Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 14 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 14

Akamtumia ujumbe Jema.
‘Sikutegemea kupata wakati mzuri namna hii na Ezra! Baada ya 
muda mrefu wa majonzi na upweke, hatimaye na mimi nimepata kicheko.’ Wakati Jema akisoma huo ujumbe kutoka kwa mdogo wake, na wa Ezra ukaingia. ‘Nina furaha ambayo sijui jinsi ya kuieleza, dada Jema. Nimepata muda mzuri sana na Jelini. Ipo jinsi Mungu amenipa kibali kwake, kwa hakika imekua tofauti kabisa na mwanzo. Tafadhali naomba uzidi kutuombea. Sijawahi penda hivi! Mpaka naogopa kumwambia, nisije kumuogopesha.’ Jema akabaki akiziangalia hizo jumbe asijue amjibu nani kwanza. Maana James ndio alikuwa amerudi, ameingia bafuni kuoga.

Akamjibu kwanza Ezra, ‘Nakuombea na tutazungumza vizuri kesho.’ Kisha kwa Jelini. ‘Ezra ni mtu mzuri sana. Na uzuri, anahofu ya Mungu. Nina uhakika hatakuumiza. Mpe nafasi. Na nakuombea.’ Akatuma huo ujumbe wa pili kwa haraka, akazima kabisa simu na kuiweka pembeni akimsubiria mumewe. Jelini aliposoma ujumbe kutoka kwa dada yake, wakabaki akimtafakari Ezra. Kwa hakika alipata wakati mzuri mpaka akajishangaa. Kwa mara ya kwanza akalala bila hata kumuwaza Colins.

Kesho Yake.

‘Nimeamka salama, na ninafuraha nikitizamia jioni yangu na wewe.’ Jelini alipoamka, akakutana na huo ujumbe. Ulitumwa saa 11 asubuhi. Akaangalia muda, ilikuwa saa 12:30 asubuhi. Akaamua kumjibu, ‘Na mimi nimeamka salama, Ezra. Uwe na siku njema. Kazi njema. Naamini kukuona tena usiku.’ ‘Bila kukosa.’ Jelini akacheka akilamba midomo yake kwa furaha.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika mida ya saa 1:30 usiku, Ezra alikuwa akiegesha gari kazini kwa Jelini. Akamtumia ujumbe. ‘Sina nia ya kukuharakisha, ila nataka kukutaarifu kuwa nimeshafika. Ukimaliza, muda wowote ule njoo garini. Nitakusubiria tu.’ Jelini aliposoma, mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi. Akashindwa kutulia kabisa wakati alikuwa na wateja wengi. Akaaga na kutoka. Ezra hakutegemea alipomuona akija garini, na yeye akatoka kumpokea.

“Vipi!? Naona unawateja wengi bado! Hutakula vizuri.” “Leo naona kumevuta. Mpaka sasahivi bado wanakuja. Nilitaka kukusalimia tu, kisha nirudi.” Ezra akacheka akimwangalia. “Nimefurahi umekuja Ezra.” “Ninafuraha ya kukuona. Umependeza sana.” “Nilikuwa busy sana leo. Nikizunguka mtaani. Nimemaliza mizunguko kwenye mida ya saa nane. Nikarudi nyumbani kuoga na kubadili, kutoa jasho. Ili hata tukikaa wakati wa kula nisikunukishe.” Ezra akacheka.

“Nisingejali. Ila nimefurahi kukuona unafuraha. Basi nenda kaendelee na kazi, ukimaliza tuje tuzungumze vizuri.” “Wewe ulikuwa na siku nzuri leo?” Na Jelini akauliza kuonyesha kujali. “Sana.” Jelini akacheka. “Mbona ‘sana’ yako inanitia wivu?” “Kwa kuwa wewe ndio umeisababisha. Nimefurahi umezungumza na mimi jana pamoja na ujumbe wa asubuhi.” “Kweli Ezra?” “Kabisa. Yaani mpaka Junior amenigundua kwenye simu, na kuniuliza kulikoni. Akaniambia hajanisikia na furaha kama ya leo kwa muda mrefu. Nikamwambia Mungu amenipa kicheko. Sikutegemea kama ungenipokea baada ya kuwa ukinikimbia.” Jelini alicheka sana, ila kwa aibu.

“Nilijua ulikuwa ukinikimbia Jelini.” “Nilikuwa na wakati mbaya! Nilihitaji muda wa kupokea taarifa fulani hivi, ambazo nilikuwa nikizikataa kwa muda mrefu. Sikutaka kujichanganya. Nilitaka muda wa peke yangu ili nikifikia maamuzi fulani, niwe nina uhakika nayo.” “Sasa umeshafikia hayo maamuzi?” Akatulia kidogo akifikiria, akamuona amepoa.

“Tuingie kwenye gari nikwambie kitu.” “Na kazini?” “Watakuwa sawa. Usiwe na wasiwasi.” “Sitaki waharibu, unichukie!” “Hapana. Ni watu wazuri, sema nakuwepo tu kama kuvutia wateja. Wengi wanapenda wakifika, wanikute mimi mwenyewe.” Wakaingia garini.

Jelini Ajifunua Kwa Ezra.

Alipokaa kitini akaanza. “Acha nikwambie ukweli.” Akaanza Jelini. “Kwa mara ya kwanza kwenye maisha yangu, nafikiri nilipenda. Nilishindwa kujizuia wala kujisaidia. Mimi sikuwa mtoto wa nyumbani au kanisani, ila mshinda baa. Nikinywa na washikaji, na klabu kwa sana tu.” Ezra akacheka akimsikiliza.

“Nakwambia ukweli.” “Nakusikiliza.” “Lakini katika hangaika yangu yote, sikuwahi penda kama nilivyompenda Colins, lakini tayari alikuwa kwenye mahusiano na msichana mwingine ambaye ni kama mchana na usiku na mimi. Na uzuri wao wao, huyo msichana alipendwa sana na wazazi wake Colins.”

“Nilimwambia Colins kuwa nampenda, akanikataa akiniambia yupo kwenye mahusiano na huyo msichana.” Ezra akabaki kimya, asiamini mtu kama Jelini anaweza kweli kutongoza mwanaume!

 “Nikaumia sana, nikaja kupata mtu mwingine, nikaanza naye mahusiano, lakini tukiwa katikati ya hayo mahusiano, Colins akarudi, akanipa sababu za kunikataa kwa wakati ule, nikashindwa kumkubali tena, japo nilikuwa nikimpenda, ila nilishakuwa na mwanaume mwingine, sikutaka kuwa msaliti. Colins hakukata tamaa, akabaki akinisubiria mpaka iliposhindikana kule nilikokuwa.” “Kwa nini kulishindikana huko ulikokuwa?” Akauliza akihofia isijekuwa Jelini alimtafutia huyo jamaa sababu ili arudi kwa Colins. Jelini akamsimulia mkasa wa mzee Kasa kwa kifupi tu. Ezra akashangaa sana.

“Katika kipindi hicho kigumu cha maumivu ya usaliti, ndipo tukaanzana na Colins kwa kuwa alisimama na mimi kunifariji. Lakini Ezra, hakuna tulilowahi panga na Colins, likafanikiwa hata mara moja. Hata kutoka kwenda kula kitu pamoja au kunisindikiza hata hospitalini! Hatukuwahi kufanikiwa. Ilikuwa ni kupanga na kuvunjika na mimi nikiishia kuwa muhanga na yeye kurudi na sababu nzuri tu zenye mashiko. Nilibaki nikisubiri pengine itakuja kuwa bora kwa sababu katikati ya hayo mahusiano ambayo ni kama hatukuwa nayo, lakini kama yapo, yule msichana akarudi kwa kupitia wazazi akitaka warudiane na Collins. Kwa hiyo kukawa na shindikizo la wazazi. Hawanitaki mimi kabisa, wanataka Collins amuoe huyo msichana.”

“Collins nilimpenda sana. Hilo sitakudanganya. Ilikuwa ni ngumu, lakini kwa sababu moyoni nilimpenda sana, nilikuwa na tumaini nikijua siku moja patatulia tu. Vurugu ikaongezeka, maana ndio kipindi hichohicho yule msichana wake akapata taarifa za tabia zangu mbaya au maisha mabaya niliyoishi nyuma na kuwaambia wazazi wa Colins.” “Haiwezekani Jelini!” “Oooh yeah. Ilikuwa mbaya sana. Alinianika kwa kadiri ya uwezo wake mpaka wazazi wenyewe wakakinahiwa.” Akamsimulia mpaka kufuatwa na bibi, babu pamoja na wazazi wake nyumbani, na Colins kuishia kuishi na Love.

“Lakini Ezra, moyo wangu ulishindwa kabisa kumuachilia.” “Kwamba ulikuwa ukisubiri pengine atarudi?!” “Kabisa. Yeye nilishajiandaa na kumsamehe kabisa. Miezi yote hiyo nilikuwa nikimsubiri tu arudi, aniombe msamaha, huku akinipa sababu nzuri, zenye mashiko kama kawaida yake, tuendelee. Ndio maana sikutaka kujichanganya na mtu yeyote yule. Nilijiweka kwenye mkao wa kumpokea. Nikabaki nikisubiri tu kama mjinga vile!” “Hapo nimekuelewa.” “Kweli?” “Kabisa. Wala si ujinga. Najua nguvu ya kupenda kwa dhati na kwa uaminifu. Si ujinga.”

“Basi mimi nilijiona mjinga. Maana kwa Kasa, nilishindwa kabisa kusamehe, ila Collins ambaye ninajua anaishi na huyo mwanamke kama mke wake kabisa, eti nilibaki nikimsubiria.” “Sasa ni nini kimebadilika?” “Nafikiri nimekubaliana na ukweli. Kwamba ameondoka. Amemchagua Love. Na kwa ukimya huu karibia mwaka sasa, inamaana yake yanakwenda sawa. Sina changu tena.” Ezra akawa kama anaswali, lakini hajui aliulizaje.

Wakabaki garini wametulia kimya, kila mmoja akiwaza lake. Akamgeukia Ezra kama aliyekumbuka kitu. “Kwa hiyo sikuwa nikikukimbia wewe kama Ezra, nilikuwa nikijitenga na kila mwanaume. Ili isitokee anarudi akanikuta katikati ya mahusiano yeyote yale. Sijui kama umenielewa?” “Nafikiri nimeelewa.” Akajibu hivyo na kutulia kama ambaye anatafuta jinsi ya kuzungumza jambo lake, ila anakwama.

“Kuna swali nataka kukuuliza. Lakini sijui niliulizaje!” “Juu ya nini?” “Juu yako.” “Wewe uliza tu. Maana mimi nafahamika sana. Hata nikikataa kukwambia ukweli, ukiamua, haitakuchukua hata siku nyingi kupata habari zangu huko mtaani. Najulikana kwa mengi mno. Kwa hiyo kuwa huru tu.” Ezra akamtizama na kusita.

“Naona tule tu.” “Ni nini hicho unachokihofia kuniuliza? Nakuahidi hutaniudhi Ezra. Mwenzio sio mwepesi wa hasira na sioni shida na maisha yangu. Yapo ambayo najua nilikosea, lakini nafikiri ndiyo yamenifanya niwe hivi nilivyo leo, na siwezi kubadili nyuma. Nilishaishi, basi. Atakayeweza kuwa na mimi kwa jumla yangu, sawa. Atakayeshindwa, pia naelewa kabisa. Hainisumbui. Kwa hiyo kuwa tu na amani. Niulize.” Ezra akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha.

“Kwa jinsi ulivyompenda Colins, unafikiri utakuja kumfungulia moyo wako mwanaume mwingine?” Jelini akafikiria na kutulia kabisa. “Naona kweli tule tu.” “Swali limekua gumu?” Ezra akauliza. “Sikujua kama utaniuliza hivyo! Nilifikiri utaniuliza juu ya maisha yangu.” “Hayo ni maisha yako ya baadaye pia, Jelini. Huwezi kukwepa. Nyuma nipo kama wewe tu. Huwezi kubadili. Najua Mungu husamehe na husahau. Wewe ndio upo kuvuna madhara ya makosa uliyokwisha samehewa. Hapo huwezi kuepuka.” Jelini akatulia.

“Asante kwa chakula. Napata harufu nzuri!” Akabadili mazungumzo kabisa. Ezra akajua, ila akawa muugwana. Akatoa vyakula na vinywaji, wakaanza kula kimyakimya.

Shauku Ya Jelini Bado Ipo Japo Mazingira Yote Bado Yanamkatisha Tamaa.

Wakati wakila kimya kimya, mwenyewe akavunja ukimya. “Acha niwe mkweli Ezra. Maadamu tunazungumza, acha tu nikwambie. Nina shauku ambayo siwezi nikaipuuza. Na sitaki kukata tamaa.” “Shauku gani?” Ezra akauliza taratibu tu kama kawaida yake, akila. “Kuja kupata mtu wangu. Mtu ambaye atakuwa radhi kunilipia garama kama Colins alivyofanya kwa huyo mwanamke wake. Anipende mimi kama Jelini niliyebeba historia mbaya. Lakini bado anibebe. Awe wangu tu. Anioe. Tuzae watoto. Najiona naweza kuwa mke wa mtu atakayenipenda kama vile Jema. Sitaki kukata tamaa, japo ni ngumu. Nimezungukwa na wanaume malaya, hawawezi kuishi na mwanamke mmoja tu. Lakini sitaki kukata tamaa.”

“Na haitakiwi ukate tamaa. Na si wanaume wote ni malaya. Niliomba usituweke kwenye kapu moja. Inawezekana kujizungumzia mwenyewe naweza kusikika najitetea, lakini naishi karibu sana na Junior. Na yeye anakazi nzuri tu, inayompa maisha mazuri. Anazungukwa na warembo wazuri wakila namna. Kazini na kanisani. Lakini wote tumekubali kusubiri mpaka ndoa. Japo Junior anaye mchumba wake, lakini hamgusi mpaka ndoa. Si kwamba hana tamaa za mwili, lakini tumekubali kusubiri, tukimuamini Mungu kwa wake bora.” Ezra akaendelea.

“Ni nini nataka kukwambia, unachotamani si kitu cha ajabu sana. Mungu hana mtu mmoja au mwanaume mmoja tu mwaminifu. Mungu ana watu wengi sana. Hata kama mimi na Junior tukaanguka kesho, hatutafilisi mbingu. Kwa hiyo usikate tamaa. Omba Mungu, subiri, weka malengo yasiyoyumbishwa na matukio, utapata unachokitaka.” Jelini akavuta pumzi kwa nguvu, akiingiza ule ushauri moyoni kwa upya, akaendelea kula.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakala mpaka wakamaliza. “Acha nirudi kazini. Nikamalizie siku, nirudi nyumbani. Nashukuru kwa chakula. Nimefurahia nyama choma.” “Karibu.” Akaitika hivyo na kubaki akimtizama. Jelini akajikusanya, akafungua mlango, na kutoka. Ezra akabaki amekaa kitini. Akamfuata.

“Ipo siku nitakujibu swali lako.” “Nilijua umeamua kulikwepa.” “Hapana Ezra. Ila kwa sasa sina jibu. Sikupanga kumpenda Colins kwa kiasi hiki. Ilitokea tu. Najipa uhuru wa kuja kupenda tena. Sitaki kujifunga au kukata tamaa kama nilivyokwambia. Inawezekana hakuwa andiko langu.” “Anaweza akaja andiko lako na usimpende!” “Mimi si muhuni na wala si muongo, Ezra. Ninaweza nisiwe kama wasichana wa pale kanisani. Ambao hawajapitia maisha kama yangu, lakini linapofika swala la mahusiano ya kimapenzi, hapo nakuwa makini.” Akaendelea taratibu tu Ezra akimtizama kupitia dirisha, akiwa amekaa ndani ya gari yake, yeye amesimama nje.

“Nina msururu wa wanaume wananitongoza kila leo. Hata leo nimepata. Lakini siwezi kuwa karibu na mtu ambaye sijamkubali na najua nia yake ni kunichezea tu. Na kwa jinsi nilivyo, nikishampa mtu nafasi ya kuwa wangu, ujue moyo wangu umempenda. Na nitampenda yeye tu, bila ya kumchanganya na yeyote yule au kuruhusu hisia ambazo hubadilika, kuingilia mahusiano yetu. Nitasimama naye katika kila hali, kwa kuwa atakuwa wangu.” Hapo kidogo Ezra akaridhika.

“Ukiwa kitandani, unataka kulala, nipigie ili nikutakie usiku mwema.” Jelini akaanza kucheka. “Jana nililala vizuri.” “Hata mimi Ezra. Nilifurahia muda na wewe. Unautulivu wa namna yako, hata sauti yako imetulia, ikanifanya nitulie kabisa.” Ezra akaanza kucheka. “Kweli! Unamfanya mtu anatulia kabisa. Hata kama kuna uchungu, mawazo mabaya, mtu akikusikiliza, anatulia.” “Sipigii kila msichana simu usiku, bwana Jelini! Sizungumzi hivi na wasichana wengine! Ni wewe tu.” Jelini akainama tu hapo mbele yake.

“Na ni kwa kuwa nataka wewe utulie, uwe na furaha, ndio maana nakupa muda wangu.” Ezra akaendelea akibembeleza asijue jinsi anavyomfariji Jelini. Akatoa tabasamu akanyanyua uso na kumtizama. Macho yakagongana. “Nashukuru Ezra. Nitakupigia.” Wakaagana, Jelini akarudi kwenye majukumu yake akiwa na hisia tofauti kabisa juu ya Ezra.

Msimamo wa Mama Jema.

Alipofika nyumbani, akamsimulia mama yake yote, asijue na Jema alishamsimulia mama yao juu yake na Ezra. Mama Jema alishampenda Ezra kwa mengi aliyoyasikia kupitia Jema. Jinsi anavyompenda Jelini na kumtaka vile alivyo. Maana Jema alimwambia mama yake, ilimbidi amsimulie Ezra ukweli juu ya Jelini, ili asije mfuata kisha baadaye kukiwa kumenoga, kuja kujua ukweli halafu akamuumiza tena mdogo wake. Jema alimwambia mama yake, alishamueleza kwa kifupi ila ukweli wote juu ya Jelini, na bado Ezra kumuhakikishia Jema, kuwa yeye anajiona ndiye mume wa Jelini. Hilo likamfurahisha sana mama Jema.

 “Sasa hao ndio wanaume. Wanakuacha na kicheko sio unalala na huzuni muda wote! Mipango mingi. Maneno mengi ambayo hayajawahi timia! Hekaheka mchana mpaka usiku! Mwishoe kuja kuitwa wachawi nyumbani kwetu.” Hilo mama Jema alishindwa samehe kabisa. Kuitwa mchawi! Tena nyumbani kwake, mbele ya wanae na mjukuu! Hakutaka hata kuwasikia hao wazazi wa Colins, na Colins mwenyewe. Na James alijua jinsi alivyoumia. Na yeye akaacha kuzungumzia mambo ya Colins kabisa mbele ya familia hiyo, japo alikuwa akimkumbuka sana Colins. Akazungumza kidogo na mama yake, akawahi kitandani akijua Ezra anamsubiria.

Aluta Kontinua.

 Alipojiweka tu kitandani, akampigia. “Nilidhani ungenisahau!” “Sina mtu wakumfikiria sasahivi, mbali na familia yangu, ndio umeongezeka na wewe, Ezra. Siwezi kukusahau.” Ezra alijisikia vizuri sana. “Halafu umenijali. Umeniletea chakula kizuri, tumekaa wote. Nimefurahi, asante.” “Nimefurahi kama na wewe umefurahia. Ila unajijua kama wewe ni rahisi sana kukufurahisha, Jelini?” Jelini akacheka.

“Ni tofauti na muonekano wako kabisa. Mtu akikuangalia kwa haraka, anaweza dhania matunzo yako ni ya kufilisi benki.” Jelini alicheka sana. “Kabisa. Lakini unatukuza vikitu vidogo sana, unavyopewa.” “Basi mimi siangalii thamani ya kitu, ila kunifikiria na kunitendea. Kama kukumbuka swala la mziki niliopenda. Kisha kuacha shuguli zako zote na kunitafutia hizo nyimbo na kuniletea! Kwangu si jambo dogo Ezra. Au kuacha shuguli zako na kuja kula na mimi, tena garini tu! Ukiwa umetoka kazini, pengine ungependa kupumzika. Kwangu si jambo dogo hata kidogo. Ndio maana nimeona ile asante ya pale haitoshi, nikuandikie ujumbe kabisa.” Ezra akacheka akimfikiria. Maana baada ya kushuka garini kwake baada ya kula pamoja, akiwa nyumbani kwake, ujumbe wa shukurani ukaingia kwenye simu yake, kutoka kwa Jelini.

“Pumzika Ezra. Tutazungumza kesho.” “Naomba na kesho tufanye kama leo. Tule pamoja.” “Utanichoka bure! Wewe kula tu, Ezra. Mwenzio naagiza chakula palepale, nakula.” “Nahisi mimi ndio nahitaji muda na wewe, Jelini. Nafurahia tukiwa wote.” “Kweli Ezra?” “Sina sababu ya kukufuata kwa kiasi hicho kama si kutaka kwangu. Ningekuwa sehemu nyingine au hata kwa Junior, mpaka muda wangu wa kulala ufike.” “Lakini kweli!” Ikawa kama imemu hit Jelini akilini. Akakubaliana naye.

 “Ndio ujue nataka kuwa karibu na wewe.” Jelini akatulia akifikiria. “Mbona kimya?” “Nina maswali mengi juu yako, Ezra.” “Kama hayana haraka, nakuahidi kukujibu ijumaa. Naamini tutapata wakati mzuri. Katikati ya juma nataka tukikutana, iwe kupumzika baada ya majukumu yetu ya siku, basi. Labda iwe unataka majibu kwa haraka.” “Nitasubiri.” “Basi lala, nitakuona kesho.” “Nashukuru Ezra. Usiku mwema.” “Na wewe.” Wakacheka na kukata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Hiyo kukutana kwa chakula cha usiku ikaendelea kama jumbe za asubuhi za kutakiana siku njema, kisha usiku wakati wa kulala pia walikuwa kwenye simu pamoja. Ezra alijitahidi kuleta vyakula tofauti tofauti, ilimradi tu kumfurahisha Jelini. Wanaingia kwenye gari, wanakula wakielezana siku zao zilivyokuwa. Vituko vya siku hiyo. Basi watacheka, kisha Jelini kurudi kuendelea na kazi, na yeye Ezra kuondoka akienda kusubiria simu ya usiku mwema kutoka kwa Jelini.

Na akaongeza safari ya mchana pia. Yaani muda wa chakula cha mchana kazini, yeye hali, anawahi kumpelekea Jelini popote alipo muda huo, maji na matunda. Ilimradi kuonyesha kumjali huyo Jelini.

Siku Moja Kabla ya Kutoka kwao.

Siku ya alhamisi wakati wakilala, kabla hawajaagana, Jelini akaita. “Ezra?” “Nipo.” “Naomba nikuombe na uniahidi utafanya.” “Sawa. Niambie.” “Ikitokea dharula yeyote ile kesho. Ukashindwa kuja au itakayosababishia tusitoke, tafadhali kabla ya saa 11 jioni, nijulishe.” Ezra akawa haamini kama bado Jelini haamini jinsi anavyojisikia ni kama ameokota alumasi kuwa naye.

“Dharula itakayonipelekea nikose kuwa na wewe kesho, ni kifo.” “Acha kusema hivyo, bwana! Mambo yanatokea.” “Kesho usiku nitakua na wewe, Jelini. Kama si kwenye chakula cha usiku, basi tutakuwa pamoja huko kutakaponilazimu tusiende kwa chakula cha usiku. Nikimaanisha itabadilika mazingira tu. Ila tutakuwa pamoja.” Jelini akacheka akifikiria.

“Ikitokea unapata mgonjwa wa gafla?” Jelini akauliza akitaka uhakika. “Nitakuja kukuchukua twende wote kwa huyo mgonjwa, kisha tuendelee na yetu.” Jelini akafurahi huyo, akabaki akicheka. “Kesho usiku ni usiku wetu. Tuombe Mungu iwe sehemu ya chakula, vinginevyo tutakuwa wote popote itakapotulazimu.” “Asante Ezra. Nashukuru.” “Na mimi nakushukuru kukubali kuwa na mimi. Pumzika, tutazungumza kesho.” Ezra akaomba kwa kifupi. Akamuombea Jelini usingizi mzuri, ulinzi wa kiMungu juu yake, biashara zake. Akaomba kila anachofanya afanikiwe na kuombea siku yao ya kesho. Wakaagana Jelini asiamini kilichomtokea. “Hapa kama ni karata, basi Jelini safari hii umelamba dume.” Akajiambia akicheka mwenyewe hapo kitandani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa Jelini&Ezra Vinazidi Kunoga.

 Ni Nini Kitaendelea KWAO! Je, wao watafanikiwa kutoka.

USIPITWE.

 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment