO sawa. Edwin amemsubiria huyo binti wakati wewe ukichumbia wanawake wengine.” “Sikukwambia mimi Junior?” “Baba, Emelda si mke wa Edwin na Ester unajua ukweli. Labda afiche.”

“Mimi sifichi kwa kuwa sina hila. Nilijuaga nimachokita, nikatulia nacho mpaka ndoa.” “Sawa Ester. Wewe mtoto mzuri. Lakini jibu. Emelda alikujibu nini juu ya Edwin? Na mama naomba hakikisha ananijibu.” “Mimi najua alichojibu ila najua nikisema hapa, mtasema namtetea Junior, ndio maana nimenyamaza. Lakini mnavyofanya si sawa!” “Umeenza mama!” “Kwani huyu Emelda yeye ni mtoto mdogo na hana hisia hajui anachokifanya?” Mama mchungaji akauliza kwa ukali kidogo.

“Kama kweli angekuwa mke wa Edwin si angemkubali basi na kuacha kufunga na kuomba kwa ajili ya Junior?” Akauliza. “Nani amekua karibu naye kati ya Junior na Edwin!? Si Edwin? Kutwa yupo naye huko kanisani! Na wewe Ester kutwa kumuuza Edwin kwake! Mbona asimkubali, halafu amekuja kumkubali Junior mara moja tu alipomtongoza?” Kimya.

“Mnataka kumchanganya Junior, na hakika sitawaruhusu.” Hapo akawa mkali kabisa. Mama mchungaji akabadili gia angani. Mbele ya kifungua mimba! Hapo akawabadilikia. “Kwani ilikuwa lazima Junior amtunze Emelda ndipo aje amuoe? Hapana kwakweli!” Akajijibu hapohapo kama ambaye asiyetaka kuingiliwa. “Kama Mungu amemuandikia Emelda, itabaki hivyo. Na naomba muache kumtisha mwanangu. Yeye sio mtu wa kwanza kuvunja uchumba! Watu wanavunja ndoa, ije kuwa uchumba! Mnataka mwanangu aingie kwenye ndoa asiwe na furaha! Hapana kwakweli.”

“Nilijua tu mama atamtetea Junior!” “Tena Ester binti yangu nakuonya mama, usikufuru. Kama yako yamekuendea vizuri, tulia mshukuru Mungu. Wako mabinti kama wewe, wamesubiri na kuishia kuachwa. Mifano unayo. Mmoja wapo ni Ezra huyu hapa tunaye mfano ulio hai. Alitulia kwa yule binti akimwaga pesa kumtunza, mbona aliachwa? Na mbona hamkusema? Leo imekua Junior ndio mnamkaba hawezi kuhema! Wakiachwa wao ni sawa, ila wao wakiacha ndio sio sawa. Acheni kumnyima raha Junior.” Mama akaendelea kama aliyepata jukwaa.

“Wakati wote mmekuwa mkimpongeza ana akili za kufikiria. Kumbe ni wakati akiwafanikishia yenu tu?!” “Mama Junior unafika mbali.” “Kabisa acha nifike. Huyu Junior na mwenzie Ezra mlikuwa mkiimba sifa zao kutwa kwa sababu waliinua huduma pale kanisani kwa juhudi zao. Kifedha ndio sitaki kuhesabu. Kiroho ndio kutwa wapo kwenye maombi wakiombea huduma na hii familia na maisha yao yote wameyatoa kanisani.”

“Na wewe Ester ni mara ngapi huyu Junior amekua akikusaidia wewe na Devin mpaka akasimama? Si huyuhuyu alijitoa mpaka akafanikisha mumeo kupata kazi BOT? Amesimama na nyinyi bila kuchoka akiwatia moyo mpaka mkafanikiwa kuoana, leo unamkejeli mwenzio!”

“Aliona ubora wenu mkiwa chini sana. Akawashika na kuwatia moyo mpaka hivi leo! Tafadhali msije sahau hilo. Na sitaacha kusema japo ni kukufuru, lakini Ester, bila Junior mumeo mpaka leo angekuwa akihangaika mtaani. Bisha, ukamuulize Devin. Kama atakuwa na yeye amesahau tutamkumbusha barua yake ya shukurani kwa Junior na Ezra.”

“Haya, alipo mchumbia rafiki yako na kukufanyia yako yakaenda, mlikuwa mkiimba sifa zake kila mahali! Kweli leo mwanangu anawaomba msimame naye katika hili ambalo kwanza hajuagi kulia shida mwanangu! Katika hili, kwa mara ya kwanza ndio anawafuata, halafu kweli nyinyi ndio mnamchagua Edwin badala ya mwanangu? Kweli!?” Wote kimya.

“Ester ukijua ukweli kabisa juu ya msimamo wa Emelda kwa Edwin, bado unasimama kinyume na kaka yako!? Na nakuonya Ester, usijerudia tena hata siku moja kujifananisha na kaka yako. Mbali ya kwamba amekupita mbali sana, Junior amesimama na wewe tokea mdogo mpaka sasa. Alikuwa akikesha kukufundisha hesabu ulizokuwa huelewi popote baba yako alikokuwa akikupeleka ukafundishwe, lakini alikuwa hachoki kukutia moyo mpaka ukamaliza chuo. Leo unajilinganisha na Junior na kuona umempita wewe! Hakika Mungu akusaidie usijisahau Ester. Acheni kumnyima raha mwanangu!”

“Hee! Imekua nongwa! Sasa na huyo Hope wenu amemuacha. Yupo kwenye uchumba na Emelda. Na hata yeye akiona hafai, basi.” “Mama Junior!” “Hakika katika hili sitataka mtu amchanganye. Akili hiihiii iliyokuwa ikisifiwa kwenye kuendeleza kanisa, kusaidia wengine, ndio nataka iachwe, ifikirie mpaka itoe mke. Msimchanganye.”

“Haya. Tuambie habari njema na mbaya. Na Ester usikate simu ubaki hapohapo na uache kulia. Maana sasahivi zamu yako imepita, waachie na wenzio.” “Zamu yake inapita vipi tena?! Bado ni mmoja wa hii familia na mawazo yake yanatakiwa sana.” “Yeye ameshaolewa, habari iliyobaki kwa sasa ni ya Junior na Ezra. Atulie na awe msaada kwa wenzie kama alivyosaidiwa yeye.”

“Mnaninyanyasa.” Akazidi kulia. “Unakumbushwa ulipotoka, ili usijisahau. Na nakuomba unyamaze Ester sio uzidi kulia ukijua baba yako hatasikiliza hapa, atabaki akikubembeleza wewe. Sio sasahivi. Tulia tumalize kilichomleta Junior na mwenzie hapa ofisini.” “Hakika humtendei haki mtoto! Umemnyanyasa kwa wazi kabisa!” “Naomba hayo tuendelee nayo baadaye. Tunakusikiliza Junior.” “Acha tu mama. Nitatafuta msaada kwengine. Twende Ezra.” Wakasimama.

“Ester, umekosa sana. Na familia huwa haziwi hivyo, na wewe unajua. Huwa tunasimama pamoja wakati wote. Mimi na Junior tumekua kwenye maisha ya kila mmoja wenu bila ya kulalamika wala kuchoka. Tumejitoa kwa hali, mali mpaka kuwasaidia kufunga na kuomba hata kwenye yale magumu yaliyokuwa yakionekana hayawezekani kwa macho. Leo mnashindwa kusimama na sisi katika hili ambalo Junior ametoa sababu za wazi tu!” Ezra akaendelea.

“Mlitaka aoe halafu yeye ndio akateseke wakati wengine wakipata sifa!? Kwa wazazi kwa sababu wameozesha kijana wao. Na kwako wewe Ester kwa sababu rafiki yako uliyemuunganishia kwa kaka yako, ameolewa bila shida. Ndivyo mlivyotaka itokee ili Junior abakie kama mlivyozoea nyinyi, kwamba abakie wakati wote akilipa garama ya furaha yenu!? Binafsi sikutegemea! Nilitegemea tofauti. Sidai, lakini nilidhania kipindi cha shida yetu na nyinyi mtasimama na sisi! Lakini mnachagua watu baki kabisa! Si sawa. Twende Junior. Nitampigia simu mama Jema nimuombe yeye msaada.” Wakatoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~

INAENDELEA…

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment