Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 28. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 28.

Akaona ampigie tu. “Samahani sana Ezra, nasikitika imeshindikana. Mama ameomba tusubiri mpaka mambo yakae sawa. Kuna makosa yalishatokea hapo nyuma, na mimi nilihusika kwenye kuchangia, ikamuacha Jeremy kwenye maswali yaliyoshindwa kujibika kifasaha. Na Jeremy anaakili sana. Huwezi kumpa majibu ya rejareja. Sasa inakua ngumu kwa mama kuamini tena mtu au watu. Ni matendo tu ndio yatamfanya aamini tena mtu na Jeremy. Samahani sana.’ “Usijali kabisa. Hata mimi naelewa. Uwe na mchana mwema, dada.” “Asante. Na kwenu pia, msalimie Junior.” “Atasikia.” Simu ikakatwa. Hapo akakwama. Akatulia akifikiria maandalizi gani mazuri na ya kuvutia ya kumkaribisha Jelini nyumbani kwa mara ya kwanza. Ila majukumu ya kiofisi yakamchukua tena.

Kwa Mara ya kwanza Jelini nyumbani kwa Ezra.

Alimrudisha nyumbani mtoto mapema tu. Akaanza maandalizi ya kwenda kwa Ezra. Kama kawaida yake, hakuna makosa kwenye mwili wake. Akajitengeneza vizuri mpaka akaridhika. Ndipo akampigia simu kumwambia yupo njiani kwenda. “Nitakuwa na wewe kwenye simu, ili usipotee.” “Nashukuru.” Akamuelekeza mpaka akafika kwa Junior. “Sasa kuwa kama unazunguka ukuta wa Junior kwa mbele. Nyumba zimepakana kabisa.” Jelini akacheka. “Nyinyi wawili sijawapatia mfano wenu!” Ezra akacheka akitoka ndani ili kumsubiria.

Kampuni ya ulinzi inayolinda kwa Junior ndio hiyohiyo akakuta sare zao hapo getini kama alivyokuta kwa Junior, ila wamemfungulia geti kabisa kama waliokuwa wakimsubiria yeye. Jelini mwenyewe akacheka akiwatafakari mapacha hao wa nje. Akasalimia hapo getini na kuvuta gari ndani. Akamuona kwa mbali kwenye ngazi za kuingilia ndani kama anayemsubiria.

    Akasogeza gari mpaka karibu yake, akaenda kumfungulia mlango na kubaki akimtizama. “Mpaka naona vibaya kukugusa Jelini!” “Kwa nini tena?!” “Jinsi ulivyopendeza na kuvutia! Unaonekana wa thamani sana. Mpaka nahisi nikikugusa nitakuchafua!” “Basi ujue nakutengenezea kitu kizuri chakushika. Wewe hustahili kushika vitu vibaya. Vizuri tu. Ndio maana.”  Akamdaka kwa uchu wote. Likawa kiss la msamaha, karibu nyumbani, na nashukuru kunipenda. Kiss kilo likavuta kwa muda wake wakutoshea tu, ndipo akamuachia.

“Nimefurahi umetenga muda kwa ajili yetu.” “Na mimi nimefurahi umenikaribisha kwako.” “Karibu sana.” Akamshika mkono kumuongoza ndani.

    Kila kitu, kuanzia nje mpaka kitasa kweli ilikuwa kama kwa Junior. Utafikiri upo nyumbani kwa Junior! Jelini akaanza kucheka alipoingia ndani. “Ni nini?” “Mimi uliponiambia nyumba zenu zinafanana, nikajiambia pengine thamani za ndani, labda makochi ni tofauti. Kwamba nyinyi mpaka makochi vinafanana!” Ezra akaanza kucheka.

“Imekua kama kasumba. Junior akinunua kitu, au mimi, hata wazazi imekua hivyohivyo, lazima kununua viwili. Wakijua kimoja changu na kingine Junior. Huna kitu utaona humu ndani, kisiwepo kwa Junior. Zaidi vitu vikubwa. Na vyombo.” Akafikiria. “Na baadhi chumbani. Maana mama huwa anapenda sana mashuka. Kwa hiyo yeye ndiye mleta mashuka.” Akafikiria zaidi. “Hata mapazia na..” “Mimi nahisi ni kila kitu.” Ezra hana mbavu.

    “Karibu. Hapa ndio nyumbani.” “Asante. Ila nyinyi hamfananii na uhalisia wenu, kabisa! Kuna nyumba nilishaingia. Nikaishangaa nikidhani ndio nyumba nzuri ya mwisho nitakuja ingia hapa mjini, ila nimekutana na hizi zenu, nimewanyanyulia mikono! Hongera Ezra.” “Asante. Sasa twende nikupe tour. Upafahamu vizuri.” Akamzungusha humo ndani, Jelini mwenyewe akapakubali.

    Kisha akamrudisha sebuleni akiwa amemshika mkono na kumuongoza kwenye kochi. Yakaanza tena makiss mengine, maana alishamuona Jelini amebabaika mpaka akajuta kumzungusha humo ndani. Alimkiss kwa kumkumbatia kwa muda mrefu mpaka akasikia sauti ya Junior ikimuonya. “Usije zidisha.” Ezra akaanza kumuachia taratibu maana ni kweli alikuwa anaanza kuzidisha. Na alivyo Jelini, alishalegea hapo mikononi mwake. Akawa anamalizia taratibu juu ya midomo, mpaka wakatulia.

    Akabaki akimwangalia na kumwambia kwa upendo kama anayebembeleza. “Naomba zawadi yangu.” Jelini akacheka akijitoa hapo mikononi, ila alijawa wasiwasi sana. “Naamini utapenda.” Akavuta pochi yake na kutoa vimfuko viwili, vilivyofungwa vizuri. Ezra akabaki kusubiria kwa hamu. Akamkabidhi vyote. “Kila moja ina herufi ya majina yenu.” Akamkabidhi kama aliyemaliza. Ezra akapokea akijua anaficha hiyo ingine.

Akafungua na kukutana na cufflinks nzuri sana, maalumu kwa mashati yasiyo na vifungo vya mikono. Wenye umaridadi hununua mashati hayo maalumu na kuweka hizo cufflinks zinazoongeza umaridadi. “Ni nzuri sana. Na zinaonekana zimekugarimu, maana na mimi huwa napenda sana kununua. Asante Jelini.” “Karibu. Nimefurahi kama umependa na kama zitawafaa.” Ezra akabaki kuziangalia akizegeuzageuza kwa kuvutiwa nazo ila akitafuta jinsi ya kudai ingine.

    Akamwangalia akakuta ametulia tu. “Asante.” “Karibu.” Akacheka kwa wasiwasi kama anayejaribu kujituliza. “Nasubiria zawadi yangu ile uliniambia ungenipa kama si kukuudhi.” “Hapana. Sio kuniudhi. Ila sitaki unielewe vibaya. Ukadhani labda nakurupuka. Au kwa kuwa nimekuona upo vizuri, nyumba yako nzuri, halafu nikawa nimeshasema sijawahi ishi gorofani, ndio maana nataka kukufunga. Sikuwa nimefikiria vizuri. Ndio maana naona hiyo ifae tu. Nisiwe kama wale wanawake wanaolazimishia mambo kwa wanaume ili wajinufaishe wao tu.” Akaongea sana akijitetea kwa hofu.

    “Kama ningekuwa kama ulivyonifikiria. Kwamba mimi ni mission town. Siishi kwenye mazingira kama haya, ungenipa na kuniambia nini?” Jinsi alivyouliza kwa kutulia bila paniki, ikamfanya Jelini atulie. Akavuta pochi yake. Akatoa kimkebe kama kilichotoka kwa sonara. Akakishika kwa mikono yake yote miwili, ila akaonekana kama anatetemeka. Ezra akafikiri pengine ni pete. “Sasa itakuwa ya ndoa! Maana wanawake hawachumbii!” Akajiuliza akiangalia kile kimkebe kizuri tu chakuvutia kwa macho.

    Kisha akamtizama na yeye, akagundua anajishauri. Akahisi anatafuta jinsi ya kubadili alichotaka kumwambia. “Tafadhali usibadili kitu cha kwanza ulichokusudia kuniambia wakati ukinipa. Usirekebishe wala kutengeneza. Niambie vile ulivyokusudia mwanzo. Na nakuahidi kwangu upo salama.” Akamuona kama anatulia.

    “Nilitengeneza cheni yenye majina yetu.” Ezra akatoa macho kwa hamasa. “Lakini nilitaka kukuomba ufikirie kwanza kabla hujaivaa. Unaweza kuiweka usiivae mpaka ukawa tayari na ombi langu, na ukishindwa unaweza nirudishia tu, usivae.” Akaendela taratibu akijihami. “Nilitaka kukuomba kama unaona nafasi kati yetu ya mpaka uzee wetu, ndio uvae.” Akamtizama kwa hofu. Alipomuona ametulia, akaendelea. “Na kama utaivaa, basi ilete maana. Kwamba kila ukiiona au ukiikumbuka ipo shingoni kwako, umkumbuke Jelini tu. Na asiwepo mwanamke mwingine unayemfikiria ukijua mimi nipo, ni wako na nakuhitaji wewe. Lakini sio kwamba nataka kukufunga ili…” Ezra akamuwahi midomo kwa kumvamia kwa uchu kama ambaye ameamsha kitu ndani yake.

    Jelini akaanza kucheka akijivutia kwake zaidi akifurahia kwamba hajamfikiria vibaya. Amependa. Akambusu kwa muda wa kutosha. Wakanogewa. Jelini akazidi kujiachia hapo kochini maana hisia zilipitiliza, Ezra naye hisia zikaendelea kupitiliza. Jelini mtamu mikononi bwana! Harufu nzuri na mihemo akipata midomo mitamu sawia, vikamfanya Ezra kuhama kabisa kihisia. Hapo alishasahau amri zote za Mungu, ila penzi la kimwana Jelini.

Uzuri alishaweka ulinzi kwenye maisha yake. Wanalindana hata kiroho, siku hiyo ikasaidia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Simu ya Ezra ikawatoa kwenye hiyo hali. Kwa upande fulani akashukuru sana Mungu. Akamuachia Jelini akihema, na kusimama kuifuata mezani. Alikuwa Junior. Akatulia kwanza ili pumzi zikae sawa, ndipo akapokea. “Nimepata dessert, naweza kuwaletea?” Alijua wazi hilo sio lengo, ila alishukuru sana nafsi mwake.

    Hawa wawili walilindana kiroho tokea wanafahamiana. Kila mmoja akawa mlinzi wa mwenzie. Na kwa kuwa Ezra alishavuka mpaka wa kumkiss Jelini, Junior akaongeza umakini kwake. Hakutaka kosa litokee kwa rafiki yake. Ikawa kama Roho wa Mungu amemshitua Junior kuwahi. Maana Ezra alishafika hatua ambayo, kama Junior angechelewa kidogo tu, pengine wangeharibu. “Aisee nakushukuru sana. Njoo.” Junior akacheka vile alivyoshukuru maana alimuelewa alicho maanisha. Akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    “Junior anatuletea dessert. Kuna sehemu tunapata dessert nzuri sana.” “Afadhali aje nimpe na zawadi yake.” “Kwanza naomba yangu. Nimefurahi Jelini!” “Sasa umefurahia nini? Mwenzio naona ni kama sikufikiria vizuri!” “Nisikilize Jelini. Mimi nimemaliza kwenye swala la kutafuta. Sitarajii kuanzisha mahusiano mengine mbali na wewe, na mimi najijua. Ni kama Junior tu. Hatuna udhaifu kwenye eneo hilo.” “Wanawake?” Jelini akauliza.

    “Tamaa za wanawake au tamaa kwa ujumla wake. Kitu tunachotaka, tunahangaika kukipata kihalali. Na tukishapata, tukajua ni chetu, tunaridhika nacho na kutulia kabisa. Nini nataka kukwambia?” Jelini akajiweka sawa kusikiliza. “Kwenye haya mahusiano yetu, mimi na wewe, mimi binafsi nimemaliza na kufunga kabisa. Sijawahi na sitarajii kukifanya hichi ninachofanya na wewe kwa mwanamke mwingine tena.” Hapo akamchanganya Jelini. Kwamba na mchumba wa kwanza hawakuwa wakikiss! Akajiuliza na kutulia.

    “Kwako imekua tofauti. Nakupenda Jelini.” Ikawa kama anayemjibu mawazo yake. “Na natamani nisije shika mwanamke mwingine tena hivi. Kwa hiyo nikikusikia na wewe unajifunga kwangu kwa kiasi hiki, hujui inanifariji kwa kiasi gani. Inanituliza na kunihakikishia kuwa sijakosea hata kukushika hivi na kuwa wewe ndio mwanamke wangu wa kwanza kukukiss.” Hapo Jelini akatoa macho waziwazi na kumfanya Ezra acheke.

    “Ezra!” “Hukumbuki nilikwambia niliokoka nikiwa kidato cha kwanza, na kumbuka nilitokea kijijini?” “Sasa na mchumba wa kwanza!?” Ezra akafikiria kwa muda akawa kama amekosa jibu. “Labda nikwambie kuwa, hakuwa kama wewe.” Jelini akawa hajaelewa. “Vile unavyomuona Hope, ni kama kwa haiba wanafanana kidogo. Si watu wa kuweka mikononi.” Jelini alicheka. Akacheka mpaka akajifunika na mto.

    “Wewe unapenda mikono, Jelini. Msichana kama Hope ni mipango wakati wote. Mnunue nini na mfanye nini. Au umsaidie nini. Wapo kiuchumi zaidi. Wakati wote mkikaa wanafikiria kitu cha kufanya tofauti na wewe, unamfanya mtu anatulia na kupumzika. Rahisi kufikiria upande mwingine wa mapenzi. Huna mahitaji ya kufanya mtu afikirie kiasi cha pesa cha kukupa.” “Kwani ulikuwa ukimsaidia kifedha?!” Ikamchanganya tena. Maana alisikia hata Hope amesoma na anakazi nzuri. Anasaidiwaje tena!

    “Unafikiri kwa nini nilichanganyikiwa? Maana hata nauli yenyewe ya kwenda huko ni mimi nilimpa. Na pesa ya kuanzia maisha huko pia nilimpa, nikijua nawekeza kwenye ‘chetu’, kama unavyopenda kusema wewe. Sasa kuja kusikia tena amepatikana mwanaume mwingine, mimi tena sipo kwenye picha, ndio kujua kumbe nilikuwa nikijenga kwenye mchanga, na mapenzi ya dhati hayakuwepo tangia mwanzo, nilikuwa nikichezewa tu.” “Pole Ezra.” Mara kengele ikalia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    “Junior huyo!” Akaenda kumfungulia. Akasikia wakinong’ona. “Aisee nakushukuru. Umeniokoa kupita nitakavyokueleza. Hakika ungechelewa, ningeharibu vibaya sana.” Jelini hakuwa akijua au kusikia wanachozungumza. Ila akasikia Junior akicheka sana wakiwa wanamfuata sebuleni.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Akasimama walivyofika pale. “Kama kawaida yako, umependeza.” “Asante Junior. Nimefurahi kukuona. Nikupokee? Boski lenyewe linavutia!” “Na vilivyopo humo ndani vinafurahisha pia. Nilitaka mlo wako wa kwanza hapa, ukamilike na uufurahie.” “Hapa nimeshafurahia! Si tutakula pamoja?” Junior akashangaa, hakutegemea. Akamwangalia Ezra na kusema. “Sitaki kuwaingilia. Huu usiku ni wenu.” “Basi nikwambie, utakuwa unapitwa. Ezra mwenzio ameniandalia chakula kizuri. Na nina zawadi yako nzuri.” Wote wawili wakacheka.

    “Unauhakika Jelini? Sitaki kuwavurugia.” “Kwanza nataka uwe shahidi yangu. Acha nikupokee kwanza, halafu nije nikwambie kitu.” Akampokea. “Asante.” Ezra na Jelini wakashukuru kwa pamoja. “Karibuni sana.” Akamkabidhi hilo boksi lenye dessert, Jelini akawa mwenyeji akikumbuka jikoni. Akapeleka huko, huku akipaangalia mara mbilimbili jinsi palivyo pazuri na kuvutia. Alidhania kwa mzee Kasa ni pazuri, akakutana na vijana hao waliotulia, wanajituma kanisani mpaka kufuta viti halafu sasa ni wa kisasa. Kila kitu hapo ndani kwao ni kizuri na chakuvutia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Wakati anarudi akasikia wakinong’ona tena. Akajichekea nafsini kwake. “Hawa wapo kama watoto!” Akawafikiria akisogelea alipowaacha sebuleni. Akakuta bado wamesimama. “Ezra ameshindwa kukushawishi ubaki?” “Hapahitajiki nguvu nyingi kunishawishi kubaki. Sina chakula cha usiku, kwa hiyo acha tu ni doee kwa watu.” Wakacheka sana jinsi alivyozungumza kama mtoto wa mtaani mtaka kula kwenye majumba ya watu, wakaa.

Shahidi.

    “Mimi shahidi mzuri sana, Jelini.” “Na huruki watu?” Wakacheka sana jinsi alivyouliza. “Sitakuruka.” “Hata ikiwa kati yangu na Ezra?” “Mimi ni mwenye haki wa Mungu. Na Ezra ananijua. Akikosea huwa namwambia waziwazi.” Jelini akacheka. Akatulia kidogo, wakaona anaanza kuogopa.

    “Chochote unachotaka kuniambia mimi, ujue kipo salama Jelini. Usiogope.” “Umejuaje!?” Akauliza akicheka kama anayetaka kujituliza. “Usiogope.” “Haya. Unakumbuka siku ile usiku nilikwambia na mimi nitakuwepo sana kwenye maisha ya Ezra. Nikakuomba na wewe uwe unamkumbusha asiniumize?” Junior akacheka na kujibu. “Nakumbuka.” “Sasa mwenzio ameniahidi nitabaki peke yangu.” Wakacheka sana, kama ambao hawakuwa wametegemea aseme hivyo.

    “Jelini!” “Kweli tena. Na ndivyo ninavyotaka. Ukimuona tu anaanza kumfikiria mtu mwingine, mkumbushe yupo Jelini.” “Japokuwa nina uhakika na Ezra kwa asilimia 100. Kwa kuwa namfahamu na yeye kama ninavyofahamu kiganja changu, kwamba hatatafuta mtu mwingine, na leo nakuibia siri, Ezra anakupenda sana Jelini. Sana.” “Kweli?” Akauliza kwa deko akimtizama Ezra aliyekuwa ametulia akiwasikiliza, kwenye hilo kochi walilokuwa wamekaa pamoja.

    “Nakuhakikishia. Anakupenda kwa asilimia zote utakazotaka kujihakikishia. Anakupenda kwa moyo wake wote. Na nakuhakikishia, kama hutabadilika, jua utabakia peke yako daima.” “Mimi sibadiliki. Ujue nilikuwa nikitamani mtu kama Ezra?” Junior akacheka akimsikiliza.

    “Mtu mwaminifu, halafu nataka nibaki peke yangu.” “Nakuongezea kitu kingine, ujue kwa Ezra utajaliwa sana, na utapendwa kupita utakavyofikiria. Kwa kuwa Ezra anakua akikufikiria wewe tu, wakati wote. Mimi ni shahidi. Usiwe na wasiwasi, na ndipo inapokuja ahadi yangu kuwa, mimi nitakuwa shahidi wako daima. Ila ujue mimi nasimamia haki Jelini. Sitapendelea kati yako au Ezra. Nitakuwa mkweli kwenu. Si naruhusiwa?” “Mimi hivyo ndio nataka.” “Basi umejipatia shahidi.” Akacheka na kufuata tena kile kimkebe.

    “Nilimtengenezea cheni ya majina yetu, kama kumkumbusha ‘sisi’. Sasa sijui ni sawa kwa wadhifa wenu pale kanisani halafu akaonekana amevaa cheni yenye majina yetu?” Akawa tena na wasiwasi akimuuliza Junior. Wawili hao wakaangaliana. “Mimi nafikiri si tatizo. Itakuwa kama pete ya uchumba kwake, watu wajue amejifunga kwako.” Jelini alifurahi huyo!

“Basi ni vile sijawazoea, bado nawaogopa. Ila ingekuwa ni watu wengine, ningesema hivyohivyo kwamba ni kama mimi nakua namchumbia Ezra.” Walicheka mpaka wakacheka. Akajifunika na mto wa makochi. “Jelini!” “Kweli tena. Sema mimi nawaogopa, ndio maana sitasema hivyo.” “Kwamba unamchumbia Ezra?” “Sasa hayo ni maneno gani na wewe Junior, mwanamke kumwambia hivyo mwanaume? Si ndio maana sisemi!” Hawana mbavu.

    “Basi usiseme Jelini. Ibaki tu siri yako. Ibakie kuwa ni kumbukumbu, kumkumbusha kuwa Jelini yupo.” “Mimi naona ibakie tu hivyohivyo. Na ingekua ni kuchumbia, ningemvalisha mwenyewe.” Ezra akacheka zaidi akitingisha kichwa. “Ila nafikiri ukimvalisha ndio italeta maana kabisa.” “Eti eeh!” Eti akafurahia hilo wazo. “Kabisa. Aikumbuke hii siku, ili siku tukimkumbusha akumbuke kwa urahisi. Na mimi nashukua video kabisa, nije niwaonyeshe mpaka watoto wenu.” “Mimi ndio maana nampenda Junior.” Wakazidi kucheka. “Nitakupa zawadi nzuri, tena sana.” “Nashukuru Jelini.” Basi akasimama akitaka kumvalisha ila Ezra akamuwahi.

    “Naomba kwanza niishike mkononi kabla hujanivalisha. Inaonekana nzuri sana na pesa nyingi.” “Sisi tunapenda vitu vizuri sana.” Wakaanza kucheka tena. Junior na yeye akasimama kuiangalia na kuhamaki. “Jelini! Hii cheni umetengeneza wapi!?” “Kwa sonara wangu. Huwa ananijulia sana. Kila kitu ninachomwambia anitengenezee, anatoa kama ninavyotaka na anampenda sana Yesu. Yupo pale Magomeni. Mtu mzuri sana.”

    Ezra akabaki akiitizama, wote kimya macho kwenye hiyo cheni. “Kwanza nzito ya hadhi. Imezungushiwa alama ya moyo iliyokerezwa vizuri sana, ikabeba herufi E iliyobeba J. Nzuri sana inavutia.” Akaithaminisha Junior na yeye akiitizama kwa makini pale mkononi kwa Ezra. “Halafu jinsi ilivyokerezwa kwa ustadi! Haichoshi kuitizama ilivyo. Dhahabu safi tena ya kiwango cha juu. Daaah!” Akasikika Ezra kwa hisia za kutosadiki na kumtizama Junior, akacheka na kurudi kukaa akiweka sawa kamera yake ya simu.

    “Asante Jelini wangu. Nashukuru mpenzi wangu.” Ikawa kama Jelini amewawahi kwenye kuchumbia.  Tena kwa kiwango cha juu. “Nimefurahi kama umependa.” “Mbali na uzuri wake wa kiwango cha juu, maana yake ndio imenifurahisha zaidi. Nashukuru kujifunga kwangu, na nakuahidi nitakuwa mwaminifu kwako Jelini. Nakuhakikishia usiwe na wasiwasi wa mapenzi yangu kwako. Niwahi au nichelewe kupokea simu zako, jua Ezra ni wako tu.” Jelini alicheka kwa aibu.

    “Hata asipokutaarifu yupo njiani kukufuata, ujue popote alipo wewe ndio upo mawazoni.” Junior akaongezea. “Kabisa. Wazo hata lakufiria kama nimekusahau lisiwahi kupita akilini mwako tena. Jua nakufikiria, na safari yoyote niliyopo ujue ni ili kukufikia wewe.” Akatingisha kichwa kukubali kwa kuridhika.

    Akamrudishia hiyo cheni, akajua ndio anampa amavalishe. Basi akazunguka nyuma ya kochi pale alipokaa, akaenda kumvalisha kwa makini. Kisha akaiweka sawa mbele akilaza vizuri zile harufi zao kisha akambusu hapo chingoni kidogo tu, akarudi kukaa pembeni yake. Ezra akamsogelea na kumkumbatia tu. Bila mengi. Junior akichukua video na kuwapiga picha.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Ila hilo tukio lilimmaliza sana Junior. Jelini ni mgeni kabisa kwao, lakini akaweza kujichanganya na kuweka kumbukumbu nzito sana kati yao, halafu ikavutia. Akabaki akijiuliza ni lini Hope amempa zawadi zaidi ya kuomba pesa na misaada mizito! Hakukumbuka. “Halafu hana hata heshima!” Akazidi kujiumiza moyoni, akiangalia zile picha alizowapiga.

    Ezra akamgundua amepotea. Akaelewa anachofikiria. Jelini na wanawake waliokuwa nao, ni mchana na usiku kabisa. Ikawa tena kama Jelini amekwenda kumchongea Hope, ila kumfuta machozi Ezra. Akashukuru hata kuachwa na mchumba wa kwanza. Akamuhurumia Junior akielewa alipo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

     “Usiache kunitumia na mimi.” Akamtoa mawazoni kusudi, na Junior akajua. Akagutuka na kurudi pale kimawazo. “Aisee nzuri sana. Nyinyi wawili mnapendezana mno. Nina ujasiri wa kusema mmebahatika.” Wakacheka kwa furaha, Jelini asijue kinachoendelea. “Asante. Basi tupige na wewe pia Junior. Iwe kumbukumbu yetu.” “Jelini! Hutaki kurukwa baadaye?” Ezra akafanya wacheke. “Acha niweke ushahidi wangu wa baadaye, asije sema hakuwepo.” Basi Junior akategesha kamera. Akategesha. Na kuzunguka nyuma ya kochi, akasimama nyuma yao. Wakapata picha za kutosha tu. Ndipo wakahamia mezani.

    Hao wawili ndio waliiandaa hiyo meza wakisema Jelini mgeni siku ya kwanza. Wakatengeneza utafikiri imeandaliwa na mama yao! Safi kwa ustadi mpaka napkins. Kama mama mchungaji anavyoandaa meza ya chakula nyumbani kwake, kwa wageni wanaofika kuwatembelea. Wakaiga kwa mama yao.  Pakapendeza.

    “Ila hiki chakula sijakipika Jelini. Imebidi kununua. Uliponiambia nirudishe akili kazini, ndipo nikagundua nina mengi sijafanya. Kuja kumaliza, muda ulishakwenda, nikajua nitakuchelewa tena.” “Mimi nataka muda na wewe Ezra. Hivi vyakula vipo tu.” “Ndio maana nakupenda Jelini wangu. Huna makuu.” Wakacheka wakikaa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Wakala kwa pamoja, Junior asiamini kama kweli Jelini ameridhia kujumuika naye usiku huo uliokuwa maalumu kwa ajili yake na Ezra!  Akabaki akimsoma kwa tahadhari, akagundua yupo sawa tu, si kwa kujilazimisha. Tena alionekana kumfurahia na kumshukuru kuwa nao usiku huo. Akimshukuru kuwa kuja kwake na kukubali kuwa nao, kumefanya waweke kumbukumbu yao ya kudumu, kitu kilichozidi kumvutia na kumpenda Jelini, akiona Ezra amebahatika kwelikweli.

    Yaliendelea mazungumzo yaliyojaa vicheko tupu. Wakaweza kufahamiana hao watatu kwa karibu. Maswali mengi na majibu. Junior alipomaliza, akaaga kwenda kupumzika. Lakini hata Ezra alijua ameondoka akiwa si kama alivyoingia hapo. Zawadi ya Jelini imemfanya afikirie yake zaidi.

    Jelini na yeye hakukaa zaidi, akijua kesho yake ni siku ya kazi. Akawa muungwana. Akaondoka bila mengi ila busu tu la mdomoni tena kwa kifupi, akaondoka akiwa amemuachia furaha ya ajabu huyo Ezra. Kila wakati mkono shingoni.

Msingi.

    Wakati anakaribia kupitiwa na usingizi wa furaha, yake na Jelini yamekaa sawa, ujumbe ukaingia. Akadhania ni Jelini, akakwapua simu kwa haraka asije haribu tena. Akakuta ni Hope. ‘Tunaweza kuzungumza?’ Ezra akampigia. Alijua amefanya makusudi mida hiyo akijua hata kama wanafuatana vipi na Junior, mida hiyo Ezra atakuwa peke yake akipumzika kwa kazi kesho yake.

    “Upo mzima?” Akaanza Ezra. “Nimeharibu Ezra, na sijui jinsi ya kurekebisha.” Akaanza, Ezra kimya. “Ni kama niliyejifunga kwenye kamba mara nyingi, sijui najitoaje! Naomba msaada wako tafadhali.” “Wakufanya nini?” Akamuuliza taratibu tu kama kawaida yake, hana papara. Mtulivu.

    “Nisaidie kurekebisha. Najua unajua kinachoendelea. Nimeharibu. Sijui nitafanya nini.” “Unajirudiarudia Hope. Bado sijajua unataka mimi nifanye nini!” Akaanza kulia. Akalia hapo kwa muda, Ezra kimya. “Najua na wewe nimekukosea Ezra. Nimemtenda ubaya Jelini. Nafikiri kuanzia hapo ndipo nilipoendelea kuharibu.” “Maadamu umemtaja, naomba tuanzie kwake. Unatatizo gani na Jelini? Na kuwa huru tu kuniambia chochote kile.”

    “Nafikiri nilibeba kinyongo tokea kwenye shuguli za Ester. Ni kama kwa namna fulani alinipuuza wakati najua kila mtu anajua mimi ni mchumba au niliyekuwa mchumba wa Junior kama bado hajaniacha. Nilitegemea angalau anitambue na kunisalimia. Sasa aliponiacha tu, nikajenga kinyongo.” Akamshangaza kidogo Ezra. “Wewe ulitegemea Jelini ambaye ni mgeni pale kanisani, afahamu kila kitu kinachoendelea pale kanisani?!” “Kila mtu anajua Ezra.” “Kwamba wewe unadhania ni mashuhuri kiasi hicho pale kanisani, kwamba kila anayefika pale ni lazima apate habari zako na uheshimiwe kwa kuwa unamahusiano na Junior!? Kweli Hope?” Hope akapoa.

    “Unakumbuka vizuri habari za malikia Vashti?” Hope kimya akiendelea kulia. “Tafadhali pata muda rudia kusoma kitabu cha Ester. Vashti alibweteka katika nafasi yake, akashindwa kumkubalia mfalme, ambaye ni mumewe, jambo dogo sana. Kujitokeza mbele ya watu, ili mumewe ajivunie uzuri wake. Lakini kwa kuwa alishalewa sifa, Vashti alikataa. Unaifananisha hiyo stori na tukio lolote lile?” Kimya.

    “Eti Hope? Hiyo habari unaifananisha na tukio lolote lile lililotokea hapa karibuni? Maana kwa kukataa kwake kujionyesha mbele ya wageni, akiwa amejiamini sana, alisababisha nafasi yake apewe Ester, mtoto yatima ambaye hakuwa hata na hadhi ya kuwa malikia. Kirahisi sana bila kutarajia, akidhania jambo kama hilo haliwezi kumpata mtu kama yeye kwa vile alivyo jidhania na ambayo ameshakwisha fanya kwenye ule ufalme wa Ahasuero. Ukumbe na yeye aliwafanyia wanawake sherehe kubwa sana kwenye jumba hilohilo la mfalme, ikafana sana. Lakini si aliondolewa?” Hope akazidi kulia.

    “Umejisahau Hope. Umesahau alipokukuta Junior. Umesahau mtu uliye naye, ukamdharau kwa kuwa ni mpole sana. Ukasahau kuwa kila mtu anao mwisho wake. Ukabweteka kwenye mafanikio anayoyasimamia Junior. Wote tunajua jinsi Junior anavyosimama na wewe. Hata ukipewa jukumu la wanawake, Junior hataondoka ulipo, akisubiria umtume kwa chochote mpaka jambo likamilike bila ya wewe kulemewa au usijikute peke yako! Huna utakapomtuma Junior akakukatalia Hope. Mchana na usiku yupo na wewe.” Taratibu bila jazba, alihakikisha anamfungua macho.

    “Haya, jiulize umekuwa ukikwama mara ngapi kifedha, Junior akakupa mamilioni ya pesa bila hata kufiria mara mbili? Unaendesha gari nzuri na kuishi kwenye nyumba nzuri, akikulipia yeye mwenyewe bila ya kujali au kuumia mapesa anayowekeza kwako! Kweli leo unamdharau hadharani kabisa na kuonyesha watu baki ni muhimu kuliko yeye!” Hope akazidi kulia.

    “Kana kwamba haitoshi, upo kwenye maamuzi yake mchana na usiku. Tena mimi nakujua Hope. King’ang’anizi mpaka kwenye mambo yake ukitaka unachoshauri wewe akikubali! Napo pia amekua akikusikiliza, na bado unashindwa kuelewa utii ni bora kuliko dhabihu! Utatoa nini chakumlipa mwanaume kama Junior kama sio kumtii, tena wala hana makuu! Huwa hatakagi mengi. Vitu vyake vidogovidogo tu! Kweli napo unashindwa!”

    “Kweli leo useme Jelini alikupuuza kwenye shuguli za Ester, eti ndio uje umuadhibu Junior!? Ushindwe kumzungumzisha vizuri mbele za watu, halafu eti ushindwe hata kukaa naye meza moja kwenye shuguli ya dada yake! Siku muhimu kama ile kwake, kweli ulishindwa kujikana kidogo tu ukiheshimu jambo muhimu kama lile kwa familia yake, unazua tension isiyo na msingi, tena kwa jeuri ya wazi kabisa kwa kiasi kile?!”

    “Ingekugarimu nini kukubali kupiga picha na sisi? Ingekuchukua muda gani? Ingekugarimu nini kutuvumilia kukaa na sisi meza moja kwa muda mfupi ule tena karibu ya mwisho wa harusi! Unamuhama mezani, mbele ya mgeni anayemuheshimu kama Jelini?!”

“Halafu eti unajivua madaraka kwa kupitia barua pepe, moja kwa moja kwa baba yake, yeye hana taarifa! Dharau ya wapi hiyo Hope? Umejiaminisha kwa kipi?” “Nimekosa Ezra. Hakika najuta. Naomba msamaha. Nipo tayari kujirekebisha. Nisamehe. Na naomba nisaidie kuzungumza na Junior.” “Hapana Hope. Unatakiwa wewe mwenyewe uzungumze naye.” Ezra akajitoa.

    “Nitengenezee mazingira. Tafadhali Ezra. Nimeingiwa na hofu ya ajabu. Siwezi hata kumsogelea. Najua wewe atakusikiliza. Junior amekasirika sana. Na najua amekata tamaa na mimi. Lakini mimi namtaka Junior. Nakuahidi nitabadilika. Nimekosea.” Ezra akapoa.

    “Tafadhali Ezra. Nampenda Junior, na sitaki tuachane. Wala sitakudanganya. Sitaki kuachwa na Junior. Na kabla ya kesho kukabidhisha uongozi kwa mzee kama alivyoniomba,” “Hapana Hope. Ni kama ulivyoomba. Wewe ndio umeomba kuacha uongozi effective immediatly. Ndicho ulichotaka na ndicho unachopewa kwa heshima kabisa. Tafadhali usianzishe jambo jingine litakalozua mkanganyiko pale kanisani. Hilo usilibadili kwa watu. Maana umeanza kwangu niliyeona barua pepe yako, hutashindwa kwa washirika wengine. Usisambaze habari ambayo siyo.” Akajua amebanwa kila kona.

    “Nimekosea kusema Ezra. Sijamaanisha kitu kingine. Na hata katika hili nakiri kwako nimekosa na naomba nizungumze na Junior kabla sijaenda kukabidhisha.” “Sasa hivi ameshalala. Nimetoka kuzungumza naye muda mfupi kabla hujanipigia, tumeagana, analala. Naomba iwe kesho. Nitaweka mazingira mkutane kwa chakula cha mchana.” “Nashukuru Ezra. Na wewe umenisamehe?” Ezra akacheka kwa masikitiko.

    “Nimekosa Ezra. Na nakuahidi nitazungumza na Jelini pia.” Alimshitua Ezra, kama aruke. “Hapo hapana Hope. Tafadhali usimsogelee Jelini. Ameshaingiwa hofu na wewe. Kwanza umemuharibu akili kwa kudharau anachokifanya.” “Sikukusudia.” “Lakini umeshafanya. Kwa hiyo HAPANA. Achana na Jelini. Wewe tengeneza yako na Junior. Jelini niachie mimi.” Hapo napo Hope akalia sana. Akajua bado kutakuwa na matabaka asiyoyataka Junior. Leo kusiwe na Ezra na Jelini kwenye maisha yao, akajua hayo mahusiano hayatakaa yakafaa.

    “Nisamehe Ezra.” “Hakika nakusamehe kabisa! Ila Jelini hapana. Hapo utanisamehe Hope. Mimi nakufahamu na namfahamu Jelini. Unaweza zungumza jambo, likabaki kwake, wewe huna taarifa au usijali au ukaja omba msamaha kama hivi, lakini lishamwingia yeye. Hapana Hope. Nitafanya chochote ila si Jelini. Acha muda uje utuweke pamoja, lakini si kwa wewe kumtafuta Jelini. Hapo HAPANA. Usiku mwema. Nitakutaarifu kesho.” Simu ikakatwa na kumuacha Hope bila ya tumaini.

    Alitamani arudi kwa Junior angalau kuna taarifa za kutengeneza na Jelini pia. Lakini hakuwa na chakufanya. Kila alipokumbuka maneno ya Ezra kwenye mahusiano yake na Junior, akazidi kukata tamaa. Jeuri aliyokuwa akimfanyia hata kabla ya hapo. Kumpuuza kwenye mambo madogomadogo! Hofu ikazidi kumuingia kila akifikiria sababu inayoweza mfanya Junior amsamehe, alikosa.

    Akajikuta ni mzigo ambao Junior atakuwa na nafuu ya kuutua. Hawakuwa na historia/msingi mzuri ya kimapenzi, ila ni kweli walifanikisha mengi kwa pamoja. Ila akakumbuka yote waliyofanikisha, hayakuwa yao. Kanisa si la Junior, ni la baba! Junior hana cha kukumbuka hapo na kumfanya atake warudiane! Usiku huo ukazidi kuwa mbaya kwa Hope. Maji yalishamwagika muda mrefu sana, asijue hata yalishakauaka. Hakuna cha kuzoa wala kudeki. Anajirudije!

~~~~~~~~~~~~~~~

Tusijisahau, kila tunachopewa ni dhamana na kuna garama ya kutunza.

TUSIBWETEKE.

Umama, ndoa, mahusiano, hata undugu ni DHAMANA, na kuna GARAMA. Siku utakapochoka tu, na kuamua kuzembea, UHARIBIFU UNAANZA KUNYEMELEA.

INAENDELEA. 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment