Akufaaye Kwa Dhiki, Ndiye Rafiki Wa Kweli.
Akapiga tena na tena
bila mafanikio. Akiwa katika kumsaka kwenye baa nyingine, simu ya James
ikaingia. “Nina hali mbaya James, tafadhali naomba
tuzungumze wakati mwingine.” “Nimepiga kutaka kujua jinsi ya kukusaidia! Jema
ameambiwa na mama yake kinachoendelea. Nataka kukusaidia.” “Nashukuru. Huyo
aliyekuwepo na Jelini, anaitwa Doro. Alikuwa akipokea na kukata. Alipopokea mara
ya mwisho na kunitukana, amenikatia, na sasahivi simpati tena kwa simu.”
“Umejaribu kumuuliza kama yupo na Jelini? Isijekuwa hayupo naye, unahangaika
kumtafuta ambako hayupo.”
“Umenipigia
ukisema unataka kunisaidia si kunichanganya zaidi James. Acha kuni…”
“Basi Colins. Nilitaka kukusaidia ili ufikiri zaidi.” “Hivyo hunisaidii ila
unataka kunichanganya zaidi. Maana ni kama unataka kuniambia pengine amerudi
kwa yule mzee!”
James akanyamaza ndipo Colins akajua ndicho alichokuwa akimaanisha.
“James?”
“Mimi nilitaka ufikiri zaidi. Inaweza kuwa sivyo. Ila uwezekano upo. Maana
anaweza hisi wote ni walewale tu. Alijaribu kwake ikawa ni swala hilohilo
mwanamke aliyekuwepo kwenye mahusiano naye tokea mwanzo, na kwako ni yale yale.
Ila tofauti yako na yake, mwenzio alikuwa akijitahidi kuwa naye. Na ndio maana
nilikwambia Colins, weka mambo ya nyumbani kwenu kwanza sawa ndipo urudi kwa
Jelini. Sasa ona tulipo sasahivi.”
“Yule mzee sio
mwenzangu na kwa taarifa yako tu, Jelini aliachana naye ramsi jana. Na leo
nimeenda kwake, Jelini hayupo huko.” James alishituka, hakutegemea. “Umechanganyikiwa wewe Colins!?” “Hakika nimechanganyikiwa na wewe unazidi kunichanganya, wala
husaidii.” “Ujue yule mzee atakuja kukuua kweli!” “Sijali. Na kingine James, japokuwa unatamani sana kunilaumu, ila kwa
sasa haitasaidia. Na kwakuwa sidhani kama mambo ya nyumbani kwetu yatakuja
kuisha. Wamenyweshwa sumu mbaya sana juu ya Jelini. Hawamtaki kwenye
ukoo. Sasa kwa kuwa wao wameshatamka wazi kabisa, hawatakaa wampokee, basi namuoa
kwa haraka sana. Sina sababu ya kusubiri tena.” James hakutegemea.
“Colins!?”
“Sasa nasubiria nini tena James? Familia nzima hawamtaki. Mimi ndio muoaji.
Pesa ya kuoa ninayo. Sina chakusema namsubiria baba wala mama. Sasa kama hutaki
kunisaidia nioe, uniambie sasahivi na wewe nikuweke kundi moja na familia
yangu.” “Naona tuanzie kwenye kumtafuta kwanza Jelini.” “Jelini nitampata tu.
Najua mimi ndiye niliyemrudisha kwa Doro, naenda kumfuata mwenyewe. Ukiweza
kunisaidia sawa, kama huwezi basi.”
“Ulitaka
nifanyaje?” “Nakutumia namba ya Doro, naomba uende ofisini, tumia mitandao ya
kazini, niangalizie mara ya mwisho kuzungumza na simu yangu, alikuwa wapi. Na
nipe taarifa zake kamili.” “Sawa.” James akaitika na kukata simu, safari
ya ofisini kwao na yeye ikaanza, ili kusaidia kumsaka Doro.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mida ya saa saba
usiku, mfanyakazi huyo wa kuajiriwa, na kesho yake saa mbili kamili asubuhi
anahitajika kazini, ndio akawa amejua baa alipo Doro, akawasili hapo. Hapakuwa
mahali pachini. Hoteli nzuri tu tena ya kitalii, akatafuta upande iliyopo baa
ambako kuna live music. Bendi ilikuwa ikitumbuiza. Akaanza kusaka mpaka
akafika kwenye meza aliyowakuta kina Doro, wanaume wengine ambao hata yeye
alikubaliana na Jelini, ni wa maana hata kwa kuwatizama hapo na pombe zao.
Walionyesha pesa ipo. Meza ilijaa vinywaji vikali na bia za kawaida pamoja na
nyama choma. Kwao ilikuwa ni kama ndio panapambazuka. Kelele na cheko za
kilevi.
Walikuwa
wameunganisha meza, akamuona Jelini amekaa katikati yao. Akamsogelea mpaka
pale na kumgusa. Jelini alipogeuka na
kukutana na Colins, alishituka sana. “Mimi sijafanya jambo baya.” Wazi alikuwa
ameshalewa sana. Wote wakawageukia wao. Jelini mbabe kwa wanaume, anazungumza
hivyo na mwanaume! Ikawatia hamasa yakumtizana huyo Colins.
“Twende.” Akamuambia hivyo. “Mimi sijafanya
jambo baya. Nilikuwa tu hapa. Na wala sijalewa. Nimekunywa kidogo tu kama
kujituliza uchungu wa kukataliwa.” Akaanza Jelini. Kama kawaida yake akilewa na
machozi hayapo mbali.
Akaanza kulia kuwa
yeye hampendi. Anamtesa moyo wake bila sababu. Hamthamini. Anampenda tu Love,
yeye hampendi. Hamjali. Akaongea mengi akilia walevi wenzie wakimpa pole na
kumtuliza. “Mimi bora uniache tu, niendelee na
maisha yangu, kuliko kuendelea kuteseka nikijua upo kwenye dunia ninayoishi
mimi, halafu umemchagua mwanamke mwingine sio mimi.” Akaendelea kulia,
hataki kuondoka na Colins. Akarudia tena yale maneno mazito anayopenda kuyasema
kwa Colins akiwa amelewa, na yakaweza kuukamata moyo wa Colins. Jinsi
Jelini alivyozungumza mpaka wenzake aliokuwa akinywa nao, wakashangaa. Alisema
kwa kumaanisha kabisa tena bila hata aibu, akimtamkia Colins.
Lakini Colins
akasisitiza nilazima waondoke. Mabesti zake wakaongeza nguvu kumwambia amuache.
“Sisi wote tupo hapa leo kwa ajili ya Jelini. Tulimmisi ndio tumekuja
kumkaribisha tena chamani.” Colins akawasikiliza na kurudisha macho kwa Jelini.
“Simama twende.
Unaondoka na mimi Jelini. Sitakuacha hapa.” Akachukua pochi yake, wenzie
wakimlaumu kwa nini anamchukua wakati bado ni mapema sana. Akamshika mkono,
akasimama bila ubishi na kumuongoza njia mpaka nje kwenye gari yake. Wakati
anamfungulia mlango, akaanza kutapika. Alitapika Jelini kama bomba.
Akamshikilia kumsaidia asijichafue zaidi maana alishajitapikia. Simu ya mama
yake Jelini ikawa inaingia, hawezi kupokea amemshikilia asikalie matapishi
yake.
Baada ya hapo,
akamfuta na shati lake alilokuwa amevaa akavua ili kumsafisha, akampandisha
kwenye gari, yupo hoi kwa pombe na kutapika. Ikabidi afungue vioo vya dirisha
kwa harufu kali.
Akarudisha simu ya
mama yake. “Nashukuru Mungu nimempata. Lakini anahali
mbaya sana. Tafadhali naomba nisimrudishe hivi nyumbani. Acha akalale, akimka
na kujisikia vizuri, ndipo nimrudishe nyumbani.” “Unauhakika Colins? Naweza
kuja kumchukua mimi mwenyewe.” “Hapa alipo amejawa matapishi, amelewa
hajitambui. Kweli Jeremy amuone akiwa na hali hii? Maana ni wa kubeba kabisa.”
“Na alimuahidi mwanae anaacha pombe!” “Tafadhali naomba mtaarifu na James. Acha
nimpeleke akampumzike. Tutazungumza kesho.” Akaendelea kukanyaga mafuta
mpaka kwake. Na akajiambia hatamwambia mzee Kasa.
Kwa Colins.
Alimfikisha kwake
akiwa amelala, akamtoa garini mpaka bafuni. Ilibidi amtoe tu nguo, amuogeshe.
Alikuwa akinuka vibaya sana. Matapishi ya pombe. Alikuwa hajitambui.
Akamsafisha mpaka akaridhika, akamuweka chini. Akamkausha na kumvalisha tsheti
yake na kumuweka kitandani, akamfunika vizuri, akapotelea usingizini kama
mzigo.
Colins akabaki
akisafisha na kufua nguo yake aliyotapikia. Akafanya yote ndipo akarudi
kitandani na kubaki akimtizama. “Kweli Jelini ni mzuri. Anavutia kila
mahali!” Ndipo akili ikaanza kumrudisha kwenye umbile la Jelini aliloliona
likiwa tupu. Akabaki akiwaza mpaka akapitiwa na usingizi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Alam ya kazini
ikamuamsha akiwa tu ndio amelala. Akajivuta hapo, kisha akakumbuka na James
hayupo ofisini. Akakurupuka. Akaandika ujumbe na kuuacha pembeni ya Jelini
kwamba akiamka akutane nao. Akajiandaa, mpaka akamaliza, Jelini amelala kama
mzoga. Akatoka kwenda kazini kuweka mambo sawa kisha arudi alete chakula, kisha
arudi tena kazini.
Alirudi mida ya saa
nne na nusu, akamkuta bado amelala vilevile kama ndio saa nne usiku. Akamtizama
hapo, alikuwa amemletea supu. Akaiweka mezani, akatoa ujumbe wa asubuhi akaandika
mwingine, akatoka. Kwenye mida ya saa nane ndipo Jelini akafungua macho
nakuanza kufikiria alipo. Akakaa kwa haraka akiwa amejawa hofu. Alishituka sana
alipojigundua hajavaa hata chupi na yupo na tisheti tu, hajui alipo, sehemu
ngeni. Akaanza kulia akijua ameshabakwa.
Akiwa kwenye hali ya
paniki, akaona karatasi pembeni yake. Akaichukua. ‘Jelini.’ Nje ilikuwa na jina lake akajua
inamuhusu. ‘Nimeweka dawa za kichwa
mezani pamoja na supu. Ukiingia bafuni utakuta mswaki wako nimekuwekea pembeni.
Mataulo masafi yapo kabatini, chukua nguo yangu yeyote itakayokufaa uvae baada
ya kuoga. Kisha kula na meza dawa kabla kichwa hakijaanza kuuma. Nimeenda
kazini. Mida ya saa 12 jioni nitakuwa nimerudi. Tafadhali nikukute hapo nyumbani.
Colins.’
Jelini akashituka kujua yupo kwa Colins. Akajaribu kuvuta kumbukumbu
kujua alikuwa wapi, imekuaje yupo pale bila mafanikio.
Kichwa kikaanza
kugonga kama kengele wakati kumbukumbu zikimrudisha alipokuwa akinywa na kina
Doro, hofu ikazidi kumuingia na aibu. Hakufanya hatua zote alizoandikiwa. Ila
kumeza dawa na kusafishwa kinywa. Akarudi kitandani, akazima kama mshumaa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Alikuja kufungua
macho, ilishakuwa usiku Colins anajikausha kama aliyetoka kuoga. Akajigeuza
upande wa pili, Colins akajifunga taulo na kumsogelea upande aliogeukia.
Akamkuta akilia taratibu. Alipomuona tu Colins akaingia ndani ya mto kama
anayejificha. Colins akajipaka lotion na kuvaa nguo ya chini pamoja na kata
mkono. Akaenda kukaa pale kitandani upande alipokuwa amegeukia.
“Vipi kichwa?”
Akamuona anapandisha mabega kukataa. Akamtoa ule mto kichwani. “Naomba
unisikilize sababu ya kuchelewa kuja kukuchukua nyumbani.” Jelini akabaki
amelala kifudifudi ameficha uso. Colins akamueleza ujio wa wazazi, bibi na
babu. “Nikidhani babu yupo upande wangu, kumbe Love alishawapa taarifa zako
nyingi, za kutisha na kumuogopesha mpaka babu. Ndio ikabidi aje
azungumze na mimi. Haikuishia hapo, akaja Love na wazazi wake kuongeza
ushahidi wa kile kinachozungumziwa.” Jelini alishituka mpaka machozi yakakata.
“Ilikuwa ni kesi
kubwa iliyoendelea kwa muda mrefu kwa sababu ni kama Love alionyesha anauhakika
na anachozungumzia, kuwa ameelezwa na mtu wa karibu sana na mzee Kasa, ambaye
na yeye ni muhanga wa mahusiano yako na mzee Kasa.” Jelini alitamani ageuke
kuwa upepo, apotee duniani.
“Akaeleza baa zote
ambazo huwa unashinda huko na waume za watu kama wale niliokukuta nao jana.”
Hapo tumbo likaanza kumuuma. Hofu na aibu. “Iliendelea hiyo kesi mpaka ikabidi
mimi niwaage. Na ukumbuke walikuwa hapa kwangu. Kesi ikiendelea hapa. Nikawaambia
ni lazima niondoke, nikufuate. Tulikuwa na miahadi. Kama ungekuwa na simu,
ningekupigia kukutaarifu kinachoendelea, lakini nikawaambia huna simu, na sina
jinsi ya kuwasiliana na wewe, na nimeshakuchelewa, lazima niondoke. Hapo
napo pakachukua muda mrefu sana.”
“Kufupisha habari,
ndipo nikafanikiwa kuwatoa hapa nikaja kwenu. Nikakusubiri mpaka saa nne usiku,
maana niliambiwa uliondoka na Doro. Ndipo nikaanza sasa kukusaka kwenye
mabaa yote niliyosikia Love akishitakia kuwa ndiko unakoshinda
huko. Kote waliniambia wanakufahamu, lakini hawajakuona muda mrefu. Ndipo
nikakufuata mpaka nyumbani kwa mzee Kasa, nikijua ulirudi huko.” Jelini
alishituka, nusura roho itoke.
“Nako huko nikagonga
mwamba. Ndipo James akanisaidia kuitafuta simu ya Doro kujua alipo. Maana mara
ya mwisho alipokea, akanitukana na kuikata.” Jelini akazidi kuingiwa hofu na
aibu. “Mambo yamefika mpaka na kwa kina Shem! Najificha wapi mimi!” Akawaza
akiwa bado ameinamisha uso kwenye godoro.
“Hatimaye nikakupata.
Ulitapika sana na kujitapikia pia. Ikabidi kukuosha kabla sijakuweka kitandani.
Kwa hiyo, sikuwa nimemchagua tena Love badala yako. Sitafanya hivyo kwa
sababu nakupenda wewe Jelini. Narudia tena, na naomba hili usije wahi sahau.
Wewe ni mke wangu, mama watoto wangu. Nilikwambia nikiamua kuwa na wewe,
sitakuacha mpaka utanihurumia. Nakupenda Jelini, na mimi nitasimama na wewe. NIMEKUCHAGUA
wewe, sitakusaliti. Kabla sijakuumiza wewe, jua mimi ndio nitaumia
zaidi. Umenielewa?” Akatingisha kichwa kukubali akilia sana.
“Naomba utulie na
uniambie kichwa kinaendeleaje.” Akalia hapo kwa muda, akamuona ananyanyuka
kwenda bafuni. Akakaa huko akamsikia akioga. Akatoka kutayarisha chakula. Baada
ya muda akamuona ametoka amevaa tisheti yake na kufunga taulo chini. “Hilo
taulo litakuwa bichi. Njoo nikupe pensi ambayo nahisi itakuenea.” “Nilimuahidi
mama na Jeremy nitaacha pombe. Na nilikusudia kuacha. Jana nilikosea.
Naomba unisamehe, Colins. Najua nimekosa. Na narudia kukosea tena na
tena. Sitarudi tena baa.” Colins akabaki akimtizama.
“Samahani
nilikosea. Hutanisikia au kunikuta tena kwenye ile hali. Sirudii tena.” Kimya. Akajifuta
machozi. “Na nashukuru hukunirudisha vile
nyumbani. Ningemuumiza sana Jeremy. Huwa namuahidi hivyo, halafu narudia tena
na tena. Mpaka akawa amechoka, haniamini tena.” “Kwa nini ulienda na
Doro, mtu unayejua wazi huko ndiko anakokupeleka?” “Kwanza
dada Doro anajua sana hayo mambo ya UKIMWI. Nilitaka aniambie ni wapi naweza
kwenda nikapimwa na nikapata majibu ya uhakika hata kama vijidudu vimeingia
muda mfupi na sehemu ya kupata dawa za waathirika. Sikutaka kusubiri tena
Colins. Nimeishi kwa hofu kwa muda mrefu. Nikajua yeye ndiye angenisaidia kwa
haraka.”
“Akanielekeza.
Lakini nilikuwa naogopa kuwa mwenyewe hospitalini, Colins. Mimi muoga sana wa
sindano. Naweza hata nikazimia kuona sindano inataka kuingia mwilini mwangu.
Muulize mama.”
“Ameniambia.” “Sasa dada Doro alipojitolea kuwa na
mimi, nikakubali kwa haraka. Hata wakati ule nilipoenda kupima, nilikuwa na
Kasa, ilibidi anifiche uso kifuani kwake ili waweze kunitoa damu. Nilikuwa
naogopa sana, nusura kuzimia.” Wivu tayari kusikia mzee alifanikiwa kuwa
naye hospitalini mpaka kumficha uso kifuani! Roho ikazidi kuuma.
“Na kwa nini
hukunisubiria?” “Nilikata tamaa Colins! Nilifikiri
ni mambo yaleyale ya Love kwanza, mimi ndio nakuwa mtu wa mwisho kunifikiria.”
Colins akatulia. Kisha akauliza. “Uliweza kupima?” “Ndiyo.
Nilipima.” Colins akabaki akimtizama kama anayemsubiria, Jelini akabaki
ameinama mbele yake akifuta machozi. “Nakusikiliza.” Akamuona kama ambaye
anajaribu kukumbuka kitu. “Sijui nimeacha wapi
pochi yangu! Ilikuwa na majibu.” “Ipo chumbani. Twende ukatoe na hilo
taulo.” Akaongoza njia, na yeye akamfuata kwa nyuma kama mtoto anayeogopa.
Wakaingia chumbani,
akamtolea kwanza pensi yake nyeusi, kama ya mcheza mpira wa kikapu. Yaani hata
hapo Jelini akapendeza! Colins akamtizama kwa kujiiba, akaenda kumtolea pochi
yake. “Naomba mimi nirudi nyumbani Colins, nikuache upumzike tu.” Akamgeukia.
“Huli?” “Hapana. Nashukuru. Lakini acha tu niondoke.” “Nilimuomba mama leo
ubaki hapa, tupate muda wa mazungumzo kati yetu. Tuwekane sawa, kabla ya
kuendelea.” “Unaona ni bora uniache tu?” Akauliza kwa upole na wasiwasi.
“Kwanza nataka kujua
kama ni sawa tukabaki wote mpaka kesho ndio nikurudishe nyumbani?” Jelini
akabaki akifikiria. “Jelini?” “Mimi naona bora niondoke tu.” “Kwa nini?”
“Sijisikii vizuri.” “Unaumwa?” Akanyamaza. “Jelini?” “Sijisikii vizuri. Labda
niende tu nyumbani. Tuje kuonana wakati mwingine.” Hapo anamjibu lakini hawezi
hata kumtizama machoni. Akamsogelea na kumshika kipanda uso taratibu akiwa
vilevile ameinama.
“Kichwa kinauma?” Akamuuliza
tena. Akapandisha mabega kukataa. “Basi twende tukale kwanza. Mimi nataka
kubaki na wewe. Twende.” Wakatoka hapo hata majibu ya vipimo alivyofanyiwa
Jelini, hawakuangalia tena. Akakuta alishaandaa meza. Sahani mbili na umma
zake, pamoja na bakuli na kijiko, kisha glasi pembeni. Mziki mtulivu, nyimbo
kama kwenye gari yake ndio zilikuwa zikisikika na hapo kwake. Akaanza kusikia
utulivu.
“Ulitapika sana jana.
Kunywa kwanza supu.” Akammiminia kwenye bakuli. Akaanza kunywa taratibu. “Nzuri.
Nashukuru.” “Karibu.” Akajiwekea na yeye chakula kwenye sahani, akakaa mbele
yake akaanza kula akimwangalia. Kimya cha muda, Jelini haelewi ni kwa nini
anataka kuwa naye. Akanywa supu mpaka akamaliza.
“Nimeharibu sana?” Akamuuliza
Colins kwa sauti ya kumbembeleza. “Unamaanisha nini na kwa nani?” “Kwako.
Wengine sijali. Wameshanizoea mimi ni mtu mbaya.” “Nilidhani uliniambia
umebadilika Jelini!” “Jana sikupanga kabisa kunywa Colins. Na Mungu ni shahidi.
Sijui ilikuaje!” “Kwa nini ulirudi baa?” “Dada Doro aliniambia niende naye
nikasalimie washikaji tu. Ameshawaambia yupo na mimi, wamesema tukutane
niwasalimie. Nikaona sio jambo baya. Na hata nilipofika pale niliwaambia mimi
nimeacha pombe. Ndio dada Doro akaniambia moja tu. Sasa sijui ilikuaje, ila
nakumbuka kukataa, sasa sijui ikawaje tena nikazidisha mpaka kulewa!”
“Doro si rafiki mzuri
Jelini. Rafiki anatakiwa kuheshimu maamuzi yako. Ukisema hunywi,
anaheshimu hilo na kukuacha si kukulazimisha.” “Nimekuumiza sana?” “Ndiyo
Jelini. Kwa sababu tulikubaliana hapo hutarudi tena. Ni kwa nini
umeruhusu Love kukuingia akilini kiasi cha kutoniamini mimi?” Akapandisha
mabega kukataa.
“Huamini kama
nakupenda Jelini. Niambie nifanye nini uamini nakupenda wewe, nimekuchagua wewe,
na nitabaki kuwa na wewe. Maana bila hivyo hatutafika mbali. Tunavita mbele
yetu. Haswa upande wangu, hawataki tuwe pamoja. Sasa kama mimi na wewe
tukishindwa kuwa pamoja, ujue wakati tutakapojaribiwa kwa hakika, hatutasimama.
Jana ilikuwa ni mimi kutotokea kwa wakati, ukapotelea kwenye marafiki wa
zamani. Wakija kukuletea uongo mwingine juu yangu na uthibitisho wao, bila
kutaka kunisikiliza na mimi, si ndio utakuwa mwisho wetu?” Jelini alilia sana.
“Nimekosa
Colins. Tafadhali nisamehe. Nakuahidi nitabadilika. Na sitarudia tena
kwenda baa, labda tuwe wote.” “Naomba utulie. Sitaki uendelee kulia. Kichwa kitaanza
kuuma tena. Ila niambie kama angalau unaniamini Jelini. Maana nimerudia zaidi
ya mara tatu, kukuhakikishia Love hatakaa akaingia katikati yetu. Ni mtu wa
mwisho kabisa sasahivi namfikiria, ila wewe.” Jelini akaendelea kulia.
Akaenda kumnyanyua
pale, wakahamia sebuleni. Akakaa na kumvuta akae pembeni yake, kisha akamkumbatia
vizuri, Jelini akasikia upendo wa ajabu. Kumsafisha matapishi akiwa amelewa na
bado kumkumbatia kwa namna ile, ikamgusa zaidi. Akalia hapo kifuani Colins
akimpapasa mpaka akatulia.
“Nitabadilika.” Akamsikia akiongea
taratibu. “Naomba kusikia umebadilika Jelini. Kuanzia kuniamini, kusimama na
mimi bila kuchoka. Hata ukisikia kitu, kama hakijatoka kwenye mdomo wangu, baki
na nilichokwambia. Nibebe kwenye udhaifu hata kwa mama yako nisitiri na kunitetea
ukijua nakupenda, sina nia ya kukuumiza.” “Na nitakusubiri Colins. Hata
ukichelewa, kuanzia sasa, nakusubiri wewe tu. Tukipanga jambo letu, nakuahidi
kulisimamia. Sitafanya vinginevyo mpaka tukubaliane tena.” “Basi hapo ujue ndio
kusimama kwetu. Na hakuna mtu atatuangusha kirahisi.” Wakatulia.
“Na mimi nikuombe
radhi kutokuwa na wewe jana hospitalini. Nilishakuwa nimevaa kabisa, nakaribia
kutoka ndipo wakanivamia. Nilipanga tutoke, twende tukapate kifungua kinywa
pamoja ndio twende hospitalini. Lakini nikashindwa, na wewe hukuwa na simu
angalau kukutumia ujumbe, kukutaarifu! Ila ujue sikukusudia.”
“Tutafanyaje kuhusu
kwenu, Colins?” “Sijui. ila ninachojua sisi tuendelee na yetu, tutakuja
kuungana nao watakapokuwa tayari.” Jelini akabaki amejilaza hapo kifuani kama
kawaida yake, akifikiria.
“Colins?” Akaita
taratibu, akiwa amemlalia, anapapaswa. Akaitika. “Hata iweje, niahidi hutaniacha
mimi.” “Nimeshakuahidi Jelini. Tafadhali amini.” “Naingiwa hofu. Maana ni kama
jana nimethibitisha walichonishitakia huko kwenu. Ila sikufanya jambo baya.”
“Unajuaje Jelini? Hivi unajua hali unayokuwa nayo ukilewa?” Akaingiwa hofu.
“Au nikuulize,
unakumbuka chochote kuanzia nimekufuata kule baa?” Kimya. “Yale maneno
uliyoniambia siku ya harusi ya James na Jema, uliyarudia Jelini. Tena mbele ya
wale niliokukuta nao, mpaka na wao wakawa wanashangaa. Hawaamini kama na wewe
umepata mtu wa kumwambia hivyo. Sasa je, unakumbuka?” Jelini akatingisha
kichwa kukataa.
“Sasa unajuaje kama
hujafanya jambo baya.” Akaanza kuingiwa na hofu. “Maana wanaweza kukufanyia na
kondomu, usijue hata kama kuna mtu alipita. Kwa hiyo kama hukumbuki chochote
kilichoendelea baada ya kulewa, tafadhali usiseme hujafanya jambo baya, kwa kuwa
hujui.” Jelini akajisikia vibaya sana. Akaficha uso hapo kifuani na kuanza
kulia tena.
“Sina nia ya
kukuhukumu, lakini nakwambia ukweli. Ndio maana mimi binafsi nachukia pombe,
kwa kuwa inauwezo wakunifanya nisifikirie na kuzungumza kile ninachotaka
kuzungumza kwa wakati ule. Ndio maana sinywi.” “Sirudii
tena Colins. Nakuahidi sitarudia tena. Hata iweje, sirudi huko tena.”
“Sawa. Mimi nitabeba maneno yako moyoni kwangu. Nakuamini.” Akaendelea
kumbembeleza mpaka akatulia.
“Twende ukalale.
Najua jana hukulala vizuri. Mimi nitakusubiria na kukubembeleza mpaka ulale.
Twende.” Colins akacheka akimtizama. “Twende.” “Ujue hapa ndio nyumba
tutakayolea watoto wetu?” Jelini akacheka akiangaza macho. “Au hujapapenda?
Unaona padogo sana?” “Maadamu wewe utakuwepo hapa, mimi napapenda.”
“Niahidi asije tokea mwenye mjengo, akakutoa hapa.” “Kasa hatanitoa
hapa.” Colins alicheka sana.
“Najua Kasa
anakutisha sana. Na sijui kwa nini!?” “Yule mzee anapesa nyingi sana bwana. Na
ni kama hazina kazi!” “Mimi nakutaka wewe Colins. Nimeridhika na wewe. Wasiwasi
wangu ni kuja kukupoteza tu, lakini si mali. Naomba yule mzee asikutishe.
Kwanza nishamkabidhisha kwa anti Sheha, huo ukurasa nimefunga. Twende
ukapumzike. Achana na mawazo ya Kasa.” Wakatoka hapo kwenye kochi, akamuona
anazima taa zote.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Napenda hizo nyimbo
zako! Zina maneno yakutuliza.” “Nitakuhamishia chumbani. Usijali.” Akamshika
mkono akimuongoza njia mpaka chumbani. “Kesho unaondoka saa ngapi?” “Kwa nini?”
“Nataka ukitoka, tutoke wote. Na mimi nirudi nyumbani.” Akabaki kama anawazo
jambo, kisha akasita. Jelini akamgundua. “Ni nini?” “Natamani unisubirie mpaka
jioni ndio nikurudishe.”
“Colins!? Nitakaa
hapa mpaka lini?” “Akili yangu inatulia nikijua upo hapa. Hata naweza kufikiria
vizuri. Niliingiwa na hofu jana! Hakika ungenihurumia. Sikujua kama nitakuja
kukupata tena, na kama hata nikikupata bado ungeniambia unanitaka mimi. Nilijua
nimekuumiza mpaka mwisho. Hutaki hata kuniona tena. Tafadhali nipe hata siku ya
kesho tu. Nikirudi nakurudisha nyumbani. Hata hivyo mama na Jeremy
hawatakuwepo. Utashinda peke yako. Sasa si heri ubakie hapa?” “Na wewe si
unaenda kazini?” “Lakini naweza kurudi hata mchana kama leo, tukala wote.”
“Kwani leo ulirudi?” “Ulikuwa umelala kama ndio usiku wa saa nne. Nikaona
nikuache tu.” Jelini akatulia.
“Lakini kama hutaki
kuwepo hapa, basi. Usijisikie nakulazimisha.” “Unajua ningetamani hata
nisiondoke hapa, Colins.” “Sijajua. Maana hata hiki chumba na bafu vilivyopo
humu havifanani na kwako.” “Acha kufanya hivyo bwana!” “Kweli Jelini. Unamiliki
chumba na bafu vya hali ya juu sana. Ni rahisi kujishuku na nilivyonavyo.”
Jelini akatulia akifikiria.
Colins akabadili nguo
hapohapo mbele yake na kujiweka kitandani akimtizama kama alivyojilaza kwenye
kitanda chake chumbani kwa Jelini. “Popote utakapokuwa wewe Colins, mimi
nitafurahia kuwepo. Sitajali ni wapi.” “Unauhakika?” “Basi naomba muda uje
ujibu hilo swali Colins. Mimi muaminifu sana. Hata nilipokuwa na Kasa, japokuwa
nilikuwa na hamu na wewe, lakini nikajionya nafsi yangu kabisa,
nikakuacha.” “Kweli Jelini!?” “Kama ungekuwa ukizungumza na Kasa mwenyewe
angekwambia jinsi nilivyoumia kwa kitendo cha kukufuata, eti na kukuonya ukae
mbali na mimi! Niliumia mpaka akajua. Lakini kwa kuwa nilikuwa naye, nikaona
nitulie tu. Sitakusaliti Colins. Nitatulia na wewe.”
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akajinyanyua pale
alipokuwa amejilaza kufikia midomo yake, mabusu yakaanza. Taratibu mkapa
yakachanganya. Akiwa kwenye ile hali ya kuwa tayari kumvua nguo Jelini, gafla
maneno ya Love aliyopenda kumkejeli nayo kitandani akimfananisha na wanaume
wengine yakamrudia. Nayo picha ya Jelini akiwa mtupu, vile alivyo mzuri ikamjia
kwa gafla. Kasa na maneno yake kuwa aliweza kumtuliza Jelini vikapita hapo
kichwani mwake, Jelini akiwa amelegea, anamtaka tu yeye.
“Upinzani mwingi kwa Jelini. Nikizembea
hapa, nisipotoa shoo ya kikabe, atabakiwa na kumbukumbu ya yule mzee.”
Colins akaendelea kuwaza huku akimpapasa Jelini aliyekwisha muona akiwa kama
alivyozaliwa siku iliyopita, na kumsafisha. Hali ilishakuwa mbaya. Yupo kwake,
ndani ya chumba chake, Jelini anatoa miguno ya hatari.
Akaendelea kuwaza katikati
ya romance ya kukata na shoka. Walikuwa wakinyonyana kama wenye uchu wa
kupitiliza mpaka wakajikuta wamelala kitandani. Jelini naye amemng’ang’ania
kama anayeomba asimuachie.
Hakuwa amevaa
sidiria, kwa hiyo hata chuchu aliziona kupitia tisheti yake tokea wanakula.
Picha ya mwili wa Jelini vikazidi kumsumbua Colins ila hofu. Anaogopa fedheha.
Kuishi kwa muda mrefu na Love, akimwambia maneno hayohayo kwa muda mrefu
vikamuingia akilini, mpaka akaamini. Gafla ikawa kama mtu amezima switch ya
umeme au mshumaa uliopulizwa. Colins akazima gafla, asitarajie mpaka
mwenyewe akashituka kwa hofu. Jelini
alipoona hivyo, akajitoa hapo kwa kuumia sana.
“Nakwenda kutumia
choo.” Akatoka hapo bila yakusubiri jibu, Colins akajua ameharibu.
Jelini amekasirika, asijue ni zaidi ya hivyo. Amehisi kukataliwa kwa hali ya
juu. Colins akabaki hapo kitandani akihema. Kama kitu kikapita kichwani, akaruka
hapo kitandani na kukimbilia upande wa bafuni alipoelekea Jelini. Akataka
kumgusa, Jelini akamuona kupitia kioo, akamkwepa.
“Tafadhali acha
kucheza na hisia zangu, Colins. Na mimi ni mwanadamu, nina hisia. Na ujue ipo
siku zitafika mwisho.” Jelini akamgeuka asiamini. “Hujaelewa Jelini!” “Juu ya
nini? Kwamba unaweza kuishi unyumba na Love, lakini huwezi kuwa na mimi?”
Colins akashituka nafsini kwake, hakujua kama ingeleta picha ya namna hiyo.
“Ni vile nakuheshimu
sana Jelini! Niliona si sawa kuendelea na chochote bila hata yakulipa mahari!
Nilitamani ukiwa mke wangu ndio niwe huru na wewe. Sikutaka kuwa kama nakuvamia
tu au nachukua kitu kisicho changu.” Akajitetea na kuzidi kuharibu.
“Sawa. Basi naomba
nirudishe nyumbani. Ila kama unaona ni usiku sana kwako, mimi naweza kwenda
peke yangu.” “Tafadhali usikasirike Jelini.” “Siwezi kukasirika kuheshimiwa!
Nakusaidia kuishi matakwa yako. Bado mimi si mke wako, kwa nini kutaka nilale
na wewe kitanda kimoja? Acha kama tutajaliwa hiyo ndoa, nitarudi tena hapa. Ila
kwa sasa tafadhali tuishi ulichokisema. Na naomba usianze kuniyumbisha
Colins. Simamia maamuzi yako, tafadhali.” Akatoa nguo palepale, akavaa gauni
yake aliyokuwa amefuliwa na Colins, Colins akimtizama.
Akatoka akimtizama,
akagutuka tena na kumkimbilia. “Acha nikurudishe. Ila huoni kama itakua usiku
sana?” “Hamna neno.” “Utawasumbua wakiwa wamelala na mimi nilishakuombea ruhusa
Jelini. Tafadhali naomba tulale mpaka kesho.” “Hapana. Ruhusa uliomba ya mazungumzo
na kuniweka sawa. Ushaniweka sawa, nimekuelewa. Kuna sababu gani tena ya
kulala hapa?” Colins akabaki kimya.
“Tafadhali acha kuwa
njia panda hata katika hili. Kama kwako huu ni usiku sana, kwangu bado ni
mapema sana. Tafadhali amua moja. Unanisindikiza au nitoke nikatafute usafiri
hapo nje?” “Naomba kukupeleka.” Akachuka pochi yake na kutoka tena hapo
chumbani.
Ikabidi Colins aanze
kubadili nguo kwa haraka. Kutoka za kulalia, ili avae kitakacho mfaa
kumsindikiza Jelini. Akamkuta mlangoni kabisa anajaribu kutoka. “Jelini
umeshindwa kunielewa. Tafadhali tulia.” “Nimetulia na kufiria kwa karibu. Naona
wewe utanichanganya Colins. Sijawahi pata mtu akaniumiza roho na akili kama
wewe. Na hivi ninavyojisikia, sitaki kuendelea kuishi hivi. Mimi sitaki kuishi
na hii hali.” “Jelini!”
“Hapana Colins. Nikijifikiria,
naona kuwa na wewe kwenye aina yeyote ya mahusiano, napoteza na napotea.
Nikijifikiria sababu ya kunifanya kumtafuta dada Doro na kuishia kunywa nikiwa
najiambia ni kidogo tu, nilikuwa nataka nijitulize kile ninachojisikia juu yako
na sikipati. Najihisi nimekwambia sana na kukuonyesha nakupenda mpaka
kwako vimekosa maana. Colins, mimi sijawahi kubembeleza mtu hivi, aisee.
Najiuliza nitaendelea hivi mpaka lini!? Jana sababu ya maumivu yako, nimevunja
ahadi ya msingi sana kwangu mwenyewe na kwa mwanangu. Nilirudi baa na kufanya
kitu ambacho sikuwa hata nampango wa kukifanya.”
“Nahisi na pengine
ndivyo inavyoweza kuwa, pengine sisi hatukukusudiwa kuwa pamoja.” “Jelini…”
“Subiri kwanza Colins. Wewe haupo tayari na mimi. Familia yako
pia hainitaki. Kwa nini unataka kunichanganya bila sababu?”
“Nakupenda Jelini.” “Pengine ndivyo unavyodhania. Lakini matendo yako sivyo. Na
mimi sitaki mtu wa namna yako maishani. Utaniyumbisha kwa uchache nilio
nao. Kwa heri Colins. Kila la kheri. Kama tuliandikiwa, basi acha muda utakuja
jibu. Pengine hata wewe utakuja kujisikia utayari na mimi, kama bado na mimi
nitakuwa bado nikijisikia hichi ninachojisikia kwako. Tafadhali nifungulie
mlango nitoke.”
“Najua nimekuumiza
Jelini. Lakini sikukusudia ni…” “Tafadhali usirudie rudie. Ulishaniambia. Mimi
nataka kurudi kwetu nifungulie mlango.” Colins akafungua mlango, akashangaa
Jelini anaongoza njia kutoka getini. “Tafadhali nisubiri nikurudishe nyumbani.”
“Huna haja yakunirudisha, wewe siye uliyenitoa kwetu.” “Jelini?” “Basi labda
nikwambie hivi, sipo tayari kupanda gari yako. Na mimi nimeona nisubiri
kutumia vitu vyako mpaka au kama tukifanikiwa kuona. Mimi huwa sikubali vitu
vya watu hovyo. Kama huamini, muulize Kasa.” Jelini akabadilika, Colins
asiamini.
“Tafadhali naomba…”
“Hapana Colins. Hakika nimekataa. Hutaendelea kunitesa kwa kiasi hichi. Heee!
Kwa nini haswa!? Hapana. Utaninyima raha na kunifanya niishi na wewe kwa
kukubembeleza mpaka lini!? Hapana kwakweli. Nimekataa. Siwezi kuwa
mtumwa.” Jelini akaondoka, Colins asiamini. Ikabidi aache gari aanze kumfuata
kwa miguu. Anatoka getini, kikampata kilichompata Kasa. Jelini mtoto wa
jiji, hajazaliwa kwenye magari. Anajua kona na vichochoro vya jiji kama jina
lake. Akikuponyoka dakika moja tu, humpati. Colins akakimbia mpaka
kituoni, hakuwepo. Akaanza kumsaka akiamini atakuwepo tu hapo. Wapi!
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Vita Ya Ndani Na Ya Nje Inaendelea Kati Ya Wapenzi Hawa Wawili Walio Hakikishiana Wana Penzi La DHATI Kati Kati Yao.
Usipitwe Na Sababu Ya Kweli Ya Kushindwa Kumtoa
Nguo Jelini Na KUMKATA Kiu Yake.
Love & Familia Ya Colins Wana Mipango KABAMBE Kuhakikisha
Colins Anabaki Kubeba Mipango Ya Wazazi? Wakiwa Katikati Ya Kutoelewana Wao Wenyewe Wawili, Colins&Jelini. Je, Watafanikiwa
Kumrudisha Colins Upande Wa Familia.
Kipi
Kitaendelea?
USIPITWE.
0 Comments:
Post a Comment