“Baba wewe unataka kujiudhi bure, na kutengeneza
kesi yako mbele ya babu na bibi. Tafadhali acha mazungumzo yanayotuweka sisi
mbali zaidi na tulipo. Nilishakwambia swala la kanisani nitalifanyia kazi.
Nikishapata sehemu itakayoendana na mimi na mke wangu, nitaanza kwenda huko.
Kwanini kutaka kugombana na mimi kila wakati? Kwa nini hutaki kuniacha
ukaangalia ninachofanya?”
“Kwa sababu unapotea,
Colins! Huyo mwanamke uliyempata safari hii anakupotosha. Hauongozi
vizuri. Unakuwa kama umeharibiwa ufahamu kabisa!” Hapo Colins akashindwa
chakujibu kabisa. Akabaki kimya akimtizama. “Unanisikia Colins?” Akacheka kwa
masikitiko. “Unanidharau mimi Colins!?” “Nasikitika jinsi unavyojiandaa kumchukia
mke wangu. Maana ulishasema hutamkubali. Hilo halikuwa tatizo. Maana si
lazima wewe umkubali, ni mke wangu mimi. Sasa kukuona unajiandaa na kumchukia
pia! Ndio nasikitika. Na tafadhali naomba niwaombe kwa heshima baba, mama, bibi
pamoja na babu. Nina ratiba imebana kidogo, nataka nitoke sasahivi halafu hichi
kilichowaleta hapa, tafadhalini sana, kwa heshima zote, naomba tukifanye wakati
mwingine hata jioni.” Hilo ombi likawa baya zaidi. Likathibitisha kulogwa
kwake.
Mambo yakazidi kuwa
mabaya, hayaishi. Bila kutarajia, Love na wazazi wake na wao akashangaa
wanaingia hapo kwake. Mashitaka yakaendelea. Love akitoa mazito na makubwa
haswa juu ya Jelini mpaka kumshangaza Colins, maana alizungumza kwa kumfahamu
haswa. Mambo yakazidi kuwa makubwa na mabaya zaidi, Jelini akimsubiria waende
hospitalini.
Kwa Jelini.
Huku kwa Jelini
alipoona Colins hafiki mpaka mida ya saa 6 mchana, na yeye wasiwasi umemzidia,
alishajiandaa tangia saa nne asubuhi. Hana simu ya jinsi yakuwasiliana naye,
akajua tayari mambo ya familia yake yameanza. Hakutaka mengi. Alishakusudia
siku hiyo akapime afya yake. Akamuaga mama yake. “Si ulisema unakwenda na
Colins?” “Mimi hata sijui kinachoendelea mama. Colins aliniambia angekuwa hapa
saa 4 asubuhi bila yakukosa. Simuoni! Na mimi nazidi kuingiwa hofu. Maadamu
nimekusudia kwenda, acha tu niende nikajue moja kwenye maisha yangu.”
“Nikisema nimsubirie
Colins, mpaka lini mama yangu? Anamaisha yake na vipaumbele
vyake. Mpaka aje anikumbuke mimi, si leo. Na ni mimi ndio naendelea kutesema,
maisha yake na watu wa nyumbani kwao yanaendelea vizuri tu.” Akaongea kwa
kusononeka kweli. Mpaka hapo hata mama Jema akashindwa chakusema. Kwa kumsikia
Colins alisikika anamipango mizuri. Ila utendaji wake, kila mara anamuumiza
mwanae. Akabaki na yeye akiwaza.
“Ila naomba simu
nimpigie dada Doro yeye anajua mambo hayo. Anielekeze vituo hivyo vinavyoweza kuona
hata kama vijidudu vimeingia hivi karibuni. Na kama nimeathirika, yeye pia
anielekeze wapi pakupata dawa. Yeye anayajua yote hayo.” Hapo mama yake
akamsifu. “Kweli umeamua!” “Nakaa kwa hofu sana. Sitaki kuendelea kuishi na
sintofahamu hii.” Akachukua simu ya mama
yake na kuingia nayo chumbani.
Old is Gold
Kwa mara nyingine,
akampata Doro. “Ulinisusa mdogo wangu.” “Mambo mengi
dada. Ila kuna nilikopita hapa katikati, kunanitia wasiwasi, nataka nikapime,
nijue afya yangu. Nisaidie kunielekeza sehemu wanayoweza kuona hata kama
vijidudu vya UKIMWI ndio vimeingia karibuni.” Akamuelekeza. “Acha niende dada japo naogopa!” “Nani anakusindikiza?”
“Naenda peke yangu. Mama anaenda kwenye biashara zake.” “Acha basi nikupeleke
mimi. Ulinifaa sana kipindi nahitaji mtu. Au hutaki, bado umenikasirikia?”
“Yaliisha bwana dada. Nashukuru. Ila sina gari na hii simu ya mama.”
Wakajipanga pakukutania ikawa nyumbani kwa Doro, Doro akiwa amefurahi sana.
Jelini alikuwa mtu wake haswa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akamrudishia simu
mama yake, na kutoka hapo akiwa amependeza haswa, maana alijiandaa akijua
anakuja kuchukuliwa na Colins, kwahiyo akatoka hapo akiwa ameumia roho, akijua
ni mambo yake tu na Love ndio yanayomfanya azidi kumpa Love kipaumbele na si
yeye. Akanyongea haswa. “Nitaweza kweli!?” Akajiuliza bila jibu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mtoto wa jiji
akaunganisha usafiri mpaka nyumbani kwa Doro. Mpaka Doro akalia kwa furaha ya
kumuona Jelini. “Ulinitupa mdogo wangu.”
“Wewe ndiye uliyeanza kunisimanga dada. Nikaona unachoongea kweli, nikarudi
kwetu.” “Najuta mpaka leo. Ni bora vile tulivyokuwa tukiishi wote akilala siku
nzima kuliko kubakiwa na mimali yote hii halafu sina mtu wa kweli. Naomba
yaishe.” Zikaanza stori kuanzia walipoachana mpaka hapo.
Safari ya hospitalini
ikaanza. Vicheko wakipeana habari za watu wanaofahamiana. Jelini muoga wa
hospitali, sie huyo. Kajawa cheko. Anatolewa damu hana habari. Yeye na Doro
kazi yao kumaliziana sentesi. Ikaendelea mpaka anapewa majibu anajulikana hana
maambukizi yeyote ya UKIMWI, likawa tena si jambo la furaha kama
kukutana na Doro, shoga yake kipenzi. Simu kwa washikaji wa kijiweni kwamba
Jelini ameonekanika zikaanza. Wakapanga kukutana mahali. Cheko.
Ikawa imeshafika
jioni ya siku hiyo ya jumapili, kwa mara nyingine tena Jelini akarudi
baa. Zikaanza kuagizwa nyama choma. Stori, cheko. Jelini akaanza kwa kusema,
“Mimi siku hizi sinywi.” Lisaa la kwanza na la pili, vishawishi vikamzidia.
“Basi nakunywa tu moja.” Haikuishia moja. Wala haikuhitaji ushawishi mkubwa
kuongeza ya tatu na ya nne mpaka akapoteza mahesabu. Stori, anacheka kama
anatekenywa! Pombe ikaendelezwa.
Ubaya, Ubaya tu.
Huku kwa Colins,
jumapili aliyokuwa akiitegemea iwe nzuri, ikageuka kuwa mbaya haswa. Kesi ikawa
kubwa. Mzee yupo akidai anamuokoa mwanae kwa mwanamke aliyepata mashitaka yake
kuwa ni malaya tu wa baa. Anatembea na wazee kama kina Kasa. Alishazaa. Hayo yote
yaliletwa na Love akiwa amesindikizwa na wazazi wake siku uliopita, ya jumamosi.
Wazazi wa Colins wakaelezwa kwa mapana na marefu juu ya Jelini, mpaka mama CJ
akajuta kumfungulia mlango Jelini.
Jumamosi.
“Hakika sikujua kile
kilio cha yule binti ni kumlilia mzee kama yule!” “Sio binti yule anti. Ni
mwanamke kabisa ambaye ana mtoto mkubwa tu. Na nasikia ni muharibifu.
Kila akiingia kwenye familia ya watu ni kuharibu kama hivi mnavyomuona Colins
ameharibika. Huko kwa Kasa nasikia ameharibu kwelikweli. Kafarakanisha watoto
na baba yao. Unaambiwa huyo mzee alikuwa akipenda vijana wake, lakini baada tu
ya kuingia Jelini, mzee amewafukuzisha kazi binti yake na mumewe. Kijana wake
ambaye ndiye kama mrithi wa huyo baba, ambaye huyohuyo Jelini nasikia
alimtongoza yeye kwanza, kijana akamkataa, akamfuata baba mtu, naye
amewafarakanisha kabisa kwa maneno ya uongo na kiuchonganishi. Huyo mzee Kasa
amemfukuza kijana wake kabisa sababu ya huyohuyo Jelini.” Love aliendelea mbele ya wazee hao usiku huo
wa jumamosi.
“Tena hapo ni baada
ya kumfukuzisha kazi binti yake huyo mzee Kasa kwenye kampuni ya baba yake.
Inavyosemekana huyo binti ndiye aliyekuwa akimkaimu baba yake kwa miaka mingi
sana. Na mumewe hivyohivyo huko Shinyanga. Lakini unaambiwa kwa muda mfupi tu
huyu Jelini alipoingia kwenye maisha yao, amefanikiwa kumtenga huyo baba na
kila mtu akabaki yeye tu mwenyewe akimtawala. Wanavyohisi huyu Jelini anatumia
nguvu za giza.” Love akazidi kuwaogopesha sana wazazi wa Colins.
“Nasikia akianza na
mwanaume, anakuwa kama hivyo Colins. Kila mtu anamuona mbaya. Wanasema anakuwa
kama anawateka ufahamu kabisa. Akisharidhika hapo, ndipo sasa anaanza kumtenga
huyo mwanaume na kila mtu ili abaki peke yake azidi kumtawala na kumfilisi
kabisa.” Love akaeleza.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ndipo sasa ikabidi
mzee ampigie simu baba yake ambaye ndiye babu yake Colins ambaye Colins
alimshitakia huko. Mzee akaeleza kwa masikitiko makubwa, na hofu kubwa sana.
Akimuomba baba yake amsaidie kumuokoa kijana wake wa pekee. Ndipo sasa babu
akaacha kila kitu na kukimbilia jijini, kufanya hicho kikao kilichochukua
karibu siku nzima.
Siku Ya Kufa Nyani, Miti Yote Huteleza.
Colins alifika
nyumbani kwa kina Jelini mida ya saa 11 jioni. Akakuta nyumba imefungwa. Huna
jinsi ya kumfanya Jeremy akufungulie mlango, kama hajaambiwa na bibi yake.
Atanyamaza ndani kimya kama hayupo. Baada ya kubisha hodi na kuchoka, akaamua
kumpigia simu mama Jema.
“Samahani
mama yangu. Namtafuta Jelini.” “Atakuwa nyumbani.” Jinsi alivyojibu,
Colins akajua si kwema. “Nimegonga, hakuna
aliyefungua.” “Basi atakuwa hajarudi.” Colins akatulia kidogo kisha
akaendelea kabla hajakatiwa simu. “Samahani kwa
usumbufu. Sijui unajua alipokwenda?” “Kwani nyinyi mlikubaliana leo mnakwenda
wapi na saa ngapi?” Colins akajua amekasirika, asijue na yeye anahali
mbaya kuliko yake.
Hapo ametoka kwa
lazima nyumbani kwake, akiwaacha wazee bado wanataka kikao na yeye. Akawaambia
lazima aondoke, kikao kiendelee wakati mwingine. “Ilikuwa
nije kumchukua asubuhi ya saa nne, lakini nikapata wageni wa gafla. Babu na
bibi wakisindikizwa na wazazi walikuja kwangu. Hivi nimelazimishia tu
kuondoka.” “Basi yeye alichoka kukusubiri. Akijua mambo yako ya familia
yatakuwa na maelezo kama hivyo, halafu yeye ndio aje akumbukwe kama hivi.
Akaona amtafute Doro, amsindikize.” Moyo wa Colins ukapasuka kama kumeangushwa
chuma.
“Doro
tena!?” “Ndiye aliyekuwepo na kuweza kumsaidia! Jelini muoga wa hospitalini.
Hajiwezi mbele ya sindano bila mtu. Wewe upo na familia yako. Mimi natafuta
pesa ya chakula kwa ajili yake na mwanae. Sasa ulitaka akwame akiwa
anakusubiria wewe ambaye kila leo kunakuwa na sababu ya msingi ya kutokumpa
yeye kipaumbele? Ulitarajia kweli akwame akikusubiri wewe mpaka lini?” Colins akaanza
kumuelewa James juu ya mama Jema na wanae. “Jelini hana
simu mama yangu. Nitampataje huko aliko?” “Sijui.” Akamjibu hivyo na
kuagwa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ikabidi akae nje ya
nyumba mpaka giza likamkuta. Saa moja, mbili, tatu, Jelini hajarudi. Saa nne
usiku mama Jema akawa anaingia, akashuka kwenye gari yake na kumsogelea mama
Jema aliyekuwa ameshushwa na pikipiki. “Bado tu upo!?” “Najua nimekosa mama
yangu. Nisaidie jinsi ya kumpata Doro. Simuamini Doro akiwa na Jelini. Nisaidie
kunielekeza anapoishi au namba yake ya simu.” Mama Jema akafikiria.
“Wewe utamchanga
Jelini, Colins. Kwa nini usiweke sawa mambo ya nyumbani kwenu kama ulivyosema,
kisha kumtafuta? Jelini alikusudia kutulia kabisa. Lakini kwa jinsi unavyo mchanganya,
nirahisi sana kurudi kule kwenye pombe zilizokuwa zikimsaidia kuficha
kinachoendelea moyoni. Asubuhi unakuwepo, jioni unapotea na
kumuacha akisononeka hapa kwa uchungu sana. Utaendelea hivyo mpaka
lini?”
“Nimeamua
kumuoa Jelini, mama yangu. Na hata babu na wazazi nimewaambia leo. Aidha
wapende wasipende, mimi nitamuoa Jelini. Love amepewa maneno machafu
sana juu ya Jelini, naye ameyabeba kama yalivyo amewaambia wazazi, wazazi nao
wameyabeba kama yalivyo na kuwamwagia bibi na babu ambaye alikuwa upande wangu.
Sasahivi wote wapo kinyume, hawamtaki Jelini kwenye ukoo.” Mama Jema akashituka
sana.
“Amesema nini?” “Mambo mengi wala
hayatasaidia. Na mimi mengine ndio nimeyasikia leo.” “Juu ya huyo Jelini?”
“Unataka nikwambie ukweli wote?” “Hata ukificha itasaidia nini? Bora niambie
tu.” “Tabia zote za Jelini kushinda baa, na zaidi mzee Kasa. Hapo ndio parefu
na papana.” Colins akamueleza mpaka yule mama akakaa chini kwenye kibambaza.
“Colins!?” “Yaani ni
mengi na marefu. Hapa nimelazimishia kuondoka. Wamejaa hapo nyumbani kwangu,
wote wananihurumia kwamba akili sio zangu, nimelogwa. Ila hitimisho la
babu, ameniambia nisimwingize Jelini kwenye ukoo wake.” “Sasa utafanyaje?”
“Kama nilivyowaambia wazazi na kina babu pamoja na familia ya Simba, Jelini
ndio mwanamke nitakayezeeka naye. Ndiye mwanamke pekee atakaye pokea kiapo
changu kanisani, kwamba, mpaka kifo. Na nitasimamia hapo. Tafadhali
nisaidie kumpata Jelini. Nina hisia mbaya sana. Asije kuwa amerudia pombe kitu
ambacho amesema ameamua kuacha kwa ajili ya mtoto. Sasa kitendo cha kutokuwepo
hapa na mtoto mpaka muda huu, hisia zangu zinaniambia vinginevyo.”
“Sasa anakoishi Doro
mimi sipafahamu. Labda tutafute namba aliyompigia Doro asubuhi wakaenda
kuzungumzia chumbani. Walichozungumza huko sijui.” Akamkabidhi simu. Colins
akapekua hiyo simu mpaka akafika namba zilizopigwa asubuhi. Akamuonyesha kama
hiyo anaitambua, hakuwa akiitambua. Akaichukua.
“Nikuulize kitu kabla
hujaondoka?” Colins akatoa macho kwenye simu akiwa anaelekea kwenye gari yake.
“Utafanyaje kweli ukimkuta baa na amelewa? Maana mimi Jelini namjua. Muoga wa
matatizo. Nina uhakika kwa asilimia 100 sasahivi atakuwa amelewa huko. Na hivi
yupo na Doro!” “Nitamchukua mama yangu. Siwezi kumuacha huko na siwezi kumleta
hapa akiwa amelewa. Najua atajisikia vibaya sana asubuhi pombe ikiisha.” “Sasa
unataka kumpeleka huko wanakomsema na tabia zake hizihizi!? Maana
itakuwa kama unakwenda kuwathibitishia huko kwenu.”
“Ninauhakika kwa
asilimia kubwa, watakuwa wameshaondoka. Na pia nitampigia simu mlinzi
kuhakikisha hamna mtu hapo kwangu ambako naishi peke yangu. Tafadhali usiwe
nawasiwasi. Mimi ndiye nimeharibu leo na kumfikisha hapo, na mimi nakuahidi
kumlinda Jelini. Wakati wote nitamlinda. Akiwa mikononi mwangu, nakuhakikishia
atakuwa salama. Ila sasahivi lazima niende kumtafuta. Siwezi kulala wala
kufikiria nikiwa sijui alipo.” “Mmmh!” Mama Jema akaguna akiumia moyoni. Maana
yeye alikuwa akimuacha tu. Hata akipotea siku tatu, alikuwa akijiambia atarudi,
leo Colins anakwenda kumsaka! Akapoa kabisa.
“Nakushukuru Colins. Na
tafadhali nijulishe pindi utakapompata. Na sijui utampataje, maana na Doro
mwenyewe ni mlevi haswa. Anaweza asipokee simu mida hii ambayo atakuwa
ameshalewa.” “Usiwe nawasiwasi.” Akaondoka kama akimbie na kumuacha mama Jema
na hukumu pamoja na mawazo.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kazi ya kumsaka
Jelini ikaanza. Akaanza kwa kumpigia simu Doro. Ikaita bila mafanikio.
Akajaribu kukumbuka jina la baa aliyosikia Love akisema ndiko anakoishi Jelini
akibadilisha waume za watu. Akiwatumia mpaka vyooni. Akafika hapo, akauliza.
Kweli walikuwa wakimfahamu Jelini na Doro, ila wakaambiwa siku hiyo
hawajaonekana hapo. Wazo la kwenda kwa mzee Kasa likamjia usiku huo.
Kwa tajiri hupotei.
Akampigia simu mwanae akitaka kujua baba yake anapoishi. Kwa mshangao sana,
Kevin akamuelekeza. “Ila mida hii mzee anakuwa
ameshalala. Hawezi kukuona. Kwema?” “Nashukuru sana. Kwaheri.” Hakutaka
mengi, akamkatia simu, safari ya kwa baba yake ikaanza.
Mafahari Wawili.
Akafika getini
akaambiwa hivyohivyo. Mzee amelala, haamshwi isipokuwa ni dharula. “Sasa hii ni
dharula. Mwambieni Colins amesema ni dharula. Lasivyo mimi naondoka, na
nikiondoka hapa, kesho hamtaelewana naye, na kibarua hapa kitakuwa kimeisha.”
Akawatisha kwa mengi mpaka wakaona bora kwenda kumuamsha. Baada ya muda akaona
anafunguliwa geti, akaingiza gari yake mpaka ndani, akamuona kwa mbali
amesimama kwenye ngazi.
Akashuka garini na
kumsogelea akimtizama tu. “Nimekuja kumfuata Jelini.” Akamwambia hivyohivyo.
Mzee akabaki akimtizama kwa muda kisha akaweka mikono mfukoni. “Jelini yuko
wapi?” “Umechanganyikiwa au unakitafuta kifo kwa nguvu.” “Hakika
sasahivi huna utakaloniambia na kunitisha. Namtaka Jelini, bila hivyo
hapa siondoki.” “Sema utaondoka maiti. Kwa sababu umebakiza dakika chake
sana nakupiga bastola, Colins.” “Mimi sijakufuata wewe, nimemfuata Jelini. Na
kwa taarifa yako, ni mke wangu. Tutazaa watoto wanne.” Kasa akamcheka na
kumuudhi zaidi Colins.
“Acha dharau.” “Sasa
kama hayo unayoongea unayaamini, kwa nini upo hapa kwangu usiku huu?”
“Namtafuta Jelini wangu.” “Kama kweli ni wako, hajakuzalia hata mtoto mmoja
bado, tayari umeshampoteza! Wewe utakuwa baba au mume wa namna gani?!”
“Usizidi kunichanganya.” “Nakwambia ukweli. Wewe ulishasikia Jelini kupotea
kipindi yupo kwangu?” Kimya kwa muda.
“Wewe ni mzembe.
Unang’ang’ania mambo usiyoyaweza.” “Namuweza Jelini.” “Yuko wapi sasa?”
“Mbali na ile baa ya Tegeta, wapi kwengine unafikiri anaweza kuwepo?” “Yaani mara
hii tu umeshamrudisha baa!?” “Acha kuniuliza maswali ya kunidhihaki.” “Mimi
nilipokuwa na Jelini, alitulia na kuacha pombe kabisa. Huko alikokuwa
akijifichia huzuni zake, ALIONDOKA. Nikaweza kumtuliza,
akatulia. Wewe umekua naye hata…” “Acha kabisa kunilaumu mimi. Wewe
ndiye uliyemrudisha Jelini huko sababu ya kupenda hovyo wanawake. Jelini
anawasiwasi akihofia umemuambukiza UKIMWI.” Kasa akakunja uso.
“Acha kujidai
huelewi. Sio wewe uliyekufumania hapa kwenye dangulo lako? Na anakujua huwa
hutumii kinga. Tokea akufumanie mpaka leo, Jelini halali vizuri sababu
ya wasiwasi pengine umemuambukiza vijidudu vya Ukimwi. Wewe ndiye
uliyemuharibu. Na nipo hapa kwa kuwa wewe unahusika kwa kumpoteza mke wangu. Na
nakuonya acha mtindo wa kunitisha. Sitishiki kirahisi. Niambie
maeneo unayodhani anaweza kuwepo, nikamtafute.” “Nini kinakupelekea kufikiri
nitakwambia alipo?” Colins akamtizama kwa muda akawa kama na yeye amegundua
kitu kwa Kasa.
“Unanipotezea tu
muda, hata wewe hujui alipo kama mimi tu.” “Nipe masaa mawili tu kama hujasikia
Jelini ameamkia hapa nyumbani kwangu.” “Nakuonya. Kaa mbali na Jelini.”
“Wewe si unataka kujifananisha na mimi? Sasa kaa pembeni uone baada ya masaa
mawili kama hutasikia Jelini ametulia humu ndani. Na ndipo utakapojua kama hili
ni dangulo au sehemu pekee iliyokuwa ikimtuliza Jelini na
kumfanya asizurule tena mtaani.” Kidogo akatishika.
“Nakwenda kumtafuta
mimi mwenyewe. Acha ujuaji kwenye mambo yasiyokuhusu. Na nikikuona karibu na
Jelini, nakuchoma kisu.” Akamtisha Kasa. “Nakupa mpaka asubuhi.
Nisipopata simu yako ya kuwa umempata Jelini, ujue mimi nitamtafuta. Na
nikimpata mimi, hakika nisikuone tena Colins. Nitakuadhibu mpaka
ujute kumfahamu Jelini. Kama unadhani nakutania au nakutisha, muulize Kevin
linapofika swala la Jelini kama huwa natania. Nitakuweka mbali na dunia
aliyopo Jelini, hutakaa ukamuona tena. Haya toka haraka kaanze
kumtafuta. Na asubuhi nipate majibu ya kueleweka si ujinga na uzembe.
Unapotezaje mwanamke kama Jelini?!” “Wewe…” “Toka na usirudie tena kunijibu.
Ondoka haraka kabla sijabadili mawazo na kuamuru ufungiwe jela, na usitoke
mapaka uje ukutane na hao watoto wa nne wa Jelini lakini ni wa Kasa.
Potea.” Colins akatoka hapo kwa haraka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jelini!
0 Comments:
Post a Comment