~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mzee Simba na mkewe
wakaomba kikao na wazazi wa Colins. Jumosi ikawa siku nzuri. Kikaandaliwa
chakula hapo kwao, mzee Simba na familia yake akiwepo na Colins wakaenda hapo.
Ikawa hali tulivu tu, na Colins ametulia haswa. Wakala na kunywa ndipo wakapata
muda wa mazungumzo.
“Kwa kuwa sasahivi
tupo ukurasa mmoja, nafikiri ni wakati muafaka wa Colins kuchukua nafasi yake,
yeye kama kiongozi. Maadamu ofisi yake ipo tayari na kila kitu kimekamilika,
naonelea jumatatu aanze majukumu yake.” Hilo likawa zuri na la kheri. “Na kwa sasa
alipo, na wadhifa alio nao, lazima abadili hata aina ya usafiri na nyumba.
Atakuwa mtu mkubwa sana. Au unasemaje Colins?” Pakatokea utani hapo kidogo,
basi mzee Simba akaonelea kampuni yao, impe gari nzuri, na yeye na Love sasa,
wahamie kwenye jumba la Kigamboni.
Huko nako wazee hao
wawili na wake zao walinunua si kiwanja tu, ni kiwanja cha MAANA, karibu kabisa
na baharini kama hoteli! Waliwekeza nguvu kwenye ujenzi wa hilo jumba, hata wao
wenyewe hawakuwa wakiishi kwenye jumba zuri la kiasi hicho. Yote hiyo
walikubaliana ni kwa ajili ya vizazi vyao. Basi likawa jambo la furaha kubwa.
Wazazi wa Colins wakafurahia kuona tena wazo linatoka kwa mzee Simba mwenyewe
wala si wao, upendo ukazidi kuongezeka katikati yao, wasijue yote hiyo ni shindikizo
la Love kwa wazazi wake.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jumapili kazi ya
kuwahamisha wawili hao ikaanza. Kwa furaha zote wazazi hao kama hawamjui Mungu,
na hawajui wanachokwenda kufanya vijana wao ni kwenda kinyume na amri ya sita.
Kuishi bila ndoa. Wakatoa baraka zao. Mpaka siku inaisha, nyumba ikachukua sura
ya wawili hao. Love na Colins. Wakaachwa hapo, Colins habishi kwa chochote, ila
kuitikia kila jambo. Maisha yao yakaanza tena, wakiishi kama walivyokuwa
wakiishi nchini Marekani. Wawili tu, ila hapo wakitumikiwa na wafanyakazi wa
ndani na nje.
Penzi Linalosubiriwa.
Mwezi ulishapita
tokea amsikie Victor. Na chuoni alisharudi kikamilifu akipambana tokea tukio la
kina Belinda. Akabaki akijiuliza nakushindwa kuuliza, kulikoni Victor
waliyetumia naye vilivyo kwenye hoteli ya maana vile! Alionekana kumkubali sana
Vai. Vai akazidi kunyongea moyoni asijue wa kuzungumza naye.
Akabaki kukumbuka
hili na lile alilozungumza Victor juu yake alipokuwa naye. Alimshusha hapo
chuoni kwa ahadi ya kurudi jioni yake watoke kwa chakula. “Hata kama alirudi
na kunikosa, ndio ashindwe hata kunipigia simu au hata ujumbe!” Ikashindwa
kuingia akilini kwa Vai na kubaki akiumia sana jinsi alivyotumika kikamilifu na
kuja kupigwa na kina Belinda kwa mwanaume aliyemuacha vibaya vile! “Hata
ujumbe!” Akazidi kushangaa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Hata hazikupita siku
mbili tangia akijiuliza hivyo. Akiwa kitengo cha mifupa MOI, alipangiwa juma
hilo na wenzie wawili, akiwa anapita nje ya vyumba vya madaktari akamuona
Victor akiwa na watu aliohisi wazi ni familia yake kutokana na mazungumzo
walipokuwa hotelini. Kijana mdogo aliyekuwa amefungwa POP mkononi. Akajua ni
mmoja wa mtoto wake. Mwanamke, aliyeonekana mtanashati tu. Kikazi. Safi.
Nadhifu. Macho kwenye simu kama mtoto wao. Moja kwa moja alijua ni Vera mkewe
Victor. Na Victor mwenyewe ambaye macho yaligongana moja kwa moja na Vai. Akawa
kama ameshituka kumuona Vai, akapigwa na butwaa kwa muda.
Vai alibaki
akiwatizama kadiri alipokuwa akiwasogelea maana walikuwa wamekaa nje tu kama
waliokuwa wakisubiria zamu yao ya kuingia chumba cha daktari. Ila hakuna
aliyekuwa akimuongelesha mwenzie kati ya watatu hao, wanafamilia. Vai
akashangaa alipowakaribia karibu kabisa, Victor akainamisha kichwa kana kwamba
hamfahamu kabisa! Akahamia kwenye simu yake kama mkewe na kijana wake.
Vai akiwa amevaa sare
yake ya kiuuguzi, akawapita bila hata salamu. Lakini kile kitendo kilimuuma
sana, kwani Victor alijifanya ni kama amemuona mtu asiyemfahamu kabisa. “Kwamba
kweli Victor ameshindwa kunigundua kwa ajili ya sare niliyovaa au ndio ameamua
kujidai hanifahamu!” Akajiuliza Vai akishindwa kuamini vile
alivyodharaulika.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Siku ikaanza kuwa
nzito. Wenzake walimuona kabisa hayupo sawa. Na kweli akili ilikuwa imevurugika
vilivyo. “Isijekuwa lengo lake ilikuwa ni kuniambukiza tu gonjwa!” Akaingiwa
hofu ya ajabu. Akijiambia pengine lengo lake lilikuwa nikusambaza tu vijidudu
vya UKIMWI, ndio akamfikia na yeye. Hapo ndio akashindwa kabisa kufanya kazi.
Akadanganya kichwa kinamuuma sana, akaruhusiwa kurudi hosteli kupumzika.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Walishatengeneza
kautaratibu kao. Bale akitoka kazini siku ya jumamosi mchana, basi atampitia
hosteli, anarudi naye kwake. Watalala hapo, kisha kesho yake wanakwenda
kanisani pamoja. Kujaliwa na Bale kuliendelea ila kukazidi kitu
kilichomchanganya Vai. Swala lake la kujifungia na Victor hotelini
hakulizungumzia tena. Wala hakumkumbusha swala la kupima. Akaendelea
kuishi naye kana kwamba hakukosea, kitu kilichovuta hisia za Vai zaidi kwa
Bale.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akarudi chumbani
kwake na kujikuta akilia sana. Akalia mpaka akamkumbuka Bale jinsi anavyomjali.
Akajikuta akimtumia ujumbe. ‘Nalia mwenzio.’
Hapohapo Bale akiwa kazini akampigia. “Nini tena!?”
Akamuuliza kwa kumjali. “Najilaumu Bale! Najilaumu
sana.” “Ni nini?” Vai akaendelea kulia. “Unataka nije?” “Hapana.
Wewe endelea tu na kazi.” “Siwezi kufikiria kama
wewe haupo sawa Vai. Niambie nini tatizo. Zungumza na mimi, pengine itasaidia.”
Akazidi kumbembeleza.
“Mwanaume
wa mwisho ameniacha mgumba. Lakini nahisi huyu wa safari hii ameniacha na gonjwa
la kufisha.”
Akaendelea akilia kwa wasiwasi. “Nimekutana naye
leo. Akiwa na mke wake na mtoto. Nimekumbuka maneno yako Bale. Huyu mtu
nilijiingiza kwake akiwa hana mpango wa kumuacha mkewe. Nikajiachia. Sasahivi
ananiona kama takataka!” “Nikuulize swali?
Lakini usikasirike.” “Nini?” Vai
akataka kujua kilichopo moyoni kwa Bale.
“Ulimpenda
Victor?”
Vai akashangaa sana. “Hapana Bale! Ila nimejidharau
na kuona nilijidhalilisha. Ni kama aliyekuwa na agenda fulani kwangu. Kama
kuniua tu.” “Au alikuona kwenye picha kama
ulivyoniambia. Akakutamani na kutaka kukutumia tu. Usiogope.” Akajaribu
kumtuliza. “Hilo ndio tatizo. Naogopa na siwezi
kwenda kupima hapa Muhimbili ninakofahamiana na watu wa maabara. Kama
nimeathirika kila mtu atajua.” “Basi nikitoka
kazini nakuja kukuchukua twende ukapime kwengine, halafu tutaenda kula.
Nitakununulia na icecream.” Ikabidi tu Vai acheke.
“Unanifanya
mimi kama mtoto mdogo! Unanidanganyishia icecream!” “Sio icecream
peke yake. Nitakupeleka na kula sehemu nzuri utakayochagua wewe.” “Mimi nataka
kuwa na wewe popote pale. Sitajali sehemu. Ilimradi uwe na mimi. Wewe unanijali
Bale, mpaka napatwa wivu siku ukipata mwanamke wa kumuoa.” Bale akajisikia
vizuri huyo! “Usipatwe wivu. Tutakuwa sawa tu.” “Wewe
ndio utakuwa sawa. Mimi nitabaki mpweke Bale. Sijapata mwanaume wa kunipenda na
kunijali hivi, kama wewe. Wengine wote niliokuwa nao wanapenda kunitumia tu na
kunitupa kama takataka!” Bale akatulia.
“Najichukia
Bale! Najiona mjinga. Narudia kosa kila wakati.” “Si tumekubaliana hutarudia
tena?” “Nimekoma.”
Bale akaanza kucheka vile jinsi alivyosema. “Unanicheka
Bele?” “Kidogo tu. Ila wewe sio mjinga. Sema inakuchukua muda mrefu kujifunza
jambo.” “Sasa si ndio ujinga huo?” “Sio ujinga. Na naamini kwa kuwa safari hii
umejifunza kiukweli na kuelewa hila za wanaume kwako, hutarudia tena.
Nitakuja tukapime. Na ujue nina zawadi yako nzuri sana.” Vai akacheka.
“Umeninunulia
nini?” “Kitu kizuri. Nimeenda kulipia leo baada ya kulipwa mshahara wangu wa
kwanza, jana. Nilipanga tokea naanza kazi, nikilipwa, mshahara wangu wa kwanza,
nikununulie kitu kizuri.”
Vai akajikuta akitokwa na machozi. “Nakufikiria Vai.
Nakufikiria sana. Ni hivyo tu uwezo mkubwa sina.” “Nakupenda Bale. Nakupenda hivyo ulivyo. Na kwangu wewe
ni tajiri wa kila kitu. Mimi sikuoni kama ni masikini. Kwa Victor nilikosea
Bale. Nilikosa. Na si kwa kuamua kwangu moja kwa moja kwenda kulala naye.
Niliamka pembeni yake siku inayofuata.” Kwa mara ya kwanza akamsimulia
ilivyokuwa. Kunywa wine na kulewa.
“Nakiri
baada ya kuamka ile asubuhi, pengine ningeondoka pale hotelini. Ila nafikiri…” Akasita. “Nilikosea Bale.” “Ila
hata kabla ya hapo ulishaamua kuniacha Vai! Uliondoka nyumbani nikiwa
nakuhitaji!” “Ni kwa kuwa nakupenda Bale.
Nakutakia mema. Hata nikikuomba unioe mimi, pengine ukakubali, sina uwezo wa
kukupa unachotamani.” “Na mimi siku ile
niliongea si kutaka kukuumiza. Nilikwambia kile nilichokuwa nakifikiria kufanya
maishani kutokana na kosa nililofanya kwenye familia ya baba yangu. Kwamba
nilijipa deni. Lakini nikiwa sina nia ya kukupoteza. Maisha hayana furaha bila
wewe Vai. Nimeshakuzoea, na sijui itakuaje bila wewe.” Ikamgusa zaidi.
“Nimeahidi
kutulia na kutoondoka Bale. Sitabadilika, mpaka uwe tayari kuendelea na
kipengele kingine. Sitakuacha peke yako tena, hata iweje. Tafadhali niamini.” “Nimeona
umejirudi na kwa vitendo. Na mimi nakushukuru. Acha nirudi kazini, na wewe
usijifungie muda huu wa kazi, ukilia kwa ajili ya kosa la nyuma. Huko ni kumpa
nguvu Victor.”
“Rudi
kujifunza, tupate hicho cheti cha unesi. Punguza hofu. Jioni tutakuwa na wakati
mzuri.” “Kama nimeathirika?” “Tutatumia dawa. Na maadamu utakuwa umewahi,
naamini tutakuwa sawa tu. Wala usiogope. Tutabadili maisha yetu kutokana na
hayo matokeo.” “Kwamba na wewe utasimama na mimi?” Mtoto wa kike
akataka uhakika. Maana alishahangaika na wanaume mpaka akachoka. Na hivi tatizo
alilo nalo ni gumu kupokelewa na mwanaume yeyote anayefikiria kuanzisha
familia! Akataka kusikia zaidi ili kujihakikishia.
“Nikasimamie wapi
tena? Sina mwingine, ila wewe Vai. Katika yote, tutasimama tu. Na Joshua anausemi
wake, anasema katika kila dhoruba itakayopiga, tuhakikishe ikishapita,
sisi ndio tubakie tumesimama. Na nilimshuhudia akiishi hivyo, aisee.
Hakuna urefu atakao takiwa aruke, yule mtu asiruke ili kufikia lake. Hakuna
dharuba iliyowahi mpiga yule kiumbe, asibakie yeye ndio amesimama. Na sisi
itakuwa hivyohivyo. Si kwa maradhi, si kwa uzima wetu. Sisi ndio tutabaki
tumesimama.” Vai alifurahi huyo, asiamini masikio yake!
“Nimefurahi.
Nimefurahi sana. Asante Bale. Hivi niliruhusiwa kurudi nipumzike lakini umenipa
nguvu mpya. Narudi tena wodini.” “Kabisa. Nitakuona baadaye.” Wakaagana wakiwa
wamejawa hisia za ajabu. Ikawa mapenzi ya ajabu yasiyoweza kutamkika. “Sijui
ndio Bale atanioa mimi!” Akaanza kuwaza Vai akirudisha sare zake mwilini.
Mara ujumbe ukaingia.
Ulikuwa ukitoka kwa Victor. Akafungua kwa haraka akitaka kujua amemwambia nini.
‘Nashukuru kutoniharibia mbele ya mke wangu. Asante.
Maana tupo kwenye kipindi tete. Mwanaume niliyedhani anamahusiano naye haikuwa
hivyo. Kumbe bado Vera ananipenda. Ameomba tujaribishe tena mahusiano. Nimerudi
nyumbani kwetu. Tunalea watoto wetu. Hali siyo mbaya. Ukweli Vera amejirudi na
hata yupo tayari kuongeza mtoto mwingine, anaamini safari hii tunaweza pata wa
kike. Na mimi nimeamua kutulia kwenye ndoa yangu.” Hapo akamuumiza roho
Vai. Akajuta kumwambia hazai. Kwamba mkewe anampa kitu yeye hataweza mpa. Ila
akaendelea kusoma.
‘Naamini
umeelewa. Ungekuwa ni wakati mwingine, mazingira mengine, wewe ndio ungekuwa
mwanamke wa kuwa na mimi. Lakini kwa sasa naona tuache iwe kama ilivyo, nijenge
kwangu. Nisiwe mwanaume wa kukimbia familia. Najua hata wewe usingetaka
mwanaume wa namna hiyo. Samahani kwa maumivu yeyote nitakayo kusababishia, ila
naomba uwe muelewa. Nakutakia kila la kheri.’ Vai akabaki amepigwa na butwaa,
asiamini alichokisoma.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ujasiri ukampungua. Furaha
yote aliyoacha Bale moyoni ikapotea. Akajiona si bora kuliko wanawake
wote duniani. Hana uwezo wa kuzaa. Hilo likampunguza ujasiri vilivyo. Hata
uzuri wake ukaanza kufifia kwenye kioo. Asijione bora.
Jioni ilipofika
akaanza matayarisho ya kutoka na Bale. Kujishuku kukawa kwingi. Anajiona hafai
tena. Ujumbe wa Victor ukaendelea kujirudia kichwani mwake na kuendelea
kumpunguzia ujasiri hata kwa Bale aliyemwaga moyo wake vilivyo. Ukweli Vai
alipendeza ila sivyo alivyojiona yeye.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Bale alipompigia simu
kuwa amefika, akatoka. Akamkuta akimsubiria nje ya gari. Msafi, kiofisi, kama
kweli mfanyakazi wa benki. Vai akacheka lakini Bale akagundua hayupo kama
walivyoagana mara ya mwisho kwenye simu. “Umependeza kweli Vai. Naamini
umeshajua pakwenda kula. Maana hivyo ulivyo, hatuwezi kwenda kula chips vumbi.”
Akacheka akijiangalia kwa kujishuku. “Asante. Lakini naomba tuanzie hospitalini
kwanza.” “Huna njaa wewe?” “Hapana. Nisindikize kwanza kupima ili nijue hatima
yangu.”
Bale akauvuta mkono
wake na kuushikilia. “Subiri kwanza.” Akabaki ameshikilia mkono wake kwa mkono
mmoja, mwingine akatoa cheni mfukoni. Vai hakutegemea. “Bale! Hii si dhahabu!?”
“Na mimehakikisha nimenunua nzuri na uzito wa kueleweka. Ikupendeze.”
Akamvalisha cha mkononi. “Hii ni ya shingoni. Na naona shingoni unayo cheni
tayari.” “Hii ni bati tu. Naweza kutoa.” Hapo hapo Vai akatoa ile cheni
aliyokuwa amevaa.
“Naomba mimi ndio
nikuvalishe.” Vai akacheka asiamini. “Mwezio sijawahi vaa dhahabu!” “Geuka.”
Akamgeuzia mgongo. Bado ilikuwa mapema tu, hata giza halijaingia. Mishale ya
saa 11 jioni. Akamvalisha na kumfanya ageuke. Cheni ilikuwa nzuri sana.
Mnyororo wa rembo za kopa, virembo vya moyo vilivyosukwa vizuri sana kuzunguka
kote. Hapakuwa na kidani. Ila ule uzito hata Vai mwenyewe aliuhisi. Alifurahi
Vai, akabaki amejishikilia shingo, ameinama mbele ya Bale hajui aseme nini.
Bale akacheka.
“Imekua kama vile
nilivyotaka iwe mwilini mwako. Umependeza sana Vai. Unamwili mzuri sana wa
dhahabu. Imekaa vizuri mkononi na shingoni.” Vai akajitizama mkononi. Akajihisi
machozi kumtoka. “Nashukuru kunifikiria Bale.
Asante.” “Karibu. Twende.” Akamfungulia mlango, akaingia.
Wazo la zawadi aina
hiyo alipata kwa besti yake, Malon. Alimuona ndio zawadi alikuwa amemnunulia
Naya siku ya graduation yake. Bale mwenyewe alipenda. Na kipindi hicho
marehemu Malon alikuwa ameishiwa kabisa. Amerudia umasikini baada ya kutoka
jela. Lakini alifanya kazi ya ulinzi, akakusanya pesa mpaka akampatia Naya
zawadi na kuja kuikamilisha seti nzima baadaye. Cheni ya mkononi, shingoni na
hereni. Aina hiyo ya zawadi ndio alijichanga mpaka akamnunulia Naya.
Sasa na yeye
alipokuwa akifikiria kitu cha kumnunulia Vai, hilo wazo likamjia kwa haraka
sana. Vai hakuwa msichana wa shida sana. Alimuona bado anatunzwa vizuri kwao.
Hakuwahi kumsikia akilia shida. Mara nyingi alikuwa akimsikia akisema kaka yake
amemtumia muda wa maongezi au pesa. Na bado baba yake alikuwa akimtunza kwa
kumlipia ada na malazi hapo hosteli. Kwa hiyo akataka kitu cha tofauti
kitakachoweka kumbukumbu kwake. Na kweli akawa amepatia. Vai amemwambia
hajawahi vaa dhahabu. Wakatoka hapo.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Walikwenda
hospitalini. Vai akatolewa damu. Walipotaka kumpa ushauri nasaa akakataa kwa
haraka sana. “Mimi mwenyewe ni nesi. Najua kila kitu. Ninachotaka ni kupima tu,
nijue moja.” Akawa mkali kidogo, Bale kimya. Hakutaka hata kujibu maswali yale
ya ushauri nasaa ya awali. Akang’ang’ania vipimo tu, bila risala. Aliye muhudumia
akawa muungwana. Akampongeza kwa kwenda kupima, akatolewa damu, wakatoka nje
kusubiri majibu.
Walikuwa wamekaa
upande wa peke yao. Bale akamuona amepotelea mawazoni, ila anazungusha cheni
yake ya mkononi. Akamsukuma kidogo kama amtizame. Akavuta pumzi kwa nguvu,
kisha akamwangalia. “Nikuonyeshe kitu?” “Nionyeshe.” Bale akakubali bila
maswali mengi.
Akamtolea simu na
kumuonyesha ujumbe kutoka kwa Victor, akamuacha asome. Bale akasoma mpaka
mwisho. Akamtizama. Akamuona anaendelea kuzungusha cheni yake mkononi. Akarudia
kuangalia muda ule ujumbe ulipotumwa. Kisha akatizama muda waliozungumza kwenye
simu. Akagundua aliupata huo ujumbe baada ya kuzungumza naye. Akagundua ndio
maana amekosa raha. Wivu ukaanza kumsumbua.
“Ndio maana umekosa
raha?” Akauliza swali la jumla tu kujua aliposimamia Vai. “Yeye kama Victor
hajaniumiza, kwa kuwa nilishaamua kuachana naye. Lakini huwezi amini katika
ujumbe wote huo mrefu, mimi nimekwama kwenye mkewe kuzaa. Imenirudisha
mbali! Huwezi amini Bale. Nimerudi kule nilikokuwa nikihangaika na yule
mwanaume wa mwisho kutafuta mtoto ili asiniache. Ulikuwa wakati wa kunyanyasika
sana kihisia.” “Kwani Victor yeye anajua kama huna uwezo wa kuzaa!?”
“Anajua.” Bale
akashangaa sana. “Yaani huo muda mfupi tu mliokuwa wote hotelini ndio
amekufahamu kwa undani hivyo!?” “Kuna kitu nilimwambia juu yetu, ndio
maana. Lakini sio kwamba tulizoeana kwa kiasi hicho!” Bale akawa bado
hajaelewa. Kabla hajauliza swali lingine, Vai akaitwa jina lake. Wakaenda
kuchukua majibu. Aliposikia tu hajaathirika, hakutaka mengi. Akashukuru
na kusimama. Ikabidi Bale naye ashukuru, watoke.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ila Vai akamuona
amepoa haswa. “Tunakwenda kula wapi?” Bale akauliza. “Victor aliambiwa habari
zako na Belinda. Akaambiwa kwako ndio ninakokuaga mara nyingi. Alipotaka kujua
mahusiano yetu, ikabidi mimi niwe mkweli.” Akamuona anainama kama anashindwa
kusema. Bale akakunja uso.
“Vai?” “Nilimwambia
kile ninachojisikia kwako.” Hayo maelezo yakawa hayajatosha kwa Bale ambaye
wivu ulishakuwa ukimtesa. “Tafadhali niambie kile ulichomwambia Victor, juu yetu
au yangu.” “Nilimwambia tulianza kama marafiki. Lakini baadaye mimi
mwenyewe, wala si wewe, mimi. Hisia zilianza kubadilika. Nikajisahau
uwezo wangu, nikatamani niwe na wewe tu, mpaka uliponikumbusha shauku yako
yakuja kuwa na familia. Ndio nikagundua mimi sitaweza kuja kukuzalia
watoto hata kama nikikuomba unioe mimi. Ndio ikabidi niondoke kwako japo moyo
ulikuwa ukiniuma. Ndio akajua mimi sizai.” Akamalizia hivyo.
Bale akavuta pumzi
kwa nguvu na kuzishusha taratibu. Ila akapata aghueni ya ajabu rohoni. Kwamba
Vai na yeye anampenda! Wakatulia hapo nje ya
viwanja vya hospitalini kwa muda kama waliopoteza dira.
Baadaye akavunja
ukimya kwa swali. “Lakini ulielewa vile nilivyokwambia juu ya mpango wangu?”
Vai akamwangalia akiwa amekunja uso kuashiria hajaelewa anachomaanisha. Maana
alikuwa mbali kimawazo. “Kwamba sikuwa na maana ya kukuumiza au kukupoteza.
Nilishajiwekea deni. Na kwa kuwa wewe ni mtu wangu wa karibu. Tunazungumza kila
kitu. Zamani sikuwa nikihitaji kuchuja jambo kukwambia ukweli, ndipo
nikakwambia bila kufikiria.” “Mimi sitaki uchuje mambo kwangu.” “Lakini
hilo liliniponza Vai. Uliniacha.”
“Nimeahidi
nitabadilika Bale. Na wewe niahidi hutabadilika.” “Hata kama jambo
litakuumiza?” “Acha niumie, ila niambie ukweli wote.” “Sawa. Twende tukale.”
Wakaondoa gari hapo hospitalini.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Hongera kwa afya
njema.” Vai akacheka. “Nimefurahi. Na nimekoma.” “Ila mimi sijafurahia wewe
kuumizwa na huo ujumbe wa Victor.” Vai akashituka. “Wewe si umetaka kujua
ukweli wote? Ndio hivyo. Wewe tuliagana ukiwa na furaha na umerudisha morali wa
kazi. Amerudi Victor na ujumbe wa kukukataa, eti unakosa raha!”
“Nimekwambia ni swala la kutozaa!” “Kwani wakati tukiagana mimi na wewe
hukuwa ukijua huzai mpaka alipokwambia Victor?” Vai akashindwa ajibu
nini.
“Mimi nahisi ni kama
ulishampenda na kumpigia mahesabu.” “Mwanzoni, ndiyo. Wala nisikatae.
Nilimpigia mahesabu. Kwa sababu alishaniambia ana watoto na anaachana na mkewe.
Nikamuamini. Ila ujue ni kipindi kile cha ujinga cha kutofikiria mpaka wewe
uliponifanya nifikirie. Lakini sio kwamba nilimpenda, ila niliona ni
kama kimbilio. Kwake isingekuwa kuna maswala ya watoto, kitu ambacho ni kama na
yeye aliniambia pale nilipokuwa nikilalamika kuondoka kwako kwa kuwa sina uwezo
wa kuzaa. Akaniambia nisikose raha kwa wakati ule, hatupo pale kutafuta mtoto.
Ndio nikabweteka. Ila mimi nakupenda wewe. Hii ni aibu tu ya kuachwa
vibaya vile, tena nikiwa nimepigwa vibaya vile na kina Belinda.” Bale akatulia.
“Tafadhali nifikirie
hata kidogo Bale. Kipigo chote kile! Tena baada ya kutumiwa muda wote ule na
Victor, halafu aje anikatae kwa namna hii, tena akijieleza mkewe atamzalia!
Kulikuwa na ulazima gani wakuniambia yote hayo kama si kunifikishia ujumbe wa
kuwa mkewe anampa kitu ambacho mimi sina uwezo wa kumpa? Si angesema tu
nimeamua kurudiana na mke wangu?” Bale kimya akiendelea kuendesha. Muda huo
ndio walikuwa wakijenga msingi wao mpya. Ni kama wote walikusudia kuanza upya.
“Tafadhali
usinifikirie vinginevyo Bale. Mimi nimeridhika na wewe.” Bale akamtizama. “Na
Mungu wangu atakuwa shahidi wangu katika hili.” Vai akaongeza akibembeleza. “Na
najua sasahivi huamini, lakini muda utajibu. Mimi mtu wako Bale.” “Nakuamini
Vai.” Hakutegemea. “Kweli Bale!?” “Kabisa. Huna sababu ya kuwa na mimi kipindi
chote kile. Nikiwa mlemavu, sina kitu, natunzwa na shemeji, kama si kunipenda. Najua
unanipenda.” Hayo maneno ndio yalimmaliza kabisa Vai. Hakutegemea.
“Ndio maana
ulinishangaza ulipoondoka! Nikajihisi kweli mimi nimjinga! Niliwezaje kukusoma
sivyo! Ikaniuma sana, na nikajilaumu kwa mengi. Lakini nimeshukuru umerudi Vai.
Naomba tuachane na ya nyuma.” “Naomba tuachane hata na la Victor basi. Huo
ukurasa niwe niliukosea, tuufunge. Naomba tuanze upya, iwe kama zamani.”
“Sawa.” Bale akakubali bila mengi mpaka Vai akashangaa. Bale huyu anajua kukosea,
kusamehewa na machungu ya kutosamehewa.
Amefikishwa sehemu mpaka akawa mwepesi sana wa kusamehe. Na asichokijua Vai,
kuwepo kwake hapo, yeye Bale anahisi ni kama Mungu anamtangazia msamaha.
Akampokea kwa furaha zote.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Walienda kula sehemu
ngeni kwao wote wawili. Lakini sehemu ya hadhi. Wakawa wanajicheka. “Tumepanda
chati.” Vai alimfanya Bale acheke sana. “Ila sasa sio tusahau vijiwe vyetu vya
zamani.” “Tena!?” “Wewe Bale vipi? Sasa tukiendelea kula hapa, tutajenga kweli?”
Bale akazidi kucheka ila akafurahia sana hilo wazo. “Hapa tunakuja mara moja
moja, sanaaaa! Lakini hatuachi kwenda kwenye vijiwe vyetu. Au unasemaje?” “Mimi
nimekukubali. Kwamba unakula ila unawaza na kesho!” “Kabisa baba yangu.” Bale
alicheka mpaka machozi maana hapo Vai aliongea kwa lafudhi ya kichaga
kabisa.
Stori zikaendelea
wakichekana kula kwa kisu na uma. “Sasa hapa tena sio tutie aibu na wewe Bale!
Tujidai ni mambo ya kawaida kabisa.” “Wewe ndio unatetemeka mikono. Mwenzio
nimeshazoea.” Vikaendelea vicheko mpaka wakamaliza. Kesho yake wote majukumu
yanawasubiri. Wakaamua kufunga siku. “Natamani turudi wote nyumbani, Vai.”
“Ujue kesho itabidi udamke alfajiri na mapeme ili uniwahishe hosteli.” “Hamna
shida. Twende.” Safari ya kwa Bale ikaanza.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Bale hulala kwenye
kochi, Vai chumbani kwa Bale. Bale akawahi chumbani kwenda kuoga wakati Vai
yupo sebuleni akimsubiri atoke amiliki chumba. Ni utaratibu wao, walishazoea
wala si kupanga. Bale akatoka akiwa ameshavaa mavazi ya kulalia, na mto pamoja
na mashuka. Akachechemea mpaka kwenye kochi kubwa. Wakazungumza hapo, wakaomba
pamoja, wakaagana kwenda kulala.
“Ulale unono.” “Bila
hata kuniambia, leo nitalala unono. Na dhahabu hizi mwilini! Aisee lazima.”
Bale akaanza kucheka. “Usifanye mchezo na nguvu ya dhahabu mwilini. Inaleta
usingizi.” “Sawa Vai.” Vai akaelekea chumbani kisha baada ya muda Bale
akamsikia akifungua mlango.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Bale alishafunga
milango ya nyumba na kuzima taa. Akanyanyua kichwa pale alipokuwa amelala, na kumuangalia
pale mlangoni alipokuwa akitoka. “Nimeshindwa kulala.” “Umetoa dhahabu?” Akamuuliza
kwa utani lakini akashangaa anajibu kwa unyonge. “Hapana Bale. Nilikwambia nakupenda
mara kadhaa. Hujanijibu hata mara moja!” Akaongea kwa kulalamika akiwa
amesimama palepale mlangoni. Bale hakutegemea. Akarudisha kichwa kwenye mto
vile alivyokuwa amejilaza kabla hajatoka. Vai akabaki amesimama palepale
akimtizama ila na yeye akahisi kukataliwa kimapenzi, amepewa nafasi ya urafiki
tu. Akajisikia kuumia vibaya sana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kemi Ametimiza Azma Yake. Na Jelini Na Yeye Amekosa. Colins
Maisha Mapya Na Love. Vai&Bale?
Usipitwe
Na Muendelezo.
0 Comments:
Post a Comment