Hakupoteza muda, akaenda kugonga chumbani kwake. Mara moja
tu, tena taratibu. Alipoona kimya, akaingia kwa kunyata. Akamuona amelala
kitandani. Moyo ukajawa furaha! Akaweka matunda aliyokuwa amemletea kwenye meza
ndogo aliyokuta ina glasi ya maji na supu imefunikwa. Akajua hajala.
Akaweka vizuri na kuamua kukaa hapohapo kitandani taratibu
kama asimuamshe wakati shida yake ni aamke. Hakuamka. Akaanza kumshika kichwa
taratibu. Yaani yeye ndio akawa anasikia raha kumshika. Akamshika kipanda uso
kama anayempima homa, mpaka akamuamsha.
Junior alitoa koti la suti na hakuwa na tai. Shati jeupe!
Msafi kama kawaida yake. “Kaka!” Akashituka, hakutegemea. Akatoa mkono kama
aliyefumaniwa. “Vipi?” “Najisikia vizuri. Sijatapika. Ila nahisi dawa za kuzuia
kutapika ndio zinanipa usingizi. Nalala kama niliyezimia. Pole na kazi.”
“Asante. Basi acha nikupashie moto supu, uje unywe. Naona mama amekuachia
hapa.” “Usihangaike kaka. Nitakwenda tu. Wewe pumzika.” Junior akakaa vizuri na
kumwangalia.
“Mbona wewe huwa unanipikia na kuniletea mpaka nyumbani na
wakati wote hujawahi ona ni usumbufu? Kwa nini kwangu unahisi ni usumbufu?”
Alishituka hakujua kama amejua. Akakwepesha macho.
“Eti Emelda? Kwa nini kwangu ndio iwe usumbufu nikitaka
kukufanyia kitu chochote? Au ulidhani bado sijajua kama ni wewe ndio unaleta
chakula nyumbani si mama?” Akabaki akiangalia shuka alilojifunika.
“Nashukuru kunijali Emelda. Asante.” Mwili mzima wa Emelda
ulikuwa ukisisimkwa. Ni Junior! “Ila nasikitika sikujua mapema.” “Upo na
majukumu mengi kaka. Unajitoa kwa kila mtu, kila mahali. Mchana na usiku
hupumziki. Ni rahisi watu kukusahau wewe.” “Mbona wewe hujawahi kunisahau?” Akanyamaza.
“Eti Emelda?” “Kwa kuwa upo kama mama yangu. Ni mpole sana.
Anajituma sana pale kijijini kwenye mambo ya watu, lakini huwa yeye akipatwa na
shida, watu huwa hawamkumbuki kabisa. Inakua rahisi kumpuuza kwa sababu
huwa anafanyaga yale mambo watu wengine hawataki kufanya.” Akaendelea taratibu
tu.
“Kukiwa kuna misiba au hata harusi pale kijijini, basi ujue
mama atafanya zile kazi ambazo watu hawaoni au hawataki kufanya.
Zakudharaulika. Kama kuchota maji na kujaza kwenye vyungu. Kuleta kuni wapishi
wapike. Na watu wakishakula, basi atabakia kusafisha na kuosha vyombo. Zote
hizo ni kazi ambazo hakuna mtu anaona wala kuthamini. Kiasi ya kwamba ikifika
kwenye kushukuriwa, yeye hafikiwi. Kwanza hawajui kama alifanya.”
“Hakuna anayemshukuru mchota maji, wakati wakunawa mikono, ila
anaye mnawisha. Hakuna anayemshukuru mleta kuni, ila mpishi. Hakuna
anayekumbuka kusafisha vyombo baada ya vyakula vya msibani na kwenye sherehe
kwa kwa watu wanakuwa wameshaondoka, na kama wapo, basi wanakuwa wamekaa sehemu
maalumu, mama yangu akifanya nyuma ya nyumba. Na wewe upo hivyohivyo kaka.”
Junior hakuamini.
“Pale kanisani unakua wa kwanza kufika na wa mwisho
kuondoka. Kila siku. Upo kwenye kila huduma, kasoro ya watoto tu ndio huko sijawahi
kukuona.” Akakumbuka maneno ya Jelini. “Ambako wewe ndio upo?” Akamuuliza.
“Ninachotaka kusema, unafanikisha kila huduma pale kanisani. Kila mtu anajua
wewe na kaka Ezra hamjui kukataa wala kulalamika mnapopewa jukumu, ndio maana
wanawatuma bila kuchoka. Lakini linapofika swala la kushukuru viongozi
wa kanisa, sijawahi ona hata mara moja nyinyi mnaitwa pale mbele na
kushukuriwa au kupewa zawadi. Wanawashukuru wale viongozi ambao nyinyi
ndio mnakuwa mnawafanikishia kazi. Hakuna anayetambua watu kama nyinyi
kaka.” “Lakini wewe unatambua na kujali.”
“Sio kama ambavyo mnastahili au unavyostahili, kaka. Wakati
mwingine natamani kufanya zaidi ila nakua sina uwezo. Nakuwa natamani
hata usikie nikikwambia pole, lakini mara zote inakua ngumu kunisikia
hata nikikwambia ‘pole’.” Junior akajisikia kuumia. Kwa asili Emelda ana
sauti ya chini. Mtaratibu sana. Pengine ndio sababu.
Akamwangalia. “Napunguza kelele ili niweze kukusikia
Emelda. Pole na samahani.” Ilimgusa huyo mrembo, akashindwa kuamini. Maana hata
alivyoisema Junior, ilijaa hisia za kumaanisha.
“Umenielewa?” Akamuuliza akivuta shuka kama amfunike vizuri.
Emelda akatulia akifikiria maana yake. Kelele moja wapo ni Hope, sasa
atamfikiaje yeye! Akatulia msichana wa kazi, asije kujipa tumaini ambalo
halipo. Akamwangalia akamuona yupo mawazoni, akaona Ezra yupo sahihi. Amalize
la Hope kabla hajaanzisha jingine, tena kwa maneno tu.
“Pole kwa kujirudia rudia mara zote bila mimi kukusikia,
na bado hujachoka na kunikatia tamaa. Na samahani kwa kushindwa kukusikia.”
Akamvuta mkono kabisa. Akaushika vizuri katikati ya mikono yake. “Lakini
nakuahidi kukusikiliza. Na unapoona unazungumza na mimi, sijasikia, tafadhali
rudia tena, na hakikisha nakusikia. Na nakuhakikishia kuanzia sasa, utajua kama
nimekusikia. Sawa?” Akatingisha kichwa kukubali. Wakatulia hapo kwa muda,
amemshika mkono vizuri na kwa upendo, akitamani asimuachie, na yeye akitamani
kama aubusu. Ila akajikaza na kumuachia taratibu.
“Acha nikakupashie supu moto. Ule kabla sijaondoka.”
Akatoka. Ila kwa hakika Emelda alishajua yupo pale si kama kaka. Akahisi habari
inataka kubadilika. Ila Hope akabaki kumfanya atilie mashaka kila kitu Junior
alichozungumza. Akapoa akiumia moyoni, akitamani kama angepata yeye bahati ya
Hope.
Akarudi na sinia ya supu. “Nikusaidie kula?” Emelda
akacheka. “Nitakula kaka. Asante. Mbona sioni yako?” “Nataka wewe ule kwanza.
Ezra atanipelekea chakula ofisini. Nitakula nikirudi, usiwe na wasiwasi.”
Akatulia kama anayejifikiria.
Akamgundua. Akamuacha tu akijua kinachoendelea kichwani
mwake, ila akashukuru Mungu hataweza kumuuliza. Maana hata yeye hakuwa na
majibu ya kumpa kwa wakati huo. Akatulia akimsubiria akila, macho kwenye simu
yake ili asimfanye akashindwa kula. Akahisi na yeye anavuta simu yake na kutuma
ujumbe. Akabaki kujiuliza anawasiliana na nani muda huo na yeye yupo! Kajiwivu
kakaanza.
Mara akaona ujumbe umeingia kwenye simu yake, akahama kwa
haraka kutoka alipokuwa akiperuzi kuwahi huo ujumbe akijua unatoka kwake. Ikawa
ni kweli. ‘Nimefurahi umekuja kuniona na kukaa na mimi
katikati ya siku yako yenye majukumu mazito. Asante.’ Akacheka taratibu
na kumjibu. ‘Sasa hivi nakuona na nakukusikia.’
Akamjibu akamuona anavuta tena simu yake. Akasoma, akamuona anajifuta machozi.
Akarudisha bila ya kujibu. Akamuacha. Akaendelea kuperuzi simu yake. Kimya
mpaka akamaliza.
“ Asante kwa supu. Nimeshiba.” “Rudi kupumzika. Kazi zote
zimeshafanywa na mama Leti. Hakuna kitu chakufanya tena. Pumzika kabisa leo.”
“Asante kaka. Asante sana.” “Karibu.” Akasimama na kutoa vyombo, Emelda
akishangaa. Yeye ndio huwa anawatumikia hapo ndani. Zaidi huyo Junior na Ezra,
leo Junior anamtumikia yeye! Ikamgusa zaidi. Akarudi kujilaza akimtizama
anavyojishugulisha hapo.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Akasafisha hapo, na kurudi kukaa hapo kitandani. Akamvuta
tena mkono akishangaa anataka kufanya nini tena na mbona harudi kazini!
“Nikuulize kitu Emelda?” Akatingisha kichwa kukubali.
“Nilipokuwa nimelazwa hospitalini, unakumbuka ombi lako siku
ya mwisho natolewa?” Jinsi alivyoshituka na kuinamisha kichwa, akajua
amekumbuka. “Kwa nini hukuniambia kama ni wewe ndio unataka nirudi
nyumbani ili uniuguze, badala yake ulimtumia mama?” Akanyamaza, ila
akahisi mikono inatetemeka, maana aliokuwa ameushika ulikuwa ukitetemeka.
Akamsugua viganja, akataka kuuvuta mkono wake akamzuia,
akabaki ameushika. “Eti Emelda?” “Nilijua nikikwambia ni mama ungeona uzito
wake, ungekubali.” “Kwa nini muda wote huo umeshindwa kuniambia kama ni wewe,
umekua ukimtumia mama? Na si katika hilo tu, katika kila kitu! Kwa nini
hukutaka nijue kama ni wewe ndiye unayenifanyia vitu?” “Isingebadili chochote
kaka.” “Lakini mimi ningependa kujua! Nahisi ingenisaidia.” “Sidhani kaka.
Sidhani.” Kwa upande fulani akakubaliana naye. Akaendelea kumsugua huo mkono taratibu,
kwa muda akiwa mawazoni akifurahia uwepo wake mpaka ujumbe ulipoingia.
Ukamtoa mawazoni
akiwa na huo mkono wa Emelda akiuchezea, hana habari, mbali mawazoni. ‘Inatosha Junior. Tafadhali rudi kazini. Kiasi.’
Alikuwa Ezra. Akaangalia muda, akashituka na kuachia mkono. “Pumzika,
tutawasiliana.” “Asante.” Akasimama kama afanye kitu, akaona kweli awe na
kiasi, akaondoka.
Ijumaa.
Jelini hakuwa na habari kama ni siku yake ya kuchumbiwa. Ila
Ezra alimtaarifu kuwa mchungaji amekubali kufika kwao kwa chakula cha usiku,
baada ya ibada ya maombi. Kwa hiyo akamwambia ajiandae, usiku huo watakuwa na
ugeni. Mchungaji na familia yake wote watakua hapo. Akamwambia mama yake,
asijue mama yake anajua na ameshamtaarifu hata Jema. Siku hiyo wakawahi kwenda
kazini na kurudi kuanza matayarisho, kila mtu kwenye familia yake na mchungaji alijua
kama anachumbiwa, kasoro yeye.
~~~~~~~~~~~~~~~
Ilipofika jioni, Jelini alikuwa amefunga kama
alivyokubaliana na kina Ezra akaenda kanisani kwa maombi kabla ya kufungua.
Akakutana nao. Noah alishakuwa tayari akipiga kinanda hapo ibadani kuashiria
alishafika. Sasa wazazi walipofika, Junior hakumuona Emelda. Akamtumia ujumbe,
hapakuwa na majibu. Uzalendo ukamshinda, akamfuata mama yake. “Emelda yuko
wapi?” “Alikwenda kusuka tokea asubuhi. Yupo kwenye matayarisho.” Yeye Junior
akajua matayarisho ya shuguli baada ya pale. Akatulia.
Ibada ikaisha safari ya kuelekea kwa kina Jelini ikaanza.
Ezra akagundua hayupo sawa. Walipofika kwa kina Jelini, ikabidi amuulize mama
yao. “Emelda anaendeleaje?” “Ameamka na nguvu, akaamua kwenda kusukwa.
Ameshinda huko siku nzima. Sisi tumeondoka hapo nyumbani hajarudi ila aliaga
tokea jana kuwa atachelewa.” Akamwangalia Junior, kimya.
Wakakaribishwa ndani, salamu. Jema na familia yake pia
walikuwepo hapo. Kukawa kumechangamka. Jelini maneno mengi akafanya kila mtu
kujisikia nyumbani na kuzoeana kirahisi. Hofu ya mchungaji waliyezoea kumuona
madhabahuni tu akizungukwa na maelfu ya waumini, Jelini akaipoozesha akawa baba
hapo kwa muda mfupi tu. Vicheko akimchokoza mpaka mama mchungaji. Mpaka Noah
alikuwepo.
Vikaendelea vinywaji, zaidi chai kwakuwa walikuwa wamefunga.
Junior akatoka nje. Ezra akaona harudi, akamfuata. “Vipi?” “Simpati Emelda!”
“Pengine atakuwa ameishiwa chaji. Mama amesema alikwenda kusukwa tokea asubuhi.
Tumsubirie, si amesema atakuja ila kwa kuchelewa?” Akakubali kuingia ndani.
Mambo yakawa yanaendelea, Emelda haji. Kila kitu
kikaanza kukosa ladha pale. Yupo kama hayupo wakati mwenzie anataka kuchumbia. Akamsogelea
mama yake. “Nani anamleta hapa Emelda?” Akawa amemchanganya mama yake. “Si
umesema atakuja ila kwa kuchelewa?” “Nilimaanisha atarudi nyumbani kwa
kuchelewa! Emelda hatakuja hapa. Yupo na matayarisho ya safari.” Junior
alishituka, Ezra akasogea.
“Safari ya wapi tena!?” Ezra akauliza. “Si aliniambia
amekuaga wewe siku ya jumapili?” “Mimi!?” Junior akashangaa sana. “Ndivyo
alivyoniambia. Kuwa siku ya jumapili pale kanisani alikuaga kuwa anakwenda kwao.
Hata hivi juzi alipougua alikuwa na wasiwasi anaweza shindwa kwenda. Kwa hiyo
yupo kwenye maandalizi ya safari ya kwao. Noah amemkatia tiketi ya basi la
asubuhi.” Junior na Ezra wakaangaliana.
“Tafadhali endelea Ezra.” “Siwezi bila wewe. Nenda ila ujue
nakusubiri.” Mama yao akawa haelewi. “Vipi?” “Narudi sasahivi mama. Ila Ezra
tafadhali usinisubiri. Endelea.” “Unapoteza muda. Nenda lakini jua nakusubiri.”
Junior akatoka akikimbia.
Maombi Ya Sirini, Yajibiwa Kwa Moto.
Ila Kwa Wakati wa Mungu.
Moja kwa moja akikanyaga mafuta kwenda kwao. Akashuka
akikimbia kama anayewahi wakati aliambiwa Emelda anaondoka kesho na si
usiku huo. Akagonga kengele mara kadhaa maana mlango ulikuwa umefungwa. Akabaki
akigonga kengele na kumpigia simu. Baada ya muda akasikia mlango unafunguliwa
kwa ndani, akahema kwa nguvu.
Akatoka Emelda amependeza, mpaka akamzubaisha Junior.
Hakusukwa kitu cha ajabu, ila rasta za kimasai. Ndogondogo kama sindano. Na kwa
kuwa zilikuwa zikimuuma, aliziachia, hakutaka kuzibana kabisa, ngozi ya kichwa
ilizidi kuuma kwa kuvutwa wakati wakusukwa.
Hakutegemea kumuona Junior pale tena usiku huo. “Shikamoo
kaka! Nilikuwa bafuni nikashindwa kutoka kwa haraka. Pole.” Akampisha mlangoni.
“Karibu.” Junior akaingia. “Nilijua utakua na kaka Ezra! Mama aliniambia leo na
yeye anachumbia.” “Sasa kwa nini na wewe hukuja?” Akawa kama analaumu.
“Nimerudi kwa kuchelewa kaka. Halafu huku kuugua siku mbili
kumenipotezea muda, nimejikuta sijajiandaa kabisa kwa safari ya kesho. Nikaona
nibaki nijiandae kwa safari. Naondoka alfajiri sana. Mambo yamekwendaje huko?”
“Sijui! Nimekuja kukufuata wewe.” Akamchanganya Emelda akahisi hajamsikia
sawasawa.
“Naulizia uchumba wa kaka Ezra. Mama ameniambia na yeye
anachumbia leo.” Junior akaona akae. Emelda akamsogelea akiwa na mshangao. Ila
akamuuliza. “Nikuletee juisi?” “Mbona unasafiri bila kuniaga?” Akauliza kwa
kulaumu. “Nilikuaga kaka! Pengine hukuwa umetilia maanani. Tulikuwa
kanisani.” Junior akashangaa sana.
“Kwenye harusi ya Ester?!” “Hapana. Kanisani kabla ya kwenda
kwenye harusi.” “Nikasemaje?!” “Ulisema sawa. Halafu hapohapo na wifi
Hope naye akaja, akakuchukua, mkaondoka. Mliniacha palepale nimesimama.” Junior
akainama kwa uchungu. Emelda akakaa taratibu, kochi la mbele yake.
“Nisingeweza kuondoka bila ya kukuaga kaka!” “Daaah! Hata
sijui niseme nini!” Emelda akawa hajaelewa. “Kwa nini?!” Akauliza taratibu tu.
“Sikujua kama unasafiri kesho Emelda! Samahani sikutilia maanani. Naomba
unisamehe nahisi sikuwa nimeelewa, pengine nilidhani...” Akaona asijitetee,
anaharibu. “Samahani.” “Hamna shida.” “Hapana. Si sawa. Si sawa kabisa!
Nakuahidi nitabadilika.” Emelda akainama akiwa amekalia mikono yake.
“Unakwenda nyumbani kufanya nini?” “Ni likizo yangu, mama
amenipa. Ndio nakwenda kumsalimia mama na wadogo zangu.” “Kwa muda gani?”
“Amenipa siku 15, kwa hiyo kama majuma mawili. Naenda kumsaidia mama kulima.
Ndio msimu wa kupanda huu.” Anaongea hajui jinsi kaka yake alivyovurugikiwa.
“Nikikuomba usiondoke kesho, mpaka tuzungumze na kujipanga
pamoja, itakuwa sawa?” Emelda akabaki amekunja uso kama asiyeelewa. “Tafadhali
Emelda. Ukiondoka tu, utanichanganya, nitashindwa kufikiria na hata
mambo niliyotaka kufanya nitashindwa. Naomba ubaki ili nitulie. Halafu kama ni
shamba, naomba tutume pesa, zitangulie kwa ajili ya vibarua. Mama alipie watu
wakumsaidia shamba.” “Mama ndio kibarua mwenyewe.” Junior akameza mate,
akapatwa na kigugumizi.
“Msimu huu anakuwa anachukua kazi kwenye mashamba ya watu,
ili kujipatia pesa za kumsadia na wadogo zangu. Kwa hiyo mimi na wadogo zangu
ndio tunakuwa tukimsaidia.” Ki ukweli hakuwa akimfahamu hata kidogo huyo binti
japo alikuwa akiishi naye nyumba moja mpaka akahama hapo kwao. “Basi tutamtumia
pesa za matumizi. Halafu nitamuomba mama asogeze siku zako za likizo mbele.
Mimi mwenyewe nitakupeleka nyumbani.” Alishangaa huyo binti, akabaki kama
amepigwa na shoti ya umeme.
“Ukiondoka tu kesho, jua nitaharibikiwa vibaya sana.
Naomba ubaki. Nipo kwenye mabadilisho, na ili niweze kufanya vizuri ni nijue
upo na mimi na upo upande wangu.” “Mimi nipo na wewe siku zote kaka.”
“Nashukuru. Basi jua sasahivi nakuhitaji zaidi. Naomba ubaki, kesho
tutazungumza zaidi.” “Ila na tiketi nilishakata, na baba pia anajua kama naondoka
kesho.” “Nitazungumza nao. Usiwe na wasiwasi. Sawa?” “Sawa.”
“Naomba nikuombe jambo la mwisho.” Emelda akatulia
akimwangalia kama ambaye bado hajamuelewa sawasawa. Siku chache tu zilizopita
alikuwa akiishi naye kama hayupo! Gafla anambembeleza! Emelda akabaki
amevurugikiwa ila akimsikiliza kwa makini akihofia asije jichanganya. Asijue
kwa Mungu miaka 1000 ni kama siku 1 tu. Hubadilisha mambo na kufanya kwa wakati
wake.
“Ezra anatakiwa kuchumbia sasahivi. Hatachumbia bila mimi
kuwepo. Na mimi siwezi kuwepo pale bila wewe kuwepo.” Aliona wazi jinsi
alivyomchanganya. “Tafadhali Emelda.” “Nilimuomba mama huko nisiende kaka.”
“Kwa nini?” Akamuona ameinama. “Eti Emelda?” “Sijui! Ila sikuwa nikitaka
kwenda. Naishia kuumia tu wakati wengine wakifurahia. Si sawa.” “Pole. Lakini nikikuomba
twende wote?” Simu ya Ezra ikaanza kusumbua hapo. Akamwangalia anavyoangalia
simu yake na kurudisha mfukoni. Kisha akamuona anatuma ujumbe mfupi na
kurudisha tena mfukoni.
“Kwani huko mlitaka msaada gani?” Akajua ni kazi. Wanataka
akawafanyie kazi. “Naweza kwenda kusaidia chochote. Mimi nilidhani ni
kuhudhuria tu, ndio nikakataa kwenda. Ila kama ni kazi, naweza kwenda.” “Hapana.
Nataka uwe na mimi. Na safari hii hautakuwa peke yako, utakuwa na mimi.
Nitaweka mazingira usiumie.” Hapo ndipo akamchanganya zaidi. Akabaki ameduaa.
Na hapo napo Junior
akazidi kumuangalia na kushangaa aliweza vipi kutooana uzuri wake. “Ni sawa
tukizungumza kila kitu kesho? Ila usiku huu naomba twende ili Ezra achumbie.
Huendi kufanya kazi, unakwenda kama mgeni wangu mimi. Mimi ndio nakuhitaji.
Nataka uwe na mimi kwenye hili.” Mwili mzima wa Emelda ulianza kupatwa baridi.
Kauli hii si ya kikaka kabisa! Hata yeye aliweza kugundua.
“Emelda?” “Abee!” Wakati anaitika simu ya mzee nayo ikaingia.
Ikabidi apokee. “Sikukwambia mimi kama usipoweka mambo
yako sawa, unazuia ndoa mbili?” “Nakuja baba.” “Tafadhali uje Junior. Mwenzio
ameshindwa kuchumbia, anakusubiria wewe. Na hapa mambo yamekaribia kuisha, wote
tunaonekana watu wa ajabu tusio na mipango.” “Samahani baba. Nakuja sasahivi.”
Akakata simu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
0 Comments:
Post a Comment