Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 18 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 18

 Alishukuru Mungu kukuta ndio mama yake amerudi, yupo bafuni kwake anaoga. Akamsalimia akiwa mlangoni na kukimbilia chumbani kwake ili asimuulize maswali. Akaoga kwa haraka na kujitupa kitandani na kuzima taa ya chumbani kwake kwa haraka kwanza ili kumkwepa mama yake, asije akaingia chumbani kwake na kuanzisha mazungumzo juu ya siku hiyo ambayo yangeishia tu kwa Colins. Bado hakujua atamwambia nini! Na pili alitaka utulivu ili afanyie kazi ushauri wa Ezra. Kuingiza taarifa za kurudi kwake Colins. Akatulia akifikiria hapo kitandani.

Ezra hakuwa amemtania. Alimaanisha. Usiku huo hapakuwa na simu ya mazungumzo ya kuliwazwa na kutakiwa usiku mwema kutoka kwake. Mwanzoni akaona ni afadhali ili aweze kufikiria vizuri. Akatulia. Lakini kadiri muda ulivyozidi kwenda, akaanza kuhangaika kitandani. Anageuka kila upande.

Kisha akagundua hapakuwa hata na ujumbe wa kutakiwa usiku mwema! Akaanza kusumbua simu. Shika, angalia, weka pembeni akisubiria ujumbe wa kutakiwa usiku mwema. Jelini mpenda kupendwa, kufuatilizwa na kubembelezwa. Hayo aliyawezea Ezra. Ule usiku mrefu, wa upweke na mawazo akijifikiria mwisho wake bila jibu akihisi ndoto zake za kuja kumiliki wake ndio amezizika, aliokuwa akipata kwa miaka mingi, kwa muda mfupi sana, Ezra alishaziba hilo pengo. Hana afanyalo ni kumfurahisha huyo kiumbe. Usiku kuwa naye kwa hili na lile, akimbembeleza kwa sauti yake tulivu, kisha kumuombea usiku mwema.

Usiku huo na yeye historia ikamrudia. Akashindwa kulala kabisa akabaki akiangalia simu yake bila kuchoka akihisi pengine Ezra atamtumia hata ujumbe mfupi wa kumtakia usiku mwema! Akasubiri, akahisi pengine uliingia huo ujumbe, umejificha kwenye jumbe nyingine. Akakwapua tena simu yake. Akaanza kuperuzi. Hakukuta za usiku huo ila za siku zilizopita. Akabaki akirudia kuanzia mwanzo wa mawasiliano yao mpaka mwisho. Akaona atulie.

Kumbukumbu za muda mtulivu aliokuwa nao juma zima zikamrudia. Kwa asili Ezra alikuwa mtulivu sana. Rahisi mno kumpuuza. Ni wale watu unaoweza kuwafanyia chochote kisha ukaomba msamaha na akasamehe. Mtulivu mpaka sauti yake. Ila alimjali sana Jelini. Jelini akaanza kutokwa na machozi kila akimkumbuka Colins.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Colins aliyekuwa naye muda mrefu, na anampenda. Akamlinganisha na Ezra aliyekuja kwenye maisha yake kwa muda mfupi. Kadiri alivyofikiria, hao viumbe wawili kwake na anachokitaka, mizani ikazidi kulemea kwa Ezra. Akamtetea hivi na vile Colins wake, mwanaume aliyempenda bila kujisingizia, lakini mizani ikazidi kulemea kwa Ezra. Jinsi anavyomjali na kumpa kipaumbele.

    Ni jumamoja tu, lakini aliweza kupanda mbegu iliyomea kwa nguvu sana na kugusa moyo wa Jelini vilivyo. Kwa hakika Ezra alikuja kama majibu ya maombi na ndoto zake, lakini ikawa amefika kwenye moyo uliokuwa umejaa Colins! Akalia akitamani kama ingekuwa tofauti. Yote ya Ezra apewe Colins.

    Akamfikiria Colins. Tokea waanzane mpaka waachane. Akavuta kumbukumbu zote nzuri. “Alinibembeleza sana nilivyomfumania yule mzee. Halafu aka..” Akakwamia hapo. Kila akikumbuka kama walishatoka na kuwa wakila pamoja kama na Ezra, akaishia kukumbuka sababu za kushindwa kuwa naye. “Ila tulishatoka kwenda kula wakati ule…” Akajaribu kumtetea. Lakini akakumbuka ndio kipindi hicho, tena mara moja akilia kusalitiwa na Kasa, kwengine kote ni sababu. Akakumbuka ahadi ya kuwa naye hospitalini kwenda kupimwa UKIMWI, akaishia mikononi kwa Doro, na kwenda kulewa kupitiliza.

Hapajawahi kuwa na kumbukumbu nzuri kati yake na Colins, ila kwa muda mfupi aliokuja Ezra, akafanikiwa kuweka historia ya namna yake. Hofu ya kurudi kuwa mpweke ikamuingia gafla mpaka kumtia hofu. Akakumbuka hali aliyomkuta nayo Ezra siku chache zilizopita. Mpweke moyoni, akihofia kuzeeka peke yake. Lakini Ezra akamjali akiacha warembo wengi pale kanisani!

    Akimkataa yeye, sio kwamba atashindwa kupata mwingine! Akakumbuka mabinti wanavyommezea mate pale kanisani. Ezra si mweupe kama Colins, lakini ukweli analipa. Analipa kimuonekano na kipato pia. Hata kwa mwanamke mjanja wa mjini anayependa maendeleo, mwenye viwango vya juu, bado Ezra analipa. Hofu ikamuingia kadiri alivyokumbuka jinsi walivyoachana naye usiku huo. Alimuacha si kwa kumbembeleza tena. Alimuacha kwa uhuru japo alikuwa ameumia.

    “Mungu wangu nimechezea shilingi chooni.” Hofu ikazidi kumuingia. Akavuta simu yake tena ili aangalie pengine Ezra amemtafuta. Lakini wapi! “Huyu Colins si wangu, na wala hatakaa awe wangu maishani. Hilo wazazi wake na dada yake wamelithibitisha kwa vitendo.” Akazidi kulia kila akimfikiria Colins, na historia yao

~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Akalia hapo mwishoni akaenda kujisalimisha chumbani kwa mama yake. Jeremy alisharudi chumbani kwake. Alishamtengenezea mwanae chumba chake. Akajaza vitu vya thamani kama alivyokuwa akitamani. Kikapangiliwa hicho chumba, ungependa kuwepo humo chumbani kwa Jeremy. Na kwa kuwa mama Jema ndiye mwenye nyumba, basi palikuwa pasafi muda wote. Kwa hiyo hakuwa akilala na bibi yake tena.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Mama Jema akashituka sana. Jelini aliingia ndani ya shuka alilojifunika mama yake akilia sana. “Kuna nini tena!? Mbona unalia?” “Colins amerudi.” Mama Jema alishituka, akawasha taa kama aliyehisi anatembelewa na nyoka mwilini. “Safari hii amerudi na sababu gani?!” Ndilo swali mama Jema aliuliza na kumfanya Jelini azidi kulia. Ila ikabidi amsimulie kila kitu.

“Utafanyaje Jelini mwanangu!? Unarudia yale maisha ya hekaheka ya huko kwa kina Colins? Na kweli umesahau jinsi walivyokuja hapa kutudhalilisha kwa matusi?” Jelini akazidi kulia. “Sijakuona ukiwa na furaha kwa muda mrefu kama siku hizi chache! Hata ulipokuwa na Colins, hukuwa na furaha hivi. Wakati wote ni hekaheka na yule kijana, ukiachwa hapa ukilia kila siku usiku. Hata siku ile ulipokuwa nyumbani kwake, nikadhani ungelala, pia mlishindwana. Usiku mmoja tu, ukiwa umelewa hujitambui, ndipo mliweza kulala nyumba moja. Lakini kesho yake mlishindwana ukarudi hapa kwa usafiri wa kuunganisha!”

    “Hujawahi kupata furaha kama uliyokuwa nayo ulipokuwa na Ezra. Ulipata utulivu, mwenyewe ulikiri yote uliyokuwa ukiyatamani na kuomba Mungu akujalie kwa mwanaume, Ezra anayo isipokuwa rangi tu. Sasa unataka uwe na mwanaume mweupe lakini huna furaha!?” Mama yake akamuuliza taratibu tu kama anayetaka afikirie.

    “Mimi nafikiri sasahivi nampenda Ezra, mama. Sijawahi pendwa kwa namna hii. Halafu Ezra ametulia mama yangu. Atabaki kuwa wangu daima.” “Nimesikia sifa zake zikiimbwa pale kanisani. Yeye na yule mtoto wa mchungaji. Wamefanikiwa lakini wametulia.” “Ndicho kilichonivutia kwake. Lakini baada ya kumsahau usiku huu, na akajua sababu ni Colins, amejitoa kabisa. Hajanitafuta hata kwa usiku mwema, wakati si kawaida yake!”

    “Nisikilize Jelini. Ezra anajua umuhimu au historia ya Colins kwenye maisha yako. Cha kwanza, ameshaumizwa na mwanamke mwingine kwa kusalitiwa. Aliachwa na kuchaguliwa mwanaume mwingine. Akatulia miaka yote mpaka kukufikia wewe. Hudhani yupo kwenye hofu ya historia kujirudia?” “Mimi siwezi kumsaliti.” “Jelini!? Tunamzungumzia Colins! Kweli?” Jelini akazidi kulia akishindwa kujibu.

    “Na cha pili, kwa jinsi ulivyonisimulia, nafikiri anataka kukupa muda ufikirie unachotaka. Kama ukirudi kwake, iwe kweli umemchagua yeye sio tu kama unasimamia maneno yako, ni kwa sababu unampenda yeye. Na hutambadilikia.” Jelini akazidi kulia.

“Mimi nakushauri kama Ezra. Tulia. Pata muda wa kuingiza taarifa za kuwa Colins amerudi. Pima kwa upana na urefu. Linganisha hao wanaume wawili. Ukiwa umetulia, na kujifikiria wewe mwenyewe. Nini unataka maishani bila kuweka hisia za mihemko. Kisha chukua hatua kama Jema mwenzio.” Hapo akamkumbusha msimamo wa Jema maishani, na mama Jema alifanya makusudi.

    “Ni kwambie ukweli mama?” “Juu ya nini?” “Japokuwa nampenda sana Colins, lakini huwezi kabisa kumlinganisha na Ezra.” Na mama Jema alijua. Ila hakutaka kusema moja kwa moja ili amsikie mwenyewe. “Japokuwa nimemfahamu Colins kwa muda mrefu, na kuwa naye kwenye chochote tutakachoita. Maana hata hayajawahi kuwa mahusiano. Niseme ukaribu, lakini hatuna mambo mazuri, au niseme sina wakati mzuri ninao weza usema tunao kama mimi na Ezra. Nafasi niliyompa Ezra ni kama tu niliyompa Colins, ila kwa Colins imekua zaidi. Nilijiachia sana kwake kwa kuwa mimi mwenyewe ndiye niliyempenda sana. Lakini naweza sema kwa Ezra nina msingi mzuri. Historia nzuri. Nimepata wakati mzuri kuliko niliowahi kuwa nao kwa Colins.”

    “Sasa hivi ni mgonjwa. Atapona na kurudisha nguvu. Lakini naona tutarudi palepale tukihangaika. Na ukweli ambao siwezi kuupuuza kwao mimi ni chaguo ambalo linawalazimu tu kuwepo. Inamaana kama Colins asingekuwa akinitafuta alipokuwa mgonjwa, wale wazazi wasingenifungulia mimi mlango. Na kila wakati nakumbuka jinsi Colins alivyokuwa akiniacha hapa usiku kucha nalia, yeye yupo kwa Love. Ezra hawezi fanya hivyo. Ezra ananifikiria mama, mpaka utamuhurumia! Halafu mtulivu sana.

    “Anakopita Ezra sasahivi, usiku huu, na mimi amenipitisha Colins. Tena zaidi ya mara moja! Kusahauliwa sababu ya mtu mwingine. Leo nimemsahau Ezra, sababu ya Colins. Roho inaniuma, na natamani ungemuona leo. Mpaka ungemuhurumia! Amenikumbusha ile hali niliyokuwa nayo, nikimsubiria Colins. Nikitegemea itakuja kufika zamu yangu. Nikisubiri na kusubiri bila mafanikio. Naumia kumfanyia hivyo Ezra, mtu mzuri. Mimi siwezi kulala tena.” “Mimi nashauri pengine tulale, halafu kesho…” Jelini akazidi kulia kwa sauti.

    “Sasa unataka tufanyaje Jelini, mama yangu mzazi, usiku wote huu!?” “Tukamtafute Ezra.” Mama Jema hakuamini. “Jelini!? Nashauri tula....” Kabla hajamaliza, akaongeza sauti ya kilio. “Sasa tunampata wapi huyo Ezra usiku huu?” “Mimi sijui! Ila ninachojua nimechezea bahati. Sitakuja tena pata mtu kama Ezra na naona wewe hujali.” “Sasa si ndio nashauri tulale mpaka kesho, tukamuulizie pale kanisani!” Jelini akazidi kulia.

Kwa Jema&James.

    Ilikuwa saa sita usiku. Mama Jema akafikiria. Akajua asipopatikana Ezra, huyo Jelini kesho ataamka akili ipo kwa Colins, na yeye hamtaki tena Colins kwenye maisha ya mwanae. Shilingi ikapinduka. Ilikuwa wazazi wa Colins hawamtaki Jelini, sasahivi mama Jema ndio hataki hata kumsikia Colins. Akafikiria kwa haraka, wazo likamjia. Jema. Hapo hapo bila ya kujali muda, akampigia simu.

    Jema akashituka sana mpaka akamuamsha mumewe. “Mama anapiga usiku huu! Si kawaida yake.” “Pokea tujue tatizo.” James akamwambia mkewe. “Kwema mama!?” “Wewe unajua anakoishi Ezra?” “Hapana mama! Kwani vipi?” “Naona leo hakuna kulala humu ndani, mpaka tumpate Ezra. Anatafutwa na Jelini.” “Si nimesikia Colins amerudi na Jelini alikuwa huko karibu siku nzima!?” “Sasa hilo ndilo tatizo.” Jema akawa hajaelewa. Ila akamsikia akilia hapo pembeni ya mama yake.

    “Mpe simu Jelini. Na mwambie aache kulia, aniambie tatizo ni nini.” Akampa simu Jelini. “Na amesema uache kulia, umuelezee vizuri.” “Wewe unajua Ezra anakoishi?” “Kabla hujaeleza mengi, naomba kukutahadharisha na kukuomba kitu Jelini. Maana mimi nakujua wewe na Colins. Msimuingize Ezra katikati yenu, mkamuumiza.” “Mimi sij…” “Hapana Jelini. Tafadhali nisikilize.” Hapo Jema akaweka ukali kabisa.

    “Nipo katika kikundi cha wakina mama wazee na wakina mama vijana pale kanisani. Hakuna mtu anamsema vibaya Ezra na Junior, kitu ambacho ni cha ajabu sana. Huwezi kupendwa na watu wote kwenye jamii moja. Lakini hii imekua tofauti. Hakuna mtu anawasema vibaya hawa vijana wawili, ndio maana nikavutiwa nao. Hawana makuu, na wanampenda Mungu sana. Ezra ni mstaarabu kama unavyomuona. Hana neno na mtu, na nasikia tabia yake ni mtu ambaye anaweza msamehe mtu bila kumuwekea kinyongo. Nimuelewa. Hana makuu.”

    “Sasa. Kwa kuwa Colins amerudi. Na nyinyi wawili tunawafahamu. Tafadhali sana. Kabla hamjafika mbali na Ezra, mwache yule kijana. Maana ana historia ngumu sana juu ya mapenzi. Alinisimulia Junior kuwa aliachwa siku chache kabla ya harusi. Mwanamke ameolewa huko nje ya nchi, na hata aliporudi na huyo mume wake wakizungu na watoto wawili nasikia akajifanya ni kama hamkumbuki kabisa Ezra. Lakini bado Ezra amelipokea na kulinyamazia.” Jelini akazidi kulia.

    “Tafadhali sana Jelini. Junior na Ezra ni kama wadogo zangu pale kanisani. Tunaheshimiana nao sana. Ni vijana waliotulia. Hawastahili hekaheka zako na Colins. Usimuingize Ezra kwenye michezo yako na Colins, isiyowahi kuisha.” Jelini alilia sana.

“Unanielewa?” Jelini akaendelea kulia. “Katika hili, ni lazima uniahidi na uniambie umeelewa Jelini. Sikutanii.” Hapo Jema akawa mkali zaidi. “Nilimsahau kidogo tu, kwa mshituko wa kumkuta Colins na hali ile, Jema. Lakini sio kwamba simjali Ezra. Hata Colins na wazazi wake nimewaambia sasahivi nipo na Ezra. Na siwezi fanya kitu kingine tena, bila makubaliano yangu na Ezra.” James akasikia akiwa amejilaza hapo kitandani alipokuwa amelala na mkewe. Akashituka sana.

    “Sio nilikusikia ukiwaambia wasitafute mtu, wewe utakuwepo kumuuguza Colins!?” James akauliza swali kwa mshangao mkubwa sana. Mama Jema akatingisha kichwa kwa masikitiko akisikiliza hapo kitandani na yeye alipokuwa amelala naye akilia. “Nilibadilisha shem. Ulipoondoka tu ndio nikakumbuka nipo kwenye mahusiano na Ezra, na…” “Jelini?!” “Kweli shem. Ni vile nyinyi hamnifahamu. Mimi nikiwa kwenye mahusiano na mtu, nakuwa mwaminifu kwake.” Jelini akaendelea akijaribu kutulia ili aaminike. Zaidi na Jema akijua ameelezwa na mumewe jinsi alivyokuwa amejaa huko kwa kina Colins, halafu sasahivi anasema Ezra! Akajua lazima aeleweke.

    “Siwezi kudanganya, nilipofuatwa kwa mara ya pili na Connie, na kuambiwa Colins ni mgonjwa sana. Halafu nikapata taarifa za kilichokuwa kikiendelea huko alikokuwa akiishi na Love, huruma ya ajabu ikaniingia. Ukweli kwa muda fulani ni kama dunia nzima ilisimama, nikajiona nipo tu mimi na Colins. Nikasahau uhakilisia wa maisha. Na siwezi kudanganya kwamba simpendi Colins jamani. Nitakuwa nikidanganya. Nampenda, na ukweli bila kificho, nilikuwa nikimsubiria muda wote huo na ndio maana nilikuwa nikikataa wanaume wote, nikidhania atarudi tena,…” “na sababu ingine nzuri?” Mama Jema akamkatisha.

    “Najua unanikejeli mama. Lakini ndivyo nilivyodhania, na nilikusudia kumsamehe tuendelee.” “Nahisi wewe si mzima wa akili wewe. Na kama uchawi kweli upo, basi wewe ndio umelogwa wala si bure.” Mama Jema akaongea kwa hasira kidogo kama aliyeanza kuchefukwa tayari. “Mwache aendelee, mama. Mwache tu.” Jema akadakia akitaka kumsikia mdogo wake. Maana alijua wakimuachia mama yao hapo, pataanza kutibuka zaidi.

    “Lakini si nilimkubali Ezra?” Akawa kama anayemuuliza mama yake kwa kujitetea. “Unataka kuniudhi Jelini? Wewe uje utukanwe hapa. Wanitukane mimi mbele yenu, bado umsubirie ili iweje tena? Tunakuja kuwa na mahusiano ya namna gani na hiyo familia inayotudharau na kushindwa hata kutusitiri? Ingekuwa sisi ni zile familia kama zao, kweli wangethubutu kuja kunitusi hapa kwangu, tena hadharani, mbele ya wanangu!? Kweli? Ushajua wameshatukana hivyo watu wa ngapi kama si sisi tu waliotuona duni?” “Jelini muache mama. Wewe eleza tukuelewe.” Jema akadakia, akijua moto unazidi kuongezeka, unakaribia kulipuka.

    “Ndio nilikuwa nikisema, ni juzi tu, tumekubaliana na Ezra, tuanze mahusiano yetu. Nikaamua kuachana kabisa na mambo yakusubiri.” “Sasa si ndio amerudi?” Jema akadakia na yeye kwa ukali. Mama Jema akafyonza kwa hasira na kutoka kabisa hapo kitandani kuelekea jikoni kuchukua maji.

    “Sawa amerudi, lakini amerudi na kunikuta mimi ni wa Ezra. Siwezi kubadilika. Hata wao nimewaambia sitafanya lolote bila kuwa na baraka za Ezra.” “Kwamba kweli Ezra akikwambia hapana kwenda kwa Colins? Hutaenda wewe?” “Hakika siendi, Jema. Siwezi kumuumiza mtu wangu sababu ya mtu mwingine. Ezra ndio jukumu langu la kwanza, Jema. Nahusika na furaha ya Ezra kwanza kabla ya mtu mwingine, ndio maana mimi nilikuwa nikimshangaa Colins, eti anakuwa radhi kumfurahisha Love na wazazi wake na sio mimi!” Hapo akaanza kuwatuliza. Wakabaki kumsikiliza. Mama Jema akarudi.

    “Ezra ni wangu. Na nimemuahidi nitakua naye. Siwezi kuyumba sasahivi. Kwa kuwa hata mimi sitaki aje ayumbe baadaye. Tumeweka msingi wetu. Hata kama hautavutia sasahivi, lakini tumekubaliana tujenge cha kwetu. Pengine ndio jaribu letu la kwanza kwenye kuanza kujenga kwetu? Siwezi kukubali tushindwe mapema hivi! Hapana Jema. Ezra ana kila kitu cha mwanaume ninayetaka awe wangu. Na nipo tayari nibaki naye tu, mengine nijue mbele ya safari. Na sitamsaliti hata iweje, labda anitamkie hanitaki tena. Lakini simuachi kwa sababu ingine yeyote ile.”

    “Hata Colins?” Jema akataka uhakika. “Hata Colins.” “Unauhakika Jelini?” Ni kama Jema aliwakilisha hofu yao wote hapo. Ni Colins jamani! “Kwa hiyo unachotaka kuniambia wewe Jema, hapo ulipo na shem. Akaja mwanaume wako wa zamani uliyekuwa ukimpenda sana, ndio utamuacha shem kwa sababu yake huyo ex wako?” “James ni mume wangu! Unawezaje kufananisha?” Akaweka na kaukali, chakupaniki, James akimtizama.

    “Basi uzito wa kiapo chako kwa shem, au ahadi zako zote ulizompa baba JJ, ndivyo mwenzio na mimi nachukulia viapo vyangu kwa kila mwanamme ninayempa. Mpaka wenyewe wanikatae. Kama walivyofanya wanaume wote isipokuwa Ezra tu. Naweza nisiwe mcha Mungu kama wewe Jema, lakini mwenzio huwa sitoe ahadi zangu za kimapenzi hovyo kwa mwanaume. Hata kama inanigarimu mwenyewe baadaye, kama nilivyoishi na Colins akiniliza wakati wote, lakini nilikuwa nikimsubiri tu. Ndivyo hivyohivyo nafanya kwa Ezra. Nakusudia kuwa mwaminifu kwake mpaka mwenyewe aseme basi. Hanitaki tena.”

“Lakini ndoa au viapo vya ndoa  siku ile ya sherehe, ni vya baadaye nikiwa nimeishi maneno yangu tokea mwanzo. Mimi sio muhuni. Neno langu kwa mwanaume sisemi hovyo. Na nikisema, nalisimamia.” Mpaka hapo wote kimya.

“Nimekutumia namba ya simu ya Junior. Alipo Ezra, masaa 24, lazima Junior ajue. Na ndio hivyohivyo kwa Junior. Ukitaka kumpata Junior, muulize Ezra. Usiku mwema. Na kuwa makini.” “Asante Jema. Na samahani shem kwa usumbufu.” “Daaah! Usiku mwema Jelini. Sina chakuongeza.” James akaongea kwa masikitiko.

“Najua unampenda Colins, shem. Najua amerudi tena. Na najua kwa mara nyingine tena amerudi na sababu nzito yakueleweka ya kwa nini alipotea muda wote huu, akiishi na Love. Lakini shem, inawezekana Colins hakuwa andiko langu. Tumejaribu sana na wewe ni shahidi, kila wakati tumeshindwa, na mimi umri unakwenda. Si binti mdogo, ni mama mwenye mtoto mkubwa tu. Nahitaji kutulia kama hivyo Jema.”

“Kumpenda Colins imekua ni adhabu kwangu! Sioni mwisho wake. Lakini na Ezra, nimetulia mpaka nafsini mwangu, shem. Madhaifu yote wanayonitukania nayo kwa kina Colins, eti Ezra ananitia moyo nayo na kuniambia ndio nguvu yangu ya sasa na baadaye! Eti kwamba ndiyo yananifanya niwe hivi nilivyo leo. Amenipokea kwa upendo wa hali ya juu, akinijua mimi ni nani na maisha yangu yote mabaya ya nyuma. Amefuta siku zangu zote zile za vilio na majonzi. Nilishasahau kulia hivi, sababu ya Ezra. Nina uhakika kama leo sikuwa nimemuumiza, nipo naye, usiku huu ningekuwa nimelala usingizi mzuri tu. Yote niliyokuwa nikiyatamani, Ezra anayo.” Akajifuta machozi na kuendelea.

“Ninachotaka kukuomba, tafadhali naomba na yeye umpokee. Ukijaribu, au kumfungulia mlango, utagundua ni mtu mzuri sana. Ni wale bahati inayomjia mtu mara moja maishani. Inaweza isije nirudia tena. Ni mwanaume ninayeona uzee wangu naye.” “Jelini!” “Kweli shem. Tafadhali mpe nafasi, utagundua ninachokwambia ni kweli. Ni mtu mzuri sana. Ukikaa naye, unajisikia kutulia, hana hekaheka. Amepoa haswa, mstaarabu wa asili. Nakuomba shem, mpe nafasi.” “Mmh!” James akaguna kwa sauti ya kuishiwa kabisa.

Wote kimya wakisikiliza. James akabaki akifikiria kwa muda. Mwishoe akasema. “Mimi ninachotaka ni uishie kwenye mikono salama Jelini. Sehemu utakayokuwa na furaha. Na kama Ezra ndiye unaona atakupa furaha, mtafute mzungumze.” Jelini alifurahi huyo kama Jema tu. “Nakushukuru sana shem. Usiku mwema. Acha na mimi nitengeneze kwangu.” Akakata na kumpigia simu Junior hapohapo akiwa kitandani kwa mama yake.

Kwa Junior.

Simu iliita mara kadhaa, akapokea. “Mimi ni Jelini. Samahani kwa kukusumbua. Namtafuta Ezra.” Kimya. “Junior?” “Ezra amepumzika.” Jinsi alivyomjibu, Jelini akajua wazi hana furaha naye. Lakini hakujali. “Wapi?” Jelini akamuuliza. Kimya. “Nilazima uniambie. Siwezi kulala bila kuzungumza na Ezra. Na usiponiambia, namfuata baba yako. Yaani mchungaji.” “Namjua baba yangu, Jelini.” “Basi namfuata usiku huu huu anisaidie kumtafuta Ezra.” “Wewe unajua anapoishi baba yangu mchungaji?” Jelini akafikiria kwa muda akakwama.

“Au unapafahamu nyumbani kwa Ezra?” Akamuuliza tena kwa kumsuta kidogo, ila kwa utulivu kama pacha wake Ezra. Kimya. I didn’t think so. Usiku mwema Jelini.” Akataka kumkatia simu kama anayemwambia anampotezea muda. “Nampenda Ezra.” Jelini kwa mara ya nyingine tena siku hiyo, akatamka. Ila kwa mtu asiye sahihi. “Hayo anayajua Ezra? Kwamba ulishawahi kumwambia kama unampenda?” Jelini akazidi kulia. Akalia wee, Junior akimsikiliza asiamini kama Jelini anamlilia Ezra!

Mwishoe na yeye akamuuliza. “Kwani unafikiri nimechelewa? Niambie tu ukweli.” Junior akavuta pumzi kwa nguvu, na kuzishusha taratibu, kimya. “Eti Junior?” “Inategemea Jelini. Wewe unataka nini?” “Mimi si mkamilifu, Junior. Nimekosea leo. Lakini simu ilikuwa mbali, na haikuwa na sauti.” “Ndio kushindwa kuwasiliana naye kwa muda wote huo?!” Akajua inamaana Junior anajua kila kitu.

“Ezra anakupenda sana Jelini. Anakujali kupita nafsi yake. Anakufikiria kwa kila dakika. Kweli umeshindwa kuwasiliana naye siku nzima, ukamuacha anahangaika! Hajui ulipo! Hajui kilichokupata! Kumbe wewe umetulia kwa mwanaume au aliyekuwa mpenzi wako!” “Nilikuwa kwenye paniki, Junior. Nilikosea. Nilipatwa na mshituko mbaya sana kukutana naye. Huyu mtu alipotea akiwa na nguvu, na akili yake. Nimefuatwa na mama yake, nikakataa. Alipokuja dada yake na kunisihi, ikabidi tu kwenda kumuona, nikakutana na kiumbe cha ajabu sana. Kijana yupo kama babu kabisa! Colins amedhoofu, amebaki kama fimbo! Amejawa madonda. Hana nywele kabisa.”

“Mimi nimuoga sana wa hospitali. Kile chumba kilijaa vitu kama hospitali. Ile hali ikanivuruga kabisa nisiwaze chochote mpaka alipokuja kuombewa na kutolewa mapepo. Kumbe ni mambo ya ushirikina. Amekuja kuwekwa huru ilishakuwa usiku. Rafiki wa shem ndiye aliyefika pale kumuombea. Hapo ndipo kila mtu akakaa sawa. Lakini hata wao niliwaambia nipo na Ezra. Na siwezi kufanya chochote hata kurudi pale mpaka baraka za Ezra. Mimi si msaliti Junior, ila nimekosa.” Akajikuta machozi yakimtoka tena.

“Nampenda Ezra wangu. Na mimi nahusika na furaha yake yeye kwanza kuliko mtu mwingine. Tafadhali nisaidie kujua alipo, nizungumze naye. Siwezi nikamuacha alale na uchungu.” Jelini aliongea kwa upendo na kuupata moyo wa Junior vilivyo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jelini ni mzuri bwana. Na yeye humuona tu kanisani jinsi alivyo wa viwango. Hata Ezra alipomwambia anajitosa kwake, alimuonya na kumwambia hatamuweza. Ikawa kinyume. Ezra akawa akimwambia juu ya Jelini, wakawa wote wakishangazwa na uhalisia wa Jelini na ule muonekano wake. Sasa usiku huo Ezra alipomwambia juu ya kurudi kwake Colins kwenye maisha ya Jelini, Junior alimuhurumia sana Ezra. Akajua historia inajirudia kwa pacha mwenzie. Sasa kuja kumsikia usiku huo Jelini akimzungumzia hivyo Ezra, akimlilia, akapoa kabisa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Tafadhali usimuumize Ezra. Ni mtu mzuri sana.” “Basi nikwambie, na mimi ni mtu mzuri sana.” Junior akaanza kucheka. “Uwe unamwambia Ezra asije niumiza mimi. Maana mimi nipo sana tu. Junior.” “Unauhakika Jelini?” “Sasa unataka uhakika wakati mimi mwenyewe sijasamehewa hapa? Wewe nielekeze alipo, nisamehewe, ndio utathibitisha uwepo wangu wa mpaka kifo, kwenye maisha ya Ezra.” Akawa kama amekumbuka kitu. “Ujue Ezra hata hajanitumia ujumbe wa ‘usiku mwema’!” “Kwa kuwa anakupa nafasi.” “Mimi sitaki nafasi mbali na yeye. Nataka nafasi kati yetu na ulimwengu.” Junior akacheka akifarijika.

“Naona kweli umeamua.” “Niambie alipo sasa!” “Alishindwa kulala kwake, akaja hapa kwangu. Yaani tumeachana hapa muda si mrefu, ameingia chumbani kwenda kujipumzisha. Na hapo nimemlazimisha sababu ya siku ndefu kesho.” “Nakuja.” Jelini akatoka kitandani kwa mama yake kama akimbie.

“Usiku huu!?” “Ni kipengele kipi ambacho hujaelewa sasa? Kwamba mimi siwezi kulala,..” “Sababu hujatakiwa usiku mwema?” “Hilo au kwamba Ezra amelala na uchungu?” “Naona nimeelewa, ila nashauri iwe kesho.” “Basi nikwambie kabisa, ushauri wako sio mzuri. Huwezi kunishauri nimuache Ezra hivyo. Ukute bado hajalala.” “Na kweli anaweza akawa hajalala, ila anahitaji kupumzika.” “Ila sio mbali na mimi. Usiponielekeza nyumbani kwako nampigia…” “Baba yangu mchungaji?” Junior akamalizia kwa swali, nakumfanya Jelini acheke.

“Safari hii nampigia mama yako. Ninayo namba yake.” “Usiku huu wa saa saba!?” “Kumbe wewe hujanijua! Hapa navaa, nimfuate Ezra wangu.” “Basi ukiwa kwenye gari unipigie nikuelekeze kwangu.” “Usimwambie Ezra mpaka nifike mwenyewe.” Junior akacheka na kukata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Je, Jelini Amekumbuka Shuka Kumekuchwa? Atabaki kwa Ezra au ni paniki tu?

Itaendelea.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment