Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 25 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 25

 
Kulikoungua Shoka La Mapenzi. Uzuri au ubaya, yeye Hope alijua mwanaume atakayeolewa naye, si kama Jelini hakuwa akijua hata kazi ya Ezra wala ofisi yake. Alishafurahia kuolewa kwenye neema. Na Junior alishamsaidia mengi sana kiuchumi, mpaka gari anayoendesha Hope ni zawadi kutoka kwa huyohuyo Junior. Halafu japokuwa Junior alikuwa chuch boy, lakini alikuwa akilipa. Kama Ezra tu. Alishajiona anakua mama mjengo. Yaani jumba lililomtoa macho hata Jelini, sasa Hope alishajiona akilimiliki. Ikamjengea kiburi kidogo, akijua hata iweje, ataolewa tu na Junior kwa kuwa kwanza alishamvalisha pete ya uchumba, tena mbele ya kanisa. Hawezi kumuacha.

    Sasa kuona na mkwe amekubali ajitoe kanisani, hofu ikamuingia. Kama na wakwe nao wanamtema, kweli kuna ndoa hapo! Tayari siku yake ikaharibika. Ikawa bora lawama, kuliko fedheha. Inamaana kanisa zima sasa litajua hana tena cheo kwenye kanisa la baba mkwe! Akazidi kuvurugukiwa maana hicho nacho pia kilimpa kiburi hata hapo kanisani, akaweza kuenea kote na kwa wote akijulikana ameshika nafasi kubwa ya kanisa kubwa kama hilo na ni mtoto wa nyumbani.

Kulikobaki Mpini Wa Mapenzi.

    Ezra akamuacha kidogo kama atulie, kisha akamuuliza. “Tafadhali naomba kujua unachokifikiria juu ya Hope. Maana mimi nakujua Junior. Zoezi la kuchumbia ulishafunga na hukuwa ukitaka kuanza tena. Ni nini kinaendelea?” “Jana wakati mume wa Ester akila kile kiapo alichomtengenezea Ester, pale mbele ya umati, ilinifanya nifikirie sana Ezra na aliyoyafanya Hope jana kama kuchorea mstari majibu yanayo niogopesha. Ulitilia maanani kile kiapo cha Devin?” Akataka kujua.

    “Nilisikiliza. Ila kumbuka hawa watu  wawili, Ester na Devin wametoka mbali sana Junior! Halafu ni Ester. Ni mwanaume mjinga tu na mpumbavu ndiye atakayeshindwa kujua kama amebahatika kupata mwanamke kama Ester!”

“Sawa. Lakini katika yote, mimi imenibidi nifikirie Ezra. Baada ya sisi kula na kunywa pale kifahari, hawa watu wawili wanakwenda kujifungia mahali kwa siku 7! Hizo siku 7 ni msingi wa siku nyingi sana za peke yao mpaka kifo.”

    “Unakumbuka kitu aliwaambia Jelini?” Ezra akatulia. “Kwamba wanaonekana wanapendana. Ester anafuraha mpaka inaonyesha usoni.” “Huwezi mfananisha Hope na Ester, Junior! Au nyinyi na wao! Na wewe unajua. Hope amekukuta na kila kitu, Ester na Devin wameanzana zamani sana. Na Ester alikataa kila mwanaume, akimsubiria Devin bila kuchoka!” “Sasa hayo ndiyo yamenifanya nifikirie tulicho nacho na Hope! Tukiwa peke yetu. Mimi na yeye. Hakuna kanisa la mzee na hakuna mipango anayopenda yeye kuisimamia. Tumebaki sisi wawili tu, tunafanyaje?” Kimya Ezra akijaribu na yeye kufikiria.

    “Ndio nikagundua HATUNA. Ni kama tunaunganishwa na majukumu tu! Muda mwingi tunazungumzia kufanikisha mambo ya watu na si yetu! Sasa inawezekana ni kwa sababu yetu yamekaa vizuri! Sijui! Au pengine tuna msingi mbovu.” Akaendelea bila jazba.

    “Na kama unaona kujifananisha sisi na kina Ester ni mbali sana, basi acha nijifananishe na wewe na Jelini. Mbona anakufuata mpaka usiku, eti hataki ulale na uchungu moyoni. Anang’ang’ania mjenge ‘chenu’, huku hakufahamu kabisa pesa uliyo nayo!” Ezra kimya. “Sema Ezra? Niambie kama wewe hujashangazwa na kitendo cha Jelini eti anakukimbilia na kukung’ang’ania hivyo, kumbe mpaka jana hakuwa akijua kama una mali hivi! Yaani ni kukupenda tu wewe! Yupo tayari kudhalilishwa na Hope, bado anabaki na wewe, bila kinyongo! Anasema atatafuta jinsi ya kuishi naye. Ili kwanza mimi na wewe tusigombane, na nyinyi mbaki pamoja! Kweli Ezra? Si wote hawa wanawake wametukuta watu wazima tu? Jelini hakujui wewe ni nani, Hope alinijua mimi hata kabla sijamchumbia! Sasa unataka kusema nini?” Ezra kimya.

    “Hakika imenifanya nifikirie mara mbilimbili. Au si kweli kama kwa muda wote, Jelini hakuwa akijua kama una nyumba kama ile!” “Mungu ni shahidi, alishituka sana, tena mpaka ikabidi nimtulize kwa kucheka kwa jinsi alivyokuwa ameishiwa nguvu.”

    “Hope haniheshimu Ezra.” “Sidhani kama ni hatokukuheshimu.” “Basi hatuna kitu chetu. Hata upendo wetu sisi wenyewe wawili sidhani kama upo wa dhati. Sidhani kama tumeunganishwa na mapenzi ya dhati. Ndio maana nimefikiria na kutaka achukue hatua chache nyuma. Bila hayo majukumu yote au pesa yangu. Abakiwe na sisi tu, nione kama anaweza kujenga chetu. Lakini mpaka sasa hana, na nasikitika ni kama amekosa sababu.”

“Sasa, sitaki ajione ana vitu vingi sana. Nikimaanisha mali, akasahau watu na utu. Ni kweli sitaki kuanza upya kwenye swala la uchumba. Ningependa kuendelea na Hope, lakini sipo tayari kumuoa alivyo. Hapana Ezra! Sina sababu ya kufanya hivyo. Nampa nafasi ya mwisho. Aitafute nafasi yake kwenye maisha yangu, kwa kuwa mimi naijua nafasi yangu kwake na nimeisimamia kwa uaminifu sana, na sijazembea. Akishindwa kuipata nafasi yake. Akang’ang’ania kuwa juu hivihivi, BASI.” “Junior!”

    “Hakika Ezra, sikutanii. Na mimi nataka mwanamke atakayenipenda na kuniheshimu! Kwa nini nijiingize sehemu itakayoninyima raha kwenye maisha yangu yote ya hapa duniani! HAPANA! Kama atashindwa kujishusha. Akang’ang’ania kuwa juu, hakika basi.”

“Kama hichi alichokifanya leo, sijakifurahia hata kidogo. Mimi ninapofanya mambo yangu huwa namshirikisha tena anapata nafasi ya kushauri. Tena kama unavyomjua Hope, anakua king’ang’anizi akitaka yeye ndio ashinde hata kwenye mambo yangu! Leo anaacha nafasi kubwa hivi, inayo heshimiwa, na anajua anategemewa, kweli anamtaarifu baba yangu kwa barua pepe! Kana kwamba hatambui umuhimu wa hiyo nafasi, eti anamwambia ni kuanzia leo! Heshima ya wapi hiyo, Ezra?!”

    “Anategemewa majukumu mazito aliyoaminiwa nayo, nani ayafanye kama si kutaka kuadhibu wazazi wangu na mimi, kwa sababu ya kumuhoji jana? Anatukomoa, akidhani tutashindwa! Anasahau ile ni kazi ni ya Mungu wala si ya mzee! Hata mzee akifa leo, ile kazi itaendelea tu. Acha tuone kama baada ya yote, sisi tutabaki tumesimama. Mwache tu.” Ezra akapoa kabisa, akabaki akitafakari.

    “Na naomba usimtafute kuzungumza naye.” Akawa kama amesoma mawazo yake. “Umepatwa na nini Junior?!” “Wewe hudhani sistaili kama ulichopata wewe? Mtu wa kukuhitaji wewe kama wewe?” “Unastahili Junior. Lakini si kwamba mimi na Jelini tutakuwa bila matatizo. Itatupasa tuzungumze na kurekebishana ili tuwe ukurasa mmoja.” “Ewaah! Iwe anataka yeye na si wewe kumuwekea kwenye akili yake. Mimi nataka kuhitajiwa wala sihitaji mtu mkamilifu. Maana na mimi si mkamilifu. Ila nataka mtu atakayenitaka mimi kama mimi na akubali tutembee pamoja na kufanya hicho unachozungumza. Sitaki kuuziwa mbuzi kwenye gunia. Tafadhali Ezra.” “Nakuahidi sitaingilia. Nitafanya kama ulivyofanya kwangu na Jelini. Atakaponitafuta, ndio nitazungumza naye.” “Na tafadhali ibakie hivyo. Akikutafuta. Akaonyesha anahitaji mahusiano na mimi, hapo sawa.” “Sawa.” Ikabidi Ezra awe mpole.

Aluta.

    Wakiwa katikati ya kazi, mida ya saa nne asubuhi hiyohiyo ujumbe ukaingia. ‘Baada ya kazi naomba mpitie nyumbani, tujipange swala la Jelini. Nataka tumalize taratibu za awali kabla sijasimama jumapili kuhubiri pale madhabahuni. Ili maswali yote ya jana, yajijibu yenyewe. Nisibakiwe kuhubiri habari za uchumba wenu.’ Ezra aliposoma akacheka na kutingisha kichwa.

    “Ni nini?” “Mimi naona usome mwenyewe.” Akamrushia simu yake. Junior akasoma na kucheka. “Mzee anataka uchumbie.” “Nimemuelewa. Sasa pete!” “Unajua size yake? Maana kwa kuzipata sio tatizo.” “Itakuwa kazi ya leo. Nitajitahidi kumchunguza mpaka nijue.” Akamuona anahamasika.

    “Nini?” “Hebu fikiria maisha yangu Junior. Yaani ndio nabahatika kila siku kuamka pembeni ya Jelini!” “Itakua Ezra. Jelini anakupenda na anakiri kukuhitaji. Na inaonekana hata kwao wamekukubali. Sioni sababu yakutokuwa. Na najua mama anaandaa mazingira ya kuja kumkaribisha tena kwenye familia, ili kutengeneza palipoharibika jana na kutambulisha familia yetu rasmi kwake na kwao.” Ezra akabaki akifikiria na kurudisha majibu kwa mchungaji. ‘Tutakuwa hapo mzee wangu na asante sana.’ Kisha akapiga simu kuomba atengenezewe matunda. Kwamba saa 5 atayapitia akiwa anakwenda kwa Jelini.

Penzi Kikohozi.

    Mara akaona simu ya Jelini inaingia ila kwa video. Alifurahi, karibia asimame, Junior akimwangalia tu. Akapokea. “Upo busy? Sitaki kukusumbua mida ya kazi.” “Nimefurahi kukuona Jelini! Umependeza sana. Unakwenda wapi!?” “Asante. Nasaka pesa mwenzio. Naenda kumbembeleza mwenye saluni moja maeneo ya Posta, anipe kazi yakumpelekea bidhaa zaidi. Alinipa kazi ndogo, lakini nimemfikiria, nimeona naweza kufanya naye biashara kubwa zaidi.” “Unaakili ya biashara wewe?” Akamuona anacheka na kushukuru.

    “Nimekumiss mpenzi wangu. Nikasema nikusalimie kwa kukuona. Japo tumeshasalimiana kwa jumbe za asubuhi.” “Nimefurahi kukuona Jelini. Na asante. Na ujue hunisumbui hata kidogo. Muda na wakati wowote ule, ukiwa na nafasi uwe ukinipigia.” “Nitafanya hivyo. Na nina zawadi yako nzuriii. Usiku si tutaonana?” “Lazima. Au unaratiba ingine?” “Sisi kwanza. Na wewe ndio ratiba yangu ya kwanza.” Ezra akacheka na kuona atoke tu hapo asimkere Junior.

    “Nakupenda Jelini.” “Mimi mwenyewe nakupenda. Ila sema mimi nakupenda sanaaa.” Ezra mfanyakazi wa mshahara kama anavyojiita mwenyewe, akaenda kutulia nje ya ofisi, BOT mjengoni, akifanya ya kimapenzi na si kazi. Wakapanga kukutana kabla hajarudi dukani kwake, hapohapo mjini, kisha akarudi ofisini.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Mida ya saa sita Jelini akampigia Ezra kuwa amemaliza, anakwenda kumsubiria maeneo ya Ocean Road, upande wa baharini karibu na hospitali ya Agakhani. Nusu Ezra aruke. Maana ilikuwa sehemu sahihi. Akapitia matunda kwenye hiyo restaurant wanayo mtengenezeaga, akakimbilia kumfuata Jelini.

    Akamkuta akimsubiria garini kwake ila ameshusha vioo na gari kazima. Jelini alifurahi huyo kama ambaye ameona nini sijui! Ezra akamdaka midomo akiwa amesimama dirishani. Wakabadilishana ndimi kwa muda tu, kisha akamuachia. “Nilikuwa sina uhakika kama utanikiss tena!” Ezra alicheka sana. “Mimi nilijua ni jana tu!” “Na leo.” Jelini akacheka, akashuka garini.

    Ezra akamdaka mkono, akaungalia kwa makini, akaubusu na kubaki ameushikilia kwa kupitanisha vidole vyao. Jelini akidhania ni mapenzi kumbe mwenzie yupo na agenda yake. “Nimefurahi umenipigia simu kwa video. Na mimi nilishakuwa na hamu na wewe.” “Kweli Ezra? Maana najua upo busy.” “Sio sana kushindwa kukupa wewe muda. Nikitingwa nitakwambia. Ila usiache kunitafuta ukihofia ubusy.” “Sawa. Ila usiku usihangaike chakula. Mimi nitaagiza.” “Hapana Jelini. Tulia kazini, mimi nitatafuta chakula. Mida hiyo wewe unakua busy wakati mimi nakuwa nilishatoka kazini, sina chakufanya.”

    “Kwanza nahisi nitakuletea chakula kutoka nyumbani. Maana leo tukitoka kazini tunapitia nyumbani kwa mzee. Najua mama lazima ataanda meza nzuri na kubwa. Huwa anapenda sana tukienda nyumbani. Kwa hiyo nitakubebea na wewe. Au unataka kitu maalumu?” “Mwenzio huwa si mchaguzi wa vyakula. Nitakula utakachokula wewe.” Ezra akacheka akimwangalia.

    “Nikuulize kitu, Jelini?” Jelini akaingiwa na wasiwasi maana alishaongeza heshima kwa huyo Ezra. “Juu ya nini!?” “Sio kitu kibaya bwana! Acha woga.” Akamtuliza. “Umeshafikiria maisha yetu? Angalau tu kupita akilini mwako.” “Nakufikiria Ezra. Nakufikiria sana. Ndio maana nimeamka tu na kuangalia simu kama umenitafuta na ndio nikakutumia ujumbe na wewe.” Ikawa kama anajitetea tena.

    “Hapana Jelini. Namaanisha maisha yetu. Tukiwa tunaishi pamoja.” Jelini akacheka na kuinama akifikiria. “Eti Jelini? Ushawahi hata kufikiria?” “Ni kwambie ukweli?” “Ndio ningefurahi.” “Kidogo umenitisha Ezra. Mimi sikukujua kwa wadhifa huu. Kwa hiyo Ezra niliyekuwa naye kwenye picha ni Ezra wa kawaida ambaye hata mambo yake ni kawaida sana. Nikajipatia picha hivyo unavyonipenda, eti ndio nitakuwa nikiishi na wewe kwa maisha yetu ya kawaida yasiyo na mambo mengi.” Ezra akawa kama hujampata vizuri.

    "Ukiwa unamaanisha nini!?” “Mimi sijasoma sana Ezra. Na huo ni ukweli. Nimeishia kidato cha pili, nikiwa na elimu ya mpaka kidato cha kwanza. Sikujua kama wewe ni mtu uliyesoma kwa kiwango hicho na kufanya kazi kubwa hivyo!” Ezra akacheka ila akiwa na swali. “Kabla hujamalizia wasiwasi wako, naomba uongeze kwenye maelezo yako, aina ya kazi uliyodhania nafanya.” Jelini akazidi kubabaika.

    “Niambie tu usiwe nawasiwasi.” “Unakumbuka jinsi tunavyokutana mida ya mchana? Unakuwa smart sana. Huvai koti la suti, lakini nadhifu sana na unakua wakati mwingine na tai kabisa au unakua unaonekana wazi umetoa tai muda si mrefu. Nikajua wewe ni misheni town.” Ezra alicheka. Akacheka mpaka machozi.

    “Bwana acha kucheka!” “Subiri kwanza Jelini. Ndio nakuwa nafanya nini?” “Unafanya kwenye ofisi za watu, unatumwa hiki na kile. Karatasi hii peleka benki hii, bandarini, TRA ilimradi kukamilisha mipango ya ofisi ya mtu.” Ezra akacheka kwa kutulia akifikiria. “Ezra wewe ni mtulivu sana, rahisi kukufikiria hivyo. Maana wengi niliokutana nao mimi ambao pengine wanakaribia tu nafasi zako, hata hawajakufikia hapo ulipo, mwanzoni sana, utawajua kama wamesoma na wananafasi kubwa kimaisha.”

    “Sasa kukutana na wewe. Huzungumzii unachofanya. Huonekani kama una shule yakueleweka kwa kiwango hicho, hakika wewe na Junior nikawachukulia poa.” “Sasa mbona kama hiki ni kitu kizuri?” Bado Ezra hakuona tatizo.

    “Si kwa upande niliosimama mimi, huku. Nishakutana na wanaume wasomi na wenye pesa. Wao wenyewe, na wanao wazunguka walinionyesha kwa vitendo na maneno, siwastahili sababu mimi sijasoma. Kwa kina Colins ndio ilikuwa waziwazi kabisa. Walinifuata mpaka nyumbani kwetu. Mbele ya mama yangu na mwanangu, wakaniambia kijana wao hawezi kuoa msichana kama wa aina yangu. Wakitaja shule na maendeleo ni moja ya vigezo ambavyo mimi sikuwa navyo.” “Acha kulia Jelini. Tafadhali usilie. Pole.”

    “Iliniumiza Ezra. Iliniumiza sana. Mbele ya mwanangu! Sasa kwako nikaona hicho kipengele sitakuwa nacho. Kuja kusikia tena na wewe ni walewale na una mjengo kama wa Junior! Na vile Hope uliyeniambia amesoma vizuri, kuja kunitambua kwa kudharau ninachokifanya!” Ezra akashituka akajikaza. “Mimi nishaanza kujishuku. Naona historia inajirudia. Narudi kulekule kwa walewale!” “Hivi ujue Jelini kwako sijakurupuka?” Akamuuliza akimfuta machozi.

    “Nilikufuata nikiwa nakufahamu kwa asilimia kubwa sana zilizoniridhisha kuwa utanifaa mimi. Na kabla hujauliza nilikufahamia wapi, jua huko vyuoni nilikopita, nilisoma na wasichana warembo tu. Hapo kazini kwetu, wapo wasichana ambao bado hawajaolewa. Inamaana na wenyewe wamesoma, au wana uwezo wa kunikaribia mimi. Nikimaanisha kwa sababu sisi pale kazini tumeshakaa muda mrefu, hata vyeo vimeongezeka. Kwa kuwa hata shahada ya pili tumesoma tukiwa kazini. Kwa hiyo tupo kwenye nafasi za juu kwa sababu tupo pale muda mrefu. Nikimaanisha wapo na wanaajiriwa binti wadogo tu mpaka sasa. Lakini mbona nilikusubiria wewe?” Jelini akakunja uso.

    “Unakumbuka ulianza kunikimbia kila unaponiona?” Jelini akacheka akiendelea kujifuta machozi. “Umeshajiuliza ni kwa nini nilirudi tena kwako?” Akapandisha mabega kukataa kama anayesema hajui. “Kwa sababu nilikupenda Jelini. Na nimekuchagua wewe hivyo ulivyo. Sijakurupuka. Nakuletea chakula pale kazini kwako na ukakikataa, ukisema hutaki kilete picha ya hongo, hilo nalo likanivutia zaidi japo nilitamani ukipokee kile chakula. Ikaniongezea moyo wa kukusubiri. Kwa hiyo jua upo na mtu anayekufahamu. Amekuchagua wewe. Na Ezra anakutaka wewe akiwa anakujua na sina mpango wa kubadilisha chochote kwenye maisha yako.”

    “Hivyo ulivyo nakutaka wewe. Na jumla yako yote. Umenielewa?” “Kwa hiyo kumbe tena una shahada zaidi ya moja!?” Ezra alicheka sana. “Kumbe nazidi kuharibu si kutengeneza?” “Bwana wewe umesoma sana bwana Ezra!” “Basi acha kuangali nilivyo navyo ila mwanaume uliyempenda tokea mwanzo. Jua hayo mengine yatatusaidia maishani. Ni ziada tu. Kwamba familia yetu itakuwa imebarikiwa zaidi. Kuna mfanyakazi na mfanyabiashara. Tutakuwa na maisha mazuri. Hapo vipi?”

    “Sasa mbona husemi kama utakuwa ukinikumbatia!?” Ezra alicheka sana. “Bwana Jelini wewe mahitaji yako madogo sana! Wenzio wakijua mchumba anapesa, wanaanza kuomba magari! Wewe unataka mikono tu?” “Na kulala nikiwa nimekumbatiwa usiku mpaka asubuhi.” Ezra alicheka hana mbavu.

    “Na nini tena?” “Usiache kunijali Ezra. Wewe unanijali sana Ezra, mpaka nabaki nikikuwaza wewe kila wakati! Usije badilika. Hata tukizaa watoto wengi namna gani, usinisahau mimi.” “Kumbe unaona mpaka watoto wetu? Wangapi?” Jelini akaanza kucheka. “Ni wengi sana Ezra. Inabidi kutafuta uzazi wa mpango.” Ezra hana mbavu. “Tuishie watatu tu?” Ezra akamuuliza akicheka. “Mimi naona watatu watoshe bwana! Wengine tuwaachie wengine.” “Nimelikubali wazo lako. Kwa hiyo jumla tutakuwa na watoto wanne, pamoja na Jeremy?” Akamuona anapoa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    “Mama hataki naye. Amesema mimi nitaondoka mle ndani lakini si Jeremy. Ujue nilimzaa Jeremy nikiwa mdogo sana.” “Uliniambia.” “Halafu nilimzaa nikiwa na uchungu. Nilikuwa sijui kitu chakufanya, mama akamchukua tokea siku namzaa. Yaani mimi nimemzaa, nalia siku ile pale leba, si kwa maumivu ya kujifungua bali sijui kitu chakufanya naye huyo mtoto. Nimetolewa, naambiwa nirudi wodini, nalia kwa hofu. Lakini nilipotoka nikakuta bado mama ananisubiria nje, amemtuma Jema akaniletee uji na supu. Sitasahau ile siku. Nilikuwa nalia, nina hofu na mtoto mkononi.” Akamfuta machozi.

    “Niliporudi tu wodini, mama akamchukua Jeremy kutoka kwenye mikono yangu. Akamfunika vizuri maana nilikuwa nalia, wala sijui chakufanya. Basi, akatusaidia mimi na mwanangu, ndio nikaanza kutulia. Ila ule uchungu haukuwa umeisha Ezra. Nilikuwa naumia naona nimepokonya utoto wangu nikiwa sipo tayari kukua. Kufupisha habari ili urudi kazini, tokea siku hiyo mama akaanza kumlea Jeremy, mimi nikatafuta kitu cha kunituliza. Pombe.

    “Nilipojua uwezo wa pombe. Kwamba ukinywa nyingi, kwa muda huo uchungu unapotea, nikaanza kuinywa kila wakati. Ikiisha tu kichwani, natafuta ingine bila kujali muda. Hivyo unavyomuona Noah, ndio ilikuwa maisha yangu. Tena naona bora Noah yeye analewa na kurudi kanisani. Mimi nilikuwa nikishinda baa. Sijui kula wala vaa ya Jeremy. Sijui uzima wake wala kuugua kwake. Sijui hata lini alipewa chango, mbali ya zile za mwanzoni kabla sijajua pombe. Nilimuachia mama moja kwa moja.”

    “Sasa alivyokuja Colins, ikawa ni mwanaume wa kwanza na yeye kuweka mipango mpaka ya Jeremy. Akitaka tukioana mpaka Jeremy atumie jina lake. Ikanifanya nimlete karibu ya Jeremy. Akampenda sana, maana alipenda anachokifanya Colins. Maswala ya puzzle, na Lego’s wakawa ndio kitu chao kinawaunganisha, wakijenga pamoja. Ndio yakatokea yakutokea, halafu Colins hakurudi tena, ikamuumiza sana Jeremy. Akabaki akipiga picha kila puzzle au legos anazotengeneza, anataka mama mtunzie hizo picha ili Colins akirudi amuonyeshe.”

    “Ndio mama ameniapisha, mbele ya Jema, kuwa pale nyumbani kwake ni kwa Jeremy. Hata akifa yeye leo, pale patabakia kwa Jeremy na mimi nisiwahi kumyumbisha kwa wanaume. Anayemtaka Jeremy, atakuwa akienda pale kumsalimia, basi. Yaani hata mimi nikihama pale, amesema niondoke na mizigo yangu tu, ili yakinishinda huko, nirudi pale, nitawakuta wao bila kumchanganya Jeremy. Amesema hakuna mwanaume wakumtoa Jeremy pale. Hata akifa, asitolewe pale ili tusimyumbishe kwenye majumba ya watu.” Ezra akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu.

    “Tutakuwa sawa Jelini. Na ahadi ya kulala umekumbatiwa, ipo, nakupa.” Jelini akacheka sana. “Usiku kucha utakuwa hapa.” Akimuonyeshea kifuani. Jelini furaha kama yote! Cheko la deko njenje. “Ukichoka?” “Tutabadilisha style za ulalaji mpaka papambazuke. Ila ukiwa mikononi mwangu.” Akamuona ameridhika.

    “Swali la mwisho kabla sijaondoka. Nani amekupa habari zangu?” “Jibu jioni. Ila ujue huna haja ya kubadilika. Nilikupenda na nakupenda hivyo ulivyo. Hope si sehemu ya maisha yetu. Habadilishi mtazamo wangu kwako. Katika watu wangu muhimu, hakuna atakayekubugudhi na kukutaka ubadilike. Ila ujue familia ya mchungaji ni waombaji sana. Hilo watakulazimisha. Huwa wana mkesha wa maombi mara moja kwa mwezi unao ambatana na mfungo, hiyo najua utakaribishwa.” “Hilo si tatizo.” Jelini akakubali bila shida. “Basi kama ndio hivyo, mpaka hapo tupo sawa. Si ndio?” Akatingisha kichwa kukubali.

    “Sisi kwanza. Ezra kama Ezra, na Jelini kama Jelini, mengine yote ni ziada na baraka zetu kutoka kwa Mungu. Mali na elimu havita tu define sisi, ila sisi kama sisi. Sisi kwanza, mengine baadaye.” “Hapo sawa.” “Na mimi si misheni town.” Jelini alicheka sana.

    “Ila nyinyi wawili mmezidi bwana!” “Mwenzio imeniongezea furaha, kuona umenikubali ukidhani nipo chini, hujanipendea mali. Maana sasahivi ni ngumu kuoa Jelini, ngumu sana. Huwezi jua anayekupenda kwa dhati au anayetaka kukutumia tu.” “Nakupenda Ezra.” “Najua. Tutazungumza vizuri usiku. Acha nirudi kazini, na nimekuletea matunda.” Jelini akafurahia kana kwamba amepewa alumasi. “Asante kujali Ezra. Asante sana. Na wewe nimekuletea matunda.” Ezra hakutegemea.

    Akafungua kwenye gari yake, kiti cha nyuma. Yalikuwa matunda mengi tu. Ila yamepambwa maalumu kama zawadi. Kadi nzuri sana ya love, na maua mekundu ya roses. Mazuri, fresh, yamefungwa pamoja. Yananukia!

    “Kama Valentine!” Ezra mwenyewe akashangaa na kushindwa kuamini. “Basi nikwambie, kwetu sisi, na mpenzi wangu Valentine ni kila siku.” Hilo likamfurahisha sana Ezra, asiamini. Akaanza kupokea. “Mbona mimi sikupi vikiwa vimefungwa vizuri hivi!” “Sio mashindano Ezra. Mwenyewe ulisema. Halafu wewe unafanya zaidi yangu. Unaacha kazi, unapambana na foleni kurudi mpaka kule Tegeta kutokea huku Posta, kuniletea mimi matunda! Hata ungeyaleta kwenye mfuko hayajaoshwa pia ningekushukuru sana.” “Umejawa shukurani Jelini!” Kisha akampa kiss ya kama dakika mbili hivi, akamuachia.

    “Asante sana, Jelini mpenzi wangu. Nimefurahi sana.” “Na usifikiri hii ndio zawadi yako ya leo! Hapana. Mimi nimekuandalia zawadi nzuriii. Ila sana.” “Mimi nilijua zawadi ndio hii!” “Hata kidogo. Jiandae kufurahi sana usiku. Wewe sasahivi rudi kazini. Mkale hayo matunda na Junior. Nimechukua matunda mengi na kuna uma mbili nikijua mtakula naye.” “Yalivyo hivi, tutavuta nyuki ofisini kwetu.” Wakaagana, na kutawanyika.

Ofisini.

    Junior mwenyewe alibaki ametoa macho wakati Ezra anaingia. “Ni Valentine, kwamba nimesahau?” “Basi nikwambie, kwetu sisi, na mpenzi wangu Valentine ni kila siku.” Junior akacheka sana jinsi alivyozungumza. “Jelini huyo?” “Nani mwengine? ‘Na usifikiri hii ndio zawadi yako ya leo! Hapana. Mimi nimekuandalia zawadi nzuriii. Ila sana’.” Junior hana mbavu vile anavyomuigilizia. “Namuuliza unataka nini, maana aliingiwa hofu na nafasi aliyojua ninayo kwenye maisha.” Ezra akamsimulia mazungumzo yao.

    “Sasa alivyotulia nikamuuliza kama ameelewa. Yaani yeye akaanza kushangazwa kwamba katika hayo maelezo yangu hakuna mpango wa kumkumbatia!” Junior hana mbavu. “Jelini! Wenzake wakiona mchumba ana pesa wanaanza mahitaji!” “Kama ulikuwepo! Nikamwambia hivyohivyo. Yeye anataka akumbatiwe na ajaliwe yeye kwanza. Hata tukiwa na watoto wengi, yeye abakie wa kwanza. Namuuliza kwani unaona tutakuwa na watoto wangapi? Anasema yeye ameona tuna watoto wengi sana, inabidi tutumie uzazi wa mpango, tuachie wengine.” Junior hana mbavu.

    “Jelini! Amenipa hayo matunda na amesema kuna uma mbili akitaka na wewe ule.” “Huyu ni wakukimbiza kanisani Ezra.” “Sasa naona tunarudi nyuma Junior!” “Katika hili usinisubiri. Endelea tu. Ukicheza tu, watakupora.” “Na alivyo mzuri! Leo yenyewe amenibabaisha. Jelini ni mzuri bwana! Inabidi tununue pete nzuri. Si unakumbuka alimwambia hata Ester anapenda vitu vizuri?” “Lazima. Anastahili. Umepata size sasa?” Junior akasimama ili kufikia matunda yaliyokuwa bado yametunzwa vizuri kwa kuvutia.

    “Nimepata aisee. Ana vidole vizuri huyo! Nina uhakika anavaa size 6.” Watu wakaanza kujaa hapo ofisini kwao, wakaanza kugawana hayo matunda na utani kibao. Ila ukweli Jelini alijua kuweka furaha kwa Ezra. Aliifanya siku yake ikawa ya furaha sana. Maua aliyaweka mezani kwake akabaki akiyaangalia huku akifanya kazi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kila penye jema kuna changamoto zake. Zipi tena kwa Jelini na Ezra?

Yapi yanawajia Wakati harakati za kuchumbia zikiendelea? Maana andiko husema,  

(1 Wathe 5:3)  'Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba... '

Huku nako marafiki hao wafanyao kila kitu pamoja, uhalisia wa maisha unaanza kuwatenga. Wakati kwa Ezra ndio kuna noga, kwa Junior kumeingia dosari.

Ni nini kitaendelea?

USIPITWE.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment