Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! – PART 3 - SEHEMU YA 29. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! – PART 3 - SEHEMU YA 29.

 Siku hiyo ya jumatano walifika ofisini kama kawaida yao bila ya kuchelewa. Ezra akamuona ni kama hayupo sawa. Alitegemea. Akampa muda kidogo kisha akaanza. “Hope alinitafuta jana usiku.” Kimya. Junior akiendelea na shuguli zake kwenye kompyuta yake. Ezra akaendelea akijua anasikiliza. “Nimezungumza naye kwa muda mrefu tu. Anajutia kosa.” Kimya. “Amekiri kufanya yote akiwa hajafikiria madhara yake, zaidi kwako. Ameomba mkutane umsikilize.” Kimya.

“Na mimi nashauri mkutane. Naomba mpe nafasi. Msikilize tu kisha utaamua. Nitaweka reservation.” Akamtajia kimgahawa kizuri, chenye utulivu na kinachoendana na hadhi yao anachojua Junior anapenda chakula cha hapo. Kimya. “Nitamwambia saa sita na nusu awepo hapo. Utamkuta.” Kimya, hata kumwangalia hakuwa akimwangalia. Ezra akamuacha akiwa na uhakika amesikia, na atakwenda.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika saa 6:10 mchana, akamuona ananyanyuka. Akajua ndio anakwenda huko. “Nikuletee nini?” Akamuuliza. “Na mimi nakutana na Jelini saa saba kamili kwa chakula cha mchana. Ameniomba anitoe kwa lunch.” Akafikiria kidogo, akatoka.

Palipomwagika Maji.

    Alifika hapo ili asichelewe kama kawaida yake, lakini akakuta Hope akimsubiria. Alikuwa kama mgonjwa, mpaka Junior akashituka. “Unaumwa!?” Akamuuliza. “Hapana. Ila nashukuru kwa kuja kunisikiliza.” Hope alikuwa amenyongea. “Najua nilikuomba msamaha siku ya jumapili na nikakuahidi nitabadilika. Lakini nimekosea tena.” Akaanza kulia. “Tunaweza kuagiza kinywaji kwanza?” Junior akauliza wakati muhudumu akiwasogelea. Akaagiza juisi ya embe, Hope akajifuta machozi na kuagiza maji ya kunywa. Muhudumu akaondoka akiwa amewaachia menu ya chakula.

    “Nimekosa na kujichanganya kupita kiasi na sijui chakufanya.” “Labda nikuulize Hope, tatizo ni nini?!” “Hakuna tatizo Junior. Mimi ndio tatizo. Nilikosea tangia mwanzo wakati unanionya juu ya Jelini. Nikashindwa kuchukulia zile taarifa vizuri, nikaendelea kuharibu. Nimekosa Junior. Nimekosea hata kuacha uongozi bila ya kukutaarifu. Nimekosea jinsi nilivyoacha. Nimekosea hata kwa Jelini. Najua nimekuumiza, ila nakuahidi kuanzia leo nitakua nikikushirikisha, na kukusikiliza. Nisamehe Junior. Nimekosa.” Junior akabaki kimya.

    “Nimekosa Junior. Nisamehe.” Ubaya wa Junior hakuwa amemtafuta tokea aombe msamaha na kuahidi kujirekebisha na kesho yake kuharibu zaidi, pia hakumtafuta. Alinyamaza kimya. Na hapo akawa amenyamaza kama anayefikiria. Muhudumu akaleta vinywaji, wakaomba asubiri swala la chakula.

“Naomba usinikatie tamaa Junior! Nimekosea, na nakuahidi nitajirekebisha.” “Labda nikuulize swali. Na naomba ufikirie kabla hujajibu.” Hope akatulia. “Ni kwa nini unataka kuwa na mimi?” Hope akababaika kama ambaye hakutegemea hilo swali. Lilikuwa swali rahisi, ila akashangaa kwake limemuia gumu. Junior akaendelea kunywa kinywaji chake kisha akaongeza.

    “Nashauri kabla hatujaenda mbali, kapate muda wa kufikiria. Maana haya yanayoendelea kwako, ukiwa kwenye mahusiano yaliyofika mbali kama hivi, sidhani kama ni kunijali hata kidogo.” Hope akashituka sana.

    “Nakujali Junior!” “Kama ungekuwa ukinijali hata kidogo, ungenifikiria ile fedheha uliyoniachia mbele ya watu siku ya jumapili. Tena zaidi ya mara moja! Yaani kwa kurudiarudia, hadharani! Binafsi nisingeweza kumfanyia hivyo hata mtu baki tu. Halafu kana kwamba haitoshi, tunazungumza usiku, kesho yake unamuadhibu baba yangu kwa mazungumzo ambayo umekiri hutarudia tena kwa kuwa ulikosa! Sasa na sasahivi tunarudi palepale kuwa ‘umekosa, hutarudia tena’. Unamaanisha nini!? Pengine mimi ndio nashindwa kuelewa?” Hope akashindwa kujibu kabisa, akabaki akilia.

    “Tafadhali tuzungumze Hope. Maana hapa tunazungumzia juu ya hatima ya maisha yetu yote ya hapa duniani. Sitataka uishi na mimi kwa kulia, na mimi sitataka kuishi bila furaha na amani. Hatuna sababu ya kufanya hivyo. Kwa nini?!” “Nakuahidi sitarudia tena Junior.” “Kwa nini?” Junior akaendelea kuuliza.

    “Nakupenda Junior. Natamani tuishie pamoja. Na sidanganyi. Ni vile tu sijui jinsi ya kutenda sawasawa. Nimekukosea adabu wewe na mzee. Ila nimekuja kufikiria, na mimi nimegundua nimekosa Junior. Nimekosa, naomba nisamehe. Nimekua na haraka ya mambo, nimekosa muda wa kujitafakari. Ila nimepata muda wa kujifikiria, nimegundua makosa mengi hata ambayo hutayataja hapa, lakini nimepata muda wakujifikiria, nimegundua nimekukosea kwingi na unahaki ya kunichoka Junior.”

    “Nimerudi kwako, nimekiri makosa yote. Kuzembea kote ambako nimekufanyia. Naahidi nitabadilika, tena kwa vitendo. Najua huwa nakulazimisha kufanya maamuzi. Lakini safari hii nakuacha kabisa. Na pete yako nakurudishia kabisa. Ukiona nastahili nafasi ya pili, na upo tayari na mimi kwa mara ingine, basi naomba unitafute. Ila kama unaona huna nafasi yangu nyingine, basi Junior. Mimi ndio nimekosa. Nimevunja mahusiano yetu. Sitakulaumu. Ila ukinirudia, hutajuta tena. Na ujue utakua huanzi upya. Upo na mtu anayekufahamu. Hutapata shida..” Akaweka pete mezani Junior asiamini.

    “Unafanya mchezo wa hatari Hope wewe!” “Hamna maana ya hii pete kama nitakukosa wewe mwenyewe Junior! Umenipa vingi. Vingine siwezi kurudisha maana kama gari ndio miguu yangu hapa mjini na ile nyumba ndio naishi hapo?”

    “Najua umekasirika, kuniacha haitakuwa shida. Ila ujue mimi nipo, na nakusubiria. Na ukinirudia hutajuta tena. Nitakuwa nikikusikiliza na kukupa nafasi hata uwe unafanya maamuzi yako bila kukuingilia. Na…” Aliendelea kutaja mapungufu yake hapo, Junior akimtizama tu. Kisha akaaga na kuondoka hata chakula hakula ila aliacha pete juu ya meza. Junior akaagiza chakula, akaendelea kula taratibu. Kimyakimya, akitafakari maisha yake.

 Ofisini.

    Ezra anatoka kula anarudi ofisini akiwa na furaha, akidhani pengine wametengeneza, akaenda kumuwekea matunda aliyomjia nayo hapo mbele yake, pembeni ya kompyuta aliyokuwa akitumia. “Jelini anakusalimia.” “Asante. Mmekuwa na wakati mzuri?” Jinsi alivyokuwa akiuliza si kama aliyekasirika ila aliyekuwa mbali kimawazo. “Utamuweza Jelini!” Akajibu akienda kukaa mezani kwake. Ndipo akagundua kuna pete ya uchumba ya Hope. Alishituka hakutarajia. Ilikuwa kama ameachiwa yeye hapo mezani kwake. Akaichua na kubaki akiitizama kisha akamtizama Junior. Busy na kazi.

    “Ni nini kinaendelea Junior!?” Ikabidi aulize. “Hope amenirudishia.” Ezra akashindwa kuelewa. Ikabidi aulize tena. “Kwa makubaliano gani?” Akamuona anacheka kwa masikitiko. “Yaani mimi namvalisha pete kwa heshima mbele ya wazazi wangu, ananirudishia mgahawani! Eti ananiambia, nitakapoona nipo tayari na yeye tena, eti mimi ndio nimtafute! Umeona wapi hiyo!?” “Subiri kwanza Junior. Kwani ilikuaje?” Junior akamueleza mwanzo mpaka mwisho.

    “Nilitamani kumsikia anapambania mahusiano yetu Ezra! Leo ananirudishia mimi pete, na kuniambia nije kumtafuta tena, kana kwamba eti mimi ndio nina shida kubwa sana na haya mahusiano! Yeye nafasi yake ni ipi sasa? Kwa nini akimbie pakiwa pametibuka, asibaki akitengeneza kama kweli ananipenda?” Ezra akatulia akitafakari.

    “Hivi unajua alishindwa kabisa kunijibu ni kwa nini anataka kuwa na mimi!” Ezra akakunja uso kama ambaye ameshindwa kuelewa. “Exactly! Na mimi nikashangaa hivyohivyo kwamba alishindwa hata kudanganya kwa kusema pengine ananipenda! Kitu ambacho wachumba huambiana hata kama hisia zinakuwa ziliisha, japo kwetu sidhani hata kama zilikuwepo!” Junior akaendelea kulalamika.

    “Nilimchumbia mbele ya wazazi na kanisa, tukawekewa mikono, na mimi nilimpa hii pete nikiwa sijaribishi. Na yeye nilimwambia huu ukurasa nafungia kwake, sitatafuta tena. Sasa sijui akajiaminisha sana, ameishi na mimi kama unavyojua. Kiburi wakati wote. Amenikosea. Kwa kuwa anajiamini sana, anarudisha pete akiwa na uhakika ni lazima itarudi tu kwake!” Junior akacheka na kutingisha kichwa.

    “Pengine hakuwa amemaanisha hivyo! Sijui! Simtetei. Maana jinsi nilivyozungumza naye ni kama hataki kukupoteza.” “Na mimi ameniambia anataka kuwa na mimi. Ndio nikamuuliza kwa nini, huwezi amini hilo swali likawa gumu kwake.” “Junior!” “Hakika siongopi. Si nimetoka kukusimulia hapa? Ndio ikabidi nimwambie akapate muda wa kufikiria kabla hatujaendelea. Halafu eti baadaye ndio anakuja kusema ni kwakuwa nanipenda. Yaani kama aliyekuwa akitafuta jibu! Kweli Ezra! Mpaka nahisi yupo na mimi kwa sababu ya pesa, misaada ninayompa, na si mapenzi.” Hapo hata Ezra akaanza kuumia.

“Ezra, mapenzi hayajifichi jamani! Hufikirii kumwambia mpenzi wako kama unampenda! Inamuwia ngumu hata kuropoka tu kama ananipenda!” Ezra akapoa kabisa.

    “Hapana Ezra. Kuna tatizo kati yangu na Hope, au nimekuwa nikilazimishia kitu ambacho hakipo kwa muda mrefu sana. Nimekaa nikifikiria na kuona hata anashindwa na Emelda!” Ezra akakunja uso.

Ukisema Cha Nini, Wapo Wanaolilia Kukipata.

    “Emelda yule wa nyumbani!?” “Kabisa Ezra. Hope amenifanya nijifikirie sana. Amenifanya nitulie na kutafakari na usiku nikashindwa kulala. Hope ambaye ni mchumba, anapitwa mbali sana na Emelda, msichana wa mama. Haya unayomfanyia Jelini wewe, ndiyo anayonifanyia Emelda ila nikipuuza nikichukulia ni wajibu wake au nikidhani mama anamtuma, kumbe ni yeye tu mwenyewe.”

    “Usiku nimerudia jumbe zake, mpaka nikashangaa.” “Junior!” “Hakika sizushi Ezra. Nikikwambia sikulala jana usiku, ujue sijalala nikijaribu kutafakari na kujiuliza nilishindwa vipi kuelewa?” Junior akakaa sawa.

    “Unakumbuka miaka miwili iliyopita mama yake alikuwa mgonjwa?” Ezra akabaki akimtizama, pete aliyovua Hope ameshika mkononi. “Acha kuniangalia kama niliyechanganyikiwa.” “Hakika naomba nielewe na mimi Junior. Mambo mengi yanapita kichwani mwangu sasahivi ila wewe ulishapata muda wa kuyatafakari usiku kuchwa. Najaribu kuyaweka sawa. Wrapping my head around it. Endelea.” Junior akakubaliana naye. Zilikuwa ni taarifa nyingi kwa wakati mmoja.

    “Mama alimpa pesa na kumwambia arudi kwao, akamuuguze mama yake. Alinifuata tukiwa kanisani siku ya jumapili. Sema sikutilia maanani. Ndio sasahivi kumbukumbu zinanijia kana kwamba nilifunga macho, ndio yanafunguka. Ila aliniambia hivi, ameshindwa kuondoka mpaka aniage. Akaniambia anarudi kwao, hajui atarudi lini, mama yake ni mgonjwa, anakwenda kumuuguza mpaka apone. Mimi moja kwa moja nikajua anataka nimuongezee pesa. Bila ya kufikiria nikampa pesa na kumwambia akiwa na shida yeyote akiwa nyumbani, asiache kuwasiliana, sisi ni ndugu, asiuguze peke yake. Nakumbuka mpaka sura yake jinsi alivyofurahia kusikia hivyo na wala si pesa.” “Kwa hiyo mlikuwa mkiwasiliana alipokuwa nyumbani?” Akampa simu yake.

    “Hayo ni mazungumzo yangu na yeye, tokea wakati ule mpaka majuzi analeta chakula nyumbani.” “Subiri kwanza Junior! Inamaana anayetuleteaga chakula nyumbani si mama ni yeye?!” “Ndivyo na mimi nilivyodhania muda wote. Kumbe wala mama hajui au hausiki. Yeye anapika, kisha anamtuma Noah au dereva atuletee. Vinawekwa kwangu ndio tunakula kama vile, nikijua ndio utaratibu wa mama kwa kuwa siku za ijumaa anajua tunakua tumefunga. Kumbe mama hausiki kabisa.”

    “Sasa wewe umewezaje kujua kama si mama?” Ezra akazidi kudodosa. “Cha kwanza hata wewe ukisoma hizo jumbe kwa kutulia, utagundua ni wazo lake, na utagundua anapika vitu vile anavyojua napenda, na ndio maana utagundua anajirudiarudia kwenye vyakula anavyotuletea. Pili, jana, ilibidi kumuuliza mama kwa umakini huku nikimchanganya na habari zako za kuchumbiwa na Jelini.” Wote wakacheka.

    “Amesemaje?” “Kwanza amefurahi sana. Ila amesema tumetia aibu, tumepitwa. Leo wanakwenda kuzungumza na mama Jema, tujipange. Ila sasa nikamchomekea kuwa sasa si itabidi atuletee chakula cha pongezi? Akanijibu hivi, yeye alitubembeleza sana tusihame nyumbani, mpaka tuoe. Tukakataa tukijiona tumekua. Akasema wazi kabisa, tukitaka chakula chake twende tukale kwake, tena kile anachompikia mumewe, ndio na sisi tule hichohicho. Vinginevyo tuoe, tuache kuchosha wake za watu.”

    “Haiwezekani Junior!” “Hakika. Ndipo nikajua huyu Emelda anapika kwa siri hata mama hajui. Na ndio maana vyakula vyake vinakuja mchana wazazi wakiwa hawapo nyumbani na sisi tupo kazini. Kama anayejiiba. Au mama anajua, amelifumbia tu macho.” Ezra akazidi kushangazwa.

    “Sasa pesa huwa anapata wapi?” “Mimi sijui anajinyima vipi mpaka anapata pesa yakupika vyakula vyote hivyo. Pengine hizi pesa ndogondogo tunazompa. Sijui.” “Mmmh! Hii imenifanya nimfikirie kwa tofauti, aisee na kunifanya nikumbuke mengi!” “Mimi zaidi mpaka najuta.” Ezra akamtizama kama mwenye swali.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kosa la Mchumba, limefungua mwanya wa KUWAZWA msichana anayefanya kazi za ndani kwa muda mrefu kwa mama mchungaji. Hatimaye wema wake UMEFIKA akilini kwa Junior. Ni nini kitaendelea? Hope atarudishiwa pete ya uchumba?

Mkakati wa kuchumbiwa Jelini unaendelea. Watafanikiwa?

Usikose muendelezo.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment