“Tokea
mchana nakutafuta Jelini! Hujapata hata wazo lakunitumia ujumbe hata kujua
kinachoendelea na wakati tulikubaliana tunakula pamoja!? Kwamba hukunikumbuka
kabisa na kuhisi pengine nipo nakusubiria?!” Jelini akajisikia kuumia. Ni Ezra.
Mwanaume anayemjali kwa kumfikiria masaa 24.
“Samahani Ezra.
Nilipata mgonjwa, ndio nikaondoka kuja kumuona. Umekula?” Dharula
aliyokuwa na wasiwasi Ezra asije mpa kama Colins alivyokuwa akimfanyia yeye, akimsubirisha
bila kikomo, siku hiyo, kwa mara ya kwanza, na yeye akampa Ezra. Kumbe
hutokea!
Wakamsikia
akimuuliza. “Sijala Jelini! Njaa inaniuma, ndio
nilikuwa nikikujaribisha kwa mara ya mwisho, nirudi tu nyumbani, nikalale.”
“Hapana. Usilale na njaa. Nakuja sasahivi na samahani sana.” “Ni nani mgonjwa?”
Jelini akasita. “Jelini?” “Acha niage hapa. Nakuja.
Tutazungumza vizuri wakati tukila. Hata mimi nina njaa. Sijala tokea asubuhi.”
“Jelini, ni nani mgonjwa?” Chumba kizima kimya, Colins akimtizama tu
pale kitandani alipokuwa amejilaza.
Kimya. “Ni nani huyo ambaye unashindwa
kumtaja!?” “Ni Colins, anaumwa.” “Oooh! Sasa naelewa. Usiku mwema Jelini. Kuwa
tu na amani.” “Tafadhali usikasirike Ezra. Nakuja tuzungumze. Sijakusahau ila
nilitingwa.” Akatoka hapo chumbani. Ila wakamsikia akimbembeleza kwa
sauti iliyojaa hofu.
“Naomba
usiende kulala ukiwa na uchungu. Na kumbuka uliniahidi hutaniacha nilale na uchungu.” “Mimi sijui kama unauchungu
Jelini! Upo na Colins, uchungu
unatoka wapi?” “Usiponiona leo. Ukaamua kwenda kwako bila ya kuzungumza na
mimi, nitaumia sana.”
Ezra akapoa.
“Unanisubiri?” Akamuuliza kwa
kumbembeleza. “Kama unataka nikusubirie, nitakusubiri.”
“Nataka kukuona Ezra.” “Basi nakusubiri.” Jelini akakata na kurudi
ndani. Akakuta kama alivyowaacha. Kimya, Colins akimtizama.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akaanza kulia. “Natamani mngeniambia siku 8 kabla.” Akaendelea
kulia kwa uchungu sana. “Muda wote kabla ya hili
juma, nilikuwa nikimsubiria Colins, nikidhania atarudi na kunipa sababu yeyote
ile kama kawaida yake, ili turudiane. Nilikataa kila mtu kwa muda wote huo, nikimsubiria Colins.”
“Ni
siku chache tu, ndipo nimemkubalia Ezra, nikiwa nimekata tamaa nikijua Colins
wangu hatarudi tena! Mmenikatili! Mmenikatili
vibaya sana. Bora mngeniambia kama Colins wangu yupo na ananitafuta.
Nisingejali usaliti wa kwenda kuishi na Love, nilikuwa nipo tayari kusamehe,
tuanze tena kuahidiana ahadi zetu ambazo hazijawahi tokea.”
“Ni
jana tu, nimetoka kumuahidi Ezra nitakuwa naye mpaka kifo. Ezra ni mtu mzuri
sana na ametokea kunipenda kwa dhati. Na ni mcha Mungu. Mwaminifu na
ameningojea kwa muda wote niliokuwa nikimsubiria Colins. Na Colins ananijua.
Nikishamkubali mtu, siwezi kuwa msaliti. Siwezi kumuumiza Ezra. Nitasimamia
maneno yangu kwake, kwa sababu nyinyi mlimtoa Colins kwenye maisha yangu.” Hasira zikapanda.
“Na wakati nikiahidi
hapa nitakuwa hapa na Colins, msitafute mtu mwingine wa kumuuguza, nilimsahau
kabisa Ezra ambaye yeye ananijali sana. Ananifikiria masaa 24 bila kuchoka,
akitafuta vitu vya kunifurahisha. Mimi ni dharula
yake ya kwanza na amenipokea kama
nilivyo. Madhaifu yote mliyokuja kunitukania nyumbani kwetu mbele ya ndugu
zangu, na mtoto wangu, bila kujali hisia zangu, Ezra amenipokea nayo akinipa
moyo ni maisha ya nyuma. Leo siwezi kumgeuka.”
“Kabla sijaendelea na
chochote hapa, nahitaji muda wa kwenda kuzungumza na Ezra juu ya Colins. Kile
ataridhia, nitafanya. Japokuwa nampenda sana Colins, lakini sitamuumiza
Ezra, kama Colins alivyokuwa akiniumiza mimi na nyinyi mkichangia.
Sitatoa ahadi hewa ambazo atakuwa akizisubiria tu, kama Colins
alivyokuwa akinifanyia mimi. Sitamsababishia Ezra maumivu kama nyinyi
wote mliyo nisababishia.”
“Mmenikatili sana. Na nyinyi wote, mpaka
Connie, sio watu wazuri. Mmefanya juhudi za makusudi kunitoa kwenye
maisha ya Colins mpaka mmefanikiwa.
Mungu anawaona.”
“Jelini umekasirika,
naomba…” “Hapana Connie. Kukasirika ni jambo dogo sana. Nina maumivu yakupita maelezo na wewe ukiwa unajua
moyo wangu na wa Colins! Umechangia bila kutufikiria.” “Nilikwambia mambo
yalivyozidi kuwa na msuguano hapa, niliamua kujitenga kabisa. Nikawa siji
kabisa hapa nyumbani.” “Ili kunusuru nafsi yako
na si kutupigania mimi na Colins. Si ndiyo?” Kimya.
“Achilia mbali hilo.
Wewe ulijua lini kama Colins wangu ni mgonjwa?” Kimya. “Kwa nini mumchome
sindano za usingizi, asinitafute?
Au kwa nini hamkunitafuta tokea mwanzo mkabaki mkimfunga kamba na kumpa
madawa ya usingizi ilimradi tu asinifikie mimi!? Kwa nini Connie, kama si chuki mliyonayo juu yangu?” Jelini
akaanza kulia tena kwa uchungu sana.
“Sio chuki mama.
Tafadhali tusamehe. Mimi nilijaribu kuja kwako mara kadhaa, ila nilishindwa na
dhamira.” “Kweli baba yangu wewe uliweza kuja
kwetu. Mbele ya ndugu zangu, na mtoto wangu aliyekuwa akimuheshimu Colins kwa
kiasi kile, ututusi kwa muda wote ule, kweli leo eti Colins ni mgonjwa,
ananitaka mimi. Eti mshindwe kuja kuniambia jambo zito kama hilo, mnamchoma
madawa ya usingizi ilimradi tu asinifikie
mimi, huku mlitoa baraka zenu aende kuishi na Love!” Jelini akaendelea
kwa machozi.
“Kweli
jamani?! Nina uhakika kama angekuwa akimtaka Love, nina uhakika kwa asilimia
zote, msingefikiria mara mbili, mngempeleka. Ila kwa kuwa ni mimi ambaye
mnaniona mbaya, mkaona shida kunisogeza karibu ya kijana wenu. Lakini wazazi
wangu, narudia tena kama nilivyowaambia siku ile mlipokuja kunitusi mimi
na mama yangu. Inawezekana mimi sijasoma, lakini nina mapenzi ya dhati
na Colins.”
Akaendelea.
“Inawezekana
mimi sijakulia kanisani kama Connie na Love, nimekua nikishinda baa, lakini
sijawahi kumsaliti Colins hata mara moja. Sijui uchawi wala mlango wa
mganga wa kienyeji ulivyo. Sijaishi ulaya, lakini mimi nilimpenda Colins kwa
moyo wangu wote bila maigizo ya kizungu. Nilisema na narudia tena, ningempenda
Colins, na kumuheshimu mpaka kifo changu. Lakini kwa kuwa mimi sio Love, sijasoma, mmenitoa kwenye maisha ya Colins.”
“Naondoka
na kuwaacha na amani yenu. Nikikubaliana na Ezra, na kama bado mtanikaribisha
kwenu, nitarudi kumuona Colins. Vinginevyo endeleeni tu na maisha yenu. Mkitaka
kumtafutia mtu baki wa kumuuguza, hiyo ni juu yenu. Sitaingilia tena, maana
nyinyi kwa makusudi, mmenipokonya hiyo nafasi.” Akaokota pochi yake, na kukusanya vitu
vyake vyote, akatoka akijifuta machozi.
Kimeumana.
Colins akavuta pumzi
kwa nguvu, akajivuta mpaka akakaa. Alikuwa kimya akimsikiliza Jelini, ila
hakuwa ameelewa mengi. “Naombeni mkae, tuanze taratibu. Na msiniambie nilale
mpaka nipate nguvu, wakati yupo Ezra kwenye maisha ya Jelini, na si Colins.”
Akaanza taratibu tu.
“Mimi nishalala na
kula, sina ninapokwenda leo wala kesho. Ninao muda wakutosha tu kurudi kulala.
Naanza na wewe Connie. Bila kunificha, leo ni tarehe ngapi, mwezi na mwaka?”
Akamtajia. “Ni kwamba sijasikia na kuelewa, au!? Umesema leo ni tarehe ngapi!?”
Connie akarudia. Colins akanyamaza kama anayejaribu kufikiria. Wakamuona
anatingisha kichwa kukataa. Akamwangalia tena dada yake. “Umesema leo ni tarehe
ngapi?” Akarudia tena ila safari hii na machozi zaidi.
“Haiwezekani! Kwani nimeugua kwa muda gani?!” Akazidi kushangaa.
Kimya. Akamtizama mama yake kama anayetaka yeye ndio ajibu. “Kwa muda mrefu.”
“Mama please!” Akamsihi kama vile anayemuomba asimzungushe. “Tokea
tukutoe kule kwa Love, itakuwa imefika miezi miwili sasa, si ndio baba CJ?”
Akamrushia mumewe mpira akitetemeka mpaka midomo kwa hofu.
Colins akarudia
kuhesabu. Akatoa hiyo miezi miwili. Akabakiwa na miezi kama nane ambayo hana
kumbukumbu nayo nzuri. Akakunja uso na kujivuta kujiegemeza kwenye kitanda
vizuri. “Labda ungepumzika kwa leo, tuta…” “Connie pls.” Akamuonya dada yake.
Kimya.
“Nina miezi 8 hapa,
achilia hiyo miwili ambayo tutakuja kuzungumza vizuri baadaye. Sina kumbukumbu
nzuri ya hii miezi nane. Najiwa kama ndoto halafu uhalisia hivi! Ila
Jelini ndio amenifanya nifikirie zaidi na kuchanganyikiwa! Labda niende kwenye
swali jingine, kwani mimi niliishi
na Love!?” “Ndiyo.” Mzee akajibu na kuendelea.
“Ulikuwa ukiishi naye
Kigamboni na ukawa ukifanya kazi kwenye kampuni zetu.” “Hapo sasa umenisaidia,
maana nilifikiri ni kuweweseka au ndoto!” Akaongea hivyo kisha akatulia kwa
muda akifikiria. Wote kimya wakijua anajaribu kuvuta kumbukumbu. Kisha akaona
aulize zaidi.
“Ilikuaje nikaishi na
Love na si Jelini!? Hapo ndio nachanganyikiwa kabisa! Maana kumbukumbu
zangu zinanirudisha mpaka kwenye makubaliano yetu mimi na Jelini kuanza
upya. Huku nikiweka mipango ya kumuoa, nikitayarisha sehemu ya kuja kuishi
naye!” Akawa kama amekumbuka zaidi.
“Tena nilishazungumza
na James, anisaidie nimuoe, ili nitulie, nikijua ni wangu. Na nilikuwa
nikipanga nimtengenezee pete ya uchumba kabisa, nimuombe tuone! Sasa
hapo ndio nachanganyikiwa! Ikawaje tena nikaishia kuishi na Love
mwanamke anayenichukia kupita kitu chochote hapa duniani!? Ananidharau
kuliko takataka yeyote ile ya mwisho ambayo unaweza kuifikiria. Hakuwa hata
akitaka nimguse kimapenzi, akisema ananionea kinyaa, na akilalamika hata
mapenzi yenyewe sijui!” Akafikiria tena kidogo, wakamuona anatingisha kichwa
kama anayekataliana na uhalisia.
“Haiwezekani kabisa nikawa nilirudi kuishi na Love kama wapenzi
wakati alikuwa akinitukana waziwazi na kunitusi hata maumbile yangu! Alikuwa
akiyatoa kasoro kwa kunitusi vibaya
sana! Au mimi ndio sijaelewa baba ulivyosema nilikuwa nikiishi na Love
Kigamboni!?” Kilisikika kilio cha mama
yao hapo, kama aliyefiwa.
“Hili sio geni kwako
mama! Inaweza nisiwe nimekwambia kwa undani hivi, lakini kwa hakika,
nisingethubutu kuja kurudi kuishi na Love! Alikuwa akinifedhehesha kwa
matusi mabaya sana! Tena bila hata huruma au kunifikiria mimi ni binadamu! Sijajiumba
mwenyewe, na ninaumia! Sasa ndio najiuliza, niliwezaje mimi kwenda kuishi na
Love na kumuacha mwanamke kama Jelini aliyerudisha hali yangu ya uwanaume!”
Akawa kama anawaza kwa sauti, anahisi pengine yeye ndio haelewi anachoambiwa.
“Hapana! Nahisi kuna
kitu hakijakaa sawa. Tafadhali naomba urudie tena baba. Unasema niliishi
Kigamboni na Love!?” “Ndiyo.” “Kwa muda gani?!” “Takribani hiyo miezi nane.”
Colins akakunja uso. Akatingisha kichwa kabisa akikataa. Kisha akawatizama.
“Nyinyi mnajua kilichonipelekea kuwa na Love na si Jelini?”
Kimya. Akaanza kumtizama mmoja baada ya mwingine. Kimya. Akazidi kushangaa.
“Ni nini
kinaendelea!? Na kama nilikuwa nikiishi na Love, yuko wapi sasa? Au kwa nini
nipo hapa na si huko Kigamboni ambako mnasema nilikuwa nikiishia naye!? Na
ninaumwa na nini?” Kimya.
Hapo wakazidi
kumshangaza. “Ni kwamba mnamajibu ya maswali yangu ila hamtaki kunijibu?!” Kimya.
Akamgeukia mama yake.
“Wewe mama, unafahamu chochote juu ya kinachoendelea kwenye maisha yangu au
nikatafute haya majibu kwengine?” Mama Colins akazidi kulia na kuanza
kusema. “Nisamehe Colins mwanangu. Nisamehe baba.
Nisamehe.” Colins akabaki akimtizama, haelewi. “Nisamehe.” “Nisamehe nini mama?! Mbona
unanichanganya na kunifanya niongeze maswali mengi zaidi? Ni msamaha wa nini unao omba?”
Maji Yalishamwagika, Hayatazoleka Tena.
“Ilikuwa hivi.” Mzee
akaona amuokoe mkewe. Colins akamgeukia. “Siku moja ya jumamosi, alikuja Love
na wazazi wake hapa. Wakaeleza mengi juu ya Jelini.” “Mbali na shutuma za kuwa
ni malaya na anashinda baa, ambazo niliwaambia najua?” Colins akauliza na kuendelea.
“Kama ndio hizo mbona wote tulikuwa tukijua na niliwaambia nafahamu hayo yote
kutokana na kuelezwa na Jelini mwenyewe! Tena baadaye nilikuja kugundua alikuwa
akishinda na pombe kichwani ili kufunika kumbukumbu ya alivyokuwa akibakwa
shuleni!” Hapo akawasimulia mpaka kufungwa kwa huyo mwalimu.
“Hayo hukutuambia
Colins!” “Sikufika kwa umbali huo, kwa sababu mlishaniita mkiwa na Love na wazazi
wake. Nikawaambia yaliyokuwa yakiwahusu kwa wakati ule, kuwa hizo shutuma
anazotoa Love kwangu si ngeni, namfahamu
kwa undani mwanamke niliyemchagua,
na nitamuoa yeye. Nilisema, pengine
hamkuwa mkiniamini!” “Yeye Love alirudi na kusema zile sio akili zako, Jelini
pia ni mshirikina.” Colins akashangaa sana asielewe pointi ya baba yake.
“Kwa hiyo!? Maana hata
hilo la ushirikina halikuwa geni!” “Alirudi na kusisitiza hata kule
kumkubali Jelini sio akili zako. Ni uchawi uliofanyiwa
na Jelini. Ndio akasema amepata mtu wa kukuombea, atakuja naye siku inayofuata,
akuombee. Alimleta hapa siku inayofuata asubuhi, ndio tukaja kwako. Yule
mtumishi aka…” Hapo Colins akakumbuka.
Akawa kama amefunguliwa macho yote. Akakumbuka
kitambaa cheupe alichofunikwa nacho puani, baada ya kuvuta hewa, akapoteza
fahamu. Yaani hapo ndipo akili inamrudia na kukumbuka kila kitu.
“Nimekumbuka!
Mlinivamia nikiwa nakwenda kutengeneza na Jelini!” Akaongea kwa kuhamaki na kuongeza. “Inamaana,
kabla sijatengeneza na Jelini, ndio na nyinyi mkanivamia kwa nguvu, tena nikiwa
nimewasihi tufanye yale maombi wakati mwingine!”
Akamgeukia mama yake
akiwa ameanza kupaniki mpaka sauti ikaweza kutoka. “Mama. Tena mama
akanilazimisha!” Akakumbuka. Adrenaline yote ikawa imepanda. Akajawa na
nguvu ya ajabu, akiwa amehamaki haswa.
“Sasa, ikawaje yale
maombi yanifanye nipoteze fahamu na si…” Akawa ni kama tena ameshachanganywa. Akashindwa
tena kuelewa. Kumbukumbu ikagomea hapo. Akaona aulize tu. “Sasa ilikuaje baba!?”
“Hakuwa mtumishi wa Mungu, kumbe yalikuwa mambo ya kishirikina!” Colins akatoa
macho na machozi. “Kwamba nyinyi ndio mlisababisha mimi
kuwekewa yale mapepo yaliyotolewa hapa!?” Hilo swali likawa gumu hakuna
aliyejibu.
“Tafadhali
malizia baba, ili nijue ilikuaje nikaishia kurudi mikanoni kwa Love.” Ndipo mzee
akafunguka. “Acha nikwambie yote bila kukutesa zaidi Colins. Hapo ulipo,
unavuna malipo ya ukaidi na makosa yangu. Si mama yako wala Connie.
Tafadhali usiwachukie wao. Mimi nahusika.”
Akamueleza bila ya kumficha. Kuanzia anapokumbuka mpaka kwenda kumchukua
Kigamboni kumleta hapo.
Colins alilia. Akalia SANA. Akalia kwa uchungu. Akalia sana. Alijikunja hapo kitandani akilia kwa kuumia na kusononeka kwa uchungu mno. Mama yake alishindwa kuangalia, akaondoka na yeye
akilia. Connie naye akaondoka akilia.
Colins alilia bila
kuweza kuongeza neno jingine. Alilia kama anayechinjwa na kisu butu. Mzee yeye
alishindwa hata kusogea, akaishia kukaa kwenye kochi la pembeni yake, hajui
aseme nini tena. Maji alisha mwaga, hawezi tena kuyazoa.
Akabaki hapo kitini kama
asiyejua chakufanya tena. Baadaye alikuja kugutuka pale chumbani pako kimya,
Colins alishanyamaza na kupitiwa na usingizi, hata asijue alipotea hapo kimawazo
kwa muda gani! Akamsogelea pale kitandani kwa kunyata kama asimuamshe. Akamnyoosha
vizuri, akamfunika, na kubaki amesimama, ameduaa.
Kwa Jelini.
Huku kwa Jelini
aliendesha kama apae. Akafika dukani kwake, akaegesha gari yake, akashuka kama
akimbie. Ezra alikuwa ametulia kwenye gari yake, kimya. Akagonga kioo,
akamwangalia. Alionekana alikuwa mbali hata hajui alipo. Akamuona anatoa lock.
Akaelewa amekaribishwa garini.
Akaingia mbele upande
wa abiria. Kulikuwa na ubaridi mzuri tu. Gari haikuwa imezimwa. Akamwangalia
Ezra. Akamuona jinsi alivyopoa usoni. Bila kutarajia akajikuta machozi
yakimtoka. Akajifuta kwa haraka. “Nisamehe Ezra.
Tafadhali nisamehe mpenzi wangu.” Ezra kusikia mpenzi wangu, akajiweka
sawa. Alijua ndio anaachwa. Gafla mpenzi! Akataka kusikia zaidi.
“Nimekosa
Ezra. Simu ilikuwa haina sauti. Na nikapaniki, kwa sababu nilimkuta…” “Kwanza naomba
utulie, tuzungumze. Sijakasirika Jelini, ila nimekuelewa. Pengine mimi
ndio niombe radhi kwa kukupigia simu hovyo. Natamani ningejua tokea mwanzo kuwa
upo na Colins, kwa hakika nisingekusumbua.” “Hujanisumbua Ezra!”
“Hapana. Ule si uungwana. Mimi si mtu wa kufanya hivyo. Ni mtu ninayeamini
ukipiga simu mara moja, kama mtu hajapokea, inamaana kwa wakati huo hayupo
kwenye nafasi ya kuzungumza. Atarudisha simu baadaye.” Akaendelea Ezra,
taratibu tu kama kawaida yake.
“Nakiri niliingiwa
hofu ya ajabu, nikashindwa kufikiria, nikidhani historia inajirudia.
Kuachwa bila kosa. Kumbe ni kweli!” “Sio na
mimi. Nilikuahidi sitakusaliti Ezra, niamini sitakusaliti.” “Colins
amerudi Jelini! Na kuonyesha ana nguvu kwenye moyo wako, ulinisahau
kabisa! Tafadhali usiniahidi tena. Tuache tu.” “Hapana.
Najua ninachokizungumzia, na hata wao nimewaambia.” Jelini akamueleza
kwa kifupi mpaka sehemu inayomuhusu yeye ya hapo mwisho.
Kidogo Ezra akatulia kuona ametajwa huko kwa kina Colins
kwamba na yeye anahusika kwenye maamuzi ya kumuuguza Colins. Ila kitendo cha
kusahauliwa kabisa siku nzima, kikamuashiria, anashika kwenye makali wakati
Colins yupo kwenye mpini. “Naomba zungumza na mimi
Ezra! Na sijakudanganya. Na sitaki kukuumiza.” Akamuona anatingisha
kichwa kukataa.Akatulia kwa muda, kisha akamuona anatingisha kichwa kana kwamba
anapingana na kilichopo mawazoni.
“Lakini Colins,
mwanaume unayempenda, mwenye viapo vyako, uliyekuwa ukimsubiria
muda wote, amerudi Jelini! Na si amerudi tu! Amejaa kwenye ulimwengu
wako! Kwa vitendo, umeonyesha leo, linapofika swala la Colins, akili,
mawazo na moyo wako vinakua ni vyake yeye tu. Huna
nafasi ya mtu mwingine! Hilo siwezi kupuuza.” Jelini akazidi kuumia. Akafikiria
akahisi ndivyo ilivyokuwa hata na kwa Colins linapofika swala la Love pamoja na
familia yake. Hata yeye husahauliwa kabisa.
“Nakuahidi sitafanya kama yeye alivyonifanyia
mimi. Sitakuumiza Ezra. Leo nimekosa. Nitatoa simu kwenye silence,
naweka sauti. Kabla sijafanya jambo, nitakujulisha japo kwa ujumbe.
Sitakusaliti hata na Colins. Sasahivi ni mimi na wewe tu. Na Colins anajua mimi
si msaliti.”
Akafikiria, moyo wake ukagoma kabisa mpaka kichwa kupinga.
“Tafadhali tule. Pata muda wa kutulia. Fikiria kwa upya. Mimi naelewa. Usiongee
jambo jingine tena. Tule tu, ukapumzike. Pata muda wa kufikiria na
kuingiza habari ya kuwa, Colins amerudi. Na nakuahidi sitakubugudhi
tena kama nilivyofanya leo. Naomba usiku wa leo, tule tu, basi. Usiniahidi
kitu kingine TENA. Tuache tu.” Jelini akapoa kabisa maana Ezra alizungumza kwa
kumaanisha kabisa si kubembeleza tena, kama anaye msaidia kuhitimisha.
Akatoa chakula. Bado kilikuwa na joto zuri kama aliyekuwa
amehifadhi sehemu maalumu ili kisipoe. Aje akikute bado ni cha moto. Jelini
akazidi kuumia jinsi Ezra alivyofika kiwango cha mwisho cha kumjali, wakati
yeye alimsahau kabisa.
Ukweli kwa masaa yakutosha kabisa, alimsahau huyo kiumbe.
Akili yake haikupitisha hata jina lake kwa bahati mbaya! Akamsikia akiombea
chakula. Akarudi pale garini kimawazo. Usiku huo wakala kimya kimya. Mpaka
wakamaliza, Ezra akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kimechanganyikana!
Jelini
Atasimamia Wapi?
Kwa Upande Wake Ezra Amekubali Yaishe. Ashajua Mwenye Kisu Kikali, Ni
Colins Ndiye Anayekula Nyama. Bora Ajiweke Pembeni. Ameondoka Na Kumuacha Jelini Awe Huru.
Colins Analia Kupokonywa Tonge Mdomoni, Na Wazazi.
Maji Yameshamwagika, Hana
Uwezo Wa Kuyazoa.
Ni
Kilio & Maumivu Pande Zote.
Ni Nini Kitaendelea?
USIPITWE.
0 Comments:
Post a Comment