Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 16 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 16

 Connie akatulia kidogo kama kumpa Jelini nafasi ya kujaribu kuingiza zile taarifa akilini kisha moyoni. Lakini hakupoteza muda asije akafikiria jingine na kugairi, hapohapo akiwa kwenye hali ya machozi, akijua aliyomwambia yamemuingia, akamuuliza “Kwa hiyo unakwenda saa ngapi?” Mpaka Jelini akacheka. “Na wewe upo kama Colins! Bwana akitaka jambo lake yule! Huna jinsi ukambadilisha!” “Sasa ndicho kinachomtesa sasahivi. Ameng’ang’ania akikutafuta bila kuchoka. Hakika anahali mbaya, na amini tunahitaji msaada wako.”

“Nitakwenda. Si ni kwenu?” “Ndiyo. Na najua una kazi. Unaweza kuniacha mimi hapa ukanipa majukumu yako nikufanyie wakati ukienda.” “Daktari mzima unataka kuuza duka la urembo!” “Naona unazidi kupendeza tu Jelini, inamaana si biashara mbaya!” Jelini akacheka akifikiria.

“Acha niende tu sasahivi kabla ya jioni watu hawajawa wengi.” Connie alifurahi, na kumshukuru sana Jelini. “Hivi hapa natangulia kukusubiria nyumbani. Au unataka nikusubiri twende wote kabisa?” “Hapana. Nitakuja tu, usiwe na wasiwasi. Siwezi danganya.” Connie akaondoka akiwa na imani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akataka kumpigia simu tena Jema, akasita. Tayari Jema alishapoteza imani kabisa na si Colins tu mwenyewe aliyekuwa mstari wa mbele kumtetea, ila hata wazazi wake. Baada ya kusikia taarifa ya kuwa anaishi na Love na anakwenda kazini kama kawaida, maisha yake yanaendelea, alishamtoa kwenye mahesabu kabisa. Halafu kitendo cha wazazi wake kuja kumtukana mama yake na Jelini, nyumbani kwao! Bila hatia! Mbele yao tena bila heshima, kilimuuma sana.

Na kwa mama yake moyo ukasita kabisa. Alishasema ameshachoshwa na mambo ya kina Colins, na hataki hata kuwasikia tena. Alisema walimdharau vibaya sana na ndio maana walipata ujasiri wa kwenda kumtusi nyumbani kwake. Na huyo akasita kumshirikisha. Akaona ampigie tu yeye kwa linalomuhusu. “Nina mgonjwa, naenda kumuona. Nikichelewa naomba unisaidie hapa dukani. Wasijione wameachwa peke yao.” Mama Jema akaitika kwa haraka bila hata kufikiria. Jelini akaelewa yupo katikati ya mambo yake, hataki kupoteza muda kwenye simu. Ila akashukuru Mungu amekubali bila maswali, na anamjua mama yake, maadamu amekubali, basi atafanya tu.

Akiwa njiani akabaki akimfikiria wakumtaarifu, akaishia kwa James shemeji yake, rafiki wa kweli wa Colins. Akamueleza ilivyokuwa. “Nikwambie ukweli Jelini, mimi nilijua kwa hakika kuna kitu hakipo sawa. Hata iweje, Colins sio mtu wa kukata mawasiliano gafla! Nijulishe kama kuna kitu kitahitajika nisaidie.” “Nashukuru shem, lakini eti nilikuwa nikiogopa!” “Wasingekuja wote kutaka msaada wako wakiwa na nia ya kukuangamiza tena ukiwa uliwaacha kama walivyoomba! Wewe nenda. Baada ya muda nitakupigia kujua unaendeleaje.” “Hilo litanitoa hofu. Nashukuru. Ila kwa sasa, usimwambie kwanza Jema. Acha nikajue kinachoendelea ndipo nitajua chakuwaambia.” “Sawa.” Wakaagana angalau akapata amani kupata baraka za shem wake.

Alishawauliza hivi, hata hao wazazi wakija kusema neno, ‘samahani,’ watarudi kuwa na mahusiano ya namna gani! Akawatoa kabisa kwenye mahesabu, tena wakizungumza kwa kupokezana na mama yao mbele ya Jelini na James. Jelini alipolikumbuka hilo, akaona amuache kumuhusisha na mambo ya kina Colins.

Na kwa mama yake moyo ukasita kabisa. Alishasema ameshachoshwa na mambo ya kina Colins, na hataki hata kuwasikia tena. Alisema Walimdharau vibaya sana na ndio maana walipata ujasiri wa kwenda kumtusi nyumbani kwake. Na huyo akasita kumshirikisha. Akaona ampigie tu yeye kwa linalomuhusu. “Nina mgonjwa, naenda kumuona. Nikichelewa naomba unisaidie hapa dukani. Wasijione wameachwa peke yao.” Mama Jema akaitika kwa haraka bila hata kufikiria. Jelini akaelewa yupo katikati ya mambo yake, hataki kupoteza muda kwenye simu. Ila akashukuru Mungu amekubali bila maswali, na anamjua mama yake, maadamu amekubali, basi atafanya tu.

Rafiki Wa Kweli.

Ukweli familia ya kina Colins walishamtia hofu Jelini. Na alijua wazi hawampendi. Akaingiwa hofu kwenda huko kimya kimya bila mtu kujua alipo, akihofia chochote kinaweza tokea. Maana hata mama yao alimkaribisha kwake akisema Colins ni mgonjwa. Na Connie naye alisisitiza alifuatwa pale hata na baba yao sababu ya ugonjwa wa Colins. Akajua imewalazimu kumfuata lakini si kutaka kwao.

Akiwa njiani akabaki akimfikiria wakumtaarifu, akaishia kwa James shemeji yake, rafiki wa kweli wa Colins. Akamueleza ilivyokuwa. “Nikwambie ukweli Jelini, mimi nilijua kwa hakika kuna kitu hakipo sawa. Hata iweje, Colins sio mtu wa kukata mawasiliano gafla! Nijulishe kama kuna kitu kitahitajika nisaidie.” “Nashukuru shem, lakini eti nilikuwa nikiogopa!” “Wasingekuja wote kutaka msaada wako wakiwa na nia ya kukuangamiza tena ukiwa uliwaacha kama walivyoomba! Wewe nenda. Baada ya muda nitakupigia kujua unaendeleaje.” “Hilo litanitoa hofu. Nashukuru. Ila kwa sasa, usimwambie kwanza Jema. Acha nikajue kinachoendelea ndipo nitajua chakuwaambia.” “Sawa.” Wakaagana angalau akapata amani kupata baraka za shem wake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi kila akifikiria anakwenda kukutana na Colins! Akajikuta akitabasamu peke yake na kulamba midomo. Alishakuwa na hamu na huyo kiumbe, akawa hana jinsi. Lakini kila moyo ulivyokuwa ukipokea hizo hisia, wasiwasi ukazidi kumuingia na uhalisia kumsumbua. Akili zikamkumbusha jinsi Colins anavyokuwa linapofika swala la Love. Yeye husubiri. Na si yeye tu, hata wazazi wake wanakuwa kama wanachanganyikiwa linapofika swala la Love.

Sasa iweje leo atafutwe yeye! Akahisi kuna kitu hakijakaa sawa. Wazo likamjia, kumpigia anti wake, mwenye saluni anakokwenda kutengeneza nywele Love, kujua kinachoendelea. Maana alisha acha kupokea yanayoendelea juu ya Love, Kemi na Colins. Akayazira, maana yalikuwa yakimuumiza tu roho.

Ukweli Halisi.

“Niambie anti langu la ukweli.” Akaanza Jelini. “Nipo kipenzi. Nipe mpya za mjini.” Jelini akaanza kucheka. “Anti kwa kupenda mpya!” “Ndio yanayotuweka mjini je!” “Wewe ndio nipe za Love.” Akaanza kucheka. “Acha nitafute mahali, nikae nikwambie kwa kituo.” “Anti!” “Kumbe! Wasomi wale wa kingereza, wamegeukana. Bi dada anadai shoga yake wa uzunguni, kampa mganga wa kienyeji akimwambia nabii sijui mtume au mtumishi, watajuana wenyewe, lakini analalamika amemlogea mwanaume. Kawa tahira kabisaa.” Jelini alishituka sana.

“Anti!” “Walahi! Bora ulijiachia anti langu. Unaambiwa mwanaume amekuwa wakufunga na kamba! Yule mtumishi alijidai alikuwa akimuombea, kumbe madawa ya kienyeji!” “Kwamba yeye alikuwa hajui?” “Bwana kama ulikuwepo hapa. Nasra alimuuliza hivyohivyo. Si unamjua Nasra mdomo hauna kufuli?” “Maana kweli! Kwani uchawi siri?” “Bwana wewe akili yako kama Nasra. Nasra akamuuliza hivyohivyo. Akamwambia, uganga wa tunguri na wa hawa matapeli wa siku hizi wa maombi vinafanana ila kama upo makini utajua tu.” “Sasa akasemaje?” “Anasema eti alikuwa akimchukua kumuombea chumbani.” “Muongo. Mshenzi mkubwa.” Jelini akawa amekasirika.

“Bwana Nasra akaambadilikia mpaka ikabidi nimtulize. Nikamwambia atanifukuzia wateja. Maana wakija hapa, wanaongea yao, sisi kuwasikiliza na kuwapamba si kuwakashifu! Sasa Nasra akawa anamwambia eti yeye mwanzo alivipenda, mpaka daktari akazidisha dozi, eti ndio ameanza kukimbia.” “Akasemaje huyo Love?” “Yeye anavyodai yule mzungu mwenzie, Kemi, ndio amemchezea mchezo. Na amemfungia simu zake, nasikia hampati tena pamoja na huyo mtumishi wake. Ni kama lishamvujia hivi!” Sasa Nasra akawa anamwambia eti yeye mwanzo alivipenda, mpaka daktari akazidisha dozi, eti ndio ameanza kukimbia.” “Akasemaje huyo Love?” “Yeye anavyodai yule mzungu mwenzie, Kemi, ndio amemchezea mchezo. Na amemfungia simu zake, nasikia hampati tena pamoja na huyo mtumishi wake. Ni kama lishamvujia hivi!” Akaendelea kumsimulia Jelini.

“Sasa tokea aanze kuusema ubaya wa mwenzie hapa saluni, na yule mwenzie, Kemi, akifika hapa, mashauzi. Anagawa soda za bure kwa kila mtu. Acha wapenda vya bure wa hapa wambadilikie! Wanamwambia hakudanganywa na Kemi, aliyataka yeye mwenyewe, ila vimemdodea, ndio hayataki matokeo.” “Na kweli.” “Basi hajarudi tena tokea siku hiyo. Nina kazi ya kuwalaumu hawa, wamenipotezea mteja mpya maana hapa aliletwa na huyohuyo mwenzie Kemi.” Akaendelea kumueleza mengi na kuzidi kumuumiza sana Jelini.

“Sasa tokea aanze kuusema ubaya wa mwenzie hapa saluni, na yule mwenzie, Kemi, akifika hapa, mashauzi. Anagawa soda za bure kwa kila mtu. Acha wapenda vya bure wa hapa wambadilikie! Wanamwambia hakudanganywa na Kemi, aliyataka yeye mwenyewe, ila vimemdodea, ndio hayataki matokeo.” “Na kweli.” “Basi hajarudi tena tokea siku hiyo. Nina kazi ya kuwalaumu hawa, wamenipotezea mteja mpya maana hapa aliletwa na huyohuyo mwenzie Kemi.” Akaendelea kumueleza mengi na kuzidi kumuumiza sana Jelini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akafika mpaka kwa kina Colins, akafunguliwa geti kama aliyekuwa akisubiriwa mpaka na mlinzi! Akavuta gari mpaka ndani, akaegesha na kubaki ndani ya gari akisikiliza kwa undani kujua kilichokuwa kikiendelea huko Kigamboni.

Connie alipoona hashuki garini, akamfuata nje. Akamfanyia ishara anyamaze, ila akamkaribisha ndani ya gari. Connie akapanda. Akamfanyia ishara yupo kwenye simu. Akataka kushuka, akamkonyeza asikilize. Jelini akaweka kwenye spika. Bado gari lilikuwa linawaka, wanakula upepo kwa ndani. Jelini waliyemkataa hajasoma, siku hizi mambo yake safi. Hapo ametulia ndani ya gari hata Connie mwenyewe anayesomea udaktari haendeshi gari nzuri kama hiyo ya Jelini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Upo anti langu?” “Nipo nipo. Nimeweka gari pembeni kukusikiliza vizuri. Aliyoyasema Kemi juu ya Love.” Akataka aendelee alipoishia. “Si ndio shoga yake alikuwa akimsema hapa kuwa ni mnyama mbaya kuliko chui! Kwamba Love hakutaka kusema nyumbani kwao kuwa huyo mwanaume wenu alianza kuugua ili aendelee kutumia yeye mshahara wake! Na nasikia shida yake kubwa ni hilo jumba la wazazi wao huko Kigamboni. Hakutaka kusema ugonjwa wa mwenzie ikaonekana wameshindwa kuishi huko, wakatolewa kwenye hilo jumba akarudi kuishi kwao. Kwa hiyo mwanaume alivyokuwa tahira, yeye akalinyamazia, akawa anajishindia tu mihela ya huyo bwana. Maana nasikia yule mwanaume alikuwa akilipwa mihela ya maana tu, kwenye hiyo kampuni ya wazazi wao, na jumba hilo ndio roho yake huyo mwanamke wake.” Akaeleza mengi mno mpaka uchungu. Connie akalia sana, akisikiliza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wasomi hao wawili, Kemi na Love wakageukana vibaya sana, wakianikana kwenye masaluni kama waliokuwa maadui, kumbe walishirikiana kuhakikisha wanamtoa Jelini kwenye maisha ya Colins, ili Kemi amlipize kisasi Jelini. Halafu kwa upande wa Love ndio hivyo, maslahi. Kemi alipomkabidhisha ushindi Love, na kuhakikisha Jelini na yeye amekosa, akawa amemaliza kazi yake. Akajiweka pembeni na kumuachia Love uwanja.

Hakutaka tena hata mahusiano na Love. Love alikuwa njia ya kusadia kulipiza kisasi tu. Lakini hapo ndipo Jelini akaamini maneno ya Colins, kuwa ni kweli Love hakuwahi kumpenda yeye kama Colins. Anti yake akawasimulia mengi mpaka akaridhika ameyamaliza, na kuwaaga.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Nisikilize Connie. Cha muhimu hapa ni maombi. Najua huwa yanasaidiaga sana. Nimeona kwa Jema. Mimi sijasimama sana kwenye dini, ndio nimeanza tu. Hata leo nimeomba kabla yakuja hapa. Tumeshajua kilichompata Colins. Akiombewa kwa ukweli, atafunguliwa tu. Usiogope.” “Ni hivyo hujamuona. Coly anatisha, Jelini wewe! Ngumu kumtambua. Sasa najiuliza huyu Love alitaka kumfungia huko mpaka lini?!” “Hayo hayatasaidia. Mwishoe wote tutajikuta njia panda, kutafuta majibu ambayo hata tukipewahayatasaidia.” Simu ya shemeji yake ikaingia.

“Hata ndani sijaingia shem. Nilikuwa nipo kwenye gari nikielezwa yaliyompata Colins. Naona ulikuwa sahihi. Nitakusimulia nikitoka hapa.” “Basi nitakupigia tena baada ya nusu saa ili nihakikishe upo salama.” “Hapa nipo na Connie, nahisi ni salama. Usiwe na wasiwasi.” “Hapana Jelini. Nataka kukusikia ukishamuona Colins.” “Sawa.” Wakaagana. Ndipo wakaingia ndani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa asili nyumbani kwa kina Colins pametulia. Ila alikuta hali ya simanzi. Wazazi walikuwa sebuleni kama waliokuwa wakimsubiria. Jelini akawasalimia akikaa. “Karibu.” “Asante. Colins yupo wapi?” “Amelala.” Jelini akatulia kidogo kama anayefikiria. “Ila hajalala kwa dawa. Hatachukua muda mrefu kuamka.” Akaongeza mama yake kwa sauti ya kusihi. “Ni sawa nikiingia kumuona? Maana mimi nina muda mfupi sana, nataka nimuone, nirudi kwenye majukumu yangu. Nimeacha pale bila uangalizi wa maana.” Kama wambebe mpaka huko chumbani!

Hatimaye!

Akaongozana na Connie mpaka kwenye hicho chumba. Jelini alishituka kumuona pale alipolala, mpaka pochi, simu na funguo za gari vikaanguka na kubaki ameshika mdomo. Alikuwa ni mzee kuliko babu yake aliyemfuata kwao na. kumuonya amuache. “Hataki kula! Ndio kinachomfanya achoke zaidi, mama anamuwekea dripu.” Jelini akamsogelea pale kitandani.

Alikuwa Colins. Akakaa taratibu. Akamvuta mkono wa kushoto ule uliokuwa upande wake na kuupakata. Kisha Connie akamuona anaingiza mkono ndani ya shati na kumshika kama vile Colins mwenyewe anavyojishika. Akautuliza huo mkono hapo juu ya ziwa lake la kushoto, kisha akampapasa kidogo. Colins akafungua macho.

Akamtizama kwa muda kama anayefikiri ni ndoto au kweli! Jelini akamuwahi kabla hajafunga macho. “Pole Colins.” “Jelini!” Akamuita kwa sauti ya chini sana, dhaifu. Ila akamsikia. “Nimekuja kukuona.” Akamuona machozi yakimtoka. Akamfuta taratibu. “Pole. Unasikia baridi?” Akakubali. Connie akamsaidia kusogeza shuka. Wakabaki  wakiangaliana.

“Nikupe chakula kidogo ule?” Akabaki akimtizama. “Ni mimi Jelini. Nataka kukupa chakula. Halafu…” Akainama kumnong’oneza sikioni akimwambia, “Nitakubembeleza ulale vizuri.” Akakubali. “Nisaidie hata uji, nimpe.” Connie kama akimbie! Akabaki akimpapasa, akamuona anafunga macho. “Usilale mpaka ule. Sawa?” Akafungua macho, akamwangalia. “Jelini!” “Nipo hapa na wewe Colins. Pole.” Akahema kwa nguvu, akamuona anatulia.

Baada ya muda akarudi na bakuli la viazi vyakupondwa na nyama ya kusaga. Vimechanganywa. “Kinanukia vizuri!” Jelini akasifia. “Kaa vizuri nikulishe.” “Acha baba aje amuweke vizuri.” Mzee akaingia kwa haraka kama ambaye alikuwa mlangoni, akasikia! Jelini akamuona vile anavyomuweka kwa makini, akamuweka akawa amemuegemeza kwenye mito. Kisha akawapisha. Akabaki akimwangalia Jelini.

“Ukikazana kula, utapata nguvu. Wewe fungua tu mdomo, na kutafuna. Nitakuwa nikikuwekea mdomoni.” Akakubali. Akaanza kumlisha taratibu kama mtoto. Anatafuna taratibu, lakini anameza. Akala mpaka akakaribia kumaliza, akamuona anajiegemeza kama alale. “Umekula vizuri. Ukikazana hivi, utapata nguvu kwa haraka. Unataka kunywa maji? Akakataa.

Connie akamsaidia kuondoa vyombo pale chumbani. Jelini akajivuta juu kabisa ya kitanda. Akaegemea kitanda. Akamuonyeshea asogee, ambembeleze alale. Akamsaidia kumvuta mpaka mapajani. Alijilaza vilevile kama alivyokuwa akimlalia zamani. Mpaka Jelini akacheka. Akaanza kumpapasa taratibu. Akageuka kumtizama. “Jelini!” Akamuita tena taratibu. “Nipo Colins. Ni mimi.” Akabaki akimwangalia. Akaanza kumchezea nyusi. Connie kurudi kuwakuta vile, akatoka taratibu.

“Jelini!” Akamuita tena. Akamvuta mkono wake, akauweka shavuni kwake. Vidole vilikuwa kama njiti! Akamshika vizuri, akabaki akimpapasa Jelini shavuni. Wakabaki wakiangaliana mpaka akamuona anaanza kusinzia. Mkono ukaanguka. Akaudaka na kuungalia jinsi ulivyokuwa na alama na kuzidi kuumia nafsini mwake. Akamuita Connie.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Nisaidie kunipa shuka jingine. Naona vipele vya baridi vinaongezeka. Na mwili upo kama unajoto!” Wakaingia wazazi wake kwa haraka kama ambao walikuwa wamesimama hapo mlangoni wakisubiria. “Acha tumpime homa.” Kweli akakutwa na homa. Haikuwa kali. Lakini baba yake akamchukua na damu, akaondoka kwenda kuipima. Akabaki amempakata kichwa akimpapasa akarudi tena kulala maana aliamka wakati baba yake akimtoa damu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

James akapiga simu. “Nipo naye shem. Lakini anahoma. Ndio ametolewa damu kwa vipimo.” “Aisee mpe sana pole. Nikitoka kazini nitapitia.” “Nashukuru shem.” Wakaagana.

Huyo Jelini hapo akawa kama amefika. Wakashangaa haondoki hapo kama alivyosema ameacha dukani hakuna mtu! Muda wote wala hakumuweka pembeni. Naye Colins akifungua macho anamuangalia kwa muda, kisha anamuita kama kuhakikisha. “Jelini!” “Nipo Colins. Usiwe na wasiwasi.” Akawa anamtuliza, kisha anarudi kulala.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wala haukufika muda wa kutoka kazini, James naye akawasili hapo. Alifurahi kumuona Colins, ikapita muonekano. “Vipi wewe?” Akawa akimuuliza huku akicheka kama aliyeokota lulu, haamini! Baba yake akarudi na dawa. “Itakuwa hayo madonda ndiyo yanampa homa. Ila hana infection yeyote ile.” Akamuanzishia dawa ya kukausha madonda.

James akamsaidia baba yake jioni hiyo kumuogesha. Akabadili mashuka, pakawa pasafi hapo kwenye hicho chumba. Wazazi wa Colins wakashangaa anafanya bila kinyongo, wakikumbuka onyo la kutokuwa karibu na kijana wao. Akafanya kwa moyo wote kama na yeye aliyekwisha kuwa na hamu sana na huyo Colins.“Kula ugali urudi mtaani bwana! Acha kula kama JJ.” Angalau pakawa na utani, ila Colins akawa akimwangalia tu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ikabidi Jelini amuite James sebuleni wazungumze. Wakatoka Colins akiwa amerudi kulala. Akamsimulia kwa sauti ya chini kama mtu aliyekuwepo pembeni asisikie. Akamwambia yote aliyosikia mchana huo, na Connie akiwa naye garini wakisikiliza. Kumbe wazazi nao walikuwa wakisikiliza kila hayo mazungumzo. Kwa hakika hao wazazi waliumia sana. Walibaki na majuto yasiyokuwa na maelezo.

“Mimi ninachoona anahitajika maombi ya kweli. Lakini mimi sijui kuomba.” Jelini akajitoa. “Mimi namjua mtu anayetembea na hofu ya Mungu. Si mchungaji, lakini yule jamaa anampenda Mungu wake. Na amefanikiwa mno kwenye kila jambo. Mungu ameweka mkono wake mpaka kwa mke na watoto wake. Anamjua Mungu na kuishi naye si kwa mazingaombwe kama hawa watumishi wa siku hizi. Ni kama Baba yake kweli. Ukiwa naye, utajua yupo Mungu aliye hai.”

“Ni nani shem?” “Bosi wake Jema. Anaitwa Joshua Kumu. Yupo busy sana. Lakini ni mtu wangu wa karibu. Mkihitaji mtu wa kuomba kwa ukweli, yeye atakuwa msaada.” Wazazi wake wakaangaliana.

“Hapa tulipo sasahivi, sidhani kama tuna msaada mwingine bila Yesu. Maana tumetumia kila dawa tunayojua ingeweza kumsaidia, lakini ni kama hivyo mnavyomuona.” Akasalimu amri baba Colins. “Na mama je!?” “Nina majuto James mwanangu, sina jinsi nikaeleza mtu akanielewa. Sijui nilipatwa na nini! Ninachotaka ni apone tu.” “Basi acha nimpigie simu. Ila huwa hatoki kabisa, akifika kwake. Ana mapacha umri karibu na JJ.” “Tafadhali mjaribu. Akishindwa leo, tumuombe wakati atakao weza.”

James akatoa simu. Akampigia. Ikaita mpaka mwisho haikupokelewa. Hakupiga mara ya pili. Akasema waache, atakuja kurudisha simu atakapokuwa na nafasi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baaada ya masaa kama mawili hivi, tena James alikuwa akikaribia kuondoka, ndipo akamrudishia simu. “Nilikuwa nikimalizia siku na kina Kumu. Hata sikuwa na simu.” “Usijali kaka.” Akamuelezea kwa kifupi. “Daah! Hiyo ni ya kushugulikia kwa haraka. Acha nizungumze na Naya, akitoa baraka zake, nije mara moja niungane na nyinyi kwenye maombi.” “Nashukuru Kumu. Na samahani kwa usumbufu.” “Bila shaka.” Akaaga. Wawili hao tokea Bale aweke ombi lakumuoa Vai, na James kuomba muda wa kufikiria, hawakutafutana tena. Ndio Joshua anamsikia James usiku huo.

Akufaaye Wakati Wa Dhiki, Ndiye Rafiki Wa Kweli.

Baada ya lisaa, Kumu akawa ameingia hapo. “Hujambo Jelini?” Jelini akacheka. “Kumbe unanikumbuka!?” “Siwezi kukusahau. Si ulisema kwenu wewe ndio mtoto mzuri. Mpole kuliko Jema.” “Kabisa. Mimi ndiye kiziwanda wa mama Jema. Ni mtoto mzuri kuliko Jema.” James akamtizama na kutingisha kichwa. Wakacheka.

“Nashukuru kwa kuja Kumu.” “Ni vile sababu ni James. Nisingerudisha simu kwa haraka. Nina watu wangu wachache sana kwenye maisha yangu, na simu zao huwa hazisubiri, pengine niwe sijaona kwa wakati. Na wenyewe wananijua mimi na ratiba zangu. Kuna mida nikiona simu zao, najua si za kurudisha kwa kuchelewa, ni dharula. Na najua pia ni kusudi la Mungu ili na mimi nishiriki kwenye maombi.” Wakamuona vile alivyo mnyenyekevu.

“Mimi mwenzio sijui kuomba. Ndio Jema amenifundisha leo. Eti ni kama kuzungumza hivi na wewe?” Wakacheka vile alivyojiwahi. “Kabisa. Huyu Mungu mwenye enzi yooote, ametupa bahati ya kutufanya na sisi kuwa WanaHuhitaji maneno ya aina fulani kuzungumza naye. Ni kama hivi mimi ninavyozungumza na wewe hapa. Na uzuri, hana tatizo la kusikiaMaandiko matakatifu yanasema, sikio lake si zito, hata akashindwa kusikia.”

“Halafu yeye mwenyewe anatuita tusemezane naye. Anataka mazungumzo na sisi. Kwa hiyo hapa tunachokwenda kumwambia ni kuwa, Colins anaumwa, tunaomba aingilie kati, amponye afya yake. Maana hata maandiko matakatifu kutoka kwenye bibilia yanasema, ‘ukiwa huwezi, basi ita wazee wakuwekee mkono’. Vinginevyo hata yeye mwenyewe angeweza kujiombea akapokea tu uponyaji.” Akazungumza nao kirahisi sana, wakabaki wakimsikiza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kumu mwenyewe anajiwakilisha haswa. Ukimtizama kuanzia juu mpaka chini, na aina ya gari aliyoacha hapo nje, harufu ya neema aliyoingia nayo hapo ndani. Jinsi alivyosimama kwa ujasiri. Nadhifu hata mida hiyo. Haonekaniki na shida ya aina yeyote ile. Ukimuona tu, utajua kuna utoshelevu ndani yake. Hata akizungumza huwezi tilia mashaka anachozungumza. Anasikika kwa wazi, kirahisi na kifasaha haswa. Mungu anayemzungumzia yeye, hajamuweka kwenye mafumbo. Alimtambulisha kwao kirahisi mpaka wakajisikia kufunguliwa wao wenyewe kwanza hata kabla ya Colins.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ndipo wakamuingiza chumbani kwa Colins. “Msiogope, na msiondoke. Njooni tuombe pamoja.” “Yule mtumishi wa kwanza alikuwa akitaka kubaki naye peke yake ili amfanyie maombi.” “Bibilia inasema, ‘wawili au watatu, wakikubaliana lolote chini ya jua, nalo litakua’. Tufunge na kuharibu roho za uharibifu, tumuite Yesu aliyekuja kutoa uzima tele, kwenye maisha ya Colins. Tushikane mikono hapa kumzunguka hapo kitandani, tuombe.” Wakafanya wote kama alivyowashauri.

Nalikuja Ili Wawe Na Uzima, Kisha Wawe Nao Tele.

{Yohana10:10}

Colins alikuwa amefungwa na nguvu za giza. Haikuchukua muda mrefu, Kumu akaamuru mapepo yatoke kimyakimya, yamuache huru, bila kuleta uchonganishi kwenye familia, asijue walishamjua mbaya wao. Na kweli, akaomba, Colins akafunguliwa. Ukweli Colins alifungua macho akionekana wazi amefunguliwa. Japo hakuwa na nguvu, lakini alionekana anao ufahamu wake.

“Wewe si kama yule mtumishi mwingine aliyeniombea. Alinifanya nisiweze kufanya ninachotaka. Halafu nikawa siwezi…” Ni kama akashindwa jinsi ya kujieleza. “Huyo ndiye Yesu tunayemtumikia. Tokea anafika hapa duniani, na pia ilitabiriwa hata kabla hajaja hapa dunia kwenye bibilia Isaya 61:1-4 kisha kuja kusema yeye mwenyewe kwenye Luka 4:18, ‘Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa.’ Hizo ndizo kazi zake Yeye.” Kumu akaendelea akiwa na furaha kana kwamba yeye ndiye aliyewekwa huru.

“Na anapopita sehemu utajua tu  kama ni Yeye amepita. Maana anaacha hizo sifa. Utasikia uhuru wa kweli.” Akazungumza na Colins kwa taratibu, wote wakimsikiliza. “Kazana kula. Umepata nguvu za nafsi na roho, lakini mwili wako unahitaji kupona. Chakula ni muhimu.” Akawaombea wote mle ndani akitubu kwa niaba yao, akawabariki na kuwaombea amani.

“Sasa sisi tuna watoto wadogo. Na mimi nashinda kazini siku nzima. Usiku wakilala hivi, ndio na sisi tunapata muda wetu. Nikichelewa kutoka hapa, nitamkuta Naya ameshalala. Naomba niwaage. Wewe James niseme baadaye.” Wakamshukuru, James akamsindikiza akimshukuru lakini ndio akawa ameongeza deni. Bale anataka kuoa dada yake kabla hajamaliza shule, na ana baraka za Kumu. Inamaana wakati yeye anasuasua kutoa jibu, Kumu na Geb wanamsubiria tu, huku wakimfanyia yake kwa haraka bila kuchelewa hata katika mida isiyo rafiki kama siku hiyo. James akabaki na deni zaidi.

Kilichokuwa Kikiendelea Kwa Colins

Baada ya muda James akarudi. “Sasa mzee?” Akimuuliza Colins kama anayetaka kumuaga. “Ni nini kilitokea James!? Mbona kumbukumbu zangu hazijakaa sawa!?” Akamuuliza kwa sauti yake ya kudhoofu. “Ni hivi Colins. Sasahivi umedhoofu sana. Kikubwa na cha msingi, kurudisha nguvu kama alivyokwambia Kumu. Hicho ndicho kiwe cha kwanza. Cha pili kinachotaka kufanana na hicho, ni chakula kingi ili upone. Mzee umechoka! Na una madonda ambayo unahitaji kutulia, kula, kunywa dawa, upone kwa haraka, urudi mtaani. Kisha ‘mengine’ ndiyo yafuate.” Colins akavuta pumzi kwa nguvu wakamuona anafunga macho.

“Umeshaoga. Umekula. Umekunywa dawa. Nashauri ulale.” “Najisikia vizuri. Yaani ndani najiona mwepesi sana. Kuna uhuru wa ajabu ndani yangu. Sijajisikia hivi mufa mrefu sana. Ilikuwa kama…” Akatulia akifikiria. “Mtu mwingine anaishi akiutumia mwili wangu kufanya anachotaka yeye si mimi. Hata nikitaka kukataa, yeye analazimishia na sina jinsi ya kupinga. Niliteseka, sikuwa na jinsi ya kujisaidia.” “Aisee pole sana. Mimi nitarudi hapa alfajiri kabla ya kwenda kazini. Nikishakuosha na kula, ndio nitaenda kazini ili nimpokee mzee.” Wakamuona anatokwa na machozi.

Wa Rohoni.

“Usiwe na wasiwasi James. Nimeagiza nesi anakuja kesho asubuhi. Ata..” Jelini akashituka kama kapata habari mbaya. “Kwamba huyo nesi ndio awe anamuogesha Colins!?” Akauliza kwa kupaniki. “Na kumsafisha madonda.” “Mhhh!” Wakamsikia akiguna. “Anahitaji muuguzi mbali ya mama yake, zaidi ninapokuwa kazini.” “Kwamba huyu nesi ni mdada!?” Swali la pili likawafanya watulie, ila kushangazwa wivu kwa Colins aliyekuwa kama kinyago! Haikuingia akilini. Wakaona haiwezekani.

“Nimempata kwenye moja ya kliniki zetu. Ni binti mzuri tu, aliyetulia. Na…” “Hapo mzee wangu ndio naona unaelekea kwenye kuongeza tatizo.” James akamuwahi, mzee asielewe. Jelini akashangaa kwa sauti kabisa. “Kwamba binti ndio aje hapa, halafu ndio aanze kumuogesha Colins!?” Akahamaki na kuongeza. “Mimi hivyo sioni kama ni sawa.” Akaongea bila hata hofu kana kwamba Colins mumewe.

“Au kwa nini usizungumze na Judy? Ni mdada mtumzima na anahekima.” Akasaidia mama Colins. “Tena hao kina dada watu wazima ndio wabaya kabisa. Unakuta wana vijimambo vyao halafu nguvu ya kumsaidia mtu kama Colins hawana. Unadhani wana msaidia, kumbe wanakuwa na lao jingine. Halafu huku nyuma wakati nyinyi hampo wanakuwa wana mnyanyasa kwa siri. Nyinyi mnaendelea na shuguli zenu huko, mnadhani mmemuacha Colins kwenye mikono salama, kumbe huku yeye anakuwa akimnyanyasa. Hivyo mimi sitaweza.” Jelini akaongeza akilalamika kabisa, kana kwamba anahusika kwenye maamuzi. Colins amelala kitandani anamtizama. Wazazi wakakwama. Ila na mshangao kama waliochanganywa tayari.

“Mimi naenda kumletea Colins maji ya kunywa.” Akatoka hapo chumbani alipoona wamenyamaza. “Nyinyi hamjamjua Jelini. Ana wivu na Colins. Hivyo hataki mtu mwingine amguse wala si sababu nyingine.” James akanong’ona. “Colins mwenyewe alivyochoka hivyo!?” Akaongea mama yake kwa mshangao akimtizama huyo Colins mwenyewe. “Kama huamini mama CJ, akirudi hapa mjaribisheni kumwambia mtamleta mwanaume. Muone kama na huyo hatamletea kipingamizi.” James akaongea akinong’ona pia.

Akarudi na glasi ya maji. “Unatakiwa kunywa maji, Colins.” Colins akamtizama vile alivyobadilika. “Usikasirike.” Colins akamwambia kwa upendo. “Watu hawaaminiki. Huwezi kuleta kila mtu karibu yako.” Akaongea akimtizama Colins lakini kama anayewaambia wote hapo chumbani. James akamfanyia ishara baba yake Colins. Akajua ndio anamwambia amjaribishe.

“Ni kweli mama. Si kila mtu wa kumuamini. Basi nafikiri nimletee nesi wa kiume mwenye nguvu ambaye anaweza kumsaidia vzuri.” “Mmmmh!” Akaguna tena na kubaki akimtafutia na huyo sababu. Baba CJ akamuwahi. “Huyo nitakayemleta nitahakikisha namuweka sawa kabisa. Colins anahitaji msaada wa ukweli. Tena mwenye ujuzi wa kiuuguzi.” “Sasa hao ndio wabaya kabisa baba CJ. Unakuta wewe si ndio unamuamini hivyo. Anajua umempa sifa zote hivyo! Kwamba wote tunamtegemea yeye hapa kwa Colins. Mwenzio anaanza kiburi na ujuaji. Yaani anaanza kuishi na Colins vile anavyotaka yeye, mwishoe anaanza manyanyaso. Wote tunakuwa tunamfuatisha anachotaka yeye. Mimi hivyo sitaki.” Nusura wacheke. Wakaamini maneno ya Colins.

“Sasa wewe unashauri vipi.?” Ikabidi mzee amuulize. “Mimi sijasema siwezi kumlea Colins, mimi mwenyewe!” Akaongea bila shida, kama asiye na majukumu yeyote yale na hapo ndio kafika. “Peke yako hutaweza mama! Na kunatakiwa utaalamu kwenye hivyo vidonda.” “Kwani si mama yake anifundishe, nifanye mimi mwenyewe! Kwanza mimi nilitaka kuwa nesi. Muulizeni Colins kama nadanganya sasahivi. Ila tu sitaki kwenda shule.” Connie akashindwa kujizuia akacheka.

“Mimi sidanganyi hata Colins ni shahidi yangu. Napenda mambo ya unesi. Ukinipa dawa ukaniambia jinsi ya kuzitumia, mimi sishindwi. Kwanza nitakuwa mtu wa kuaminika kuliko hawa wasichana wanakuja hapa, wanaanza kumchungulia tu na kumshikashika bila adabu. Wanakuwa wanamuona kama sijui nini! Hapana. Hivyo mimi SITAKI.” Hapo Jelini anakatalia wazazi wa Colins, halafu sasa ni nyumbani kwao, kijana ni wao, ndio ameitwa tu kuona mgonjwa, lakini anavyokataa, na mabega juu, kwamba yeye hataki, kana kwamba yeye ndio amewakaribisha kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Mimi sijasema siwezi kumlea Colins.” Akaongeza huku ameshikilia glasi yake yenye maji, na kuangalia yale maji aliyosema anampa mgonjwa. Analalamika hapo mbele ya kila mtu kama alie vile, kuona anapokonywa mgonjwa! Hapo hakumbuki lolote isipokuwa Colins. Si majukumu mazito aliyonayo ya kibiashara, mama yake ambaye ndiye msimamizi wa hizo biashara na kupanga kila kitu, mtoto wake. Kikubwa zaidi hata Ezra hakupita akilini mwake. Akili na mawazo yake vyote vilikuwa hapo kwa muda wote asikumbuke lolote ila Colins tu. Kila kitu hataki tena.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Basi mama. Mimi nahisi tufuate ushauri wako. Ukihitaji msaada utatuambia.” Akaongeza mama CJ kumtuliza. “Mimi msaada ninaotaka ni wa shem tu. Ndiye namuamini na Colins. Na nyinyi mmeona jinsi alivyomuogesha leo na kumvalisha kwa furaha bila shida. Watu baki sitaki.” Mabega yakamsaidia kukataa. Akaweka glasi chini, asimpe mgonjwa. Akaanza kumfunika huyo Colins akiwa hasikii baridi. James akawatizama akicheka na kutingisha kichwa.

“Sasa huyo ndio Jelini, halafu sasa ujumlishe na Colins mwenyewe ambaye ubishi ndio umezaliwa kwake. Halafu ndio uwe nao siku nzima. Ujikute katikati yao! Lazima kichwa kichemke.” Wakaanza kucheka. “Sisi wote tunawajua hawa wawili. Na huwa wanawezana wao wawili tu. Huna jinsi ya kubadilisha uamuzi wa hata mmoja wao, isipokuwa wao wenyewe. Na usiombe uwe katikati ya ugomvi wao. Utakaukwa mdomo. Hawashauriki. Msimamo mkali. Kila mtu kashika pakali. Basi mimi na Jema ndio tunabaki kuhangaika.” Mpaka Jelini mwenyewe akacheka.

“Sasa wewe shem unataka tena vitoto vidogo vianze kujazana humu ndani!?” “Si umepewa mpaka watu wazima wewe?” Akapandisha mabega kukataa. Wakacheka tena, lakini kwa faraja. Maana huyo Jelini anayemng’ang’ania huyo Colins, hapo kwenyewe yupo njema. Jelini ni mzuri bwana! Na anajua kujiwakilisha popote.

“Nyinyi wazazi wangu tulieni. Huyu Colins atakuwa sawa kabisa. Tupeni mimi na Jelini hata juma mmoja tu. Tutatathimini hali nzima. Lakini naamini atapata nguvu. Uzuri Colins mwenyewe si mvivu wa kula. Naamini baada ya muda mfupi sana atakuwa na nguvu yakuweza kusimama mwenyewe bafuni na kuoga. Tukianza kumletea wauguzi hapa, tutampa hali ya ugonjwa, hatatoka hapa ndani kwa haraka.” James akaongeza.

 “Atakuwa sawa tu. Asubuhi na jioni nitakuwa nikipita. Na muda na wakati wowote wazazi wangu mtakaponihitaji, mnipigie. Huyu Jelini ndio tutakuwa tukiwasiliana.” James akaaga na kutoka kwa haraka na yeye kuwahi mkewe lakini wakiwa wameweka mipango na mikakati endelevu ya faraja kwenye hiyo familia.

Rudi Kwenye Uhalisia.

Wakamgeukia Jelini. Baada na yeye kuaga. Ila mama CJ akawa kama amekumbuka kitu baada ya Jelini kusema atarudi hapo alfajiri na kushinda naye siku nzima. “Sasa na wewe Jelini kazi?” Ndio akagutuka. Akabaki ameduaa. Anamwambiaje mama Jema aliyekwisha kinahiwa na hiyo familia? Wamfukuze kwa kijana wao akiwa mzima, leo ageuke kuwa muuguzi wakati hajiwezi!

“Ulisahau?” “Nilikuwa wala sikumbuki tena! Hivi leo nimemuachia mama biashara zote!”  Akabaki ameduaa ndio kama taarifa zinamfikia na kumgutusha kumpa uhalisia wa mambo. Zikaanza kupita taarifa nyingi kwa wakati mmoja. Maisha yamebadilika. Haipo kama ilivyokuwa tokea aachane na Colins. Mengi yalishaendelea. Wakamuona anaanza kusaka pochi yake kwa kupaniki. Wakabaki wakimwangalia.

Akaipata na kuifungua kwa haraka kama anayewahi kitu. Akapora simu yake mwenyewe ndani ya hiyo pochi. Ndipo akakutana na missed calls zakutosha kutoka kwa Ezra. Kabla hajatulia simu nyingine ya Ezra ikawa inaingia. “Mungu wangu, Ezra!” Jelini alishituka kama aliyefumaniwa, mpaka pochi ikamuanguka na vitu vyote vya ndani kumwagika, na kusambaa. Pale chumbani wote, mpaka Colins kimya wakimuangalia.

Alionekana kupaniki kwa kuvurugikiwa haswa. Ni kama kwa muda fulani hivi, ulimwengu wote ulisimama, ilikuwa yeye na Colins tu. Kumbe yupo na Ezra! Aliyempa viapo vyake na asubuhi hiyo pia akagongelea msumari. Kwa makubaliano mengi ikiwepo kula chakula cha usiku huo pamoja. Kuonana kabla ya kulala. Kuzungumza kabla ya usingizi kuwatoa kwenye ulimwengu huu wenye mengi. Akabaki ameduaa akiitizama simu yake, vitu vilivyokuwepo kwenye pochi vilivyozagaa hapo na kumzunguka na vyenyewe vikimwangalia kama wenyeji wake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ni Nini Kitaendelea Katikati Ya Wanaume Hao Wawili?

Nani Zaidi?

Je, Ni Nani Atabaki Kwenye Moyo Wa Jelini?

Na Nani Atamfikisha Kanisani Mrembo Huyo?

Inaendelea.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment