Mtaka Cha Mvunguni, Shariti Uiname. Siku ya jumapili baada ya ibada, na kupata muda na familia wa chakula cha pamoja, wachaga hao akili zikahamia kwenye kusaka pesa, kasoro Jema na watoto ndio wakarudi nyumbani. Sasa Jelini akiwa kwenye duka lake akashitukia mama Colins amesimama dukani. Akamsalimia, akaitika na kuanza kuagiza vitu. Jelini akamuacha Fiona ndio amuhudumie, yeye kimya anaendelea na mambo mengine. Mara Ezra akafika hapo na yeye.
Akampungia mkono.
Jelini alifurahi! Kwa hakika hakutegemea kuja kumuona tena hapo dukani kwao kwa
jinsi ilivyoishia vibaya mara ya mwisho alipomletea chakula. Maana hata
kanisani siku hiyo hawakusalimiana. Akajikuta akicheka na kutoka kabisa getini
kumfuata nje ambako na mama Colins alikuwepo upande huohuo ila wakajivuta
karibu na alikoegesha gari yake.
“Kwamba
umeshabadilisha nguo kabisa!” “Nilisharudi nyumbani, nikapumzika, ndio nikaona
nikuletee hii CD. Nakumbuka jana pale ukumbini, ulisema ulipenda sana nyimbo
zake.” Jelini akashangaa sana. “Ezra! Kwamba ulikuwa ukinisikiliza na
ukakumbuka!?” “Kabisa. Siwezi kukupuuza.” Ikamgusa Jelini, hakutegemea. Akamwangalia
kwa mshangao usoni lakini uliojaa shukurani. “Nashukuru kujali. Naanza kuziweka
hapahapa dukani. Iwe ikiimba kila wakati.” Akabaki akiangalia ile CD, akamuona
anacheka.
“Jelini bwana! Sasa
unacheka nini?” “Nimefurahi, asante.” “Karibu. Na leo utakaa kazini mpaka usiku
sana?” “Hapana. Jumapili huwa tunafunga mapema. Kwa nini?” Akamuona anasita. “Niambie
tu Ezra!” Akamsihi kwa kubembeleza kidogo. “Ungependa baada ya kazi twende tukapate
icecream?” Mpaka akasisimkwa. Akajikuta akijibu. “Ningependa Ezra.
Nimekua busy, sijapata muda wa kukaa chini hata kufanya mambo madogo kama hayo.
Nashukuru pia kwa ofa.” Ezra alifurahi, asiamini.
Ukweli Jelini
alionekana kufunguka kwake tofauti na mwanzoni. Akajipongeza kwa juhudi zake za
kuinama, afikie cha uvunguni. “Usijali. Jiandae kupumzika na kupata icecream
nzuri.” “Nashukuru.” Hakutaka kumpotezea muda zaidi, akaaga na kuingia kwenye
usafiri wake wa haja! Gari nzuri sana ya kisasa, ikatangaza ipo neema kwa Ezra.
Akaondoka akamuacha Jelini hapo nje baada ya kumpungia mkono. Wote wakionekana
na furaha.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakati anarudi ndani,
mama Colins naye akaondoka bila ya kusema kitu ila kwa hakika alifanya manunuzi
ya haja. Alitoka hapo na mifuko kibao! Jelini akajiuliza bila yakupata jibu. “Hawa
watu vipi!?” Akazidi kuwaza ila safari hii hakumwambia mama yake. Ile huzuni
ya kuona wamemkataa asiwe na kijana wao, siku hiyo ikapoozwa na furaha ya kutolewa
na Ezra.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kadiri masaa
yalipokuwa yakisogea, wasiwasi ukaanza kumwingia na kumuibia furaha yote ya
kutoka. Alitamani arudi nyumbani aoge, ajitengeneza kama alivyokuwa akijiandaa
alipokuwa akiambiwa na Colins watatoka. Lakini! “Historia isije jirudia.”
Akawaza na kupoa kabisa. Furaha ikamuisha kabisa, akabaki na wasiwasi wa Ezra
asije aka mcollins. Akanyongea kabisa.
Ilipofika majira ya
saa moja, akimalizia mahesabu, wanakaribia kufunga na Fiona alishaondoka tangia
saa 11 jioni, alibakiwa na Chalii tu, akamuona Ezra. Hakutegemea. “Umekuja?!”
Ezra akawa kama hajaelewa lile swali la mshangao. “Nimewahi sana nini?” “Hapana.
Sikutegemea kama ungerudi! Nisubiri, nakuja sasahivi.” Kwa hakika akawa
amemchanganya Ezra mpaka kutoelewa kama ni amewahi au amekuja siku isiyo
yenyewe. Ila kule kuambia anatoka baada ya muda mfupi, kukamtuliza.
Baada ya muda Jelini
akatoka na pochi yake, akamkuta akimsubiria nje ya gari. “Sehemu niliyofikiria
twende, sio mbali na hapa. Ni sawa tukiondoka na gari yangu, kisha
nitakurudisha hapa uchukue gari yako ndipo urudi nyumbani?” “Sawa.”
Akamfungulia mlango, akaingia, akamfungia mlango na kurudi upande wa dereva.
Alionekana alijiandaa
na hiyo safari. Maana alibadili nguo kabisa. Akavaa mavazi ya kutoka, ila casual
simple. Alionekana ni kijana anayejijali. Aliweza kupata harufu nzuri,
marashi ya kiume. Jelini akajishuku. “Na mimi nilitamani kurudi nyumbani
angalau nioge na kubadili, lakini sikuwa na uhakika kama ungerudi.” Ezra akawa
bado hajampata vizuri.
“Kwamba ningevunja
miahadi yetu, au sijaelewa vizuri?” “Mipango hubadilika!” Ezra akaguna na
kumtizama maana hata ile zungumza yake ilibeba simanzi kidogo. “Labda isiwe na mimi,
Jelini. Siwezi kupanga kitu na wewe nikagairisha tu. Na huwa sipangi kitu
ambacho sina uhakika kama nitafanya.” Jelini akatulia tu.
“Au nimekupa dalili
zozote za kukuonyesha mimi ni mbambaishaji?” “Hapana Ezra. Imekua kinyume na
ndio maana umeona nimekubali kutoka na wewe. Nafikiria ni kujishuku tu.
Nilihofia unaweza pata dharula ukashindwa kurudi.” “Nafikiri kama kungetokea
dharula ingine, basi wewe ndio ungekuwa dharula yangu ya kwanza.”
Jelini akacheka kwa kuridhika, na kunyamaza. Ila hilo lilibeba maana
kubwa sana masikioni kwa Jelini, yeye asijue tu. Akalitunza moyoni na kuzidi
kuvutiwa naye. Ezra akawa muungwana, mara yake ya kwanza kutoka naye, hakutaka
kumkera na maswali mengi.
“Sasa wewe siku yako
ya kupumzika ni lini kama unafanya kazi mpaka jumapili?” Jelini akacheka akijifikiria.
“Maisha yangu yote kutoa miezi inayokaribia na nane sasa, yalikuwa ni kupumzika
tu. Kula, kunywa na kulala tu. Haya maisha ya kazi hivi, nimeanza hata mwaka
haujaisha.” Ezra akacheka na kumtizama huku akiendesha. “Usiniambie ndio
ulikuwa ukila bata kwa kiasi hicho!” “Sio kitu kizuri bwana! Nimebadilika. Kwa
hiyo sasahivi nimejikuta sina chakufanya. Nimebadili ratiba. Badala ya starehe,
nafanya kazi. Ili nisijikute nimekaa tu, nikaanza kufikiria ujinga.” “Safi
sana.” Akampongeza akicheka kama aliye na maswali mengi, ila kukusudia muda uje
ujibu.
“Na wewe?” “Kwa sasa
mimi ni mtu wa mshahara. Jumatatu mpaka ijumaa. Asubuhi mpaka jioni, basi.
Baada ya mida hiyo nipo tu huru kufanya yangu, ndio utanikuta kanisani. Sina
ratiba ngumu.” Jelini akatulia mpaka wakafika hiyo sehemu. Kweli hapakuwa
mbali.
Wakaingia ndani
kuagiza icecream wanazotaka, wakapewa na kurudi kutafuta sehemu ya
kukaa. Jelini akajisikia vizuri. Ezra
akamuona akivuta pumzi mara kadhaa kama ambaye anajaribu kutulia, na kweli
akatulia. Akawa akimwangalia kwa makini tu, huku akiendelea kula.
Akawa kama amekumbuka
kitu. “Ezra!” Akamuita na kumuangalia, asijue huyo Ezra macho yako kwake muda
wote. “Asante kurudi kunichukua, na kunitoa.” “Itabidi unisaidie Jelini. Nahisi
kuna kitu hapo sielewi!” “Nilitamani kutoka kwa muda mrefu. Nikafanya majaribio
mara kadhaa, ikashindikana. Tena nikiwa nimeshajiandaa kabisa. Nafikiri
ikanitia hofu ya kutoka hivi na mtu mwingine, ikawa ni mpaka iwe na mama pamoja
na Jema. Hata leo nilitaka nirudi nyumbani nikajiandae, lakini nikaogopa nisije
nikajitia tena nuksi. Nikajiandaa halafu ukapatwa dharula, ukashindwa
kutoka.” Ezra akakunja sura kidogo.
“Kwamba nikwambie tutoke,
kisha nisitokee?!” Jelini akatulia kama anayefikiria. Kisha akaona
afupishe. “Nilitaka kukwambia nimefurahi umekua mwaminifu, umesimamia hii
miahadi, na tumetoka. Asante.” Ezra akawa haamini kusikia hivyo kutoka kwa mrembo
Jelini. Ila akaanza kumsoma tofauti na muonekano wake. ‘Amejawa shukurani.’
Hilo ndilo likabaki kwa Ezra.
“Nafikiri mimi ndio
natakiwa kukushukuru zaidi Jelini. Umekubali kutoka tena baada ya siku ndefu ya
kazi. Mwenzio nilirudi nyumbani, nikapata mpaka muda wa mapumziko. Kwa hiyo
nimefurahi umekubali kutoka. Naona mimi ndio natakiwa kukushukuru.” Jelini akacheka
taratibu na kuendelea kula hiyo icecream.
“Nikuulize kitu
Jelini?” Akamwangalia. “Huwa unapenda kutoka na kwenda kula wapi?” Jelini
akacheka akifikiria. “Au nikurahisishie. Huwa unapenda vyakula gani?” “Nafikiri
si vyakula pekee, ila ule wakati wakutoka na kufurahia kwa pamoja ndio huwa
napenda zaidi. Nimekuona wewe sio mkorofi, mtu mzuri, ndio maana nimekubali
kutoka na wewe. Mimi huwa sizoei mtu hovyo.” Ezra akacheka kama anayejaribu
kuelewa.
“Hunifahamu kabisa
Jelini! Na ulikataa ukaribu na mimi. Umejuaje kama si mkorofi na ni mtu
mzuri? Maana nyakati nyingi tumekuwa tukikutana sehemu zinazolazimisha kuwa na
haiba nzuri. Nikimaanisha ni rahisi nikaigiza.” Jelini akamkumbuka maneno ya
shemeji yake yaliyofanana na hayo. Akacheka.
“Ni kweli Jelini.”
“Unafikiri nakataa basi. Ila katika vitu nimeamini hapa duniani, ni tabia huwa haijifichi. Popote
anakofahamika mtu. Utakapomuulizia huyo mtu, utatambulishwa kwake kwa tabia
zake. Na ikitokea kama ni mbaya. Au uliishi hilo eneo ukiwa na tabia hizo
mbaya, kisha mtu akaenda kukuulizia hapo, atatambulishwa Jelini mwenye zile
sifa. Utasikia, ‘unamzungumzia Jelini yule,…’ hapo zinatajwa zile sifa zako
zote mbaya. Ila kwako imekua tofauti Ezra. Watu wanakusifia kuwa ni muungwana
na unajua kujishusha.” Ezra akacheka akifikiria.
“Nimeambiwa pia huwa
hupendi kumuudhi mtu.” “Jelini!” “Wewe umeniambia nijichanganye pale
kanisani. Biashara matangazo. Sasa?” Ezra akacheka sana. “Watu wanaongea.” “Ni
kweli.” “Sasa unatakiwa kushukuru. Upoje Ezra?” “Si kwa kiburi, lakini
sikutegemea! Najua nabii hana heshima nyumbani kwao. Na mimi pale
kanisani ni kama nyumbani. Sikutegemea kusikia mtu akinisema vizuri!” “Na hilo
ndilo limenipelekea kukuamini. Nilijua si taarifa za uongo. Kwa sababu
zingekuwa mbaya, wangesema tu. Hawakuwa na sababu ya kukusema vizuri kama ni
mbaya.” Ezra akacheka na kutulia.
Kisha akamchokoza.
“Sasa kwa sababu umeshasikia mimi ni mtoto mzuri, kwa hiyo hata nikikuomba
tutoke tena kwa chakula cha usiku si utakubali?” Jelini alicheka sana.
Hakutegemea. “Ezra!” “Nitafanyaje na mimi nishasifiwa? Au nimewahi sana?”
“Ulitaka tutoke lini na twende wapi?” “Hii nitataka uchague wewe, na nataka
upate muda wa kujiandaa kabisa, ukijua wewe utakuwa dharula ya kwanza kwangu.
Nilazima nitakuja kukuchukua. Kwa hiyo upendeze kwa kadiri ya upendavyo,
tutoke.” Jelini akajikuta akifurahia.
“Kweli Ezra?” “Sina
sababu ya kukudanganya. Na mimi napenda muda na wewe.” Hivyo alivyozungumza
vizuri, Jelini akamtizama na kuangalia chini, akabaki akifikiria. Ezra akabaki
na maswali. Jelini aliyemfuata mwanzo, alikuwa mgumu sana kwake. Lakini Jelini huyu
anaonyesha ni kama ni bahati kuwa naye! Hilo likamshangaza kidogo na kubaki
akimtafakari akimwangalia vile alivyoinamia icecream yake.
Akajikuta amejisahau.
Akimwangalia kiumbe cha ajabu mbele yake. Kwa hakika moyo wake ulifurahia
kupokea macho yanachochukua. Akavuta pumzi kwa nguvu akimtizama. Yaani pale
amekaa tu mbele yake, alivutia. Ezra alitamani azungumze kitu, akazuia maneno
yake asije haribu.
Ila akamuita
taratibu. “Jelini!” “Abee!” Akamtizama kike haswa, kiasi chakumlainisha Ezra vilivyo.
“Tunakwenda wapi kwa chakula cha pamoja?” “Ni sawa nikifikiria kisha
nikujulishe kabla ya siku yenyewe?” “Ambayo ni lini?” “Najua mpo mwishoni
kwenye maandalizi ya harusi. Sitaki kukuingilia.” “Tafadhali niingilie tu.”
“Ezra!” “Mimi nakupa ruksa. Panga, kisha nijulishe. Kama itashindikana,
nitakwambia, tubadili muda pamoja. Ila tafadhali hii harusi isitufanye
tushindwe kutoka. Kwanza harusi si yetu, ni ya upande wa bwana harusi. Sisi ni
kama tulimaliza yetu siku ya jumamosi. Kwa hiyo muda nilio nao, unaweza
kuupangia utakavyo.” Jelini akamtizama vile alivyokuwa akizungumza naye kwa
upendo! Akajisikia kutulia kabisa.
“Ulifikiria lini?” Akamuuliza
kama kumrahisishia. “Ijumaa kwangu sio siku ngumu kama jumamosi.” “Muda gani
mzuri?” Ezra akauliza bila ya kulazia damu. “Nilikuwa nikifikiria
kuanzia saa moja usiku. Lakini na wewe pendekeza muda.” “Ijumaa, saa moja
usiku.” Ndio akawa na yeye amependekeza hivyo. Jelini hakuamini. Akabaki
akimtizama.
“Ujiandae, nitakuja
kukuchukua popote utakapotaka.” “Ila tafadhali sana Ezra. Ikitokea unapatwa na dharula,
nijulishe kabla ya huo muda. Ikiwa mapema zaidi nitashukuru ili nisi…” “Jelini,
naitizamia hiyo ijumaa kwa hamu sana. Hakuna jinsi nikagairi. Labda uzima
wangu.” Jelini akatulia.
“Sawa?” “Acha muda
uje ujibu Ezra. Ahadi za maneno naona moyo umeingiwa hofu, ngumu kuamini mpaka
vitendo. Ila jua na mimi naitizamia sana hiyo siku. Na ujue nitapendeza.”
Ezra akacheka. “Zaidi ya hivyo!?” “Acha masihara Ezra. Mwenzio napenda
kupendeza. Nivae vizuri, nijitengeneza ndio naona raha.” “Ndio maana sijawahi
kukuona hovyo hata mara moja!” “Nawekeza kwenye muonekano wangu, na sina uvivu.
Hivi leo ni kwakuwa sikuwa na uhakika tu. Ila ingekuwa ni wakati ule,
ningesharudi nyumbani, nikaoga na kujitengeneza kwa ajili ya kuja tu kula icecream.
Nilimiss kutoka!” Hapo akaongea kinyonge kidogo.
“Basi itabidi tufanye
juhudi za makusudi tuwe tunatoka mara kwa mara.” Jelini akacheka na kutulia.
“Mbona hujajibu?” “Nimekwambia nimeingiwa hofu na ahadi, Ezra. Acha tufanye
moja baada ya jingine.” “Nini kilikuogopesha?” “Nitakuja kukwambia wakati
mwingine kama tutafanikiwa. Kwa sasa naomba tufurahie hii icecream tu.”
Ezra akawa muungwana, akatulia.
Hawakuwa wamezoeana
sana, na hawakutaka kuvuka mipaka. Kila mmoja akawa anajiwinda na neno lake.
Ila utulivu wa aina yake. Baadaye wakaanza kuzungumzia mambo ya pale kanisani.
Watu wanao wafahamu. Kidogo wakapata kitu cha kuzungumza mpaka wakamaliza.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakati wapo njiani
akimrudisha kwenye gari yake, Ezra akaanza. “Nikiomba namba ya simu kwa
mawasiliano, nitaharibu?” “Hapana Ezra. Ni sawa.” Hapohapo akamtolea simu yake
na kumkabidhi. Jelini akajua ndio anatakiwa kuandika namba. Akaweka namba yake
na kuandika, ‘Jelini’. Kisha akamrudishia.
Akashukuru na kuweka pembeni, akiendelea kuendesha mpaka akamfikisha nje ya
duka lake.
“Nashukuru Ezra.
Nimepata wakati mzuri. Nimefurahi.” Ezra akacheka akimtizama. Jelini akainama
akiwa bado amekaa kitini. “Naona unashukuru kwa kitu kidogo sana Jelini! Mbona
ulishashukuru. Au umesahau?” “Nakumbuka.” “Na unakumbuka kukwambia mimi ndio
nimefurahia zaidi?” Akatingisha kichwa kukubali na tabasamu. Ezra alijaa vizuri
ndani ya hilo gari, kiume. Akavutia. Kadiri Jelini alivyojishusha, ikamuongezea
ujasiri yeye kama mtoto wa kiume, maana Jelini anatisha. Ni wa viwango,
inahitaji moyo kumtongoza. Ila usiku huo baada ya kuwa naye, ikamfanya Ezra
amfikirie tofauti.
“Kwa hakika
nimefurahia muda wetu, na ninatizamia siku yetu ya ijumaa. Na mimi ujue
nitapendeza.” Jelini akaanza kucheka. “Sitaki kukuangusha.” “Huwezi. Wewe
wakati wote ni msafi, Ezra. Sijawahi kukuona ukijikosea.” Ezra akacheka sana.
“Kweli. Unajijulia. Halafu mtulivu mpaka usoni. Unazungumza taratibu, huna
haraka. Pale kanisani wanakuigilizia unavyozungumza.” Ezra alicheka sana,
asiamini.
“Haiwezekani Jelini!
Nani huyo?” “Wewe usiulize sana. Ila ujue watu wanakuangalia sana. Na
wanakusifia.” “Basi itabidi niongeze nidhamu.” Wakazungumza kidogo, Jelini
akashuka asiamini baada ya muda mrefu sana wa upweke, usiku huo hatimaye
amepata muda mzuri hivyo na Ezra.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakati anakaribia kulala, ujumbe ukaingia. ‘Uwe na usiku mwema. Ezra.’ Akacheka akirudia kusoma,
kisha akajibu. ‘Asante. Na wewe ulale unono.’ Akatuma
huo ujumbe na kuongeza. ‘Na asante kwa namba pia.
Niliogopa kujichukulia.’ ‘Karibu. Lakini nijisingejali kama ungechukua.
Ingenifurahisha zaidi kuona na wewe unataka mawasiliano na mimi, kuliko
kulazimishia.’ Ezra akamjibu kwa haraka tu. ‘Tafadhali
usione kama unalazimishia.’ ‘Sitaki kuharibu kama mwanzo.’ Akamchokonoa
kidogo kujua anaposimama.
‘Sikuwa
nikikufahamu Ezra. Niliogopa nisiharakishe nikajiumiza tena. Nimezungukwa na
mianzo mizuri, lakini hakunaga muendelezo. Nabakia kuumia na kusubiria bila
kikomo. Moyo wangu umechoka, nafikiri nikaongeza kujiwinda.’ ‘Pole. Lakini mimi
nina mwanzo na mwisho wangu hautakuwa wa maumivu.’ Jelini akasoma, na
kushindwa kujibu. Akajihisi machozi kumtoka. Akamkumbuka Colins.
‘Nakuahidi
Jelini.’
Ezra akaongeza. ‘Tafadhali acha muda ujibu Ezra.
Tutembee hatua kwa hatua. Ahadi zinaniogopesha kwa sasa.’ ‘Sawa.’
Akajibu hivyo na kuongeza. ‘We are equal, but not
same. Nikimaanisha wanaume wote tunaweza kufanana, lakini haina maana
tunatenda sawasawa. Tunatofautiana. Tafadhali usituweke wote kwenye kikapu
kimoja. Utanipunja nafasi ya kutenda yale ninayotamani kwako, nikihofia
utanifananisha na waliotangulia. Au kuhofia hutaniamini. Nataka ujue,
nina maanisha kila neno nitakalokwambia. Na nakuahidi, nitasimamia
maneno yangu kwako, kwa garama yeyote ile.’ Jelini aliposoma, akajibu
kwa haraka.
‘Na hiyo
nimesikia ni moja ya sifa zako. Kwamba ukiahidi jambo, unatenda hata kama
itakugarimu wewe. Na hiyo nimesikia akisema mama mchungaji wakati wakikusema
kwenye kamati ya kitchen party. Walikuwa wakisema yule msimamizi wa ule
ukumbi ni mkorofi sana. Mmoja wao akawa na wasiwasi unaweza ukakimbia jukumu la
kusimamia ule ukumbi siku ya kitchen Party ukijitoa kwa ukorofi wake na
kusema kwanza ni ya wanawake. Ndio mama mchungaji akasema, hata iweje, maadamu
uliahidi kufanya, eti utafanya kwa garama yeyote ile mpaka ikamilike.
Akasema anakufahamu upo hivyo tokea kijana mdogo sana na mpaka sasa katika hilo
hujabadilika. Akawa anawaambia katika hilo lisiwasumbue kabisa, wakuachie tu.’ Hilo likamshangaza
sana Ezra, hakutegemea.
‘Waw!
Ametukuza mimi na Junior yule kijana wake mkubwa.’ ‘Alisema yeye ni kama mama
yako wa pili. Ndio maana nimepata ujasiri kwako Ezra. Isingekuwa hivyo,
ingekuwa ngumu.’ ‘Nashukuru kwa kuchukua hiyo hatua ya kwanza, naomba nikuombe
hatua ya pili.’ ‘Ipi?’
Jelini akauliza.
‘Ni sawa
nikipiga?’
Jelini akajawa furaha, mpaka akajishangaa. ‘Ni sawa
tu.’ Alipotuma tu huo ujumbe, Ezra akapiga. “Nashukuru
kwa ruhusa ya kupiga. Sikujua masharti ya namba.” “Muda na wakati wowote ule.
Nisipojibu ujue nina majukumu tu, ila nitarudisha simu yako.” “Kama ndio hivyo,
nashukuru.” Wakatulia kidogo. Kisha akaendelea.
“Nilitaka
kuomba hatua ya pili.” Jelini
akacheka taratibu. “Naruhusiwa?” “Nakusikiliza.” “Basi
ndio hicho ninachotaka kukuomba. Hatua ya pili, ni unisikie. Mimi kama
Ezra, nisikie ninachokwambia mimi. Sio kile kilichozoeleka kusikika
kwenye masikio yako. Inaweza ikawa ngumu, lakini tafadhali naomba na mimi unipe
nafasi ya kunisikia.” Ikamgusa Jelini. “Nitajitahidi
Ezra. Na wewe univumilie. Inaweza isiwe rahisi, au kwa haraka, lakini nakuahidi
nitajitahidi.” “Nashukuru.” Wakatulia kama wanaoona uzito kuagana.
“Jelini?” Akavunja ukimya. “Nipo.” “Leo ni jumapili. Inamaana kuja kuonana tena ni mpaka
ijumaa?” Ikawa kama anayelalamikia muda. Mbali. “Nilifikiria
ndivyo tulivyokubaliana.” Akajibu Jelini kwa kubembeleza kama na yeye
ameshapatwa hamu naye. “Naruhusiwa hata kupita kazini
kukuona? Nakuahidi sitakuchukulia muda mrefu sana. Ni salamu tu. Au nitakuwa
nikikubugudhi?” “Hapana Ezra. Ningependa kukuona. Tuwasiliane tu. Ili usije
kuja pale nikawa nipo sehemu nyingine. Maana nakuwa nikizunguka sehemu zingine
pia. Sikai tu pale.” “Uzuri nimepata baraka zako juu ya mawasiliano, basi
tutakuwa tukiwasiliana ili tuwe tunapata muda wetu.” Jelini
akacheka baada ya kusikia hivyo.
“Angalau
niwe najua siku yako iliendaje. Si kwa simu. Nikuone kabisa. Maana kwa simu
unaweza ukaniambia tu, upo sawa. Kumbe siku imekua na changamoto, ilikunyima
raha.” “Si nitakusimulia kwa simu tu! Usihangaike.” Akajibu kwa deko. Ila
asiamini. Maisha yalishamfanya ajione si kitu, hapo anaona bahati ya mtende. “Hapana. Simu itanipunja. Tukiwa pamoja hata kama kwa muda
mfupi tu, ni tofauti na simu. Acha simu iwe ikilazimu. Au nazidisha? Ninawahi
sana?” “Mimi nataka uzidishe.” Ezra alicheka sana, asiamini. “Jelini!” “Wewe zidisha tu. Ndio nitafurahi.” Ezra
akaamini maneno ya Jema.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Maana ukimya wa Ezra,
kumbe alikuwa akizungumza na Jema. Alimtafuta na kuzungumza naye kwa mapana juu
ya Jelini. Ezra alimwambia jinsi alivyompenda Jelini. Na akamwambia anajiona
yeye ndio mume bora kwake, wengine watamsumbua tu. Jema alicheka sana.
Kwa kuwa alishampenda
Ezra, akamuibia siri nyingi sana juu ya Jelini. Akamwambia jinsi anavyopenda kupendwa,
kubembelezwa na kufuatilizwa yeye tu. Hapo Ezra anamfahamu Colins
vizuri tu. Hata mahusiano ya Colins na James, Jema alishamwambia. Na Jema ndiye
aliyemwambia amchukulie taratibu sana mpaka amfungulie yeye mwenyewe mlango.
Ila akamwambia akishafungua tu mlango mmoja, aingie kwa nguvu zote bila ya
kuzembea. Full swing!
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Acha
nikuache upumzike, Ezra. Najua kesho kazini.” “Basi chakula cha usiku,
nitaleta, tuje tule wote kwenye gari ndipo urudi kazini.” Jelini akabaki kama
na kigugumizi. “Muda gani huwa unakula, nije tule wote.
Nitaleta mimi. Usihangaike.” “Si nitakuwa nikikusumbua sana!” “Kumbuka mwenzio
ni mwajiriwa. Nikimaliza kumpa mwajiri muda wake, kesho sina kipindi kanisani,
nakuwa sina lakufanya. Sasa kwa kuwa wewe upo na majukumu mpaka usiku mwingi,
naomba nikupunguzie la chakula. Akili ifikirie tu kazi. Niambie muda unaotaka kula,
nije tule wote.” “Asante kujali.” Ikamgusa Jelini, akajikuta akicheka.
“Eti
nimefurahi!” “Kweli Jelini?” “Sana. Nashukuru kujali. Wewe ukipatwa njaa, njoo
uje tule. Mimi sina muda maalumu.” “Muda gani unakuwa na wateja wengi sana?”
“Kuanzia saa 11 jioni mpaka saa 1 usiku. Hapo panakuwa pamejaa sana pale
dukani.” “Kumbe bora nimeuliza! Basi muda wetu wa chakula utakuwa saa mbili
usiku. Au tutakuwa tunachelewa sana kula?” “Nimefurahi! Sasahivi siwezi
kufikiria tena. Wewe njoo tu.” Ezra akacheka. “Nitakuona kesho
Jelini. Ulale vizuri, na uamke na furaha hiyohiyo.” “Na wewe Ezra. Bye.”
Ndipo wakafanikiwa kukata simu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ukweli Ezra Ameingia Full Swing! Mzima Mzima Bila Kulazia
Damu.
Nini Kitaendelea Kati Ya Jelini & Ezra, Wanaoanzisha Jipya Huku
Colins Akimsaka?
Usipitwe Na Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment