“Nakwambia sijalala usiku nikimfikiria yeye na aliyokuwa
akinifanyia. Alihangaika kweli, lakini kinachoniuma, nakumbuka siku ya
mwisho karibia natoka, alinikuta peke yangu pale chumbani wewe umeenda kulipia
au sijui ulikuwa wapi! Aliniomba rasmi kuwa anaomba nikitoka pale, nikakae
nyumbani kwa siku chache mpaka nipate nguvu.” Junior akatingisha kichwa kwa
masikitiko.
“Nini?” “Aisee mpaka najichukia. Maana alijitahidi kabisa
kuniomba, ila alijawa hofu, mimi nikapuuzia.” “Yeye alisema ni kwa nini alitaka
ukaugulie nyumbani?” “Alisema ingekuwa rahisi ‘kwa mama’ kuniona
na kuhakikisha nakula vizuri na nakupata mapumziko yakutosha.”
“Alimtumia mama?” “Ndivyo alivyoniambia. Sasa ukumbuke wakati ule ndio
nimeanzana na Hope, akili ilikuwa haipo kabisa. Nikamjibu tu kwa kifupi,
nitakuwa sawa. Akapoa kabisa, hakuzungumza tena, akaondoka.”
“Sasa iliyokuwa mbaya, ambayo nakumbuka ilikuwa siku ile
namchumbia Hope. Yaania nilikumbuka jana, hakika nilishindwa kulala.”
“Ilikuaje?” “Yule binti hakula Ezra. Maana kwanza nilimuona pale kanisani kama
macho mekundu sana. Kama aliyekuwa
akilia. Sasa kulikuwa na hekaheka watu wakitupongeza, nikashindwa kabisa
kuzungumza naye. Jioni si ndio mama akawa amealika marafiki, familia ya kina
Hope na wale majirani kwa chakula kwa ajili ya kufahamiana zaidi. Sasa kuna
kitu nilikuwa nafuata jikoni, nakumbuka kumsikia mama akimwambia ni lazima ale.
Hawezi kuendelea kufunga siku muhimu kama ile.”
“Sasa mimi nikawapuuza nikijua ni kawaida ya mama na wale
wanae pale. Noah na Emelda. Kutwa kuwabembeleza. Nikafanya yangu, nikarudi
sebuleni. Sasa soma hizo jumbe ndio utakubaliana na mimi kama aliumia baada ya
kuona nimechumbia, na utagundua huyu binti bado ananisubiria mimi.” Kazi
ya kusoma hizo jumbe ikaanza. Ezra alianzia mwanzo kabisa, taratibu akisoma.
Junior akabaki ametulia.
Ezra alisoma mpaka mwisho na kubaki ameduaa. “Haiwezekani
Junior! Uliwezaje kutoelewa!?” “Hapo unazungumza kwa sababu nimekwambia haya.
Lakini simama upande wangu, na vile Emelda alivyo na anavyotuheshimu. Angalia
jumbe zake zilivyojaa heshima. Ni ‘kaka’ wakati wote. Hata akiwa ananipa
maji kanisani, au akileta zile juisi pale kanisani unaweza fikiria ametumwa na
mama.” “Kwamba na juisi zile wanazotuma kila jumapili wakija kanisani ni yeye?!”
Ezra akawa bado haamini. “Nakuhakikishia ni yeye. Na zile chupa zakutopooza
anazowekaga mle, ni yeye. Mama yako hana habari hata.”
“Sema zilituchanganya maana ni ladha kama juisi anazotengeneza
mama kabisa. Na chakula akipika Emelda ni kama amepika mama, ndio maana inakua
ngumu kugundua. Na upaji wake wa kitu ni rahisi kufikiria ametumwa. Maana
anaweza kunikuta nipo busy pale kanisani, anapenyeza chupa mkononi mpaka
nimgeukie. Ndio ananipa na yako, napo nashukuru na kuendelea na yangu nikijua
mama ndiye amemtuma maana mama ndiye…” “Anayependa kusisitiza maswala ya kunywa
maji.” Akamalizia Ezra.
“Sasa kumbe ni kwa mwanae yule mnywa pombe, ndiye
anamsisitizia maji na chakula. Na kuhakikisha baba hapungukiwi maji kanisani.
Lakini sio sisi.” Ezra akacheka akifikiria. “Na imekua kasumba yake. Kila maji
unayoona nakupa siku za jumapili ni yeye Emelda anakuwa amenipa.” “Na haachi
kuja na chai yetu kila siku ya ijumaa kwenye maombi!” “Ewaaah! Sasa usifikiri
ni mama. Ni yeye mwenyewe.” Ezra akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha.
Akamwangalia, wakabaki wakiangaliana. “Sasa utafanyaje
Junior!?” “Ninachojua sasahivi ni mgonjwa, naenda kulipa fadhila.” “Subiri
kwanza Junior. Naomba fikiria kabla ya kuanzisha jambo jingine.” “Wewe umesoma
hizo jumbe?” “Ndiyo.” “Haya, fungua na kwenye chat zangu zote na Hope,
kisha tulia fikiria mahusiano yangu na Hope. Kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Kisha
nakupa nafasi ya kuja kunishauri. Ila sio leo. Nataka upate muda wa kutafakari.
Halafu uje uniambie kama naanzisha jambo jipya, au napokea jambo ambalo nililifungia
macho.”
“Junior?!” “Unashangaa nini na wewe umepewa nafasi ya
kunishauri? Mimi siendi kufanya jambo la ajabu. Emelda ni mgonjwa.” “Anaumwa
nini?” “Mama ameniambia eti baba anamlaumu Noah, amemuambukiza malaria ya baa.”
Wakaanza kucheka.
“Kwa hiyo ni malaria. Sasa mimi nawajua pale nyumbani,
wanaweza wakawa wamepuuza, wanamuombea tu. Nataka niende nikamuone mimi
mwenyewe.” Ezra akabaki akimwangalia, Junior akaanza kucheka kama sio yeye
aliyekuwa amekasirika.
“Acha kunitizama hivyo!” “Unauhakika Junior?” “Kadiri
ninavyoendelea kufikiria, ndivyo ninavyopata uhakika Ezra. Huyu binti amenijali
kama hivyo unavyomfanyia Jelini. Tofauti yetu ni mimi nimekosa
shukurani.” “Nafikiri si kukosa shukurani, ila ni kutambua,kutoona na
kumwambia yeye mwenyewe kwamba unathamini anachokifanya.” Ezra akatulia
na kurudia kusoma jumbe moja iliyokuwa imemgusa.
“Junior!” Junior akamwangalia. “Ni kama huyu binti anakusubiria!”
“Ewaah! Kuna ujumbe hapo ni kama ameniambia kwamba hatachoka kunisubiri.”
“Na unakumbuka hata Ester alimwambia kwamba na yeye akue, aondoke pale ndani,
aache kunyang’anyana ziwa na Noah, unakumbuka alimjibu Ester kuwa yeye atakuwa
mtu wa mwisho kuolewa mle ndani? Tena akasema hivi, wote tukishaoa, ndipo
atajiridhisha kuwa zamu yake ndio imefika, anatakiwa kuondoka. Unakumbuka
Junior?” “Nakwambia ndio ilikuwa kazi ya jana hiyo. Nimekumbuka mengi,
nikashindwa kulala. Na Emelda ni mzuri tu. Asingeshindwa kuolewa na kuondoka
pale ndani.” “Sawasawa. Najua najirudia Junior. Lakini tafadhali niambie
utafanya nini?”
“Nimeshakwabia na najua huna tatizo la kukumbuka.” “Acha
kucheka Junior! Ujue hili jambo ni zito sana? Umeliangalia kwa kona zote?”
“Mpaka kanisani, wazazi, Hope na wengine wote. Ila ninachojua kila jambo
linatokea kwa sababu. Mimi sikutaka Hope anirudishie pete!” “Junior! Unajua
hilo halikuwa lengo lake.” “Then, too bad. Hainihusu. Maandiko
yanasemaje?” “Tafadhali acha kunukuu maandiko kwenye kipindi kama hichi! Mimi
nimeshachanganyikiwa.” Junior hana mbavu.
“Maandiko yanasema, ‘everything, works together for good, for those who
loves God.’ Sasa..” “Junior!?” “Sasa mimi ndiye niliyeandika bibilia
jamani!? Unamzuiaje Mungu kufanya yake katika kunipatia mema? Au wewe huamini
katika maombi tunayoomba kila siku?” “Tafadhali taratibu Junior. Please.”
“Sawa.” Akakubali akicheka.
“Naomba niagizie matunda kama unayomnunulia Jelini.” Ezra akabaki
akimtiza. Junior amebadilika, anacheka kama siye yeye aliyekua amepoa. “Kwamba
wewe umefurahia kurudishiwa pete au? Mbona sikuelewi?!” “Soma andiko hilo Ezra.Warumi 8:28 ‘nasi twajua
ya kuwa katika mambo YOTE Mungu hutenda kazi pamoja na
wote wampendao, katika kuwapatia MEMA, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake’.
Hilo ni neno la Mungu. Sasa mimi kosa langu ni kufurahia neno!? Tena naomba
ongeza na maua.” “Maua hapana Junior. Hapo HAPANA. Peleka matunda
kwanza.” “Sawa.” Akakubali na kurudisha macho kwenye kompyuta yake, akicheka.
Ezra akatulia kama amepigwa na butwaa. “Sikusikii ukiagiza
matunda Ezra! 9:45 mimi natoka hapa, navizia muda wa wazazi kutoka pale ndani,
ili kuepusha maswali mengi.” “Hapa namuwazia mama na kumuhurumia. Maana hiki
ndicho kile kipindi mzee anakabidhisha watoto wakiume wote ni wa mama. Na huwa
hajui alikosea wapi, maana yeye amekamilisha kazi yake vizuri kwa
Ester.” Junior hana mbavu.
“Ila mama anampenda sana Emelda.” Akaongeza Junior mwenyewe.
“Hilo tu ndilo la kushukuru Mungu, ila sasa ushajiuliza katika hili
atalichukuliaje?” “Mimi hilo halinitii wasiwasi kama pengine nimemsoma Emelda
vibaya.” Akamuona anaanza kuvunjika moyo.
“Iweje niwe nimemfikiria sivyo kwa sababu mawazo tu
yalinipelekea huko? Maana katika kuwaza kama na mimi nilishabahatika kujaliwa
hapa duniani na mwanamke, ndio nikaishia kwa Emelda. Nikajivunja moyo
nikijiambia pengine alikuwa akifanya hayo yote kwa kutumwa na mama! Ndio
ikabidi kuanza kufanya uchunguzi.” “Sasa hayo mashaka ndio yanata kukupokonya
furaha yako Junior.” Akamuhurumia tena.
“Nisikilize. Naona umewaza vizuri. Nenda muda ambao pale
nyumbani mtakuwa peke yenu, umsome. Kwanza akikuona umekwenda kwa ajili yake,
jua itamshitua. Lakini hakikisha unatuliza hiyo hali ili kuweza kumsoma
moyo wake. Msichana akikupenda na kama ni wako utajua tu, Junior. Japokuwa
Jelini alikuwa kitisha, kama ni wa viwango vingine kabisa, na…” “Hata mimi
nilikukatisha tamaa ili usije umia.”
“Ewaa! Lakini ndani ya moyo wangu nilijua nampenda na
kumtaka yule binti. Haikuwa kwa haraka, lakini ona ilivyokuwa sasahivi. Sasa
kwako kama ni kweli, ndio ujue itakuwa rahisi kabisa sababu anakusubiri. Usiogope.”
“Nashukuru Ezra.” Tayari Ezra akawa tena upande wake, hataki kumuona tena
anarudia ile hali ya kutokuwa na furaha.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Nikwambie kitu lakini usishituke?” “Husubiri hili likae
sawa kwanza Junior ndipo tuanze bomu jingine?!” Junior akazidi kucheka. “Hope
aliponiacha pale, baba alinipigia simu kunitaarifu kuwa anakutana na Hope leo
ndipo wakutane na mama Jema jioni. Sikumficha. Nilimpigia picha ile pete juu ya
meza, nikamwambia Hope amenivulia na kunirudishia. Sikumwambia mengi ila mzee amesikitika
sana. Akasema hivyo sivyo alivyodhania mwisho wetu.” “Ila utamwambia ukweli.” Hapo
akamtibua kidogo.
“Ukweli kwamba ameniachia mimi jukumu la kutengeneza,
akijipa yeye thamani kwamba nilazima nitamvalisha yeye tena hii
pete? Kwamba ni yeye tu amebakia hapa duniani? Na mimi nina jukumu la kunyenyekea
yeye akinidhalilisha! Kwa nini? Hana hata chembe ya kunijali kama Emelda
ambaye nimekua nikimpuuza!” “Sina nia ya kukuudhi Junior. Na mimi nataka upate
kitu kizuri. Ila nataka kusiwe na hila. Tafadhali Junior. Uchumba si
ndoa. Unaweza kuvunjika, lakini nataka kama tunamalizana na Hope, tumalize kwa
heshima. Ni sawa?” “Sawa.” Akatulia.
“Mbona sasa ni kama umeshafanya maamuzi yako?” “Ndiyo.”
“Junior! Sio kwamba umesema kesho tutazungumza?” “Kwani ni mara ngapi nakua
nimeamua jambo na kubadilisha? Wewe njoo na hoja zakueleweka bila kuangalia
jamii na watu watasemaje, ila mimi kama Junior. Ukinifikiria furaha yangu hapa
duniani, na kile ninachostahili. Watu wengine mpaka wazazi hao najua
hatutashindwa kuwakabili endapo sisi wawili tutaamua kusimama pamoja.”
“Sawa.” Ezra akamkubalia. Hapo akatulia.
Penzi.
Alijikuta amewahi
kidogo. Kwa hiyo akaegesha gari pembeni ya nyumba mpaka alipoona gari ya wazazi
wake ikitoka, ndipo na yeye akaingia. Akasalimia mlinzi getini na kuvuta gari
yake mpaka sehemu ya kuegesha magari. Akashuka kama akimbie na matunda yake mkononi.
Akashukuru Mungu
kukuta hata Noah hayupo. Akayaweka jikoni na kuelekea chumbani kwa Emelda.
Akagonga mara kadhaa na kusubiria, baada ya muda akamsikia anafungua.
Alishituka sana kumuona Junior pale.
“Shikamoo, kaka.” “Marahaba. Vipi? Pole nimekuamsha.” “Hamna
neno. Pole na kazi.” Akamwambia kwa kujali. “Asante. Pole na wewe kwa kuumwa.”
“Nashukuru. Kama hujawakuta kina mama, waliniambia wataenda kanisani, na baada
ya hapo kuna mahali watapitia, watachelewa kurudi. Labda ukakutane nao kanisani
kabla hawajatoka.” Akamwambia akijua wazi yupo pale kwa ajili ya wazazi.
“Mama ameniambia unaumwa, ndio nimekuja kukuangalia.” Akawa
kama hajamuelewa. Junior akaelewa ila akajua ni haki yake. “Unajisikiaje?” “Ni
kutapika ndiko kunanichosha. Hakuna kitu kinakaa ndani. Hata nikinywa maji tu,
natapika. Umekula mchana?” Akabadili mazungumzo.
“Nipo hapa kwa ajili yako Emelda. Nataka kujua
unavyoendelea.” Jinsi alivyozungumza, akajua imemuingia, kwani alimwangalia na
kuinamia mlangoni. “Kwa nini husemi ukiwa unauma?” Kimya akiwa ameinama,
wamesimama hapo mlangoni. Lakini ikawa hali si ya kaka na dada tena. Junior
huyu amekuja kivingine.
“Umekunywa dawa ya kuzuia kutapika?” Akatingisha kichwa
kukataa na kuongeza. “Kila kitu nikiweka mdomoni, natapika. Hata nahisi dawa
zenyewe za malaria, nimezitapika. Ndio mama amesema tusubiri tuone, kama mpaka
kesho homa itakuwa kali, anipe dawa zingine.” Junior hakupenda hilo.
Akatoa mkono mfukoni na kumshika kipanda uso. “Una joto
kali! Mama amekupima?” “Amenipa dawa, nikatapika ndio akaniambia nipumzike,
akirudi atanipa zingine.” “Pole sana. Twende nikupeleke hospitalini. Angalau
wakuchome sindano ya kuzuia kutapika, ndipo uweze kutumia dawa za malaria.”
“Mimi naogopa sindano, kaka. Umesahau? Bora nijaribishe vidonge tena.” “Si
umeniambia umejaribisha umekua ukitapika?” “Acha nijaribu tena.” “Unayo maji?”
“Mama ameniachia hapo chumbani. Wewe nenda kapumzike kaka. Najua unachoka. Mimi
nitakuwa sawa.” “Usijali. Tuone dawa unazotumia.” Wakaingia ndani.
Akaangalia hizo dawa, kweli zingemsaidia kushusha homa.
Akampa na chupa ndogo ya maji aliyoikuta hapo pembeni ya kitanda, Emelda
akimwangalia kwa kujificha asiamini kama ameingia hapo na ametumia muda wote
huo kwake! Akawa hajui ni nini kinaendelea.
Akameza akitarajia baada ya hapo ataondoka, lakini wapi! “Jipumzishe
tuone kama hazitatoka. Usipotapika, nitakupa na matunda. Nimekuletea.” Emelda
akahisi pengine malaria imempanda kichwani, anasikia na kuona mazingaombwe.
Junior akiwa anamuelewa kabisa kwa jinsi alivyoishi naye kwa kumpuuza,
akajiongeza. Akamnyooshea mashuka ya kitandani kwake, akaweka kama nafasi ya
kulala na kumuwekea mto. Akamgeukia maana alizubaa akimtizama. “Panda ulale.
Mimi nitakuwa hapa na wewe.” Akapanda bila ya kuongeza, akashangaa anamfunika
kabisa, akalala ubavu ila akimwangalia.
Akashangaa anakaa hapohapo kitandani na si kwenye kitanda
cha pembeni ambacho kilikuwa cha Ester au kuondoka kabisa. Mapigo ya moyo
yakaanza kwenda kasi. Akamshika kipanda uso. “Unajoto kali! Acha nikuletee
taulo la maji.” Wakati Junior anasimama, na yeye akaruka kitandani kukimbilia
bafuni kutapika. Kilikuwa chumba chake na Ester, na bado vitu baadhi vya Ester
vilikuwemo humo.
Akamfuata na kwenda kumshika mbavu akiwa anatapika ili
asiumie zaidi. Emelda alitamani asimalize kutapika. Hatimaye ameshikwa na
Junior! Ikawa mix feelings. Kilio cha furaha na uchungu kikaanza. “Pole
sana.” Akambembeleza. Alitapika kidogo nje ya choo. Wakati anajisaficha uso na
mdomo, akashangaa Junior anaanza kusafisha matapishi yake. Kwa hakika hakuwa
akielewa. Akamaliza na kurudi chumbani wakati Junior akimalizia kusafisha hapo
bafuni. Akabaki amekaa kitandani hata haelewi.
“Nakupisha ubadili nguo, twende hospitalini. Pole.”
“Asante.” Akatoka na kwenda kumsubiria sebuleni. Baada ya muda akatoka. “Vipi?”
“Nikitapika najisikia afadhali. Ila nachoka! Hapa natamani kulala tu.” “Pole.
Twende. Wakishakupa dawa, utalala.” Wakatoka hapo kuelekea hospitalini.
~~~~~~~~~~~~~~~
Sasa Emelda akashangaa sana aina ya hospitali aliyopelekwa.
Viwango vyake na yeye haviendani kabisa. Kulekule alipokuwa amelazwa yeye
Junior ndio akampeleka na yeye. Akashangaa sana. Lakini kwa kuwa usiku huo
kulikuwa na mengi ya ajabu, akaona atulie tu. Yeye mwenyewe Junior akaandikisha
kila kitu, ndipo wakaenda kumuona daktari. Muda huo tayari giza lilisha ingia,
wagonjwa si wengi. Wakabaki kusubiria nje, baada ya muda mfupi na wao zamu yao
ikafika. Wakaingia.
“Natapika. Hata mama aliponipa dawa, hazikukaa sana,
nikatapika.” Akamwambia hivyo daktari. “Unatumia dawa gani?” Akamwangalia
Junior. “Mama amempa za malaria.” Junior akamsaidia. “Ulipima?” Hilo swali
likamfanya na Junior kumwangalia. “Noah alikuwa na malaria, ndio nilivyoanza
kutapika na homa wakasema itakua malaria tu. Wakanipa dawa kama za Noah.” Hayo
anamwambia Junior, daktari akisikiliza, mpaka Junior akaishiwa nguvu. Ila
aliwajua wazazi wake. Akajua hata huyo Noah naye atakuwa hajapimwa alipewa tu
dawa.
“Ni sawa akifanyiwa full blood picture. Ili tujue ni
nini?” Ikabidi tu Junior aombe. Wakaandikiwa vipimo, wakaenda maabara kutolewa
damu. “Naogopa kaka! Siwezi kabisa sindano.” Junior akacheka akimwangalia.
“Wewe usiangalie. Wakiwa wanakuchoma na kutoa damu, usiangalie mpaka
watakavyokwambia wamemaliza.” Akatulia lakini wazi akionekana hajaridhika.
Wakatafuta sehemu na kukaa baada ya Junior kuweka kikaratasi
walichopewa na daktari sehemu ya dirisha la maabara. Tena akaenda kukaa karibu
yake kabisa, Emelda akainama pembeni yake akijichezea mikono yake. Na yeye
akainama pembeni yake kabisa kama anayemchungulia pale alipojiinamia. “Siku
nyingine ukiumwa, usiache kuniambia. Umesikia?” Akamwambia kwa upendo, na
kuzidi kumchanganya Emelda.
“Kuanzia leo, ukiumwa na chochote, unijulishe.” “Upo na
majukumu mengi na muhimu, kaka. Kazini na kanisani, hupumziki! Nakuhurumia.
Naona mengine upunguziwe.” Junior akasikia kujaliwa huyo, moyo kwatu,
kama aliyekuwa na kiu, anapewa maji.
“Sio katika ugonjwa wako. Nalo ni muhumu kwangu. Usiache kunitaarifu. Sawa?” Akatingisha kichwa kukubali, wakatulia mpaka walipoitwa na kutolewa damu. Akapatwa hali ya kichefuchefu tena, akakimbilia kutapika. Akatapika mpaka watu wa nje wakabaki kusikiliza, Junior akaingia ndani kumsaidia. Baada ya muda wakatoka. Akaenda kumuombea apate angalau sindano ya kuzuia kutapika wakati wakisubiria majibu.
Kwa kuwa alikuwa ametapika sawa, wakaona wampe na dripu
kabisa. Akapewa chumba cha mapumziko, akawekewa hiyo dripu akiwa ameshikwa na
huyo Junior, kaka yake. Wakamuweka sawa, na kuwaacha hapo, Emelda alishapitiwa
na usingizi. Junior akabaki amekaa hapo akimtizama kama asiyeamini wakati ni
Emelda yuleyule ambaye alikuwa mbele ya macho yake, akimtunza bila kuchoka ila
hakuwahi kumuona!
~~~~~~~~~~~~~~~
Junior anacheza karata nyingi kwa wakati mmoja. Huku akiwa ameshika
pete ya uchumba, moyo umeshahamia kwa msichana wa kazi za
ndani wa mama yake, aliyeshindwa kumuona wakati wote.
Pete
itawekwa kidoleni kwa nani? Inarudi kwa Hope anayejulikana mpaka
kanisani na kwa wazazi, au kwa Emelda?
Uchumba wa Ezra na Jelini?
INAENDELEA.
0 Comments:
Post a Comment