Ilipofika mida ya saa mbili kasoro Ezra na Jelini wakafika
hapo. Junior alishamwambia tokea wapo kwa wazazi kuwa anampeleka hospitalini.
Alichofanya ni kwenda kumchukua Jelini na kwenda naye huko. Akabakia yeye ndio
dharula yake ya kwanza hata hapo hospitalini.
“Vipi?” “Aisee homa ilikuwa kali sana na anatapika kweli!” “Malaria hiyo!” “Kama kawaida ya mama, kaanza kumpa dawa hata hajapimwa!” Wakacheka kwa masikitiko. “Mama! Hajaacha tu?” “Naona ni kasumba iliyokataa kutoka. Ndio amechukuliwa damu, tunasubiria majibu. Vipi Jelini, mbona leo umepoa?” “Mimi maneno mengi nje ya hospitali. Nikishaona hivi halafu na sindano ipo mwilini mwa mtu, ndio nazidi kupoteza uchangamfu. Haya sio maeneo yangu kabisa.” Wakaanza kumcheka.
“Ila poleni.” “Asante.” “Ila huyu kama mimi namfahamu. Si
anakuaga kule kwa watoto siku za jumapili?” Jelini akauliza akimwangalia
Emelda. Ezra na Junior wakatizamana. Hawana uhakika maana huyo ni mtu wa mwisho
kabisa waliyekuwa na taarifa naye japo ndiye aliyekuwa akiwalisha kila siku ya
ijumaa baada ya maombi ya siku nzima.
“Au nimekosea? Maana mwanzoni pale kanisani walitaka Jeremy
awe anakwenda kwa watoto. Huyu akampokea. Nilipoenda kumchukua Jeremy, akaniambia ni mtoto mwenye tabia nzuri.
Nikamtania nikamwambia ni kama mama yake. Akacheka na kuniambia tumefanana naye
pia. Ni mtaratibu sana huyu dada. Au nimemfananisha?” Kimya. Akaendelea kuvuta
kumbukumbu. “Na nilishamuona na mama mchungaji, kwenye harusi ya Ester.
Akicheka mashavu yake yanabonyea hivi.” “Basi ni yeye.” Wote wakaitika kwa
pamoja na kucheka. Maana Jelini alipiga ikulu. Kweli Emelda akicheka anabonyea
mashavu.
“Nilijua tu! Poleni sana. Kumbe ni dada yenu anaishi kwa
mchungaji!?” Kimya wakishindwa kujibu hilo. “Poleni.” “Asante. Vipi kazi
lakini?” “Namshukuru Mungu, mambo si mabaya. Na wewe?” “Siwezi kulalamika.
Nipo.” “Njoo tukae hapa Ezra, tusiongee sana, mgonjwa apumzike.” Wakaenda kukaa
kochi la pembeni, refu. Wakatulia. Ezra na Junior wakaangaliana, Ezra
akatingisha kichwa kama ambaye haamini, Junior akacheka kimyakimya.
Hope.
Huku kanisani baada ya bible study mchungaji na mkewe wakaelekea ofisini ili kukutana na Hope. Hakuwepo kwenye mafundisho, ila akafika hapo kama aliyevizia muda wa kipindi uishe, akutane na mchungaji. Hakutegemea kumkuta na mama mchungaji. Akampokea kwa furaha tu japo alionekana amenyongea. Mchungaji hakutaka mengi. Akamshukuru kwa huduma yake hapo kanisani, kujitolea kwake na kumwambia, “kama kungekuwa na watenda kazi kama wewe hata wanne tu katika kila kanisa, hakika tungekuwa mbali. Wewe ni mtenda kazi unayefanya kana kwamba unafanya kwa Bwana kabisa. Kwa hakika Mungu wangu asikupungukie.”
“Na tuna zawadi yako kutaka kukushukuru.” Akaongezea mama
mchungaji, lakini kwa Hope akashangazwa kwa nini hata haulizwi ni kwa nini
anaacha! Alitarajia mazungumzo ili apate pakujieleza na kuomba abakie.
Asijue usiku huo una mengi, wanawahi kwa mama Jema. Na pengo
lake limeshazibwa. Hawakumuulizia la kheri wala la shari zaidi ya
shukurani kubwa sana kwake na hiyo zawadi. Na yeye akakabidhisha funguo zote, ila
kabla hajatoka, mama mchungaji akamuwahi. “Hope binti yangu, milango hapa ipo
wazi. Na hapa ni nyumbani mama. Ukipumzika. Ukajisikia unayo nguvu ya
kuendelea, tafadhali usiache kurudi. Sisi bado tunakuhitaji. Hii kazi ya
Mungu ni kubwa mwanangu, na watenda kazi ni wachache. Tunakuhitaji binti
yangu.” Hilo likamfurahisha sana Hope. Angalau akajisikia vizuri. “Nimeelewa
mama. Acha niweke mambo sawa, akili ikitulia, nitarudi tena.” Wakambariki na
kuondoka wakiwahi kwa mama Jema.
~~~~~~~~~~~~~~~
Wakiwa kwenye gari ujumbe ukaingia. ‘Nimemkuta
Emelda anatapika sana na homa ipo juu, tupo hospitalini.’ Mama yake
akasoma kwa sauti. “Wapigie na waambie tukitoka huko, tutawapitia.” Mama mtu
akapiga, akaweka spika kama kawaida yake ili asijirudie kwa Ezra akijua lazima
wapo pamoja. Wote wapate ujumbe kwa pamoja. “Tukitoka
kwa mama…” “Tupo na Jelini hapa.” Junior akawahi asije toa siri.
Akacheka.
“Na mimi nimekuja kuona mgonjwa mama.” “Afadhali.
Ndio maana kanisani sijakuona!” Akamchokoza akijua haendi kanisani vipindi vya katikati. “Mwenzio naanza ijumaa hii, na nafunga na Ezra.” “Na
mimi Jelini!” Junior akamuwahi akilalamika. “Sijakusahau Junior! Na Junior pia, halafu sisi wote watatu tunakuja kanisani
kwenye kipindi cha maombi.” Wakacheka.
“Ingekua mimi, ningemwambia mchungaji ijumaa hii
ndio iwe siku ya kutoa ile ahadi yake. Tunafunga pamoja, halafu mnakuja
kufuturu kwa mama Jema.”
Wote wakacheka kwa pamoja na mchungaji.
“Jelini!” “Sasa mama wewe umeshawahi
kula ndizi iliyopikwa na mchanga mwenyewe? Machalali?” “Sijawahi Jelini,
mwanangu.” “Umeona? Ningekuwa mimi ningembembeleza mchungaji na kumpaga mpaka
akubali. Unabakiwa na kazi ya kufunga tu, nakuomba. Chakula mnakula kwa mama
Jema, halafu mnaenda kulala tu. Au wewe unaona wazo baya?” “Naona wazo sio baya. Acha ‘nimpange’ mchungaji.” Akamuigilizia.
“Ndio maana mimi nakupenda.” Wote wakacheka.
“Jelini? Wewe si umesema hospitalini panakuogopesha huongei
sana?” “Mimi mwenzio nataka kutembelewa na mchungaji, nyumbani kwetu, ndio inabidi kuchangamka. Ila na wewe
unakaribishwa Junior. Wewe wangu.” “Sawa Jelini.” Wakacheka na kuagana kwamba
watawapitia na hapo, Jelini asijue anajipangia surprise yake mwenyewe.
~~~~~~~~~~~~~~~
Ilipofika muda wa saa nne usiku mchungaji na mkewe wakawa
wanaingia hapo. Wakasimama wote kusalimia. “Kumbe bora ulivyomleta wewe! Mimi
alinikatalia huyo! Alikuwa anatapika kuanzia asubuhi. Kila nikimwambia twende
wakakuchome sindano, hataki.” “Sasa kwa nini umwambie mambo ya sindano wakati
unajua anaogopa?” “Sasa ameishia wapi? Si yaleyale tu. Hapo si ana sindano!”
“Usingemwambia sindano, angekuja mama! Halafu ndio aje akutane na sindano
huku.” Kama kawaida ya Ezra hakosi neno la kuchangia kwa Junior.
“Acha nikwambie Jelini mwanangu. Huyu na Noah wote hawataki
sindano. Ukiwatajia tu hospitalini, akili inakimbilia kwenye sindano.” “Basi na
mimi nipo hivyohivyo mama yangu. Hospitalini sipapendi, nipo hapa mpaka
sasahivi sababu ya Ezra na Junior. Ila si vinginevyo.” Stori zikaanza, Ezra,
Junior na mchungaji wakatoka nje. Wao wakabaki hapo ndani wakisubiria dripu
iishe, waondoke.
Baba na Vijana wake.
“Mambo yamekwendaje kwa mama Jema?” “Kule unajina kubwa!”
“Acha baba!” Wote hawakuamini, maana alinyimwa kuwepo kwa Jeremy. Ikawapoozesha,
kumbe! “Yule mama anaonekana amekufurahia na yupo tayari kwa wewe uoe binti
yake wakati wowote. Anasema humdharau binti yake. Unampenda na kumjali kwa
dhati. Umemfanya atulie na anasema Jelini anakupenda sana. Tukampa wazo hilo la
ijumaa. Amelipenda kwa sababu anasema kwao jumamosi ndio siku kubwa ya biashara
zake na binti yake. Kwa hiyo ataandaa mazingira mazuri nyumbani kwake, ili
ufanye unachotaka.” Ezra alifurahia sana.
“Asante baba yangu.” “Kwako naona kunakaa sawa. Ila naona
kwa Junior tunaanza tena upya! Ni nini kinaendelea Junior? Kwa nini
urudishiwe pete ya uchumba ambayo Hope alikuwa akijivunia nayo sana?” Ezra
akamtizama kama kumkumbusha aseme ukweli.
“Yeye alipenda vitu vyangu kuliko mimi
mwenyewe baba. Na hilo limekuwa likiendelea kwa muda mrefu nikiendelea
kulifungia macho mpaka siku ya jumapili ndio kama nimefunguliwa macho. Hope
amenipuuza kwa muda mrefu sana akiamini sitaweza kuja kumuacha kwa
sababu ya jinsi nilivyo, na anajua nitahofia kuchafua sifa pale
kanisani. Akajiaminisha na kunidharau huku akinitumia atakavyo.
Lakini baba, na mimi nataka kupendwa na kuheshimiwa kama wanaume wengine.”
“Unataka kuniambia Hope haku..” “Kile ulichokiona siku ya
harusi ya Ester ni muendelezo wa mambo mengi na mimi kufumbia
macho baba yangu. Muulize Ezra kama nasingizia. Ana jeuri fulani hivi
ambayo unaweza kuifananisha na ujasiri lakini sio ujasiri. Ni kujiaminisha.
Sasa safari hii naona ni kama amenisaidia kunifikisha mwisho.” “Junior! Mwisho
tena!?” Baba yake akashangaa sana.
“Hakika ile pete haitarudi kidoleni mwake tena.” Mzee
akamwangalia Ezra. “Na mimi nasikia sasahivi mzee wangu.” “Kwamba wewe hukuwa
ukijua?” “Kwa sehemu na alikubali kesho tuzungumze akiwa amenipa muda wa
kufikiria kwanza. Hivi sasahivi na mimi ndio nashangazwa na haya maamuzi.” “Nimegundua
moyo wangu umehama kabisa. Na tafadhali kumbuka maneno yako baba.
Ulisema hutatutafutia mke.” “Umepatwa na nini Junior!?” “Baba, na mimi
nataka ndoa kama yako! Hilo ni kosa!?” Akauliza kwa ukali kidogo. Mzee
akabaki akimtizama.
“Ila swala la ndoa ni la maisha yote yaliyopo hapa duniani.
Nafikiri Junior ana haki yakupendwa na kujaliwa baba yangu. Hope ni kama tu
Hellen. Tulimfungia macho tukidhani ndivyo inavyotakiwa kuwa, kwa kuwa kwanza
hatukuwa na mfano mzuri wa mahusiano, ndiye alikuwa msichana wangu wa kwanza,
tukadhania pengine nikijitahidi kumuonyesha upendo kwa kumpa na kufanya
kila anachotaka na nikija kumuoa itabadilika.”
“Lakini kumbe alikuwa akinitumia, na akaniacha
kikatili kiasi kile! Mtu anayekupenda kwa dhati anakuheshimu na kujali hata
hisia zako. Haiitaji kumfundisha kukujali au kumuonyesha upendo mwingi ili
kukupenda. Nimeliona kwa Jelini. Kama mapenzi yapo, yapo tu baba yangu. Kwa
hiyo nafikiri Junior ndiye ana haki ya kusimamia anachojisikia.” Ezra
akamtetea huyo Junior japo naye ndio anasikia hapo kama ndio MWISHO Hope.
Lakini bado akasimama naye akimtetea.
“Hivi nyinyi mmehesabu garama ya hayo maamuzi yenu
lakini?” “Japokuwa maamuzi ni ya Junior. Na wote tunakubaliana muoaji ni
Junior, anahaki na kuchagua mke wake. Kama na wewe mzee wetu utakubaliana na
hilo na ukakumbuka ulituahidi hutatuchagulia wake, basi kwenye madhara
ya hili tunaomba utusaidie kusimama na sisi.” Ezra akawa
anazungumza, amemkingia kifua Junior kama yeye ndio muoaji.
“Tunajua si kwenye jamii tu, hata kanisani hapatakuwa
sawa. Tunahitaji msaada wako kusaidia hili liishe vizuri japo inaweza isiwe kwa
amani.” Mzee wao akawatizama na kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Junior akahema kwa nguvu. “Nashukuru Ezra.” “Hapana Junior.
Naomba tuzungumze. Na tafadhali nisikilize. Maana umenibadilikia.” “Utanisamehe
Ezra. Ila nimeshindwa kuendelea kumfumbia macho Emelda. Nimejisikia kuumia na
kuona nimemtelekeza kwa muda mrefu wakati yeye hajawahi kunikatia tamaa!
Nimemkuta mgonjwa, yupo peke yake wakati mimi nipo! Hakika sitaendelea
kumfumbia macho tena. Kwanza sina sababu yakufanya hivyo. Kwa nini!? Kama
niliweza kuweka muda wangu mwingi kwa watu baki, ni zaidi kwake.”
“Hope hakuwa mtu baki. Ni mchumba ambaye ulimchumbia
kanisani.” “Alikuwa mchumba. Tafadhali tusirudi tena nyuma. Na katika
hili nakuhitaji Ezra.” “Lakini taratibu Junior! Tafadhali, taratibu.” “Siwezi
tena. Kwa hiyo tutafute njia ingine. Lakini ‘taratibu’ hapana.”
Junior akaweka msisitizo.
“Kwamba umeshampenda?” “Nafikiri.” “Junior?” Akaanza
kucheka. “Acha kunichanganya.” “Mimi nahisi nimepatwa na hisia za tofauti, na
sijawahi jisikia hivi. Hakika siwezi kujisaidia Ezra. Akilia, nasikia kuumia
kupita kiasi! Mimi si mtu wa kushika matapishi, lakini yake nimeshika, tena bila
ya kufikiria! Mwili mzima ulisisimka nilipomshika kumpima homa.”
“Junior!” “Sasa si ndio nakutoa kwenye kuchanganyikiwa? Hapa
nakusaidia wewe. Halafu alipokuwa amelala nikamshika kidogo, hakika sijawahi
jisikia hivyo! Nusura nimpakate kichwa nimbeleze alale akiwa miguuni kwangu.”
Ezra alimtizama kama anayeshindwa kummaliza, Junior hana mbavu.
“Kumbe kupenda ndio raha hivi!” “Naomba tuhitimishe
na Hope kwanza.” “Sawa. Kwa hiyo wakati wewe ukiweka mipango ya kuhitimisha,
mimi naendelea na Emelda.” “Umepatwa na nini Junior?!” “Wewe ndio unashindwa
kunielewa Ezra na unanisikitisha. Nimekwambia sitaendelea tena kumpuuza Emelda.
Sitapoteza muda wangu kwa watu baki. Emelda kwanza, ndio mengine
baadaye. Au hutaki tuoe tena?” Mara daktari akawa anaingia chumba
alichopumzishwa Emelda.
Junior akataka kikimbilia, Ezra akamuwahi. “Naomba usubiri
kwanza.” “Ni nini tena!?” “Emelda ataruhusiwa kurudi nyumbani.” “Najua.” “Najua
unajua, kwa hiyo?” “Nitamru..” “Hapana Junior. Hutamrudisha wewe
nyumbani. Acha wazazi warudi naye.” “Ezra!” “Subiri kwanza Junior. Kesho
wanapotoka mida yao ile ya saa nne, wewe ndio urudi nyumbani ukamwangalie.
Lakini usiku wa leo, tafadhali naomba uishie hivi. Tafadhali Junior. Baby
steps.” “Hapo hapana.” Akamtibua.
“Basi, basi! Sio baby steps. Tutembee hatua moja
baada ya nyingine.” “Hapo sawa. Ila si kwa kunichelewesha.” “Sawa Junior.” Hapo
wakakubaliana, na kurudi ndani.
Daktari akamruhusu, akiwa ameridhia arudie dawa ya malaria
usiku huo baada ya kula. Ilikuwa ni ya kunywa mara moja tu, ila akaandikiwa
dawa za kuzuia kutapika tena. Wazazi wakaondoka na Emelda. Ezra na Jelini.
Junior akaondoka peke yake.
~~~~~~~~~~~~~~~
Alipofika tu nyumbani ujumbe ukaingia. Alikuwa Emelda.
Safari hii akaona. Akataka kumsikia na kuelewa. Akaweka kila kitu pembeni,
kisha akaenda kukaa kabisa ili asome asije akokosa ujumbe mzima. Ila ujumbe
ulikuwa mfupi tu. ‘Nashukuru kaka.’ Junior
akarudia tena na tena akitamani kama angeandika zaidi.
Akaamua kumjibu kwa swali. ‘Naweza
kupiga?” ‘Mama ananiandalia chakula. Pumzika tu kaka. Sisi huku tupo salama.
Ila usiache kula.’ Emelda akajibu. ‘Nataka
kuzungumza na wewe.’ Moyo wa Emelda ukajaa furaha, japo hakujua anataka
kuzungumza nini. Ujumbe mwingine ukaingia. ‘Au
nakusumbua, unataka kupumzika?’ Ni Junior, kaka yake wa siku nyingi. Huo
ujumbe ukawa si kawaida yake. Kwanza huwa hajibu jumbe zake. Usiku huo
anawasiwasi wa kumsumbua! Emelda akapatwa na sintofahamu.
‘Hapana kaka. Hunisumbui kabisa. Nakuonea huruma,
najua unatakiwa kuamka alfajiri sababu ya kazi.’ Junior akasikia kujaliwa huyo, kana
kwamba ni mara yake ya kwanza wakati ni kawaida ya Emelda ila hakuwahi
kumuelewa wala kumsikia. Akamjibu huku akimfikiria. ‘Usijali.
Naomba kuongea na wewe kabla hujalala na pakiwa pametulia. Nijulishe.’
‘Nitafanya hivyo.’ Akajibu na kuficha simu chini ya mto ili mama yao
akiingia asione.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akaamua kuoga kabisa na kujiweka kitandani akisubiria simu
ya Emelda. Baada ya muda akaona simu yake. Akakata, kisha akampigia yeye. “Umekula vizuri?” “Ndiyo.” Akajibu kwa utulivu. “Na umeshiba, hujatapika?” “Sijatapika. Asante kunipeleka hospitali.
Nilikuwa namkatalia mama.” “Usiwe unaugua peke yako. Uwe unanijulisha.” “Unakua
na mambo mengi kaka. Wakati mwingine inakuwia ngumu kunisikia.” Emelda
akazungumza kwa upole, lakini Junior akamuelewa.
“Nakuahidi kubadilika. Kuanzia sasa nitakuwa nikikusikia.
Ni ahadi nakupa.” Emelda
hakuamini! Akajisikia machozi kumtoka. Alishamfungia huyo Junior,
akimuomba Mungu amfungue macho kwake, lakini wapi! Mpaka akakata tamaa. Akajua amebakia
kumchukulia ni msichana wa kazi za ndani tu. Hamuoni kama ni mwanamke anayeweza
kuwa zaidi ya hivyo.
“Umenisikia?” “Ndiyo.” Akajibu kwa heshima. “Kesho nitakuja kukuona. Nikuletee nini? Niambie chochote
unachojisikia kula. Na hunisumbui.” “Unamjua mama anavyopika. Kutakuwa na
vyakula vingi. Usihang…” “Sio usumbufu. Huna hamu na kitu chochote?” “Sina
kaka. Pengine sababu ya kuumwa. Sina hamu na chakula kabisa.” “Basi nitakuletea
hata matunda. Pumzika. Nitakuona kesho.” “Asante kaka. Uwe na usiku mwema.” “Na
wewe pia, Emelda.” Simu ikakatwa na kuwaacha hao wawili wote mapigo ya
moyo yakienda kasi.
Alhamisi.
Asubuhi hiyo alimkuta Ezra alishafika ofisini. “Nimezungumza
na Hope, nimemuomba leo mchana mkutane tena.” “Hapana Ezra. Leo mchana nina
ratiba ya muhimu sana.” Akakataa bila ya kufikiria. “Hivi unafikiri
utamalizaje swala lako na Hope?” “Sijakataa, ila isiwe leo mchana.” Akafikiria
kwa haraka, kisha akaongeza. “Na kesho pia sitaweza.” Ezra akabaki
akimwangalia.
“Ni nini sasa?” Umepatwa na nini Junior!?” “Mbona sijakataa!
Ila si leo wala kesho. Pengine tufanye jumamosi, mida ya saa nne asubuhi.”
“Hapo sasa unaongea. Sasa utamwambia nini?” “Kwamba naahirisha uchumba.”
“Hivyo tu?!” “Basi niambie wewe unavyotaka nikamwambie, nitamwambia. Ila kwa
sasa sina sababu ingine. Na nataka kumaliza majukumu yangu hapa kwa haraka ili
saa nne niende kwa Emelda kama ulivyosema jana.” Hapo akamkazia sauti
kama usinigeuke.
“Kama unakwenda saa nne, inamaana mida ya saa sita utakuwa
umesharudi!” “Hapo sasa unanigeuka Ezra, na si kawaida yako. Jana
uliniambia nini?” “Wewe unataka ukakae nyumbani mpaka ukutwe pale na wazazi!?”
“Sina ninachoficha tena.” “Hapana Junior. Mpaka uhitimishe kwanza na
Hope, ndipo uanze jambo jingine. Mfikirie mama.” “Sawa. Lakini sasahivi nina
mgonjwa, siwezi kukutana na Hope. Mwambie jumamosi.”
“Sawa. Jumamosi saa nne asubuhi. Nyumbani kwako?” “Hapana!”
Akashituka kabisa. “Kwa nini afike kwangu na tunaachana!? Tafadhali iwe sehemu
ingine tena nashauri iwe ya wazi kabisa. Tunaweza kwenda wote.” “Hatutafanya
hivyo! Huo hautakuwa ustaarabu. Ulitongoza mwenyewe, nenda kaitimishe
mwenyewe.” Akamkatalia.
“Sawa. Lakini sio nyumbani kwangu. Hapo hapana Ezra.”
“Kwa nini?” Akamuona anasita. “Junior?” “Sasa anafuata nini kwangu?” “Junior?”
Ezra akasisitiza akiwa anajua kuna anachoficha. “Nitakuwa na Emelda. Nataka
mida ya saa sita, aje nyumbani tuzungumze. Sasa sitaki aje akute hata dalili za
Hope.” Ezra akachoka kabisa.
“Yaani ile saa nne ninapokwenda kukutana naye kwa
kuhitimisha, nampelekea kila kitu chake alichoacha kwangu, tunaagana kwa
amani. Simdai, hanidai. Hakaribishwi tena kwangu.” “Hope atajua kwa hakika ule utabiri wangu
juu yenu haukuwa utabiri, nilijua kinachoendelea. Nikabaki kumsanifu
tu!” Akawa amemchanganya Junior.
“Utabiri gani tena!?” “Umeniponza Junior!” “Nini tena!?”
“Mimi nilimwambia juu ya mfano wa kitabu cha Ester. Juu ya malikia Vashti…”
Kabla hajamaliza, Junior akawa ameelewa. Acha acheke. “Wewe nabii aisee!” “Acha
kucheka Junior! Hope atajua muda wote mimi namuwekea mipango ya kukutana na
wewe, lakini najua yupo Emelda!” “Huna jinsi ya kurekebisha hilo.” Ezra
akabaki akimwangalia.
“Wewe endelea na mipango ya saa nne, ya siku ya jumamosi.
Kama hataweza, basi tena mpaka jumatatu. Na isiwe kwako.” “Unajua kwangu
siwezi kumruhusu tena, sababu ya Jelini.” “Basi na mimi sababu ya Emelda.”
“Unaiga Junior!” Hana mbavu kama mazuri.
“Wewe changamka, tuoe, tutulie. Tengeneza mazingira
mazuri, jumamosi tufunge ukurasa wa Hope. Kesho unachumbia wewe. Jumapili
tunatangaza uchumba. Mnaombewa. Watu wakishamaliza maneno kati yangu na
Hope. Pakipoa tu pale kanisani, namchumbia Emelda. Ndani ya miezi
mitatu, tunaoa, tuanzishe familia. Au unasemaje?” Hapo akampata Ezra.
Junior wa mipango, Ezra akacheka. “Hatutakuwa tumeharakisha
sana?” “Pesa tunayo. Wanawake wanaotupenda tunao, tatizo ni nini?” “Namaanisha
kwa upande wako na Hope, mpaka Emelda, kisha ndoa? Watu hawatakuelewa Junior!”
“Nani amekwambia sasahivi wananielewa? Mimi shida yangu Emelda. Akinielewa yeye,
akukubali ndoa, naoa. Mengine nitajua mbele ya safari. Kwanza
nimeshapata jibu la swali lako.”
“Kwamba kama unampenda?” “Ndiyo. Nikiongea naye najisikia
tofauti. Furaha ya ajabu! Bwana yule binti ananipenda na kunijali Ezra!”
“Kwamba baada ya pale ulimpigia simu tena?” “Sio kwa haraka! Mama alipoenda
kulala! Wewe vipi Ezra!” Ezra akatingisha kichwa kwa masikitiko, Junior hana
mbavu.
~~~~~~~~~~~~~~~
Itaendelea….
0 Comments:
Post a Comment