Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 49. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 49.

Mzee akiwa kwenye maandalizi mazito kupika na kurudia kufanyia mazoezi ya jinsi atakavyozungumza na Jelini huku akikosoa hiki na kile kwamba hakifai, atoe hiki aongeze kile, akapokea simu kutoka kwa Ndosi. “Nina habari si njema sana mzee wangu.” “Usiniambie kwamba Jelini haji tena!”  “Amesema atatuma mtu jumamosi ijayo kumchukulia hivyo vitu vyake.” Kasa alitupa simu mbali sana na yeye. Kisha kuanza kupasua meza iliyokuwa na chakula. Kwa kuwa sahani na mabakuli vilikuwa vya kioo, dongo vile vizito vya ukweli, vilianguka na kutopasuka. Basi akasaidia kupasua moja baada ya nyingine. Wafanyakazi wake walipoona hivyo, kila mmoja akaenda kujificha kivyake mpaka amalize ndio warudi kusafisha. Kisa, Jelini!

Kwa Jelini.

Jelini akarudi kwa dada yake akamkuta amebaki peke yake. “James ameondoka na yeye sasahivi. Mama yeye naona ni kama mliongozana. Hakukaa sana baada ya wewe kuondoka. Ila amefurahia pesa ulizompa huyo! Anasema imekua kama ameokota alumasi!” Jelini akacheka tu akikaa. “Vipi lakini kichwa?” “Naendelea vizuri. Hapa nimekurudishia gari nimfuate mama. Nataka nijifunze anavyofanya kazi. Mama anajuhudi Jema! Mpaka nahisi mimi nimechukua uvivu kutoka kwa huyo mwanaume aliyempa mimba yangu.” Jema alicheka sana.

“Haki tena Jema. Mimi mpaka nasema pengine ndio maana mama aliachana naye, labda alikuwa mvivu sana!” “Na baba yangu mimi naye?” Wakaanza kucheka wakifikiria baba zao na sababu za kutokua na aina ile ya mama kama mke. “Ila bwana umejua kumfuta mama machozi!” “Mwenzio mimi amekuwa akinifuta machozi maisha yangu yote. Na mwanangu.” Akamuona amepoa.

“Unafikiria nini?” “Unakumbuka vile nilivyokuwa na mimba ya Jeremy?” “Halafu ulikuwa mdogo Jelini, halafu mkali haswa!” “Ni hofu na uchungu Jema. Ukumbuke nilikuwa nikibakwa kikatili mno. Kwa hiyo nilikuwa na maumivu ya roho na mwili muda wote mpaka niliposhika mimba akaniacha, ndio mwili ukapona ila si maumivu ya roho! Halafu nilikuwa silali sababu ya hofu ya kuja kumtoa mtoto kulekule kwenye maumivu, halafu nilikuwa sijui nakuja kufanya naye nini!”

“Sasa kitendo cha chupa kupasuka, nalia, mama akanisaidia mpaka kunipeleka hospitalini, nikadhani ataondoka, lakini akabaki na mimi! Halafu kujifungua tu, akamtawala mtoto kama wake! Pale ndipo nikarudisha tumaini, na hofu kupungua.” “Na mama alihangaika na Jeremy  jamani! Kuanzia mpo hospitalini mpaka mnatoka, kama yeye ndiye kazaa!” “Kumbe unakumbuka Jema?” “Kabisa.”

“Ile ilinisadia sana kutulia, na ndio kumpenda mama kukazidi. Hakujua tu alichonifanyia, ila nikikubwa zaidi ya hizo pesa anazohangaika nazo sasahivi. Mama hajawahi kunichoka mimi na mwanangu hata mara moja Jema. Akimuongelea Jeremy ni kama mwanae wakuzaa!” “Mimi nafikiri ndivyo anavyomuhesabu.” “Kabisa. Mimi sikuwa nikijua umwa ya huyu mtoto wala vaa yake. Ni mama. Nilikuwa nikiishi naye, nina uhakika wa maisha yangu na mwanangu na sijui bwana alikuwa akifanyaje! Wakati wote Jeremy alikuwa msafi na anachakula bila kuzembea!” “Si kama sisi tu! Mama hajawahi kutulaza njaa aisee yule mwanamke! Muhangaikaji hivyohivyo, siku zote!” Wakatulia kidogo wakimfikiria mama yao.

“Ila ninachotaka kusema Jema, hiyo pesa ilipotea njia ili imfikie mama wala si yangu. Mimi nikiishika tu, itaisha yote kwa matumizi yasiyo maana. Lakini sasahivi mimi na Jeremy tunakula vizuri kweli pale nyumbani. Mama anafanya manunuzi ya pale ndani na kulipa bili zote bila kuwapigia simu kina mama mdogo kuwakopa! Hilo linanifariji, hujui tu Jema.” “Hata yeye mwenyewe anasema anapambana msirudi tena kule kwenye kuombaomba. Na naona wanajipanga hapa na James, atafanikiwa sana tu. Mungu atasaidia.” “Na mimi nitaongeza nguvu.” Akaongeza akiwaza.

“Lakini isiwe sasa, Jelini.” Hakutegemea. “Nataka kuwa kama wewe Jema!” “Mimi nilifanya kazi kwa bidii kwa kuwa sikuwa mgonjwa. Wewe ni mgonjwa Jelini. Hizo dawa za kupunguza maumivu zisikudanganye, ukajisahau, baada ya muda ukarudia hali mbaya zaidi ya hiyo. Jiuguze mpaka upone kabisa, ndipo uhamishe akili kazini.” “Jema wewe! Mwenzio nipo nyuma sana!” “Najua na mimi nakuunga mkono kwenye kutoka hapo. Ukipona tu, hata mimi nitakuhimiza.”

“Ni kwambie ukweli Jema?” “Nini?” “Ukweli hiki kichwa si chakupona hivi karibuni. Sitaki tu kusema. Nilimsikia yule daktari akimwambia Kasa siku moja hospitalini wakidhani nimelala, alisema ndani nimeumia sana, mbaya ni kichwa. Mpasuko ulikaribia ubongo kwamba hata fuvu la kichwa lilipasuka ndio kufikia karibu na ubongo. Alisema itachukua muda mrefu sana kupona. Sikutaka tu kumwambia mama.”

“Basi mama amejua kupitia Colins.” Jelini akakunja uso kwa mshangao. “Colins halali kwa ajili yako Jelini. Anahangaika sana.” Hakuamini. “Na mimi!?” “Kabisa, mpaka utamuhurumia. Alimwambia James, hakumbuki kulala usingizi mzuri tokea usiku wa kwanza ametoka hospitalini kumuona Love, akiwa amevunja miahadi yenu, kisha kukukosa kwa simu. Anasema hakumbuki kulala tena.” “Lakini nilimpigia simu siku inayofuata Jema! Hakupokea simu yangu wala kurudisha ujumbe. Mimi nikaona nimuache tu.” “Mimi sijui nini kilitokea Jelini, lakini yule kaka ni majibu ya maombi yako.”

“Colins hawezi Jema. Ana Love. Na ikifika kwenye swala la Love, yupo radhi kufanya lolote ilimradi iwe Love KWANZA. Mimi hivyo siwezi Jema. Na mimi nataka mtu wangu wa peke yangu kama hivyo wewe. James anakupenda Jema. Kweli unataka mimi niishie na mtu kama Colins!?” “Mimi nahisi bado hujamjua Colins kama ambavyo mimi nimeweza kumfahamu sasa hivi. Hivi unajua simu zote anazokupigia James, anakua amesimamiwa na Colins, akitaka.., au acha niseme akilazimisha akupigie, ajue jinsi unavyoendelea?” “Colins!?”

“Hakika tena. Wanagombana hapa na James, mpaka nawafukuza ndani nawaambia wakamalizie malumbano yao huko nje. Maana James analalamika mambo anayotaka akufanyie mwishoe wewe utakuja kumuona anavuka mipaka.” “Wala nisikudanganye. Mpaka nilimgusia mama ila kwa mipaka kidogo. Nikajiuliza, kujali kwa shemeji, ndio kujali gani huko!?” “Basi ni Colins huyo. Hata Chaz ujue anatumwa na yeye huyohuyo Colins kwa jina la James.” “Jema!” “Sikudanganyi Jelini. Haya, dawa pia ni yeye mwenyewe Colins.” Jelini akabaki ametoa macho.

“Colins!?” “Hakika Jelini. Yaani umemkuta hapa leo, sababu aliombewa msamaha kwa mama, alipoambiwa tu amesamehewa na akajieleza hakukusudia kukuumiza ni shindikizo la wazazi, hapohapo akaja kuanza kuweka mashariti ya jinsi gani uhudumiwe.” Jema akamueleza yote.

“Colins anakupenda Jelini!” “Ila mimi sitaweza Jema. Japokuwa nampenda sana, lakini siwezi. Kwao wana mambo yakizungu na umoja ambao huo sitaweza. Mimi nataka mtu atakayenipenda na kunijali kama hivyo yeye anavyomfanyia Love. Sasa leo aje anioe halafu aniache ndani aniambie nakwenda kwa Love sijui familia imesema hiki au kile! Hakika sitaweza Jema. Mshauri tu aache.”

“Natamani kama haya ungekuwa ukizungumza na James. Maana yote hayo James ashamkaripia nayo. Tena sio kama hivyo wewe. Ni kwa kugombana kabisa.” “Sasa anasemaje?” “Hata leo amemwambia na mama. Kuwa huo utaratibu wa kwao yupo kwenye kuweka kikomo. Hivi hapa hata nyumba ametuambia anarekebisha kwa ajili yako na watoto wenu. Amemwambia mama amemuita hata babu yao ili aje awaweke wazee wake sawa. Ili aheshimiwe, abaki kuwa na wewe tu na mjenge familia yenu.” “Jema!?”

“Kama huamini muulize mama. Amejieleza leo hapa, mpaka utamuhurumia. Mwenzio anamipango na wewe, tena mikubwa. Na anajua amekuumiza sana tu. Ila anasema anataka aweke mambo sawa ndipo akurudie. Hataki kurudi kisha kukuumiza tena na mambo ya kwao. Anachotaka arekebishe kwanza kwao ndipo akurudie.” Jelini akabaki kimya akifikiria.

Penzi Lisilo Changanywa Na Pesa.

La Dhati.

Ilipofika mida ya jioni Jelini na mwanae wakaondoka kurudi nyumbani. Bado mama yake hakuwa amerudi nyumbani. Kwa kuwa walishakula nyumbani kwa Jema, Jeremy akapitiliza chumbani kwake kufanya yake, mama mtu chumbani kwake kubadili nguo. Lakini akiwa anamfikiria sana Colins. Moyo wote upo kwa Colins. Hakujua kama anamuhangaikia kwa kiasi hicho. Moyo ukajawa penzi, akashindwa kujua chakufanya. Tatizo akabaki Love. Akamtumia ujumbe.

‘Nashukuru sana kwa msaada unaonipa hapa nyumbani na dawa. Asante.’ Colins alipopata tu huo ujumbe, akili ikaruka na kujua moja kwa moja ni Jelini. Akamjibu. ‘Nakufikiria Jelini wangu. Nakufikiria sana. Nipe tu muda.’ Jelini akafikiria, akaona amjibu. ‘Naomba wewe endelea tu na maisha yako, Colins. Mimi sitaweza, kwanza sitaki. Na mimi nataka mtu wangu kama hivyo Love alivyokupata wewe.’ Wakati anatuma  huo ujumbe, akamsikia mwanae analia chumbani. Akashituka sana. Akarusha simu kitandani na kukimbilia chumbani kwake.

Akakuta analia, amekaa chini, vitu vyake vimezaa sakafuni. “Kuna nini!?” “Nimeteleza na kuangukia treni yangu, imevunjika yote.” Akazidi kulia. “Umeumia?” “Nimeharibu treni yangu yote!” “Usilie, njoo tujenge wote. Nitakusaidia.” “Wewe hujui.” “Jeremy naye, si utanifundisha!” Akazidi kulia. “Nakuahidi nitakaa hapa chini nijenge na wewe.” “Wewe hujui. Na nikianza kukufundisha ujue ndio nazidi kuchelewa.” “Basi kama hutaki kunifundisha, uwe unanituma vitu nakuletea.” “Nimejenga muda mrefu sana. Mimi sitaki tena.” “Jeremy wewe unakata tamaa! Ujue ukirudia tena hutachukua muda mrefu kama mwanzo kwa kuwa sasahivi unajua sio kama mwanzo. Njoo mtoto mzuri. Njoo tuanze.” Akaendelea kulia amekaa chini.

Jelini akaanza kukusanya. Vilikuwa vimesambaa chumba kizima. Sakafu hiyo mtelezo. Marumaru inang’aa, kitu kikianguka hakuna ukinzani. Kazi ya kuvikusanya ikaanza akimbembeleza. “Ujue wewe Jeremy ni mtoto mzuri sana? Halafu mimi nakupenda, unaakili. Na nina kuaminia. Ukianza sasahivi, mpaka muda wako wa kulala ukifika, utakuwa umefika mbali sana.” Akampamba hapo kwa maneno mengi, akanyanyuka kumsaidia mama yake kukusanya huku akilia taratibu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda wakiwa wameshakusanya vyote hapo chumbani, Jelini ndio amekaa chini kabisa kumuaminisha atamsaidia, wakasikia kengele mlangoni. “Narudi kuja kukusaidia. Usidhani nakimbia.” Jeremy akamwangalia bila kujibu akaendelea huku akifuta machozi na kamasi.

Kufungua mlango Colins. Akashituka sana. “Kwanini unapenda kunitesa bila sababu Jelini?” “Mimi nimefanya nini!?” “Kwa nini hujibu jumbe zangu na hupokei simu?” “Nikikwambia kwa maneno, hutaamini. Twende nikuonyeshe. Kwanza hata simu yenyewe sijui ilipo! Nifuate chumbani kwa Jeremy. Kule anakojenga vitu vyake.”  Hapo akapunguza sauti kama anamnong’oneza. Akashangaa kidogo ila akamfuata nyuma.

Kuingia, wakamkuta ameanza kulia tena huku anaanza kujenga. “Treni ya kaka imeparanganyika. Aliidondokea.” Hapo Jeremy akaongeza kilio. “Usilie Jeremy. Acha nikusaidie. Sasahivi nakurudishia iwe kama ulivyoijenga mwenyewe. Na nitakapofika ilipokuwa, niambie ili nisikumalizie.” “Nilikuwa nakaribia kumaliza! Reli yote ilikuwa tayari. Nimeharibu bahati mbaya.” “Usilie. Acha tuanze pamoja. Muda si mrefu itarudi kuwa kama mwanzo.” Colins akaanza kazi ya ujenzi wa treni ya Jeremy.

“Basi hata nitumeni kitu jamani! Mbona mnanitenga?” “Wewe hujui. Utaharibu zaidi.” “Mwaya Jeremy! Basi bwana kama hutaki msaada wangu.” Jelini akatoka kwenda kufuata simu akijua yapo majibu ya Colins.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akarudi chumbani kwake alipokumbuka alipokuwepo nayo mara ya mwisho. Akaikuta kitandani. Akakuta missed calls 5. Akashangaa sana. Akakimbilia ujumbe. ‘kwa jinsi ninavyokupenda, mimi nisingekukatia tamaa Jelini. Na wala nisingekususa kwa kumuachia mwanaume mwingine. Hujui ni kwa kiasi gani nilikuwa nikikusubiri. Hata nilipopigwa marufuku, nilibaki nikikusubiria tu, bila kukata tamaa.’ Mpaka Jelini akakaa kitandani. Akajifikiria, akaona atoke.

Kurudi chumbani kwa Jeremy akakuta Colins amekaribia kumaliza, Jeremy anafuraha huyo, cheko nje nje. “Muone!” “Anko anajua sana.” “Lakini hapa palipobaki nakuachia Jeremy. Malizia mwenyewe.” “Asante. Ila wewe unajua sana. Mbona unafanya harakaharaka hivyo! Mimi nimechukua siku nyingi kufika hapo ndio maana nilikasirika.” “Sasa nisikilize Jeremy. Hii spidi inakuja kwa kurudia kujenga zaidi ya mara moja. Hiki unachokifanya wewe unakumbuka nilikwambia nilifanya mara nyingi kwa miaka mingi zaidi ya umri wako?” “Nambuka.”

“Sasa ujue ajali kama hizi huwa zinatokea sana. Hata mimi nilikuwa nikiharibikiwa au kuweka LEGO moja au mbili sehemu isiyo sahihi. Kwa hiyo wakati mwingine nilikuwa nikibomoa ili nichomoe hiyo LEGO nyuma kuja kuweka mbele. Cha kwanza na muhimu, huu mchezo unafundisha kutokata tamaa. Kuna mambo mengine utakuja kupitia ukiwa mkubwa, yapo kama hivi vitu/LEGOs zikiwa hazijajengwa. Lazima kukaa chini na kuanza hatua ya chini kabisa mpaka kufika mwisho na uwezo wa kutatua tatizo kubwa kabisa. Kukata tamaa isiwe sehemu yako. Umeelewa?” “Sirudii tena anko. Ikiharibika, nitaanza tena.” “Hapo umenifurahisha. Haya endelea.” Wakatoka na Jelini.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Umekula?” “Hapana.” “Kuna chakula, acha nikupashie moto ule.” Akaongea hivyo na kuondoka akimuogopa kumuangalia. Colins akamfuata jikoni. “Katika mahusiano niliyokuwa nayo na Love, wakati wote alinionyesha hanitaki ni kama namghasi. Nikaishi naye nikijibidisha kumuonyesha naweza kuwa kile anachotaka bila mafanikio.” Jelini akabaki akimsikiliza ila kushindwa kumtizama kabisa akiwa ameshajua anachomaanisha.

“Ulipokuja wewe, na kuonyesha kunijali na kunihitaji mimi kama Colins, ikanitia moyo Jelini. Lakini umenibadilikia vibaya sana. Uliniacha nimesimama nje ya geti!” Jelini akaumia sana. “Leo unaniandikia ujumbe wa kunikataa!” “Ila siku ile nilikuaga Colins na nikakwambia kichwa kinaniuma naenda kulala.” “Hakika mimi siwezi kukufanyia hivyo Jelini! Eti uje kwangu, nikuache nje ya geti! Hata nisingeweza kulala.” Jelini akazidi kuumia.

“Nahisi nachanganyikiwa Colins. Sijui chakufanya, sijui nafasi yangu ni ipi! Najihisi ni kama nakulazimisha tu, ndio maana ikitokea Love anakuhitaji, inakuwa rahisi kuniacha mimi.” “Si kweli. Si rahisi hata kidogo, Jelini. Mwenzio nimeshindwa kulala usingizi mzuri tokea usiku ule. Sikuwa na jinsi Jelini. Ila nipo kwenye kutengeneza. Tafadhali usinichukie kiasi cha…” “Sijakuchukia Colins. Ila sielewi! Sijui hata nafasi yangu itakuja kuwa wapi kwenye maisha yako! Naishia kuumia tu kila wakati!”

Jelini akamuona anafungua vifungo vya shati kwa juu. Akakunja uso. “Unataka kujua nafasi yako?” Jelini akabaki ametulia. “Au ni kweli umenikatia tamaa kabisa?” akapandisha mabega juu kukataa kama kawaida yake. “Basi nipe mkono wako wa kulia.” Jelini akiwa haelewi akanyoosha mkono.

Akasogea mpaka karibu yake na kuuweka moyoni mwake. Jelini alikuwa akitetemeka mwili mzima. Amemshika Colins kifua! “Maadamu hayo mapigo ya moyo yanaendelea kudunda kwenye huu mwili, ujue hakuna mwanamke mwingine kwangu ila wewe tu Jelini. Itabaki hivyo mpaka uje uhakikishe hakuna unachosikia kwenye huu moyo wangu, ndio ujue umepoteza mtu wako wa peke yako.” “Kweli Colins? Maana na Kasa alisema maneno yanayo fanana kama hayo, lakini nikaja kumfumania na mwanamke wake. Kama hivyo wewe na Love.”

“Mimi sio yule mzee. Na swala la kuachana na Love sio nita, ni nimeshaachana naye. Hayupo kwenye maisha yangu na wala hatawahi akarudi. Umebaki peke yako na itabaki hivyo mpaka kifo changu.” Jelini alifurahi, akabaki hajui chakufanya. Ila akatoa mkono hapo kifuani. “Naomba amini mimi ni wako mpaka kifo, na anza kuishi na mimi hivyo.” “Nilikata tamaa Colins.” “Isiwahi kutokea. Si kwangu. Ujue nitabaki na wewe mpaka unichoke.” “Mimi siwezi kukuchoka. Mwenzio nakupenda Colins.” Kisha akaongeza.

“Safari hii jishike na wewe mapigo yako ya moyo.” Colins akacheka akijishika ila nje ya kifua. “Mmmh!” Akataka kujua anataka kusema nini baada ya kujishika. “Basi, kila unapoyasikia hayo mapigo yako ya moyo. Popote ulipo. Muda wowote, hata kama mimi hunioni, ujue yupo Jelini anayekupenda kwa moyo wake wote, mpaka niondoke hapa duniani. Hakuna ulimwengu utakaokuwepo wewe, nisikupende Colins. Ujue nitakupenda mpaka kifo chako.” Colins akataka kumuwahi ambusu.

“Bado sijapima, Colins! Tafadhali naomba tusubiri.” “Siwezi. Bora uniue wewe kuliko kuja kufa na kitu kingine. Siwezi kuishi bila wewe Jelini. Niruhusu angalau kukukumbatia na kukubusu tu. Mengine naweza kusubiri.” Jelini akafurahi huyo. Alipomuona amelainika, akamsogelea. Colins alipoipata midomo ya Jelini tu, na yeye hali ikabadilika. Jelini akajiachia hoi hajiwezi mikononi kwa Colins. Alikuwa haamini.  Amepata midomo ya Colins! Akajisogeza zaidi. Wakalemewa kabisa, Colins akajikaza kiume, akamuachia taratibu, wote wakihema.

“Nimefurahi Colins! Nimefurahi sana.” “Sasa umefurahia nini?” “Wewe kunikiss hivyo! Nimepatwa na hisia za ajabu! Sijawahi jua kama zipo ndani yangu hisia za namna hiyo! Asante.” “Nakupenda Jelini. Nakupenda sana. Usije wahi sahau hata siku moja.” Akatigisha kichwa kukubali akicheka. “Sasa unacheka nini!?” “Nimefurahi sana. Hujui tu.” “Kweli Jelini?!” “Mimi sijui bwana! Lakini ninavyojisikia kwako Colins, aisee ni hisia za tofauti! Acha nikupashie chakule ule, nikubembeleze ulale.” Colins akacheka asiamini.

“Nakaribishwa tena chumbani?” “Si umesema hujalala vizuri tokea siku ile?” “Nimechoka Jelini. Nikilala sitaweza kuamka mpaka kesho. Acha tu nikalale kwangu. Nahisi leo nitalala. Na hivi nimekukiss. Nitalala.” “Nimekumiss Colins. Ndio maana.” “Hata mimi nimekumiss Jelini wangu. Acha nile nikukumbatie.” Ikawa kama ameahidiwa ulimwengu. Akamuwekea chakula mezani. “Ukimaliza kula, njoo chumbani kwangu.” Kisha akakimbilia kuoga wakati akila.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alipomaliza kuoga akavaa nguo za kulalia kabisa. Ila za stara. Akamtumia ujumbe mama yake. ‘Colins yupo nyumbani. Amechoka sana.’ Mama yake hakujibu. Akampigia. “Sasa mbona hujibu!?” “Nina mambo mengi Jelini. Na ninajua kuna unalolitaka tu. Sasa hata nikikushauri kitu utanisikiliza?” “Sasa ushauri gani mama jamani! Mimi nataka abaki na mimi.” “Kwamba ahamie hapo?!” “Kuna ubaya gani? Si analala tu, kesho anaondoka? Tena ni kama akipitiwa na usingizi. Sio kwamba anahamia!” “Nyinyi wawili mnajuana wenyewe Jelini. Hakuna mnayemsikiliza. Nyinyi endeleeni.” Jelini akaanza.

“Ameniambia ananipenda mimi, mpaka kifo chake.” Mama Jema akacheka akimfikiria Jelini. “Weza kuta na mimi nimepata mtu wangu mama. Nampenda sana Colins.” “Basi taratibu mama yangu mzazi. Taratibu ili uone ndoa.” Jelini akatulia akifikiria. “Unanisikia?” “Ameomba nimpe muda.” “Hata mimi ameniambia. Lakini asije akabweteka tu.” “Sasa nitafanyaje mama? Nampenda Colins, sitaki nianze kumwambia mambo akanikimbia tena. Naomba nimchukulie taratibu. Kama nimeandikiwa basi atakuwa wangu, kama si riziki basi mama yangu.” “Na kweli. Haya, acha mimi niendelee. Nitarudi kwenye saa nne.” “Jeremy yupo chumbani kwake, bado anajenga vitu vyake.” “Leo ameniomba achelewe kulala. Nitakuja kumtoa huko mimi mwenyewe, wewe muache tu.” “Nashukuru mama yangu.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akasikia mlango unagongwa taratibu. Akajua tu ni Colins. Moyo ukajawa furaha. “Ingia tu.” Akaingia. “Umeshiba?” “Nakuridhika pia. Sitaki sisi tukosane Jelini. Inaninyima raha, kila kitu kinakosa ladha.” “Kwa kuwa nilikuwa sijakuelewa Colins.” “Kwa hiyo sasahivi umenielewa?” “Ndiyo, na nakushukuru kunijali.” “Utaendelea kutafuta mtu mwingine?” “Hapana Colins! Mimi nakutaka wewe.” Colins akacheka kwa furaha akimsogelea.

“Na mimi nakutaka zaidi Jelini wangu. Natamani ungeenda kunibembelezea kwangu sio hapa.” Jelini akacheka akifikiria akiwa amemuelewa. “Siwezi kumuacha Jeremy. Halafu bado nina hofu. Acha nikapime kwanza. Panda kitandani ulale.” “Nimechoka Jelini! Naweza kupitiwa na usingizi mpaka kesho bure.” “Ndio itakuwa vizuri.” “Nilale hapa!?” “Usiwe na wasiwasi.” Colins akafikiria, akasita. “Hata hivyo siwezi kulala bila ya kuoga. Acha tukae wote, kisha nirudi tu nyumbani.” “Si uoge hapa? Nitakupisha.” “Siwezi Jelini. Utanisamehe. Hii ni nyumba ya mama, haitakuwa heshima. Ingekuwa kwako hapo sawa.” Jelini akamuelewa.

“Basi kwa kuwa sasahivi umetulia. Rudi nyumbani ukapumzike. Tupange kuonana tena kesho.” “Utakuja nyumbani?” “Ukinikaribisha, nitakuja.” “Pale napaandaa kwa ajili yetu. Mimi, wewe na watoto wetu. Huitaji kukaribishwa. Muda na wakati wowote njoo tu.” Jelini akafikiria mawazoni na kucheka.

“Nini?” “Nimefurahi Colins! Ila usije badilika tu.” “Mimi si kigeugeu Jelini. Na nimekupata wewe mwenye kila kitu, nitafute nini tena? Sina sababu. Nakupenda na nakuahidi nitabaki na wewe tu. Nipe tu muda niweke mambo sawa. Nakuahidi tutafunga ndoa kabisa.” “Kweli Colins!?” “Jelini wewe ni mke wangu. Moyo wangu ndivyo unavyokuhesabu. Nakupenda, hata James anajua. Na naomba na mimi unihesabu hivyo. Usije tafuta mtu mwingine. Utaniua Jelini.” “Wakati mimi ndio nilikupenda kwanza, Colins wewe! Wewe ndio usije tafuta mtu mwingine.” “Siwezi.” Yaakanza mabusu tena.

Hapo yanaendelea, Jelini ananguo za kulalia. Colins akajitahidi kutovuka mipaka. Wakahamia kitandani. Wamelala huku romance inaendelea. “Nikuombe kitu Jelini?” “Nini?” “Kesho uje tushinde kwangu mpaka usiku. Au unawasiwasi na mtoto?” “Umesahau nilikuwa nikishinda baa?” Colins akaanza kucheka. “Usicheke bwana! Ninachotaka kukwambia, nilikuwa nikizurula, nikitoka hapa naweza nikaondoka hata siku tatu au nne. Mpaka wakawa wameshazoea ni kama sikuwa nikiishi hapa. Kwa hiyo mama amemfundisha huyo Jeremy, anajua kujitegemea mwenyewe. Hapo alipo, anamaagizo ya mpaka anakwenda kulala. Wewe mjaribishe tu muulize pengine saa tatu unatakiwa kufanya nini. Atakwambia.” “Haiwezekani Jelini!”

“Mama hakuwa na jinsi Colins. Nilikuwa naishi na pombe kichwani muda mwingi sana. Hakuwa akiniamini naye. Na yeye mama muhangaikaji. Ikabidi amlee hivyo. Ila hata mimi na Jema tumekua hivyohivyo. Alikuwa akitufungia ndani ili akahangaike kutafuta pesa. Na kama unavyopaona hapa, tumekua hapakuwa na majirani wengi. Hayo majumba yamekuja kujengwa miaka ya karibuni tu. Kwa hiyo alivyotulea mimi na Jema, ndio hivyohivyo na Jeremy. Anakua na maagizo yake ya mpaka usiku.” “Hasahau?” “Si mama atampiga mpaka achanganyikiwe! Hathubutu kusahau. Halafu Jeremy yupo kama Jema. Hataki matatizo. Mimi ndio alikuwa akinipiga sana.” Colins akazidi kucheka.

“Nikuulize kitu kingine. Wakati ulipokuwa ukiondoka hapa nyumbani kwa hizo siku tatu au nne, ulikuwa ukienda wapi?” Akamjaribisha tena kuona kama kuna jibu la tofauti na mwanzoni. “Kwa dada Doro. Anamihela huyo! Kwake pazuri kweli halafu chumbani kwake amefunga A/C, basi nilikuwa nalala mchana na usiku kwa raha ya upepo mwanana. Akienda kazini, ananiacha nimelala, jioni tunakwenda baa. Alikuwa kampani yangu kubwa sana. Ndiye aliyekuwa akinipa pombe za bure na nguo nzuri na za maana. Maana dada Doro anapenda kuvaa bwana! Na hapendi kurudia sana nguo. Basi huko ndio nilikuwa nikiishi. Nikimkumbuka mwanangu ndio nilikuwa nakuja hapa kidogo, narudi kwa dada Doro.”

“Kwa hiyo mpaka sasa hivi mnamawasiliano?” “Kasa alihakikisha anamtoa kabisa kwenye maisha yangu. Kwanza wivu, halafu alikuwa akisema haniongozi vizuri. Halafu naye Kasa alitukuta tupo kwenye kutoelewana vizuri, kwahiyo kwa kifupi sijawasiliana naye muda mrefu sana.” Colins akabaki akifikiria.

“Kuna jambo nataka kukuuliza, ila ni kama nasita. Sitaki kukuumiza.” “Juu ya nini!?” “Natamani kujua kilichotokea kati yako na baba yake Jeremy.” “Naomba usiwahi kumtambua kama ni baba yake. Inaniuma sana. Wewe muite tu mwalimu. Mwanangu ni mtoto mzuri sana, hawezi yule kuwa baba yake.” “Akija kutaka kumfahamu?” “Hakika hatamfahamu. Mbona mimi na Jema mpaka leo hatujui baba zetu! Hakika sitaki.” Akatoka kabisa hapo kitandani.

“Naomba usikarike Jelini. Njoo. Nikatika kutaka kufahamiana na kuweka msingi wetu. Ujue kwangu Jeremy atabaki kuwa kama watoto tutakao kuja kuzaa pamoja? Pale nyumbani kwa James, sikuwa nikiongea tu. Namuhesabu ni kama mtoto wetu wa kwanza, watakao zaliwa baada yake ni wadogo zake. Na tukioana tu, nataka nimuombe mama tumchukue tuishi naye.” Jelini hakutegemea.

“Colins!?” “Kabisa. Sasa wewe ulifikiria tutakuwa tukiishi bila yeye?!” “Pale kwa Kasa hakuwahi kukaribishwa hata mara moja ila mimi tu! Na wala hakuwahi kutaka kukutana naye watoke kama hivyo wewe ulivyotaka kutoka naye mkaogelee!” “Sasa hiyo itakuwa familia ya namna gani? Nataka tumu adopt kabisa awe wetu moja kwa moja na tuwe na dhamana naye. Wote tunatumia ubini mmoja.” Jelini akatulia kabisa. Colins amekuja na gia kubwa. Akakusudia kumfunga kabisa Jelini. Atake nini tena!

“Mwenzio nimejifunga kwako Jelini. Nimejifunga mazima kabisa. Labda uniambie kama unawazo jingine.” “Sina Colins. Ila siamini! Ujue wewe unaonekana kijana wa kileo, mtoto wa mjini, hufananii na mipango uliyo nayo!” Colins alicheka sana.

“Kweli! Unaonekana kama wale vijana ambao bado wanajirusha. Starehe kwa sana. Mambo ya club na totoz. Ila ukiongea hivi, unasikika kama mtu mzima! Mawazo ya kikubwa si ya kitoto! Mwenzio sijategemea!” “Nakupenda Jelini. Umekuja kunifuta majonzi nikiwa sijatarajia. Ukanionyesha upendo wa kipekee. Halafu yale maneno uliyoniambia siku ya harusi ya Jema na James, ambayo uliniambia hukumbuki, yalinibadilisha sana moyo wangu.”

“Hivi nilisema nini!?” “Hakika sitakwambia mpaka uje uyarudie tena mwenyewe. Maana niliuliza, nikaambiwa, mlevi hazungumzi kitu ambacho hakipo ndani yake. Ila pombe inamsaidia kukitoa tu. Mwenzio nasubiri tu, naamini ipo siku utakuja kuniambia tena. Maana ulimaanisha Jelini.” Jelini akatulia akijaribu kukumbuka bila kufanikiwa, huku Colins akiwa amejilaza hapo kitandani akimwangalia, yeye amekaa.

“Hakika sikumbuki Colins. Ila najua nakupenda wewe kuliko mtu mwingine yeyote yule niliyekwisha kuwa naye. Nikikwambia hata nilivyokuwa na Kasa nilikuwa nikikuwaza wewe, utaamini?” Colins hakujibu, kitu kilichomshangaza Jelini. Akatulia kabisa.

“Nakupenda Colins.” “Lakini mimi yule mzee ananiumiza kichwa Jelini! Sijui nifanyaje?” “Huko sirudi tena Colins. Tafadhali usiwe na wasiwasi.” “Lazima na siwezi kuzujia. Japokuwa uliniahidi kutorudi kwake, na nikakuomba ukiwa unarudi huko mimi niwe wa kwanza kujua, lakini leo ulikuwa ukirudi kwake Jelini! Hilo linanitisha, wala sitakudanganya. Najiambia kama nisingekuwepo kwa James leo asubuhi, inamaana pengine sasahivi ungekuwa uko kwake, mimi tena basi.”

“Nisingefanya kitu Colins! Nikuchukua tu vitu vyangu!” “Ambavyo uliniahidi unaachana navyo Jelini! Lakini bado umeendelea kuvifuatilia. Hivyo vitu vimekua na nguvu kubwa sana kwako kuliko ahadi na makubaliano yetu. Inanifanya najuta kuzaliwa masiki. Najuta kuwa sina hela kama za yule mzee. Maana na mimi kama ningekuwa na uwezo kama wake, inamaana pengine…” Akaona anyamaze tu. Jelini akatulia akikumbuka alivyomtuma Sheha. Akafikiria. Akamuona anasimama kufuata simu yake. Jelini ni mzuri bwana! Hata hapo tu Colins alikuwa akila kwa macho.

Mtaka Chauvunguni, sharti ainame.

Ni Colins.

Akamuona anapiga simu. “Ndosi?” “Kwema?” “Samahani nimekupigia muda mbaya.” “Bila shaka. Kwema? Mbona umenyongea?” “Nilifanya kosa. Sikuwa nimefikiria vizuri kwenye swala la kufuata vitu vyangu kwa Kasa. Tafadhali mwambie sivitaki tena. Anaweza kumpa yeyote amtakaye.” “Jelini!?” Haikuwa ikiingia akilini hata kwake. Na kwa kiasi alichomfahamu Jelini, alijua anamsimamo mkali. Anapelekaje taarifa kama hizo kwa mzee!

“Hakika tena Ndosi. Acha tu iishie hivyo. Na wewe nakushukuru kwa kila kitu. Hutanipata tena kwa hii namba. Na tafadhali usijaribu kunitafuta tena. Nimemalizana rasmi na Kasa, inamaana hata wewe tumemaliza. Sina nililobakiza kwako. Mambo yote umenifanikishia vizuri tu, nashukuru. Nakutakia kila la kheri.” Akamaliza na kukata simu bila ya kusubiri jibu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akamuona anampigia tena mtu mwingine. Colins akimtizama tu. “Anti langu?” “Niambie mtoto mzuri.” “Usiende tena kunidaia vile vitu.” “Jelini! Kwahiyo unanitosa anti?” Sheha akaishiwa nguvu kabisa. “Hapana anti. Miahadi yetu ipo vilevile. Ila usije kwenda kule, ukanitaja. Nishamwambia wakili wake, vitu vyote sivitaki tena.” “Sasa mimi nitaenda kwake nimwambie nini?” “Nitakuelekeza anga zake. Anapoendaga kwa chakula cha jioni, na maeneo yake anayopenda kuwepo. Anti wewe mjanja. Hutamshindwa malaya yule.” Hilo likamfurahisha sana Sheha mpaka acheka.

“Kama hivyo sawa. Tena naona hiyo ndio itakuwa nzuri zaidi. Maana nikikutumia wewe, anaweza akakataa akidhani nitakwambia. Acha nikamtege kivyangu.” “Na wala ukifanikiwa huko huna haja ya kuniambia. Wewe endelea naye tu.” Sheha akafurahi kama kapewa limwengu. “Nakushukuru mnooo.” “Wala usijali. Kila la kheri.” Akaaga.

“Sasa usije nisahau Jelini.” “Nakutumia sasahivi. Na tusije mzungumzia tena mimi na wewe. Wako kabisaaa. Ufanikiwe, usifanikiwe, ni juu yako. Sitaki tena. Ukimtaja kwangu ujue tutakosana anti.” “Hilo tena! Ndio raha yangu. Maana nilikuwa nikihofia usije nitangaza nikifanikiwa.” “Sio mimi, na wala hutanisikia nikimwambia mtu. Labda uropoke mwenyewe. Wewe mawindo mema.” “Mungu akupe heri.” Jelini akacheka na kukata.

Akamuona anaanza kuandika ujumbe huku akifikiria mpaka akamaliza na kutuma. Akamuona tena anaizima simu kabisa. Colins akimtizama tu. Kisha akatoa line nyuma. Simu akaiweka mezani, akamuona ile line ameingia nayo chooni kwake. Baada ya muda akasikia choo kikimwaga maji. Akajua ameitupia chooni. Akatoka na kumuona anaingia chumba kidogo cha nguo, akatoka amevaa koti linalofanana na kigauni kizuri sana chakulalia alichokuwa amevaa. Silk safi nyeusi. Na vile alivyokuwa mweupe, ikatoa uzuri wa aina yake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akarudi kukaa kitandani. “Nimemalizana ramsi na Kasa. Safari hii nakuahidi hutakaa ukamsikia tena. Na samahani, nilikosea. Vile vitu vilikuwa vikiniuma roho Colins, nikakosa uvumilivu. Lakini sivitaki tena. Huko sirudi, naomba uniamini.” Colins akazidi kumpenda Jelini wake. Love hakuwa akikosea. Mara zote hakuwahi kukiri kosa, na hata alipokosa basi amekoseshwa na huyohuyo Colins. Akafurahi na kumsogelea na kumlalia hapo mapajani. Jelini akaona raha! Akamshika kichwa vizuri.

“Naomba nikubali hivi nilivyo Jelini. Naweza nisiwe na mali nyingi, lakini mimi tajiri wa mapenzi.” Jelini akacheka. “Sitakusaliti. Utabaki wewe tu.” “Umenisamehe sasa?” “Naamini tutakuwa sawa. Kwanza niambie ni nini umefanya? Sijaelewa mazungumzo ya simu ya pili.” “Kuna dada namuunganisha na Kasa.” Colins akakunja uso. “Huyo dada anatafuta watu kama Kasa, na yeye Kasa anapenda watu kama huyo dada. Sasa kwa kuwa mimi simtaki tena, akaniomba nimpe yeye. Ndio nimemuachia.” “Jelini!”

“Kasa ni malaya yule. Hataishi bila mwanamke mmoja. Sasa kwa nini shoga yangu asinufaike naye, akatulia. Maana yeye shida yake ni pesa. Hana shida na umalaya wa mtu kama Kasa. Hivi kipindi hiki cha bunge, ametoka Dodoma kutafuta pesa, hana neno. Kwanza mwenyewe anasema hataki mwanaume wa peke yake ili asimgande, aendelee na maisha yake. Anapenda sana starehe anti Sheha. Alishazaa watoto wake wawili, wanasomeshwa na baba yao, yeye starehe tu. Hataki kuolewa au kuwekwa ndani na mwanaume. Kwa hiyo nimewaunganisha na naachana nao. Na wewe naomba tuache kumzungumzia. Usinirudishe tena huko. Nishatoka. Inatosha.” Wakatulia kidogo. Ukawa kama umezuka ukimya fulani. Jelini akimpapasa kichwani.

Akawa kama amekumbuka kitu. “Lakini bado hujanijibu Colins. Najua nilikukosea. Nilivunja ahadi. Umenisamehe?” “Yameisha na nimesamehe. Ila tafadhali naomba turudie maagano yetu Jelini. Kuna vishawishi vingi na vitaendelea kuja. Yule mzee ni jaribu la kwanza. Mengine yanakuja. Tusiposimama sisi wenyewe, tukateteana kwa hao wanaojaribu kutuingilia, tutashindwa haraka sana. Mwenzio nataka niishie kwako tu.” “Nashukuru Colins. Na ujue mimi sitakusaliti. Na mimi nitabaki na wewe tu. Na si kwamba najitetea, hata ningeenda kwa Kasa, na ningemkuta, japo nilimuomba mwanasheria wake amwambie amtaarifu kwamba nitaenda kuchukua vitu vyangu, nikijua anaweza asiwepo awe kazini, lakini Colins, hata ningemkuta, nisingefanya naye kitu.” “Huwezi kujua Jelini!” “Najua na ninajiamini.”

“Wanaume kama Kasa, ndio ilikuwa kampani yangu. Na sikuwahi kushawishika. Mimi si limbukeni na wala si dhaifu wa ngono. Kwangu nakiona ni kitendo kikubwa sana ndio maana yule mwalimu aliniuma Colins.”

“Alikuwa akinifanyia kama mnyama! Halafu hata baada ya pale hakuwa na shukurani kwa kutumia mwili wangu. Anaweza maliza haja zake na kuanza kunipiga.” “Kwa nini tena!?” “Kunitisha tu kwamba nisije sema. Yaani ilimradi tu. Mara ya mwisho nilipomwambia nimeshika mimba. Jamani alinipiga, mpaka nikazimia.” “Jelini!?”

“Kweli Colins. Alikuwa akinipiga eti nimtaje aliyenipa mimba. Mimi mzembe, najiachia tu kwa wanaume. Yeye hausiki na huo ujauzito. Nikija mtaja atamuua mama yangu na Jema. Bwana alinipiga siku ile!” “Naomba usilie Jelini wangu. Natamani kama ningejua tokea mwanzo. Na ningekuwepo na wewe mahakamani. Niliumia sana. Na sikujua kama ndio sababu iliyokuwa ikikufanya uishi na pombe kichwani kila wakati!” Akajinyanyua pale alipokuwa amemlalia mapajani akimsikiliza na kuanza mabusu kama kumtuliza.

Yakaendelea mabusu ya muda, Colins akamuachia. “Acha niondoke nisije nikashindwa kuwa na kiasi, nikaishia kulala kwa mama mkwe bure.” Jelini akacheka akimwangalia anavyonyanyuka. “Kesho umekubali kuja tushinde wote?” “Nataka asubuhi nianzie hospitalini. Anti Sheha ameniambia siku hizi kuna vipimo vyakupima UKIMWI hata kama vijidudu vimeingia muda mfupi.” “Unataka nikusindikize?” “Ningeshukuru Colins. Maana naogopa kweli!” “Basi usiende, unisubiri nitakuja kukuchukua twende wote mida ya saa nne asubuhi bila kukosa. Na acha woga. Uwe umeathirika au la, zipo njia nzuri tu tutashauriwa na kujua jinsi ya kuishi kuanzia sasa. Na usiulize swali jingine mpaka kesho tutakapojua matokea.” Ikabidi tu acheke.

“Ulijuaje?!” “Najua upo kwenye wakati wa kutaka kupata majibu yote sasahivi. Na najua utakaribisha hofu isiyo na sababu. Leo ulale ukijua kila kitu kitakuwa sawa.” “Nashukuru Colins.” Akamsindikiza, kijana huyo akaondoka bila mengi mpaka akamshangaza Jelini na kumuacha na maswali yasiyo majibu yakueleweka.

Siku Ya Miahadi Mingine Tena, Na Jelini

Kesho yake akiwa anajiandaa kwa furaha kubwa sana, akijua siku hiyo Jelini atakuwa nyumbani kwake, akasikia hodi mlangoni. Akatoka na kubaki na mshituko mkubwa sana. Hakutegemea aliowakuta hapo mlangoni. Babu yake, bibi pamoja na wazazi wake. Akawasalimia na kuwakaribisha ndani akiwa bado na mshituko. Alitegemea babu yake afike mjini ili azungumze naye yeye kwanza, ndipo akamrekebishie kwa baba yake, lakini ujio wake ukawa kama wakushitukiza! Na sura aliyoingia nayo hapo, si kama yupo upande wake, yupo na aliokuja nao!

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ni Usiku Uliopita Tu, Ametoka Kutoa Ahadi Nzito Kwa Jelini, Na Makubaliano Ya Kuanza Upya.

Je, Safari Hii Colins Atafanikiwa Kwa Jelini Aliyetupa Kila Kitu Kwa Ajili Yake, Au Ndio ‘Sikio Halizidi Kichwa’?

USIPITWE NA MUENDELEZO.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment