~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kazi ya kwenda kwa
kina Jelini kumsaka bila mafanikio ikaendelea. Mchana wakati wa chakula,
anatoka kazini anakwenda kwa kina Jelini. Atagonga mpaka achoke. Muda ukiisha
anarudi kazini. Akitoka jioni kazini, anarudi tena kwa kina Jelini. Atakaa hapo
mpaka anachoka na mbu, anaondoka. Jelini hakuwa na simu. Alimsikia akitupa
chooni line ili kumridhisha. Walinzi nyumbani kwao walishaondolewa na
mama Jema. Hakuna wa kufungua geti aingie ndani ni mpaka wenye nyumba watake
wao. Colins akagonga mwamba.
Siku alipomtuma
kijana wa kazi, Chaz, kwenda kufua na kusaidia usafi, hakufunguliwa mlango.
Akampigia simu Colins. “Hakuna mtu. Nimegonga kwa muda
mrefu hakuna aliyefungua.” “Umejaribu kumpigia simu mama yao?”Colins
akauliza. “Labda nijaribu. Ila naye kupokea simu ni
shida! Mara nyingi siku na muda ambao huwa nakwenda, walikuwa wakiniachia geti dogo
wazi, naingia kwenda kugonga mlango tu ndani.” “Mjaribishe mama yao, kujua kama
kuna mtu ndani.” Chaz akakubali bila shida. Na yeye anataka pesa.
Baada ya kupiga sana
simu bila kupokelewa, akaonelea atume tu ujumbe. ‘Ni
mimi Chaz, nipo hapa nje ya geti, nimekuja kufua na kufanya usafi.’
Baada ya kama dakika 20 hivi akajibiwa. ‘Wala
usihangaike kurudi tena hapo. Naona uhitaji hakuna tena. Tunashukuru sana kwa
msaada wako. Siku njema.’ Ikabidi ampigie simu Colins kumpa taarifa.
Hilo likazidi kumtesa Colins.
Nyongo Mkalia Ini.
Akaanza kunyongea,
utengano na Jelini ukazidi kumla ndani kwa ndani, hana wa kuzungumza naye.
Anamwambiaje James? Amsimulie nini na aache kipi? Amwambie ukweli juu ya
kuogopa kwake kulala na Jelini? Maana kwa Jelini yeye amechukua ni kukataliwa,
na akajua ndivyo atakavyomwambia mama yake na Jema, na Jema naye kumwambia
James. Watajua bado anamshikilia Love, kumbe ni zaidi ya hivyo. Ni ndani zaidi
ya watakavyomuhukumu. James anamjua Colins si mcha Mungu wa kiasi chakushindwa
kuparanganyisha amri ya 6. Si tatizo hata kidogo, kwa hiyo hata yeye alijua
James atamuona ni mbambaishaji tu.
Akabaki akiwaza.
Nyumbani hapakaliki sababu ya tuhuma kali sana juu ya Jelini ambaye hata
hawawasiliani! Chakula kwa Colins asiyeweza kupitisha mlo, kikaanza kukosa
ladha. Cha asubuhi kikapelekwa mchana, cha usiku kikapuuzwa. Ikawa asubuhi,
ikawa usiku, Jelini hapatikaniki. Sauti ya mzee Kasa akimtisha kuwa hao
watoto anaopanga kuwa nao na Jelini wataishia kuwa na wao kina Kasa kama
Kelvin, ikazidi kumla ndani kwa ndani. Usingizi ukaanza kukosekanika. Usiku
badala ya kulala, anacheza game.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
James akamaliza
likizo yake, kurudi ofisini, anakutana na Colins ambaye hakumtarajia. Alijua
ukimya wake kwake, ni kwakuwa yake na Jelini yanamuendea sawa, kumbe aibu ya kumshirikisha
ukweli wa kile kinachoendelea. Na Jelini naye safari hii akakosa cha
kumlalamikia mama yake akijua mama yake akijua ndio Jema naye atajua. Sasa Jema
ajue amemnunia Colins kwa kukataa kulala naye akimwambia wasubiri mpaka
ndao!? Jelini akalibeba moyoni, hata mama yake asijue kama Colins hayupo kwenye
picha.
Na mama Jema naye
biashara zimechanganya, akili na muda wake wote kwenye biashara zake, Jelini
yupo nyumbani akilea kichwa na mwanae, kuanzia mambo ya shule mpaka nyumbani.
Hilo mama Jema akalifurahia, angalau amepokelewa mtoto, akili zinabaki kwenye
pesa tu. Akitoka hapo asubuhi ni mpaka usiku mwingi tu. Maisha yakaendelea
wasijue moto unawaka ndani ya Colins.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Kwema wewe!?” “Kwema
kaka. Vipi JJ?” “Anakimbia sasahivi. Anaita mpaka baba!” Colins akacheka maana
huyo JJ hata mwezi alikuwa hajatimiza! “Sasa akili imerudi kazini au bado unawaza
ulezi?” “Lazima. Maana sasahivi atahitaji ada ya shule. Lazima kuongeza nguvu
kwenye utafutaji.” Colins akatingisha kichwa.
“Usifanye masihara!
Lakini mbona kama upo hovyo? Kwema?” “Kwema tu.” James alimjua Colins. Hawezi kujificha
kwake. Akamuacha akijua akiwa tayari atayasema mwenyewe. Kazi zikaendelea, siku
tatu zikapita akimuona kabisa hayupo sawa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Siku na hiyo akiwa
anasimama, ametoka kwenye meza yake, maana zinaangaliana na ya James, akataka
kuanguka. Hapakuwa na chakumfanya aanguke. James akaacha kila kitu, akamtizama.
“Vipi wewe!?” “Naona giza.” James akashituka na kusimama haraka, akamsogelea.
“Kwa nini?!” “Nahisi sukari ipo chini sana.” “Kwamba hujala?” Akanyamaza. “Sasa
hapa utakufa, kama huniambii jambo linaloeleweka.” “Unataka nini tena?
Nishakwambia sukari ipo chini. Nenda kaniletee hata Fanta.” James akatoka hapo
mbio. Akaenda kwenye fridge yao, akachukua soda, akarudi nayo, akamkuta
amesimama palepale ila ameegemea meza. Akamshikisha.
Akainywa yote kwa
haraka na kurudi kukaa. “Naenda kuleta soda ya pili.” “Sasa nitajaza tumbo kwa
soda tu?” Ikabidi James asimame. “Sijui unataka nini!” Akanyamaza. “Labda
nikuulize, mara ya mwisho kula wewe ilikuwa lini?” “Sikumbuki.” “Haya tutoke
tukatafute chakula.” Akamuona habishi. Wakatoka.
Akamuendesha mpaka
kwenye mgahawa ambao wanapenda kwenda kula. Akaagiza wakati James akizungumza
na mkewe. Akagundua ameagiza supu tu. “Acha kunitania na kunipotezea muda
wangu. Ndio chakula gani hicho?” “Nimepoteza hamu ya kula kabisa. Yaani hii
nitakunywa kama dawa?” “Kwa nini? Unaumwa?” Akanyamaza. “Jelini anajua?” Ikabidi
aanzie tu karibu, akimjua Colins.
“Jelini hanitaki
tena.” “Umefanyaje safari hii!?” “Mbona kama unanishutumu mimi moja kwa moja!?”
“Haya samahani. Kwa nini hakutaki?” “Wewe vipi James?” “Kwa upotezaji huo wa
muda, ukinizungusha kwa kutaka kunilaumu, narudia swali la kwanza, safari
hii umefanya nini?” Colins akabaki akijishauri huku akijitahidi kunywa supu
yake. James naye akaona aagize supu. Kimya kwa muda.
Ukweli.
“Unakumbuka
nilikwambia niliishi na Love?” James akamtizama. “Kama mke na mume kabisa.”
“Nakumbuka.” “Sasa katika moja au mengi ya malalamishi yake ni ufanyaji wangu
wa mapenzi. Alikuwa akilalamika wakati mwingine ni kama namchafua tu.” “Kwamba hujui au?” “Aisee
mpaka aibu!” James akafikiria kwa haraka na kuongeza swali zito zaidi. “Alikuwa
akilalamikia maumbile?” “Aisee mpaka
ikanimaliza kabisa na kushindwa kabisa hata kufanya naye mapenzi.” Colins
akaendelea bila ya jibu la ‘ndiyo’ au ‘hapana’ ikawa kama James amenena.
“Nikaja kugundua
ameanzisha mahusiano nje. Nikamuuliza kwa nini na wakati tunaishi nyumba moja!
Akasema mimi ndiye nimemsababishia. Sijui chochote kitandani, halafu nina…” Akasita
na kubaki kama asiyejua azungumze nini ili asijidhalilishe zaidi. “Kwa
ujumla wake ni kwamba haridhiki. Si ndivyo?” James akaona amrahisishie.
“Ndiyo. Kwa hiyo
akasema amekaa hivyo kwa muda mrefu akinivumilia ila akiteseka sana. Na yeye ni
binadamu, ikabidi kutafuta mwenye mashine ya kiume kweli, ili apunguze haja
zake. Lakini yeye si malaya. Kwamba kama mimi ningeweza kutumia vizuri
hata kidogo nilicho nacho, yeye angeridhika.”
“Subiri kwanza
Colins. Wanawake zako wengine kabla yake
walikuwa wakisemaje? Maana isijekuwa hicho ni kisingizio chake tu!” “Sikuwahi
kuwa na mwanamke kabla James! Yeye ndio mwanamke wangu wa kwanza. Na kama
unavyomjua mama. Katika hilo, alihakikisha ananiweka sawa tokea mdogo
sana. Kwa hiyo ikaniingia akilini. Kwamba si kitendo unafanya tu hovyo.
Kwa hiyo katika maswala ya ngono, mimi si kwamba nimekubuhu. Yeye ndio mwanamke
wangu wa kwanza, na akaishia kunitia kilema.”
“Sasa inahusianaje na
Jelini?” “Imeniathiri James! Nikiwa na Jelini, naweza nikasisimkwa
kabisa. Tena napatwa na hisia ambazo naweza sema sijawahi pata maishani. Nikiwa
kwenye hiyo hali, gafla hofu ya ajabu inaniingia kiasi ya kwamba nashuka
kama ‘joka la Kibisa’. Sasa siku ile uliponisaidia kumsaka Jelini, si
nilienda naye kwangu?” “Nakumbuka.”
“Aisee tulipata
wakati mzuri! Mzuri sana, wa ajabu. Mimi mwenyewe siku ile nilitamani
sana kufanya naye mapenzi. Tukiwa kwenye ile hali, si hofu ikanijia tena
mpaka nikaanza kutetemeka!” “Haiwezekani! Mbele yake!?” “Kitandani kaka.
Sasa akajua kabisa. Maana nilikuwa juu haswa, nakaribia kumtoa nguo, ndio
nikanywea kama mtoto wa kiume aliyezaliwa leo. Akatoka kitandani.”
“Sasa kwa kupaniki,
maana na yeye nilikuwa nimemuandaa, yupo juu haswa. Ikawa kama nimemkatili,
nikamwambia naona tusubiri mpaka ndoa. Si na yeye akajua kama niliishi na Love
kama mke! Akaniambia bado namuwaza Love ndio maana nimeshindwa kulala
naye. Akaondoka usiku huohuo, sijamsikia tena mpaka leo.” “Duuuuh!” James
akakwama.
“Sasa hapo ndio nini?
Mimi nakwambia yote hayo, wewe unaishia kusema ‘duuuh!’” “Acha kunikasirikia
bila sababu. Nafikiria.” “Sasa unafikiria nini? Maana mimi nakutegemea wewe
unisaidie. Na wewe unakwama!” James akabaki ametulia. “Na wakati ukifikiria,
acha nikuongezee upande wa Kasa.” “Kasa, yule mzee tena?!” “Aisee bado hajakata
tamaa kwa Jelini, mpaka napagawa!” Akamsimulia mazungumzo yote kati yake na
mzee. James akabaki hoi.
“Nahisi dunia si
yangu kabisa. Nimkose Jelini!” “Itabidi urudi kwa gia kubwa.” James akawaza kwa
sauti. “Ndio nafanyaje?” “Hivi ulivyonielezea mimi, ndio na yeye umwambie.”
Alishituka Colins, mpaka akapaliwa. “Sasa nini?” “Hakika nataka kujua upande
uliopo James! Upo kama hunitakii mema vile! Maana mimi nilipanga chochote
kilema nilichonacho, nikinyamazie mpaka ndoa. Aje akutane nayo ndani ya ndoa.”
“Kwamba ujifiche kwake, ukidhani mkiwa ndani ya ndoa ndio itakuaje?” “Si
hataweza kuniacha tena!? Wewe vipi James? Unakuwa kama hunifikirii!” “Akija
kufanya kama Love?” Hapo Colins akapoa.
“Wewe hutamani kuja
kuwa na mwanamke atakayekupenda hivyo ulivyo mpaka kifo chako?” “James!
Tunamzungumzia Jelini, kaka! Mimi sio mwanamme wake wa kwanza. Jelini
hazinguliwi na pesa, kwa kumsikia mwenyewe anapenda mikono. Unakumbuka
kilio alichomlilia yule mzee? Unafikiri ilikuwa bure? Halafu unataka nijitoe
mwenyewe? Aniache mapema hivi hata sija..” “Sasa bora vipi? Ajue, akuache
ujue moja kabla hujamuingiza kanisani, au ajue ndani ya ndoa kisha akuache na
kanisani mlishafungishwa mpaka kifo?” Kimya
Colins akifikiria.
“Ni bora umwambie
ukweli ujue kama ni wako au si wako. Akibaki na bado akakupenda
si ndio utajua unafunga ndoa ya mpaka kifo! Acha
kucheza mchezo wa ajabu Colins! Ndoa si kama hivi anavyojifungia kwa mama yake,
wewe upo kwako. Ndoa ni mpo naye nyumba moja. Kikitibuka huko ndani ya
ndoa, halafu kina Kasa wakajirudi?” Colins akatulia. Akajua kimemuingia ila
hofu.
“Nisikilize Colins. Mimi
nimeishi na wewe, nakufahamu. Ni mtu mzuri sana. Mwanamke yeyote atakaye bahatika
kuolewa na wewe, na akaridhika, mtakuwa na ndoa nzuri sana.” “Unafikiri hivyo?”
“Ila uanze vizuri sasa. Sio kuweka msingi mbaya. Ungekuwa ukimuoa mwanamke kama
aina ya kina Jema, ni rahisi kumwambia mpaka ndoa. Ameokoka. Anaogopa
kumtenda Mungu dhambi. Lakini wewe umeenda kuchagua mwanamke wa viwango vingine
kabisa, halafu anakujua na wewe upo katika ulimwengu wake. Huna sababu ya
kumwambia mnasubiri. Kwa nini?” “Namuheshimu.” “Kwamba mwanamke mliyekuwa
mkiishi naye mwanzo, tena kwa muda mrefu huo hukuwa ukimuheshimu?” Kimya.
“Hizo ndio sababu
zinazokufanya ukataliwe. Uongo wa waziwazi.” “Sasa hata nikitaka
kumwmabia, nampataje? Jelini alitupa chooni namba yake ya simu kwa ajili ya kuniridhisha.
Akitaka aniaminishe hatakaa akarudi tena kwa yule mzee. Nisaidie.” James
akashituka na kutoa macho. “Sikutumi ukamwambie maswala ya mapenzi! Acha
kupaniki hovyo. Nataka tu umwambie tukutane tuzungumze.” “Hapo sawa. Nilifikiri
unataka uanze yale mambo yako!” “Mimi sio mjinga.” James akamwangalia kwa
kumsuta na kuendelea kula.
“Ni mjinga kidogo tu
kwa Jelini.” Akajirudi nakumfanya James amtizame tena. “Acha ushabiki James!”
“Labda nikusaidie, sio ujinga, ni unakuwa unachanganyikiwa.” “Naona unaanza
matusi, huna msaada.” “Nitazungumza naye. Ila sitoi ahadi.” “Hata hilo
tu nashukuru. Ila iwe leo sasa.” “Umeanza Colins!” “Kwa hiyo unataka mpaka nije
kufa? Utamwambia nini mama yangu?” “Daaah! Colins ukianza jambo lako! Basi
nitakwenda kwao leo.” “Hapo sawa. Sio sasa tena uende usiku ambao unajua wazi
wamelala!” “Unataka nikazungumze na Jelini au hutaki?” “Basi. Ila ujue sitalala
nitakuwa nikisubiria simu yako.” “Hata bila simu yangu, hulali. Acha
kutaka kuja kunibebesha lawama.”
Kwa Jelini.
Jioni baada tu
yakutoka kazini akapitia kwa kina Jelini. Akamkuta ametulia kimya nyumbani
kwao, mtoto wake anafanya yake. “Karibu shem!” “Nashukuru japo najua umeshajua
ni kwa nini nipo hapa.” “Kama ni juu ya Colins, acha nikwambie ukweli shem.”
Hofu ikamuingia. Asije anza kuzungumzia mapenzi naye! James mtu wa maadili sana
na mipaka.
“Mimi Colins simtaki
tena.” “Jelini!” “Mimi sina hela wala si kwamba ni tajiri nitegemee starehe
kwenye hilo. Raha yangu ni moyo wangu. Sasa kuwa na Colins kwangu ni
adhabu shem! Inakua ni kumbembeleza yeye kila wakati kwa kila jambo,
wakati mimi ndio…” “Unataka ubembelezwe.” “Hapo umemaliza. Nataka mimi ndio nibembelezwe
na nipendwe mimi tu. Sio kama hivi mimi na Colins. Hivyo SIWEZI na SITAKI.” “Colins anakupenda
Jelini.” “Upendo wa hivyo mimi shem siutaki. Ujue kwa nini nilimlilia
sana Kasa?” James akajiweka sawa.
“Unataka kujua au na
wewe hutaki?” “Ni kwa nini?” “Mwenzio alikuwa akinibembeleza kama yai!
Ananifikiria mimi mchana na usiku, na kutafuta jinsi ya kunifurahisha
kila wakati. Alivyogundua mizawadi yake hainifurahishi, akatafuta kujua ninachokipenda.
Huwezi amini shem, yule mzee na biashara zake na utajiri wake wote, akiwa na
mimi ni mimi tu. Akili, mawazo na mikono yake ni mimi tu.”
“Atakaa na mimi kama
vile kijana wa kijiweni asiye na mipango mizito. Na simu ya kazi anazima
inabaki simu ya familia tu, tena ya dharula. Na tena kama sio dharula,
akipigiwa na wanae mimi nipo naye, anawaambia kabisa, atazunguza nao kesho yake
akiwa kazini, ndio maana wanae wakaanza kunichukia.” “Sikujua hivyo!”
Ubaya Ubaya Tu.
Ubaya Bayana.
“Mimi nimeambiwa na
mashoga zangu wa saluni. Aliyempa habari zangu za uongo Love, ni mwanae Kasa.
Anaitwa Kemi. Maana mimi aliponiambia Colins eti Love ameongea habari zangu kwa
wazazi wake, akiwa na uhakika kuwa ameambiwa na mtu wa karibu sana na Kasa, ikabidi
nianze uchunguzi. Nikaanza kujua anakoenda saluni Kemi na Love. Nikapajua.”
“Jelini! Umejuaje yote hayo!” “Umesahau mimi mtoto wa mtaani shem? Shule
niliyonayo ni ya mtaani. Mashoga zangu ni wa mtaani. Saluni ndio mitaa yangu ya
kujidai. Huna utakaponisema saluni, maanti zangu wasinifikishie ujumbe.”
James akachoka.
“Sasa ndio nikaambiwa
Kemi amemuahidi Love atamsaidia kunitoa kwenye familia, sijui ‘umoja
wao wa familia’ kama walivyofanikiwa kunitoa kwenye familia yao.”
“Kwao walikutoaje?” “Hata sijui shem! Mimi ninachojua ni kwa Kasa niliondoka
mimi mwenyewe. Na yule mzee ananitaka mpaka kesho. Sema tu mimi simtaki
tena. Naona nitulie mpaka nije mpata mwanaume kama yeye ila anioe ndoa.”
“Sasa si ndio Colins!”
“Shem wewe hujaelewa. Mwenzio simtaki tena Colins. Ananiumiza roho bila
sababu. Kwanza kwao wana mambo mengi. Wataninyima raha bure. Mimi simtaki
tena.” Akaongea kama jambo la kawaida.
“Mimi nilifikiri
ulimpenda Colins!?” “Wala nisikudanganye shem. Kwa mara ya kwanza nahisi nilipenda.
Ila kama mapenzi ni vile, mimi sitaki tena. Bora nije niolewe na mtu
nisiyempenda kama Colins, ila niwe na raha.” “Jelini!” “Kweli shem. Mbona Kasa
sikuwa nikimpenda au niseme sijawahi kujisikia kwake kama vile nilivyokuwa
nikijisikia kwa Colins, lakini tulikuwa tuna raha shem! Asikwambie mtu.
Tulikuwa tukianza stori zetu, tunacheka mpaka machozi, tena ujinga tu. Na si
unamuona yule baba alivyo na maakili na hela, lakini tulikuwa tukiongea ujinga,
tunacheka bila kuchoka.”
“Anaweza akanipigia
simu katikati ya kazi, mchana kweupe, ananiambia amekumbuka hiki na kile
tulichokuwa tumezungumza labda siku iliyopita, akaanza kucheka peke yake, tena
saa ingine katikati ya mkutano mpaka watu wanamshangaa. Basi hapo tena tunaanza
stori. Hakuna chakuumizana roho, wala sijui ujinga kama huu unaoendelea kati
yangu na Colins. Mimi hivyo sitaki.” James akachoka kabisa.
“Sasa nikamwambiaje?”
“Mwambie mimi simtaki tena.” “Jelini!” “Basi tafuta jinsi ya kuzungumza
naye, ila ukijua mimi simtaki tena.” “Hutapata mwanaume kama
Colins, Jelini. Ame…” “Mimi mwenyewe sitaki mwanaume kama yeye.” James
hoi. “Wakuninyima raha! Hapana shem. Nyinyi mna mambo mengi yakuwafurahisha.
Kweli mimi kidogo nilicho nacho pia nikigawe! Leo ni yeye. Halafu nasikia tena
ndugu zake wapo kinyume na mimi! Akuuu! Kwa nini! Kwanza hayo ndio yatakuwa
maisha gani? Yaani yeye aninyime raha, na ndugu zake pia! Akuu.”
“Na kwa Kasa mbona
kama watoto wake walikuwa kinyume na wewe?” “Bwana yule mwanaume pale nilimuheshimu,
shem. Alisimama kama simba akinilinda, mpaka wanae walikuwa wakiniogopa. Wewe
unafikiri kwa nini Kemi alinichukia?” “Ulichukua nafasi yake.” “Basi umemaliza.
Alikuwa akimwambia kabisa, azungumze naye akiwa ofisini maana akiwa nyumbani
yupo na Jelini.” “Jelini!?” “Muulize Kelvin atakwambia maana na yeye kilimpata
kitu. Alijidai kunidharau, eti mimi mtoto wa mtaani tu, malaya, nashinda
baa. Maneno kama hayo anayosambaza Love huko kwa kina Colins. Acha baba yake ambadilikie.
Muulize, atakwambia. Mimi ndio maana nikabaki naye. Maana Kasa alinijua ndani
na nje, lakini bado akaniheshimu. Nikiongea, ananisikiliza. Nikiwa naye,
utafikiri dunia nzima tupo peke yetu! Huwezi mfananisha na Colins kwangu hata
kidogo. Ndio maana mimi nililia sana nilivyomfumania.” James akabaki ameinama. KAKWAMA.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Shem wewe ungeenda
tu kumpumzika.” “Basi nikuombe jambo la mwisho.” “Juu ya nini?” “Naomba ukutane
na Colins mzungumze.” “Basi kumbe wewe shem hujui! Nilikuwa kwake, tukazungumza
kila kitu. Akanieleza kwa mapana na marefu ndio nikaja kufikiria, nikajua
yeye hatakuwa mume wangu. Ananinyima raha.” Jelini akawa amemaliza,
akabaki akimwangalia shemeji yake. Kimya.
“Yaani kama hujaelewa
shem, mimi na Colins hatuna chakuzungumza tena. Sitaki tena.”
“Nimekuelewa Jelini. Ila naona kama unatupa bahati.” “Acha tu ipotee.
Nitajua mbele ya safari. Kwanza mimi mwenzio sipo kama Jema. Maswala ya kuolewa
hivi na kutulia nyumbani! Sio kabisa. Sasa hapa katikati nikataka kujaribu,
ndio nimeona kumbe ndio vigumu hivyo! Sitaki tena. Nikupe chakula shem?”
“Naona Jema
ananisubiria nyumbani.” “Ameniambi. Ujue Jema anakupenda sana?” “Najua Jelini.
Hata mimi nampenda mke wangu. Ananivumilia kwa mengi.” “Nikwambie shem,
uvumilivu unakuja kama mpo na mtu upande mmoja. Jema ameshajua upo naye katika
kila upande, ndio maana anakuvumilia. Huwezi kuvumilia usilolijua!” Hapo James
akakubaliana naye.
“Au uongo shem? Utamvumilia
mtu mwenye vifichovificho?” “Huwezi.” “Basi umemaliza. Mimi mwenzio si mbaguzi
wa watu. Kila mtu ninayemfahamu mtaani mshikaji wangu. Mpaka mateja mimi wangu.
Ndio maana mimi nazurura mpaka usiku, nasindikizwa na vibaka, mpaka utashangaa.
Kila kona hapa mtaani napajua na watu wake. Napenda na kuheshimu watu wote. Nawajua.
Na kuna maeneo japo wanaudhaifu wao, hata hao mateja nawavumilia. Huko saluni
naweza nikaenda, nikatoka nimependeza lakini sijalipa hata shilingi. Kwa sababu
sisi wenyewe tunajuana na kufaana nyakati ZOTE. Nikichoka au mambo sio
mazuri, nakwenda mtaani kucheka. Sasa leo niolewe, niwe na mawazo,
halafu eti nifungiwe ndani sina hata wakuzungumza naye! Akuu!” Hapo akapandisha
mabega kabisa na kunyanyuka kochini.
“Acha nikupe mzigo wa
Jema. Tena mama alinituma kwake leo, nimeona uvivu kutoka. Najua atampigia
kumuulizia kama nimepeleka.” “Sawa.” James akapewa huo mzigo tena Jelini akiwa
amesimama kumuashiria ndio waagane. Na yeye akawa muungwana, akaondoka.
Mjumbe Hauwawi.
Akiwa njiani
akampigia simu Colins. Akatafuta hekima ya kuzungumza naye. “Kwa jinsi nilivyomsikia Jelini, si kwamba hakupendi, ila
anawasiwasi na aina ya mahusino yenu. Anachoona yatamfanya aendelee
kuishi bila furaha. Ndio maana anaona asitishe.” Hapo akajisahau. “Kwamba hanitaki tena, sio kwamba anasubiria mpaka ndoa!?”
“Acha nikwambie ukweli Colins, anavyosema mazungumzo
yenu ya mwisho au ulichomwambia mwishoni, kilimfanya arudi kwao afikirie
zaidi.” James akaendelea kwa makini tu ila kwa uwazi.
“Yeye
binafsi anasema anakupenda sana. Lakini imekua adhabu. Ni bora vile alivyokuwa
na yule mzee, hampendi kama wewe, lakini alikuwa na furaha. Anasema kwako wewe
anakupenda sana, lakini imekuwa ni adhabu, na yeye hataki. Wewe unamjua Jelini
alivyo.” “Daah! Sasa kwa nini hukumwambia tukutane tuzungumze?” Lawama kwa James. “Nimemwambia Colins. Ila anasema mara ya mwisho mlikuwa
nyumbani kwako. Mkapata muda mzuri tu wa kuzungumza na wewe ukaongea vizuri tu.
Sasa hicho ulichomwambia eti ndio kimemfanya akafikirie na kugundua, hataki
tena. Ila habari njema, harudi tena kwa yule mzee. Amesema anajua yule mzee
bado anamtaka, lakini amekusudia hatarudi tena.” Akamueleza kwa kifupi
ila kwa makini mazungumzo yake na Jelini, mwishoe akasikia akimuaga bila ya
nyongeza. “Nashukuru kaka. Salimia familia huko.” Siku
zikaendelea ila taratibu isivyo kawaida kwa Colins. Mchana mrefu, usiku mrefu
zaidi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kemi Anaendeleza Mashambulizi. Amefanikiwa Kuingia Mpaka Kwenye Ukoo
Wa Kina Colins Kupitia Love. Mwisho Wake Ni Nini?
Jelini Na Colins Huo Ndio Mwisho?
Usipitwe.
0 Comments:
Post a Comment