Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 24 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 24

Huku kwa Junior, alihakikisha anapata muda na Hope. “Najua umechoka, ila tafadhali 
naomba tuzungumze.” Hayo alianzisha kabla hajamshusha nyumbani kwao. “Nashukuru kwa msaada wa pale kanisani, na harusi ya Ester. Lakini kuna mambo yanayotuhusu sisi moja kwa moja…” “Unamaanisha Jelini?” Junior akatulia akimwangalia.

    “Maana kama ni huyo Jelini, mimi simfahamu na wakati nilipotaka kumfahamu, alinidharau. Nikaona nimuache tu. Maana najua Ezra ni rafiki yako wewe na…” Hope alizungumza kwa kupaniki mpaka akamshangaza Junior. Akatulia kimya akimsikiliza. Aliongea na kuongea bila Junior kupata sababu yakueleweka.

    “Kwa hiyo ndio hivyo.” “Umemaliza? Maana mimi ndiye niliyekuwa nikizungumza.” Hope akagundua Junior amebadilika. “Nakusikiliza.” Junior akatulia kidogo kisha akaendelea. “Najua unafanya vizuri sana kanisani. Lakini mambo yanayotuhusu sisi. Nikimaanisha mimi na wewe, nafikiri ndiyo tuyape kipaumbele. Kama bado unaona kuna nafasi kati yetu.” Hope alishituka hakutegemea.

    “Kwamba leo unaona kuna tatizo kati yetu sababu ya Jelini!?” “Sababu ya mahusiano YETU. Wakati wote, wewe umekuwa kipaumbe changu. Chochote kinachokuhusu wewe, nimekua nikikitilia maanani, na kukuunga mkono bila kuzembea. Kitendo cha mimi kutaka kukutambulisha Jelini. Mtu wa muhimu sana kwa Ezra, ukakipuuza kwa kumdharau waziwazi kwa kazi anayofanya, mbele yao, binafsi sijapenda Hope.” “Kwa sababu nilikuwa na haraka na pia kwa kuwa nilishakutana naye kwenye shuguli za Ester nikajua ni kama tumeshafahamia, na tungefahamiana naye zaidi kwenye mazingira tulivu.” Akajua anajitetea tu na akawa ameshajichanganya.

    “Nisikilize Hope. Kila kitu ni ziada, ila mimi na wewe ndio wa kwanza na muhimu. Sijui kama unanielewa? Siwezi kukupuuza wewe sababu ya kukimbilia majukumu mengine. Sijawahi kufanya na sitarajii kufanya hivyo. Ezra ni mtu muhimu sana kwangu.” “Naona kuliko mimi.” Akalalamika.

    “Nisikilize Hope. Ulinikuta na ramani nzima ya maisha yangu, akiwepo Ezra.” Hope hakuamini! Kwa mara ya kwanza Junior alimbadilikia vibaya sana. “Kama Ezra angekuwa tishio kwenye mahusiano yetu, ningekuwa tayari kubadilisha. Ila ulinikuta na Ezra. Nikakutambulisha kwake, akakupokea na kukuheshimu. Anakujali kwa hali ya juu sana, kama mimi tu. Leo sina wasiwasi kwamba nikioa na nikawa na watoto, endapo nikatangulia na kumuacha yeye, mke wangu na watoto hawatapata shida. Atalinda familia yangu, na mimi nitamfanyia hivyohivyo. Samahani kukwambia hili, sipo tayari kubadilisha hilo.” Mpaka Hope akaishiwa nguvu.

    “Sijui kama unanielewa Hope? Maana Jelini ni mtu muhimu sana kwa Ezra. Nilitarajia umrudishie fadhila. Kama vile alivyokupokea wewe na kukusogeza katikati yetu, nilitegemea ungemfanyia hivyohivyo Jelini, lakini si kumfanyia kama ulivyomfanyia leo! Kwa mara ya kwanza leo, wewe, umeanza kutengeneza madaraja ambayo hayajawahi kuwepo nyumbani kwetu tokea Ezra anakuja kwetu. Mama ameona na baba ameona wameomba tuzungumze.” Hope alishituka sana, akazidi kuishiwa ujasiri.

    “Pale kwetu Ezra anapendwa sana. Mama aliapa kumlea kama vile mimi. Baba ameomba tukizungumzie hiki kitu mapema, kabla hakijaleta matatizo. Leo Ezra kwa mara ya kwanza amejiona hastahili kuwa pamoja na sisi! Ameshindwa kujumuika na sisi, ameenda kukaa nyuma kabisa kama mtu baki! Hapana Hope. Tafadhali kama kuna tatizo naomba tuzungumze.”

    “Maana tumejaribu mara nne, lakini umemkataa kabisa Jelini! Tumeanza kwenye swala la picha. Ukakataa bila kufikiria ni kwa nini Jelini na sio mtu mwingine katika picha kama ile! Tukakuacha. Tukakujaribu mara ingine baada ya ile picha  yako kukamilika, pia ukakataa! Tena unakataa bila adabu, mbele ya watu, wazazi wakikuangalia! Halafu ukatufuata nikataka kukutambulisha kwake nikidhani pengine hujaelewa kuwa Jelini yupo pale kwa sababu kwanza mimi na Ezra tulimkaribisha, pili ni mtu wa Ezra! Lakini pia ukakataa! Haya, baba ametufuata, kutaka turudi kukaa mbele, meza uliyokuwa umekaa wewe ambayo ilikuwa maalumu kwa ajili yetu akiwepo na Ezra. Na ilikuwa wazi kabisa! Eti wanahamia pale, wewe unahama! Kweli Hope?! Pengine unipe sababu nitakayoweza kuielewa.” Hope kimya.

“Tafadhali unijibu Hope. Ndoa si kitu cha kufikirika. Ni uhalisia kabisa. Tunajenga kitu chetu. Sasa kama wewe hupendi ninavyopenda mimi, hudhani kama itakusumbua? Tutakuwa na maisha gani hayo?” “Kwa hiyo unataka kusema nini?” “Ndio nakuuliza wewe! Na katika hili tafadhali tuzungumze. Nataka kukusikia Hope. Na ukweli leo haikuwa nzuri. Hata Noah mwenyewe ameongelea hili. Tena yeye amesema mbele ya Ezra na Jelini, kuwa umemkataa Jelini. Sasa nataka kujua sababu.” Alivyoona amekabwa, akabadili gia.

    Akaanza kulia. “Mimi simfahamu Jelini, na hata nilipotaka kumfahamu wakati wa kitchen party alionekana hayupo tayari. Kama hakutaka ukaribu na mimi kabisa. Ndio nikaamua kuachana naye.” “Ulitegemea umfahamu vipi au urekebishaje hilo wakati ulikataa utambulisho, na hata alipokuja kukaa na sisi ulimkimbia?” Junior akaendelea kumkaba, na hapo Hope akajua katika hilo hatatoka. Machozi hayakusadia kabisa. Mchumba aliweza kuendelea na hoja yake akiyapita hayo machozi yake. Akasalimu amri.

    “Nimekosa Junior. Nitajirekebisha.” Hapo Junior akapoa. “Nashukuru Hope. Tafadhali linapofika jambo letu. Sisi wawili, kama familia, naomba ulitilie maanani. Maana baada ya yote, sisi tunabaki peke yetu. Sitaki tubaki peke yetu, baada ya kufanikishia kila mtu, hata kanisani, halafu eti sisi wenyewe tunakuwa tumeparanganyika! Hakuna amani! Hakuna heshima! Hakuna upendo! Hilo hapana kwakweli. Sisi kwanza, mengine baadaye.” “Sawa.” Akajibu hivyo na kuaga. “Usiku mwema.” Kisha akashuka garini.

    Ila ukweli aliingiwa hofu. Hakutegemea. Ni kama usiku huo Junior anayemfahamu yeye, mpole na anamuongoza katika kila jambo, usiku huo alichora mstari. Ni kama alivuka mstari ambao Junior alikuwa akiulinda kwa garama kubwa sana na hakutaka chochote kitokee, kwa garama yeyote ile. Ni kama alikuwa tayari kabisa kumuacha! Furaha yote ya harusi ikamuisha. Akanywea kabisa, asiamini.

Ezra&Junior.

    Ezra alipofika tu nyumbani akamtumia ujumbe Junior. ‘Nampenda sana Jelini. Ameahidi kusimama na mimi mpaka kifo. Nakusudia kumuoa. Inamaana atakuwa kwenye maisha yangu ya hapa duniani daima.’ Junior aliposoma huo ujumbe, akaelewa. Alishakuwa amepanda kitandani, tayari kukamilisha hiyo siku kwa usingizi. Ila mawazo yalimzuia kulala. Akaamua kumfuata nyumbani kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~

    “Nakuomba unisamehe Ezra.” “Tafadhali naomba unielewe. Sio katika kuombana msamaha, ila kuelewa alipo na anakotoka. Jema ametueleza historia yake. Kwa mara ya kwanza Jelini ndio anafanya kitu na kinaeleweka. Inawezekana kwa wengine kinaweza kisiwe cha kisomi, lakini Jelini amefanikiwa kwenye anapowekeza juhudi zake. Ametoka kwenye kudharauliwa kwa maisha aliyoishi. Mimi kwangu ni nguvu yangu. Udhaifu wa kule ndio natumia mimi kama silaha ya kumvuta kwangu. Sasa kama anakutana na yale aliyoyaacha kule, ana sababu gani ya kubaki kwangu na Colins amerudi!?” Ezra akaendelea kwa msisitizo.

    “Leo umemsikia akisema wazi kabisa alidhania huku kwa watu tunao mjua Mungu ingekuwa tofauti. Sasa ana sababu gani ya kubaki na mimi, apitie yaleyale?” “Samahani sana Ezra. Tafadhali naomba unisamehe. Ila nimezungumza vizuri na Hope. Naamini ameelewa. Ameomba msamaha, na ameahidi kubadilika. Tafadhali naomba unisamehe. Nahisi ni kama sikuwa nimeandaa mazingira mazuri kwa ajili ya Jelini! Kwa sehemu nimejisikia kuhusika kuchangia usiku aliokuwa amejiandaa nao vizuri, kuuharibu. Lakini unajua nampenda Jelini. Siwezi rudia kosa tena. Tutahakikisha safari ingine akija, anajisikia nyumbani.” “Nashukuru.” Bado alikuwa na nguo za harusini.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Akahisi kana kwamba ndio ameingia, na bado alikuwa akichat. Akajua ni Jelini tu. “Kwamba ndio umerudi?!” “Tulikuwa tumekaa palepale hotelini, kwenye gari yangu. Ndio nimehakikisha Jelini amelala, na mimi nataka nikalale.” Akamuona anacheka kwa hisia. Akajua ni mapenzi tu. “Nini?” “Ni mengi Junior! Acha tuzungumze kesho kazini.” “Acha masihara!” Ezra akacheka kama anayevuta kumbukumbu.

    “Kwa kifupi, nataka ujue, maishani mwangu kote, sijawahi shika mikononi mwangu, kitu kizuri na cha thamani kama Jelini.” Junior alicheka sana. “Junior! Acha kaka! Mimi na utuuzima huu, sijawahi aisee! Akitulia hapa kifuani! Acha!” “Pesa haioni ndani?” “Hii ya madafu? Hakuna kaka. Mtoto kama sufu! Halafu sasa anajua kutulia mikononi! Nimeshindwa kujizuia.” “Acha masihara Ezra!” “Aisee nimeshindwa Junior. Nimepata kiss hiyo, haijawahi tokea!” “Ezra!” “Kabisa. Na nikahakikisha nimeitendea haki, mpaka Jelini mwenyewe ameikubali.” Junior akacheka ila akawa kama anayefikiria.

    “Najua nimeku disappoint. Lakini, Junior! Nimeshindwa. Kwanza alikuwa akitaka kunibusu shavuni. Wakati nageuka ikawa kama bahati mbaya. Midomo ikagusana. Akapaniki kwa kuwa nilishamwambia nasubiri mpaka ndoa. Akajua ameharibu. Akataka kuondoka kwa kupaniki. Nikasema nimtulize kwa kumkiss kidogo, asiondoke akiwa amepata wakati mgumu ukumbini na pale. Nikajua akiondoka usiku ule, vile, nitakuwa nimepoteza pointi zote.”

    “Aisee yule mtoto  ni mtamu Junior! Nimesalimu amri. Sikujua kama unaweza mkiss mtu zaidi ya dakika 5 mfululizo, na bado usiridhike! Aisee utanisamehe kwa kuvunja maagano yetu.” “Hapana. Umebahatika Ezra. Mimi nakuelewa. Lazima uweke msingi unaooleweka, lasivyo utakosa thamani. Na uzuri Jelini anakupenda na mwenyewe anakiri anakuhitaji. Halafu anaonekana anahekima. Moyo wake hauna hila.” Aliongea kama ambaye anawaza yake. Ezra akaelewa ikabidi ajishushe.

    “Nisikilize Junior. Hope unamjua jinsi alivyo. Na wewe ulimpenda kama alivyo na ile haiba yake. Kwa hili, ameomba msamaha, na amesema atajirekebisha, si ndivyo?” “Lakini leo amenifanya nifikirie mara mbilimbili. Kitendo cha kunikatalia bila adabu mbele ya watu! Hakika kimenishitua sana Ezra. Sana. Unajua mpaka baba ameniomba nizungumze naye.” “Haiwezekani Junior!” “Kabisa. Wakati wanaondoka na mama, wakaniomba niwasindikize kwenye gari yao. Mama amesema Jelini anaonekana ana moyo mzuri sana. Upo wazi kuusoma moyo wake. Anaonekana ana upendo na kujali. Hana hila na mtu. Anasema alimuona hivyo tokea anatambulishwa kwake na Jema, kwenye swala la kitchen party. Baba ameomba nizungumze na Hope, tujue kuna tatizo gani.” “Sasa yeye amesema kuna tatizo gani!?” Ezra naye akataka kujua.

    “Kwani anamfahamu  vizuri Jelini!?” “Ni kumuona tu! Na ni kama aligusia eti huko kwenye shuguli za Ester, eti ni kama Jelini alimpuuza. Akawa akimuongelesha sijui Ester na mama tu na watu wengine, yeye akampuuza! Sasa sijui ni kweli au ni kujitetea tu, lakini bado sidhani kama hiyo ni sababu yakutosha. Aisee mama hajapenda kabisa. Na ameongea kabisa, kwamba tuweke sawa hilo jambo. Jelini ni binti mzuri na alijiandaa kwa wakati mzuri. Kitendo tulichomfanyia, kitamnyima uhuru wa kuja kurudi tena kwenye shuguli zetu.” Hapo Ezra akanyamaza.

    “Sijui Ezra! Sijui aisee!” “Naomba tufanye kama alivyosema Jelini.” “Ule ni ushauri mzuri sana, lakini sipo tayari kuutekeleza Ezra.” Mpaka Ezra akashituka. “Hapana aisee! Sina sababu ya kufanya hivyo. Kwa nini?! Ifike sehemu achague kama atakuwa mmoja wetu au la.” Ezra akajua amekasirika. Akamtuliza.

    “Leo tumekuwa na siku ndefu. Tena tokea jana. Hatukulala vizuri sababu ya Jelini. Leo ni Hope. Tafadhali tuchukue hatua moja nyuma, tutulie. Ona jana kwangu mambo yalivyokaa sawa! Tafadhali tutulie.” Akazungumza naye, mpaka akamuona ametulia kabisa. Ndipo wakaagana na kwenda kujipumzisha kwa kazi kesho yake.

Jumatatu.

    Wakati wakipanga mipango ya jinsi ya kumsuprise Jelini na pete ya uchumba, wakiwa ofisini kwao, akapata ujumbe kutoka kwa baba yake. Ilikuwa kama barua pepe iliyopigwa picha kisha akamtumia kijana wake. Akaifungua. Ezra akamuona kadiri anavyosoma, ndivyo anavyobadilika. “Ni nini?!” Akamuona anatingisha kichwa kwa masikitiko huku akiendelea kusoma. Akasimama kutoka kwenye meza yake na kwenda kuchukua simu ya Junior.

    Ilikuwa barua kutoka kwa Hope, akimuandikia mchungaji wa kanisa, ambaye ni baba mkwe wake, kujiudhuru haraka iwezekanavyo, kwenye nafasi yake. Hakutoa sababu. Lakini akasema kuanzia siku hiyo, anajitoa madarakani. Ezra akatulia kwa sekunde kadhaa na kumtizama Junior. “Utafanyaje?” Akamuona anafikiria, kisha akampigia simu baba yake.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Akamsikia akimsalimia na kwenda moja kwa moja kwenye pointi ya msingi. “Kwanza niombe radhi kwa hili la kushitukizwa, baba.” “Wewe unajua sababu!?” Mzee akauliza. “Hapana. Mimi ndio naisikia kutoka kwako hata mimi hajaniambia. Sasa kwa sababu hajasema sababu, naweza hisi ni hasira sababu nilizungumza naye jana. Na huku ni kuzira tu. Tumempa majukumu makubwa sana pale kanisani. Na kwakuwa kila kitu kinakwenda sawa, anaweza bweteka, akadhania ni juhudi zake mwenyewe kumbe hii ni kazi ya Mungu. Na Mungu ana  watu wengi sana.” Ezra kimya akisikiliza.

    “Sasa kwa kumsaidia, tafadhali mjibu kuwa maombi yake yamepokelewa. Na ungependa makabidhiano yote kabla ya ijumaa ili kujipanga vizuri.” “Una uhakika Junior?!” Mzee mwenyewe hakutegemea. “Kabisa baba.” “Sasa nani atashikilia hayo majukumu? Nashauri tuzungumze naye, tumsihi aendelee.” “Hapana baba. Hutambembeleza Hope. Hiyo ni kazi ya Mungu, na sisi wote tumekubali kutenda kazi pamoja na wewe. Atakayeweza kusimama na kumtumikia Mungu kwa moyo wa unyenyekevu, atakaribishwa. Ambaye hawezi, basi. Hatutambembeleza mtu. Hatuwezi kuendesha mambo kwa namna hiyo.” Junior akaendelea ila hata kumshangaza baba yake. Kwamba mchumba asibembelezwe! Akatulia kusikia mwisho wake.

    “Nitasimamia hiyo nafasi mpaka utakapopata mtu mwingine atakayeweza kuikaimu. Ila kwa sasa mwache tu.” Ikabidi Mzee akubali tu. Hakuwa na jinsi kwa sababu ni Junior na ameahidi kusimamia mwenyewe. Hata hivyo Junior ndio kama mwenyekiti anayewaongoza wote bila wao kujua, ila baba yake alijua. Ana jinsi yake ya kuongoza kwa chinichini huku akikupa wewe sifa. Kama huna akili ya kufikiria, unaweza kujikuta una vimba kichwa, kwa akili ya Junior.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Hope akaandikiwa barua ya kukubaliwa ombi lake. Mzee wito ni mchungaji, aliiandaa vizuri tu hiyo barua. Kiuchungaji kwa kondoo wake. Kwamba ombi lake limepokelewa kwa heshima. Akamshukuru kwa kujitolea kwa hali na mali. Hapo akataja majukumu mazito ya kikanisa aliyokuwa akiyafanya na kuyakamilisha kwa uaminifu na juhudi zake akijitolea bila kuchoka. Mchungaji akamshukuru kwa dhati. Na kumtaarifu kuanzia siku hiyo anapokelewa majukumu yote ya ukatibu. Itaandaliwa barua ya kupeleka benki, ya kutolewa kwenye waweka saini kwenye hundi za kanisa. Atatolewa katika security system zote za kanisa ambazo kabla ya ijumaa aliombwa afike ofisi za kanisa akabidhishe funguo zote za jengo na mafaili ya kanisa.

Kiberiti Kilichojaa.

    Hope alikuwa akitingisha kibiriti, akakuta safari hii kimejaa. Alipopokea hayo majibu, alishituka mpaka tumbo likaanza kumuuma. Hakutegemea hivyo hata kidogo. Alichotaka kukifanya mchungaji, ndicho alichodhania kingefanyika. Kuitwa na kubembelezwa. Kwa kuwa ni kweli aliiwezea hiyo nafasi. Pamoja na shule yake, akaweza kuongoza ibada zote mbili. Hakutegemea kuvuliwa uongozi kwa barua pepe moja tu! Ukweli alitishika. Hofu ikamuingia akijua ameharibu. Akatamani ile lawama ya jana yake usiku, kuliko hiyo fedheha. Inamaana itajulikana si kiongozi tena! Akazidi kufedheheka.

~~~~~~~~~~~~~~~

Nafasi Zinazowajia Watu Maishani Na Kutufanya Tubweteke, Tukiona Tunastahili. Iwe Ndoa, Malezi Kwa Watu Mungu Ametuamini Nao Hata Wafanyakazi Wetu Wa Ndani, Mahusiano, Kazi, Biashara.

 Inaweza Fika Mahali Ukokosa Sababu Ya Kung’ang’ania Ulicho Nacho, UKADHARAU, Mpaka Mungu Anapokitoa Mkononi Mwako Na Kumkabidhi Mwingine Ndipo Unaona UMUHIMU WAKE.

Wakati Mwingine hubahatika Kupata Nafasi Ya Pili, Na Wakati Mwingine Tunapoteza Kabisa.

Umakini Na Tulivyo Navyo Mkononi, Ni Muhimu Sana. Weka Heshima Kwenye Chako/VYAKO Na Kumbatia Kwa Moyo Wako Wote Na Akili Zako Zote Kana Kwamba Hakutakuwa Na Kesho,

Au Hutaki Upokonywe.

Kila Kitu Tulicho Nacho Ni Dhamana Tu, Na Vyote VINA Muda.

Usikubali Majuto Yakaja Kuwa Mjukuu.

INAENDELEA.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment