Akamsimulia mama Jema juu yake na Bale. Hakumficha kabisa.
“Lakini ona heshima aliyoweka huyu mchungaji hapa! Haijachukua hata lisaa.
Lakini ameweka msingi ambao si rahisi si kwa Ezra tu, hata kwa Jelini mwenyewe,
hawezi kuuvunja. Hawa wawili kuanzia sasa, watatembea wakijua jicho la wazazi
lipo kwao. Hata wakikumbana na changamoto zingine, wanazisogelea kwa kuzitatua
si kukimbiana.”
“Najua usingependa kulisikia hili, lakini mama Jema, kwa
hakika namuhurumia sana Colins. Anampenda sana Jelini. Na anamkosa kwa
sababu ya wazazi kuchangia. Acha na mimi nijitoe kwenye mahusiano ya dada
yangu.” James na yeye akaaga.
Akiwa garini anataka kuondoka akashitukia mama Jema anamfuata tena kumpa
maagizo ya kina Colins. Kwamba akifika huko, asije sahau pointi za
msingi za kuzungumza nao. Aliongea kwa msisitizo na kwa kituo kama aandike, ili
wamuelewe na wasije sahau. James aliposema ameelewa na atafikisha ujumbe kama
ulivyo, ndipo akamruhusu kuondoka.
Heshima Haiombwi.
Njiani akaona ampigie simu Bale. “Mnaendeleaje?”
“Aisee sisi niwazima kabisa, tunamshukuru Mungu, ila sipo na Vai.” Alishituka
James, akajua ameshamuharibia dada yake. “Kwema!?”
“Kwema kabisa. Anamitihani ya vitendo kesho, nimetoka kumshusha hosteli
akajisomee na wenzie.” James akahema kwa nguvu kama aliyepata aghueni.
“Mnaendeleaje na familia?” Akauliza Bale. “Sisi ni wazima kabisa, ila nilitaka kukushukuru kwa jinsi
ulivyojitoa kwa Vai. Asante sana Bale.” Bale hakuamini, akapata ububu.
“Acha niwe mkweli kwako. Vai na Viola wamekua ni
kama wakijiangalia wenyewe kwa muda mrefu. Najua nimezembea kwa sehemu fulani.
Ni kweli niliwakatia tamaa. Hichi anachokifanya Vai, sikujua kama anaweza kuja
kukifanya, na najua unachangia Bale. Asante sana.” Alijishusha James,
usingetegemea azungumze hivyo na Bale. Dunia shule ya kila mtu. Lazima ujifunze
tu.
“Nampenda Vai, James. Namuhesabu ni kama
nawajibika kwake moja kwa moja. Ni sehemu yangu. Na Vai ananipenda kwa dhati.
Amenivumilia nikiwa sina kitu kabisa. Sitaki mtu mwingine aje afaidi
alikopanda yeye. Anastahili kula kila matunda yangu. Nampenda Vai. Na
nitakusubiria bila kuchoka, mpaka mnipe baraka zenu, nimuoe.” Akaongea Bale kama
anayemsihi James.
“Kama ni kumuoa, ulitaka iwe lini?” “Akiwa likizo.
Atakuwa na likizo ndefu tu. Naweza kufanya yote, na mpaka anarudi chuo tunakuwa
tumemaliza. Joshua ameniahidi kunisaidia mpaka nikamilishe maswala ya ndoa. Na
nakuhidi sitamuharibia maisha. Nitahakikisha anamaliza chuo. Na kumtunza
vizuri.” “Nakamini Bale. Kitendo cha kuwepo chuo mpaka leo! Najua kwa hakika unachangia.”
Ukweli alimfanya Bale
ajisikie vizuri.
“Acha nizungumze na mzee, nitampa Joshua taratibu
zote. Lakini kwa sasa wewe ndio umtaarifu Joshua. Ninaona unastahili heshima
yangu Bale. Sio sawa kukutumia majibu kwa kupitia Joshua. Wewe ndiye unatunza
dada zangu. Naona bora nikurudishie hiyo heshima.” “Nakushukuru sana James.
Asante.”
Akaaga bila mengi zaidi, huku akielekea nyumbani kwa kina Colins.
~~~~~~~~~~~~~~~
Hapohapo akamtumia ujumbe Joshua.
‘Mungu wa Elia, amejibu kwa moto. James amekubali nimuoe Vai. Anakwenda
kuzungumza na baba yao. Atakupa taratibu zinazofuata.’ ‘Hongera sana.
Nitamsubiria wakati na sisi tukijipanga. Nina uhakika kila kitu kitakuwa sawa
Bale. Lakini wakati tukisubiria, tafadhali fuatilia ile hati ya kile kiwanja
chako. Naomba iwe kipaumbele. Huwezi kuendelea kuishi hapo ukiwa unafamilia.’
‘Sawa. Lakini sina pete ya kumchumbia Vai. Nataka pete nzuri SANA.’ Joshua alivyosoma
hivyo akacheka na kumjibu. ‘Nitakupigia, tujipange kuoa
kwa heshima.’ Bale alifurahia sana kusikia hivyo. Ni Joshua! Kwake
haliharibiki jambo.
Akatulia akianza kujifikiria atakavyoishi na Vai kama mkewe.
“Vai ni mzuri sana.” Akaishia kuwaza hivyo akicheka. Kisha akamtumia
ujumbe Vai mwenyewe. ‘Nakupenda Vai.’ Hapo hapo
Vai akamjibu. ‘Ushani miss?’ ‘Tokea nakushusha hapo.’
Vai akacheka. ‘Na mimi nakupenda Bale. Kesho tutakuwa
wote, usijali. Nenda mazoezini kupoteza muda. Usiwe mpweke muda mrefu.’ ‘Naona nitafanya hivyo. Wazo zuri. Maana naona tokea uondoke
hapa, dakika hazisogei kabisa. Nakwenda gym.’ Vai akacheka
alivyosoma hivyo.
Bale akapata wazo na kumtumia ujumbe James. ‘Tafadhali usimwambie Vai kama umetoa baraka zako, kwetu.
Nafikiria jinsi ya kum surprise na pete ya uchumba.’ James
alisoma akiwa kwenye mataa akielekea kwa kina Colins, na kujibu tu kwa kifupi. ‘Sawa.’
Kwa kina Colins.
Alifika nyumbani kwa kina Colins akakuta kumetulia, ila wote
wapo sebuleni, kasoro Colins. Akasalimia na kukaa. “Vipi Colins?” “Yupo hapo
chumbani.” Akatulia kidogo asielewe ile simanzi ni ya nini wakati Colins
amerudishiwa ufahamu wake, inamaana ni kama nusu ya uponyaji wake! Asijue
kilichokuwa kikiendelea usiku uliopita. Akaomba kwenda kumuona Colins,
akakaribishwa. “Ila nilikuwa na ujumbe wenu, kutoka kwa mama Jema. Nitaomba
nafasi na nyinyi wote ili mnisikilize. “Bila shaka.”
~~~~~~~~~~~~~~~
James akaingia chumbani kwa Colins. Akakuta hajalala,
ametulia tuli kitandani, macho kwenye luninga. Akamtizama alipoingia. “Vipi?”
Colins akajiweka sawa. “Sasa hivi unafanya kazi na nani? Maana kwa muda wote
huo ambao sikuwepo pale, si watakuwa wamejaza nafasi yangu?” Akauliza taratibu
tu kwa sauti ya chini, lakini James aliweza kumsikia na kumuelewa. “Ndiyo.”
Akatulia.
“Vipi lakini?” “Nimegundua nimepoteza miezi kama 10 ambayo
sina ufahamu wa kuiishi kabisa!” “Hukumbuki chochote kabisa!?” “Ilikuwa
kama ndoto. Wewe si unajua ndoto? Hapakuwa na uhalisia halisi. Kumbukumbu nzuri
ziliniishia siku wazazi na Love walipokuja kwangu, wakanilazimisha maombi, na
mimi nikipambana kutoka ili nimuwahi Jelini. Yule mtu aliyekuja nao
aliponifunika kitambaa usoni, nahisi nilipoteza fahamu. Ndio sikumbuki tena.
Yaani jana ndio nimejua imeshapita zaidi ya miezi 10 tokea siku ile.” James akakaa
kama mwenye mengi kichwani. Kimya kikapita kwa muda ila akimuhurumia sana
Colins.
Akawa kama amekumbuka kitu. “Aisee samahani leo nimechelewa
kuja. Siku ya ibada leo. Nakwenda na familia. Kama upo tayari tukaoge.”
“Nashukuru. Nipo sawa kabisa. Labda unisaidie kutoka hapa ndani, angalau nione
nje.” “Una madonda kwenye nyayo mzee, utakanyagaje? Sio tutayatonesha zaidi?”
“James. Ipo wheelchair. Unaweza tumia. Acha niifungue ipo hapohapo
chumbani.” Akaingia mzee kwa haraka. Akaifungua na James akamuweka hapo.
Akamtoa mpaka sebuleni. “Sasa kabla sijamtoa Colins nje,
tafadhali naomba nifikishe ujumbe kutoka kwa mama Jema. Na maadamu wote mpo
hapa, naomba niwakilishe.” Wazazi na Connie pamoja na Colins wakabaki
wakimtizama James. Akaona akae kwa kuwa na wao walikuwa wamekaa.
Tajiri Na Mali Zake, Msikini Na Mkokoteni, lakini
ni wake!
“Labda nianzie mbali kidogo.” Akaanza James. “Jelini
alipokuwa shule ya sekondari, kuna mwalimu alikuwa akimbaka na kuwa akimpiga
sana akimtishia asiseme. Atamuua mama yake na Jema. Nafikiri alishajua
hawana mzazi wakiume, wanalelewa na mama tu. Akatumia huo mwanya kumtumia
Jelini vibaya sana. Jinsi alivyoeleza, alikuwa mpaka akimtuma kwake, kisha
kwenda kumtumia huko vibaya, kikatili kisha kumpiga akimtisha
asiseme.” James akaendelea.
“Kile kitu kikamuathiri sana Jelini, na hakuweza kusema. Ikaendela
hivyo mpaka akashika mimba ambayo pia anasema alipomwambia, alimpiga
mpaka akapoteza fahamu. Na kumtisha asije sema. Akafukuzwa shule. Nyumbani
akijulikana kama mtoto mbaya sana. Swala la shule akawa hataki tena, akijua
historia itajirudia. Hicho kitu kikazidi kumuhuzunisha mama yake wasijue jinsi
ya kumsaidia.”
“Baada ya yote akajaliwa mtoto, akiwa nyumbani, hataki shule
wala kazi, ndipo akakutana na rafiki aliyemtambulisha pombe. Alipogundua
uwezo wa pombe kuwa unaweza kunywa halafu usikumbuke chochote kwa muda,
akaanza ulevi, akishinda baa na sehemu yeyote inayopatikanika pombe au
anayoweza fikia pombe, ili tu alewe. Si kunywa kama ladha, alikuwa
akitafuta ile hali ya kulewa ili asikumbuke yale mambo aliyokuwa akifanyiwa na
yule mwalimu. Shule hataki, na akaingiwa na hofu ya ajira pia. Hataki kuajiriwa
akihofia asije angukia kwa bosi ambaye anaweza mfanyia kama yule mwalimu.”
“Kwa hiyo, akawa mtoto ambaye yupo tu. Sehemu zinazo
patikana pombe ndio ikawa sehemu yake rafiki. Ni mwaka jana tu, ndipo ameweza
kusema na yule mwalimu kukamatwa na kuhukumiwa kifungo cha maisha. Ikawa
kama nafuu ya Jelini, wameanzisha biashara na mama yake. Kwa mara ya kwanza
maishani, Jelini ameweza kutulia na kufanya kitu kinachoeleweka. Na ukweli
anajuhudi sana. Japokuwa hajasoma kwa viwango vya juu, lakini anaakili
ya biashara kama mama yake. Chochote unachomuona anacho sasahivi, ni juhudi
yake yeye mwenyewe Jeilini, akifikiria na kujituma mchana na usiku.” James
akatulia kidogo.
Kisha akaendelea. “Hili hata Colins analijua. Mama Jema
anajua watu wanadharau binti zake sababu wanalelewa na yeye ambaye watu
wanamuona ni duni, hawana baba. Kitendo kama kile mlichomfanyia
yeye. Kumfuata nyumbani kwake. Mbele yetu sisi. Mkimtusi na kumpa
shutuma mbaya sana. Huku mkimdhalilisha kwa sauti ya juu, anajua
kwa asilia 100, hamuwezi kufanya hivyo kwenye familia kama hizi zenu,
jamii yenu ya wasomi, iliyowazunguka.” Hapo James akawapa sekunde kadhaa za
kuingiza hilo kichwani.
Kisha akaendelea kwa msisitizo. “Nikimaanisha hivi,
mlichokifanya kwake na binti yake, ni kweli bila kupinga, kuwa hamuwezi
kwenda kufanya hivyo kwenye nyumba ya kina Love.” Hapo James akaweka tena kituo
akiwatizama kwa zamu.
“Ukimya huo, unaashiria ni kweli. Sidhani kama baada ya
kujua alichokifanya Love kwa Colins, nisiseme sana, pengine mlishaenda kwa kina
Love, mkafanya kama mlichokifanya kwa Jelini.” Kimya. “Kwa ukimya huo,
inamaana, japokuwa kwa Love mnao uthibitisho wa ubaya wote, lakini hamtakwenda
kufanya kama mlichokifanya kwa mama Jema, na binti yake, mbele yetu.”
Akaendelea.
“Sasa amenituma niwaambie, mlichokifanya kwake lilikuwa ni kosa
kubwa sana. Kwanza kisheria, pili hata mbele ya jamii. Mlimfuata
nyumbani kwake, mkamfanyia fujo mbele ya watoto wake, mkimtupia tuhuma
mbaya na za uongo, kwamba yeye na binti zake, ni wachawi.” Colins kimya
akisikiliza lakini machozi yakimtoka kama mvua.
“Mama Jema anasema, amelinyamazia hilo. ILA. Hapo ameweka
msisitizo. Kitendo cha kumfuata Jelini. Popote alipo. Nakumtoa kwenye kile
ambacho mlimtukana mkimsema vibaya hawezi kukifanya. Sasahivi Jelini anaendesha
maisha yake vizuri na kwa utulivu, nafikiri mmemuona. Yupo bora kuliko hata
wasomi wengi tu, mama Jema anasema HILO ni kosa ambalo, hatalinyamazia,
na hatasamehe.”
“Ameomba rasmi. Mtu yeyote wa kutoka hapa kwenu, asipotee
njia hata kwenda kununua kitu dukani kwa Jelini. Asiwahi kusikia mtu
anamsogelea Jelini hata kwa salamu. Ameomba, alipo Jelini, nyinyi msiwepo.
Na ikitokea mnamuona sehemu, mumuwache kabisa. Anasema mlisema wazi
kabisa, ‘hamtaki mtu kama Jelini awe na kijana wenu’, anasema walitii,
wakakaa pembeni. Anaomba ibakie hivyo.”
“Amenituma ramsi, niwaambie, kukiuka haya,
nikutangaza vita na yeye. Na amenituma kuwaambia, katika hiyo vita, yeye
atashinda, na mtakimbia huu mji. Naomba niweke msisitizo. Kwa sasa haya
maneno yanaweza kusikika ni kama vitisho tu. Lakini jamani, nawasihi, mfanye
kama sisi tulivyoheshimu maneno yenu. Tulikaa mbali. Hamtaki kuingia
ugomvini na mama Jema. Hamtamuweza. Atawashitaki vibaya sana. Mpaka mje
mmalizane naye, haitaleta maana tena.”
“Maadamu mmepata mlichokuwa mkikihangaikia japo si
kwa njia sahihi, basi tukae kwa usalama. Jelini hatarudi tena hapa. Inamaana
kile mlichotamani kukiona kwa kijana wenu, hatimaye kinakua. Sasahivi nyinyi
wazazi wa pande zote mbili mmeshinda, kasoro Colins, na najua wazi hata
Jelini anampenda sana Colins, lakini mmesaidia kuwatenganisha kwa
nguvu nyingi sana. Kwa hakika mmefanikiwa.”
“Niombe tuanze sasa, kuishi kuanzia hapa. Tujenge
mahusiano mapya mkijua hawa watu hawapo tena kwenye maisha yenu, Colins yupo
huru. Ni hilo tu. Nyinyi ndio mpo kwenye nafasi ya kutekeleza au kutotekeleza
hayo ya mama Jema. Mimi ni mjumbe tu.” Pakazuka ukimya. Akasimama. “Basi acha
nimtoe Colins hapo nje.” Hakuna aliyejibu. James akazunguka nyuma ya kigari na
kumtoa Colins nje.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Alipotulia akamgeukia James. “Bado una mawasiliano na Chaz?”
“Ndiyo, lakini siku hizi anafanya kazi kule Car wash. Nimempa kazi
kule.” Akawa kama amekwama. “Ulitaka nini?” “Nataka mtu wakunisaidia kwa kama
majuma mawili tu. Nina uhakika baada ya hapo nitaweza kujitegemea.”
“Nitazungumza naye. Nahisi yeye atatufaa kwa sababu kwanza anakufahamu, halafu
hanaga shida. Yeye bora pesa iingie.” “Nitashukuru sana.” Akatulia hapo kwa
muda akitafakari kwa kina maisha yake kuanzia hapo. Kimya kati yao kama
waliopoteza mtiririko mzima wa mazungumzo yao, wakati walikuwa marafiki
waliokaribia udugu! Maisha yamewabadilikia! Kimya chakutosha kikapita. Baadaye akaomba
arudishwe chumbani.
Aluta Kontinua.
Ilikuwa lazima maisha yaendelee kwa picha yeyote ile.
Sasa yanaendeleaje! Ndio hapo. Alipoingia hapo sebuleni akaomba James asubiri.
“Baba!” Mzee akamwangalia, japo kwa shida. “Naomba ukitoka, nisaidie vitu vya
mazoezi ili nianze kujenga misuli tena. Najihisi mwili hauna nguvu kabisa.
Nahitaji kuanza taratibu kurudisha uelewa na kwenye viungo vyangu pia.” “Sawa.”
Kisha akamgeukia mama yake.
“Naomba nisaidie
virutubisho vya aina yeyote ile ila vyenye uhakika kunisaidia kuupa mwili nguvu
kwa haraka na kuujenga kuanzia ndani. Unaweza kuchanganya. Vikawa vya hapa
nyumbani lakini zaidi naomba vile vyakunywa kama GNLD. Nirudishe virutubisho
vilivyopotea.” “Sawa.” Akakubali mama mtu.
“Halafu baba, kabla ya kulala usiku, tafadhali naomba uje
chumbani, tujipange jinsi ya kuweza kulinda ile kazi kule kwenye hospitali
yenu. Ili nikipona, nirudi kazini. Au unafikiri watakuwa wameshapata mtu
mwingine?” Hawakuamini. Lakini mzee akajikaza. “Ningejua.” “Basi naomba
tujipange vizuri. Hata kuwapelekea barua ya ugonjwa. Kuwataarifu nipo kwenye
matibabu. Nikipona nitarudi kazini. Nashauri iwe mapema ili mzee Simba
asije pata sababu.” “Nitafanya hivyo.” “Nitashukuru sana.”
“Na Connie, naomba uende Kigamboni, ukanifutie laptop zangu
zote. Au vitu vyangu vitakuwa hapo kwangu?” “Nyumba yako tuliikodisha Colins. Hivi
nimeshazungumza na huyo mpangaji, kumuomba mwezi huu iwe mwisho, ili urudi
kwako. Kwa hiyo vitu vyako vyote vipo Kigamboni.” “Hamna haja yakufanya hivyo. Acha
ibaki kama mlivyopanga. Nikipata nguvu, mimi nitarudi kuishi Kigamboni.” Ukweli
aliwashangaza na kuwatia hofu kidogo. Maana ni kama safari hii anafanya
kila kitu wanachokitaka bila kushurutishwa! Colins! Ikawa ni jambo jema,
lakini likawaacha na maswali mengi mno. Kimya.
James akamtoa hapo sebuleni baada ya kumuona amemaliza. “James,
kabla hujaondoka, nisaidie chakula kabisa. Nile ndio nipate usingizi wa mchana.”
Akamuomba akiwa anamuweka kitandani. James akamfanyia yote. Akasaidia na
kumpeleka chooni, alipoomba aachwe alale, ndipo akaondoka sasa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Hatimaye Juhudi Za Wazazi Wa Colins Zinazaa Matunda. Ni Kama Colins Amesalimu
Amri, Anatembea Kwenye Ramani Ya Wazazi
Wake.
Lakini, Ni Nini Anapanga Huyo Colins?
Ni Kweli Amekubali Kuwa, Sikio Halizidi Kichwa, Au?!
Usipitwe Na Ya Harusini Alikokaribishwa Jelini.
Mazito Na Makubwa Yapo Mbeleni.
0 Comments:
Post a Comment