Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 19 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 19

Akataka kutoka hivyohivyo, lakini akaingia kuoga kwa haraka akavaa gauni refu mpaka chini. Akajipaka marashi mazuri, akatoka kwa haraka kama akimbie. “Kazi ipo!” Aliishia kusema mama Jema. Aliendesha akielekezwa na Junior mpaka kwake.

“Bado amelala?” Akanong’ona wakiwa hapo nje alipokwenda kumpokea. “Alitoka kuchukua maji, najua hawezi kulala kwa urahisi. Alishapita hapa alipo, kwa uchungu na maumivu makali sana. Ni kama historia inajirudia.” “Sio na mimi. Mimi sio tapeli. Na ndio maana mwanzo nilishindwa kabisa kumkubalia. Sikuwa tayari. Sasahivi nipo tayari naye. Hawezi kulala akiwa na hali hiyo. Naomba nikaribishe tu nikamuone.” Akaongoza njia.

Akamuona anacheka. “Jelini! Sasa unacheka nini?” “Ujue mtu akikuona pale kanisani, anaweza kukuchukulia poa! Kumbe mwenyewe mambo yako safi.” Mpaka Junior akacheka. “Kweli. Kwako kuzuri. Na si kuzuri tu, kwa viwango. Nitakusifia zaidi baadaye. Maana nilijua ni zile nyumba hazina hata geti, nitaanza kuibiwa vioo vya gari yangu kisha radio. Lakini nikasema bora wachukue tu, mimi nipatane na Ezra.” “Jelini!” “Haki tena. Nilijua ni uswahilini, nje kuna kuna…” Akaanza kuangaza macho akicheka. “Mwaya kwako pazuri sana. Maua yako pia mazuri sana. Kumepangiliwa kwa kisasa. Maua yamewekwa kwa mpangilio mzuri. Halafu mwenyewe unaishi gorofani!” Junior akacheka akimwangalia.

Akamfungulia mlango wa kuingia ndani. “Asante kunikaribisha kwako.” “Karibu sana.” “Nikimfuata alipolala ni vibaya?” Akanong’ona. “Hapana. Na huna haja ya kunong’ona. Vyumba vya kulala vipo juu kabisa.” “Junior naye! Si useme juu gorofani!” Junior alicheka mpaka akainama. “Jelini wewe ni mtundu!” “Sijawahi ishi gorofani mwenzio.” “Basi karibu. Chumba chake kipo…” “Wewe naona ungenisindikiza tu, nisijeingia ambapo sipo.” Junior akaongoza njia akicheka huku akimtafakari Jelini. Hakujua kama yupo hivyo ndio akamuelewa Ezra. Akamfikisha juu na kumuonyeshea chumba kwa kidole.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akamuona anasogea kwa taratibu mpaka kwenye hicho chumba. Akamuona ana vuta pumzi mara kadhaa nje ya mlango kwa hofu, mpaka akashagaa. Akabaki akimtizama. Kwamba Jelini ana hofu na Ezra! Akabaki akijiuliza akimtizama. Akamuona akihema mara kadhaa na kufuta mikono kwenye gauni kama iliyoanza kutoa jasho. Kisha akashika kitasa, akaachia na kurudi kwa Junior aliyekuwa bado akimtizama.

“Au labda nikanywe kwanza maji? Mimi nahisi nina kiu sana.” Ujanja wote akaona umemuishia. “Huna kiu, Jelini. Ingia tu.” Akataka kumkabidhi pochi yake. “Nishikie pochi yangu.” Junior hakuamini. “Unanipa pochi!?” “Sasa hivi nishaingiwa hofu, siwezi kufikiria tena. Halafu hii pochi ishakua nzito. Bora ningeacha tu kwenye gari. Sasa wewe jiulize, usiku huu pochi ya nini?” Akaanza kulalamika. “Au labda nirudi nikaiweke tu kwenye gari?” Akajua amepaniki. “Nipe nikushikie.” Akamkabidhi na kurudi kwenye chumba.

Pegu zisizooza.

Jinsi alivyopanda upendo na kujali kwa huyo Jelini, Jelini mwenyewe akajikuta anayavulia maji nguo, ili kufika ng’ambo ya pili alipo Ezra. Safari hii akamuona akifungua mlango taratibu na kuingia akinyata. Ezra alipoona mlango unafunguliwa bila hodi usiku huo, akajua moja kwa moja ni Junior. “Junior?” Akaita akiwa anajiweka sawa kitandani. “Ni mimi Jelini.” Ezra alishituka, hakutegemea. Akawasha taa ndogo, ya meza ndogo, pembeni ya kitanda kwa haraka. “Jelini!?” “Umenizimia simu, sikupati Ezra.” Akaanza kulia. “Njoo hapa.” Akabaki amesimama karibu ya mlango akijiliza. Ezra akatoka kitandani na kwenda kumshika mkono na kumvutia kitandani. Akamkalisha.

“Nataka uamini sijakuzimia simu. Ila nilitaka kukupa nafasi.” “Mimi sitaki nafasi mbali na wewe. Nataka tusimame pamoja. Ndio tumejenga tu msingi wetu! Jaribu la kwanza tu kutujia, tayari nyumba imeanguka! Umenikimbia! Hujanitakia usiku mwema! Hujazungumza na mimi na kuniombea usingizi mzuri! Umenizimia simu! Hivyo mimi sijapenda Ezra.” “Nisamehe Jelini. Ila nilitaka kukupa nafasi. Na sikujua kama..” Akasita.

Jelini akaendelea kulia taratibu. “Usilie nikwambie ukweli.” Akamsaidia kumfuta machozi kama mtoto mdogo. “Acha niwe muwazi Jelini. Unahistoria kubwa sana na Colins. Mimi ndio nimekuja tu kwako. Sikujua kama kwa sasa natakiwa kufanya nini isipokuwa kukupa nafasi.” “Yote niliyokwambia, ujue namaanisha Ezra. Mimi sijakudanganya.” “Hata kwa Colins?!” Akataka uhakika, bado haamini, kama ilivyokuwa kwa Jema tu.

“Sasa hivi wewe ndio jukumu langu la kwanza Ezra. Hata Colins ananijua. Mimi si msaliti.” “Hayo ndio nisiyoyataka Jelini! Sitaki uwe na mimi sababu ya kutunza ahadi. Nataka kuwa na mtu anayenipenda mimi kwa dhati, na kunichagua mimi kama Ezra. Lakini kwako imekua ngumu hata kuniambia unanipenda, Jelini!” Jelini akapoa.

“Uliniambia ni kwa kiasi gani unampenda Colins, lakini hajawahi hata kuropoka kwangu! Nikajiambia pengine unahitaji muda, utakuja kujisikia ninachojisikia kwako, na kukwambia kila wakati, tena nakurudiarudia. Lakini kabla hata hujafikia hapo, ndio taarifa za uliyesema unampenda SANA, na ulikuwa ukimsubiri muda wote na msamaha wake mkononi, amerudi. Kisha kunisahau kabisa! Ulitegemea nifanye nini?” Ezra akamuuliza taratibu tu.

“Nimekosea Ezra. Sio kwamba najitetea. Lakini pengine ungemuona Colins, ungeelewa kuchanganyikiwa kwangu. Yule mtu huwezi kumtambua kama hutaambiwa ni yeye.” Akamueleza mazingira yote jinsi ilivyokuwa mpaka kuombewa na kurudishiwa ufahamu wake.

“Lakini Ezra, sipo na wewe kwa kukuhurumia. Mimi najijua. Maisha yangu bila mtu kama wewe, yatabaki kuwa hovyo tu. Na inawezekana wewe mwenyewe sijakwambia, lakini nakuhitaji, na ndio maana unaniona usiku huu nipo hapa. Ile hisia ya kufikiri tu eti maisha yangu yanarudi tena kuwa kama zamani bila wewe, nahisi sitaweza. Nakupenda Ezra na nakuhitaji kwenye maisha yangu. Na ninaomba tubakie sisi wawili. Nisamehe kwa nilichofanya. Nimekosa. Nakuahidi nitajitahidi niwe kama wewe unavyonijali.” Ezra akavuta pumzi kwa nguvu akifikiria.

“Nakupenda Ezra.” Ezra akacheka na kumtizama. “Nilivyokuwa nikisubiri nikusikie!” “Watu wanalitumia hilo neno sana. Tena hovyohovyo tu, mpaka linakua linapoteza ladha ya maana yake. Mtu anakuona mara moja tu, hakujui, anakwambia hilo neno. Kwangu nilitaka nikikwambia, ulisikie na kuleta maana, sio kulirusha tu. Lakini kuanzia sasa nitakuwa nikikwambia. Na ujue namaanisha.”

“Na Colins? Maana hatuwezi kuepuka swala la kurudi kwake.” “Ndio tuamue mimi na wewe. Na wenyewe nimewaambia. Na namaanisha Ezra. Sitafanya chochote juu ya Colins, bila baraka zako.” “Kweli Jelini?!” Ezra hakuamini.

“Najua unaweza usiamini Ezra. Lakini mimi ninasimama na wewe. Wewe ni wangu mimi. Nisipokulinda nje na kukutetea, hakuna atakayekulinda. Nahusika na furaha yako kwanza. Na kila mtu nimemwambia. Siwezi nikaenda kutengeneza kwa watu, wakati kwangu kuna teketea. Najua ndio tumeanza. Kamsingi ketu kanaweza kasilete maana hata kwetu. Lakini mwenzio nathamini chetu. Changu mimi na wewe. Tumeanza kidogo, lakini tukiwa pamoja, na sisi tutajenga kitu kitakacholeta maana baadaye. Naomba usinikatie tamaa.” Ezra hakuamini.

“Sikujua kama mwenzangu ndio unachukulia kwa uzito huo! Nilijua msingi wetu hata nchi moja haujafika, hauna maana!” “Mungu aliumba dunia yote kwa kutamka tu. Na sisi tumetamka. Tumekubaliana. Naomba uamini itakua. Mimi nimeamini. Na kama baba yake Junior alivyofundisha, alisema nyumba yeyote lazima ipate majaribu. Nina uhakika hili ni jaribu letu la kwanza Ezra. Usiniache nipambane peke yangu, nitashindwa. Mimi najijua. Nisaidie katika hili nifanye vizuri, lakini tubaki sisi ndio tumesimama.” “Daah! Hujui ni kiasi gani nilikuwa nikimlilia Mungu nipate mtu kama wewe Jelini! Kumbe ndio unaimani ya kiutu uzima hivyo!” Jelini akacheka akijifuta machozi.

“Sikujua kama una msimamo wa kiasi hicho!” “Nakupenda Ezra. Na nimeamua kuwa na wewe. Nitatulia na wewe tu, ili na sisi tuwe na kitu chetu kizuri chenye amani na utulivu kama jinsi wewe ulivyo. Nakutaka wewe Ezra.” Ezra akataka kumkumbatia. Jelini mpenda mikono, akajiweka vizuri kwa kupandisha kabisa miguu kitandani, akajipanga vizuri, Ezra akamkumbatia kwa furaha zote ila kwa heshima kidogo asije pitiliza. Mikono juu kabisa ya mwili wake.

“Nimefurahi! Nimefurahi sana Jelini. Hujui tu. Sikutegemea! Maana tulifanya michezo mingi sana juzi kwenye makubaliano yetu. Sikujua kama imeleta maana.” “Linapofika swala la mahusiano ya kimapenzi, huwa sina mchezo. Nisingekwambia ili tu kukufurahisha. Kama ningekua sikutaki, au sijakupenda, wala usingekaa na mimi kwenye gari lako tukala. Mimi sipo hivyo. Kwenye mahusiano ya kimapenzi, sijui kwa nini Ezra! Nimeipa heshima kubwa sana. Ndio maana nafikiri nimeshindwa kuendana na wengi.”

“Siwezi kukuahidi wewe, na mwingine. Siwezi nikakubali mtu yeyote yule anishike hivi halafu na mwingine tena akanishika hivi! Siwezi. Na huwa sifanyi hivyo kwenye mwili wangu. Nimekukubalia wewe, tafadhali amini nitatulia na wewe tu.” “Nashukuru Jelini. Nimefurahi sana. Asante kwa kunifuata usiku huu. Kwangu inamaana kubwa sana. Nilikuwa na wakati mgumu kupita nitakavyokueleza.” “Najua. Pole mpenzi wangu. Tutakua sawa.” Wakatulia huku wamekumbatiana.

“Nimefurahi Jelini! Nimefurahi sana. Natamani ungejua moyo wangu.” “Unaupendo wa dhati Ezra. Siwezi pata mwanaume kama wewe. Umebeba majibu yote ya kilio changu. Nilikuwa nikitamani mwanaume kama wewe. Siwezi kuzembea. Nilikosa.” “Hayo yameisha na nimesamehe. Nafikiri na wivu pia ulikuwa ukinisumbua.” Jelini akambusu kwa muda mrefu shingoni. Lilikuwa busu moja tu, aliloweza kuligandisha sehemu moja ya shingo kwa muda mrefu, bila mengi, lakini Ezra alilipata mpaka rohoni. Kisha akajirudisha kumuegemea kifuani akiwa amemkumbatia vizuri.

Baada ya muda akajitoa. “Sasa hivi nasikia usingizi. Acha nirudi nyumbani, nikuache na wewe upumzike.” “Ni sawa nikipata muda wa kufikiria juu ya swala la Colins?” “Kabisa. Ukiwa tayari nijulishe. Ila natamani tusimtupe sasahivi akiwa mgonjwa sana. Sitaki waje waone sisi ni wakatili, hatujali. Nimeshamuweka sawa juu yetu. Na Colins anajua msimamo wangu. Na anajua siyumbishwi. Naomba, katika swala la ugonjwa nisijiweke pembeni kabisa. Nifanye kwa vile mimi na wewe tunaona ni sawa. Ila ukiona tu kuna mazingira yanakusumbua, tafadhali usinyamazie. Tuzungumze.” “Sawa. Basi tutajipanga vizuri kesho. Si bado wazo la harusini lipo?” “Kabisa. Ulipo ndipo nitakuwepo Ezra. Sisi kwanza, ndio ratiba nyingine.” Ezra akacheka asiamini.

“Najisikia kukupenda zaidi Jelini! Kumbe wewe ni wa kuaminika hivyo!?” “Kwa sababu nakuhitaji Ezra. Mwenzio sitaki kukupoteza.” “Hutanipoteza.” “Bado mimi ni dharula yako ya kwanza?” Ezra akacheka sana. “Naona kama umebakia peke yako vile!” Jelini akacheka taratibu. “Usingizi umekulemea?” “Sana. Halafu imekua gafla. Nafikiri nilipatwa na hofu ya gafla, nikapaniki, nikijua hunitaki tena, nimekuumiza. Usingizi ukapotea kabisa! Lakini sasahivi nakuona unafuraha, akili imetulia ndio na usingizi umekolea.” “Basi acha nikurudishe nyumbani. Junior atatufuata kwa nyuma, ili nirudi naye.” Jelini akacheka akiwa na usingizi.

“Usijali. Nitafika tu. Wewe pumzika.” “Naomba kukurudisha Jelini. Ndio nitakuwa na amani.” “Sawa.” Wakatoka hapo chumbani, wakamkuta Junior yupo chini sebuleni kwenye kompyuta yake.

 ~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alipowasikia wakishuka ngazi akanyanyua uso kuwatizama. “Naona nyuso za furaha.” “Na usingizi.” Akadakia Ezra na kuongeza. “Naomba tumrudishe nyumbani.” “Bila shaka.” Safari ya kumrudisha kwao ikaanza, kimya garini. Ezra anaendesha gari ya Jelini, Junior anafuata nyuma mpaka nje ya geti. Ezra akashuka na kwenda alikokuwa amekaa Jelini. Akamfungulia mlango. Jelini akashuka. Wakajikuta wamekumbatiana tena. Akamnong’oneza sikioni akiwa amemkumbatia. Jelini mpenda mikono, alijituliza hapo kana kwamba mwenzie ndio haondoki tena.

“Ukalale unono, ukijua Ezra yupo na anakupenda sana.” Akajisikia vizuri, akamsikia akicheka taratibu hapo kifuani kwake. Akambusu pale kifuani alipokuwa amemlalia, akajitoa. “Na wewe urudi kulala kwa amani, ukijua Jelini ni wako, na hakuna wakukupokonya. Hata Colins.” Ezra akacheka. Akambusu kwenye kipanda uso. Mlinzi akafungua geti, Jelini akarudi kwenye kiti cha dereva ili kuingiza gari. Ezra akarudi kwenye gari ya Junior, wakaondoka wakati walipojiridhisha geti limefungwa baada ya Jelini kuingia.

Ezra & Junior.

     Akamuona akicheka kama asiyeamini. “Aisee amenibusu shingoni, mwili kama umepigwa shoti ya umeme!” Junior alicheka sana. “Mimi sikujua kama anamsimamo hivi!” “Ila na wewe ulionyesha kumpenda aisee! Asingeweza kukuachia kirahisi hivyo.” “Ila sikutegemea kama ni mpaka kwa Colins!” “Sasa mmekubalianaje?” “Aisee sijui Junior. Nishauri.”

    “Kwa nini?” “Kwa jinsi alivyoniambia, amewaambia hata nyumbani kwa kina Colins, hataweza kuendelea kufanya chochote mpaka sisi tukubaliane. Lakini Colins ameshanitisha sana aisee! Sijui nafanyaje! Sitaki apone halafu aje anipindue. Nimempenda Jelini. Siwezi pata mwanamke mzuri vile, halafu mwenye msimamo kama wake. Anayejali hisia zangu! Sijawahi aisee!” “Halafu kumbe ndio mtundu vile!” “Nilikwambia.” Wakaanza kuzungumza juu ya Jelini, wakicheka.

    “Sasa utafanyaje?” “Sijui Junior! Ila ninachojua kwa hakika, sitaki kumpoteza Jelini kwenye maisha yangu. Na sitaki kumfungulia au kumpa mwanya Colins. Kwa hakika ananitisha. Hawa watu wanahistoria Junior!” “Nakuelewa kabisa. Inamaana haitachukua muda au nguvu kubwa kurudi walipoishia.” “Daah! Na sitaki kumpa wakati mgumu Jelini! Ameomba kwa kipindi hiki kama tunaweza tusimtupe. Amsaidie. Lakini aisee sijui ndio inakuaje! Naona hofu ya kumpoteza inazidi kufunika maamuzi yangu! Nisije nikakosea Junior!”

    “Kabla ya kulala, nashauri na hili tuliombee. Ila nashauri hii furaha ya sasahivi, ikusaidie ulale, usikaribishe hofu, ikakupokonya furaha yote. Tulia kwanza. Wakati mwingine kuna mambo yanajijibu. Tufanye kama kawaida yetu. Tusiharakishe.” “Hata katika hili!?” “Zaidi katika hili.” Junior akaweka msisitizo akiendelea kukanyaga mafuta, kurudi kwake.

Shilingi Imepinduka.

Jelini akarudi na kuingia chumbani kwake kwa kunyata ili asimsumbue mama yake. Akajitupa kitandani na kupotelea usingizini mpaka mida ya saa tatu asubuhi mama yake akaingia hapo chumbani kwake. “Hatuendi kanisani?” “Lazima. Nimepitiwa tu usingizi.” “Vipi mambo yako na Ezra?” Akauliza akikaa kitandani kwa Jelini. Jelini naye akajiweka sawa.

“Naona tumewekana sawa. Nimemuomba msamaha, na kumuelezea hali ilivyokuwa. Na ameelewa. Ezra ananipenda sana mama. Mpole na najua wazi tutakuwa na maisha mazuri. Hana hekaheka. Halafu nitakuwa peke yangu. Nishapata mwenzio mtu wangu wa peke yangu, niliyekuwa nikimtafuta.” Mama Jema akacheka akitingisha kichwa. Alimjua Jelini.

“Kila mtu niliyekuwa nikimwambia alikuwa anaona haiwezekani. Wakawa wanaona mimi natafuta vitu visivyowezekana. Mbona imewezekana? Shem ametulia. Na huyo Ezra pia. Unakumbuka ulivyoniambia nisikate tamaa? Ona sasahivi na mimi nimepata.” Mama Jema akawa anamwangalia vile alivyojawa furaha.

“Na kwa Ezra kweli utatulia.”Akaongeza mama Jema kwa furaha kama anayemsifia. “Ila nimemuomba kama tunaweza msaidia Colins kipindi hiki mgonjwa.” Hapo ndipo alipo haribu.

“Unasema umemuomba Ezra nini?!” “Kwamba kwa kipindi hiki Colins ni mgonjwa, nisaidie.” “Unasaidiaje?” Akaanza mama Jema. Jinsi alivyouliza, Jelini akajua anatakiwa kuongeza umakini. “Kwa ugonjwa.” “Ndio nakuuliza, wewe mwenzangu na mimi, ambaye huna shule ya unesi. Pale kwao amezungukwa na madaktari na mama yake ni nesi. Halafu wana wafanyakazi chungu mzima! Wewe ulitaka kwenda kusaidia nini, na kama nani?” Kimya, maana aliona ameshaanza kubadili gia.

“Walikuja hapa, wakakuita wewe mjinga. Hujasoma. Huna mbele wala nyuma. Mchawi. Wakakutusi hayo yote. Wakasema ‘mtu kama wewe’ hufai kwa kijana wao. Kwamba gafla leo umesahau?!” “Sijasahau mama. Ila…” “Ila nini kama sio ukichaa huo? Wao waje wanitukane hapa. Wakatae na kijana wao. Leo unataka kuharibu biashara nzima. Ambayo umehangaikia tokea akuache hapa huyo Colins. Yaani kama vile jana ulivyotelekeza biashara, ukaacha pale dukani bila mtu! Na hukufanya chochote jana, wakati kawaida yako siku ya jumamosi ndio siku unatengeneza pesa zaidi! Ukaacha kila kitu, ukakimbilia huko kwa kina Colins, tena kwa kuitwa tu. Unawazimu wewe mtoto!?” Mama Jema akazidi kulipuka.

Sauti ikaongezeka, Jeremey akagonga taratibu na kuingia. Alimjua bibi yake huwa anamuweza vizuri sana mama yake, lakini si kwa ukali wa siku hiyo, tena asubuhi waliyokuwa wakijiandaa kwenda kanisani! Yeye alishakuwa tayari. “Kaniletee simu yangu haraka sana. Ipo kitandani.” Jeremy akatoka kwa haraka, akimuacha mama yake akilia, wote wamekaa hapo kitandani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Simu ikaletwa akiwa anawaka kwelikweli kama moto. Akapigiwa simu Jema. “Namalizia kujiandaa tutoke. James ameshatoka na JJ. Tukutane kanisani.” “Hapana. Njooni hapa. Tena sasahivi. Maana wanataka kunichezea mimi?” “Ni nini tena mama Jema!? Huu ni muda wa kani…” “Kwamba unaona kanisani ni muhimu kuliko kuitikia wito wangu?” “Nakuja mama yangu mzazi. Sasahivi nakuja. Yaani hapa natoka mlangoni, safari ni ya kwako hii wala si kanisani.” Simu ikakatwa kama itupwe. Mama Jema anawaka kwelikweli. Anagomba, Jelini analia kitandani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Shilingi Imepinduka Pabaya.

Ilikuwa Familia Ya Kisomi, Ya Kina Colins, Hawamtaki Jelini KWA Kijana Wao. Sasa Safari Hii ni Mama Jema Ndio Hamtaki Msomi, Na Mwenye Hela, Colins Kwa Binti Yake.

Je, Jelini Atafanyaje? Kweli Atabakiwa Na Msimamo Aliotangaza Usiku Uliopita,

 Hata Kwa Colins!?

ITAENDELEA.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment