Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 6 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 6

Maisha lazima yaendelee. Huku kazini kwa kuwa Colins alikuwa mtu wa watu, wakamvumilia mpaka wakachoka. Amepotea kazini. Viongozi wanamtafuta kwa simu mpaka wakajaribu kwenda kwake, hawakumpata. Baada ya mwezi ikabidi nafasi yake ijazwe. Alipotaka kupewa James, mchaga akaikataa. “Mimi sina muda wa vikao zaidi ya huu ambao nishaupa kampuni. Nina mambo mengi, na ninafamilia changa. Haya mambo ya vikao vya
mpaka usiku, yangu yatakwama. Ila nashukuru kwa kunifikiria.” Wakajaribu kumbembeleza James ambaye tayari anajua hiyo kazi. James akapiga mahesabu ya muda atakao takiwa kuongeza hapo kazini akipunja muda kwenye biashara zake, akaona kiasi cha pesa wanachopanga kumlipa hakiwezi kutosha kufidia pesa anayotengeneza nje ya kazi. Akakataa kabisa, ila akaahidi akiletwa mgeni, japo atakuwa kiongozi wake, atamfundisha kazi.

Nafasi ya kazi ikatangazwa, baada ya majuma matatu, nafasi ikajazwa na kijana mdogo tu. Hakuna aliyemuona wala kumsikia Colins. Maisha yakaendelea.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Huku kwa Jelini yeye akabakiwa na sababu moja tu. Amekataliwa na wakwe sababu hana kazi. Akajiona mvivu. Wala la uchawi halikumuingia akili. Kwanza ni kama aliliacha palepale. Akakazana kazi yeye na mama yake. Mama Jema alijawa na furaha, Jelini akawa mtu ambaye hakumtegemea. Akili imechangamka, biashara akaijua vizuri na kujiongeza. Tabia kama za Kasa, akaiga. Kuamka alfajiri, kulala usiku ulioshiba, tena bila malalamiko.

Mashoga zake wote wenye masaluni yeye ndio akachukua kazi ya kuwapelekea kila bidhaa ambayo wangetaka kununua. Basi anakusanya oda kwa simu, anatuma kijana kushusha kwenye masaluni. Mama Jema hakuamini hiyo akili. Akawa anaingiza pesa kwa kujituma, na maneno yake mengi kwa wateja. Kila mteja yeye ni besti yake. Ukimkuta dukani, maneno mengi akikusifia kwa hili na lile na cheko, mpaka utanunua. Wakawa wanampenda. Kila anayefika dukani, anataka kumkuta cha maneno. Naye kuongea alijaliwa, hachoki na hakosi neno kwa kila mtu. Na hivi hakujaliwa dharau japo ni mzuri wa kuvutia, basi utapenda kumsikiliza maana hutahisi hila nyuma ya cheko lake.

Ataongea hapo na kutoa ushauri akikusifia, basi lazima umsikilize. Kwanza yeye mwenyewe alijaliwa ngozi laini kama mtoto mchanga. Akikwambia tumia kitu fulani, lazima ukubali ili uwe kama yeye, kumbe yeye ngozi na uzuri ni vya kuzaliwa. Akianza kusifia nywele alizonazo hapo, utanunua hata kama bei kubwa, ilimradi ukasuke ili upendeze kama yeye. Maisha yake yakaendelea akihangaika, na yeye hakumsikia wala kumuona Colins hata kwa bahati mbaya.

Ila habari za masaluni zilizokuwa zimeenea ni Kemi na Love kuwa wamemkomoa. Alitaka kuiba mwanaume wa Love, wakamuwahi. Wakajaribu kumchafua, lakini Jelini mtu wa watu, hayakwenda mbali. Ila akajua kwamba Colins anaishi na Love, kwenye jumba la kifahari, Kigamboni. Akabaki akimsononekea Colins wake, akawa hana jinsi. “Colins amemchagua Love kwa kuwa yeye amesoma ana mihela.” Ndicho kilichobaki moyoni mwake.

Maisha yakaendelea ila hakuacha kumkumbuka Colins. Hakupata mwanaume kama yeye. Mwenyewe alimuona mzuri kuliko kila mtu, halafu moyo wake ulimpenda sana Colins. Akabaki akisubiria aje atokee Colins mwingine.

Kila mwanaume anayemjia, sio mweupe. Akija mweupe, basi si mweupe sana kama Colins. Sauti yake na midomo pia vitakuwa na tatizo, havifanani na Colins. Hawaongei vizuri, ilimradi tu. Ila hakukata tamaa ya kuja kuwa na mtu wake. Biashara ikapanuka na yeye akawa wakusafiri kwenda kufuata bidhaa nje ya nchi. Sehemu mbalimbali ilimradi alete vitu vya tofauti nchini. Ikawa kweli biashara ndio kipaji chake. Alifanya kwa moyo na ikamkubali.

Kwa Kasa hakutaka hata kuhisi tena. Kwanza mwanae ndio alitibua kabisa. Hata kama kungekuwa na kimwanya, Kemi akasaidia kabisa kufunga, Kasa asijue ya mtaani. Kuwa mwanae ndiye anamnyima penzi la Jelini. Akajibakia peke yake na wala hakutaka kujua kilichoendelea kati ya Kasa na anti yake aliyemuunganishia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jema hakuacha kuwaombea na kuwasisitiza wawili hao mambo ya kanisani. Akawakaba, ikawa hakuna jingine analozungumza nao hao wawili isipokuwa kuanza kuishi ukristo. Uzuri Jema mwenyewe alionyesha ukristo wa vitendo wakaanza kumsikiliza. Shuguli ikawa mama Jema. Umwambie awe mkrito wa kukaa kanisani na nyumbani siku nzima ya jumapili asifanye kazi! Hapo pakawa pagumu.

“Ndio ujinga huo ninao uzungumzia mimi. Mnafundishwa nini humo kanisani siku nzima?” “Sio lazima mama. Tunaenda ibada moja tu. Masaa mawili, hayazidi matatu. Ukitoka, unaenda kutafuta pesa. Halafu mara moja tu kwa juma! Kweli ushindwe mama jamani! Mimi na watoto wangu wote tutakuwa tukienda kanisani. Mwenzio James kakubali.” Mama Jema akamtizama James, James akacheka. “Na usinigeuke James.” “Mimi mbona nimekubali!” “Sasa mwambie mama. Wewe anakusikiliza.” Wote wakamgeukia James.

“Mimi na familia yangu ni dini ya Jema.” “Acha bwana kusema hivyo James, wakati tulikubaliana vizuri!” “Haya basi. Sisi, familia yetu, ni watu wa Mungu. Jumapili, siku moja tu, hatutashindwa kumpa Mungu masaa mawili tu. Yeye ametulinda, amekua na sisi. Hata hizo biashara tunazohangaikia, ni Mungu ametupa.” Jelini hana mbavu maana ongea yake kama anayemnukuhu Jema, mkewe anamtizama tu.

“Au nimekosea mama JJ?” “Wewe mshawishi mama bwana, acha kuwa na wasiwasi na mimi.” “Uangaliaji wako ndio unanitia wasiwasi. Kwa hiyo mama Jema. Mimi na familia yangu. Tukiamka siku ya jumapili, sio kuwaza biashara. Tunaenda kumuabudu Mungu aliyetupa vyote, ndio ratiba nyingine zinaanza. Hata JJ anabarikiwa siku si nyingi.” “Makubwa! Haya huko kanisani ni wapi? Ndio huko wanakolia?” “Ni…” “Sasa hapo kazi yako imeisha, naendelea mwenyewe.” James akanyanyua mikono juu kama anayemuachia ukumbi mkewe.

Jema akazungumza nao hao watatu siku hiyo ya jumamosi asubuhi wote walijikuta kwa Jema akiwa ndio anamalizia likizo yake ya uzazi. Akazungumza nao mpaka watatu hao wakakubali kuanza kwenda kanisani siku ya jumapili, ila wakimpa Jema mashariti mengi juu ya huko kanisani, kama sio wakristo! Lakini Jema akawachukulia taratibu tu akiwang’ang’aniza na kuwatia moyo kwamba hawatakaa huko siku nzima. Akawaambia kanisa lao linazingatia muda. Akafanya ushawishi mpaka wakafika muafaka. Jema alifurahia sana. Kumuingiza mama yake kanisani! Kwake ukawa muujiza wa kama kumuombea kipofu na kuona.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakristo hao wakaanza maisha ya kanisani mara moja kwa juma. Angalau wakajitahidi. Mpaka Jeremy akawa akienda kanisani. Wakitoka wanakaa kula wote kwa pamoja, kisha James, Jelini na mama Jema wanaelekea kwenye biashara zao. Jema na mwanae pamoja na mama wa kazi ambaye aliletewa kumsaidia mtoto, wanarudi nyumbani na Jeremy. Akisha kula usiku na kuoga, Jelini anakwenda kumfuata kwenda kulala. Jumapili walikuwa hawafanyi kazi mpaka usiku mwingi. Maisha yakaendelea.

Kila Jambo Na Wakati Wake.

Mguu wa Bale ulikuwa umefika na alitakiwa kwenda kuwekewa na kujaribisha kutembea. Alishafanyia mazoezi hata kabla mguu wenyewe haujafika, kwani hakuacha kwenda mazoezini tokea apone kidonda. Huyo Bale alifanya mazoezi ya huo mwili  wake kwa kujituma bila ya kuchoka. Ukimwangalia tu, utajua ni mtu wa mazoezi. Aliweza kuishi na mguu mmoja akitumia gongo moja bila shida. Akajua kugeuka na kufanya yake kwa wepesi sababu ya kuzingatia mazoezi na wataalamu waliokuwa wakilipwa na Joshua hapohapo kitengo cha MOI.

Alipopata taarifa kuwa mguu wake umefika, anaweza kwenda kuwekewa, akamtumia ujumbe Joshua. ‘Mguu umefika. Nina mpango wa kwenda huko siku ya jumatano asubuhi mida ya saa nne baada ya kikao cha ofisini. Nakushukuru Joshua. Asante.’ ‘Anytime. Hongera.’ Akamjibu tu hivyo. Akajua yupo busy siku hiyo ya jumatatu, akamuacha.

Akaona amtaarifu na Vai. Ilikuwa bado mapema tu siku hiyo ya jumatatu. Hapohapo akampigia. Bale akashangaa anampigia simu mida hiyo, ila akapokea. “Sasa kwa nini usubirie mpaka jumatano na wewe ulikuwa ukisubiria huo mguu kwa hamu!?” Vai akaenda moja kwa moja kwenye lake bila hata kupoteza muda. “Si umesema upo unafanya round wodini wewe, mbona umepiga!?” Akaanza kucheka mwenyewe. “Madaktari wawili walikuwa wakibishana hapa, wamekutana wote wajuaji, naona wameamua kurudi ofisini kuwekana sawa, ndio warudi tumalizie roundi. Kwa hiyo tumekaa tu hapa tukiwasubiria. Sasa kwa nini unasubiri mpaka jumatano?” Akarudi kwenye lake.

“Jumatatu na jumanne panakuwa busy sana na vikao vingi hapa makao makuu. Ila jumatano baada ya kikao cha kitengo asubuhi, panakuwa pametulia, ndio naona niende.” “Kwamba ukiwaomba ruhusa kesho kwa jambo la muhimu hivi unaona watakukatalia?” Bado haikuwa ikimuingia akilini. “Hapana. Mimi bado ni mgeni Vai. Na najiona nitakaa sana hapa. Nataka kujifunza mengi bado nikiwa mgeni, ili isichukue muda mrefu kuweza kuaminiwa kwa makubwa. Kwa hiyo ni uamuzi wangu, hakuna wakunikatalia.”

“Au nikazungumze na mtu wa MOI akusubirie jioni ukitoka kazini?” Bado akasisitiza iwe mapema. “Usiwe na wasiwasi Vai. Mguu ni wangu mpaka kifo changu. Acha unisubirie tu.” “Eti nakuonea huruma, umesubiria muda mrefu hivyo! Nataka ufurahi.” Bale akacheka. “Mimi ninafuraha hata bila huo mguu.” “Utaongeza kitu.” “Najua. Lakini acha iwe siku ya jumatano, hata Joshua nimeshamwambia itakuwa siku ya jumatano. Sitaki niwe myumbishaji.” Hapo akaharibu kwa Vai. Akanyamaza, maneno yote yakaisha.

“Mbona kimya tena?” “Hata nikiongea chochote najua haitasaidia tena. Unamuheshimu sana Joshua, Bale! Chochote kinachomuhusu yeye hutaki kiharibike!” Bale akanyamaza. “Kwamba upo tayari usiweke mguu leo, ambapo mimi nakushauri, na nakuahidi kwenda kuzungumza nao wakusubirie mpaka uje, uondoke na mguu wako leo hii, eti mpaka jumatano ilimradi tu, usibadili kwa Joshua! Hudhani kuwa ataelewa!?”

“Nafikiri si yeye moja kwa moja. Nataka kubakia mtu wa maneno yangu, Vai. Nisiyumbe yumbe. Nikiamua kufanya jambo, nilisimamie kwa garama yeyote ile. Nipo kwenye kujifunza uadilifu, kufikiri kabla sijaahidi au kupanga. Ili ikitokea nakosea, basi nilipe garama mpaka nijifunze kufikiri vizuri kabla sijatenda nikiwa nimepima madhara ya mpaka mbeleni. Tafadhali naomba unielewe. Nimeshafanya haraka, na kuyumbayumba bila kuwa wa msimamo, nimeharibu mpaka baadaye zangu. Inanigarimu sana mpaka hata sasa. Acha nijufunze kuwa mtu wa maneno yangu.” Alianza vizuri, lakini hapo katikati akampoteza tena. “Sawa.” Vai akajibu akisikika anakubali ili yaishe tu hivyo.

Bale akajua. “Mbona kama umekosa raha?” Akataka kukataa, lakini akaona aseme tu kwa njia ya swali. “Katika huko kufikiria kwako kabla ya kupanga mambo, na mimi nitakuwa nikihusishwa?” Bale akatulia akijua lazima kuongeza umakini akizungumza na Vai. “Maana kama ukibakia na aina hiyo ya msimamo kwenya maamuzi yako ambayo unakuwa umeshapanga na kuamua kuyasimamia, na mimi nakuwa labda nina wazo la tofauti, itakuaje sasa? Au huoni tena maisha yetu ya pamoja?”

“Naona Vai. Basi niseme kuanzia leo, nitajifunza kukushirikisha mambo. Ili tuwe tunaamua pamoja. Si ni sawa mke wa Bale?” Ikawa kama sabuni moyoni kwa Vai. Ikaosha takataka zote. Akajisikia kupendwa haswa. Akacheka taratibu kwa furaha. Bale huyo, anajua kujishusha bwana. Anayo nafasi nzuri kimaisha. Kazi inayolipa vizuri kwamba kuna uhakika wa maisha ya kueleweka baadaye. Vai atake nini tena! Akabaki akijichekesha.

“Unacheka nini sasa?” “Nimefurahi kuitwa ‘mke wa Bale’.” “Si kushirikishwa kwenye maamuzi?” “Mimi nataka niwe mke wako kwanza. Mengine naona tutawekana tu sawa. Wewe sio mbishi.” Bale akacheka akifikiria. Naya angemsikia huyu! Bale si mbishi! Hata Bale mwenyewe akashindwa chakujibu, akabaki kimya tu, mwishoe madaktari waliokuwa wakiongoza roundi hapo wodini wakarudi, Vai akaaga kwa haraka na kurudisha simu mfukoni, akarudi kundini.

Siku Iliyokuwa Ikisubiriwa Kwa Hamu.

Bale alifika hospitali ya Muhimbili majira ya 3:30 asubuhi na kwenda mpaka kitengo cha MOI, akakuta Vai akimsubiria. “Sasa wewe nesi wangu, mida hii unasubiria mpenzi huku, cheti tutapata kweli?” Alikuwa amevaa sare zake za kiuuguzi. Akapendeza mwenyewe! Akacheka. “Nisingeweza kukosa. Nimeomba ruhusa. Usiwe na wasiwasi. Sasa mbona umependeza hivyo!” “Mbona unaongea kama si kitu kizuri?” “Mimi naona wivu bwana! Ndio kila mtu anakuona hivyo?” Bale akazidi kucheka. “Usijali. Nakuwakilisha vizuri.” Akajua kumpatia Vai, akawa akiishiwa manung’uniko.

“Kama hivyo sawa. Nishaingia ndani. Nishampanga kila mtu, hapa unasubiriwa wewe tu.” Bale akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha tararibu. “Mbona hufurahii tena?! Ujue kuanzia leo hutahitaji tena gongo. Unarudi kutembea kama kawaida. Yaani ukitoka kwenye ule mlango pale, unatoka bila gongo kwa kuwa umeshafanyiwa mazoezi yote na wote wanakusifia unafanya vizuri.” “Najua. Lakini naomba usiingie na mimi ndani. Nisubirie nje mpaka nitoke.” Vai hakuelewa. “Kwa nini?!” “Naomba tu usiwepo Vai.” “Kwa nini?” Bale akasita. Vai akaumia sana.

Akaona bora tu amwambie hofu yake. “Sitaki kukuvunja moyo Vai. Ili kama ikitokea sijafanikiwa kutoka na huo mguu, isikuumize. Najua na wewe ulikuwa ukiusubiria huo mguu kwa hamu.” Vai akaumia sana. “Nafanya kwa ajili yako Bale. Uwe na mguu, usiwe na mguu, mimi nitabaki kukupenda hivyohivyo. Sitajali. Nitasimama na wewe katika kila hali, na si kwa hili tu. Ni katika kila jambo. Mimi ni wako Bale.” “Basi twende wote ili nipate pakuegemea endapo chochote kisipokwenda kama tunavyo tarajia. Huu mguu ni wa garama sana, Vai. Kila mtu anausubiria kwa hamu, hata hao waliokuwa wakinifanyia mazoezi wanausubiria kama kitu cha ajabu sana. Nahofia kusije haribika jambo. Ukawa ni mguu sahihi lakini mguu wangu mimi ukashindwa kuupokea. Itakuaje?”

 “Naomba tusiazime matatizo ya baadaye Bale. Sasahivi, tuliposimama hapa, mimi nimefurahi kukuona wewe, na wewe umefurahi kuniona. Tupo salama. Si wagonjwa. Maisha yetu yanaendelea kama kawaida. Ukiwa na mguu, usiwe nao, sisi tupo sawa. Hakuna kitakachoharibika. Naomba matatizo ya baadaye, tuyaache yabakie hukohuko baadaye.” Hilo ndilo alilompendea Vai. “Ni sawa?” “Naona upo sahihi. Twende. Na asante kunifariji.” Wakaongozana mpaka ndani.

Haikuchukua muda mrefu. Mguu wenyewe ulikuwa laini kiasi ya kwamba haukuleta maumivu yeyote kwa Bale. Akatembea nao bila shida. Baada ya muda mfupi sana, wakaruhusiwa. Bale akatoka akitembea asiamini Mungu amemrudisha kwenye kusimama wima kama zamani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakatoka, na kumkuta Joshua na Jema wamesimama nje, pembeni kidogo kama waliokuwa wakiwasubiria. Walishituka, hawakutegemea. Yeye Bale kashituka kumuona Joshua pale. Maana tokea siku ya jumatatu alipomrudishia majibu ya, Anytime. Hongera.’ Hakumsikia tena. Ndio anamuona ametokezea hapo, muda na siku ileile aliyomwambia angekwenda kuwekewa huo mguu. Hamjui Jema. Kwa upande wa Vai yeye akashituka kumuona wifie pale na mtu mgeni kwake, hamjui Joshua. Wote wakabaki na mshangao wasijue wanashangaa watu wawili tofauti, waliopo pamoja. Bosi na msaidizi wake.

“Tulikuwa na kikao maeneo ya Posta mpya, kilipoisha tu, nikamuomba Jema muda mfupi, tupitie hapa ili nihakikishe kila kitu kimeenda sawa.” Muda wote huo Bale macho kwa Joshua, asiamini. Bwana Joshua akiwepo mahali huwa uwepo wake unatoshea. Alivyonyooka! Kisha kusimama kimamlaka kama anayejua yeye ni nani! Safi. Kuanzia utosi mpaka kiatu alichovaa. Hapo amesimama tu, amejiwakilisha vilivyo. Nadhifu haswa.

Vai akazidi kuchanganywa. Jema amemjuaje Joshua! Kwa nini Joshua amuombe Jema muda?! Na Jema naye akabaki amepigwa na butwaa kuona wawili hao bado wako pamoja! Hakujua kama baada ya mumewe kuwasha ule moto, bado wawili hao wangebaki kwa ukaribu ule tena wa kushikana mikono! Akabaki kimya akiwatizama.

“Usinge hangaika Joshua!” “Sio usumbufu hata kidogo. Nimefurahi kukuona unatembea vizuri aisee. Kumbe kweli mazoezi yanasaidia! Hongera.” “Halafu mguu wenyewe mzuri kila mtu alikuwa akiushangaa pale. Wenyewe wanasema hawajawahi ona mguu kama huu kwa macho ila tu mitandaoni. Imekuwa ndio kwa mara ya kwanza kuingia hapo kwao. Unanisapoti vizuri, sihisi maumivu hata kidogo. Nakushukuru Joshua.” “Nimefurahi kama umefaa.”

Akamgeukia Vai. “Kwa ushikwaji huo mkono, naamini wewe ndiye Vai.” Wakacheka na kujiangalia vile walivyoshikana mikono, wakaachiana kwa haraka. Hawakuwa hata wanajua kuwa wametoka wakiwa wameshikana mikono. “Ndio.” Vai akajibu akicheka kwa hofu kidogo, akijua Joshua anajua alimuacha Bale na kujifungia hotelini na Victor.

“Bale, huyu ni Jema, msaidizi wangu. Bila yeye, huwa kazi haziendi. Hapo alipo ananihesabia dakika, nitoke hapa. Kuanzia naingia kazini mpaka natoka, kila dakika yangu yeye ndiye anayeipanga nini chakufanya. Na pia ni mke wa James. Yaani wifi yake Vai.” Bale alishituka, mpaka akapaliwa na mate. Akaanza kukohoa mfululizo baada ya kusikia ni mke wa James. Joshua akajua.

“Aisee pole sana. Jema ana maji kwenye gari.” Jema ndio akajua anatumwa maji. Akatoka hapo kwa haraka. Wakawa wakimfuata nyuma. “Naamini kila kitu kitakuwa sawa.” Wakatoka nje wakakutana na Jema naye anarudi na chupa ya maji. Akamkabidhi Bale. “Nashukuru. Ila nataka ujue, sipo kumchezea Vai. Nampenda Vai. Na najua simstahili kwa jinsi nilivyoishi nyuma, lakini Jema, nilikosa, na nimekusudia kubadilika.” Wote kimya, Jema hakutegemea.

“Kwamba kumbe huyu Bale ndiye anayevunja ratiba za Joshua, asubuhi hii muhuimu hivi, ili aje kumuona yeye!” Hakutegemea kama Joshua ndio yupo karibu hivyo na Bale. Joshua bosi wake. Naya besti wake lakini hakutaka kabisa kuzungumzia Bale, ila na yeye alishajua hawana mahusino mazuri kwani Naya alishamueleza ubaya aliotendewa na kaka yake. Akaingiwa hofu fulani hivi. Akajikaza na kumgeukia Joshua. “Zimebaki dakika 5 tu. Tafadhali nakuomba usizidishe. Sitakuwa na muda mwingine tena. Natangulia garini.” Akaondoka Jema. Hapo alipo alikuwa amependeza haswa. Kiatu cha juu kama kawaida yake, usingejua kama ni mama JJ. Akaacha hapo harufu nzuri ya manukato.

Joshua na yeye akaona aage. Hawakuwa mbali na gari. Wakati anakaribia gari, Vai akamuita. Bale hakutegemea. Akamkimbilia akimuacha Bale nyuma. Joshua akageuka akiwa amekaribia gari. “Nampenda Bale. Sipo kumtapeli. Najua ulijua nili nili..” Akasita mbele ya Joshua akiwa anatetemeka. “Nimemuomba msamaha. Na nimebadilika.” “Labda nikuulize Vai. Maana sitaki ucheze na hisia za Bale. Unaweza kuwa umesikia mabaya mengi sana juu yake, ikakufanya ubweteke.” Akaanza Joshua kimamlaka na kuzidi kumtisha.

Jema akiwasikiliza tu ndani ya gari maana alikaa kiti cha mbele na dereva, Joshua hukaa nyuma, wao wasijue kama wanasikilizwa na Jema. Maana wakati wote hawazimi gari. Inamaana vioo vimefungwa kwa ajili ya A/C. Joshua akajua dereva na Jema hawatasikia mazungumzo yao, akawa huru kuzungumza na Vai. Kumbe Jema kwa makusudi alishusha kidogo kioo ili kusikiliza anachotaka kumwambia bosi wake. Vai naye hakuwa akimuona kwakuwa alikuwa amezibwa na Joshua mbele yake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Vai Mbele Ya Joshua. Joshua Anataka Kumuuliza Nini Vai ? Atafanikiwa Kujibu Maswali Ya Joshua na kumshawishi?

Jema Naye Amegundua Umuhimu Wa Bale Kwa Joshua. Itabadili Kitu?

Itaendelea.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment