Wakati huo ukweli
ukiendelea kwenda ndipo na masikio yakazidi kusikia habari za vijana hao
wawili. Ezra na Junior ambaye ni mtoto wa mchungaji wa hapo kanisani. Vijana
waliojituma hapo kanisani bila kuchoka. Akiwa ndugu mtazamaji tu, mwenda
kanisani siku za jumapili tu, akagundua ni kweli hao vijana wapo hapo na
mabinti wanawahangaikia. Ikawa popote alipo hapo kanisani, hata akiwa chooni
tu, basi atasikia wasichana wa hapo wakimsema Ezra kwa kuvutiwa naye.
Hata akiwa amesimama nje
ya kanisa wakisubiriana au Jema akisalimia kina mama wa hapo kanisani, basi
masikio yalisikia habari za Ezra hata kwa kina mama watu wazima wakimsifia
amefanya hiki au kile, ilimradi akasikilizishwa. Au wakitumana kwake
kuwa wakitaka jambo liende bila maswali na lisiharibike, basi iwe Ezra au
Junior. Akaanza kumfikiria Ezra aliyekwisha mkataa na kumkwepa.
Ila akagundua warembo
wanamsema zaidi yeye, sababu ni kama Junior alikuwa na mchumba anayejulikana
mpaka kwa wazazi. Kwa hiyo akagundua anayewindwa zaidi na yupo ndotoni mwa
warembo wa hapo, ni Ezra. Halafu sasa, kanisa lenyewe lilikuwa na
warembo wanao jielewa, si wachovu au useme wamekosa soko. Kwa hiyo
wanapomzungumzia mwanaume mmoja kwa kurudia rudia, lazima uweke umakini.
Kadiri siku
zilivyozidi kwenda na majuma kukatika, upweke umeongezeka, akaanza sasa
kama kijiwivu kwa Ezra huku akimnung’unikia nafsi mwake, hana wakumwambia. “Kwa
hiyo alikuwa akinijaribisha tu!” Akajilalamisha kadiri siku zilivyozidi
kwenda na Ezra kujifanya kana kwamba hawaoni kabisa. Hakukosea hata
kuwasogelea.
Akabaki akitamani hata wapishane hapo kanisani ili amsalimie,
akumbuke na yeye bado yupo, lakini ikawa kama aliyejiapia, hatakosea kukutana
nao hata kwenye kikapu cha kutoa sadaka. Hapakuhitaji maswali, hata wao wakaamini
Ezra ameweka juhudi za makusudi kuwakwepa. Akiwaona mahali, basi
hatapita hapo kabisa. Na hakurudi tena sehemu anayofanyia kazi Jelini.
Naye Jelini ikawa
kama amepata mkosi, hapakutokea tena mwanaume wa kumtongoza kwa
mahusiano ya maana. Si wa wazee kama kina Kasa wala vijana aina ya Ezra. Akapoa,
na kuanza kujidharau maana waliobaki ni wale vijana waliokuwa wakivutiwa tu na
umbile lake, wanataka tu kumtoa nguo, waone na kuonja vya ndani. Akapoa. Akijiona
ashazeeka, si binti mdogo tena. Akakumbuka sababu za kukataliwa kwa kina
Colins. Akaumia. Akabaki kujiambia, “Kwanza nishazeeka, nina mtoto. Vijana kama
kina Ezra wanataka vibinti vidogo.” Akajikatia tamaa. Akaamua kutuliza akili
kwenye biashara zake na mama yake.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ikawa mchungaji
anaozesha binti yake. Mdogo wake Junior waliyefuatana naye. Likawa jambo la wengi
pale kanisani na watu kulibebea umaana. Maandalizi yakifahari yalishakuwa
yakiendelea. Maana kanisa lenyewe kwenye ibada ya asubuhi ni ya wale waliosoma,
halafu waswahili wanaoishi Bongo, lakini lugha yao na familia ni ya umombo.
Basi hao walikuwa na ibada yao maalumu. Saa tatu asubuhi, mpaka saa nne na
nusu. Hiyo iliendeshwa kwa wakati bila kupitisha hata dakika. Mchungaji
aliwatengezezea muda wao na watoto wao. Wakitoka hao mida hiyo ndio wanakuja
wenzetu na sisi wakina mama Jema.
Wao ibada yao ya
kiswahili. Napo walitunziwa muda. Ila si kama hawa wa asubuhi. Na hawa wa ibada
ya kwanza, wao ndio wale mchungaji akisema kuna mchango, wanataka kujua
kiwango. Kikishatajwa, basi hiyo hela inakusanywa bila kutafutana. Kila mtu
anatamka kiwango chake, ifikapo mwisho wa juma pesa hiyo inakua ilishafika
kwenye akaunti za kanisa bila kigugumizi.
Sasa iliposikika
harusi ya binti wa mchungaji, tena binti wa pekee, kila mtu alijitolea bila
shida kufanikisha shuguli nzima. Na Jelini akapata tenda ya kukodisha kiti
kikubwa cha kukalia maharusi pamoja na vitambaa. Ikawa anatakiwa nusu ya hiyo
seti nzima kupeleka ukumbini siku ya kupamba kitchen party. Halafu
kwenye sendoff akawa amekodishwa seti nzima ili sasa, wakae maharusi na
wasimamizi wao pia. Jelini mpenda vizuri, alinunua hiyo seti kwa pesa nyingi
sana, halafu nzuri mno. Akiiweka na rembo zake hapo jukwaani, hata kabla ya
maua, panapendeza. Wenye uwezo huwa hukodisha vitu vyake.
Jumamosi.
Siku hiyo ilikuwa
siku ya kitchen party. Ilikuwa ikifuatiwa na sendoff. Mida
aliyokubaliana na mpambaji kufikisha vitambaa, hilo kochi na marembo yake hiyo sehemu
ya kukalia, ukafika. Jelini akafika hapo ukumbini na kijana wake mmoja.
Wakaanza kushusha vitu taratibu. Maana vingine vikishafika kwenye jukwaa ndipo
unajengea sehemu ya kicho kiti ambacho kipo kama kochi hivi. Wakati wamebeba na
huyo kijana, wanaingia ukumbini, akamuona Ezra ndani ya huo ukumbi kama na yeye
anaweka sawa mambo fulani upande wa vinywaji.
Aliwaona wakati
wakiingia, maana aliyekuwa naye, alikwenda walipokuwepo kina Jelini kutoa
maelekezo. Akaelekeza sehemu waliyotaka bibi harusi na mpambe wake wakae.
Jelini akauliza maswali wakati kijana wake akiendelea kuleta baadhi ya vitu vya
kuunganisha kwenye hicho kiti/kochi. Kisha Jelini na yeye akatoka kama
kusaidiana na kijana wake.
Wakati wakiendelea,
kuingia na kutoka wakibebelezea vitu ndani Ezra akawasogelea karibu ya gari
waliyokuja nayo. “Nashawishika kusaidia, lakini nahofia isije ikaleta picha
ingine.” Jelini akamwangalia, moyo ukabadili mapigo yake.
Amemuongelesha! Hakuamini, lakini alikuwa amemuelewa anachomaanisha. “Hamna
shida. Kuwa tu na amani. Hata hivyo tunamalizia.” Japokuwa alitamani aseme ‘ndiyo’
kwa haraka sana, maana alishakua na majuto ya kumkataa kwa haraka wakati ule wa
mwanzoni mwanzoni, akijua Colins atarudi. Lakini akaona amuwekee pozi. Ni
Jelini! Na pia alimuigiliza usemi wake Ezra mwenyewe wa ‘kuwa tu na amani’.
Akacheka taratibu na kuondoka kurudi ndani bila nyongeza. Jelini na kijana wake
wakaendelea kusombelea mpaka wakamaliza.
Ikaanza sasa kazi ya
kutengeneza hiyo sehemu ya kukalia hapo jukwaani. Ukumbi una joto, makubaliano
ya A/C ni kuwashwa muda wa shuguli. Ulikuwa ukumbi mzuri sana, madirisha vioo
tupu sababu ya A/C kitu kilichopelekea joto endapo A/C hiyo haijawashwa. Jelini
mwenyewe alikuwa akitokwa na jasho anajifuta na mtandio. Kazi ikaendelea hapo ukumbini
kila mtu akifanya lake ilimradi kumaliza kwa wakati. Halafu sasa na yeye Jelini
wa mengi, biashara mtaani bado zinamsubiri. Akawa amekazana, awafungie kila
kitu, awapishe wapambaji wamalizie, na yeye ahamie kwenye kusaka pesa
kwengine.
Ezra akawasogelea
tena pale jukwaani. “Mimi nipo upande wa vinywaji. Nagawa maji kwa kila mtu
hapa ukumbini. Kama ukiangalia, utagundua kila mtu anachupa ya maji ya kunywa,
niliyowagawia mimi. Sasa sijui na nyinyi hapa mngependa maji? Sitaki
ilete picha ya hongo.” Jelini akajua bado anamanung’uniko juu yake. Hilo
likamfurahisha kidogo kuwa bado hajamsahau. Maana angemsahau, asingekumbuka
alichomwambia.
Ezra mwenyewe
zungumza yake ya utulivu kweli. Hana papara. Hapo yupo kazini, lakini jinsi
yeye Jelini alivyomuona, alimuona yupo vizuri. Akavutiwa naye. “Tunashukuru
kutukumbuka na sisi. Naona Chalii ndio amelemewa zaidi.” “Bila shaka.”
Akamkabidhi huyo kijana wake maji. “Na wewe?” “Kama yapo mengi na mimi
ningeshukuru kama ningepata.” Akazungumza kwa sauti ya kujishusha, kama aliyejirudi.
Akamkabidhi na kushukuru. Ezra akaondoka bila ya nyongeza. Akayanywa karibu
yote, akaendelea na kazi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Usiku kwenye mida ya
saa tano Jelini akawa amerudi tena hapo ukumbini na gari ya mama yake aina ya
pickup, kuchukua vitu vyake. Akamkuta Ezra na yeye amekaa nje pamoja na watu
wengine kama ambao na wao wanasubiria kuisha kwa hiyo shuguli. Jelini alijua
shuguli ingekuwa inakaribia kuisha. Hakutaka mtu ashike hivyo vitu vyake,
kuhofia kuharibiwa. Kwa hiyo aliwahi kidogo kuhakikisha hachelewi kuhofia asije
kuta amesaidiwa kutolewa hapo alipoviweka.
Akawasogelea pale
walipokuwepo. Kama kawaida yake, hajikosei. Kutoka mida anaweka vile vitu hapo
ukumbini mpaka mida hiyo, alisharudi nyumbani kuoga na ndipo kuendelea na
shuguli nyingine. Kwa hiyo hata hapo alijiwakilisha vizuri kama kawaida yake.
“Nilijua na wewe
ungekuwepo katika wahudhuriaji humo ndani?” Ezra akamdaka kwa hayo maneno. Jelini
alifurahi huyo, akajisogeza karibu. Maana alikuwa hajui asimamie upande upi kwa
hao aliowakuta hapo. “Bado hatujafahamiana hata na mama wa bibi harusi. Bado
sisi ni wageni. Tenda yenyewe imekua kama bahati tu, nilimuomba Jema
akamuonyeshe mama mchungaji picha, na kuomba kama watataka niwakodishe kwa bei
nzuri, ndio naona kamati ikapenda, nikapewa kazi ya hicho kiti na vitambaa.”
“Ila umeshakaa sana pale kanisani Jelini. Inabidi uanze kujichanganya. Wewe
mfanyabiashara bwana. Na biashara matangazo.” Jelini akacheka. “Au kuna watu
maalumu unawalenga?” “Hapana. Hilo lipo kwenye kulifanyia kazi.” Angalau usiku
huo, wakazungumza kidogo.
Ikamtuliza Jelini
kuona sio kwamba amemfungia vioo moja kwa moja. Na akajua wazi kujishusha kwake
mchana, na kupokea maji kwa shukurani ndio kumemfanya azungumze naye tena usiku
huo. Akafurahi na kuomba bahati kama hiyo ije ijurudie tena au hata arudi tena
kazini kwake.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Lakini ikawa kimya. Hakumuona
wala kumsikia tena. Hata siku ya jumapili, hakumuona kwa karibu ila kumuona kwa
mbali akizungumza na kucheka na watu wengine. Akanyongea. “Mimi nilidhani
ndio yameisha, jumapili angenitafuta hata anisalimie tu!” Akajilalamisha
kwa uchungu nafsi mwake. Akasikia kunyongea na upweke kumzidia. Ikawa jumatatu,
ikawa jumanne, kimya.
Jumatano.
Akiwa dukani kwake,
ni kama akamuona baba Colins. Akashituka sana akihisi pengine amemfananisha,
kisha akawa amepotea gafla. “Nilitaka kushangaa! Yule baba awe anatafuta
nini kwangu!” Akawaza akiwa anaangaza macho kuhakiki kama sio yeye. Maana
duka lao lilikuwa limetengwa na vyuma vya urembo lakini kama ulinzi kwamba wezi
washindwe kuwaingilia ndani. Kwa hiyo mteja unaona kila kitu ndani. Ukichagua,
unaonyeshwa au kupewa kwa kupitia dirisha ambalo si dogo sana, lakini si rahisi
mtu kuingia.
Ijumaa.
Ikawa hivyohivyo siku
ya ijumaa. Safari hii akamuona kabisa baba Colins. Ila safari hii ni kama
akasogea kabisa karibu na duka, akasimama kwa muda kama anayejishauri.
Akaangalia simu yake kidogo, Jelini akamuona anaondoka bila salamu. Hilo likamshangaza,
asielewe.
Jumamosi.
Siku ya jumamosi
ambayo alikuwa akiandaa hilo kochi au kiti kikubwa cha maharusi kwenye tafrija
ya sendoff, akiwa anaweka kwenye gari na marembo yake, akamuona tena
baba Colins ameegesha gari yake mbele yake. Akashuka garini kabisa, Jelini
akajidai kama hajamuona. Akaendelea kusombelea vitu akiweka garini. Akasimama
nje ya gari yake kama anayemsubiria kisha akamuona anaondoka tena bila salamu.
Hakumsemesha ila Jelini akaogopa sana.
Akiwa njiani,
akampigia simu mama yake. Akamuelezea kuanzia kumuona mara ya kwanza mpaka siku
hiyo. “Nilivyomuona leo si kama anayekuja kwa shari!”
“Sasa anataka nini kama si kutaka kunitibua tu?” Mama Jema
akaanza kulipuka. Hataki na wanae! “Labda tuache
tuone.” “Hakika iwe heri, lakini si kukubugudhi. Hapo tutaonana wabaya.”
Akamtuliza mama yake kwa maneno mengi, wakacheka na kuagana.
Subira Yavuta Kheri.
Safari hii akakuta
kama Ezra anamsubiria amsaidie. Akamchokoza. “Huogopi nitaona kama ni hongo?”
Wakaanzia hapo utani, kila kitu wakawa wakitaniana ni ‘hongo’. Angalau ukaribu
ukaanza. “Jambo haliishi Ezra jamani!?” “Ulinipiga stop mbaya! Mpaka
wema ukaoza!” Wakataniana, mpaka wakamaliza, Jelini akazidi kuvutiwa na haiba
ya Ezra. Alikuwa na furaha huyo. Ezra yupo naye akimsaidia! Kila mtu akawa wakiwaangalia
wao jinsi wanavyocheka. Halafu ule ukaribu, wakusaidiwa na Ezra, kila mtu
akaona jinsi anavyojituma hapo kwa Jelini. Mara maji ya kunywa, mara amsogozee
hiki, ikawa ilimradi tu mpaka wakamaliza. Jelini mwenyewe alijua amejaliwa
kwa namna yake.
Alipomaliza, akiwa
anamsindikiza kurudi garini, Jelini akaanza. “Sasa leo na wewe si ni mualikwa?”
“Sema mimi ni mualika.” “Acha masihara Ezra!” “Esta ni kadada kangu.
Kama ungekuwa umepazoea kanisani na watu wake, ungegundua, yule mtoto mkubwa wa
mchungaji ni rafiki yangu sana.” “Kumbe!” Akajifanya hafahamu sana mambo yake wakati
alikuwa akimfuatilia sana tu. “Basi hongereni. Sasa mbona mimi sijaalikwa?”
“Niliogopa isije ikaleta picha ya hongo.” Jelini alicheka sana.
“Nakutania bwana! Ila
niliambiwa siku za jamamosi kwako ndio kazi inakuwa imepamba moto. Hushikiki.” Jelini akajua kumbe na yeye alikuwa
akimfuatilia! Hakumsusa moja kwa moja. Akafurahi na kujibu, “Wala aliyekwambia
hajakosea. Leo ndio nakusanya pesa ya jijini. Wenye kufunga ndoa, najitahidi na
mimi nipate kidogo. Kama sio viti kama hivi, basi kukodisha vitambaa vya meza
na maua yake. Mapambo ya bibi harusi, ilimradi tu kuwe na neema na kwetu.” “Hongera
sana.” Akacheka, kama ambaye hajui azungumze nini tena.
“Ila harusi ni juma
lijalo, tena ni jumapili. Nakukaribisha tuwe wote.” Kwa mshituko, akahisi kama
hajamsikia vizuri. Akaogopa asijichanganye. Gafla akajihisi kufa ganzi, hajui
ajibu nini! Ilishapita muda mrefu, karibia mwaka, hajatongwazwa na wanaume kama
Ezra. Ikampa ububu wa sekunde.
“Ishakuwa hongo tena,
nini?” Akauliza kwa utani kidogo ila hata na yeye akiwa na wasiwasi asije
kataliwa kwa mara ya pili. “Hapana! Nilikuwa najaribu kufikiria kama nina kitu
nilishakipanga siku hiyo ya jumapili. Nisije kukubali halafu nikashindwa.” Akajaribu
kuzungusha. “Kama kuna mipango mingine, uwe tu na amani. Tusiharibu mipango ya
muhimu.” Ikawa kama anahitimisha, aachane naye.
Jelini akajua bahati
haitarudi mara ya tatu. Akawahi. “Nafikiri sina kitu kinachonishikilia, na
mimi naweza hudhuria.” Akakubali kike. Mpaka Ezra mwenyewe hakuamini
kama amekubali. “Sasa mbona kama huamini!” “Sikutegemea ukubali hivyo kirahisi!
Basi kesho nitakupa kadi.” “Sawa.” Kama walioogopa wasije haribu, wakaagana
hapohapo. Akaondoka akicheka huku akimfikiria Ezra. “Acha na mimi nitoke
kidogo, nipumzishe mawazo.” Akajiwazia moyoni.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jelini Akiwa Amekata Tamaa Ya Kumsubiria Colins, Kijana Ezra Anafanikiwa
Kupenya Akilini Kwa Jelini.
Baba CJ naye?
Chelewachelewa, Utakuta Mwana Si Wako.
Nini Kitaendelea?
0 Comments:
Post a Comment