Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 20 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 20

Baada ya muda mfupi, James na familia yake wakawasili na kukuta hiyo kelele kutokea
chumbani kwa Jelini. Jema akamkabidhi mumewe mtoto, akasogea kwa kujihami, mpaka mlangoni. Akamkuta mama yake anawaka kwelikweli, Jelini analia kitandani. “Shikamoo mama.” Akasalimia kwa kujihami, Jema asiyependa fujo. “Wewe hukuwepo hapa wakati huyu akitukanwa kuwa hajasoma, mchawi, hawataki mtu kama huyu aolewe na Colins?” Jema akabaki ameduaa, hajui ajibu ndio au hapana.

“Usinitanie Jema wewe!” Jema akajua kibao kitamgeukia muda si mrefu. “Au unataka na yeye yampate kama aliyokufanyia Temu?” Akajua tayari. Ameshaletwa mchumba aliyemtapeli yeye zamani, akajua tayari kibao kimemgeukia. Anatakiwa kurudisha akili hapo kwa haraka sana kabla hapajaharibika kwake zaidi. “Mmelogwa nyinyi wawili?!” “Kama ni siku ile walipokuja wazazi wa Colins, tulikuwepo. Na hata James alikuwepo. James njoo hapa chumbani.” Akatoka mbio kumuita mumewe, maana akajua huo moto utaendelea na kwake, bora alete mume kumkumbusha alishaolewa.

James akasogea na mtoto wake aliacha sebuleni akamwambia Jeremy amwangalie. Akamkuta Jelini akilia, amejikunja kitandani, mama Jema anawaka. “Wakati wakisema Jelini hafai kuwa na kijana wao, nyinyi mlikuwepo hapa?” “Tulikuwepo.” James akajibu kwa haraka akikumbuka uchelewaji wa kujibu kwa Jema.

“Kwa hiyo kilichobadilika leo nini mpaka kumfuata mwanangu, kama si kunitafuta mimi?” Akaendelea mama Jema. Kabla hajajibu, akaendelea. “Walikuja kumtusi huyu, na kunivua nguo mbele yenu hapa! Nilinyamaza kimya, kama mjinga vile, mpaka wakamaliza yao. Wakasema Jelini hafai. Leo anajenga kwake, eti ndio wanakwenda kumvuruga!” Kimya.

“Walisema hajasoma. Nikanyamaza tu. Amejianzishia vitu vyake. Vinaenda vizuri, wanaanza kurudi kinyumenyume kutaka yeye ndio akwame. Aharibikiwe. Kisha mambo ya kijana wao yakienda sawa, waanze kumtusi tena mwanangu, huku wanamuunganisha kijana wao na mtu mwingine!”

    “Sasa nakutuma kwao, James.” Jema akajivuta pembeni kabisa. Alishaingiwa hofu. “Wakati ukizungumza na James, mimi naona nikanyonyeshe.” “Unataka kuniudhi Jema wewe?” “Mimi naona nikae tu hapahapa kitandani, ulipo wewe mama yangu. Mtoto atanyonya hata baadaye.” Haraka akaenda kukaa palepale kitandani.

“Wakumbushe jinsi walivyonikosea. Kuja nyumbani kwangu na kunitusi mbele ya familia yangu. Waambie hilo nililinyamazia. Ila.” Hapo akaweka kituo akimtizama James kwa ukali. “Nikija kusikia wamemfuata Jelini popote pale, hakika wanaanzisha vita na mimi. Na waambie huwa sikubali kushindwa. Wao si wanajiona wasomi sana wamefanikiwa, watu wao ni wa viwango vya juu?” James kimya, mpaka rangi ya sura imembadilika.

    “Sasa waambie wamemuanza mama Jema, sina shida ya kuwamaliza. Wakithubutu kumsogelea Jelini tena, au kurudi hapa nyumbani kwangu tena, hakika wataniona mbaya. Na waambie vita yangu hawaitaiweza. Waliona wanangu dhaifu kwa kuwa hawana baba. Hawana mwanaume wa kuwatetea kama wao walivyokuja kumtetea kijana wao hapa kwangu, sasa waambie wasimamie hapohapo na wakumbushane hapa si pakurudi. Hakika watakimbia huu mji.” Akaendelea.

    “Mwambie Colins, hapa kwangu amenyea kambi, sitaki kumuona tena. Nilimpenda, nikamuheshimu, lakini hakuishiwa sababu. Kutwa akitoa sababu zisizoisha, asifanye lolote kwa Jelini ila kumliza kila wakati, na kumrudisha baa ambako alitoka. Nalo pia nikalivumilia nikiamini maneno yake. Ila kamwambie wazazi wake, bibi na babu yake, walirudi kugongelea msumari wa mwisho. Hapa kwangu apaone chumba cha maiti. Sio pakuja kutembea.”

    “Kama walivyomkataa Jelini, kamwambie na mimi nimemkataa. Jelini hataolewa na mwanaume kama yeye. Akatafute kwingine. Sasa na wewe Jelini unisikilize na unijibu.” Kama James aondoke vile, lakini miguu ikawa mizito.

“Maana wewe nahisi kichwa chako si kizuri. Kuna aliyekudondosha ulipokuwa mchanga. Na kwa sababu sio mimi, basi ni Jema.” Jema akabaki kimya. “Maana humu ndani nilikuwa mimi na Jema tu. Sasa atakayekuwa amekugonga kichwa, ukawa mpuuzi wa kiasi hicho, huwezi kufikiria hata kidogo, unakimbilia kulekule ulikofukuzwa na matusi, ni nani kama sio Jema?” Wote kimya.

    “Wewe unaacha biashara jana, unakimbilia kwa mpuuzi yule!” Mama Jema akaendelea akiwaka kwelikweli. “Akiwa mzima, wanakutusi na kukufukuza. Wanampa ujana wake mwanamke wanayeona anafaa. Akiwa mgonjwa ndio wanakutafuta wewe mjinga, wanayejua unaweza acha shuguli zako, zisizo muhimu kwao, ukamuuguze. Ulimkuta huyo mwanamke wake hapo kwao?” Jelini kimya akilia.

    “Usinitanie Jelini wewe?” “Sijamkuta mama.” “Sasa hujioni kwamba wewe ni mjinga wa kupindukia!? Kwa nini wewe uwepo huyo mwanamke wanayeona anafaa yeye asiwepo hapo?” Kimya. “Au unaona sawa vile walivyokuja kunitukana mimi hapa?” Jelini akapandisha mabega kukataa.

    “Sasa unijibu na usinipotezee muda. Unataka undugu na kina Colins au unabaki hapa na mimi pamoja na Jeremy?” “Kwamba utanifukuza!?” Jelini akauliza akilia, asiamini. “Tena sasa hivi na mizigo yako. Na nisiwahi kukuona tena hapa. Maana wao si ndio unawataka? Ukiwafuata tu, kule yakishindikana, nisikuone ukirudi hapa. Maana na Colins lazima yatashindikana tu. Sasa hapa usirudi.” “Mama umekasirika, pengine…” “Jema!?” “Basi mama yangu, mzazi. Basi mama.” Akajirudi kwa haraka.

    “Wewe unaona hivi anavyoyumba yumba huyu ni sawa? Nakuuliza Jema? Unataka aendelee kuyumba hivi mpaka amyumbushe na Jeremy! Mungu amempa mtoto mtulivu. Aliyeamua kutulia humu ndani. Ameona havinogi, akaenda kuniletea mwanaume mpaka humu ndani alikotulia mtoto! Tena mwanaume asiye na maana! Amemvuruga Jeremy mpaka leo amebaki na maswali juu ya huyo Colins, na hakuna mwenye majibu ya maaana yakumpa.”

    “Mimi nishakuapia sitaleta mwanaume mwingine tena humu ndani, ukaamini. Mbona sasa unani…” “Kwa hiyo unataka niwe na kazi ya kukuapisha kwa kila jambo? Sasa hivi tena nikuapishe kuwa na biashara hutaacha sababu ya wanaume? Unaniona mimi mjinga sana?” Jelini akapandisha mabega kukataa.

    “Mbona ulipokuwa na Ezra, biashara zilikuwa zikienda, tena anakufuata mpaka kazini. Anakusubiria. Mnakula naye pale na kuhakikisha unarudi tena kazini. Huaribikiwi. Anakutengenezea mazingira mazuri ya kazi. Mpaka cooler si umepewa wewe ili ukiwa na shuguli zako njiani, usihangaike kwa vinywaji? Sasa umeona vimetulia, roho yako inakutanga, unakwenda kutafuta hekaheka. Si wazimu huo ni nini?”

    “Wewe badala ufikirie swala la mtoto wako la baadaye, unakimbizana na wanaume wenye maisha yao. Ushajua Jeremy akimaliza hapo anakwenda shule gani? Maana ada ya hapa ilishalipwa. Huko kwengine?” Kimya. “Na nakuonya Jelini huyu mtoto asirudi chini!” “Mimi simrudishi Jeremy chini.” “Mpaka sasa ushakusanya ada yake kiasi gani yakumfanya aendelee kusoma shule inayoendana na shule anayosoma sasahivi?” Kimya.

    “We Jelini?” Akamuita kwa ukali. “Badala umfikirie mwanao na maisha yake ya baadaye, unakimbizana na wanaume wasio na maana. Na biashara unafunga! Unafikiri mimi nahangaika mchana kutwa kwa ajili ya nani?” Kimya.

    “Sasa wakati wewe ukihangaika na wanaume, mimi nishajua akimaliza hapo anakwenda wapi, na ada yake ndio nahangaika mchana na usiku, kuikamilisha. Kama huyu baba alivyomlipia ada mpaka amalize, asikwame, basi na mimi amenitia shauku, nafanya kama yeye. Ndio maana mwenzio nikipata faida, naigawa mara tatu. Kuendeleza biashara, ada yake huyu, na kulipa mishahara. Wewe akili hiyo huna. Upo radhi uache kila kitu, mpaka familia yako, ukimbilie huko wasikokutaka. Sasa leo niambie, nijue moja, utoke hapa, usinichanganye. Unanielewa Jelini?” Jelini akazidi kulia.

    “Eti unamwambia Ezra, unataka ukamuuguze Colins! Unaakili wewe au umechanganyikiwa? Halafu yeye awe na kazi ya kukusubiria tu ukimuuguza mwanaume wako! Kwanza wewe kama nani? Kama sio kukazania kubaki kwenye fungu la kukosa tu! Apone huko, aanze sababu nyingine, na Ezra alishaoa. Hivi unaakili wewe? Kwanza jibu swali langu. Maana ushakua mkubwa, upo huru kufanya ujinga wako, lakini si hapa ndani, tena mbele ya Jeremy. Hutamchanganya Jeremy. Sasa unaenda kwa kina Colins au unabaki hapa na sisi?” “Mimi siendi tena.” Jelini akajibu na kilio.

    “Umesema nini Jelini wewe?” “Nimesema mimi siendi tena huko kwa kina Colins. Natulia na Ezra. Na nimesema sitamleta mwanaume hapa. Mbona sasa huniamini?” “Nipe sababu ya kukuamini, uone kama sitakuamini. Kichwa chako kipo kama kimegongwa msumari, hutulii! Ni jana tu umetoka kusamehewa na huyo Ezra, eti leo unamwambia urudi kwa kina Colins, ukamuuguze! Unawazimu wewe mtoto!?”

    “Mimi natulia mama.” “Hakika tulia Jelini. Tulia kama mwenzio Jema, upate kitu kizuri.” “Mimi mtoto mbaya. Hunipendi tena. Unaniona sifai. Unanifukuza kwako.” Akazidi kulia Jelini, ila Jema alitegemea ndio njia yake yakumtuliza mama yao. “Hunitaki. Unanifukuza nikapotelee huko nje!” “Si kwa kuwa hutulii?” “Mimi najua kunipendi tu mama. Unataka niondoke humu ndani. Nikaharibikiwe moja kwa moja.” “Sitaki uharibikiwe ndio maana nakukumbusha.” “Sasa badala unisaidie nikiwa karibu yako, unanifukuza! Utafikiri mimi sio mtoto wako. Wakati ulikuwa ukiniambia majuzi tu hapa nimebadilika, nimekua mtoto mzuri, nina juhudi kama Jema! Sasa hivi mimi tena sifai.” Akazidi kulia.

    James akazidi kuchanganyikiwa, lakini akashangaa mama Jema amepoa kabisa. Jema alivyoona tu hivyo akamfanyia ishara mume wake aondoke. James akawa hajaelewa halafu anaogopa. “Nenda kamwangalie mtoto James.” Kama akimbie maana alijua panapoelekea ni kufukuzwa na yeye humo ndani. Maana na yeye ni timu Colins.

    “Mimi humu ndani ndio peke yangu mimi sipendwi! Nakua mtu baki tu, wengine wote unawataka.” “Na kweli ulitulia, ukawa unafanya vizuri. Kwa nini sasa ulikubali kudanganywa na kina Colins? Unaacha mambo yako kwa ajili ya watu kama wale? Wanakudharau wenzio kama hujui.” Hapo mama Jema anaongea ametulia kabisa kama sio yeye.

“Mimi kichwa kimeanza kuuma.” Akaendelea kulia. “Nyamaza mama yangu mzazi kichwa kisizidi kuuma tena. Maana kilikuwa kimepoa kabisa, mpaka Colins amerudi nacho. Mshenzi kabisa! Jema kalete maji ya kunywa. Mama mzazi anywe dawa.” Kama akimbie vile na yeye. Break ya kwanza kwa mumewe.

    “Vipi, ndio kumeshapoa?” James akauliza akinong’ona. “Bado. Hapo Jelini atamlilia. Ili abakie akimbembeleza yeye.” “Haiwezekani Jema!” “Kumbe hujawajua hawa! Muulize Jeremy. Ndio kazi yao. Sasa na yeye Jelini anamfanyiaga kusudi. Atalia hapo, mpaka mama apoe kabisa, abakie yeye ndio mbaya. Sasa sio leo. Ujue ndio na ibada tumechelewa.” “Au tusiende?” James akachomekea. “Usinitanie James!” “Ni wazo tu Jema! Leo mbona kama mmeniamulia jamani!” “We Jema? Kinachokushinda kuleta maji kwa haraka ni nini? Au unaona raha hivi mwenzio anavyolia?” “Naleta mama.” Akakimbilia jikoni.

    Baada ya nusu saa ndio nyumba ikapoa, Jelini akapewa dawa ya maumivu ya kichwa, akarudi kulala. Akaachwa hapo yeye ndio amelala, wengine ndio wakaenda kanisani.

Mtaka Cha Uvunguni.

    Ikawa kama Ezra alikuwa akiwasubiria wao. Wakati wakiingia akagundua Jelini hayupo nao. Akili ikapaa. Akajua ameenda kwa mgonjwa, Colins. Akaanza kuhangaika, hawezi hata kupumua. Junior akamuona. “Vipi?” “Jelini hayupo nao.” Akaongea hivyo tu, Junior akaelewa. Akaangaza macho, akagundua kila mtu kwenye familia yao yupo kasoro Jelini. Akachukua simu ya Ezra, akaandika ujumbe. ‘Shalom dada Jema. Samahani kwa usumbufu. Sijamuona Jelini. Yupo mzima?’  Akamuonyesha, Ezra akamuangalia na kuutuma. Baada ya muda mfupi akapata majibu. Asifungue asome, akamvuta Junior. “Amejibu!” Akampokonya tena simu. ‘Shalom! Jelini tumemuacha amelala. Anaumwa kichwa.’ Wakaangaliana.

    Wakatoka nje kabisa ya kanisa. “Lazima nimuone. Lasivyo sitatulia.” “Sawa.” “Lakini aliniambia kwao haparuhusiwi mwanaume, isipokuwa huyo mwanaume ameenda na wazazi.” Junior akafikiria kwa haraka. “Tumuwahi mzee kabla hajasimama kuhubiri.” Ezra akafikiria, wakacheka kwa pamoja. “Atalalamika maana leo siku ya harusi. Lakini tumwambie ni 911.” “Mtumie ujumbe mwambie arudi ofisini, nimuhimu sana.” Junior akaandika kwenye kikaratasi. “Sasa hivi hashiki tena simu mpaka baada ya mahubiri. Ujumbe wa simu tutachemsha.” Wawili hao wakakubaliana.

    Wakamkabidhi shemasi hicho kikaratasi walichoandika, kwamba amfikishie mzee pale mbele alipokuwa amekaa, kwa haraka kabla hajaenda madhabahuni. Mzee aliposoma, ‘911, ofisini kwako.’ Akageuka nyuma kumtafuta mtumaji ambaye alijua lazima ni Junior au Ezra. Ndio lugha yao hiyo. Alipomkosa akaelekea ofisini.

    Akawakuta wakimsubiria. “Kuna nini!? Mbona 911.” “Jelini ni mgonjwa, na kwao hapafikiki bila kijana, kusindikizwa na mzazi wake.” Akaongea hivyo Ezra, na kumuacha mchungaji ameduaa. “Kukusaidia tu, Jelini ni mdogo wake Jema, mke mtarajiwa wa Ezra. Tupo kwenye hatua za awali. Karibuni sana utajulishwa.” Mzee akabaki akimtizama Junior.

Ezra akapokea. “Nampenda. Na bila kumuona leo, siwezi kufikiria.” “Tutarudi Milimani.” Junior akaongeza. Mzee akashangaa sana. “Ndio ipo serious hivyo!?” “Kabisa. Jelini ni mke wangu.” “Mbona…” Akataka kuwauliza tena, lakini akaona hana huo muda kwa wakati huo. “Labda maswali mengine iwe kesho. Lakini hivi mnakumbuka kama leo ni harusi ya dada yenu?” “Esta ameshapata wake. Tumebaki sisi. Au unataka leo ndio iwe harusi ya mwisho?” Junior akaongeza. Walishawazoea hao wawili. Uhitaji wa Junior ujue ndio wa Ezra.

    “Naomba utusindikize, tafadhali. Hatutakaa sana. Nakuahidi hautachelewa.” “Hivi mnajua kama Ester hatakubali kuolewa leo bila mimi?” “Nakuahidi hutachelewa. Na tutakueleza kesho kwa kituo, ila ujue ni muhimu.” “It’s either now, or never.” Akaongeza Ezra. “Na ili usichelewe, ibada ikiisha tu, usianze kusalimia watu. Wewe sema una udhuru.” Mzee akakabwa, akichangiwa na maneno kutoka kwa kila mmoja wao hapo, akashindwa cha kujibu, akaondoka kurudi kanisani. Wakabaki wakiangaliana.

    “Tuma ujumbe kwa Jema, mwambie baada ya ibada tunaomba kwenda kumuona Jelini. Na tutafuata mashariti ya mama.” Na yeye Ezra akaandika ujumbe hivyohivyo kama alivyozungumza mwenzie. “Ongeza hatutakaa sana, kwa hiyo wasisumbuke kwa chochote.” Ezra akaongeza na kutuma. Hapo wapo ofisini kwa mzee wao. Ibada ikiendelea. Wakabaki wakisubiria majibu kama watoto wadogo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Jema aliposoma ujumbe akashangaa na kumuonyesha mama yake. “Soma kuanzia hapa.” Akamnong’oneza mama yake. Mama Jema akasoma kuanzia mazungumzo yao asubuhi hiyo wakimuulizia Jelini mpaka mwisho. “Mashariti gani?” Akamuuliza mama yake baada ya kumuona amemaliza. “Kwa hiyo unataka nikuambie sasahivi katikati ya ibada?” Alivyoulizwa hivyo akarudisha akili kwa haraka.

    “Mimi naona kweli nisubiri tu. Maana leo!” Mama yake akamtizama na kumrudishia simu yake. “Sasa nimjibuje? Maana ndio ujue anakuomba ruhusa.” “Sawa.” Jema akacheka akitingisha kichwa. Akajua Ezra amepokelewa. Akamjibu Ezra bila ya kuchelewa. ‘Mama amewakaribisha nyumbani. Karibuni sana.’

~~~~~~~~~~~~~~~

    Walipopata hayo majibu hapo ofisini walipokuwa wakisubiria, acha wafurahie huko ofisini, kama watoto wadogo.

    Baada ya kumaliza mahubiri, wakamsikia mzee anamalizia kwa kusema, “Japokuwa leo nina ozesha binti yangu, lakini nina dharula ingine itanipasa niwahi kutoka mara tu baada ya ibada. Nikikamilisha hilo, ndipo tutakutana harusini na tutasalimiana tukiwa na vinywaji mkononi. Mungu awabariki.” Ndipo akashuka, Junior na Ezra wakasimama kama mshale kurudi ofisini kwa mzee wao. Wakamkuta na yeye ndio anaingia.

~~~~~~~~~~~~~~~

    “Tafadhalini tuwahi.” “Tunakushukuru mzee wangu.” Junior akaongeza kwa furaha sana kama yeye ndiye Ezra. “Ila hamtanipeleka ukweni mikono mitupu.” “Hilo usijali mzee wangu. Wakati wewe unatumika pale mimbarini, tulishatuma mtu kununua vitu. Hivi hapa anarudi na kila kitu tulichoagiza.” “Hivi nyinyi mkoje!? Ningekataa!” “Ni imani tu. Sisi tuna imani na wewe mzee.” Hakutaka kujibu. Akazunguka kwenye meza yake, akaweka vitu vyake ili atoke nao.

    “Mshitue Jema, mwambie mzee ana haraka, ndio tunatoka kwenda kwao.” “Nyinyi mpaka kutongoza, mnatongoza pamoja!?” Wakacheka, Ezra akaandika ujumbe kwa haraka. Akatuma.

    Jema alipopata huo ujumbe, akamuonyesha mama yake. “Jema!” Akashituka hakutegemea. “Ndio nashangaa kumbe dharula aliyotangaza mchungaji pale ni Jelini!” “Mimi sikutegemea! Nilijua ni…’ Akakwama. “Acha niwahi nyumbani. Sasa na nyinyi msichelewe.” “Tulete nini?” “Nina vinywaji. Pitia sambusa na vitu vidogovidogo. Sasa sio uje kesho.” “Sikawii mama Jema! Mbona leo hivi?” Mama Jema akaondoka kwa haraka akiwa na Jeremy.

Full Swing.

    Akafika kwake akaanza kuandaa vitu akasahau kumuamsha muhusika. Jema na mumewe wakiwa wanaingia getini, wakaona na gari ya mchungaji pamoja na gari ya Ezra. “Kazi ipo!” Ikabidi James ashuke awakaribishe ndani. “Ingizeni tu magari ndani.” Wakaongozana. Wakawakaribisha ndani. Mama Jema akatoka kuwasalimia.

“Imekua gafla, hatujajiandaa vizuri. Karibuni sana.” Heshima ikaongezeka maana na huyo mchungaji alikuwepo. “Usijali mama. Sisi tunashukuru kwa kutufungulia tu mlango. Maana naona na harusini kusingeendeka bila kumuona Jelini!” Akaongea mchungaji akimtizama Ezra na Junior, wakacheka.

    “Hatutakaa, na wala usihangaike kwa chochote hata maji.” “Kweli mchungaji!  Hutaki kutuachia baraka?” “Hapana mama. Huku tu kunifungulia mlango, tena kwa gafla hivi, mmegusa moyo wangu. Tukimuona Jelini, tukafanya maombi mafupi, siku nyingine tutarudi tukae na tule kabisa.” Mchungaji ndiye akawa mzungumzaji, Junior na Ezra kimya.

    Ndipo akaenda kuamshwa Jelini, mpenda usingizi. Hapo alikuwa ndio kama saa sita usiku. Kalala hana habari. Alikuwa kwenye usingizi mzito. “Vipi mama?” Mama yake akamuamsha kwa upendo. “Sasahivi kichwa kimepoa.” “Una wageni.” Jelini akashangaa sana. “Wageni gani?!” “Ezra na…” Alivyosikia tu Ezra akatoka kitandani mbio. “Ungeosha hata uso bwana Jelini! Vipi wewe?” “Ezra amekuja kuniona!” Wakasikia sebuleni na kuanza kucheka.

    “Osha hata uso bwana! Jiweke sawa ndio utoke. Yupo na mchungaji.” “Mama! Yule mchungaji mkuu, baba Junior!” Akashituka nakufanya wacheke zaidi. “Mimi nimeingiwa hofu.” “Sasa ufanye haraka utoke, wanaharaka.” Jelini akakimbilia bafuni na kutoka akiwa na nguo ileile ya jana yake aliyoenda kuombea msamaha. Alilala nayo na kuamka nayo. Kabla ya kwenda kuoga ndio akamtibua mama yake. Likatokea la kutokea, akabembelezwa na kurudi kulala na nguo zake vilevile.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Akatoka na cheko la aibu. “Kwetu hapajawahi tembelewa na mchungaji.” Akaanza Jelini akiwasogelea pale sebuleni. Wote wakasimama wakicheka. Akamsalimia mchungaji kwa kumpa mkono. Mtoto wakichaga akaweka na goti la kinyakyusa. Akitoa heshima. “Pole sana mama.” “Asante. Lakini msingehangaika. Naendelea vizuri. Hapa nilijitegeshea alam, ili niamke na kujiandaa, niungane na Ezra kwenye harusi.” “Sio usumbufu hata kidogo. Pole.” Wakajikuta wakiongea wote kwa pamoja.

    Jelini akacheka akimtizama Ezra na kumsogelea pale alipokuwa amesimama. Akamshika mkono kwa upendo mbele ya wote. “Nimefurahi umekuja kuniona.” Wote wakacheka. “Na mimi nimekuja Jelini!” “Wewe bado sijakuona kabisa Junior.” “Kweli Jelini?” “Nakutania bwana. Junior wewe mtu wangu sana tu. Nimefurahi mmekuja. Wote. Na mchungaji ndio zaidi. Nimefurahi nahisi nishapona kabisa.” Hapo anaongea mkono kamshika Ezra.

    Akamtizama na cheko la deko. “Nimefurahi. Nimefurahi sana.” Akarudia kwa kunong’ona. Lakini akasikaka na kufanya wacheke. Ezra akaubusu ule mkono aliokuwa ameushika, kwa upendo mkubwa sana, kiasi cha kumshangaza mchungaji. Mchungaji alikuwa haamini kama kuna mahusiano mazito hivyo, yalikuwa yakiendelea, yeye mpeleka mlimani, bado haja taarifiwa! Ameachwa bado akiombea mke kwa huyo Ezra!

    “Pole. Ila ungeniambia.” “Sikutaka kukutia wasiwasi.” Jelini cha deko akajibu kwa upendo akimtizama. “Wala haijasaidia.” Akadakia Junior, mzee wao akiwatizama kama aliyejawa na maswali lakini hawezi uliza pale, zaidi siku hiyo ambayo muda si rafiki kabisa. Ukweli ilikuwa ni 911 kwake. Kama emegency ya America. Maana hapo alikuwa kama ametekwa nyara, si sehemu alidhania angekuwepo siku hiyo, zaidi muda huo ambao anasubiriwa na binti yake wa pekee aende akamtoe kanisani kwa atakaye kuwa mumewe.

    “Sasa si uwakaribishe wakae?” Mama Jema akaingilia. Maana wote walibaki wamesimama wakiwaangalia Jelini na Ezra. “Mimi naomba tufanye maombi tukiwa hivihivi tumesimama, na uturuhusu tuondoke mama. Estar hataolewa leo, asiponiona pale na kumsindikiza mpaka mbele madhabahuni akafunge ndoa. Nitarudi rasmi, nikae tuzungumze vizuri kukiwa kumetulia. Tule na kunywa mpaka mtufukuze.” “Bila shaka. Tunaelewa.” Mchungaji akashuka sala fupi ila nzuri. Akatamka baraka pale, akamuombea Jelini na kuwakabidhi wote kwenye ulinzi wa kimungu. Bila kurudi kukaa, akaaga.

    Wakawasindikiza mpaka nje, mchungaji akaomba apokelewe mizigo iliyokuwa nyuma ya gari yake. Wote hawakutegemea. Walikuwa wamejifungasha kama ambao si dharula. James na kina Junior wakasaidia kushusha na kuingiza ndani. “Msingehangaika jamani. Vitu vyote hivi!” “Si usumbufu hata kidogo, mama. Ubarikiwe wewe na watoto wako wote. Siku zenu zikawe za baraka na amani.” Akaongeza mchungaji. Baada ya kumaliza kutoa vitu vyote, akaingia kwenye gari yake na kuondoka kwa haraka akiwaacha Ezra na Junior hapo nje.

~~~~~~~~~~~~~~~

     Walipomaliza tu, Jelini akamdaka tena Ezra. Akamshika tena mkono vizuri. “Asanteni sana. Junior, asante kwa upendo wenu.” “Karibu Jelini. Siku nyingine usiache kutuambia bwana! Ili na sisi tujue. Usimuachie mama mzigo peke yake. Jua na sisi tupo. Tunahusika moja kwa moja.” Akaongeza Junior kwa kujali, Jelini akasikia kupendwa huyo! Akamtizama Ezra  na kucheka. “Nitafanya hivyo. Sasa acha na mimi nijiandae, nitakuja japo kwa kuchelewa. Naweza nikakosa ibada ya ndoa, lakini sitachelewa.” “Usijali. Nitakuwa nikikusubiri.” Ezra akaongea akimtizama. Bado Jelini alikuwa amemshika mkono.

    “Kwani harusi yenyewe inafanyikia wapi?” Jema akauliza akiwa anamsogelea Junior. “Wametaka kufungia harusi baharini.” Wakaona Ezra na Junior wanacheka wakitingisha vichwa baada ya Junior mwenyewe kusema hivyo. “Ester!” Ezra akaongeza na kufanya wacheke. “Lakini si sehemu mbaya.” Jema akaongeza na yeye akicheka.

    “Siyo sehemu mbaya kabisa, ila garama sana. Maana wamekodi huo upande wa bahari na  wamekodi ukumbi hapohapo.” “Lakini wanaonekana wamepaandaa vizuri kwakweli. Upande wa bahari wanapofungia, kulikuwa kunatengenezwa tokea jana. Wamefanya vizuri kwakweli. Ila pesa yake ni ndefu sana.” “Hongereni sana.” Akadakia mama Jema. “Asante mama yangu. Natamani tungejua mapema, wote tungejumuika kwa pamoja.” “Hamna shida. Jelini atatuwakilisha.” Ungemuona anavyozungumza mama Jema, ungejua tu amefurahi. Nao hao wawili wakaaga na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ezra Ameingia, Full Swing. Mzima Mzima, Bila Kubakiza. Yeye Amekuja Na Gia Kubwa, Mpaka Mzazi, Tena Mchungaji, Aliyetamka BARAKA kwa mama Jema na wanae. Ametimiza Yote Anayoyataka Mama Jema.

Ni Nini Kitaendelea?

Kwa Kina Colins? Ndio amekosa kabisa? Maisha Yake Yatakuaje Baada Ya Kurudi Na Kukutana Na Yote Yanayoendelea?

James ametumwa kwao. 

INAENDELEA.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment