~~~~~~~~~~~~~~~
Njiani akampigia simu Ezra, kuwa ndio anaelekea huko
ukumbini. Mapigo ya moyo ya Ezra yakaanza kwenda kasi. Ni Jelini.
Akatoka kabisa nje ya hoteli kumsubiria. Hata yeye alikuwa amependeza. Mavazi
ramsi ya harusi. Aliliona gari la Jelini likiingia. Akasogea kule alikopata
nafasi ya kuegesha gari yake.
Akaenda mpaka mlango wa dereva. Akafumfungulia. Ukweli Ezra
alibabaika kwa wazi kabisa alipomuona Jelini. Alipendeza kupita kawaida.
“Jelini!” Akacheka akijua anachomaanisha. “Umependeza mno! Na hiyo rangi
ya gauni imekukaa vizuri sana mwilini mwako!” “Nimefurahi kama umependa.
Nilitaka ufurahi. Sitaki kukuabisha.” “Wewe ni mzuri Jelini. Hakuna
utakachovaa kikaniabisha. Umependeza sana.” “Asante. Ila na wewe suti
yako imekukaa vizuri sana. Imekupendeza na inaonekana ni ya pesa nzuri sana.”
Ezra akacheka akiwa kama haamini.
“Samahani nimechelewa.” “Hamna shida. Nimefurahi umekuja
kuungana na sisi.” “Nipo hapa kwa ajili yako wewe Ezra. Mimi hao wengine
siwafahamu.” Ezra akacheka kwa furaha. “Basi nimefurahi umeungana na mimi.
Asante.” “Karibu. Sasa sasahivi wanafanya nini?” “Ni picha tu. Kuna sehemu
nzuri sana humo ndani ya kupigia picha.” “Sasa si utapitwa? Twende ili usikose
picha za familia, za ukumbusho.” “Hamna shida. Kuna ambazo nishapiga. Ila nina
ombi moja.” Jelini akacheka akikubali.
“Naomba leo tupate picha moja, nipate za kuweka na mimi kama
kumbukumbu.” “Ninavyopenda picha, utachoka wewe.” “Kweli hutaona usumbufu?”
“Wewe nisumbue utakavyo.” Akacheka akimtizama. “Aisee siamini! Jelini
umependeza kupita hivi ninavyokwambia.” “Asante. Nimefurahi kama
nimekuwakilisha vizuri.” “Naona umepitiliza.” Wakapiga baadhi ya picha zao hapo
nje. Mpaka Ezra mwenyewe akaridhika ndipo wakaongozana mpaka ndani walipokuta wateja
wengine wakila, wakaendelea kwenda upande wa harusini, wanakopiga picha.
Junior alipowaona wanawasogelea, akaacha umati na kuwafuata.
“Jelini umependeza sana!” “Asante Junior. Hata na wewe umependeza sana.”
“Asante. Vipi kichwa?” “Kimepoa.” “Pole.” Wakawa wanaitwa hao wawili wapige
picha na maharusi bila wasimamizi.
Ilikuwa wapige hiyo picha na maharusi, wao kina Ezra, na wachumba
zao pia. Sasa Junior yeye ndiye anamchumba rasmi, Ezra angekuwa hana mtu. Yaani
mchumba. Lakini Jelini si ndio amekuja sasa! Inamaana wangekuwa tayari 6. Picha
ingekuwa imekamilika. Wakageuka ili kuwasogelea maharusi watu
wakimshangaa zaidi Jelini jinsi anavyovutia.
“Nafikiri tunaweza piga na Jelini.” Junior akatoa wazo
lililomfurahisha sana Ezra. Lakini mchumba wa Junior akadakia kwa haraka na kwa
sauti ya juu. “Ni sisi tu na maharusi.” Ikawa kama anamkataa Jelini.
Jelini akawa muungwana, maana alishamuelewa kuwa hamtaki kwenye hiyo
picha. Akajiwahi ili kuleta amani. “Nyinyi endeleeni tu, mpate picha ya
ukumbusho.” “Na wewe unatakiwa kwenye kumbukumbu hii ya harusi. Twende.” “Sasa
hiyo itakuwa picha yenu. Hii ni yetu, na watu wanasubiria. Acheni kuvutana.
Njooni.” Akasisitiza huyo mchumba mtu, na kufanya kila mtu kubaki wakiwatizama
wao.
Ni kama kile kitu Ezra na Junior hawakukipenda! Jelini
hakuwa amemuona mchungaji. Akasikia sauti yake kwa pembeni. “Jelini, mama,
umepona kichwa?” Akageuka na kumuona. Akacheka na kumgeukia tena Ezra kabla
hajaenda kwa mchungaji aliyekuwa kama anaokoa jahazi katika sakata la
picha. “Nenda kapate picha ya ukumbusho, mimi naongea na mchungaji.” Ikambidi
Ezra akaungane na maharusi, Junior na huyo mchumba mtu bila wasimamizi.
“Shikamoo tena.” Jelini akamsalimia mchungaji akimsogelea.
Akacheka na kuitika. “Marahaba tena.” Jelini mwenyewe akacheka. “Vile tu
kuja nyinyi pale, mimi nimepona kabisaaa. Ujue wewe ni mchungaji mkubwa sana,
halafu mchungaji mashuhuri, halafu tena ni mtu mzuri sana?” Mchungaji akacheka
asijue kama ni swali au comment! “Kuja nyumbani kwetu ni kama muujiza! Nimefurahi
sana mmefika kwetu. Sisi hatupatagi wageni wa maana kama yako. Kwahiyo
ukumbuke ahadi yako. Urudi tena. Nitakupikia vitu vizuri vitupu. Halafu
vingiii.” “Jelini hujambo?” Alikuwa mama Junior, mke wa mchungaji.
Akamsalimia na goti la kinyaki. “Umependeza sana
binti yangu. Sana.” “Asante mama. Na wewe umependeza, kama mchungaji. Na
hongereni kwa kuozesha. Shuguli zenu zote zimekua nzuri sana!” Hao
wanafahamiana kwa karibu, tokea Jelini awakodishe vitu vya shuhuli ya huyo
binti yao. Ndio ukaribu ukaongezeka na mama mchungaji huyo anayezungukwa na
wakina mama wa maana.
“Ujue wenzio leo tumetembelewa na mchungaji nyumbani kwetu?”
Mama Junior akaanza kucheka. “Tumekuwa wamaana wenzio! Na ameahidi atarudi
tena.” “Na mimi nimepewa taarifa. Kichwa kimepona?” “Mimi naona hakitakaa kiume
tena.” “Sababu ya mchungaji?” “Kabisa!” Wote wakacheka.
Akaguswa bega, akageuka. “Ezra!” Hivyo alivyomuita na cheko
limemjaa usoni kama ameona alumasi. “Naomba nikatishe mazungumzo kidogo, twende
tukapige picha.” “Sawa.” Jelini akakubali bila shida. Wakati Ezra na Jelini wakiwasogelea
maharusi, huyo mchumba wa Junior akaondoka hapo kwa maharusi walipokuwa
wakipiga picha, kama ambaye hataki kupiga picha nao. “Mbona sasa
unaondoka?!” Akauliza Junior kwa mshangao. “Mimi nishamaliza, naendelea na
mengine.” Akaondoka.
Jelini akaendelea kuwasogelea maharusi. “Nyinyi couple
yenu nzuri sana. Mmependezana. Na mnaonekana mnapendana sana. Mmependeza
mno.” Sasa Ester alishamuona Jelini siku ya kitchen party yake na akajua
ndiye mwenye vile viti walivyokalia, wakapata na muda wa kusalimiana na kama
kawaida yake, Jelini maneno mengi, akamsifia sana Ester akimpamba kwa maneno
mengi. Hao maharusi wakacheka kwa pamoja. “Wewe Jelini kila kitu chako kizuri,
mpaka viti!” “Sasa kwani mimi siku ile nilikwambiaje?” “Unapenda vitu vizuri.”
Akajibu Ester nakufanya wacheke kidogo.
“Ila Ester umependeza sana! Na hiyo furaha usoni, inaonekana
inatoka ndani yako inakufanya hata ulivyopambwa uvutie! Umependeza sana.”
“Asante Jelini. Na nashukuru kwa kuja.” “Mimi mwenyewe nimefurahi kuwa hapa.
Acha tupige picha tuwapishe wengine. Tutazungumza wakati mwingine. Nisikuchoshe
na maneno mengi, leo siku yako.” Wakapiga picha, na kusogea pembeni.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akamshika Ezra mkono kama anayetaka kumnong’oneza kitu, Ezra
akampa sikio. “Sasa mbona siwaoni wazazi wako? Au hawajaja?” Ezra akatoa
tabasamu fulani hivi, lakini Jelini akajua sio la furaha. “Nitakwambia
baadaye.” Jelini akakubali kwa kutingisha kichwa akimwangalia kama ameanza
kumuhurumia kutoka na sura iliyobadilika gafla baada ya swali.
~~~~~~~~~~~~~~~
Wakaona waondoke hapo, wakatafute sehemu ambayo itakuwa na
sehemu ya kukaa. Wakaenda sehemu ya wateja wengine ambao hawaja hudhuria harusi
hiyo, nje tu, karibu na baharini. Wakakaa hapo wakisubiria kuingia ukumbini.
“Samahani kwa kile kilichojitokeza pale kwenye kupiga picha.” “Wala usijali.
Najua kila mahali kuna mipango yake. Ila ujue nimefurahi umekuja kuniona.
Nimefurahi sana Ezra. Sikutegemea!” “Nakupenda Jelini. Naona tatizo lako
ni langu. Sitaki upate shida peke yako.” Jelini akacheka kidogo na kupotelea
mawazoni. Akajua amerudi kwa Colins kimawazo.
“Samahani sijakupa jibu juu ya Colins mpaka sasa.” Akamshitua
Jelini na kumrudisha hapo kimawazo. “Hap…” Kabla Jelini hajamalizia anachotaka
kusema, wakasikia Junior akimuita Ezra. Wakageuka kwa pamoja “Mbona mmejificha
huku!?” “Nimeona kuna upepo mzuri. Vipi?” Akasogea Junior kama mwenye kitu
chakutaka kusema, akasita. Ezra na Jelini wakabaki wakimwangalia. Alikuwa bado
amesimama.
“Labda niombe radhi kwa kile kilichotokea pale kwenye picha.
Tafadhali usijisikie vibaya. Hope ni mtu wa mipango. Na ikiwekwa anapenda
kuisimamia.” “Usijali kabisa. Mimi mbona naelewa tu. Mambo hayawezi kwenda
vizuri bila utaratibu. Ona kulivyopendeza! Hongereni sana.” “Asante.” Jelini
akawaona bado hawapo sawa.
Akaona abadili hiyo hali. Akaanza kucheka. “Sasa unacheka
nini?” Junior akamuuliza na yeye akianza kucheka. “Kwa hiyo nyinyi mpo kama
mapacha? Maana na suti zenu nzuri, halafu pia zimefanana!” Wakacheka.
“Mmependeza sana.” Angalau Junior akaweza kukaa hapo.
“Kwani nyinyi mmefahamiana kwa muda gani?” Wakaangaliana na
kucheka. “Tokea kidato cha kwanza. Shule ya sekondari Pugu. Tulipangiwa bweni
na cubic moja. Kuanzia hapo ndio tukawa pamoja.” “Mpaka chuo!?”
“Alichosomea Ezra, na mimi ndio nimesomea. Alama alizopata yeye darasani na
mimi hivyohivyo.” “Basi mlikuwa mkiigiliziana.” Wakaanza kucheka.
“Jelini! Sasa kwa nini usiseme tulikuwa tukisoma pamoja?”
“Ndio mpate kila kitu sawa!? Mimi nina wasiwasi na nyinyi bwana.” Utani ukaanza
hapo. Wakajisahau.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akawafuata kijana mmoja hivi, akaanza kuongea kabla
hajawafikia. “Mnaitwa na dingi.” “Acha kumuita hivyo bwana!” Akakoroma Junior
akisimama, yeye akikaa. “Sasa mbona wewe unakaa?!” “Anawaita nyinyi. Sio
mimi. Maana anataka kunichanganya tu. Bora nikae hapa.” “Huwezi kukaa hapa
wakati muda wa kuingia ukumbini umefika. Acha kumkorofisha mzee, wakati unajua
leo ni siku ya Ester. Twende.” Junior akazidi kumsisitiza. “Kwani nyinyi
mnajisikije bila kuniona mbele ya macho yenu kila wakati? Si nimesema nakuja!?”
“Acha ubishi Noah. Twende.” Ezra akaweka msisitizo. “Au unataka na sisi tutumwe
kuja kukuita?” Ezra akaongeza swali.
Mara huyo Hope akaja na yeye. “Mbona mnatafutwa, halafu
nyinyi mmejificha huku?” “Hatukuwa tumejificha, tumekaa tu huku kwenye upepo
mzuri. Vipi?” Akajibu Junior akimsogelea. Jelini na Ezra walishakuwa wamesimama
tangia aanze kulalamika. Jelini alishamuona ni kama hajampenda, na yeye
akajituliza. Huyo Noah akawa amebaki amekaa tu akiwatizama.
“Huyu ni Jelini.” Junior akawa anatoa utambulisho
kama kutaka wafahamiane zaidi. “Namfahamu. Si anafanya biashara ya kukodisha vitu
vya harusi huyu? Namfahamu vizuri sana.” Akajijibu mwenyewe ila kama kwa dharau
kidogo akimpuuza huyo Jelini. Akafupisha kabisa utambulisho na kuongeza. “Mnatafutwa.
Tusiendelee kupoteza muda hapa, tukitengeneza mapumziko yetu, au kikundi
kingine wakati leo ni shuguli ya Ester. Sio sawa. Twendeni.” Akajibu hivyo na
kuongoza njia. Junior alipoa, mpaka ungemuhurumia. Ezra akamgeukia Jelini,
akamshika mkono akamuongoza njia. Jelini akawa anamfuata kwa nyuma, kimya.
Ukumbini.
Walipofika ukumbini, Ezra akafanya makusudi kujivuta mpaka
wote wakaingia na kukaa, akaenda kutafuta sehemu ya kukaa kama waalikwa tu
wengine, Jelini asijue kuwa walishakuwa na sehemu maalumu ya kukaa hao ndugu wa
bibi harusi. Tena akatafuta sehemu mwisho kabisa ya ukumbi kama anayeepusha
shari. Shuguli ikaanza, ndugu wa bibi harusi wamekaa sehemu maalumu upande wa
mbele kabisa. Ukweli ilikuwa shuguli ya kifahari. Kwamba huyo Ester alikuwa
akiolewa pazuri. Jelini na Ezra wakajituliza hapo nyuma.
Alipomuona Ezra amepotelea mawazoni, akavuta kiti karibu
yake kabisa, akamchukua mkono wake na kuupakata vizuri. Ezra akatoa tabasamu.
“Hii harusi inaonekana imeandaliwa kwa kiwango cha juu sana!” “Jamaa mwenyewe
anayo pesa.” Akajibu Ezra. “Nimefurahi upo hapa na mimi.” “Mimi mwenyewe
nimefurahi tupo wote.” Hapo wanaongeleshana wapo karibu, wanaangaliana kana
kwamba ukumbi mzima wapo peke yao, mambo yakiendelea.
Katikati ya harusi ikawa kama Junior ndio amempata Ezra.
“Mbona mmekaa huku!?” Jelini akamtizama Ezra. “Nimeona hapa patatufaa. Hamna
shida. Vipi?” “Nilikuwa nikiwatafuta, muda wa utambulisho. Twendeni.” “Nakuja.”
Akajibu Ezra. “Na Jelini?” “Naomba yeye tumuache tu. Ila mimi nitakuja.” Junior
akafikiria kidogo, akaona akubaliane naye. Akaondoka.
“Unisubiri, nitarudi baada ya utambulisho.” “Hamna shida.”
Wakaangaliana kwa muda, Jelini akacheka taratibu na kuinama. Akambusu shavuni
na kusimama kisha akarudi kumnong’oneza. “Nakupenda Jelini. Usije sahau.” Kisha
akaondoka bila yakusubiri jibu, ila ni kama alibadilika. Hakuwa na ile furaha
aliyomkuta nayo alipoenda kumpokea garini. Akajua mambo ya Hope hakuyafurahia.
Jelini akatulia na kupotelea mawazoni.
~~~~~~~~~~~~~~~
Mchungaji akapewa nafasi ya kutambulisha alioongozana nao.
Jelini akajiweka sawa. Akaanza kusema kuwa Ester anao kaka watatu. Junior, Ezra
na Noah. Ndipo akaelewa Noah ni kijana wa mchungaji. Swali likabaki ni mdogo wa
Ezra au Junior wa kuzaliwa tumbo moja? Lakini mchungaji akaongeza kuwa akitoka
huyo Ester ndio Junior kijana wao wa mwisho. “Sasa huyu Ezra yeye wazazi
wake na ndugu zake wa kuzaliwa pamoja mbona siwaoni?!” Akajiuliza macho
mbele.
Hapo mama mzazi wa Ester alikuwa pembeni ya mumewe. Kisha
akasikia akitambulishwa Hope ambaye ni rafiki kipenzi wa Ester na mchumba wa
Junior. “Kumbe hawa wapo serious!” Akajiwazia Jelini akisikiliza
utambulisho na vigelegele. Mchungaji akatambulisha wote mpaka kina bibi na babu
za bibi harusi, lakini akamalizia na utambulisho uliomshitua sana Jelini.
“Yupo mgeni wetu mwingine. Na leo nilikuwa naye baada ya
ibada. Hapa nimemtizama simuoni tena. Lakini naye ni binti yangu, rafiki wa
Junior na Ezra. Jelini upo wapi, mama?” Jelini alishituka, akatamani kuingia
chini ya meza ila ikabidi asimame kupunga mkono lakini akaitwa pale mbele
walipo ndugu wote. Ikabidi aende kwa haraka ila akasogea alipo Ezra, maana
alimnyoshea mkono kama anayempokea. Akamvutia karibu yake. Akatulia pembeni ya
Ezra.
“Jamani kazi mliyonipa, nimekamilisha kwa ufupi. Hawa ni
wachache wanao wakilisha familia yangu. Nina watu wengi sana. Nikiendelea hapa,
nitaharibu ratiba nzima. Kwa hiyo kama kuna picha ya ukoo wa Ester, naomba hawa
wawakilishe.” Ezra na Junior wakajua mzee amefanya makusudi kutaka picha
ya familia na Jelini akiwepo ili kutuliza lile tukio zima la
picha kule nje.
“Tafadhali tunamuomba na Ester apate picha na sisi. Ikawe
ukumbusho wake. Awe anakumbuka na wanyumbani.” Mchungaji akaongeza na kuamsha vigelegele.
Vikashamiri wakati bibi harusi akiwa anashuka jukwaani walipokuwa wamekaa
maharusi, ili kuungana na hiyo familia yake. Baba yake akaenda kumpokea
akicheza. Watu wakazidi kushangilia maana Ester naye akaanza kucheza na baba
yake, wakirudi pale walipoacha familia. Ukweli ilipendeza sana. Walijawa
cheko muda wote. Zikapigwa picha za kutosha, Jelini na Ezra wakarudi kule
walipokuwa wamekaa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mc akatangaza ni wakati wa keki. Hilo zoezi likaendelea
likawa linafuatiwa na chakula. Ndugu wa maharusi waliokuwa wamekaa viti vya
mbele, walitakiwa waongozane na maharusi. Inamaana Ezra alitakiwa kuwa mbele
kwenye hivyo viti maalumu, lakini akawa nyuma na Jelini. “Nenda mimi
nitakusubiri.” “Unataka nikuletee nini?” “Chochote utakachopenda wewe, mimi
nitakula.” Ezra akasimama na kuondoka.
Baada ya muda akashangaa Ezra na Junior wanakuja pamoja,
halafu Noah amewabebea vinywaji na chakula chake amebeba Junior. Ikabidi wale
waliokuwa wamekaa nao kwenye ile meza, wawapishe, wahamie meza ingine ya
pembeni. Ilikuwa na nafasi. Wakawashukuru. Jelini akacheka akiwatengenezea
mazingira ya kuweka chakula, Ezra akamuwekea sahani yake yenye chakula na
kinywaji. Halafu wote wakakaa hapohapo mezani, wakaanza kula huku mziki wa
taratibu ukiendelea.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Unakunywa nini Noah?” “Hivi unajua nimeondoka kule mbele
sababu ya maswali kama hayohayo, bro! Tafadhali niacheni leo nifurahie.” “Mbona
swali dogo tu lakini unapaniki? Unakunywa nini?” “Si unaona ni kopo la Coca
hili!” “Lakini ni kinywaji gani kipo ndani? Na ukumbuke ahadi uliyomuahidi mama
na baba.” “Siwezi kulewa hapa. Wewe usijali. Hapa nashitua tu, nikitoka hapa
ndio naenda sasa kunywa.” Junior akamtizama na kuendelea na kula.
“Kule nje utambulisho wako ulikatishwa. Wewe ni nani
tena?” “Wewe hukusikia baba akimtambulisha pale mbele?” Junior akamuuliza, akaanza
kucheka. “Usipoangalia bro, familia yako itakua ya kijeshi aisee! Maana demu
wako ni afande aliyekimbia kwata. Naona na wewe ameanza kukuambukiza.
Hukuwa hivyo! Maana kuna ubaya gani kufanya mazungumzo na mtu ambaye
mimi nataka kumfahamu? Maana demu wako wazi kaonyesha hataki
undugu naye. Sasa mimi ninayeonyesha…” “Umeshalewa Noah, na wakati leo umeahidi
watu wote hutalewa. Siku ya leo umesema unampa Esta.” Ezra akaingilia lakini
Noah akaanza kucheka tena, kama asiyejali.
Akamgeukia Jelini. “Mimi naitwa Noah. Wewe ni nani
mwenzangu?” “Naitwa Jelini.” “Safi sana Jelini. Kwanza bwana wewe umzuri
sana. Halafu umependeza sana.” “Asante Noah. Na wewe umependeza.” “Ila sasa
wewe kupendeza kwako si kwa mavazi! Yaani wewe ni mzuri haswa. Jelini
wewe mkali bwana! Halaf…” “Inatosha Noah.” Akazidi kucheka. “Hutaki nimpe sifa
zake, bro? Nani atamsifia kama sisi wakaribu yake tuna….” Wakamuona anaangalia
mbele kisha anaficha kopo lake hilo la Coca. “Mzee huyo!” Akainamia
sahani yake. Kimya.
“Kwa nini nyinyi mmekaa huku nyuma, wakati nawategemea kule
mbele?” “Mimi nakuja baba.” Noah akawahi kwa makusudi tu. “Namaanisha Ezra na
Junior. Wewe umeshalewa. Na nakuomba utulie.” “Unapata dhambi za
bure baba yangu! Sasa mimi nimelewa saa ngapi, wakati unaniona nakunywa Coca?” Hapo anajitetea na cheko. “Tafadhali naomba
muhamie mbele ili tutoe zawadi ya familia pamoja. Na Noah, tafadhali usiku wa
leo naomba uishe vizuri. Mama yako aondoke hapa na furaha.” “Sawa baba.”
Akakubali akicheka.
“Na ameuliza.” Akawa kama anasita kusema alichotumwa na
mkewe. “Amesisitiza ule.” Akaona amalizie tu hivyo. “Lakini hivyo sivyo
ulivyotumwa baba! Kwani wewe umetumwa nini?” Noah akamuhoji na tabasamu kubwa
akijua hataki kusema, anaona si muhimu.
“Achana naye baba. Wewe mwambie mama tupo naye na atakula.” Junior
akamsaidia baba yao, akaondoka. “Familia hii bwana! Sasa mtu anatumwa, lakini
hataki kufikisha ujumbe wote. Kama sijapata kitu chakula ninachokipenda? Maana pale
nahisi nyama nimepunjwa na mama anataka kujua hilo.” “Tafadhali muache mama,
Noah. Mwache apumzike na afurahie. Wewe unataka kufuatwa nyuma kila siku kama
mtoto mdogo!” Ezra akawa kama anamgombesha. “Na nyama ya nyongeza hii hapa. Usiende
kumsumbua mama.” Junior akamuongeza nyama kutoka kwenye sahani yake. Noah
akashukuru akicheka, akaendelea kula nyama tu bila kitu kingine.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Tafadhali naomba utangulie Junior ili nibaki na Jelini.
Nitakuja wakati wa zawadi. Asikae hapa muda mrefu peke yake.” “Mimi nitabaki
naye.” Akajitolea Noah. “Tunashukuru kwa msaada wako, lakini hapana.”
“Watu hawana imani na mimi!” “Naomba uhamie mbele Noah. Namaanisha uondoke sasahivi.”
Noah akasimama akicheka. Akamimina kinywaji chote kilichokuwa kwenye kopo mdomoni,
kisha akachukua Coca ya kaka yake, akajiwekea kwenye hilohilo kopo na kuondoka
akicheka.
“Nakwenda kuangalia viti kule mbele. Nikipata vya kututosha, nitakutumia ujumbe mje.” “Wazo zuri.” Junior akaondoka. “Naomba kukushauri Ezra. Hii shuguli ni leo tu. Mimi na wewe ni mpaka kifo.” Ezra akacheka na kumbusu shavuni. Jelini akafurahi huyo, akashukuru akicheka. “Nafurahi kusikia hivyo! Hujui tu.” “Nashauri nenda ukawe nao. Mimi nakusubiri hapa. Ikiisha, tutapata muda wetu.” “Nashukuru kwa ushauri wako, lakini siwezi kukuacha hapa Jelini. Akili yangu itashindwa kufanya kazi kabisa. Hujui ni kiasi gani nathamini kila sekunde ninayokuwa karibu na wewe. Nataka kuwa na wewe kila wakati.” Jelini akacheka na kumbusu na yeye shavuni, wasijue watu wanawatizama, wao hawana habari.
Junior akatuma ujumbe kuwa amepata nafasi yao, wahamie
mbele. “Tafadhali naomba nivumilie Jelini. Siwezi kumuacha Junior peke yake. Hatatulia
kule mbele, na ndio tutasababisha kufuatwa huku nyuma na kila mtu. Naomba
tuongozane, tukakae mbele. Nahisi wanakaribia kumaliza.” “Wewe wala usihangaike
kuniomba. Ulipo ndipo nitakuwepo. Niongoze vile utakavyo.” Wakaongozana mpaka
alipokuwa Junior.
Meza moja na Hope pamoja na Noah. Wakamuweka Jelini katikati
yao. Wakatulia hapo. Lakini baada ya muda mfupi sana, Hope akasimama na
kuondoka. Hakurudi kukaa hapo tena mpaka harusi ilipoisha. Jelini
hakujua alihamia wapi, na hakutaka kugeukageuka asije zua jingine. Akajituliza
na kunyamaza.
Iliisha muda mzuri tu. Saa tatu wakawa wamemaliza. Ezra
akamuaga Junior kuwa atakuwa na Jelini, mpaka muda wa kwenda kulala. “Tunaweza
kuzungumza hapo nje kabla hamjaondoka?” “Bila shaka.” “Acha niwaage mchungaji
na mama mchungaji. Nisiondoke kimya kimya.” Jelini akajipenyeza katikati ya
umati uliokuwa umewazunguka, maana na wao walikuwa wakipokea pongezi ya
kuozesha binti yao wa pekee. Akaaga na kutoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ndio Mwanzoni Tu, Na Huku Nako, Anakutana Na Kipingamizi
Kingine.
Kule Ilikuwa Love, Huku Hope.
Mambo Yanaendelea.
Je,
Itakuwa Ni Kuruka Majivu NA Kuishia Kukanyaga Moto?
Kule Colins Alipambana, Wazazi Wakamshinda Nguvu. Je, Huku Ezra
Atafanyaje?
Je, Ni Bora Jelini Kurudi Alikotoka (Colins) Au Aendelee Tu Na
Safari(Ezra)?
Kwani Ni Nini Shida Ya Hope
Kwa Jelini?
INAENDELEA.
0 Comments:
Post a Comment