Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 3. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 3 - SEHEMU YA 3.

Penzi Kikohozi. Siku ya ijumaa usiku, Jelini akapokea simu ya shemeji yake kwa kutumia simu ya mama yake. “Shemeji yako anataka kuzungumza na wewe.” Akapokea simu maana na mama yake ndio alikuwa ameingia tu kutoka kwenye shuguli zake. “Shem, naomba kwa

heshima yangu tu, msikilize Colins. Tafadhali kubali kuonana naye mzungumze. Hali yake mbaya. Amedhoofu, hali kabisa.” “Nikwambie ukweli shem, mimi mwenyewe nina hamu na Colins wangu. Hivi hapa nilipanga kesho niende nikamuone. Nimejuta kuongea vile. Nahisi bado nilikuwa na hasira nikihisi hanitaki. Ila nikajiambia nitajitahidi kumuonyesha nampenda mpaka aje anipende.” James akacheka kwa aghuheni.

“Kweli nimegundua nampenda Colins. Siwezi kuishi bila yeye. Akiniambia ananipenda hata kwa kunidanganya, nakubali.” “Hakudanganyi. Colins anakupenda sana. Ila kuna alikopita kwenye mahusiano ya nyuma, ndio maana unamuona vile. Mimi namfahamu Colins. Ukimuonyesha unampenda, na unataka kuwa naye kama hivi ulivyoniambia, atapata ujasiri, naamini atakuwa kile unachotamani.”

“Nashukuru shem. Mimi naona yeye ndio aje kesho. Nimpikie vitu vizuri, ale, kisha alale ndio aende kwake. Safari hii nitamsikiliza anachosema na kumkubalia bila kumpinga ili atulie. Nampenda Colins wangu. Ujue aliniambia kama mapigo yake ya moyo bado yanadunda, nijue mimi ndio mwanamke wake tu, hatakuwa na mwingine?” James akacheka. “Kweli Shem. Sasa nitake nini kingine?” “Na mimi ameniambia hivyohivyo. Atatoka hapa duniani akiwa anakupenda wewe tu.” Jelini akafurahi. “Mwambie namsubiria.” “Nashukuru shem.” Wakaagana Jelini akaanza kurukaruka kwa furaha. “Kazi ipo!” “Si kidogo.” Akajibu Jelini akicheka.

Jumamosi.

Jelini akadamka kwenda sokoni akimjua Colins anaweza kufika hapo wakati wowote. Akataka awahi ili akifika hapo asimkose. Akarudi na kuacha geti wazi, akiwa amerudishia tu. Kazi ya kupika ikaanza. Jelini cha uvivu alipika mpaka basi. Kila alichopika akaona hakitatosha. “Kingine nitamfungashia akale kwake.” Akawaza moyoni. “Na akija, nitamwambia nashukuru kwa heshima ya kunisubiria mpaka ndoa.” Hayo anazungumza na cheko huko jikoni, mama yake alishaondoka kwenda kwenye biashara zake.

Akafanya yote huko jikoni mpaka akasafisha jiko, Colins hajafika. Akaenda kuoga ili akija amkute msafi. Akajitengeneza vizuri na nguo ya heshima tu si kimtego. Colins hakutokea. “Labda atakuja jioni.” Akajipa moyo. Mpaka saa nne na nusu usiku mama yake anaingia hapo na kukuta vyakula mezani, Colins hakuwa ametokezea. Akafunga milango yote akimuhurumia mwanae. Jelini alishakuwa amerudi chumbani kwake. Akaona hata asimuulize. Ni kawaida ya Colins kutotokea, ila kurudi na sababu. Kazi ya kuweka vyakula kwenye friji ikaanza mpaka mwisho. Akaona aingie tu chumbani kwake bila kutafuta ya undani.

Jumapili.

Hakuna Msiba Usiokuwa Na Mwenziwe.

Siku ya jumapili Jelini akiwa bado chumbani, anaona hata shida kutoka asije akaulizwa na mama yake juu ya Colins, kwenye mida kama ya saa nne asubuhi. Mama yake alikuwa na yeye chumbani kwake akijiandaa atoke, wakasikia hodi getini. Wakapata ugeni mzito. Babu, bibi, na wazazi wa Colins wakawatembelea. Ikawa kama hali ya kushitusha kidogo, ila Jelini akadhani sababu ya kumkataa Colins, basi wameamua kuja kutoa posa. Ikawa hali ya sintofahamu. Ila kwa jinsi walivyoingia na kukaa hapo sebuleni, hata mama yake akaanza kuingiwa wasiwasi.

“Kwema jamani?!” Akaanza mama Jema baada ya kufunga mlango na kukaa. “Labda uturuhusu tuanze kwa maombi kwanza ili kumuharibu mkuu wa anga wa mahali hapa. Ili kila tunachozungumza, kieleweke.” Akaongea bibi mtu, Jelini na mama yake wasielewe. “Maana zipo nguvu za giza, zinaweza kuteka watu ufahamu, wakafanya mambo bila kujijua. Ila sisi tunasimama kinyume cha kila aina ya nguvu za giza…” Bibi akajawa jazba na nguvu ya ajabu. Akasimama kabisa na kuanza kukemea.

Anazunguka hapo aking’oa na kuharibu kila falme za giza. Akimtenga Colins na kila alicholishwa. Hapo mama Jema akamwangalia Jelini, na yeye akawa haelewi. Akapiga simu kwa James na kumuacha asikilize. Bibi aliomba huyo bila kuchoka, akilia na kumsihi Mungu amtete Colins. Hiyo kelele ikamfanya hata Jeremy atoke chumbani kwake aende akaangalie. Ikawa hali ya sintofahamu, maombi yakiendelea.

“Hodi ya mlangoni, Jema, mumewe na mtoto ndio iliyomfanya bibi apoe maana alikuwa akisaidiwa kwa sauti za uombaji za kawaida za waliokuja nao. James na familia yake wakaenda kukaa hapohapo sebuleni, ndipo bibi akaanza kupoa.

“Kwema jamani?” Akauliza James akimtizama baba yake Colins kisha mama yake na wengineo. “Sisi tumekuja kuwekana sawa.” Wote kimya baba Colins akizungumza. “Colins ni kijana wetu na tumemlea katika mazingira, tamaduni na imani yetu. Hata fikiria yake na penda yake, inaendana na kile alichokuzwa na sisi.” Babu akawa akitingisha kichwa kukubaliana na anachozungumza baba Colins.

“Kitendo cha Colins, kuanza mahusiano na mtu kama Jelini, kimekua cha kushitua na kushangaza sana.” “Mtu kama Jelini?!” Mama Jema akauliza. “Samahani mama. Naomba waache wamalize tu. Tafadhali sana.” James akataka kusikia.

“Mbona jibu ni rahisi tu. Baba yake anapozungumzia Mtu kama Jelini, anamaanisha asiwe mwenye haiba kama ya Jelini.” Babu akaongeza kwa haraka na kuendelea. “Colins amelelewa kuwa kiongozi wa familia. Akizingatia uchumi wa familia nzima. Sio wake tu, ukoo mzima. Na hiyo sio kwake tu. Ni kwa vijana wetu wote wanaozaliwa kwenye ukoo wangu. Na ndio maana wote utakuta wanaoa wanawake wenye maadili. Wacha Mungu, wanaojua na kuelewa jinsi ya kubeba familia kwenye maombi kama hivi mlivyomsikia bibi yake akiomba. Waliosoma, nikimaanisha wenye kipato chakusaidia uchumi wa familia.” Babu mwenyewe amekaa hapo anaonekana bado salio benki linasoma. Mzee mwenye neema.

“Endelea.” Akamtaka baba Colins aendelee. “Kwa hiyo chochote mlichotegemea kitokee kati ya Jelini na Colins,” “Kwanza mtambue kabisa, tumeshatengua katika ulimwengu wa roho. Hakuna silaha itanyanyuka kinyume ya Colins ikafanikiwa. Kila ulimi utakaotamka jina la Colins kwa ubaya wa kutaka kumfanya mateka, tumeshauhukumu mkosa. Tunatengua kila laana.” Bibi alimkatiza mtoto wake na kuendelea kwa muda mpaka wenyeji wao wakabaki wametoa macho.

Mama Jema hajui kanisa, wala mganga. Hanaga vita na shetani wala Mungu. Hajawahi kukemea pepo, wala haombi Mungu. Maisha yake yanajiendeaga tu. Sasa akakutana na wakristo wenye imani ya namna yake. Kulisemwa ya kimungu hapo, akabaki amepigwa na mshituko. Hiyo fujo ya kimungu ikaendela hapo mwishoe wakahitimisha kuwa Jelini aachane kabisa na kijana wao. Hawataki kumuona tena hata nyumbani kwa Colins.

“Bora mmeongea hivyo, maana mlikuwa mnanichanganya. Sijui mnaomba au mnaongea! Ila mimi niwaambie ukweli kabisa, mwenzenu nampenda Colins.” Jelini kama kawaida yake akaongea kirahisi tu. “Na angenioa mimi, ningekuwa nampenda, namuheshimu na kuwa naye katika kila hali kwa kuwa nampenda Colins wangu.” Wote wakabaki wamepigwa nabutwaa kama ambao hawakutegemea.

“Ila bora hivi mlivyokuja nimejua nyinyi sio wazazi wazuri kwa watoto wenu. Mnalazimishia watoto wenu mambo wasiyoyapenda. Kwahiyo hata mimi pia sitaki tena kuwa karibu na nyinyi mtakuwa watu wakulazimishia mambo yenu tu kila wakati na watoto wangu sitaki wawe kama nyinyi. Kwa hiyo wala msiombe Mungu, eti sijui nisije kwenu! Hata mimi japokuwa nampenda sana Colins, lakini sitaki tena. Hatuji tena kwenu. Hatutaki tena. Na nyinyi hapa kwetu pia hatutaki mje tena. Mnaleta fujo na kelele ambazo kwanza sisi hatuwaelewi! Mkiondoka hapa, msirudi tena.” Jelini akaongea bila shida na akamaliza.

“Mimi sijui nyinyi mnaongelea nini, lakini Colins niliyezungumza naye mimi siku ya ijumaa, siye huyu mnayemuwakilisha hapa.” James akaongeza kwa Jelini. “Si kwa sababu sio akili zake!?” “Mimi si mshirikika wala mcha Mungu sana kusema najua kila kitu. Ila wazazi wangu, hiki mnachokifanya kwa Colins si sawa, na kinaniashiria kabisa hamjaweza kumsikiliza Colins mwenyewe mkajua kinachoendelea kwenye maisha yake. Mimi nafanya kazi na Colins na nipo naye karibu sana. Namjua…” “Sema ulikuwa ukifanya naye kazi.” Baba mtu akamkatiza James na kumchanganya James kidogo.

“Colins ni mtawala wa mali nyingi sana ambazo sisi tumezitafuta kwa jasho letu. Kuanzia jumatatu anaanza kazi kwenye mali za familia kama mtawala na kiongozi sio hicho anachokifanya huko ambacho hakiongezi chochote kwenye maisha yake ila kumpa pesa ya kula tu. Colins anauwezo mkubwa sana lakini kwa muda mrefu sana amejifunga kwenye vichache, ndio anaanza kuchukua hatua sasa kama mtawala. Tafadhali acha kumfuata nyuma na kumchanganya.” “Nahisi mimi nitakuwa kama Jelini tu, msiwe na wasiwasi juu yangu. Wala sitamsumbua ili awe kile mnachokitaka awe.” James na yeye akajiweka pembeni.

“Naona mpaka hapo tupo sawa. Hapatakuwa na lawama baadaye.” Akaongeza baba Colins akisimama kuashiria kikao kimeisha. “Sio kutoka kwa familia hii.” Akaongeza James na yeye akisimama kama wageni wao. “Ila mama Colins, tafadhali mwangalie Colins. Hali kwa muda mrefu sababu ya kuchanganywa na hayo mambo ya kwenu.” “Wala si kwetu.” Akadakia bibi mtu. “Sawa. Naomba nirudi kwa mama Colins. Mimi nimemshuhudia Colins akitaka kuanguka mara kadhaa kwa njaa. Hali na halali. Hayupo sawa. Kwa hiyo wakati mkiendelea kumuombea, tafadhali mama, kumbuka na swala la chakula.” “Atafunguliwa na atakuwa huru tu.” Bibi akaongeza kibabe, chakushangaza mama Colins hakujibu wala kuongea, ila na yeye walimuona akichangia kwa nguvu zote kwenye maombi. James akaenda kufungua mlango kuwaashiria waondoke. Na wenyewe bila shida, wakaondoka bila ya kuaga.

Kwa Kina Jelini.

 “MmmmH! Lakini mimi nahisi kuna kitu hakijakaa sawa. Kwa nini waje wao bila Colins?” Jema akawaza kwa sauti. “Unakumbuka hali niliyokwambia anayo Colins? Hana nguvu hiyo ya kufanya fujo zote hizi. Colins amedhoofu mpaka ikabidi kumuombea azungumze na Jelini. Na nilivyompa majibu kuwa Jelini alishakuwa na hamu naye, atamuandalia chakula aje, akataka kuja usiku uleule.” “Kweli shem?” Jelini akauliza kwa kunyongea.

“Hakika. Mimi ndiye niliyemkataza na kumsihi alale mpaka kesho yake. Aje kwako akiwa ametulia na akili inaweza kufikiria, maana alikuwa hoi. Nikamtisha nikamwambia akikujia tena vile alivyo, ataharibu zaidi maana atakuwa hana uwezo wa kufikiria vizuri. Ndio akakubali kulala ila akaniambia asubuhi na mapema sana atakuwa hapa. Sasa kutotokea hapa siku ya jumamosi halafu leo wanatokea hawa! Na mimi nipo kama Jema, nahisi kuna kitu hakipo sawasawa.” Pakazuka ukimya wa muda.

Wakamsikia mama Jema akiguna. “Nini mama?” Jema akauliza. “Nahisi, sitaki kukuza, ni kama wanahisi pengine Jelini amemloga kijana wao!! Au niwe sijaelewa!” “Eti hata mimi nilihisi kama wanatuona sisi wachawi!” Jelini naye akawa kama hajaelewa.

“Sitaki kuongeza ubaya kwenye ubaya, lakini kwa jinsi walivyokuwa wakiomba, ni kama kuharibu hapa nguvu zilizotumwa kwa Colins, ambazo zinamshikilia. Kwamba wanajua amelogwa na nyinyi au Jelini. Kwa hiyo kuwa hapa nyumbani kwa kina Jelini ndio wamekuja kung’oa mzizi wote wa uchawi.” Maelezo ya Jema yakawatoa macho wawili hao, mama na mwana. Wote hawajui uchawi wala nguvu za Mungu.

“Makubwa! Haya nashukuru kwa kuja kwa haraka. Mimi natoka kwenda kutafuta pesa.” “Na mimi nakuja mama. Sitaki kuendelea kuonekana mvivu na kila mtu. Kwanza kichwa chenyewe hata hakisumbui kama nikiwahi kunywa dawa. Kama Jema hutajali kwenda na Jeremy naomba muende naye nitakuja kumchukua.” “Hapana Jelini. Wewe unataka kuniharibia ratiba yake huyu. Nataka saa mbili na nusu awe ashalala. Ukianza kumzungusha kwenye majumba ya watu, utamchelewesha. Mwache abaki hapa. Chakula kipo. Anajua muda wake wakula, kuoga na kulala. Utaratibu uleule. Kugusa kitasa cha mlango ni mpaka…” “Kuwake moto.” James akacheka vile Jeremy alivyomalizia kwa haraka.

“Kumbe ndio maana Colins alikuwa anasema alikuwa akija hapa, anagonga mpaka anachoka!” “Kabisa. Huna funguo za humu ndani, mimi au Jelini tusipokuwepo, huwezi kuingia.” “Utaratibu huo sisi tumekua nao tokea wadogo. Huyu Jelini ndio alikuwa matatizoni kila siku, maana ndani hawezi kutulia, mpaka aende mtaani. Sasa mama akirudi kwa kushitukiza halafu asimkute, anaenda kumfuata mtaani anakoenda kucheza. Utamsikia anarudi naye kamshika mkono, analia. Anakuja kufungiwa tena.” Wakaanza kucheka. Angalau wakajisahau machungu ya kina Colins. James na familia yake wakaondoka, Jelini na mama yake wakaingia mtaani. Jeremy akarudi chumbani. Maisha yakaendelea.

Kwa Kina Colins.

Kilichotokea Siku Ya Jumamosi.

Huku kwa Colins kumbe asubuhi aliyokuwa amepanga aende kwa kina Jelini, Love alifika hapo kwake akiwa na wazazi wa Colins, Kemi Kasa na baba wa makamu tu. Kemi alisema ndiye atakayewasaidia kumkomboa Colins. Wakawa wamejiandaa haswa kumkabili kwa siku hiyo. Sasa walipofika hapo, Colins akabisha kuwakaribisha wakae, akiwaambia safari hiyo hataki kabisa kupotezewa muda kwa vikao visivyo isha. Hapo ndipo aliharibu.

“Mnanipotezea muda na maneno mengi yasiyoisha. Nishasikiliza mnachotaka, niacheni na mimi niamue. Hamuwezi kuniburuza mimi kama mtoto mdogo, kiasi cha kunijia nyumbani kwangu muda na wakati mnaotaka nyinyi! Hapana kwakweli. Leo iwe mwisho na naomba tuheshimiane. Naombeni tokeni. Halafu hichi mnachotaka kiendelee, tukipangie muda mwingine.” Colins akaweka msisitizo tena akiwa amesimama.

“Yaani wewe Colins kweli unakataa hata maombi kweli!” Love akashangaa sana kwa sauti kama anayetaka kuhamasisha wengine. “Hayupo sawa huyu. Na hizi si akili zake. Colins siwakukataa maombi.” Akaweka msisitizo. “Lazima umpe nafasi mtumishi wa Mungu kuomba. Ameacha shuguli zake zote na kuamkia kwako halafu unataka umfukuze bila maombi!? Hapana. Mama Colins zungumza naye.”

“Ni maombi tu Colins, mwanangu. Haitachukua muda mrefu.” “Umepatwa na nini mama wewe! Kwa nini umekuwa mtu wa hivyo na unaelewa kila kitu? Kweli wewe niliyekuamini na mambo yangu ya ndani hivyo ndio leo unakuwa mgeni wa kila kitu na kumkumbatia Love na kumuacha aendeshe mambo vile anavyotaka!?” “Ni kwa kuwa nakutakiwa mema Colins. Hata kama kulikuwa na tofauti zetu, lakini siwezi kukuacha ukapotea hivihivi. Nakupenda, nimejirudi lakini bado tu huoni!” “Si akili zake. Mimi nashauri mtumishi aanze kuomba.” Kemi akaweka msisitizo.

Wakati Colins anakataa, wakaanza kusema ni mapepo. Huyo muombaji akafanikiwa kumuangusha chini, Colins ambaye hakuwa na chakula mwilini, ukimlinganisha na mtumishi aliyelipwa na kupambwa na Kemi pamoja na Love, na ahadi kemkem endapo atafanikisha shoo nzima. Kwa hiyo alijawa mukari wa kazi kufanikisha. Kusukumana kukaendelea, akimuombea akiwa amemminya sakafuni akimpaka mafuta. Yale mafuta yakamchefua Colins, akaanza kutapika.

Hilo nalo likawa jambo la kufurahisha, akasema anatapika vitu alivyolishwa na Jelini. Akahangaika hapo sakafuni akiwa amekabwa vilivyo mpaka akawa amejichafua kila mahali. Hatua ya mwisho akasema anamuwekea kitambaa cha upako, hicho ndicho kilichommaliza kabisa. Colins akanyamaza kimya. Mtumishi akasema sasa ametulia, akaoshwe, apumzike.

Love akajitolea kwenda na mtumishi ndani akamuogeshe, apumzike na akasema atakuwa naye mpaka atakapoamka. Hilo zoezi lilichukua muda wa kutosha tu asubuhi hiyo. Lakini wazazi wakaondoka wakiwa wamepewa tumaini kuwa, yote mabaya aliyokuwa amelishwa, basi yametolewa. Colins yupo huru ila anahitajika kuendelea kuombewa. Kwamba mtumishi bado analo zoezi endelevu. Na wenyewe wakamlipa, ila iliitwa sadaka ya shukurani, Colins akaachwa mikononi mwa Love, shoga mpya Kemi, na mtumishi.

Jumapili.

Sasa walipotokea kwa kina Jelini, maneno ya Jelini, vile walivyokuwa wakiwashangaa pale na kile wanachokifanya, bibi kuomba akikemea, na James kumalizia kuzungumza naye ramsi, kitu kikaanza kumsumbua mama Colins. Akawa hajui sawasawa nini hakipo sawa, lakini hajui aseme nini. “Kuanguka kwa Colins, inaweza kuwa kweli ni njaa!” Akawaza mama Colins na kushindwa kuongea kwa wenzie waliokuwa wameongozana, zaidi wakwe. Mama mkwe wake anajulikana kama mama mwenye hekima, mcha Mungu na anatembea na roho ya uonaji. Leo aje aseme vinginevyo, wakati asubuhi hiyo pia walitoka nyumbani kwa Colins akaomba sana!

Akazidi kuwaza kwa hofu ila asiseme. Hao wakwe sio wakwe njaa. Wasomi, wanapesa na hata mumewe na nduguze, wanawaogopa mbali na heshima. Kikubwa, anamuunga mkono mumewe anayetaka jasho lao lisipotee, akimtaka kijana wao awe mtawala wa mali zote. Sababu ikawa nzito, iliyoungwa mkono mpaka na wakweze, leo yeye peke yake anapingaje? Akalinyamazia kimya, ila akili kumkichwa.

Palipotulia, akaenda kununua dripu ya maji ya sukari, akaenda nyumbani kwa Colins. Akamkuta mama Simba na binti zake hapo, wamejaa sebuleni wakiongea yao na kucheka. Alipouliza juu ya Colins, akaambiwa na Love amerudi kulala muda si mrefu, alikuwa hapo akizungumza nao. Haikuwa kweli, alimdanganya tu mama Colins. Huyo Colins hakutoka kitandani tokea wamuweke hapo akiwa na mtumishi.

Akaomba kwenda kumuona, akamkuta amelala. Na wenyewe wakaingia hapo chumbani. Wakamuona anampima pressure.  “Atakuwa tu sawa. Na hivi hayo majini aliyokuwa ametupiwa yameondoka, hapo tu nikukazana maombi na apumzike kwa muda wakutosha.” Akaongeza mama Simba. Mama Colins akabaki kimya akimtizama kijana wake. Walipoona hajibu, wakatoka. Alipoachwa tu peke yake na mwanae, akamuwekea maji yale ya kuongeza nguvu mwilini, kwani pressure ilikuwa chini sana. Na walitoka hapo hata hawakutaka kujua majibu ya pressure aliyoyapata kwa Colins. Hilo huyo mama likamshangaza.

Nesi huyo hakuchukua muda kupata mshipa wa kijana wake, akamuwekea mwanae drip. Akalifungulia kwa haraka ili limpe nguvu. Akabaki amekaa hapo chumbani peke yake. Hawakurudi. Akakaa mpaka likaisha, Colins akawa bado amelala. Akatoka. Kuzungumza na Love.

“Naona bado amelala. Sasa kama kuna msaada wowote unaotaka, nijulishe ili usaidiwe, ibakiwe kazi yake tu huyo. Hata nguo nitamtuma kijana aje achukue, afue. Na chakula nitawaletea.” Love akashukuru, mama Colins akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Nini kitaendelea?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment