Ilipofika mida ya saa
12 jioni, akaona ampigie simu Love. “Nipo kazini,
nimebanwa na kazi.” “Colins yupo wapi? Maana hapatikaniki kwa simu.” “Yaani
Colins amebadilika! Hapa najitahidi kumtunzia siri kwa baba. Hataki kazi. Kazi
yake kuzurula tu.” Yakaanza mashitaka ya Colins kwa muda mrefu
wakutosha. Akimlalamikia Colins.
“Labda
nirudi kwenye swali la msingi. Yuko wapi au wewe unajua huwa ana kwenda
kuzurula wapi?” “Sijui. Tena wakati mwingine inabidi kumuomba mtu akamtafute,
ndioo..” “Huyo mtu anakwenda kumtafutia wapi?” Mzee hakutaka maneno mengi zaidi. “Sijui. Ila huwa mara nyingine anafanikiwa kumpata, ndio
ana..” “Unaweza kunipa namba ya simu ya huyo unayemtuma kwenda kumtafuta?” “Ni
kijana wangu wa kazi.” Hiyo sentensi ikamchanganya kidogo baba CJ.
“Ukimaanisha
nini unaposema ni kijana wako wa kazi?” “Wa hapo nyumbani! Maana hapo ni kama
pangu tu. Colins hana muda napo kabisa na ni mimi ndiye namlipa mshahara, maana
sijui hata Colins anapeleka wapi pesa yote anayolipwa mshahara. Yaani…” “Love,
shitaka lolote utakalonipa juu ya Colins, halitasaidia mpaka nimpate Colins
mwenyewe. Sasa je, naweza kupata namba ya simu ya huyo kijana anayejua
pakumpata?”
Mzee akaweka msimamo. Maana Love ni mzuri sana wa maneno. Usipokuwa makini,
anakupoteza lengo.
“Sio kwamba
anajua sehemu yakumpata! Na yeye anakuwa kama anabahatisha.” “Sawa, naweza
kupata namba yake?” “Nafikiri si ustaarabu kuanza kugawa tu namba ya mtu. Mimi
nashauri nimpigie, akamtafute, kisha nimwambie unamtafuta. Atakaporudi hapo
nyumbani, atawasha simu yake, atakupigia. Usiwe na wasiwasi. Colins atakupigia
tu. Wewe nenda kapumzike. Na mimi mwenyewe nikimaliza kazi, nitarudi.” “Sawa.
Nashukuru. Nisipomsikia leo, kesho itabidi nimuwahi kabla hajatoka.” “Usiwe na
wasiwasi, usiku mwema.”
Wakaagana.
Kila alipotaka
kuondoka roho ikasita kama mkewe. Alishaingia kabisa kwenye gari, akawasha ili
aondoke, lakini moyo ukasita kabisa. Mwishoe akaamua kubaki tu hapo garini.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Alikaa hapo mpaka
mida ya saa tatu, akasikia watu wakiingia getini wakisukumana. Akatoka garini.
Akaona vijana wawili. Mmoja anamvuta mwingine. Akashukuru Mungu yule anayevutwa
hakuwa Colins. Maana alikuwa akivutwa si kwa heshima kabisa, kama mnyama!
Kadiri walivyokuwa wakimsogelea, aliweza kumuona huyo kijana anayevutwa alivyo
mwembamba, ndevu ndefu na nywele nyingi tu. Hakuwa akizungumza ila kupinga tu,
kama ambaye hakuwa akitaka kurudi hapo. Baba CJ akasimama vizuri akiwatizama
akijua watakapomsogelea, ndipo awaulize kama wanamjua Colins.
Hilo zoezi
likaendelea mpaka wakampita na kuendelea kumburuza mpaka kupandisha ngazi zote
mpaka juu kabisa, nje ya geti dogo la kuingilia mlango wa ndani. Akaona
anamfunga na kamba aliyoitoa mfukoni kama aliyokuwa amejiandaa nayo. Mikono
yote miwili na miguu. Akamfunga na kuikaza kabisa. Baba CJ akakunja uso. Kwamba
kwa nini amfunge mwanadamu vile kama mnyama! Akabaki akiwatizama kwa juu, yeye
yupo chini kabisa ya ngazi.
“Sasa hapo usiondoke
mpaka dada mwenyewe aje. Na amesema akukute.” Baba CJ akashituka sana.
Akapandisha ngazi akikimbia. “Huyo ni nani!?” Akauliza akijaribu kumtizama kwa
karibu. “Mimi mwenyewe nilimkuta, lakini Eva yule aliyekuwa akifanya kazi humu
ndani aliniambia, alikuaga mwanaume wa dada kabla hajachanganyikiwa.
Ndio dada anakua akimtunza tu.” Nusura baba CJ aanguke kwa mshituko.
“Colins?!”
Akamtizama. Weupe ule kama wa mkewe, uliisha wote. Akafifia kama
aliyekuwa akiungua na jua. Hapo alipo hakuwa hata na viatu! Mchafu. Amekonda.
Yupo kama takataka kweli. “Tafadhali mfungue?” “Ataondoka hapo, na dada amesema
nimfunge mpaka arudi.” “Kabla sijakuua, tafadhali mfungue kijana wangu. Hichi
ulichomfanya, naweza nikakufanyia na wewe. Nikakuacha hapa mpaka huyo dada yako
akakukuta hapa ulipomfunga yeye.” “Samahani sikujua kama ni…” Akasita. “Mimi
Eva aliniambia anahisi huyu ni yatima ndio maana dada amejitolea kumsaidia.”
Baba CJ akaanza kumfungua mwenyewe kwa haraka.
Alipomfungua tu,
akasimama na kutaka kuondoka. “Colins?” Akamgeukia baba yake. “Unataka kwenda
wapi?” Akaonekana na yeye hajui. “Umekula?” Akanyamaza. “Funguo za kuingilia
ndani zipo wapi?” Akawa hajui.
Kibao Kimegeuka.
Akutana Na Love Halisi.
Akampigia tena Love. “Nipo na Colins hapa kwenu.” Love alishituka sana. “Nilifikiri uliondoka!” Akaropoka. “Tunaingiaje ndani?” Baba CJ akauliza. “Atakuwa na funguo zake mwenyewe. Mimi nikitoka nafunga,
nabakia na funguo zangu.” “Kwa jinsi alivyo hivi, kweli atakuwa na funguo za
nyumba nzima kweli huyu!? Unajua mara ya mwisho atakuwa amekula lini!?” Hapo
akaharibu.
Love akambadilikia mzee,
asiamini. Akaanza kwa kulalamika kwamba anamsingizia yeye hamtunzi
Colins wakati anayo majukumu mengine mbali na Colins! Kabla taarifa hazijafika
kichwani sawasawa, binti akaanza kumlilia kwenye simu, mzee hajaweza
hata kujibu, akasikia mzee Simba ameunganishwa kwenye simu, Love analia
kwelikweli, anamshitakia baba CJ kwa baba yake kuwa anamgombesha kuwa anamtesa
mwanae. Love aliongea mengi akilia. Mzee alipatwa na hali, hawezi hata
kujibu kwa mshituko asiamini kama ni Love aliyekuwa akimtetea sana kwa Colins.
Usiku huo akajifunua kwa wazi kabisa.
Sasa baba yake, mzee
Simba akapokea. “Unawezaje kuzungumza na binti yangu
bila mimi?! Yameanza lini sisi kuingilia mambo ya undani? Kweli ulitaka binti
yangu aache kazi zake, ukijua garama aliyolipa kusoma, wakati Colins akikataa
shule! Leo amefanikiwa ndio unataka abaki nyumbani akimlea Colins ambaye
amechagua maisha yake ya ajabuajabu tu!?” Hizo shutuma
zikaendelea wawili hao wamewaka kwelikweli na kumuacha baba Colins na mshituko
mkubwa, haamini.
Mpaka hapo, ikawa
kama Love ndiye aliyekuwa akimsaidia Colins kwenye maisha. Kukubali kuwa
na mtu kama Colins ambaye hajasoma kama yeye Love. Mvivu. Hana uchu wa
maendeleo. Love aliendelea kulia huku akisema madhaifu ya Colins, baba yake
akimtuhumu baba Colins, mwishoe baba CJ akaona ahitimishe. Alilo nalo mbeleni
ni zito kuliko hayo matusi yao. “Tutazungumza
wakati mwingine.” Akawaambia hivyo tu, na kukata simu.
Mtu Chake.
Akamchukua Colins na
kumuingiza ndani ya gari yake. Ikaanza safari ya kurudi kwake. Alifunga milango
yote tena akaweka child lock ili asije akaruka garini. Akiwa njiani simu
ya mkewe ikaingia. “Ulimpata Colins?” “Nipo naye hapa.
Narudi naye nyumbani.” Mama Colins akawa hajui afurahi au ajiulize kwa
nini usiku huo arudi naye nyumbani! Ila akauliza. “Kwema?”
“Hali yake si nzuri. Anahitaji uangalizi wa karibu ambao pale anapoishi na
Love, hawawezi kumsaidia.” “Unamaanisha nini!?” “Labda ukimuona, utajua ni nini
nazungumzia. Ila naomba kuwepo na chakula laini. Anaonekana hajala muda mrefu.”
Mama Colins akaingia jikoni yeye mwenyewe kuanza kupika uji.
Wana Kulitafuta, Wamelipata.
Aliposikia gari,
akakimbilia nje. Akabaki akisubiria Colins ashuke. Maana aliyeshuka hapo hakuwa
Colins aliyemtarajia. Akazunguka upande wa pili kuona kama yupo hapo. “Mbona
sasa hujaja naye!? Umemshusha wapi!?” Baba CJ akabaki amesimama huku amemshika
mkono akijaribu kumuongoza njia aingie ndani. Alikuwa akiyumba kama mlevi au
mgonjwa wa kuhara na kutapika. Tena aliyesumbuka kwa muda mrefu mpaka akaishiwa
nguvu.
“Baba CJ!?” “Huyu
hapa ndiye Colins.” Akarudi kumtizama, kisha akamtizama tena. Mama ni mama.
Katikati ya uchafu ule kuanzia wa mandefu na harufu mbaya, aliweza kumtambua
mwanae. Mama CJ alipatwa hali mbaya, nusura aanguke. “Sasa katika hili, naomba
ujikaze mama CJ, nisaidie ili tumsaidie huyu. Anakuhitaji sana.” Ikawa kama
amemsaidia asianguke kwa mshituko, akamrudisha pale, ila akaanza kulia kwa
kadiri alivyokuwa akimwangalia. “Umepatwa na nini
Colins mwanangu!?” Akamuuliza na machozi. “Unaumwa
baba?” Akamuuliza kwa kumuhurumia, Colins hakujibu. Alikuwa akitoa
harufu mbaya sana. “Acha nimsaidie kuoga kwanza.” Baba yake akamvutia ndani
maana alikuwa kama amezubaa tu.
Kazi ya kumsafisha
ikaanzaa, mpaka akatakata na kumbadili nguo. Akamrudisha sebuleni. Akabaki
amekaa, ameinamia chini, ameshikilia moyo kwa mkono wa kulia, ule mkono wa
kushoto ameegemeza kichwa. “Unajisikiaje Colins?” Mama yake akamuuliza
akimsogezea uji. Kimya. “Colins?” Kimya. Wazazi wake wakaangaliana. “Halafu mbona kama miguu ina madonda?!”
Akamsimulia alichokutana nacho akiwa analetwa na huyo kijana wa Love. Akazidi
kulia.
Baada ya muda
wakamuona ananyanyuka, anataka kutoka nje. Baba yake akamuwahi. Akasimama kwa
haraka na kukimbilia mlangoni. “Unakwenda wapi?” Akabaki kama na yeye hajui.
Akataka ampite atoke, akamrudisha. Hilo zoezi likaendelea. Anamrudisha kukaa,
anakaa kidogo. Anakuwa kama amekumbuka kitu, anasimama kutoka. Ila kila akirudi
kukaa, anashikilia moyo kwa muda, kisha anasimama anakuwa anataka kutoka.
Mwishoe wakaamua kumchoma sindano ya usingizi, wamuwekee maji ya sukari, apate
nguvu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kazi ya kumuuguza
hapo ndani ikaanza. Hawataki kumpeleka hospitalini kwa aibu. Lakini kila
akiamka, anatafuta mwanya wa kutoka hapo ndani. Ila kichwani akawa hataki
kabisa kuguswa. Ikabidi baba yake amnyoe upara kabisa ili iwe rahisi
kumsafisha. Colins akawa kama kababu kalikokosa matunzo. Na muda wote huo,
hakuna hata mmoja kwenye familia ya Simba aliyewatafuta hata kuulizia hali
yake. Wao wakashika moja la kuuguza.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Connie alipopata
habari kuwa kaka yake hali sio nzuri na yupo nyumbani, akaenda kumuona. Maana
ilikuwa kama siri hapo mwanzo. Wazee hao wakidhani wakimficha, akala vizuri,
basi hali yake itarudia kama kawaida. Lakini ikawa ni mtu anayetakiwa ulinzi,
lasivyo anatoroka. Mzee akapunguza shuguli za kikazi, akawekeza muda kwenye
kumuuguza. Ndipo Connie alipotaka kujua mbona hamuoni sana huko hospitalini, na
kila akipita ofisini kwake anaambiwa hayupo, ndipo ikabidi aseme ukweli. Ndipo
akaenda kumuona kaka yake.
Alishituka sana
kumkuta kaka yake kwenye ile hali. Hakutegemea kama ni yeye. “Ilikuaje!?”
“Hakuna anayejua.” Akaelezewa mazingira waliyomkuta, akalia sana. Na mpaka hapo
Love hakusikika tena. Siku hiyo ikabidi tu alale nyumbani kwani alikuwa kama
amechanganyikiwa, akasema hataweza kufanya chochote hata akirudi chuoni.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kesho yake akaomba
asifungiwe wala wasimpe dawa ya usingizi. Yeye atashida naye hata kutoka naye,
ajue anapotaka kwenda. Kweli wakafanya hivyo. Alipomaliza tu kusafishwa na baba
yake, mama yao akaanza kumlisha akiwa ameinamisha kichwa chake, kakishikilia na
mkono wa shoto, wakulia kashilia moyo kama kawaida yake. Akimuita, ananyanyua
kichwa, akimwambia afungue mdomo, anafungua, anamuwekea chakula. Anarudi kama
alivyokuwa amekaa. Ameshikilia moyo wake. Connie akamwangalia kwa muda, kisha
wakamuona ananyanyuka, anatoka kabisa pale. Hapo hajavaa hata viatu!
Connie akaanza
kumfuata nyuma taratibu. Tembea yake yenyewe taratibu kama aliye mwenye vidonda
vinavyomuuma kwenye nyayo. Akatembea, kufika getini akakaa chini kabisa.
Akamuona anaanza kulia. Mama yao hakuwa mbali. Connie aliumia sana.
Na yeye akaenda kukaa
naye hapohapo chini. Jua lilishakuwa kali. Chini bila viatu, panachoma.
“Pole Colins. Niambie unataka nini.” Akajifuta machozi nakubaki amejishikilia.
Kitu kama kikapita
akilini kwa Connie, akakumbuka mpaka akasimama kwa mshituko. “Nimekumbuka mama!”
Mama yake akasogea, mzee alishatoka.
“Ni nini?” “Hivyo
unavyomuona anashika moyo. Ni kiapo aliapiwa na Jelini. Colins
aliniambia, aliambiwa na Jelini, tena mwenyewe anasema ilibidi aandike kwa
kumnukuhu. Akapiga micha pale alipoandika alichoambiwa na Jelini, akanitumia na
mimi kama kuthibitisha. Acha nikuonyeshe ujumbe wenyewe. Maana alinipigia akiwa
na furaha huyo, ndipo akanitumia na huu ujumbe.” Akaanza kutafuta kwenye simu
yake mpaka akaupata ujumbe.
Akamkabidhi simu mama
yake. ‘Kila unapoyasikia mapigo yako ya moyo. Popote ulipo. Muda
wowote hata kama mimi hunioni, ujue yupo Jelini anayekupenda kwa moyo wake
wote, mpaka niondoke hapa duniani. Hakuna ulimwengu utakaokuwepo wewe,
nisikupende Colins. Ujue nitakupenda mpaka kifo chako.’ Mama Colins
alilia sana.
“Kumbe
ndio maana anajishika moyo, kisha anaanza kutafuta!” “Usilie sasa! Yeye
hapo alipo anaonekana bado hajajua anachokitafuta. Ndio maana anahangaika.
Amebakia na hicho kiapo moyoni, hakumbuki.” Mama Colins akalia sana.
“Nitafanyaje
Connie?”
“Nikumtafuta Jelini, aje amuone labda atatulia.” Mama yao alishituka sana. “Hivi alivyo Colins ndio atataka mumuona kweli! Alipokuwa
mzima tulimfuata na…” Akamsimulia jinsi walivyomuendea Jelini nyumbani
kwao na kumuita mchawi, Connie akashangaa sana.
“Kweli mama na wewe
ukaenda, wakati Colins alishakwambia ukweli wake wote juu yake na Love!?”
“Sijui niliingiwa na nini!? Kulikuwa na shindikizo kila mahali nikawa kama
nimezidiwa nguvu, na mimi nikabaki nikienda kama upepo, nikiomba hiyo fujo
itulie. Mama Simba naye akawa kutwa kwenye simu akiomba nisimamie hilo jambo
liwezekane! Akaja na bibi yenu naye. Kama unavyomjua akikazania jambo.
Akalivalia njuga, nikabaki sijielewi! Ilikuwa mbaya mno.” “Mmmh!” Connie
akaguna kwa kuchoka. Hajui hata aanzie wapi kulaumu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakamuona Colins
anasimama, anataka kutoka nje kabisa. Connie akamuwahi. “Nisikilize Colins.
Sasahivi jua ni kali sana. Utaanguka njiani. Kwanza umedhoofu. Hutaweza kufika
mbali.” Akatulia kidogo, kisha wakamuona
anatoka. Akamfuata tena. “Turudi ndani. Ikifika jioni, nitakusindikiza
tukamtafute wote Jelini.” Hapo akamuona kama amekumbuka kitu. Akarudia kwa
sauti ya chini. “Jelini!” Wakamsikia kama aliyekumbuka vizuri sasa. “Ndiyo. Si
ndiye unayemtafuta?” “Jelini!” Akarudia
tena, ila safari hii na machozi. “Utakuwa sawa Coly. Twende ukapumzike ndani,
halafu jioni tutoke tena. Sawa?” Akamshika mkono wakawa wanarudi ndani. Mama
yao akilia sana.
Na kweli jioni
akamvalisha sendozi nyepesi, wakatoka wakitembea akimsindikiza kumtafuta
Jelini. Mwenyewe alikuwa dhaifu. Akitembea kidogo, anakaa. Wakafanya hilo zoezi
mpaka giza lilipowakuta huko mtaani, mama yao akaja kuwachukua na gari
kuwarudisha nyumbani. Kwenye gari akalala kwa kuchoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Hayo ndio yakawa
maisha yake huku baba yake akiwa anatumia madawa ya kila namna kumtibu bila
kufanikiwa kurudisha akili yake. Asubuhi anatoka hata na mama yake, wanajidai
wanakwenda kumtafuta Jelini. Wakitembea akichoka, wanarudi nyumbani. Jioni tena
hivyohivyo, wanatoka naye kumdanganyishia kumtafuta Jelini mpaka achoke,
wanafuatwa na gari popote wanapokuwa wamefikia, maana hapo anakua amemaliza
nguvu zote na wazi anakuwa na maumivu ya nyayo zilizojaa madonda, hawezi tena
kutembea kurudi nyumbani. Na mara zote anaishia kulala kwenye gari kwa kuchoka
kutembea akimtafuta Jelini.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ni Nini Kimempata Colins Katikati Ya Maombi Hayo Ya Mtumishi Aliyeletwa Na Kemi? Dawa Yake?
Jelini Yuko Wapi?
0 Comments:
Post a Comment