Wakajikuta wakicheka.
“Ndio unapendeza hivyo!” “Mimi napenda kupendeza. Na wewe umependeza sana Ezra.
Unanukia vizuri!” “Asante. Ila kweli umependeza sana, mpaka naanza kufikiria ni
wapi nikupeleke.” “Wewe wala usijali. Mwenzio kupendeza ndio kawaida yangu.”
Ezra alicheka sana.
“Sikutanii. Mimi
naweza kupendeza hata sehemu ambayo unaweza dhania hapahitaji kupendeza.
Napendeza tu kwa ajili yangu, ndio najisikia raha. Sijali mazingira wala
walionizunguka.” “Ilimradi wewe upendeze?” “Kabisa. Na kama nipo na Jeremy,
nataka na yeye pia apendeze sanaaa.” “Ndio maana kila wakati ni msafi?”
“Kabisa. Napenda sana awe nadhifu. Naona ndio starehe yangu.” “Hongera. Basi
tuondoke hapa.” Safari ikaanza, wakifikiria pakwenda.
“Usiogope garama,
nitakusaidia. Leo nilitamani kutoka, niende sehemu nzuri sana. Nipumzike.”
“Sijali garama, ila sehemu utakayoifurahia. Na mimi nataka usiku mzuri.”
“Mwenzio nataka usiku mzuri ambao naona nishaanza kuupata, ila na wa hadhi.” “Umeshaupata!?”
“Kabisa! Umekuja kunichukua Ezra! Nimefurahi.” Mwishoe wakakubaliana sehemu ya
kwenda. Wote walipafurahia, na wakajua watapata huduma nzuri zitakazofanana na
wao kwa usiku huo. Ezra akaelekea huko.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Walifika na kutafuta
sehemu nzuri wakakaa kwenye kona yao. Wakiangaliana. Muhudumu akafika kwa
haraka, wakaagiza vinywaji, na kutulia. “Wewe huwa unapenda nini?” Ezra akaanza
kwa swali. “Kupendwa.” Ezra alicheka mpaka machozi, maana Jelini alijibu
kwa haraka bila kufikiria. “Usicheke sasa nikwambie.” “Nakusikiliza Jelini. Ila
sikutegemea! Wenzio huwa hawasemi hivyo.” “Mimi vingine vyote sitaki.
Naweza kujitafutia mwenyewe. Kwanza sasahivi ni kama nina kila kitu.” Hapo Erza
akakubaliana naye. Jelini alikuwa mambo safi.
“Ehee!” Akataka
aendelee. “Nataka mtu anipende kwa dhati. Mimi tu, na anifuatilize. Anipe mimi
kipaumbe. Katika watu wote, mimi ndio niwe mtu wake wa kwanza.
Anibembeleze mimi tu kila wakati.” Ezra akaanza kucheka tena maana Jelini
alikuwa akijieleza kama aliyekuwa amejiandaa kwa hilo swali.
“Sitajali kama
akinipenda sanaaa. Ndio nitafurahi. Umeelewa sasa?” “Nimeelewa Jelini.”
Akakubali akicheka huku akimtizama, mara kinywaji kikaletwa, akainamia glasi
yake na kuanza kunywa bila wazo la pili.
“Labda niulize swali
jingine.” “Karibu.” Ezra akaanza kucheka akimwangalia. “Usicheke sasa!” “Sawa
Jelini. Itakuaje sasa ikija kutokea mtu akakupenda hivyo na wewe usimpende?”
“Wala sitampa mtu bahati ya kunipenda kabla mimi mwenyewe sijampenda kwanza.”
“Waw!” Ezra akajiweka sawa.
“Sasa wewe utapata
wapi muda wa kunipenda wakati haupo na mimi? Huna namba yangu ya simu wala
hukai karibu yangu! Utanipendaje sasa? Si mpaka nikupe nafasi ya kuwa karibu na
mimi ndio utaweza kunipenda!” “Lakini kweli!” “Umeona sasa?” Ezra akatulia
akifikiria.
“Swali jingine.”
Jelini akaanza kucheka. “Bora niulize nijue vizuri.” “Wewe uliza.” “Hudhani
huyo mtu akipata hiyo nafasi atakua akihofia kukosea. Atabaki akibabaika mpaka
atakosea kweli kwa hofu?” “Ujue huyo mtu atakuwa hajanipenda kwa dhati. Mtu
anayekupenda kwa dhati hajitahidi kukufurahisha. Na wewe utamuona tu. Inakuja so
natural. Anakuwazia furaha yako kuanzia asubuhi mpaka usiku. Anafikiria
kula yako. Hata kama anakua amechoka, anatoa muda wake anakuja kula na
wewe. Anahakikisha umeshiba. Anataka kujua siku yako iliendaje. Na si kwamba
anakuuliza tu, anakua anakusikiliza kila neno. Halafu ukimwambia kitu, hasau.” Hapo
Ezra akatulia kwa furaha maana alisema yote anayomfanyia yeye.
“Jelini wewe umejawa shukurani
mpaka unanifanya nianze kujichunguza mimi mwenyewe.” “Kwa nini tena?” “Aaah!
Sijui bwana! Ila sijawahi kukutana na mtu anayeweza kugeuza jambo dogo,
akalikuza kwa shukurani kama wewe. Na hufananii hivyo kabisa! Unafurahishwa na
vitu vidogovidogo sana!”
“Acha nikuulize Ezra,
kisha uniambie tu ukweli. Wewe unapata mtu. Sio kwamba ni wa kijiweni. Hapana.
Anashuguli zake. Nyingi tu tena za maana. Kumbuka huyu mtu anaamka saa 11
asubuhi. Anaratiba nyingine za kifamilia pia. Kanisani. Lakini bado akiona jua
kali, hata kama yupo njiani akiwa na shuguli zake, lakini anachepuka hata
kukuletea maji, anahakikisha unayanywa hayo maji, ndipo anaondoka.” Ezra
alicheka sana. Maana alimfanyia hivyo Jelini akimwambia anaweza kuwa busy
akasahau kunywa maji. Alimletea chupa ya maji akiwa anawahi kanisani.
Akasubiria mpaka alipoimaliza, ndipo akaondoka.
“Halafu mchana. Muda
wake wa chakula, anakuletea wewe matunda na maji pia. Na jioni. Mtu huyohuyo
mwenye majukumu yake, eti anakufuata kazini. Anakusubiria kwenye gari mpaka mle
naye. Kana kwamba haitoshi, anakutafuta tena usiku. Kukusikia kama ulirudi
nyumbani salama. Nakutaka kusikia siku yako iliishaje. Na hasau wafanyakazi wako
wote na vituko vyao.” Hapo Ezra alicheka sana. Maana alianza kuwa akiwaulizia
wafanyakazi wa Jelini kwa majina na vituko vyao. Basi watazungumza wakicheka
viroja vya siku mpaka kuagana.
“Acha kucheka bwana!
Sasa wewe niambie, hivyo ni vijikiti vidogovidogo?” “Hapana Jelini.” Ikabidi tu
akubaliane naye tena. Maana alishakuza tena aliyomfanyia. “Umeona eeh! Sasa utafananisha
na kuhongwa nyumba au gari halafu mtu hakujali? Anakua na mambo mengi na
wanawake wengine akikunyanyasia mamali aliyokupa! Akuu! Mimi hivyo sitaki.
Sasahivi hata mimi nikitaka gari ingine naweza kujinunulia mwenyewe bila
hongo.” “Hapo nimekuelewa Jelini. Nimeelewa sana.” Wakatulia na muhudumu
alikuwa amefika.
Jelini mzoea kula nje
na alishaishi na Kasa, anajua majina yote kwenye menu. Akachagua kwa urahisi tu
mpaka Ezra akamshangaa wepesi wake. “Naona mwenzangu wewe mwenyeji kwenye
maeneo haya!” “Sitakudanganya. Mimi sinaga shida kucheza kwenye viwanja vya ugenini.”
Ezra alicheka sana.
“Ujue Jelini wewe ni
mtundu sana!” “Acha nikusaidie Ezra. Mimi sina neno.” Akaongea kwa urahisi tu,
na kuanza kumtajia vile vyakula mpaka Ezra akapata anachotaka. Wakamuagiza
muhudumu, akaandika na kuondoka baada ya kuwaongezea vinywaji.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Jelini?” Jelini
akamwangalia maana aliomba abakie na menu, asome kitu atakachoweza kuagiza
chakula cha kuondoka nacho. Jeremy alimwambia hatalala anasubiria chakula cha
hotelini.
“Abee!” Akaitika
akifunga menu. “Eti unafikiri naweza kufaa nikawa mtu wako?” “Yaani hapo ndio
unanitongoza!?” Ezra hakutegemea, ilibidi acheke yu. Maana alianza kwa hofu
sana akikusanya nguvu. “Nyie jamani Ezra! Sasa hivyo ndio unanitongozaje
jamani! Huna swaga kabisa! Mimi sijavutiwa.” Jinsi alivyolalamika na kupandisha
mabega kabisa, Ezra akashindwa hata kumtizama. Alicheka sana.
“Bwana nitongoze
vizuri na maneno mazuri sio hayo maneno ya jumla hivyo!” “Jelini!” “Kweli hivyo
mimi sitaki. Wenzako wanasemaga yale maneno mazuri. Mpaka wengine wakinywa maji
eti wananiona kwenye glasi.” Ezra hana mbavu.
“Sasa hii ndio kali
Ezra. Mwingine anasema yeye halali, usiku ananiota.” Ezra akazidi kukaukiwa ila
yeye Jelini analalamika. “Sasa anakuotaje hajalala?” “Ndio ushangae sasa.
Lakini wewe huoni hizo ngonjera zinavutia? Wewe umekuja kirahisi sana bwana!
Mimi hivyo sitaki.” “Basi nisamehe Jelini. Naanza upya.” “Sasa sio
sasahivi na wewe Ezra! Tusubiri kidogo mshituko uishe! Maana umenishitua sana.
Hujanitendea haki.”
“Kipengele cha
kunisamehe je?” “Nitakufikiria Ezra. Umecheza sana chini ya kiwango. Na
nitakuja kusimulia na wanao, jinsi ulivyoanza vibaya.” Ezra alishituka nafsini
mwake, hakutegema Jelini kuzungumza hivyo. Ila mwenyewe aliongea kama kitu cha
kawaida sana, akarudisha macho kwenye menu. “Inamaana ameshaona uzee wangu
na yeye!” Ezra hakuamini. Akapoa kabisa mpaka kuhisi kutetemeka.
“Huyu Jeremy
ananinyima raha bwana! Nakuwa nawaza chakumpelekea mpaka mimi mwenyewe sifaidi!
Naomba uniwie radhi. Nimpigie simu, nimuulize anataka kula nini, asinipe mimi
kazi ya kumchagulia.” “Usijali.” Akatoa simu kuzungumza na mwanae.
Akawa akimwangalia
kwa kujiiba akiwa anazungumza na mwanae. Anacheka na mwanae hana mbavu. “Sasa kumbe unajua unachokitaka, kwa nini hukuniambia tokea
mwanzo?!” Akamsikiliza akicheka, mwishoe akamuaga. “Kweli Jeremy maneno
mengi kama mama yake!” Akaongea hivyo akirudisha simu kwenye pochi. Ila
akagundua Ezra amepoa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Sasa mbona umepoa
tena?” “Nilikuwa nikikupa nafasi ya kuzungumza na Jeremy.” “Hanaga kumaliza
kama mama yake. Mama kila siku anatuambia. Tuna maneno mengi. Tukianza kuongea,
hatumalizi.” “Yeye si mzungumzaji?” “Mama Jema!?” Akamuuliza kwa mshangao na
kuanza kucheka. “Kwa nini?” “Labda awe na lililomfurahisha. Hanaga muda wa
maneno mengi, kwanza hanaga mazoea ya kijinga. Ila mimi na Jeremy tunamjualia.
Tunaweza kumkalisha kwa muda atusikilize. Lakini si hivihivi. Na nahisi Jema
yupo kama mama au yeye kazidi. Jema mkimya na mpole sana.” Wakaletewa chakula,
wakaanza kula.
Ya Ezra.
“Zamu yangu ya
maswali.” Ezra akamtizama. “Wewe mchumba wako ilikuaje?” Ezra akaanza kucheka
tena. “Kwa nini udhani kulikuwa na mchumba?” “Hivyo ulivyo na unazungukwa na
warembo hivyo! Kweli usiwe na mchumba?” “Hukukosea. Ila aliniacha alipokwenda
masomoni.” Jelini akatoa macho. Ezra akacheka na kunyamaza.
“Tuanze taratibu.
Kwamba mlikosana au mlikuwa na matatizo kwenye mahusiano yenu?” “Hapana Jelini!
Nilimvisha mpaka pete ya uchumba nikawa nataka kumuoa kabisa ndipo ikaja hiyo
nafasi ya kwenda masomoni. Kwa mujibu wake, hiyo nafasi ya masomo ni kitu
alikuwa akikisubiria kwa muda mrefu sana, na ndio yalikuwa maombi yake. Akasema
lazima aende. Junior alipomwambia tufunge ndoa kwanza, ndipo aende, akasema
akirudi likizo ndipo tutafunga ndoa. Basi, vikao vikaanza. Huku tukiwasiliana.
Ilipobakia kama miezi miwili arudi nchini, ndio tufunge hiyo ndoa, mawasiliano
yakaanza kusuasua.”
“Kumpata ni kwa
shida, na kila ukimpata analalamika yupo busy. Zilipobakia siku kama 20,
akamtafuta Junior, akamwambia yeye haoni maisha yake tena huku nchini, ameamua
kuishi huko.” “Sasa na wewe?” “Naona na wewe ulikuwa kama Junior. Alimuuliza
hivyohivyo. Akasema…” “Umfuate?” Jelini akamalizia kwa swali. Ezra akacheka kwa
masikitiko.
“Bora ingekua hivyo.
Alimwambia aniambie niendelee tu na maisha yangu. Yeye ameanza kule upya.”
“Jamani!” “Na hakutania. Nafikiri ndani ya mwaka uleule tulisikia ameolewa,
tena ana mtoto.” Jelini akabaki ametoa macho.
“Yeap. Hiyo ndio
historia yangu. Sio ndefu sana, ila imekamilika. Mbaya zaidi familia yake ipo
palepale kanisani. Dada zake utakuwa unawajua na kaka yake. Na wenyewe
walikwenda harusini. Mmoja nafikiri kama hakumsaidia yeye, basi alimfuata huko,
anaishi naye.” “Ezra!” “Kabisa. Na ukumbuke na vikao vya harusi hapa nchini,
pale kanisani, vilikuwa vikiendelea, na ndugu zake walikuwa bega kwa bega na
mimi kuhakikisha nafanikisha kila jambo. Lakini waliponigeuka, ikawa ni
kama mimi tena natakiwa nisiwe mbinafsi. Nielewe nafasi aliyokuwa
nayo huko. Inawezekana halikuwa andiko langu, na mengine mengi. Ikabidi
niwe mpole. Nikubali yaishe. Kuwe na amani.”
“Maana habari zake za
harusi, mtoto wa kizungu aliyezaa na…” “Kwamba ameolewa na mzungu?” “Sasa
unafikiri wazazi wake wangetoa baraka zao hivihivi? Wanasema huyo mzungu ndiye
atamsaidia kuishi kule kwa utulivu. Maana na yeye atakuwa raia huko, sababu
huku harudi na mengine mengi. Sasa kashazaa na mtoto wa kizungu tena, mimi nina
faida gani? Basi habari zangu zikafukiwa uvunguni, zikawa sasa ni zake na za
mume mpya wakizungu.”
“Jamani Ezra!”
“Ilikuwa mbaya Jelini! Nilikaribia kuchanganyikiwa, nisiamini. Nilikuwa
nikijiuliza nilipokosea mpaka kuachwa vile! Halafu sasa hakuna pakuhuzunikia,
ikawa ni kama yeye amebahatika. Nikabaki kujiuliza, kwamba kweli hawa
watu wamesahau kabisa kama mimi ndiye niliyekuwa mchumba halali! Lakini
ikawa ni kama machozi ya samaki.”
“Nikabaki kusimama na
baba yake Junior, ambaye ndiye mchungaji pale, Junior na mama yake. Ukweli
hawakuacha kunifariji. Alipoona akili haijatulia, alinitoa kabisa hapa mjini.
Akanichukua mimi na Junior, tukaenda Milimani kuhubiri injili.” Jelini
akaanza kucheka. “Na nikikwambia Milimani, ujue ni kwenye kusubiri giza
liingie ndio mkaoge mtoni. Hamna umeme. Ila hali ya hewa nzuri.” “Na yule
mchungaji hashindwi.” Akasadiki.
“Siku saba!
Tunahubiri injili. Mpaka anatuambia tunarudi mjini, moyo umepoa, zimebaki stori
za Milimani tu. Ukikaa na sisi watatu, utakuja kugundua ni neno tumelizoea
sana. Tunamtania mchungaji. Mtu akisumbua tu, tunamwambia ampeleke Milimani.”
Jelini alicheka sana. “Hata Junior naye yupo hivyohivyo. Ukishamsikia tu
akikwambia huyu ni wa Milimani, ujue huyo mtu hayupo sawa.” “Pole Ezra jamani! Pole
sana.” “Asante. Ila ikawa kama imenitia hofu ya mahusiano kabisa. Sikurudia
kutongoza tena.” “Hapo nakuamini kabisa.” Ezra alicheka sana.
“Kwa utongozaji ule!
Unaonekana uliondoka kwenye game muda mrefu sana. Lakini usijali.
Taratibu.” “Sijaharibu?” “Matendo yako yamenivutia Ezra, kuliko maneno.”
“Kweli?” “Kabisa. Mimi ni muwazi, nisingekudanganya. Kwanza wala usingekuwa
hapa na mimi. Si unakumbuka hata nilikukatalia chakula mara ya kwanza?” “Usinikumbushe.”
Jelini akaanza kucheka.
“Mimi sihongeki kwa
urahisi Ezra. Kwanza sitaki. Ila wewe mtu mzuri. Mkweli. Unasimamia
maneno yako. Hayo mashairi ya kudanganywa kupendwa, nayasikia mpaka masikio
yamezoea.”
“Kwa hiyo bora nisijayasema tu?” “Usijitoe
kirahisi hivyo Ezra, bwana! Lazima wewe uniambie. Wewe nataka kukusikia.
Na sio useme mara moja halafu eti tukiwa wazee husemi tena!” Ezra akazidi
kucheka kwa furaha. “Mpaka uzeeni?” “Yaani uwe unarudia rudia tu.”
“Hutachoka?” “Usijali, nitakuwa sikumbuki. Kila ukisema nitakua naona mpya.”
Ezra akacheka akimtizama. Asiamini kama anazungumza na Jelini kirahisi hivyo.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Walikula mpaka
wakamaliza. Akaletewa chakula cha Jeremy, akamchukulia na mama yake. “Naomba
nilipie Ezra. Tafadhali. Jeremy kuna chakula chake anapendaga. Ni garama. Na
nimemchukulia mama nyama choma. Bei ni kubwa. Nimejiandaa.” “Usijali. Na mimi
nilijiandaa.” “Lakini kwa ajili yetu tu. Sio ukoo mzima! Siku nyingine
utalipia, ila leo acha iwe sisi tu.” “Jelini, acha nilipie. Kwanza nimefurahi
jinsi unavyojali watu wa nyumbani kwako. Sijali kulipia.” “Najua. Ila hawa ni
jukumu langu. Tafadhali acha nilipie.” “Na mimi ni jukumu langu.” “Hata
kutongoza hujatongoza bado! Inakuaje jukumu lako?” Ezra akaanza kucheka.
“Nimesema najiandaa.
Nitakutongoza Jelini. Mbona pressure?” “Sasa unajuaje kama nitakukubali?” Ezra
akamtizama kwa makini kama anayejaribu kumsoma. “Maana naweza kukataa.”
“Jelini! Wewe unayeona mpaka uzee wetu pamoja, kweli unikatae.” Jelini
alicheka sana, kama mazuri.
“Basi mama pia amenigundua. Nimekua na furaha. Moyo umekua mwepesi.
Anasema mpaka usoni naonyesha.” “Sasa ukamwambia sababu ni nini?” “Nikamwambia
nahisi Ezra atakua ananipenda.” Ezra alicheka mpaka akapaliwa. Jinsi
alivyoongea, eti kama kwa soni vile. Kisha akajificha.
“Jelini! Sijakupatia mwenzako.” “Mimi nataka ibakie
hivyohivyo.” “Hutaki mwenzio?” “Sitaki.” Akakataa na kupandisha mabega kabisa.
“Unataka ujaliwe wewe tu?” “Peke yangu.” “Na sitakutafutia mwenzio. Kama
utabaki kwangu. Ukaamua kuwa na mimi. Ukaniahidi katika yote, hutabadilika.
Maisha yako ni yangu. Utasimama na mimi katika yote, ujue utabaki peke yako.
Nitakupenda Jelini, mpaka na wewe utajua nakupenda. Nitatunza furaha yako kwa
kadiri ya uwezo wangu. Na kama mimi nikishindwa, basi nitamuomba Mungu wangu.
Sitakuacha ulale na uchungu moyoni. Utakalobeba litakuwa langu. Na
sitabadilika.” Mpaka machozi yakamtoka Jelini.
“Ila hizo ahadi zangu, ni pale utakapoamua kubaki na mimi.
Usilie sasa!” “Mimi nimefurahi.” “Kweli?” “Sana.” “Kwa hiyo?” “Acha
kwanza nifurahie bwana Ezra! Mbona kama unakua mtu wa wivu?” Haya
anaongea na machozi kibao. Ezra hana mbavu. “Mwenzio
napendwa!” “Na kweli unapendwa na Ezra.” Akajifuta machozi akatulia.
Akamuona ananyanyuka anamfuata muhudumu. Akamuona
anazungumza naye kitu. Akamkabidhi kikaratasi. Akaenda kulipia na kurudi na
bili yao akamkabidhi Ezra. “Mbona kidogo hivi?” “Nimelipa chakula cha mama na
Jeremy.” “Jelini! Kwa nini umefanya hivyo?” “Ili wapate hamu ya wao siku
nyingine ukiwakaribisha, waje. Wasidandie bahati yangu.” Japokuwa alizungumza
kwa utani, lakini Ezra alipoa kabisa. Akamuita muhudumu kwa ishara, akafika
hapo, akamlipa. Jelini akamuona jinsi alivyopoa.
Usiku wa Ahadi.
“Asante kwa chakula Ezra. Nimefurahia.” Jelini akavunja
ukimya mara walipoingia garini, kabla Ezra hajatoa gari. “Karibu. Na mimi
nimefurahia.” Akalazimishia tabasamu. “Ila sasahivi huna furaha. Naomba
nisamehe na unielewe Ezra. Nimeingiwa hofu, kila kitu nachukua tahadhari.” Ezra
akamwangalia.
“Usiondoke kwanza. Acha nikwambie. Katika siku chache
nilizokuwa na Colins, ni kama alimzoea sana Jeremy. Jeremy akampenda sana.
Hakuacha kumuulizia akitaka kuja kumuona tena. Nilikuwa sijui jinsi ya
kumwambia maana ni kama alimuamini sana Colins. Sasa kitendo cha wazazi wake
kuja kunivamia nyumbani na maneno mabaya sana kwangu na mama, mbele ya kila mtu
mpaka Jeremy, kilimchanganya sana, mpaka ikabidi mama azungumze na mimi na
kuniapisha.” “Juu ya nini?”
Jelini akafikiria akaona amwambie tu. “Jeremy nilimzaa
nikiwa mdogo sana. Mama akamchukua kama mwanae. Anamlinda kwa kila namna na
Jeremy ni mtoto mzuri sana. Mama anasema hataki nimchanganye. Aje aige tabia
za wanaume wa ajabu ajabu. Sasa alichoniapisha ni kwamba, nilichokifanya
kwa Colins, nisiwahi kurudia tena.” Ezra akatulia kama kujaribu kuelewa.
“Colins alikuwa akija nyumbani anaingia mpaka chumbani
kwangu na kwa Jeremy. Nilimuweka kwa haraka karibu ya Jeremy. Wakazoeana sana,
kisha akaondoka na asigeuke nyuma ila maneno mabaya ya wazazi wake. Kwa hiyo amenionya
nisilete tena mwanaume mle ndani, isipokuwa nina uhakika naye kwa
asilimia 100. Na afike pale akiwa na wazazi wake, ameenda kutoa mahari, na
sivinginevyo.” Ezra akaelewa ndio maana hakukaribishwa hata ndani.
“Na ukiangalia ni kweli Ezra. Mama anahaki. Pale ni kwake.
Ametutunza mimi na mtoto wangu mpaka sasa. Hata mara moja, hajawahi leta
mwanaume pale ndani. Tafadhali nipe muda nirekebishe makosa. Nimeishi maisha ya
ajabuajabu sana. Yaani sasahivi ndio kama nahisi nitatulia, kwa sababu
nimekuchunguza, nimeamini wewe umetulia Ezra. Ndio maana napata moyo, najiambia
pengine safari yangu ya kuhangaika imefika mwisho. Kwa maneno tu, hakuna
atakayeniamini. Maana nishawaahidi sana, na kurudia makosa sana. Naomba muda
uje uwaaminishe. Tafadhali nivumilie.”
“Nimeelewa Jelini.
Ila kama kweli umeamini mimi si myumbishaji. Nitabaki na wewe, kwa nini
usinipe nafasi tukaanza wote?” “Sikujua kama unataka Ezra.” “Kweli nisitake
nafasi ya kuweka msingi pamoja na wewe! Hudhani kwamba itatusaidia? Na
si lazima ikawa matangazo. Ni maisha yetu mimi na wewe. Hakuna sababu ya
wengine kujua. Tufanye kimyakimya ila kwa makini tukijua watu wanatuangalia, na
Mungu pia anatuangalia.” “Sawa Ezra. Basi katika hilo naomba msaada wako. Na
univumilie. Taratibu. Mabadiliko yote hayatakuja kwa haraka.” “Naelewa.”
Akamuona akicheka.
“Nini?” “Kwahiyo tunaanza msingi wetu?” “Mimi sina
kipingamizi Ezra. Wewe unanipenda na unatabia nzuri. Hata mama anakusifia.
Tuanze taratibu, tuone tutakapofikia.” Hilo likamfurahisha sana Ezra.
Kakubaliwa na Jelini! Hakuamini. Akajinyanyua kutoka kitini, akambusu shavuni.
Bwana Jelini alifurahi! Akabaki amejishika shavu akicheka. Ndipo akaondoka
gari.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ukawa usiku wa namna yake. Kwa mara ingine tena, Jelini
akajikuta anatoa kiapo kwa mwanaume mwingine tena. Tena kwa furaha tu
wala asijilazimishe. Alikusudia kweli kutafuta ndoa, kwa udi na uvumba
bila kuchoka. Palishindikana kwa Colins. Akasubiria kwa muda wote huo akiamini kama kawaida yake, atarudi
tu. Lakini ikawa kimya, asijue jinsi Colins anavyomtafuta.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Usiku huo alipofika tu nyumbani, akampigia Jema akiwa na
mama yake. Wanazungumza na Jema kwenye simu, wao wapo chumbani kwa Jelini.
Akawasimulia jinsi hilo juma lilivyokwenda mpaka usiku huo wa ahadi.
“Ila wanamsifia kweli pale kanisani.” Mama Jema akaongeza. “Na mimi hizo sifa ndio zikanifanya nimpe nafasi. Lakini
mpaka sasa sijajuta. Aisee Ezra anajali jamani! Anaweza nifuata, eti kunipa tu
maji ya kunywa! Matunda na maji ya kunywa ni kila siku mchana ananiletea popote
nilipo. Anakula na mimi chakula cha usiku. Ananijali sana.” “Na Jelini unavyopenda kupendwa wewe!” Jema akaongeza.
“Nakubembelezwa.” Akaongeza yeye mwenyewe mama
yake akimtizama yu. Wakazungumza mengi watatu hao wakicheka, ila Jema akagundua
Colins hajatajwa usiku huo hata mara moja. Na yeye akaona amuache tu.
Jumamosi Ya Mazito&Maamuzi Magumu.
Mida ya saa nne asubuhi, siku hiyo ya jumamosi Ezra
akamfuata tena kazini. Alipomuona kwa mbali, akatoka kwa haraka akiwa amejawa
furaha. Ezra akamshika mkono na kumvutia upande aliokuwa ameegesha gari lake.
Kisha wakasimama nje ya gari. “Nimekuwahi kabla hujaanza kuwa busy.” Jelini
akafurahi. “Ulilala vizuri?” “Sana. Na wewe?” “Na mimi, nikijua nina Jelini
kwenye maisha yangu.” “Sasa sio uwe busy, uanze kusahau hilo.” Ezra akaanza
kucheka. “Si mpaka uzeeni?” “Mimi naona nibadilishe. Iwe mpaka kifo.”
Ezra hana mbavu, furaha imemjaa.
“Nimekuletea hii cooler. Ndogo tu. Inaweza kukaa hata
kwenye gari yako bila kukubugudhi. Yakutunzia maji ya kunywa.” Jelini akaanza
kucheka, huku akichungulia ndani ya gari, akiitizama. “Asante kujali Ezra. Ila
mimi sijatoka, nitatoka baadaye. Nitakunun…” “Sio mashindano Jelini!
Nimefikiria jinsi unavyozunguka mchana kutwa, joto, jua kali, na hapa dukani
mnatumia feni tu. Unatokwa jasho, unahitaji maji ya kunywa wakati wote.” “Wewe
unanifikiria sana Ezra! Ila ujue na mimi nakufikiria bwana. Nitakununulia zawadi.”
Ezra hana mbavu.
“Tena nitakunununulia zawadi nzuri sana mpaka ushangae.”
“Kuna zawadi moja kubwa ninayotaka kutoka kwako Jelini. Unataka kuijua?” Jelini
akatingisha kichwa akicheka kwa deko, huku akimtizama.
Akamshika mikono yake yote miwili kwa upendo sana
akimtizama. Kisha akamwambia. “Niahidi hutaniacha mimi. Niahidi utabaki
kuwa wangu tu. Na nakuahidi hutajuta Jelini. Nikubali tuwe wote, tufunge huu
ukurasa wa kutafuta, tuanze kujenga kwetu. Nilikwambia hutajuta?” Jelini
akacheka. “Mpaka sasa sijajuta.” “Basi haitakuwa ni mwanzo tu. Kama ulivyoona
uzee wetu, ujue tutabakia hivihivi tukipendana.” “Na mimi nataka tubakie
hivihivi, tena wawili tu. Hatutaki
mtu mwingine.” Ezra akacheka akimwangalia kama anayesubiria jambo, lakini
Jelini akawa amemalizia hapo.
Ezra akagundua hajawahi kumwambia kama na yeye anampenda.
Akajisikia kuumia kidogo, ila akaona amchukulie taratibu. Pengine bado hofu ya
kukataliwa baada ya kumwambia Colins anapenda,
ilikuwepo. Ila akashangaa anamwachia mikono. Hapohapo nje. Hadharani.
Akamkumbatia. Kisha akatulia kabisa mikononi kwa Ezra. Ilibidi amshike tu vizuri,
maana alikuwa ameegemea kwenye gari. Akatulia hapo kwa muda kama ambaye hana
majukumu. Ezra naye akamuacha tu, ila akiwa amemshikilia vizuri, kisha
akamuachia yeye mwenyewe kama aliyetosheka.
“Nimefurahi Ezra. Asante kwa muda wako na zawadi.” “Karibu.
Usiku baada ya kikao, nitakupigia. Kama utakuwa na nafasi, nitakuja tule wote.”
“Si ulisema kikao cha mwisho kinaweza kikachukua muda mrefu sana?” “Ndiyo na
hapana. Maana leo tunahitimisha kila kitu. Kinaweza kuvuta. Lakini pia ukumbuke
harusi si yetu. Na sisi ni waalikwa. Ila tunajipanga kinyumbani tu. Ila tutawasiliana.”
Akambusu juu ya kipanda uso, Ezra akaondoka Jelini akimwangalia anavyoondoa
gari. Kisha wakapungiana mkono, ndipo akageuka kurudi dukani kwake.
Mama ni mama tu.
Wakati amegeuka
akirudi ndani, uso kwa uso na mama Colins kama aliyekuwa akimsubiria hapo
pembeni ya duka, muda wote. Akashituka sana. Akabaki ameduaa akishindwa
kusogea. “Colins anaumwa.” Jelini akakunja uso wa mshangao. “Kama ungependa
kumuona, yupo nyumbani.” “Unataka nije halafu jambo litokee, mnisingizie mie mchawi
ndio nimemloga! Akuu! Mimi sitaki. Nyinyi mna imani za ajabu!
Mimi sitaki ukaribu na nyinyi.” Jelini akaingia ndani.
Mama Colins akaondoka
akiwa amekata tamaa kabisa. Mbali na maneno aliyoyasema, amekutana na kijana
Ezra anayeonekana mambo safi, halafu anamjali Jelini, wakati kijana wake hata hatizamiki!
Akaondoka hapo njia nzima akilia kwa uchungu na majuto. Akafika kwake, akakuta
Colins amelala. Ndipo akaweza kueleza yote aliyoyakuta hapo, akiwepo kijana
Ezra, jinsi alivyowaona wawili hao. Na majibu ya Jelini. Connie na baba yake
wakabaki kimya kila mtu akiwaza lake.
Mchana wa Siku Ya Jumamosi.
Alipokuwa kwenye
mizunguko yake. Alikuwa ameenda kupeleka vitambaa na maua ya urembo kwenye
ukumbi, vikiwa vimekodishwa, na yeye amevurugikiwa kabisa, akaona ampigie simu
Jema. Alishatoka kazini tokea saa sita mchana. Akawa nyumbani tu na JJ, James
kama kawaida yake akili ilishahamia kwenye biashara. Akamuelezea akiwa njiani
kurudi dukani kwake.
Jema akasikiliza
mpaka mwisho. “Wewe unataka kufanya nini?” Akamuuliza
akitaka kujua moyo wake ulipo, katikati ya wanaume hao wawili. “Nimeshindwa hata kuweka kitu mdomoni tokea yule mama
aniambie Colins ni mgonjwa! Nashindwa hata kufikiria Jema! Na leo ni siku yangu
nakua busy sana. Lakini nimekua kama nimepoteza dira kabisa! Ni Colins!
Huwezi jua yule mzee alikuwa akija pale kumbe kutaka kuniambia lakini anashindwa!
Pengine hali yake sio nzuri! Nina wasiwasi mpaka tumbo la hedhi limenianza.”
“Pole. Sasa
unakumbuka nilikwambia lazima uanze kuomba?” “Hata sijui naanzia wapi, Jema!”
“Mwambie Mungu upo njia panda. Kwanza ukiwa ndio umekubali tu kuwa na Ezra.
Yaani ndio kwa mara yako ya kwanza umemfungulia mlango mtu mwingine, halafu ndio
unapata taarifa za Colins aliyekuwa amepotea karibu mwaka sasa.” “Hivyo tu!?” Jelini hakuamini kama ni rahisi hivyo.
“Wala
huhitaji maneno mengi kwa Mungu anayeijua mpaka kesho yako. Anachotaka
usemezane naye tu, ili apate njia ya kuzungumza na wewe. Hata akikujibu,
akileta majibu yake, uwe kwenye mkao wakupokea. Anza. Na uombee hata hiyo hali
unayojisikia. Weka gari pembeni, pata muda wa kuomba. Mwenzio huwa naomba mpaka
chooni. Pata muda sasahivi, omba kabla hujatingwa na kitu kingine, ukashindwa kuomba.” Jelini akajicheka
ila kweli akaegesha gari, akaanza kuomba. Kuomba kwenyewe akawa anaongea kama
alivyoambiwa na dada yake mpaka akamaliza ndipo akaondoa gari kurudi sasa
dukani kwake.
Watafutaji Wasio Choka.
Connie akafikiria,
akashindwa kuvumilia. Akatoka moja kwa moja mpaka anakofanyia biashara zake
Jelini. Jelini hakutegemea, akabaki akimwangalia hapo dirishani. “Naomba
tuzungumze Jelini. Tafadhali, na samahani kwa kukupotezea muda.” Alivyopoa huyo
Connie, huwezi kumjibu vibaya, ni mpaka uwe mwehu.
Jelini akatoka.
Wakasogea pembeni. “Najua wazazi wamekuudhi. Na mimi mama amenisimulia. Kwa
hakika binafsi nimeumia, pole sana.” Jelini akabaki kimya akimtizama tu.
“Unapofuatwa na baba, daktari, akisema Colins anaumwa, ujue ni kweli anaumwa.”
“Mimi hajaniambia kama Colins anaumwa! Amekuwa akija hapa, hasemi kitu, kisha
anaondoka bila hata salamu!” Connie akawa kama hajaelewa ila akaona aendelee.
“Anyways, pengine itakuwa anasumbuliwa
na dhamira. Lakini Jelini, Coly nimgonjwa. Na kama ulishawahi kumpenda
kama yeye anavyokupenda…” “Colins hanipendi mimi. Amemchagua Love, ndiye
anayeishi naye. Labda kama na hilo hujaambiwa.”
“Mimi sijui
kilichoendelea hapo kati. Maana kulikuwa na mvutano mkali, mimi nikaamua kuacha
kabisa kwenda nyumbani, nitulize akili kwenye shule. Mara ya mwisho kuwasiliana
na Colins, ni aliponipigia simu na kuniambia haya maneno.” Akamtolea simu yake
na kumpa asome. Baada ya kusoma maneno yake mwenyewe aliyokuwa amemwambia
Colins, kama ahadi au kiapo, akamuona amepoa kabisa. Akamrudishia simu.
“Sasa hayo maneno
aliyarudia kwangu, kisha akaenda kuyaandika yeye mwenyewe, tena kwa mkono wake.
Kama utagundua hapo hiyo ni picha. Alipiga picha pale alipokuwa ameandika.
Mbaya zaidi, japokuwa pengine wewe hayo maneno yamepoteza maana kwako, lakini
yamebaki moyoni kwa Colins. Hakika anakutafuta. Mpaka wakati mwingine
inabidi kufungwa kamba asitoke. Maana anatoroka kwenda kukutafuta na yeye nguvu
hana na akili yake ni kama haipo sawa!” Jelini alilia sana.
“Colins unayemfahamu
wewe, si huyu anayekutafuta sasahivi. Ameisha kila kitu mpaka akili, lakini
amebakiwa na hayo maneno yako tu. Anaishi kwa madawa ya usingizi ili
asitoke nje kukutafuta ndio maana umeona mpaka baba ilibidi akutafute.
Aliposhindwa ndio nafikiri mama akaja. Amerudi nyumbani akilia anasema
tumeshachelewa. Wewe umeendelea na maisha yako.”
“Mimi nimekuja tu,
japo wazazi wamekata tamaa. Nakusihi, kama ulimaanisha chochote
ulichomwambia hii siku, basi tafadhali Jelini, hata kama umepata mwanaume
mwingine, nakuomba, nipo chini ya miguu yako, nenda ukamuone Coly.
Pengine itamtuliza, nakumfanya apoe. Sasahivi anafungiwa kama mgonjwa wa
kichaa. Anaishi kwa madawa kitu ambacho akiendelea hivyo kwake si nzuri.
Amedhoofu, hali, anaishi kwa dripu tu! Ana madonda ya miguu, kwa kutembea akikutafuta
wewe. Hataki yaguswe hayo madonda mpaka awe amelala.” Jelini akazidi kulia.
“Hata kama sisi umetukasirikia, basi muhurumie Coly. Ni hilo tu.”
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
MAMBO
YANAENDELEA…
Ezra Naye Akiwa Ndio Amepata Tu Kiapo Cha Jelini Na Asubuhi Hiyo
Kuweka Ombi Maalumu Akitaka Ndio Iwe Zawadi Pekee Kutoka Kwa Jelini Kwenye
Maisha Yake, Na Connie Naye Amekuja Kudai KIAPO Cha Kaka
Yake.
Je, Jelini Atasimamia Wapi?
Kwa Ezra Ambaye Hata Hajabahatika Kuambiwa Neno Nakupenda Au Colins Aliyelowa
Mvua Ya Neno Hilo, Na Ndiye Aliyekuwa Akisubiriwa Na Msamaha Wake Mkononi.
USIPITWE NA MAZITO YA SIKU Hii Ya JUMAMOSI.
Ya Maamuzi Magumu.
0 Comments:
Post a Comment