Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 5. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 5.

Ukimya wa muda ukapita. Bale akiwa amelala vilevile, na Vai kushindwa hata kusogea 
pale mlangoni kwa aibu akijuta hata kwa nini alianzisha hayo mazungumzo. Baada ya muda Bale akakaa.“Njoo hapa.” Akimuonyeshea kwenye kochi alilokuwa amekaa. Vai akaenda kukaa kwa unyonye. “Matendo yangu yameshindwa kuongea na moyo wako kabisa?” Vai akapandisha mabega kukataa kinyonge. “Nimeshindwa kulala Bale. Nimebaki nikijiuliza. Nakosa raha. Natamani kukusikia. Nimerudia mara nyingi kukwambia nakupenda. Hujajibu hata mara moja! Nashindwa nieleweje.”

“Ni vile nilishindwa kutamka Vai. Ila nahisi mimi hisia zilibadilika muda mrefu hata kabla yako. Hayo mashaka uliyonayo sasahivi, yakutokuzaa, mwenzio nilishahesabu sio kitu.” “Bale!” “Ukilinganisha na vile ninavyokupenda! Hakika mimi sitajali, hata Joshua nilimwambia. Na ndio maana nilikwambia nilijilaumu ulivyoondoka. Nikajiambia ningekwambia mapema, pengine,…” “Wala si pengine. Ni nisingeondoka Bale. Mimi nakupenda sana.” Bale akacheka.

“Nakupenda Vai.” Vai akacheka. “Sasa hivi nimefurahi. Nimekusikia.” “Nakupenda na ndio maana nakujali wewe tu. Sijawahi jali mwanamke hivi, nafikiri ndio maana haikuchukua muda mrefu kujua wewe nakupenda.” “Sasa utafanyaje swala la watoto?” “Hivi umeshajua kuna yatima wangapi wanalelewa kwenye vituo vya Yatima hawana wazazi?” Vai hakutegemea.

“Bale!” “Ni kiasi cha kuamua jinsia, umri kisha kwenda kuomba. Hata ukitaka wakuanza kunyonyesha mwenyewe, utapata. Ukitaka wakiume au wakike, utapata. Si lazima ubebe mimba ndio uwe mama, Vai. Usifungwe hapo. Sisi tukipanga idadi ya watoto tunaotaka, na jinsia zao, na muda, tunaanzisha tu familia bila shida.” Vai alihisi mwili unatetemeka.

“Unanielewa? Kwamba ukitaka baada ya ndoa tuanze na wakiume, mchanga kabisa. Ukataka uanze kunyonyesha mwenyewe, tunaanzia hapo. Tunamchua huyo. Anakuwa wetu. Tukiwa tayari na wapili, hivyohivyo kama tunao kwenda kupata leba, ila inakua Mungu amewapitishia tumboni kwa mtu mwingine. Wote tunakua tunatumia ubini mmoja, wanakua chini yetu. Tunawalea kwa kadiri Mungu atakavyotuwezesha. Wanakua wetu. Basi.” Vai alipatwa na baridi iliyomfanya afe ganzi. Akabaki kimya.

“Unaona hapa ninapolala?” Vai kimya. “Ukiwepo hapa nyumbani, mto nageuzia upande huu, macho pale mlangoni unapolala. Hata kama sina usingizi, haichukui muda nalala, nikijua Vai wangu yupo sehemu salama. Na hivi unalalaga wakati wote unaniacha nacheka hapa, ndio inanifariji vilivyo Vai. Sikukuzwa sehemu yenye amani hivi. Sio kila wakati niliona wazazi wangu wakicheka kama hivi sisi. Vai wewe unaridhika kwa kila jambo, hata maji! Kweli watoto hawa wanakuja na kupita mikononi kwetu ndio watutenganishe! Mimi nimekataa. Ni bora kuwa na wewe, na haya maisha yetu. Acha mengine iwe ni baraka za nyongeza tu. Nimeridhika na wewe hivyo ulivyo.” Vai hakutegemea.

“Kumbe ni afadhali nimezungumza na wewe Bale! Sasa ulipanga haya yote uje uniambie lini!?” “Ukimaliza chuo.” “Bale wewe! Hudhani kwamba nilitakiwa kusikia haya mapema? Ili nitulie. Swala la kutokuzaa lilikuwa likininyima raha mpaka ujasiri mbele za wenzangu! Lakini sasahivi umebadili mtazamo wangu kabisa. Nashukuru.” “Sasa sio utoke hapa, uende kwa mwingine, umpe wazo langu, mkaanzishe naye familia.” Vai alicheka sana.

“Maana wanadamu hamkawii! Familia ni mimi na wewe Vai.” “Si rahisi hivyo Bale. Ni mpaka mtu akubali na kupokea kama hivyo wewe. Kwani yatima wameanza leo? Wanaolilia watoto si wapo tokea vizazi na vizazi? Lakini wengi wanateseka wakiingia kwenye ndoa. Manyanyaso. Wanaume wakitaka watoto waliozaa wao wenyewe. Mimi nishahidi Bale. Mwanaume huyu wa mwisho, nilikuwa siwezi hata kulala kwa raha. Hakuna tunachozungumza isipokuwa kushika kwangu mimba. Mchana na usiku ndio swali. Nilikonda kwa wasiwasi.”

“Basi huo ukurasa tunafunga kabisa. Tushajua ni sisi tu. Wengine wataongezeka juu yetu. Tena tutachagua sisi kwa muda na nafasi yetu.” “Umenitua mzigo! Ni vile tu hujui Bale. Na milele nitakukumbuka kwa hili.” Bale akacheka akimwangalia. Wakawa kama hawajui wafanye nini, mwishoe Vai akanyanyuka kwenda kulala.

Akaenda kujilaza kitandani akitafakari. Akasikia Bale akichechemea kuelekea hapo chumbani. Akagonga taratibu. “Umeshalala?” “Bado. Ingia.” Akafungua mlango. “Natamani kama…” Akasita. Vai akatoka kitandani akitamani hata amkumbatie. Japokuwa alikuwa amesimama kwa kusaidiwa na gongo, lakini Bale alilipa. Akajisogeza mpaka mwishoni mwa kitanda na kukunja miguu akimtizama kwa upendo.

“Nakupenda Vai.” Akajua hilo silo lililomleta. Vai akacheka taratibu na kuinamia magoti akaanza kuchezea vidole vyake vya miguu taratibu Bale akibaki kumtizama kama anayejishauri. Mwishoe akamsogelea. Akakaa pembeni yake.

“Haraka zimeniponza kwenye mengi, na wewe ni shahidi.” Akaanza Bale taratibu. “Hapa nilipo hisia zangu zinanituma mambo mengi, lakini naomba tusubiri Vai.” Hilo hakulitegemea. Alijua kufunguliwa kule kwa mlango, hatimaye usiku huo atampata Bale ambaye moyo wake ulishampenda kupita maelezo. “Tafadhali naomba unisubiri mpaka ndoa.” Akamalizia hivyo na kukata hisia zote za Vai. Akabaki ameinamia magoti ila akaitika kwa kichwa kukubali.

Bale akamuona vile alivyo nyongea. “Umekasirika?” “Hapana. Ila najiuliza ni lini hiyo ndoa!” Vai hakutaka kujivunga. “Ukimaliza tu chuo.” “Kwamba mpaka mwakani!?” Hilo swali likamfanya Bale asielewe. Vai ni mwanafunzi. Ila akaona aulize. “Nilifikiri unataka mpaka umalize chuo.” “Mimi naona ungemuuliza tu muolewaji.” Bale alicheka sana. Hakutegemea.

“Sasa wewe unasema ulifikiri, wakati mimi mwenyewe nipo hapahapa!” “Sawa Vai. Wewe ulitaka kuolewa lini.” “Kama na wewe, hata kesho.” Bale akabaki ametoa macho. “Mimi kwako sitajivunga.” “Na chuo!?” “Kwani mbona nipo hapa na bado chuo nakwenda? Unanisaidia kusoma na mambo mengine mengi tu.” Vai akaendelea. “Nimeishi na wewe hapa mbona hushangai hata likizo nilikuwa hapa na hakuna aliyenitafuta?” Hilo likamfanya Bale afikirie.

Nimeugua hapa mara ngapi, na mbona usimuone mama yangu kunitafuta ili aniuguze ila wewe ndio umehangaika na mimi mchana na usiku?” Hilo nalo likawa kweli. “Mimi nataka unioe, nitulie na wewe, wajue Bale ana mke wake kihalali, waache kukuvizia.” Bale hakutegemea. “Nani anivizie mimi?!” “Huko unakofanya kazi, unavaa vizuri sana, unapendeza na kuvutia, kanisani pia. Na huko unapokwenda kufanya mazoezi na kuacha misuli wazi, wadada wakikuangalia.” Bale akaanza kucheka, asitegemee wivu wa Vai kwake.

“Mimi nataka unioe, mimi, Bale. Katika hilo wala sitasubiri.” “Wazazi wakikataa?” “Kwani unawaoa wao?” “Vai!” “Hakika sikusubiri Bale. Chelewachelewa nitakuja kukuta mwana si wangu. Mimi nitakuja pata wapi mwanaume anayenipenda hivi kama wewe?” “Nitakusubiri.” “Basi mimi sitaki unisubiri. Nataka unioe.” Ilibidi tu Bale acheke akifikiria.

Ikabidi tu kuuliza. “Tunaanzia wapi?” “Kwa kaka. Twende nikupeleke kwa kaka. Mfahamiane. Akishakuona sio muhuni, na mimi nikamwambia nakupenda, kisha nikaomba unioe, najua atakubali.” “Sasa mbona unazungumza juu ya kaka na si baba!?” “Wazazi wetu wamempa dhamana kaka, anayo mamlaka naweza sema hata baba hafanyi kitu bila kumuuliza yeye. Sasa bora tuanzie kwake. Akikubali yeye, ujue kwengine huko ni taarifa tu.” “Sawa.” Bale akakubali bila shida.

“Lini sasa?” “Mama unataka ndoa wewe!” “Hakika na wewe, Bale, NATAKA. Tafadhali nioe nipumzike.” “Na mimi najua nitapumzika Vai. Namaanisha nikikwambia nakupenda.” “Basi sasa si unioe tu?” “Mimi sina kipingamizi. Wewe ndio familia nzima niliyo nayo, na Joshua. Na yeye anajua nakupenda wewe. Kwa hiyo mimi nakuachia wewe uongoze mambo, niambie tu chakufanya mapema ili nisimshitukize Joshua.” “Sawa. Basi ngoja nimtafute kaka kesho, nimuombe twende kwake.” “Sawa.” Acha Vai aanze kushangilia hapo mbele ya Bale, Bale akicheka.

“Wewe cheka tu. Ni mpaka upite nilikopita mimi, kisha umpate mtu kama Bale, ndio utanielewa. Nilikuwa namwambia Victor, Bale wangu ananipikia kisha anakuja kunichukua chuo nikale.” “Naona umeniuzauza huko kwa Victor!” “Mwenzio nilikuwa natamani ageuke awe wewe, ndio niwe naye pale siku ile. Nakupenda Bale wangu, halafu kuna jinsi umenizoeza, sina jinsi nikawa na mwanaume mwingine nikaridhika.” “Basi kweli tuone tu.” Wakajipanga hapo ndipo wakaagana kulala.

Shemeji.

Dunia Duara.

Watu husema hujui utakayekutana naye kesho. Dunia ni ndogo sana. Kuwa muungwana hata kwa mtu unayepishana naye barabarani, maana huwezi jua hata dakika tano ya mbeleni. Unaweza anguka hapo barabarani, yeye ndio akawa mtu wa pekee wa kukusaidia.

Ilikuwa majira ya saa 11 jioni wakati Bale na Vai wakigonga mlango wa nyumbani kwa aliyekuwa kaka yake Vai. Maana walifunguliwa geti na mlinzi wa zamu, Bale akavuta gari mpaka karibu na nyumba. Alikuta magari matatu hapo nje. Akahisi kuna wageni wengine ndani. Akatembea vizuri tu na gongo lake mpaka mlangoni, Vai akamtengeneza shati vizuri na kumkaribisha kabla hajagonga mlango.

“Mkewe mpole sana, wala usiwe nawasiwasi.” Akajaribu kumtia moyo. Bale akavuta pumzi kwa nguvu na kujipanga hapo mlangoni kuja kukutana na kaka mtu ambaye alipewa heshima na Vai kuliko hata baba yake. “Wana mtoto mdogo, tusibonyeze kengele mara mbili, tusije muamsha.” Vai akanong’ona.

Mara mlango ukafunguliwa. Ila ikawa tofauti na matarajio ya Vai. Kaka yake alishituka kana kwamba ameona jini mnyonya damu. “Unafanya nini hapa nyumbani kwangu wewe Bale!?” Vai akakunja uso na kumtizama Bale ambaye alibaki ameduaa na yeye.

“Mimi sijataka ubaya na wewe Bale, ndio maana uliniona nimekaa mbali na wewe tokea mwanzo kabisa. Sina ubaya, na sitaki matatizo na wewe.” Vai akashangaa sana. “Kaka James, huyu ndio mwanaume nilikwambia nitakuletea leo mfahamiane!” “Umechanganyikiwa wewe Vai!?” James alishakuwa mwekundu na alionekana ameingiwa hofu haswa.

“Unamleta huyu nyumbani kwangu kwa mke wangu na mtoto?! Kweli?” Wazi James alionekana amepaniki. “Nimekufanyia nini mimi? Kwa nini unataka kuleta matatizo nyumbani kwangu?” “James, sijaja kuleta matatizo.” “Mwanzo ndio kunakuaga hakuna matatizo wakati lako likikuendea sawa. Lolote likikaa vibaya, likaenda visivyoendana na wewe, huna ubinadamu Bale. Kila mtu anakufahamu. Unageuka katili kuliko simba. Huwezi kujizuia. Huna mipaka. Si kwa baba yako mzazi, wala ndugu mliozaliwa tumbo moja! Unaadhibu kwa kuangamiza.”

“Ndio maana mimi umeona nilijitenga kabisa na wewe. Sikutaka matatizo kabisa na wewe. Sikutaka kwa la kheri wala la shari. Kweli leo Vai unakuja kumleta huyu karibu na familia yangu!?” Vai alibaki kimya akitetemeka kama kifaranga kilicholowa maji kwenye baridi kali. Yeye na dada yake wanamuogopa sana James. Kuliko hata baba yao mzazi.

“Uliahidi kubadilika na kutulia Vai. Haya ndio mabadiliko yako?” “Tafadhali usimlaumu Vai, James. Bale aliyekutana naye yeye, siye unayemfahamu wewe. Nimebadilika na nime…” “Basi, kama kweli umebadilika, tafadhali ondoka kwangu. Na naomba unapoondoka, iwe amani Bale. Mimi sitaki vita na wewe wala visasi. Sitaki ugomvi tafadhali.” Ikawa kama anamsihi kwa hofu.

“Naomba amani kati yetu ila isiwe kunifuata kwangu wala karibu na familia yangu. Hata katika haya kama lipo limekukwaza, naomba nikuombe radhi. Ondoka kwangu kwa amani kabisa, kaendelee na maisha yako.” “Nimebadilika James na nampenda Vai.” “Tafadhali ondoka Bale. Hata kwa wazazi wangu naomba usifike. Nakuomba kwa heshima kabisa bila ugomvi wala kisasi. Kaa mbali na familia yangu.” Kwa hakika hilo alisisitiza.

“Waache wazazi wangu, hata wao hawajakufanyia kitu. Tafadhali nakusihi Bale. Kuwe na amani. Uondoke na usinitumie majambazi wala moto wa kutetekeza familia yangu. Mimi sitaki ugomvi na wewe, na nimekuaga hapa kwa amani kabisa, na Vai nishahidi.” Bale aliumia sana. “Tafadhali sana.” James akaendelea kusihi. Bale akaona aondoke tu.

Akachechemea kugeuka aondoke. “Bale amebadilika kaka.” “Unamjua alivyokuwa kabla?” Akasikia kaka yake akimuuliza Vai kwa ukali. “Nakuuliza Vai? Unamjua Bale wewe?!” Bale akaendelea kushuka ngazi, Vai akimtizama machozi yakimtoka. “Unaongea ujinga tu. Ulikuja hapa, ukazungumza hivihivi kuwa safari hii unatulia mpaka umalize chuo. Hata hujafika nusu ya chuo, umerudia tabia zako zilezile za wanaume. Unashida gani Vai wewe?!” Akaanza kumgombesha.

“Yaani chuo cha miaka miwili tu, kinakushinda kutulia na kumaliza! Unataka nini kitokee maishani ili utulie. Unajua alichofanya familia yake huyu?” “Amenisimulia, na …” “Unajua alichomfanya mtu aliyekuwa rafiki yake kipenzi, mtu wake wa karibu, pale walipopishana naye?” Vai akaendelea kulia.

“Huyu mtu ni mwema jambo lake linapomuendea sawa. Hana msamaha kwa yeyote aliyekuwa kinyume naye. Na ikifika kwenye hasira yake, hana anayemuangalia. Anateteketeza. Ndio maana mimi nimeishi naye mbali kabisa. Nilijitenga naye. Lakini wewe umeenda kuniletea matatizo nyumbani kwangu! Unaleta msiba kwenye ukoo wetu!” “Bale amebadilika kaka. Na yupo kanisani ana…” “Kwani baba yake mzazi, rafiki yake na ndugu zake aliwachoma moto akiwa wapi?!” James akamuuliza kwa ukali akimshangaa sana.

“Wewe vipi Vai? Unaongea nini? Alikuwa kanisani akipiga kinanda na muimbaji kabisa! Akaua familia yake yote, si kwa sumu! Aliwateketeza kwa moto kabisa. Yaani kuwaunguza mpaka kifo, akabaki na mtu aliyekuwa aking’ang’ania ni mwema. Naye alipompinga tu na kuwa kinyume naye, alimteketeza kwa moto. Kama nadanganya, muulize mwenyewe.” Vai akazidi kulia akiwa nje ya mlango, kaka yake amesimama mlangoni kama anayeulinda baya lisiingie.

“Kama huniamini, muuulize ni lini aliijua dini unayodhani anayo sasahivi. Swala la kanisani si jipya kwake. Amezaliwa na kukua kanisani. Acha upumbavu wako. Anaye dada yake. Lakini hata yeye anamuogopa, muulize hata kama anafunguliwa milango ya kwa familia ya dada yake na wanaishi hapahapa Dar. Bale ni tishio, kila mtu anamfahamu. Kweli unakwenda kumzoa huko na kumleta kwangu! Hakika sitakusamehe Vai. Ondoka, na wewe hapa usirudi. Tutakutana kwa wazazi. Ila, usiwahi hata kumuonyesha mlango wa nyumba ya mama, au kwa baba. Unanielewa Vai?” Vai alikuwa akilia sana maana kaka yake alikuwa akichemka haswa ila anagomba kwa sauti ya chini kama anayeogopa Bale asimsikie ndani ya gari.

“Hakika hatika hili nitataka uniahidi Vai. Maana wewe mtoto ni kama umekatwa masikio. Husikii la yeyote. Umesikia?” Akamvuta kabisa, Vai akazidi kulia mpaka Jema akatoka. “Naomba muachie. Tafadhali James. Mwache.” Akamwachia. “Sawa Jema. Lakini katika hili naomba zungumza naye na akujibu kama amesikia na kunielewa. Sitaki ampeleke huyu mtu kwa wazazi.” “Atakuwa amesikia. Eti Vai?” Akatingisha kichwa kukubali.

“Haya ondoka. Na ukahakikishe Bale hatufuati nyuma. Sina ugomvi naye. Ondoka Vai.” James akamfukuza Vai kwa sauti ya chini ila ya kitisho haswa, huku akiangalia lilipokuwa gari la Bale. Jema akamsaidia kumshusha ngazi kwani alikuwa akilia haswa. “Taratibu usianguke.” Jema akawa akimwambia huku amemshika mkono. Alipomfikisha chini ya ngazi akamuachia, Vai akarudi garini, wakaondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kilisikika kilio cha Vai tu garini. Bale akaendesha akiwa amepigwa na butwaa hajui aseme nini, mpaka kwake. Vai akashuka garini moja kwa  moja akaingia chumbani na kujitupa kitandani. Bale akamfuata. “Naomba nisikilize Vai.” Akageuka akilia sana. “Alichozungumza kaka yako, si uzushi. Ni kweli kabisa. Na ndio maana hata yeye nimemwambia, yeye anamzungumzia Bale wa zamani, wewe unamfahamu Bale wa sasahivi. Kaka yako anafanya yote hayo kulinda familia yake au yenu, kitu ambacho mimi nilishindwa. Mtoto wa kiume wa kwanza, kama yeye tu, lakini yeye yupo kwenye kujenga na kulinda, mimi niliangamiza familia yangu.”

“Yupo sahihi na katika hili, nimemuheshimu zaidi.” Vai hakutegemea. “Kwamba unaniacha Bale!?” Bale akatulia akifikiria. “Hunitaki tena?” Vai akarudia swali. “Hapana. Huko tulishapita Vai. Ila kuna kitu Joshua aliniambia hata juu ya Naya. Mungu hana shida na kusamehe, endapo ukitubu kwa dhati. Nimesamehewa na Mungu anayeona sirini. Lakini aliniambia, sitaacha kulipa garama ya makosa yangu.”

“Kwa Naya nilielewa na kuamua kumuacha kabisa kwa kuwa kwanza, hakuna jinsi nitakwambia, nafasi alizonipa Naya kujirudi hata kipindi cha uhai wa baba yetu, nikashindwa kujirudi kabisa. Naya anakumbuka hivyo vipindi vyote. Alifanya kwa hasira, upendo mpaka kunibembeleza, nitulie na kusubiri, lakini ilishindikana. Nikaharibu vibaya sana. Nimempokonya Naya, baba yetu ambaye hakuwa akijua kuishi bila yeye. Na najua maisha yake hayatakuja kurudi kuwa sawa, hata iweje bila baba. Labda katika ulimwengu ujao. Nimemkatili vibaya sana mpaka wakati mwingine natamani ubaya niliomfanyia baba ndio angekuwa mama, useme alizungumza kitu, akaniudhi. Baba yetu alikuwa mkimya sana, Vai. Nilimdhihaki na kumdharau vile nilivyotaka, lakini alikuwa kimya kabisa.”

“Kingine kinachonifanya nimuache Naya, ni ubaya niliomtendea yeye mwenyewe hata baada ya kifo cha baba. Ilikuwa mbaya sana Vai. Mno. Mimi mwenyewe nilikuwa nikikumbuka, siwezi kulala. Hayo yote, James kaka yako anayajua si kwa kusimuliwa, ni kwa kuishi kwenye hayo maisha akishuhudia kupitia Geb ambaye ni kama Joshua tu. Chochote kinachoendelea kwa Joshua ujue ni Geb, na Geb ni rafiki wa James tokea shule ya sekondari na akaja kumuoa mdogo wa James.” “Ni Nanaa. Tumekua pamoja.” Vai akamsaidia.

“Ewaaa! Nanaa. Kwa hiyo kwa kifupi, alichozungumza James, au ilipo hofu ya James, si kitu cha kufikirika, amenishuhudia nikitenda ubaya wa kupita kiasi.”

“Cha mwisho kinachonifanya niwe mbali na Naya, ni mumewe. Joshua katika hilo ameweka msimamo wa waziwazi kabisa, ni mpaka Naya mwenyewe atakaponitafuta. Hapa nilipo nazungumza na Joshua kila kitu, kasoro mambo yake na Naya. Hajawahi hata kuropoka kumzungumzia Naya kwangu, mara chache nikitaka kujua hali yake, jibu ni, ‘anaendelea vizuri’ au ‘Mungu anasaidia’, basi. Sijui alivyo, sijui chochote juu yake. Mimi, Bale, nimesababisha kweli ukoo mzima hawatutaki.”

“Lakini kuhusu wewe, wewe ni maisha yangu ya sasa na ya baadaye. Sitakaa mbali na James. Ninataka kuomba anipe nafasi.” “Hatuwezi kurudi tena kwa kaka wala kwenda nyumbani kwetu, Bale. Katika hilo siwezi kumkaidi kaka.” “Mimi sitamtafuta, ila nitarudi kupitia Joshua.” Hapo Vai akakaa.

“Kama alivyo Roho mtakatifu wangu mbele za Mungu, akinisaidia kuomba maana mimi sijui, ndivyo atakavyokuwa Joshua kwao. Joshua anajua ni kiasi gani nakupenda Vai. Anajua nimebadilika kwa kuishi na mimi, maana alinipa nafasi. Na uzuri yeye anaheshimika sana kwao. Nitazungumza naye na kumueleza ilivyokuwa, kisha nimuombe ushauri na kuomba akazungumze na James. Nitaheshimu kauli za James. Sitarudi kwake mpaka Joshua atakaponiambia yupo tayari niende.” Hapo Vai akafurahi sana maana japo hajawahi kukutanishwa na Joshua, lakini alishapata habari zake, akajua hakuna kitakacho shindikana. Alishajua yupo upande wa Bale, na Mungu ni baba yake, yupo upande wa Joshua, akajua mpaka hapo, huyo Mungu wake hata katika lao, atawarekebishia tu.

Kwa Joshua.

Ilikuwa mida ya usiku, simu ya Bale ilipoingia. Joshua alipoona namba ya Bale, alikuwa na Naya. Walikuwa kwenye wakati mzuri sana. Wawili tu, watoto wamelala. “Naomba nitoke, nipokee simu ya Bale. Si kawaida yake kupiga mida hii. Lazima ni kitu muhimu.” “Acha mimi niwapishe.” “Huna haja yakufanya hivyo. Acha mimi ndio nitoke.” “Hata hivyo ninataka kula kitu, njaa inaniuma. Naona wanao wamenyonya chakula chote.”  Naya akanyanyuka pale alipokuwa amemlalia mumewe na kuelekea jikoni.

“Kwema?” Joshua akapokea simu na hilo swali. “Nimegundua leo kuwa Vai wangu, ni mdogo wake wa mwisho James.” Joshua akafunga macho. “Nilikwenda kwake leo, aisee ilikuwa mbaya sana.” “Pole sana Bale. Natamani ningejua kabla hujakwenda kwake.” “Sikujua Joshua.” “Aisee James anakuogopa sana, na alishaniita kikao mimi na Geb, akiwa na wasiwasi wa Nanaa ambaye alishakugombeza, sijui kitu kama hicho.” Bale akawa hakumbuki.

“Alivyosimulia Geb, maana na mimi nilikuwa sielewi, wanasema ulikwenda ofisini kwake ukiwa na madai ya mali za baba yenu, ndio ukaishia kwa mkewe, sasa kaka yake alipojua, aisee ilikuwa mbaya. Alikuwa na wasiwasi wa waziwazi na akataka akaandikishe polisi kabisa ili chochote kikimpata Nanaa, wajue ni wewe, isiwe kama Naya. Yalikuwa ni mazungumza ya muda mrefu sana akitupinga akisema mimi nilizembea kufikisha taarifa zako polisi, ndio maana ulipomteka nyara Naya, polisi walishindwa kunisaidia. Akakataa kurudia kosa kwa dada yake. Ilibidi Geb amuonyeshe ushahidi wa kubadili ulinzi na umakini kwa dada yake. Ndio kidogo akatulia. Sasa ukiniambia leo ulikwenda kwake!”

“Aisee ilikuwa mbaya sana.” “Naweza kupata picha.” Kilichomtia wasiwasi Bale ni ukimya wa Joshua kama ambaye na yeye hajui chakufanya. “Joshua!?” “Tafadhali nipe muda nifikirie chakufanya Bale. Mimi nipo na wewe na nakuamini, na ni kwa sababu nilipata neema ya kukupa nafasi ingine baada ya kutambua na kujutia makosa yako. Nimeona mabadiliko yako kwa vitendo ndio maana unaona nakuamini. Naomba na wewe umuelewe James na umpe nafasi. Yeye anamfahamu Bale wa zamani. Hajabahatika kukufahamu Bale wa sasahivi. Itahitaji neema ya Mungu hata kuweza kuwa karibu na wewe. James anakuogopa si kwa kujisingizia, ni kweli anakuogopa HASWA. Tafadhali mpe muda.”

“Namuelewa Joshua. Namuelewa kabisa. Ila nampenda sana Vai.” “Naelewa. Ila ujue Vai amempenda mtu ambaye yupo kwenye kulipa garama. Haitakuwa rahisi, na yeye ajiandae. Na usimfiche kitu ili aweze kukusubiri. Na kwa upande wangu nipe muda. Usimtafute tena James wala kukamkaribia kwa namna yeyote ile mpaka nitakapokwambia. Lini! Sijui. Nitakapokuwa tayari juu ya hili, nitakujulisha.” “Nakushukuru Joshua. Na samahani kukuingiza matatizoni.” “Hapana. Ni changamoto tu na lazima tutakutana nazo. Usipokata tamaa, utafanikiwa.” “Nitasubiri. Nitakusubiri Joshua. Na nitazungumza na Vai. Uzuri ananipenda na yupo tayari kuwa na mimi. Najua na yeye atakuwa mvumilivu.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Naya alikuwa sehemu akisikiliza, walipomaliza akaingia na kumuona mumewe amebaki ameshikilia simu, kama anayewaza. Akamuhurumia. “Pole Joshua.” Naya akamtoa mawazoni. Akamtizama. “Naamini kila kitu kitakuwa sawa. Ni muda tu.” “Hivi ni kwa nini unahangaika hivyo na Bale!? Mimi mwenyewe nipo kama James tu. Namuogopa kuliko kawaida. Huyu mtu ni mwema, yake yakimuendea vizuri. Huofii atakuja kukugeuka pale mambo yake yasipoenda kama anavyotaka yeye?” Akajua alikuwa akisikiliza.

“Joshua, huyu mtu ni mkatili kuliko nitakavyokwambia. Hana utu wala ubinadamu pale anapotaka jambo lake liende anavyotaka yeye. Alinitesa vibaya sana akiwa na Malon, bila yakujali kama mimi ni ndugu yake! Na si mara moja, Joshua. Aliishi akinitesa na akijua nateseka, kisha kuendelea kunitesa. Kweli unapanga kumsogeza kwenye familia ya James isiyokuwa na hatia? Unataka kuleta misiba kwenye ukoo wa kina James wabakie ukiwa kama ukoo wetu?” “Naomba usilie Naya. Tulia nikwambie kitu. Njoo ukae hapa.” Naya akakaa.

“Naomba nikuulize swali. Na ufikirie kabla hujajibu.” Joshua akamtuliza. “Kama baba Naya angekuwa hai. Yupo pale Kiluvya. Unafikiri angefanya nini na Bale?” Naya akalia sana akikumbuka jinsi baba yake alivyohangaika na Bale mpaka kifo chake. “Lakini kumbuka mwisho wake na huyu Bale, Joshua. Kweli unataka tuangamie hivihivi?” “Simtetei Bale, ila kama ungepata nafasi ya kumsikiliza Bale yule aliyekuwa na bangi kichwani, haogopi mtu. Nia yake ni kuumiza watu akitaka kufikia yake, ndio ungegundua hakuwa amekusudia kuua. Hakutaka kumuua baba yenu ila kama kumkomoa. Malon yeye ndio alikuwa na agenda ya kuua, akatumia hasira ya Bale kutekeleza azma yake.”

“Na kumbuka wakati huo Bale alikuwa ameshaharibiwa hata fikra yake na bangi. Alifanya kile bangi inamtuma afanye. Sitetei, ila nataka ujue nilipopita mimi mpaka nikapata neema yakumpa nafasi ya pili. Na kingine, huwa kila wakati najiuliza swali kama nililokuuliza wewe. Kama baba Naya angekuwepo mwenyewe, angefanya nini? Hilo ndilo linanifanya nisizembee kwa Bale, na nafikiri ndipo nilipobeba roho ya ubaba kwa baba yenu Naya. Alikuwa yupo radhi kufa, ili akamuokoe Bale. Hakuogopa mauti. Alikuwa tayari kukabili kifo, ilimradi tu akamuokoe Bale. Na ndio katika kipindi hicho, ndipo nikapata sababu ambayo nimebaki na Bale mpaka sasahivi.” “Sababu gani?” Naya akauliza.

“Baba Naya akiwa kwenye mfungo, akimsihi Mungu rehema juu ya Bale, aliniapisha mbele za Mungu, juu ya watoto wake. Aliniachia nyinyi wote. Naya, yule mzee alinisihi mbele za Mungu, nakunitaka nimuahidi sitakuja kubadilika kwa watoto wake. Nyinyi wote, ni kama aliyekwisha ona mwisho wake tokea zamani. Akajua yeye atakufa, atawaacha nyinyi watatu. Na alinipa uhuru wa kukataa. Lakini nikakubali. Nikijua Mungu atanisaidia. Na ukweli sijawahi kujuta hata kwa Bale. Hajanipa sababu ya kutomuamini tena tokea nianze kutembea naye. Mungu wake amenionyesha waziwazi, amemsamehe na anatembea naye, mpaka nikaona wivu juu yake.”

“Siku moja tulikuwa hapa, ile siku tuliwaalika wakina Magesa na James waje hapa tumshukuru Mungu kwa sababu ya wewe kupata ujauzito, likatokea lakutokea, kina Jema wakaondoka baada ya Magesa kuzungumza vile na Jema. Unakumbuka nilikuaga nikakwambia lazima nitoke nje nizungumze na Bale?” Naya akakubali akilia.

“Naya, sikuwa nikijua ni nini kilikuwa kikiendelea kwa wakati ule, lakini Roho wa Mungu aliniambia nilazima, nimpigie simu Bale, nimwambie bado hajamalizana naye. Na anao mpango juu yake.” “Joshua!?” “Hakika Naya. Na jinsi nilivyokuwa nimesukumwa, halikuwa jambo la kumwambia baadaye, ilikuwa ni haraka. Ilinibidi baadaye, nafikiri hata mwezi ulipita, nilimuuliza Bale ni nini kilikuwa kikiendelea usiku ule. Maana ilikuwa ni kama Mungu anaokoa kitu.”

“Ndipo anasema alifika mahali, alijawa na majuto, hofu akijua ameharibu sana hapa duniani, hana jinsi ya kuja kutengeneza tena, amepoteza kila mtu. Na neno samahani pekee katika ulimwengu huu halitakaa likatosha, akakusudia kujiua. Pale nilipompigia simu, alisema alishakuwa tayari kujiingiza kwenye kitanzi, ajiue.” Naya alilia sana.

“Sasa najiuliza, kama huyu Mungu mwenye enzi YOTE, amemsamehe, na bado anamipango naye, mimi ni nani mpaka nizuie, au kupinga au kutokubali kutenda kazi na Mungu? Kwangu ni heshima Naya. Nahesabu Mungu ameniamini naweza kuhusika na mtu kama Bale, akaleta mabadiliko. Na hata leo mimi nikikataa kusimama na yeye, nakwambia kabisa, Mungu atainua mtu mwingine kutimiza kusudi lake, kama kwa Sauli aliyekuwa akiua watu wa Mungu, kanisa, mpaka Yesu akamtokea na kumuuliza, ‘kwa nini unanitesa?’ Kuna waliosimama na Sauli, ambaye ni Paulo, mpaka akafanya kanisa kusimama imara mpaka leo na kuna waliompinga. Lakini si kusudi la Mungu limesimama?” Joshua akaendelea taratibu tu bila kutaka kumtibua mkewe.

“Mimi nilikataliwa na watu wa nyumbani kwetu. Lakini kusudi la Mungu kwangu si liliweza kutimia. Utukufu wa Mungu unajitangaza kupitia mimi, mpaka mwenyewe huwa naogopa na wewe ni shahidi Naya. Lakini Mungu mwenyewe alikusudia KUSUDI lake litimie kupitia mimi, hata wale walionifahamu walipokataa, alitumia hata misikiti kunilinda, na kugeka nyumba yangu ya kulala, japo makanisa yalishindwa.”

“Nilijua misikiti inayogawa sadaka na chakula siku za ijumaa. Nilijua muda gani wa swala, muda gani na wapi pakujificha nikalala salama mpaka asubuhi. Ninachotaka kukwambia ni hili, hakuna wakuzuia kusudi la Mungu. Akiamua kufanya jambo lake, kwa hata vile visivyostahili, hakuna wakumzuia. Ni aidha ukubali kutenda naye kazi, ili akiwa anapita kwa mlengwa na wewe uliyekuwepo karibu na huyo mtu upate hata vimanyunyu vya baraka. Maana mimi namjua Mungu. Hawezi kukutumia bure. Anakutumia haswa, ila ni mzuri sana kwenye malipo. Ila kama ukishindwa, ni bora ukae pembeni kabisa, mwache kusudi lake litimie.”

Ninachokuhakikishia Naya, Bale ni Mungu aliyepo kazini na ipo siku watu watashuhudia kwa macho, wasiamini kama Mungu anaweza kufanya jambo jipya kwenye visivyostahili. Historia tunayoisoma juu ya Sauli, nahisi, Mungu anataka kuirudia, watu waishuhudie kwa macho. Bale amebadilika, Naya. Ni msikivu, mvumilivu na anaweza kufikiria mtu mwingine mpaka huwa wakati mwingine namuhurumia.”

“Alitakiwa kupata mguu mwezi mmoja uliopita. Ule mguu ukawa tayari kwa ajili yake kabisa. Ukamfaa. Siku aliyotakiwa kwenda kuwekewa, akakutana na mtu ambaye yeye hana mguu hata mmoja na ule mguu ungemfaa yeye. Bale akaomba apewe yule mtu, yeye akasema atasubiri. Hilo nimekuja kujua siku nimempatia kazi, aliponiomba aanze kazi akishapewa mguu. Bila kufikiria nikamwambia, lazima aanze kazi mguu utakutana naye mbele ya safari.”

“Maana nafasi yenyewe ilinijia kimaajabu, nikajua tu ni Mungu wake ameamua kumpa hiyo nafasi ya kazi. Maana ni kama huyo kiongozi wao wakitengo cha HR mwenyewe katika mazungumzo yetu akawa akinilalamikia hilo pengo na kuniambia bado hajaweza kuliziba, linamcheleweshea kazi. Moja kwa moja akili ikanikumbusha Bale. Ikawa kweli ni yake, kwenda tu, wakampenda. Sasa jinsi alivyojiuza vizuri, nafikiri na Mungu wake alikuwa amekusudia kumpa yaliyo juu, hakika wamemuanzishia malipo na marupurupu ya juu sana, Bale mwenyewe alinipigia akilia kwa hofu. Hata hakutegemea, maana alitaka kuwatajia pesa ndogo endapo wangemuuliza. Sasa turudi mwanzo alipotaka asubiri mguu na mimi kumwambia asisubiri mguu. Akakubali japo nilijua hataki kuonekana kazini ambayo ni sehemu ngeni, kama ni mlemavu, ila akakubali.”

“Ndipo sasa baada ya kama siku tatu mbeleni nikakumbuka alitakiwa awe alishakuwa na mguu! Ikabidi sasa kumuuliza, ndipo akanisimulia hicho kisa. Kwamba aliona bora ampe yule jamaa mguu, ili angalau na yeye aweze kusimama kama yeye. Sikutegemea Naya, kwa sababu Bale alikuwa akisubiria kwa hamu sana huo mguu. Na nilikwisha lipia, lakini Bale yule tuliyemjua ni mbinafsi, anaye angalia yake tu, aliugawa ule mguu kwa aliyeona anauhitaji zaidi yake!”

“Anatembea na mguu mmoja mpaka leo, akisaidiwa na gongo, na anafanya kazi bila malalamiko. Na huko kazini kwake nimeambiwa na bosi wake, anajituma kupita anavyotumwa. Na mwepesi kuelewa. Ila na mimi nilivyojua amegawa mguu wa kwanza, nimeagiza mguu wa pili uje bora, kuliko wa kwanza. Umegarimu sana, lakini nimetaka uwe na uwezo mkubwa, akiwekewa uwe na uwezo kama mguu wake. Usimchukue muda mrefu kuuzoea. Hata leo akitaka kuwa mwanariadha wa dunia, basi huo mguu usimzuie. Na nimefanya hivyo makusudi ili tu kumtia moyo.” Naya akaondoka kabisa hapo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Vai alipoambiwa majibu ya Joshua, kwa upande fulani akakata tamaa. Hazai! Lakini Bale amempokea. Sasa leo kaka hamtaki tena! Hilo likamnyong’onyeza kabisa Vai aliyepewa uzuri wa namna yake, lakini hofu ya kushindwa kuzalia wanaume watoto, ikamfunga nakubaki akijidharau. Hapo kwa Bale aliona ndio mwisho kabisa, ukizingatia alishajaribu kwa wanaume aliodhani ndio wangemkimbilia! Waliokwisha kuwa na familia zao, wanatafuta tu starehe! Victor akamrudisha chini kabisa.

Akabaki amenyong’onyea. “Tafadhali tuwe wavumilivu, kila kitu kitakuwa sawa.” “Usije nibadilikia Bale. Ukaona kwangu haviwezekaniki, ukakimbilia kwenye urahisi.” “Siwezi kubadilika kwa sababu kwako sipo kwenye majaribio. Sitafuti tena kwa kuwa nimeshakupata wewe. Hilo zoezi la wanawake kwangu nimefunga na Mungu wangu ni shahidi. Katika hilo tafadhali usitie shaka.” Akazidi kumbembeleza na YEYE akihofia Vai asije tafuta mwingine mwenye historia isiyo kama wake. Ukizingatia uzuri wa Vai! “Hakuna mwanaume atashindwa kumpokea kwa mikono yote miwili. Mimi mlemavu, halafu jamii inanihesabu ni muuaji! Ataishi na hiyo historia ngumu mpaka lini!” Wawili hao wakajikuta kila mmoja amekwama kwenye insecurities kwa sababu ya maisha waliyoishi nyuma na kusahau thamani yao.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kitakacho Endelea?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment