Vai akaona aendelee.
“Mimi sina uwezo wa kuzaa, Joshua.” “Nafahamu hilo.” Akajibu kama anayetaka
aende moja kwa moja kwenye kujibu swali lake. Vai akazidi kutetemeka mpaka
midomo. “Kwa hiyo aliposema vile nikapaniki na
kuamua niondoke kwa kuwa nampenda Bale. Na nilijikuta tu nikimpenda. Nikaona
kuwepo kwa ukaribu ule na pale tulipokuwa tumefikia kimahusiano, maana tulianza
kama marafiki wa kawaida tu. Ila mimi ndio nikaanza kumpenda. Tukawa tupo
karibu sana. Nikajua kuwepo vile kunaweza kumfanya akashindwa kupata mwanamke
atakayempa anachokitaka. Ndio nikaondoka ili nisimkwamishe. Na ukweli Bale
hakuonekana kujali sana kuondoka kwangu. Maana alinirudisha mpaka chuo, na
kuniacha wala asinitafute tena hata kwa salamu. Nikajua kweli ameamua kutafuta
msichana mwenye uwezo wa kuzaa ili amuoe.”
“Na uliposikia
nipo hotelini na mwanamme mwingine ilikuwa…” Akameza mate ambayo ni kama yalisha
kwisha kumkauka kabisa mdomoni. Mrembo akapata dry mouth ya hali ya juu.
Joshua kimya
akimtizama. Akajikausha machozi fasta. Akaendelea asipoteze muda. “Ukweli si
kwamba nilipanga. Mimi sinywi pombe. Sasa nilipotoka kwa Bale, nikiwa
hosteli, siku moja rafiki yangu akanikaribisha chakula cha usiku akiwa na
mwanaume wake na huyo rafiki yake. Tulipofika huko, wakanishawishi au nisema
nikanywa sweet red wine, waliniambia ni tamu kama juisi. Nilipoonja
kweli ilikuwa tamu, nikajua sitalewa. Nikaendelea kunywa mpaka nikalewa kabisa.
Ndio nikaja kuamka chumbani na huyo mwanaume. Halafu
huyo rafiki yangu niliyekuwa naye usiku uliopita na hao wanaume, aliniacha na
huyo mwanaume hapo hotelini na kuja kumpigia Bale simu kunisemelezea.”
“Ila
nirudi kwa upande wangu. Nilikosea tokea mwanzo, Joshua. Naomba msamaha
kwako na nimeshamuomba msamaha Bale pia. Si kitu nilikuwa nimepanga.” Jema akazidi
kushangazwa.
“Bado hujajibu ni kwa
nini umerudi?” Joshua akazidi kumbana. “Niliugua. Na hapa mjini kwa muda
mrefu sana, Bale ndio amekua akiniuguza. Hata
nikiwa chuo, nikiugua, yeye ndio mtu pekee atahakikisha napata matibabu na
kupona kabisa. Mama yetu yupo busy sana, na baba naye anaishi Moshi, anamaisha
yake. Kaka James pia anamaisha yake. Na si
mtu ambaye tumezoea kumtafuta kwa matatizo kama hayo. Au hatuna mazoea ya
karibu na kaka ya kiasi hata chakutafutana kwa salamu tu, mpaka iwe kuna jambo
muhimu sana. Sio kama anavyoishi na Nanaa. Kwangu na Viola ni tofauti kabisa.
Hayupo karibu kabisa na sisi.” Jema akajisikia kuumia.
“Kwa
hiyo nimejikuta nabakiwa na Bale tu. Nilipougua, sikuwa na jinsi. Ikabidi
kumwambia. Bale alikuja kunichukua na kuniuguza kwake mpaka nikapona na
kuhakikisha muda ule ambao nilishindwa kuwepo darasani, ananisaidia kusoma
mpaka kufikia wenzangu. Ndipo kwa mara ya kwanza kipindi hicho nikamwambia
ukweli kwamba mimi nampenda, na nilikosea. Na yeye akanieleza upande wake.
Ninachotaka kukuhakikishia ni nampenda Bale. Amenipokea hivi nilivyo.
Tuna maisha ya upendo na amani. Tunabebana katika kila hali, kitu ambacho
sijawahi pata kutoka kwa mwanaume yeyote yule.”
“Nilikosea,
nimetubu, nakuahidi hutasikia baya langu tena. Kwakuwa shida yangu
ilikuwa mwanaume kama Bale, sina sababu ya kuhangaika tena. Nimetulia.
Bale ndio sababu nipo chuo mpaka sasa. Anasoma
na mimi. Ananielekeza. Ananitia moyo kwa sababu mimi sijajaliwa akili nyingi za
darasani. Lakini Bale anasoma na mimi, na hachoki. Nafanya vizuri chuoni, kwa
sababu yake. Najua najirudia rudia, na wewe unaharaka. Lakini nakuhakikishia
nampenda sana Bale. Na nitatulia naye mpaka kifo.”
“Lakini kaka yako
hamtaki! Utafanyaje?” Moyo wa Jema ulipasuka kusikia hivyo, kama kuliangushwa
chuma sakafuni. “Kwamba huyu Joshua yupo kimya juu ya hili muda wote, kumbe
anajua jinsi James alivyomfukuza Bale!” Jema aliingiwa hofu, asiamini muda
wote huo Joshua anamchora tu yeye na James. Asiwaambie chochote ila kufanya
kama kila kitu kipo sawa. “Inamaana na Naya anajua!” Akabaki kujiuliza bila
jibu huku akisikiliza.
Vai akajifuta machozi
akijaribu kutulia ili kuzungumza amuaminishe Joshua. “Tupo kwenye maombi. Mimi
naamini kama Mungu aliweza kumsamehe Bale kwa makosa yote mabaya aliyo tenda. Halafu
wewe mtu baki ukampokea na kumtunza kwa heshima kubwa hivi, naamini Mungu
atagusa na wengine. Inaweza isiwe kwa haraka kwa
sababu ukweli Bale alikosa sana. Tumekubaliana hatutafanya chochote,
tutabaki tukimuomba na kumsubiria Mungu mpaka yeye mwenyewe Mungu
atakapofungua mlango kwa wakati wake yeye. Ni hilo tu.” Hapo akaongea
lugha ya Joshua. Akapa moyo wake.
Akamuona amevuta
pumzi kwa nguvu na kuzishusha. “Bale anakupenda sana Vai. Tafadhali usije wahi
bweteka.” Vai akazidi kuumia nakushindwa kuzuia machozi. “Sithubutu, kwa sababu hakuna mwanaume atanipokea na kunipenda
hivi nilivyo, kama Bale. Mimi najua
ninachozungumza. Sithubutu. Naomba na wewe unipe nafasi nyingine Joshua.
Bale anakutizama sana wewe. Akipata baraka zako, najua atafurahi. Ni hilo tu.”
“Nitazidi kuwaombea. Muwe na siku njema.” Jema aliposikia tu hivyo akapandisha
kioo kwa haraka. Mpaka Joshua anageuka, akajifanya hakuwa hata akiwatizama.
Wakaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Lakini Jema akabaki
na maswali mengi sana mpaka kumtia hofu. Kwamba Joshua ndio yupo karibu hivyo
na Bale! Halafu anajua kama Bale alifukuzwa vibaya vile nyumbani kwake na
mumewe! Halafu hata asilizingumzie hilo hata na yeye au James, eti akabaki tu
kimya! Kikamsumbua sana Jema asijue Joshua anawafikiria nini. Akapotea kabisa
hapo garini. Lakini ni kawaida yao. Huwa mbali na kazi au vitu vya muhimu,
hawanaga stori na Joshua. Ila James na Joshua wapo karibu sana. Wanazungumza
sana tu. Kimya kikapita hapo garini, dereva akiendelea kukanyaga mafuta
akitafuta barabara ya Cocacola.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Bale akamsogelea pale
alipokuwa akisindikiza gari ya Joshua kwa macho. “Tutakuwa sawa Vai. Usiwe na
wasiwasi.” Vai akajifuta machozi. “Nenda tu kazini.
Tutazungumza baadaye.” “Siwezi kuondoka nikakuacha huna raha. Nataka
ufurahie pamoja na mimi. Tumepata mguu na umefaa. Usilie, nyamaza. Nisindikize
kwenye gari.” Wakafuatana.
“Halafu ulikuwa
sahihi, Bale. Inamaana ungebadilisha siku, inamaana Joshua angekuja hapa leo,
akakukosa. Ningekuponza.” “Kama tungekubaliana kubadili, ningemtaarifu. Lakini
sikutegemea kama angekuja aisee! Joshua yupo busy. Si umeona jinsi muda wake
unavyobanwa na Jema? Hata dakika moja kwake ni muhimu mno. Eti imenigusa
kiajabu sana. Sijatarajia kabisa kumuona hapa kwa hili, siku kama hii!” “Hata
mimi nimeona jinsi anavyokuthamini aisee. Si kawaida.” Wakabaki wakizungumza
mpaka Vai alipotulia ndipo wakaachana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
‘Usisahau
nakupenda Vai. Na sitabadilika.’ Ujumbe ukaingia akiwa yupo na wenzake
darasani. Akajisikia kupendwa, akabaki akifikiria ni lini Mungu atafungua hiyo
milango, wapokelewe kwao, aolewe na Bale, nafsi yake itulie. Maana kila wakati
alibaki akiota kuibiwa tu huyo Bale.
Kila Jambo Na Wakati Wake.
Ijumaa.
Naya alijua mumewe
yupo kikaoni, akasubiri mpaka akamaliza kikao cha mwisho wa siku, akampigia. “Jema ameniambia ndio mmemaliza siku.” “Aisee namshukuru
Mungu, juma lilikuwa na mengi, lakini nimehitimisha. Naona Jema amenikaba mpaka
ameishiwa cha kunipa kesho, ameniambia kesho nipo huru.” Wakacheka. “Ameniambia jinsi alivyokubana hili juma zima.” “Hata muda
wangu wa chakula cha mchana, alichukua yeye. Ikabidi tu nitangaze mfungo wa
lazima. Akinipa hata dakika 5 nazungumza na Mungu wangu tu.” Naya
akatulia kidogo.
“Mama Kumu,
upo?” “Ulikuwa ukiwaombea kina Bale?” Naya akauliza kwa upole. “Usiwe na wasiwasi, wewe na wanao pia mlikuwa mkitajwatajwa
hapo katikati.” Naya akamuhurumia mumewe ila akacheka. “Nakuja nyumbani muda si mrefu ili niwawahi kina Kumu kabla
hawajalala.” “Kama ulikuwa umefunga, basi naona utangaze na mkesha pia. Leo
wamelala mpaka jioni hii. Yaani mama G amepita ndio amewaamsha kwa lazima.
Tumewaogesha, akaondoka na kunitakia mkesha mwema. Wamejaa hapo kwenye chumba
chao cha kuchezea, wamechangamka kama ndio jua kali nje. Hivi nimetoka hapa
mlangoni ili nizungumze na wewe.” Joshua akacheka lakini ndio akajua
hiyo simu haikuwa ya salamu tu, kuna jambo.
“Niambie
mama Kumu.” “Sijui niiwekaje hili!” Akaanza kama anayesita. “Hata ukianzia katikati, unajua mimi nitakuelewa tu. Niambie
chochote kilichopo mawazoni mwako.” “Ni sawa kesho tuandae mazingira,
tuwakaribishe kina Bale?” Joshua alishituka, akapatwa ububu wa gafla.
“Nimeumia
kuona anafukuzwa kwenye majumba ya watu, Joshua. Watu wote tunamkimbia, umebaki
peke yako ukimkumbatia bila kuchoka. Nimeshindwa kutulia na lile swali lako la
kama baba Naya angekuwepo, angefanya nini juu ya Bale. Nikakumbuka baba
alivyokuwa tayari kukosa harusi yangu ili akamtafute yeye. Mbaya zaidi baba
hakumpata, akaishia mikononi kwa Malon aliyekuwa na hasira mbaya kwa wakati
ule. Sijui alimwaminisha nini mpaka Bale akafikia vile. Lakini katika yote,
nakumbuka baba hakuacha kufunga na kumuomba Mungu kwa ajili yake. Hakumkatia
tamaa mpaka kifo chake.”
Naya akaendelea kuzungumza kinachoendelea moyoni mwake.
“Halafu
nikakumbushwa maneno ulizungumza na mimi siku moja ulikuja kunichukua kwenda
kazini. Ilikuwa asubuhi sana. Tulikuwa tumekosana na Bale sababu ya huyohuyo
Malon. Ukaniambia mimi ni mzaliwa wa kwanza kwa sababu na lazima niishi kama
dada yake si mshindani wake. Maneno yanayofanana na hayo, mpaka nikampigia simu
na kuzungumza naye, hakuamini maana aliondoka nyumbani na kwenda kwa Malon,
Mbeya, tena baada ya kumuacha ile mara ya kwanza.” Naya akaendelea,
Joshua kimya akijua Roho wa Mungu alikuwa akishugulika na nafsi yake mpaka
amesalimu amri.
“Anyways,
ninachotaka kusema ni kwamba, mimi kama Naya au mama Kumu, nina hofu
naye sana. Naogopa hata kumsogeza karibu na kina Kumu. Lakini nahisi na mimi
nitakaa sana hapa, kama sitaamua kuchukua hatua. Sitatoka hapa na nitaendelea
kumuadhibu kwa makosa ambayo alishasamehewa na Mungu. Nimeona na mimi nitembee
na wewe kwa imani tu.” “Nakushukuru Naya. Asante sana.”
“Mimi
ndio natakiwa kukushukuru Joshua. Bale ananihusu mimi zaidi kuliko wewe
uliyekubali tu kutuchukua ukisimama kwenye nafasi ya baba Naya. Nashukuru
Joshua. Naomba nivumilie. Nilihitaji muda. Bale alinitenda ukatili mbaya sana.”
“Na mimi nilijua ndio
maana sikukuharakisha. Naamini kwenye wakati wa Mungu. Na nakuahidi Naya,
tutakuwa salama. Namuwekea dhamana Bale, amebadilika. Tafadhali niamini.
Nimemuona kwa maneno na vitendo, mpaka utahisi amekua mtu mwingine kabisa.
Sijawa kipofu katika hili kiasi cha kukubali kumleta karibu ya familia yangu,
kama Mungu hajaruhusu. Nisingekubali kuhatarisha maisha yako na watoto
hivihivi.” Naya kimya akiendelea kulia.
“Sasa hizi
ni habari njema, mama Kumu. Usilie. Wanao watahisi haupo sawa, na mimi
baba yao sijasimama kwenye nafasi yangu. Wataniona hovyo.” Naya akaanza
kucheka. “Hivi wewe unajua wanao bado ni wadogo
sana hawaelewi kitu.” “Hata kidogo. Wanahisia
zote, wanaelewa kila kitu. Ndio maana wakiona unaimba na wao wanacheka na
kupiga makofi. Wakikuona umepoa, na wenyewe wanapoa. Wanakuangalia sana usoni
na wanafanya kila kitu kutokana na hisia zako. Tafadhali tubakie kwenye hili.
Mwenzio nimefurahia sana. Mungu amefungua mlango ambao sikuwa nikijua
utafungukaje! Na sikuwa nikijua hata nimuombe nini Mungu juu ya hili. Nikawa
nikimuachia tu Roho wa Mungu, azungumze naye Mungu mwenyewe. Ila naona na huko
mbinguni watapumzika.” Naya akaanza kucheka akilia.
“Jinsi
walivyosumbuliwa?”
“Si kidogo mama. Pakipoa kidogo tu, natuma maombi
mengine. Hata nikiwa naoga, nikimkumbuka tu baba Naya, na maisha yenu niliyowakuta
nayo pale kwenu Kiluvya siku ya kwanza mliponifungulia mlango nyumbani kwenu,
na Bale akanipikia, basi namwambia Mungu, ‘tafadhali kumbuka rehema’. Naona akaona afupishe hili jambo, ahamie kwako. Sasa
kabla hapajapoa, acha nimtafute Bale, niwakaribishe nyumbani kesho. Najua kwake
itakuwa…” Akakosa neno. “Acha nimpigie.”
“Joshua?” Akamuwahi kabla ya
kukata simu. “Nipo mama.” “Utafanyaje juu ya James? Kila nikifiria jinsi alivyowafukuza kwake, inaniuma, japo namuelewa.”
“Sijui Naya. Kwa mara ya kwanza, nimekosa neno
au maneno sahihi yakuzungumza na James. Ni kama wakili, aliyelipwa pesa nyingi
kusimamia kesi ya mtu, halafu hana jinsi ya kushinda kwa sababu ushahidi wote
unaonyesha mtu wake ni mkosaji, na adhabu ndio halali ya huyo mtuhumiwa. Hakuna
ubishi, hakuna kupinga kwa sababu kweli huyo mtu amekosa. Ndipo nilipo
mimi.”
“Lakini
Naya, aisee acha huyu Mungu, abakie kuwa Mungu. Ndio maana naogopa sana
kugusa utukufu wake. Ana njia zake za ajabu sana, ndipo nilipo mimi sasahivi.
Na namshukuru Mungu, hata wao, wamekubali kumsubiria Mungu.”
“Juzi
nilimpigia simu Bale, nilijua ni siku yake ya maombi. Akaniambia na Vai yupo
hapo kwake walikubaliana waombe pamoja. Basi nikaungana nao kwa njia ya simu.”
“Joshua?” “Kabisa Naya. Hakuna kinachoharibika mbele za Mungu, kwa kupitia
maombi. Na hakuna aliyefilisi mbingu kwa kupewa na Mungu alichoomba. Kumejaa
hazina isiyoisha.”
“Nilikuwa
njiani kurudi nyumbani. Nikaomba nao, nikawapa neno moja tu kwa ufupi,
nikawaacha wakiwa na amani kabisa. Hawa watu wawili wanapendana, Naya. Na
wameamua kubebana vile walivyo mpaka utashangazwa na nguvu ya msalaba.
Na hata ukiwaona kwa macho, uta…” “Subiri kwanza Joshua. Kwani wewe
ulishakutana nao?”
Joshua akajua amekamatwa. Asijue Naya anajilaumu kupitwa kwenye maisha ya kaka
yake.
“Ndiyo,
Naya. Kama juma moja hivi limepita, Bale alifanikiwa kuwekewa mguu wake.
Ilikuwa siku ya jumatano, asubuhi, na mimi nikaenda huko MOI kushuhudia kile
Mungu amemfanyia, ndipo nikakutana na Vai. Kumbe alikuwepo pale kumsindikiza.
Ninachotaka kusema ni hawa watu wawili, ni binadamu walioamua kubebana
vile walivyo. Hata wao ukiwatizama, utajua ipo amani katikati yao. Na
wanamsubiria Mungu.”
“Kwa kujibu
swali lako. Nitafanyaje kwa James, SIJUI. Ila ninachojua, huyu Mungu
aliyeanzisha kazi yake kwa Bale, hatatulia mpaka ikamilike. Na kwa sababu
alizungumza na mimi pia na kuniambia hajamalizana naye, basi namuachia yeye
mwenyewe. Ila najua hao malaika wangu wa zamu, watakuwa wamesha choka.
Nahisi na wenyewe wanamwambia Mungu, kubali kwa haraka, hili jambo liishe. Wote
tupumzike.”
Naya akacheka akilia.
“Asante
Joshua wangu. Ujiandae kwa usiku mzuri sana.” Akamsikia
akifurahia. “Sasa uache utoto.” “Acha nifurahie
marupurupu yangu kutoka kwa Mungu, Naya. Acha wivu.” “Ujue ukianza kujisifu
nitagairi.” “Huthubutu. Utashangaa hulali, unakesha. Mungu anakuadhibu
kwa sababu….” “Nyie Joshua jamani! Kumbe ndivyo unavyo…” “Nakwambia sio mimi ni
Baba yangu, anajua kunipa yaliyo mema. Na nilikwambia huwa malipo yake si
madogo. Sasa wewe usimjaribu.” Naya alicheka mpaka machozi.
![]() |
lingerie |
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Hatimaye Milango Ya Kwa Dada Yake Bale Imeanza Kufunguliwa.
Itakuaje Wakikutana Ndugu Hawa Waliobaki Wawili Tu, Tena Baada Ya
Muda Mrefu Wakiwa Wameumizana Sana?
Colins Yupo Wapi? Anafanya Nini
Na Anaendeleaje Na Mpenzi Aliyepata Baraka Kutoka Kwa Wazazi?
Bado Jema Anataarifa Ya Umuhimu Wa Bale Kwa Joshua. Itakuaje?
Usikose Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment